Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Na Tulikweze Jina la Yehova Pamoja
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Machi 1
    • Na Tulikweze Jina la Yehova Pamoja

      “Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.”—ZABURI 34:3.

      1. Yesu aliweka mfano gani mzuri wakati wa huduma yake duniani?

      USIKU wa Nisani 14, 33 W.K., Yesu na mitume wake waliimba sifa za Yehova pamoja katika chumba cha juu cha nyumba moja huko Yerusalemu. (Mathayo 26:30) Hiyo ilikuwa mara ya mwisho kwa Yesu kufanya hivyo akiwa pamoja na mitume wake. Hata hivyo, ilifaa kwake kumalizia mkutano huo kwa njia hiyo. Tangu mwanzo hadi mwisho wa huduma yake hapa duniani, Yesu alimsifu Baba yake na kulitangaza jina Lake kwa bidii. (Mathayo 4:10; 6:9; 22:37, 38; Yohana 12:28; 17:6) Kwa kufanya hivyo, alitoa mwaliko huu mchangamfu wa mtunga-zaburi: “Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.” (Zaburi 34:3) Alituwekea mfano mzuri kama nini wa kufuata!

      2, 3. (a) Tunajua jinsi gani kwamba Zaburi ya 34 ina umuhimu wa kinabii? (b) Tutazungumzia nini katika habari hii na ile inayofuata?

      2 Saa chache baada ya kuimba sifa pamoja na Yesu, mtume Yohana alishuhudia tukio lingine tofauti kabisa. Aliona Bwana wake na wahalifu wawili wakiuawa juu ya miti ya mateso. Askari-jeshi wa Roma walivunja miguu ya wale wahalifu wawili ili wafe haraka. Hata hivyo, Yohana anaripoti kwamba hawakuvunja miguu ya Yesu. Askari-jeshi hao walipomfikia Yesu, alikuwa tayari amekufa. Katika Injili yake, Yohana alitaja kwamba tukio hilo lilitimiza sehemu nyingine ya Zaburi ya 34: “Hakuna hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa.”—Yohana 19:32-36; Zaburi 34:20, Biblia Habari Njema.

      3 Zaburi ya 34 ina mambo mengine mengi yanayowapendeza Wakristo. Hivyo, katika habari hii na ile inayofuata, tutazungumzia hali ambazo Daudi alikuwa akikabili alipoandika zaburi hii na kisha tutazungumzia mambo yenye kutia moyo yaliyo katika zaburi hiyo.

      Daudi Amkimbia Sauli

      4. (a) Kwa nini Daudi alitiwa mafuta awe mfalme wa Israeli ambaye angefuata? (b) Kwa nini Sauli ‘alimpenda sana’ Daudi?

      4 Daudi alipokuwa kijana, Sauli alikuwa mfalme wa Israeli. Hata hivyo, Sauli aliacha kutii naye akapoteza kibali cha Yehova. Kwa sababu hiyo, nabii Samweli alimwambia hivi: “Yehova ameurarua utawala wa kifalme wa Israeli kutoka kwako leo, naye hakika atampa mwenzako ambaye ni bora kuliko wewe.” (1 Samweli 15:28) Baadaye, Yehova alimwongoza Samweli amtie mafuta Daudi, mwana mdogo zaidi wa Yese, awe mfalme wa Israeli ambaye angefuata. Wakati huohuo, kwa sababu ya kuondolewa roho ya Mungu, Mfalme Sauli alisumbuka sana kihisia. Daudi, aliyekuwa mwanamuziki stadi, aliletwa Gibea ili amtumikie mfalme, na muziki wa Daudi ulimtuliza Sauli ambaye ‘alimpenda sana’ Daudi. —1 Samweli 16:11, 13, 21, 23.

      5. Kwa nini mtazamo wa Sauli kuelekea Daudi ulibadilika, na Daudi alilazimika kufanya nini?

      5 Kadiri wakati ulivyopita, Yehova aliendelea kuwa pamoja na Daudi. Yehova alimsaidia Daudi kumshinda Goliathi, lile jitu la Wafilisti, naye alimtegemeza na hivyo Daudi akaheshimiwa katika Israeli kwa ustadi wake wa kijeshi. Hata hivyo, kwa sababu Yehova alimbariki Daudi, Sauli alimwonea wivu, naye akamchukia Daudi. Mara mbili Daudi alipokuwa akipiga kinubi chake mbele za Sauli, mfalme huyo alimrushia Daudi mkuki. Mara zote mbili, Daudi alifaulu kuhepa mkuki. Sauli alipojaribu mara ya tatu kumuua Daudi, mfalme huyo wa Israeli ambaye angefuata alitambua kwamba anapaswa kukimbia ili kuokoa uhai wake. Mwishowe, kwa sababu Sauli aliendelea kumsaka ili amuue, Daudi alilazimika kukimbilia nje ya eneo la Israeli.—1 Samweli 18:11; 19:9, 10.

      6. Kwa nini Sauli aliagiza wakaaji wa Nobu wauawe?

      6 Alipokuwa akielekea kwenye mpaka wa Israeli, Daudi alisimama katika jiji la Nobu, ambako maskani ya Yehova yalikuwa. Inaelekea kwamba Daudi aliandamana na kikundi cha wanaume vijana alipokuwa akikimbia, naye alitafuta chakula kwa ajili yake na wenzake. Sauli alipata habari kwamba kuhani mkuu alikuwa amempa Daudi na wanaume wake chakula kidogo na ule upanga ambao Daudi alikuwa ameuchukua kutoka kwa Goliathi aliyeuawa. Kwa hasira, Sauli aliagiza kwamba wakaaji wote wa jiji hilo, kutia ndani makuhani 85, wauawe.—1 Samweli 21:1, 2; 22:12, 13, 18, 19; Mathayo 12:3, 4.

      Aponea Tena Chupuchupu

      7. Kwa nini Gathi hapakuwa mahali salama pa Daudi kujificha?

      7 Kutoka Nobu, Daudi alikimbia umbali wa kilomita 40 hivi upande wa magharibi na kuingia katika eneo la Wafilisti. Hatimaye, akafika kwa Akishi, mfalme wa Gathi, mji wa nyumbani kwa Goliathi. Labda Daudi alifikiri kwamba Sauli hangemtafuta huko Gathi. Hata hivyo, muda si muda, watumishi wa mfalme wa Gathi walimtambua Daudi. Daudi aliposikia kwamba alikuwa ametambuliwa, ‘aliogopa sana kwa sababu ya Akishi mfalme wa Gathi.’—1 Samweli 21:10-12.

      8. (a) Zaburi ya 56 inatuambia nini kuhusu yale yaliyompata Daudi huko Gathi? (b) Daudi aliponea chupuchupu jinsi gani?

      8 Kisha, Wafilisti wakamkamata Daudi. Huenda huo ndio wakati ambapo Daudi alitunga zaburi yenye kugusa moyo ambamo alimwomba Yehova hivi: “Uyaweke machozi yangu katika kiriba chako.” (Zaburi 56:8 na utangulizi) Hivyo, alionyesha uhakika wake kwamba Yehova hangesahau huzuni yake, lakini angemtunza kwa upendo na kumlinda. Daudi alifikiria njia ya kumpumbaza mfalme wa Wafilisti. Alijifanya mwenda-wazimu. Alipoona hivyo, Mfalme Akishi aliwakemea watumishi wake kwa kuleta “mwenda-wazimu” mbele yake. Kwa wazi, Yehova alibariki mbinu ya Daudi. Daudi aliondolewa jijini, na hivyo akaponea tena chupuchupu.—1 Samweli 21:13-15.

      9, 10. Kwa nini Daudi aliandika Zaburi ya 34, na huenda alikuwa akiwafikiria nani alipotunga zaburi hiyo?

      9 Biblia haisemi ikiwa wale waliomuunga Daudi mkono walikimbilia Gathi pamoja naye au walimlinda katika vijiji vya karibu vya Israeli. Vyovyote vile, lazima walifurahi sana kukutana kwa mara nyingine wakati Daudi alipowasimulia jinsi Yehova alivyomwokoa tena. Zaburi ya 34 inategemea kisa hicho kama utangulizi wake unavyoonyesha. Katika mistari saba ya kwanza ya zaburi hiyo, Daudi anamsifu Mungu kwa kumkomboa naye anawaalika watu wanaomuunga mkono wajiunge naye katika kumkweza Yehova kuwa Mwokoaji Mkuu wa watu Wake.—Zaburi 34:3, 4, 7.

      10 Daudi na wanaume wake walijificha katika pango la Adulamu kwenye eneo lenye milima la Israeli, karibu kilomita 15 mashariki ya Gathi. Wakiwa huko, Waisraeli ambao hawakuridhishwa na hali za maisha chini ya utawala wa Mfalme Sauli walianza kuja na kujiunga nao. (1 Samweli 22:1, 2) Daudi alipotunga maneno ya Zaburi 34:8-22, huenda alikuwa akiwafikiria watu hao. Vikumbusho vilivyo katika mistari hiyo ni muhimu pia kwetu leo, na bila shaka tutafaidika tukizungumzia kwa undani zaburi hiyo yenye kupendeza sana.

      Je, Hangaiko Lako Kuu Ni Kama la Daudi?

      11, 12. Tuna sababu gani za kumsifu Yehova daima?

      11 “Nitambariki Yehova nyakati zote; daima sifa yake itakuwa katika kinywa changu.” (Zaburi 34:1) Akiwa mkimbizi, lazima Daudi awe alikuwa na mahangaiko mengi ya kimwili. Lakini kama maneno hayo yanavyoonyesha, hakuacha mahangaiko yake ya kila siku yavunje azimio lake la kumsifu Yehova. Alituwekea mfano mzuri kama nini tunapokabili magumu! Iwe tuko shuleni, kazini, pamoja na Wakristo wenzetu, au katika huduma ya hadharani, tamaa yetu kuu ni kumsifu Yehova. Hebu fikiria sababu nyingi sana tulizo nazo za kufanya hivyo! Kwa mfano, hakuna mwisho wa yale tunayoweza kujifunza na kufurahia kutokana na kazi za ajabu za uumbaji za Yehova. Hebu fikiria yale ambayo ametimiza kupitia sehemu ya kidunia ya tengenezo lake! Ingawa si wakamilifu, Yehova amewatumia wanadamu waaminifu kutimiza mambo mengi sana katika nyakati za kisasa. Kazi za Mungu zinatofautiana jinsi gani na kazi za wanadamu ambao wanaabudiwa na ulimwengu? Je, hukubaliani na Daudi ambaye pia aliandika hivi: “Hakuna yeyote aliye kama wewe katikati ya miungu, Ee Yehova, wala hakuna kazi zozote kama zako.”—Zaburi 86:8.

      12 Kama Daudi, tunachochewa kumsifu Yehova daima kwa sababu ya kazi zake zisizo na kifani. Zaidi ya hilo, tunasisimka kujua kwamba Ufalme wa Mungu sasa uko mikononi mwa Mrithi wa kudumu wa Daudi, Yesu Kristo. (Ufunuo 11:15) Hilo linamaanisha kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu. Wakati ujao wa milele wa wanadamu zaidi ya bilioni sita uko hatarini. Hakujawahi kamwe kuwa na uhitaji mkubwa kama sasa wa kuwatangazia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na yale ambayo utawafanyia wanadamu hivi karibuni na kuwasaidia wamsifu Yehova pamoja nasi. Bila shaka, jambo kuu maishani mwetu linapaswa kuwa kutumia kila nafasi kuwatia wengine moyo wakubali “habari njema” kabla haijawa kuchelewa mno.—Mathayo 24:14.

      13. (a) Daudi alijisifu katika nani, na ni watu wa aina gani walioitikia? (b) Wapole wanavutwa kwenye kutaniko la Kikristo leo jinsi gani?

      13 “Nafsi yangu itajisifu katika Yehova; wapole watasikia na kushangilia.” (Zaburi 34:2) Daudi hakujisifu kwa yale ambayo alitimiza. Kwa mfano, hakujigamba kuhusu jinsi alivyompumbaza mfalme wa Gathi. Alitambua kwamba Yehova alimlinda alipokuwa huko Gathi na kwamba aliponyoka kwa sababu Yehova alimsaidia. (Methali 21:1) Hivyo, Daudi hakujisifu mwenyewe, lakini alijisifu katika Yehova. Kwa sababu hiyo, wapole walivutwa kwa Yehova. Yesu alitukuza vivyo hivyo jina la Yehova, na hilo liliwavuta watu wanyenyekevu na wenye kufundishika ili wamkaribie Yehova. Leo, watu wapole wa mataifa yote wanavutwa kwenye kutaniko la kimataifa la Wakristo watiwa-mafuta, ambalo Yesu ndiye Kichwa chake. (Wakolosai 1:18) Mioyo ya watu hao wapole inaguswa wanaposikia jina la Mungu likitukuzwa na watumishi wake wanyenyekevu na wanaposikia ujumbe wa Biblia, ambao roho takatifu ya Mungu inawawezesha kuelewa.—Yohana 6:44; Matendo 16:14.

      Mikutano Inaimarisha Imani Yetu

      14. (a) Je, Daudi alitosheka tu kumsifu Yehova faraghani? (b) Yesu aliweka mfano gani kuhusiana na mikutano ya ibada?

      14 “Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.” (Zaburi 34:3) Daudi hakutosheka tu kumsifu Yehova faraghani. Aliwakaribisha wenzake kwa uchangamfu wajiunge naye katika kulikweza jina la Mungu. Vivyo hivyo, Yesu Kristo, yule Daudi Mkuu Zaidi, alifurahia kumsifu Yehova hadharani, kwenye sinagogi la kwao, kwenye sherehe katika hekalu la Mungu huko Yerusalemu, na akiwa pamoja na wafuasi wake. (Luka 2:49; 4:16-19; 10:21; Yohana 18:20) Ni pendeleo lenye shangwe kama nini kufuata mfano wa Yesu wa kumsifu Yehova katika kila nafasi tunayopata pamoja na waamini wenzetu, hasa sasa kadiri ‘tunavyoona siku ile kuwa inakaribia’!—Waebrania 10:24, 25.

      15. (a) Mambo yaliyompata Daudi yalikuwa na matokeo gani juu ya wanaume wake? (b) Tunafaidika jinsi gani tunapohudhuria mikutano yetu?

      15 “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha.” (Zaburi 34:4) Mambo hayo yaliyompata Daudi yalikuwa muhimu kwake. Kwa hiyo, aliendelea kusema hivi: “Huyu mwenye kuteseka aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na Yeye akamwokoa kutoka katika taabu zake zote.” (Zaburi 34:6) Tunaposhirikiana na waamini wenzetu, tuna nafasi nyingi za kusimulia mambo yenye kujenga kuhusu jinsi Yehova ametusaidia kuvumilia hali ngumu. Hilo linaimarisha imani ya waamini wenzetu, kama masimulizi ya Daudi yalivyoimarisha imani ya watu waliomuunga mkono. Katika kisa cha Daudi, watu walioandamana naye “walimtazama [Yehova], wakang’aa, nazo nyuso zao hazingeweza kuona haya kamwe.” (Zaburi 34:5) Ingawa walikuwa wakimkimbia Mfalme Sauli, hawakuona haya. Walikuwa na hakika kwamba Mungu alikuwa akimtegemeza Daudi, na nyuso zao ziling’aa. Vivyo hivyo, wapya wenye kupendezwa na pia wale ambao wamekuwa Wakristo wa kweli kwa muda mrefu wanamtazama Yehova awategemeze. Kwa kuwa wamesaidiwa na Yehova kibinafsi, nyuso zao zenye kung’aa zinaonyesha azimio lao la kubaki waaminifu.

      Thamini Msaada wa Malaika

      16. Yehova amewatumia malaika wake jinsi gani kutuokoa?

      16 “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.” (Zaburi 34:7) Daudi hakuona kwamba ni yeye tu angeweza kuokolewa na Yehova. Ni kweli kwamba Daudi alikuwa mtiwa-mafuta wa Yehova, mfalme wa Israeli ambaye angefuata; lakini alijua kwamba Yehova anatumia malaika wake kuwalinda waabudu wake wote waaminifu, haidhuru ni watu mashuhuri au ni wa hali ya chini. Katika nyakati zetu pia, waabudu wa kweli wamelindwa na Yehova. Katika Ujerumani ya Nazi na pia Angola, Malawi, Msumbiji, na nchi nyingine nyingi, wenye mamlaka wameendesha kampeni ili kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova. Jitihada zao hazijafaulu. Badala yake, watu wa Yehova katika nchi hizo wanaendelea kusitawi huku wakilikweza jina la Mungu pamoja. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anawatumia malaika wake watakatifu kuwalinda na kuwaongoza watu wake.—Waebrania 1:14.

      17. Malaika wa Mungu wanatusaidia katika njia gani?

      17 Kwa kuongezea, malaika wa Yehova wanaweza kuelekeza mambo ili mtu yeyote anayewakwaza wengine aondolewe miongoni mwa watu wa Yehova. (Mathayo 13:41; 18:6, 10) Hata ingawa huenda hatujui, malaika wanaondoa vitu vinavyokwaza ambavyo vinaweza kutuzuia tusimtumikie Mungu, na wanatulinda kutokana na mambo yanayoweza kuhatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Jambo muhimu zaidi ni kwamba wanatuongoza katika kazi ya kutangaza “habari njema ya milele” kwa wanadamu wote, kutia ndani maeneo ambako kazi ya kuhubiri inaendeshwa chini ya hali hatari. (Ufunuo 14:6) Visa vinavyothibitisha kwamba malaika wanasaidia vimesimuliwa mara nyingi katika vichapo vya Biblia vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.a Visa hivyo ni vingi sana hivi kwamba hatuwezi kusema kuwa vinatukia vyenyewe tu.

      18. (a) Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike na msaada wa malaika? (b) Habari inayofuata itazungumzia nini?

      18 Ili kuendelea kufaidika na mwongozo na ulinzi wa malaika, tunapaswa kuendelea kulikweza jina la Yehova hata tunapokabili upinzani. Kumbuka kwamba malaika wa Mungu anapiga kambi “kuwazunguka wanaomwogopa [Yehova]” tu. Hilo linamaanisha nini? Kumwogopa Mungu kunamaanisha nini, na tunaweza kusitawisha sifa hiyo jinsi gani? Kwa nini Mungu mwenye upendo anataka tumwogope? Maswali hayo yatazungumziwa katika habari inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 550; Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2005, ukurasa wa 53-54; Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 2000, ukurasa wa 5-6; Januari 1, 1991, ukurasa wa 27; na Februari 15, 1991, ukurasa wa 26.

  • Furahia Maisha Katika Kumwogopa Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Machi 1
    • Furahia Maisha Katika Kumwogopa Yehova

      “Mwogopeni Yehova, enyi watakatifu wake, kwa maana wale wanaomwogopa hawakosi chochote.”—ZABURI 34:9.

      1, 2. (a) Dini zinazodai kuwa za Kikristo zina maoni gani tofauti kuhusu kumwogopa Mungu? (b) Tutazungumzia maswali gani?

      WAHUBIRI wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ambao wanafundisha kuhusu kumwogopa Mungu, mara nyingi wanafanya hivyo kwa msingi wa fundisho lisilo la kimaandiko la kwamba Mungu anawaadhibu watenda-dhambi katika moto wa milele. Fundisho kama hilo linapingana na yale ambayo Biblia inafundisha kumhusu Yehova akiwa Mungu wa upendo na haki. (Mwanzo 3:19; Kumbukumbu la Torati 32:4; Waroma 6:23; 1 Yohana 4:8) Wahudumu wengine wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanafundisha jambo tofauti. Hawataji kamwe kumwogopa Mungu. Badala yake, wanafundisha kwamba Mungu anawaendekeza watu na kukubali karibu kila mtu haidhuru anaishi maisha ya aina gani. Biblia haifundishi hilo pia.—Wagalatia 5:19-21.

      2 Kwa kweli, Biblia inatutia moyo tumwogope Mungu. (Ufunuo 14:7) Fundisho hilo la Biblia linatokeza maswali fulani. Kwa nini Mungu mwenye upendo anataka tumwogope? Mungu anataka tumwogope kwa njia gani? Kumwogopa Mungu kunaweza kutufaidi jinsi gani? Tutazungumzia maswali hayo tunapoendelea na mazungumzo yetu kuhusu Zaburi ya 34.

      Kwa Nini Tumwogope Mungu?

      3. (a) Una maoni gani kuhusu amri ya kumwogopa Mungu? (b) Kwa nini watu wanaomwogopa Mungu ni wenye furaha?

      3 Akiwa Muumba na Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, Yehova anastahili kuogopwa. (1 Petro 2:17) Hata hivyo, woga huo si hofu inayopita kiasi ya mungu mkatili. Ni kumcha Yehova na kumheshimu sana kwa sababu ya cheo chake. Pia kunamaanisha kuogopa kutompendeza. Kumwogopa Mungu ni sifa bora inayofanya maisha ya mtu yawe mazuri, haimfanyi mtu ashuke moyo au atetemeke. Yehova, “Mungu mwenye furaha,” anataka viumbe wake wa kibinadamu wafurahie maisha. (1 Timotheo 1:11) Hata hivyo, ili tufurahie maisha ni lazima tuishi kulingana na matakwa ya Mungu. Kwa watu wengi, hilo linamaanisha kubadili mtindo wao wa maisha. Wote wanaofanya mabadiliko yanayohitajika wanaona ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi Daudi: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia. Mwogopeni Yehova, enyi watakatifu wake, kwa maana wale wanaomwogopa hawakosi chochote.” (Zaburi 34:8, 9) Wote wanaomwogopa Yehova hawakosi chochote chenye thamani ya kudumu kwa sababu wana uhusiano mzuri na Mungu.

      4. Daudi na Yesu walitoa uhakikisho gani?

      4 Ona kwamba kama ilivyokuwa katika siku zake, Daudi aliwaheshimu wanaume wake kwa kuwaita “watakatifu.” Walikuwa sehemu ya taifa takatifu la Mungu. Pia, walikuwa wakihatarisha maisha yao ili kumfuata Daudi. Ingawa walikuwa wakimkimbia Mfalme Sauli, Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova angeendelea kuwatimizia mahitaji yao ya lazima. Daudi aliandika hivi: “Wana-simba wenye manyoya shingoni wamekuwa na vichache na kukaa njaa; lakini kwa wale wanaomtafuta Yehova, hawatakosa chochote chema.” (Zaburi 34:10) Yesu aliwapa wafuasi wake uhakikisho kama huo.—Mathayo 6:33.

      5. (a) Wafuasi wengi wa Yesu walikuwa watu wa hali gani? (b) Yesu alitoa shauri gani kuhusu kuogopa?

      5 Wengi kati ya watu waliomsikiliza Yesu walikuwa maskini, Wayahudi wa hali ya chini. Hivyo, Yesu “akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Je, watu hao wa hali ya chini wangekuwa na ujasiri wa kumfuata Yesu? Ili wafanye hivyo, walihitaji kusitawisha woga kumwelekea Yehova, badala ya kuwaogopa wanadamu. Yesu alisema: “Msiwaogope wale wanaouua mwili na baada ya hilo hawawezi kufanya jambo lolote zaidi. Lakini nitawaonyesha ninyi yule mnayepaswa kumwogopa: Mwogopeni yule ambaye baada ya kuua ana mamlaka ya kutupa ndani ya Gehena. Ndiyo, ninawaambia ninyi, Mwogopeni Huyo. Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao husahaulika mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”—Luka 12:4-7.

      6. (a) Wakristo wameimarishwa na maneno gani ya Yesu? (b) Kwa nini Yesu ni mfano bora zaidi wa kumwogopa Mungu?

      6 Wale wanaomwogopa Yehova wanaposukumwa na maadui wao waache kumtumikia Mungu, wanaweza kukumbuka shauri hili la Yesu: “Kila mtu anayekiri kuwa pamoja nami mbele ya wanadamu, Mwana wa binadamu atakiri pia kuwa pamoja naye mbele ya malaika za Mungu. Lakini yule anayenikana mbele ya wanadamu atakanwa mbele ya malaika za Mungu.” (Luka 12:8, 9) Maneno hayo yamewaimarisha Wakristo, hasa katika nchi ambako ibada ya kweli imepigwa marufuku. Watu kama hao wanaendelea kumsifu Yehova kwa busara kwenye mikutano ya Kikristo na katika huduma yao ya hadharani. (Matendo 5:29) Yesu anaweka mfano bora wa “kumwogopa Mungu.” (Waebrania 5:7) Neno la kinabii lilitabiri hivi kumhusu: “Roho ya Yehova itatua juu yake, roho . . . ya kumwogopa Yehova; naye atakuwa na shangwe katika kumwogopa Yehova.” (Isaya 11:2, 3) Hivyo, Yesu ndiye anayestahili zaidi kutufundisha faida za kumwogopa Mungu.

      7. (a) Wakristo wanakubali jinsi gani mwaliko kama ule uliotolewa na Daudi? (b) Wazazi wanaweza kufuata mfano mzuri wa Daudi jinsi gani?

      7 Kwa kweli, wote wanaofuata mfano wa Yesu na kutii mafundisho yake, wanakubali mwaliko kama ule uliotolewa na Daudi: “Njooni, enyi wana, nisikilizeni; nitawafundisha kumwogopa Yehova.” (Zaburi 34:11) Kwa kawaida, Daudi aliwaita wanaume wake “wana” kwa sababu walimheshimu akiwa kiongozi wao. Kwa upande wake, Daudi aliwasaidia kiroho wafuasi wake ili wawe na umoja na kupata kibali cha Mungu. Huo ni mfano mzuri kama nini kwa wazazi Wakristo! Yehova amewapa mamlaka juu ya wana na binti zao ili ‘waendelee kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’ (Waefeso 6:4) Kwa kuzungumzia mambo ya kiroho kila siku pamoja na watoto wao na kwa kujifunza Biblia pamoja nao kwa ukawaida, wazazi wanawasaidia watoto wao kufurahia maisha katika kumwogopa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

      Jinsi Tunavyoonyesha Kwamba Tunamwogopa Mungu

      8, 9. (a) Ni nini kinachofanya maisha ya kumwogopa Mungu yapendeze sana? (b) Kuulinda ulimi wetu kunahusisha nini?

      8 Kama ilivyotajwa mapema, kumwogopa Yehova hakumaanishi kujinyima shangwe. Daudi aliuliza hivi: “Ni nani mtu yule anayependezwa na uhai, ambaye anapenda siku za kutosha ili kuona mema?” (Zaburi 34:12) Kwa wazi, kumwogopa Yehova ni jambo muhimu ili kuwa na maisha marefu na kuona mema. Hata hivyo, ni rahisi kudai hivi: “Ninamwogopa Mungu.” Lakini ni jambo tofauti kabisa kuthibitisha hilo kwa mwenendo wetu. Hivyo, Daudi anaeleza jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu.

      9 “Linda ulimi wako na yaliyo mabaya, na midomo yako isiseme udanganyifu.” (Zaburi 34:13) Mtume Petro aliongozwa na roho ya Mungu kunukuu sehemu hii ya Zaburi ya 34 baada ya kuwashauri Wakristo watendeane kwa upendo wa kindugu. (1 Petro 3:8-12) Kuulinda ulimi wetu na yaliyo mabaya kunamaanisha kwamba tutaepuka kueneza porojo yenye kudhuru. Badala yake, sikuzote tutajitahidi kuwa wenye kujenga tunapozungumza na wengine. Zaidi ya hayo, tutajitahidi kuwa wajasiri na kusema kweli.—Waefeso 4:25, 29, 31; Yakobo 5:16.

      10. (a) Eleza maana ya kugeuka kutoka katika yaliyo mabaya. (b) Kufanya yaliyo mema kunahusisha nini?

      10 “Geuka kutoka katika yaliyo mabaya, na kufanya yaliyo mema; utafute amani, na kuifuatia.” (Zaburi 34:14) Tunaepuka mambo ambayo Mungu anashutumu kama vile ukosefu wa adili katika ngono, ponografia (picha au habari za ngono), wizi, kuwasiliana na pepo, jeuri, ulevi, na matumizi ya dawa za kulevya. Tunakataa pia burudani ambazo zinakazia mambo kama hayo yenye kuchukiza. (Waefeso 5:10-12) Badala yake, tunatumia wakati wetu kufanya yaliyo mema. Jambo zuri zaidi ambalo tunaweza kufanya ni kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ili kuwasaidia wengine wapate wokovu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kufanya yaliyo mema kunatia ndani pia kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, kutunza Jumba letu la Ufalme, na kuwasaidia Wakristo wenye uhitaji.

      11. (a) Daudi alionyesha jinsi gani kwa matendo mambo aliyohubiri kuhusu amani? (b) Unaweza kufanya nini ili ‘kufuatia amani’ kutanikoni?

      11 Daudi aliweka mfano mzuri katika kufuatia amani. Mara mbili alipata nafasi ya kumuua Sauli. Katika pindi zote mbili, alijizuia asitende kwa ujeuri na baadaye alizungumza na mfalme huyo kwa heshima, huku akitumaini kwamba angerudisha amani. (1 Samweli 24:8-11; 26:17-20) Tunaweza kufanya nini leo wakati hali fulani inapotisha kuvuruga amani ya kutaniko? Tunapaswa ‘kutafuta amani, na kuifuatia.’ Hivyo, tunapohisi kwamba kuna matatizo katika uhusiano wetu pamoja na mwamini mwenzetu, tunatii shauri hili la Yesu: “Kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako.” Halafu tuendelee na shughuli nyingine za ibada ya kweli.—Mathayo 5:23, 24; Waefeso 4:26.

      Kumwogopa Mungu Kunaleta Thawabu Kubwa

      12, 13. (a) Watu wanaomwogopa Mungu wanapata faida gani sasa? (b) Waabudu waaminifu watapata thawabu gani kubwa hivi karibuni?

      12 “Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.” (Zaburi 34:15) Masimulizi ya shughuli za Mungu pamoja na Daudi yanathibitisha kwamba maneno hayo ni ya kweli. Leo, tunapata shangwe nyingi na amani ya moyoni kwa sababu tunajua kwamba Yehova anatulinda. Tuna hakika kwamba ataendelea kutimiza mahitaji yetu hata tukiwa chini ya hali zenye kufadhaisha sana. Tunajua kwamba hivi karibuni waabudu wote wa kweli watakabili shambulizi lililotabiriwa la Gogu wa Magogu nao wataiona ‘siku ya Yehova yenye kuogopesha.’ (Yoeli 2:11, 31; Ezekieli 38:14-18, 21-23) Haidhuru hali tutakayokabili, maneno haya ya Daudi yatatimia: “Wao walilia kwa sauti, naye Yehova mwenyewe akasikia, naye akawakomboa kutoka katika taabu zao zote.”—Zaburi 34:17.

      13 Wakati huo, tutasisimka kama nini kuona Yehova akilitukuza jina lake kuu! Kuliko wakati mwingine wowote, mioyo yetu itajawa na heshima nyingi zaidi, na wapinzani wote watapata uharibifu wenye kuaibisha. “Uso wa Yehova uko dhidi ya wale wanaotenda yaliyo mabaya, ili kumbukumbu lao liondolewe mbali duniani.” (Zaburi 34:16) Itakuwa thawabu kubwa kama nini kupata ukombozi huo mkubwa na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu!

      Ahadi Ambazo Zinatusaidia Kuvumilia

      14. Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia tujapokabili misiba?

      14 Kwa sasa tunahitaji uvumilivu ili tuendelee kumtii Yehova katika ulimwengu huu uliopotoka na wenye chuki. Kumwogopa Mungu kutatusaidia sana kuwa watiifu. Kwa sababu tunaishi katika nyakati za hatari, watumishi fulani wa Yehova wanakabili hali ngumu sana ambazo zinawavunja moyo na kuponda roho zao. Hata hivyo, wanaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba wakimtegemea Yehova, atawasaidia kuvumilia. Maneno haya ya Daudi yanatoa faraja ya kweli: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” (Zaburi 34:18) Inatia moyo kwamba Daudi aliendelea kusema hivi: “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.” (Zaburi 34:19) Hata tukikabili misiba mingi kadiri gani, Yehova ana nguvu za kutosha kutukomboa.

      15, 16. (a) Daudi alipata habari kuhusu msiba gani baada ya kutunga Zaburi ya 34? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia majaribu?

      15 Muda mfupi baada ya kutunga Zaburi ya 34, Daudi alisikia kuhusu msiba uliowapata wakaaji wa Nobu, Sauli alipowaua wakaaji hao na wengi kati ya makuhani. Ni wazi kwamba Daudi alifadhaika sana alipokumbuka kuwa Sauli alikasirika kwa sababu alikuwa ametembelea jiji la Nobu! (1 Samweli 22:13, 18-21) Hapana shaka kwamba Daudi alimwomba Yehova msaada, na bila shaka alifarijika kujua kwamba kutakuwa na ufufuo wa “waadilifu” wakati ujao.—Matendo 24:15.

      16 Leo, tumaini la ufufuo linatuimarisha pia. Tunajua kwamba jambo lolote ambalo maadui wetu wanaweza kufanya haliwezi kutuletea madhara ya kudumu. (Mathayo 10:28) Daudi alionyesha usadikisho kama huo kwa maneno haya: “Yeye anailinda mifupa yote ya mtu huyo [mwadilifu]; hakuna hata mmoja uliovunjwa.” (Zaburi 34:20) Andiko hilo lilitimia kihalisi kuhusiana na Yesu. Ingawa Yesu aliuawa kikatili, hakuna mfupa wake hata mmoja ‘uliovunjwa.’ (Yohana 19:36) Kanuni ya Zaburi 34:20 inatuhakikishia kwamba hata wakabili majaribu gani, Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, “kondoo wengine,” hawatapata kamwe madhara ya kudumu. Kwa njia ya mfano, mifupa yao haitavunjwa kamwe.—Yohana 10:16.

      17. Ni msiba gani unaowangoja watu wasiotubu ambao wanawachukia watu wa Yehova?

      17 Hali ya waovu ni tofauti. Hivi karibuni watavuna mabaya ambayo wamepanda. “Msiba utamuua mwovu; na wale wanaomchukia mwadilifu watahesabiwa kuwa na hatia.” (Zaburi 34:21) Wote wanaoendelea kuwapinga watu wa Mungu wanakabili msiba mbaya sana. Wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo, “watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.”—2 Wathesalonike 1:9.

      18. Ni katika maana gani “umati mkubwa” umekombolewa leo, na wataona nini wakati ujao?

      18 Zaburi ya Daudi inamalizia kwa uhakikisho huu: “Yehova anaikomboa nafsi ya watumishi wake; wala hakuna yeyote kati ya wale wanaomkimbilia atakayehesabiwa kuwa na hatia.” (Zaburi 34:22) Karibu mwisho wa utawala wake wa miaka 40, Mfalme Daudi alisema: ‘Mungu aliikomboa nafsi yangu kutoka katika taabu zote.’ (1 Wafalme 1:29) Kama Daudi, hivi karibuni wale wanaomwogopa Yehova watashangilia watakapokumbuka jinsi walivyokombolewa kutokana na hatia yoyote waliyokuwa nayo kwa sababu ya dhambi na kuokolewa kutoka katika majaribu yao yote. Tayari, Wakristo wengi watiwa-mafuta wamepokea thawabu yao ya kimbingu. Sasa, “umati mkubwa” kutoka katika mataifa yote unajiunga na mabaki ya ndugu za Yesu katika kumtumikia Mungu na hivyo wanakuwa na msimamo safi mbele za Yehova. Hiyo ni kwa sababu wanaonyesha imani katika nguvu za kukomboa za damu iliyomwagwa ya Yesu. Katika Utawala wa Miaka Elfu Moja unaokuja wa Kristo, faida kamili za dhabihu ya fidia zitatumiwa kwa ajili yao na kuwasaidia wawe wanadamu wakamilifu.—Ufunuo 7:9, 14, 17; 21:3-5.

      19. Washiriki wa “umati mkubwa” wameazimia kufanya nini?

      19 Kwa nini “umati mkubwa” wa waabudu wa Mungu utapata baraka hizo zote? Kwa sababu wameazimia kuendelea kumwogopa Yehova, kumtumikia kwa heshima na woga, na kumtii sana. Kwa kweli, kumwogopa Yehova kunafanya maisha yafurahishe sasa na kunatusaidia ‘tushike imara ule uzima ulio wa kweli,’ yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Timotheo 6:12, 18, 19; Ufunuo 15:3, 4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki