-
“Uhalifu wa Kikatili”Amkeni!—2003 | Februari 8
-
-
“Uhalifu wa Kikatili”
MARIAa alianza kufanya ukahaba akiwa mtoto mwenye umri wa miaka 14. Mama yake ndiye aliyemlazimisha kuishi maisha haya yenye kuchukiza sana. Alimwambia kwamba wanaume wangevutiwa sana na urembo wake, na angepata pesa nyingi. Wakati wa jioni, Maria alipelekwa na mamaye kwenye hoteli moja yenye vyumba vya kulala ambako walikutana na wanaume. Kila usiku, Maria alifanya ngono na wanaume watatu au wanne ambao walimlipa mamaye aliyekuwa karibu.
Carina mwenye umri wa miaka 13, anayeishi karibu na Maria, alilazimishwa pia kuwa kahaba. Kama wazazi wengine wengi waliokuza miwa katika eneo lao, wazazi wa Carina walimwingiza katika kazi ya ukahaba ili awaletee pesa zaidi za matumizi. Kwingineko, Estela aliacha shule akiwa mtoto mdogo asiyejua kusoma wala kuandika, akaanza kufanya kazi ya ukahaba mitaani. Naye Daisy alikuwa na umri wa miaka sita hivi alipobakwa na nduguye—tangu hapo alibakwa mara nyingi. Alianza ukahaba akiwa na umri wa miaka 14.
Katika sehemu nyingi ulimwenguni, tatizo la watoto makahaba limeenea kwa njia yenye kutisha sana. Matokeo yanasikitisha. Mara nyingi watoto wanaofanya ukahaba kwa ukawaida au pindi fulani-fulani, hufanya pia uhalifu na kutumia dawa za kulevya. Wengi wao hukata tamaa na kujihisi hawafai wanapoona kwamba hakuna tumaini la kuacha maisha hayo yenye taabu.
Watu mashuhuri wanatambua matokeo mabaya sana ya ukahaba wa watoto. Aliyekuwa rais wa Brazili Fernando Henrique Cardoso alisema hivi waziwazi: “Ukahaba wa watoto ni uhalifu wa kikatili.” Maelezo haya mazito kuhusu ukahaba wa watoto yalichapishwa katika gazeti moja la Brazili: “Nchi ambazo zimekubali ukahaba kuwa jambo la kawaida, na ambazo zinauendeleza kwa sababu ya [pesa], zinakabili matokeo mabaya ya zoea hilo kila siku. Faida yoyote ya kifedha ambayo huenda ikapatikana haiwezi kamwe kulinganishwa na misiba inayompata mtu binafsi, familia na jamii kutokana na zoea hilo.”
Hata hivyo, ukahaba wa watoto unaenea licha ya kwamba watu fulani wanajitahidi sana kukomesha tatizo hilo. Ni nini kinachosababisha hali hiyo yenye kusikitisha? Kwa nini watu wengi hukubali au hata kuendeleza uhalifu huo?
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa katika mfululizo huu wa makala.
[Blabu katika ukurasa wa 3]
“Ukahaba wa watoto ni uhalifu wa kikatili.”—ALIYEKUWA RAIS WA BRAZILI FERNANDO HENRIQUE CARDOSO
[Blabu katika ukurasa wa 4]
“Matendo yote ya kuwatumia watu wengine vibaya kingono yanavunja heshima ya binadamu, na hivyo yanakiuka haki za msingi za binadamu, haidhuru umri, jinsia, jamii, kabila au tabaka la mtu anayetendewa hivyo.”—UNESCO SOURCES
-
-
Kwa Nini Tatizo Hilo Linaenea?Amkeni!—2003 | Februari 8
-
-
Kwa Nini Tatizo Hilo Linaenea?
JE, WAJUA kwamba biashara haramu ya kuwauza wanadamu ni uhalifu wa tatu kwa ukubwa ulimwenguni, baada ya ulanguzi wa dawa za kulevya na uuzaji wa silaha? Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa linasema kwamba kuna ukahaba wa kila aina unaoongezeka kwa kasi sana.
Katika nchi moja ya Amerika ya Latini, Tume Maalumu ya Uchunguzi iliripoti kwamba kuna zaidi ya wasichana wadogo makahaba 500,000, licha ya kwamba ukahaba si halali.
Katika nchi nyingine, kuna watoto makahaba 300,000 hivi mitaani, hasa katika maeneo yenye ulanguzi wa dawa za kulevya.
Imeripotiwa kwamba wasichana wapatao milioni moja katika nchi za Asia hutumiwa kama makahaba na kutendewa kama watumwa. Nchi nyingine ni vituo vikuu vya ngono na ukahaba wa watoto.
Kwa sababu ya kuenea sana kwa magonjwa yanayoambukizwa kingono, kama vile UKIMWI, wateja huwa tayari kulipa pesa nyingi zaidi ili wafanye ngono na watoto ambao wanadhaniwa kuwa mabikira na ambao huenda hawajaambukizwa. “Tatizo hilo linazidi kuongezeka kwa sababu hofu ya UKIMWI inawafanya wanaume watafute wasichana na wavulana wenye umri mdogo zaidi,” aeleza Luíza Nagib Eluf wa Wizara ya Sheria nchini Brazili. Alisema: “Kuwatumia wasichana na wavulana wadogo vibaya kingono ni tatizo kubwa sana la kijamii linalowakabili wanawake maskini nchini Brazili.”
Umaskini na Ukahaba wa Watoto
Ukahaba wa watoto husitawi katika maeneo yenye umaskini na taabu. Afisa mmoja wa serikali alisema kwamba ukahaba na utumwa wa watoto nchini mwao “unahusiana moja kwa moja na kuvunjika kwa familia na kunasababishwa na taabu na njaa.” Wazazi fulani wanadai kwamba waliwauza watoto wao kuwa makahaba kwa sababu ya umaskini. Watoto wa mitaani hufanya ukahaba kwa sababu wanaona ndiyo njia pekee ya kujiruzuku.
Gazeti la O Estado de S. Paulo linaeleza kwamba msichana anayeshirikiana na genge la mitaani huenda mwishowe akawa kahaba. Huenda akalazimika kuiba na kufanya ukahaba mara kwa mara ili apate chakula. Hatimaye anakuwa kahaba kabisa.
Nyakati nyingine vijana hupelekwa nchi nyingine kufanya kazi ya ukahaba. “Mara nyingi makahaba wahamiaji hutuma pesa nyingi kwa familia zao ambazo zinaishi katika nchi maskini sana za Asia na Afrika,” charipoti kichapo UNESCO Sources. “Nchi hizo zinaendeleza ukahaba kwa sababu watalii kutoka nchi tajiri huja tu kufanya ngono na vijana na watoto makahaba.”
Gazeti la Time linaripoti hivi kuhusu hatari zinazowakabili watoto wa mitaani walio makahaba katika jiji moja la Amerika ya Latini: “Baadhi ya makahaba hao wana umri wa miaka 12 tu. Kwa kawaida watoto hao wanaotoka kwenye familia zilizovunjika, hulala mahali popote wakati wa mchana, na kurandaranda kwenye madisko usiku wakitafuta mabaharia wa kufanya ngono nao.”
Msichana mdogo kahaba aliyelewa dawa za kulevya hutendewa unyama ambao kwa kawaida hangekubali kamwe. Kwa mfano, gazeti la Veja linasema kwamba polisi waligundua kaseti 92 za video zilizorekodiwa na daktari mmoja, zinazoonyesha zaidi ya wanawake 50 wakiteswa kinyama baadhi yao wakiwa wasichana wadogo.
Licha ya matukio hayo yenye kushtua, kijana mmoja kahaba alisema: “Siwezi kamwe kupata kazi yoyote ya kuajiriwa inayoweza kutosheleza mahitaji yangu kwa sababu sina ujuzi wowote wa kazi. Familia yangu inajua kazi ninayofanya, na sitaki kuacha maisha haya. Mwili ni wangu, nami nautumia kama nipendavyo.”
Hata hivyo, wasichana hawa hawakukusudia kamwe kuwa makahaba. Mfanyakazi mmoja wa huduma za jamii anasema kwamba makahaba wengi watoto “wangependa kuolewa” na wanatamani kupata mchumba anayewafaa kabisa. Ingawa kuna hali ngumu zilizowaingiza katika maisha ya ukahaba, mchunguzi mmoja anadai hivi: “Jambo lenye kusikitisha zaidi ni kwamba wengi wao walibakwa wakiwa nyumbani kwao.”
Je, Ukahaba wa Watoto Utakoma?
Hata hivyo, kuna tumaini kwa watoto hao wanaoteseka. Kuna makahaba wenye umri mbalimbali ambao wameacha maisha hayo. (Ona sanduku “Watu Wanaweza Kubadilika,” kwenye ukurasa wa 7.) Neno la Mungu, Biblia, limesaidia mamilioni ya watu kotekote ulimwenguni kuwa majirani wema na washiriki waaminifu wa familia. Twasoma hivi kuhusu watu ambao hapo awali walikuwa waasherati, wazinzi, wezi, wenye pupa, na walevi: “Baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa. Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.
Leo, kama ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, kuna watu ambao wanabadili maisha yao na kuwa watu wazuri. Hata hivyo, jitihada zinahitajiwa ili kukomesha tabia ya kuwatumia wengine kingono. Serikali na mashirika fulani yanajitahidi kukomesha watalii wanaofanya ukahaba na ukahaba wa watoto. Lakini kwa kweli, wanadamu hawawezi kukomesha taabu na umaskini. Watungaji wa sheria hawawezi kuzuia mawazo na mielekeo inayosababisha ukosefu wa maadili.
Ufalme wa Mungu ndio utakaotatua matatizo hayo yote wala si jitihada za wanadamu. Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Mara nyingi umaskini huchangia ukahaba wa watoto
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Matokeo Mabaya Sana
Daisy alikuwa na umri wa miaka sita tu alipobakwa na ndugu yake. Kwa sababu hiyo, akaishi na kaka yake hadi alipofikia umri wa miaka 14, kisha akaanza kufanya kazi kwenye klabu ya usiku. Baada ya siku chache, Daisy akawa mgonjwa. Alipopata nafuu, wasimamizi wa klabu hiyo walimwambia alipe pesa walizomdai, hivyo akaamua kuwa kahaba. Mwaka mmoja hivi baadaye, hakuwa amelipa deni hilo, na ilionekana kwamba hangeweza kamwe kukamilisha deni hilo. Hata hivyo, baharia mmoja alimlipia deni lililobaki, na kumpeleka hadi jiji jingine ambako alitendewa kama mtumwa. Daisy alimwacha mwanamume huyo na baadaye akaishi na mwanamume mwingine kwa miaka mitatu halafu wakafunga ndoa. Alijaribu kujiua mara tatu kwa sababu ya matatizo mengi mazito katika ndoa yao.
Hatimaye, yeye na mumewe wakaanza kujifunza Biblia. Lakini Daisy alijiona hafai kuwa Shahidi wa Yehova. Alipoonyeshwa kwenye Biblia kwamba Yehova Mungu anakubali watu wanaofanya mabadiliko yanayofaa, alijiweka wakfu kwake. Daisy alijitahidi sana kufanya mambo yanayofaa, lakini alihisi kwamba hayatoshi na hivyo alishuka moyo pindi kwa pindi. Ingawa hivyo inatia moyo kwamba amekubali kusaidiwa ili awe na usawaziko na kushinda hisia za majuto zinazomsumbua kwa sababu ya kubakwa na maisha yake ya ukahaba alipokuwa mtoto.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Watu Wanaweza Kubadilika
Yesu Kristo alipokuwa duniani, aliwahurumia watu wenye dhambi, waliotaabika. Alijua kwamba makahaba wangeweza kubadilika haidhuru umri wao. Yesu hata aliwaambia hivi viongozi wa kidini: “Kwa kweli nawaambia nyinyi kwamba wakusanya-kodi na makahaba wanaenda mbele yenu kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mathayo 21:31) Ijapokuwa watu hao wenye mioyo inayofaa walidharauliwa kwa sababu ya namna yao ya maisha, walisamehewa walipotia imani katika Mwana wa Mungu. Watenda-dhambi wenye kutubu walikuwa tayari kuacha maisha yao ya ukahaba ili wapokee baraka za Ufalme wa Mungu. Kisha, waliishi kupatana na kanuni za Mungu za uadilifu. Leo pia, watu wa kila namna wanakubali kweli ya Neno la Mungu halafu wanabadili maisha yao.
Fikiria mambo yaliyompata Maria, Carina, na Estela, waliotajwa kwenye makala ya kwanza. Mbali na kukinza shinikizo la mama yake la kumtaka aendelee kufanya ukahaba, Maria alijikakamua sana kuacha kutumia dawa za kulevya. Anasema hivi: “Nilitumia dawa za kulevya ili nitulize hisia za kujiona sifai kwa sababu ya kuishi maisha ya ukahaba.” Maria anaeleza jinsi alivyokaribishwa na kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova: “Nilivutiwa na upendo ambao nilionyeshwa na washiriki wa kutaniko. Wote—watoto kwa watu wazima—walinitendea kwa heshima. Niliona kwamba waume ni waaminifu kwa wake zao. Nimefurahi sana kukubaliwa kama rafiki yao.”
Alipokuwa na umri wa miaka 17, Carina alitembelewa na Mashahidi wa Yehova. Alianza kujifunza Biblia, ingawa aliendelea na kazi yake ya ukahaba kwa muda fulani. Hatua kwa hatua, alianza kuthamini kweli za Biblia. Akaamua kuhamia mji mmoja wa mbali, na huko akawa Shahidi wa Yehova.
Estela, ambaye alikuwa kahaba na mlevi wa kupindukia alipokuwa mtoto, alianza kupendezwa na Biblia. Hata hivyo, alikata shauri kwamba Mungu hawezi kamwe kumsamehe. Lakini, punde si punde, alifahamu kwamba Yehova Mungu huwasamehe watu wanaotubu. Sasa Estela akiwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo aliyefunga ndoa na mama mwenye watoto watatu, anasema hivi: “Nina furaha na ninamshukuru sana Yehova kwa sababu aliniokoa kutoka kwenye maisha hayo machafu na amenikaribisha katika tengenezo lake safi.”
Masimulizi hayo yanaunga mkono maneno ya Biblia ya kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mara nyingi watoto makahaba hutumia dawa za kulevya
[Picha katika ukurasa wa 5]
© Jan Banning/Panos Pictures, 1997
-
-
Kuwatumia Watoto Vibaya Kutakoma Hivi Karibuni!Amkeni!—2003 | Februari 8
-
-
Kuwatumia Watoto Vibaya Kutakoma Hivi Karibuni!
“KATIKA Azimio la Watu Wote la Haki za Binadamu, Umoja wa Mataifa ulitangaza kwamba watoto wana haki ya kutunzwa vyema na kusaidiwa,” ndivyo unavyosema utangulizi wa Mkataba wa Haki za Mtoto. Utangulizi huo unasema hivi pia kuhusu umuhimu wa familia: “Mtoto anahitaji kukua katika mazingira ya kifamilia yenye furaha, upendo, na amani ili utu wake usitawi kikamilifu na kwa njia inayofaa.” Hata hivyo, kusudi hilo halijatimizwa.
Haitoshi tu kuzungumza kuhusu ulimwengu bora unaowafaa watoto. Maadili yanazidi kuzorota, na watu wengi wanaliona kuwa jambo la kawaida. Utekelezaji wa sheria hauwezi kudhibiti pupa na ukosefu wa maadili ulioenea kotekote. Mara nyingi wazazi huendeleza mambo maovu badala ya kuwapenda na kuwalinda watoto wao. Basi kwa nini tutarajie kwamba ukahaba wa watoto utakoma?
Ijapokuwa ulimwengu huu mwovu umeshindwa kuhakikisha kwamba watoto wote wanaonyeshwa upendo nyumbani na wana wakati ujao salama, hivi karibuni Muumba wetu atakomesha kila namna ya uovu na ukosefu wa maadili kingono, kutia ndani ukahaba wa watoto. Karibuni, Yehova Mungu ataushangaza ulimwengu kwa kuingilia mambo ya wanadamu akitumia Ufalme wake. Mungu atawahukumu watu wote wanaowatumia wengine vibaya na kuwashawishi kutenda maovu. Wale tu wanaowapenda wanadamu wenzao ndio watakaookoka na kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:21, 22.
Hebu wazia furaha itakayokuwapo wakati watoto na watu wazima watakapoishi bila kuvunjiwa heshima na kutumiwa vibaya kingono! Hata madhara ya kihisia-moyo na ya kimwili yanayotokana na kutumiwa vibaya na kutendewa jeuri yatatokomea kabisa. Wale waliotendewa vibaya kingono wataweza kuishi bila kumbukumbu mbaya au madhara ya mambo yaliyowapata. “Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17.
Wakati huo, hakuna mtoto atakayeteswa au kutumiwa vibaya kingono. Mambo kama vile furaha, upendo, na hali ya kuelewana hayatakuwa ndoto tu. Andiko la Isaya 11:9 linatangaza hivi kuhusu wenyeji wa ulimwengu mpya wa Mungu: “Hawatadhuru wala hawataharibu.”
Kwa kweli, kutakuwa na shangwe iliyoje wakati umaskini, matumizi ya dawa za kulevya, familia zenye huzuni, na maadili maovu yatakuwa yametoweka kabisa! Kutakuwa na amani, uadilifu, na usalama kotekote. “Watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.”—Isaya 32:18.
-
-
Kuwatumia Watoto Vibaya Kutakoma Hivi Karibuni!Amkeni!—2003 | Februari 8
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
Kuwatunza Watoto Kunaweza Kuzuia Familia Isivunjike
● “Wazazi wangu walinitia moyo kusoma kwa bidii shuleni na kujifunza ustadi fulani. Hawakujaribu kunilazimisha nifuate mapendezi yao, lakini walinisaidia kuchagua shule zilizokuwa na mitaala niliyotaka.”—Tais.
● “Mimi na dada yangu tuliandamana na mama yetu tulipoenda kununua bidhaa. Mbali na kutusaidia kutumia pesa vizuri, alitusaidia pia kutonunua mavazi yasiyo ya kiasi au yanayoonyesha uchi.”—Bianca.
● “Tulipoenda kwenye karamu, sikuzote wazazi wangu waliniuliza ni nani wangehudhuria, ni muziki wa aina gani ungechezwa, na wakati ambapo karamu ingeanza na kumalizika. Tulihudhuria karamu nyingi pamoja tukiwa familia.”—Priscila.
● “Nilipokuwa mtoto mchanga na tineja, nilizungumza kwa uhuru sana na wazazi wangu. Mwanashule mwenzangu aligundua jambo hilo akasema hivi: ‘Ninavutiwa sana kuona ukizungumza jambo lolote kwa uhuru na wazazi wako. Mimi hata sijihisi huru kuzungumza na mama yangu, kwa kawaida mimi huwauliza watu wengine mambo nisiyojua.’”—Samara.
● “Nilifurahia miaka yangu ya utineja. Niliwatumaini watu na niliangua kicheko daima. Nilistarehe sana nikiwa na rafiki zangu na tulipiga gumzo pamoja. Wazazi wangu walijua kwamba huo ni utu wangu, na hawakujaribu kunilazimisha kubadili utu wangu. Lakini kwa fadhili walinisaidia kutambua kwamba nilihitaji kuwa mwangalifu na kujiendesha kwa adabu nikiwa na watu wa jinsia tofauti.”—Tais.
● “Kama vijana wengine wengi, nilipendezwa mno na watu wa jinsia tofauti. Baba yangu aliniwekea umri ambao ningeweza kuanza kutafuta mchumba. Badala ya kuudhika, nilitambua kwamba wazazi wangu walinijali na walitaka kunilinda nisiumie wakati ujao.”—Bianca.
● “Niliona ndoa kuwa kifungo kizuri sana, hasa kwa sababu ya mfano mzuri wa wazazi wangu. Daima walikuwa na uhusiano mzuri na walidumisha mawasiliano mazuri. Ninakumbuka wakati nilipokuwa nikichumbiwa, mama yangu alinipa mashauri kuhusu jinsi ya kutenda katika hali fulani na alinieleza jinsi ambavyo jambo hilo lingeathiri ndoa yangu.”—Priscila.
-