Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Pesa na Maadili—Historia Inatufunza Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Februari 1
    • Pesa na Maadili—Historia Inatufunza Nini?

      MNAMO Aprili 7, 1630, watu 400 hivi walisafiri kwa meli nne kutoka Uingereza hadi Amerika. Wengi wao walikuwa watu wenye elimu ya juu. Wengine walikuwa wafanyabiashara wenye mafanikio. Wengine hata walikuwa wabunge. Uchumi huko Uingereza ulikuwa umezorota sana, hasa kwa sababu ya vile Vita vya Miaka 30 huko Ulaya (1618-1648). Kwa hiyo, bila kujua hali itakuwaje, waliamua kuacha makao yao, biashara zao, na watu wao wa ukoo na kusafiri ili kutafuta maisha bora.

      Hata hivyo, watu hao wenye kusudi hawakuwa wafanyabiashara wenye pupa. Walikuwa Wapuriti wenye bidii waliokuwa wakikimbia kwa sababu ya mateso ya kidini.a Kusudi lao hasa lilikuwa kuanzisha jamii inayomwogopa Mungu mahali ambapo wao na watu wao wa ukoo wangeweza kupata mali bila kuvunja kanuni za Biblia. Muda mfupi baada ya kufika Salem, huko Massachusetts, walipata shamba dogo karibu na pwani. Wakayaita makao yao mapya Boston.

      Ugumu wa Kutafuta Pesa na Kudumisha Maadili

      Kiongozi na gavana wao, John Winthrop, aliwahimiza watu wawe na mali za kibinafsi na kufaidi jamii katika koloni hiyo mpya. Alitaka watu wawe na pesa na maadili. Lakini ilikuwa vigumu kusawazisha mambo hayo mawili. Kwa sababu alitazamia matatizo, alizungumza na wenzake kirefu kuhusu umuhimu wa kuwa na mali katika jamii inayomwogopa Mungu.

      Kama viongozi wengine Wapuriti, Winthrop aliamini kwamba hakuna kosa kufuatia mali. Alisema kwamba kusudi la mali ni kuwasaidia wengine. Hivyo, kadiri ambavyo mtu ni tajiri, ndivyo anavyoweza kufanya mengi zaidi. Mwanahistoria, Patricia O’Toole, anasema: “Wapuriti walichukia kuzungumza kuhusu utajiri. Waliuona kuwa baraka kutoka kwa Mungu na pia kishawishi kikubwa cha kiburi . . . na dhambi nyingine za mwili.”

      Ili kuepuka dhambi inayoweza kusababishwa na utajiri na starehe, Winthrop aliwasihi watu wawe na sifa ya kiasi na ya kujizuia. Hata hivyo, punde si punde, raia wenzake walikuza roho ya ubinafsi na hilo likahitilafiana na jitihada zake za kuwalazimisha wampende Mungu na wapendane. Wapinzani walianza kumpinga Winthrop kwa kuwa waliona kwamba anaingilia shughuli zao za kibinafsi. Baadhi yao walianza kuwachochea watu wakubali kuanzishwa kwa bunge lenye washirika wanaochaguliwa kwa kura ambao wangehusika katika kufanya maamuzi. Wengine wao walihamia jimbo jirani la Connecticut ili kufuatia mapendezi yao.

      O’Toole anasema: “Kazi nzuri, ufanisi, na demokrasia, yalikuwa mambo muhimu katika maisha ya Wapuriti wa Massachusetts, na yaelekea yote yaliwachochea watu kuwa na mapendezi ya kibinafsi badala ya lile wazo la Winthrop la kutumia utajiri ili kuwafaidi wengine.” Mnamo mwaka wa 1649, Winthrop alikufa maskini akiwa na umri wa miaka 61. Ingawa jamii hiyo iliendelea licha ya matatizo mengi, Winthrop alikufa bila kuona mabadiliko yoyote.

      Jitihada Zaendelea

      Mbali na John Winthrop, kuna watu wengine ambao wametamani maisha bora. Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu hutoka Afrika, Asia Kusini-Mashariki, Ulaya Mashariki, Amerika ya Latini, wakitazamia kupata maisha bora. Baadhi yao huchochewa na mamia ya vitabu vipya, semina, na vituo vya Intaneti vinavyotolewa kila mwaka, ambavyo vinaahidi kuwajulisha watu siri ya kutajirika. Ni wazi kwamba bado watu wengi wanajitahidi kupata pesa huku wakitumaini kwamba hawataacha kufuata maadili.

      Kwa kweli, matokeo yamekuwa yenye kusikitisha. Wale wanaojitahidi kuwa matajiri, mara nyingi huacha kufuata kanuni zao na nyakati nyingine hata imani yao. Kwa hiyo, huenda ukajiuliza: “Je, mtu anaweza kuwa Mkristo wa kweli na wakati uleule awe tajiri? Je, kuna wakati ambapo kutakuwa na jamii iliyo na ufanisi wa kimwili na wa kiroho?” Kama makala inayofuata inavyoonyesha, Biblia inajibu maswali hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika karne ya 16, Waprotestanti wa Kanisa la Anglikana waliotaka kuondolea mbali uvutano wote wa Kanisa Katoliki katika kanisa lao, waliitwa Wapuriti.

  • Maisha Yenye Kuridhisha Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Februari 1
    • Maisha Yenye Kuridhisha Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu

      DAVID,a mume Mkristo ambaye pia ni baba, alihamia Marekani, akiwa na uhakika kwamba alikuwa amefanya uamuzi unaofaa. Ingawa hakufurahia kuacha mke na watoto wake, alikuwa na uhakika kwamba angeboresha maisha yao ikiwa angepata pesa zaidi. Hivyo, alikubali mwaliko wa watu wa ukoo huko New York na punde si punde akapata kazi huko.

      Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, David alianza kukata tamaa. Hakuwa na wakati wa kutosha kwa ajili ya mambo ya kiroho. Hata wakati fulani karibu aache kumwamini Mungu. Aligundua uhalisi wa mambo alipoanguka katika kishawishi. Hatua kwa hatua, kufuatia utajiri wa kimwili kukamfanya aanze kupuuza vitu vyote vilivyokuwa muhimu kwake. Alihitaji kufanya mabadiliko.

      Kama David, watu wengi huhama nchi maskini kila mwaka wakitumaini kuboresha hali yao ya kiuchumi. Hata hivyo, mara nyingi hali yao ya kiroho huzorota. Baadhi yao wamejiuliza, ‘Je, Mkristo anaweza kufuatia utajiri wa kimwili na wakati uleule awe tajiri kumwelekea Mungu?’ Waandishi na viongozi wa kidini wanaojulikana sana husema kwamba inawezekana. Lakini David na wengine wametambua kwamba si rahisi kuwa na mali na wakati uleule kudumisha maadili.—Luka 18:24.

      Pesa Si Mbaya

      Pesa zimebuniwa na wanadamu. Kama vitu vingine vingi ambavyo vimebuniwa, pesa zenyewe si mbaya. Zinatumiwa kununua vitu. Hivyo, zikitumiwa vizuri, zinaweza kutimiza kusudi zuri. Kwa mfano, Biblia inakubali kwamba “pesa ni ulinzi,” hasa dhidi ya matatizo yanayohusiana na umaskini. (Mhubiri 7:12) Hata hivyo, inaonekana kwa wengine “pesa ndizo hutokeza jibu katika mambo yote.”—Mhubiri 10:19.

      Maandiko hushutumu ulegevu na hupendekeza kufanya kazi kwa bidii. Tunapaswa kuandalia familia zetu, na tukiwa na vitu vya ziada, tunakuwa na “kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Waefeso 4:28; 1 Timotheo 5:8) Isitoshe, badala ya kupendekeza kuishi maisha ya kujinyima, Biblia inatutia moyo tufurahie vitu tulivyo navyo. Inatuambia ‘tuchukue fungu letu’ na kushangilia katika kazi yetu ngumu. (Mhubiri 5:18-20) Katika Biblia kuna mifano kadhaa ya wanaume na wanawake waaminifu waliokuwa matajiri.

      Wanaume Waaminifu Waliokuwa Matajiri

      Abrahamu, mtumishi mwaminifu wa Mungu alijipatia kondoo na mifugo wengi, fedha na dhahabu nyingi, na mamia ya watumishi wa nyumbani. (Mwanzo 12:5; 13:2, 6, 7) Pia yule mtu mwadilifu Ayubu alikuwa na mali nyingi kutia ndani, mifugo, watumishi, dhahabu, na fedha. (Ayubu 1:3; 42:11, 12) Wanaume hao walikuwa matajiri hata kulingana na viwango vya kisasa, lakini pia walikuwa matajiri kumwelekea Mungu.

      Mtume Paulo anamwita Abrahamu, “baba ya wale wote walio na imani.” Abrahamu hakuwa mchoyo wala hakupenda sana mali zake. (Waroma 4:11; Mwanzo 13:9; 18:1-8) Pia, Mungu mwenyewe alimtaja Ayubu kuwa “mtu asiye na lawama na mnyoofu.” (Ayubu 1:8) Sikuzote alikuwa tayari kuwasaidia maskini na wenye kuteseka. (Ayubu 29:12-16) Abrahamu na Ayubu walimtegemea Mungu wala si mali zao.—Mwanzo 14:22-24; Ayubu 1:21, 22; Waroma 4:9-12.

      Mfano mwingine ni wa Mfalme Sulemani. Akiwa mrithi wa kiti cha Mungu huko Yerusalemu, Sulemani alipewa hekima kutoka kwa Mungu na pia utukufu na mali nyingi. (1 Wafalme 3:4-14) Alikuwa mwaminifu katika sehemu kubwa ya maisha yake. Hata hivyo, baadaye “moyo [wa Sulemani] haukuwa mkamilifu kwa Yehova.” (1 Wafalme 11:1-8) Mambo yaliyompata yanaonyesha hatari za kuwa na utajiri wa kimwili. Fikiria baadhi ya hatari hizo.

      Hatari za Utajiri

      Hatari kubwa zaidi ni ile ya kupenda pesa kupita kiasi na kupenda kile ambacho pesa zinaweza kununua. Kwa watu wengine, utajiri hukuza tamaa isiyoweza kutoshelezwa. Mwanzoni, Sulemani alikuwa ameona kwamba wengine wana mwelekeo huo. Aliandika hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.” (Mhubiri 5:10) Baadaye, Yesu, na pia Paulo, walionya Wakristo kuhusu upendo huo wenye hila.—Marko 4:18, 19; 2 Timotheo 3:2.

      Tukipenda pesa sana badala ya kuziona kuwa njia ya kutimiza mambo, itakuwa rahisi kuanguka katika vishawishi vya kila aina, kutia ndani udanganyifu, wizi, na hila. Yuda Iskariote, ambaye alikuwa mmoja wa mitume wa Kristo, alimsaliti bwana wake kwa vipande 30 tu vya fedha. (Marko 14:11; Yohana 12:6) Wengine wamependa pesa sana hivi kwamba wanaziabudu badala ya kumwabudu Mungu. (1 Timotheo 6:10) Hivyo, sikuzote Wakristo wanapaswa kujitahidi kuwa wanyoofu kuhusu kusudi lao la kutafuta pesa.—Waebrania 13:5.

      Pia, kufuatia mali huleta hatari zisizoonekana wazi. Kwanza, wingi wa mali humchochea mtu kujitegemea. Yesu alizungumzia jambo hilo aliposema kuhusu “nguvu za udanganyifu wa utajiri.” (Mathayo 13:22) Pia, Yakobo, mwandikaji wa Biblia, aliwaonya Wakristo wasimsahau Mungu hata wanapofanya mipango ya biashara. (Yakobo 4:13-16) Kwa kuwa pesa zinaweza kutupa kiasi fulani cha uhuru, wale walio nazo wanakabili hatari ya kuzitegemea badala ya kumtegemea Mungu.—Methali 30:7-9; Matendo 8:18-24.

      Pili, kama David aliyetajwa mwanzoni alivyogundua, mara nyingi kufuatia utajiri huchukua wakati mwingi na nguvu nyingi za mtu hivi kwamba pole kwa pole anaacha kufuatia mambo ya kiroho. (Luka 12:13-21) Pia kwa matajiri, kuna kishawishi cha kutaka kutumia vitu walivyo navyo hasa kwa kufuatia anasa au mambo ya kibinafsi.

      Je, inawezekana kwamba Sulemani alidhoofika kiroho kwa sababu ya kulemewa na starehe za maisha? (Luka 21:34) Alijua kwamba Mungu alikuwa amekataza mapatano ya ndoa na mataifa mengine. Hata hivyo, alijipatia wanawake elfu moja hivi. (Kumbukumbu la Torati 7:3) Ili kuwafurahisha wake zake, alijaribu kuchanganya imani. Kama ilivyotangulia kutajwa, hatua kwa hatua, moyo wa Sulemani uligeuka ukaacha kumfuata Yehova.

      Ni wazi kwamba mifano hiyo inathibitisha ukweli wa shauri hili la Yesu: “Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24) Basi, Mkristo anaweza kushughulikiaje matatizo ya kiuchumi yanayowakumba watu wengi leo? Swali muhimu hata zaidi ni, je, kuna tumaini lolote la kuwa na maisha bora wakati ujao?

      Maisha Yenye Kuridhisha Yatakuwapo Hivi Karibuni

      Tofauti na wazee wa ukoo kama vile Abrahamu, Ayubu, na taifa la Israeli, wafuasi wa Yesu wana utume wa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19, 20) Ili kutimiza utume huo, wakati na jitihada ambazo huenda zingetumiwa katika kufuatia mambo ya kimwili, zinahitajiwa. Hivyo, ili tufanikiwe, ni lazima tufanye kama Yesu alivyotuambia: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme [wa Mungu] na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:33.

      David alikuwa karibu kupoteza familia yake, imani yake, na uhusiano wake pamoja na Mungu. Hata hivyo, alirekebisha maisha yake. Kama Yesu alivyoahidi, David alipoanza tena kutanguliza kujifunza Biblia, kusali, na kuhubiri, mambo mengine yakawa shwari. Hatua kwa hatua, uhusiano wake pamoja na mke na watoto wake uliboreka. Akapata tena shangwe na uradhi. Bado anafanya kazi kwa bidii. Ingawa hakupata utajiri, kisa chake chenye kuhuzunisha kilimfunza mambo muhimu.

      David ametambua kwamba halikuwa jambo la hekima kuhamia Marekani, naye ameazimia kutoruhusu tena pesa ziongoze maamuzi yake. Sasa anajua kwamba vitu vyenye thamani zaidi maishani, yaani, familia yenye upendo, rafiki wazuri, na uhusiano pamoja na Mungu, haviwezi kununuliwa kwa pesa. (Methali 17:17; 24:27; Isaya 55:1, 2) Bila shaka, kufuatia maadili ni jambo lenye thamani sana kuliko utajiri. (Methali 19:1; 22:1) David na familia yake wameazimia kutanguliza mambo yaliyo ya maana zaidi.—Wafilipi 1:10.

      Mara nyingi jitihada za wanadamu za kuwa na jamii yenye ufanisi na iliyo na maadili hazifanikiwi. Hata hivyo, Mungu ameahidi kwamba Ufalme wake utaleta vitu vingi vya kimwili na vya kiroho ambavyo tunahitaji ili tuwe na maisha yenye kuridhisha. (Zaburi 72:16; Isaya 65:21-23) Yesu alifundisha kwamba ili tuwe na ufanisi wa kweli, ni lazima kwanza tutambue uhitaji wetu wa kiroho. (Mathayo 5:3) Hivyo, tuwe matajiri au maskini, kutanguliza mambo ya kiroho sasa ndiyo njia bora ya kila mmoja wetu kujitayarisha kwa ajili ya ulimwengu mpya wa Mungu ulio karibu. (1 Timotheo 6:17-19) Bila shaka, huo utakuwa ulimwengu wenye ufanisi wa kimwili na wa kiroho.

      [Maelezo ya Chini]

      a Jina limebadilishwa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki