-
Kutumia MuhtasariFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 25
Kutumia Muhtasari
WATU wengi huogopa kutumia muhtasari. Wao hufurahia zaidi ikiwa wameandika au kukariri kila jambo wanalotaka kusema.
Lakini ukweli ni kwamba kila siku sisi huzungumza bila kutumia muhtasari. Sisi huzungumza na jamaa zetu na marafiki bila kutumia muhtasari. Sisi huzungumza bila muhtasari tunapokuwa katika huduma. Hatutumii muhtasari tunaposali kutoka moyoni, iwe tunasali binafsi au kwa niaba ya wengine.
Unapotoa hotuba, je, kuna tofauti yoyote kati ya kusoma hotuba yako na kutumia muhtasari? Ingawa kusoma hotuba kunaweza kufanya utumie maneno yanayofaa na yaliyo sahihi, kufanya hivyo hakugusi mioyo. Mara nyingi ukisoma sentensi chache, utaanza kufuata mtindo fulani ambao ni tofauti na kawaida yako ya kuzungumza. Akili yako ikizama katika maandishi yako na kusahau wasikilizaji, huenda wengi wasisikilize kwa makini kama ambavyo wangesikiliza iwapo wangeona kwamba unawajali kweli na habari unayozungumzia inawahusu. Njia bora zaidi ya kutoa hotuba inayochochea kabisa ni kuitoa bila kutazama sana maandishi.
Kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni kutusaidia katika maisha ya kawaida. Tunapokutana na marafiki, je, sisi hutoa karatasi na kuwasomea mambo tunayotaka kuwaeleza eti kuhakikisha tunatumia maneno yanayofaa zaidi? Tunapokuwa katika utumishi wa shambani, hatubebi maandishi ya kusoma, eti kwa sababu tunaogopa tutasahau mambo fulani ambayo tungependa kuwaeleza watu. Unapotoa onyesho katika shule kuhusu kutoa ushahidi katika hali hizo, jizoeze kuzungumza kwa njia ya kawaida kwa kadiri iwezekanavyo. Ukitayarisha vizuri, utaona kwamba muhtasari ambao umeandika au umeshika akilini hutosha kukukumbusha mambo makuu ambayo unataka kuzungumzia. Lakini unawezaje kufaulu kutumia muhtasari?
Panga Mambo Unayotaka Kuzungumzia. Ili uweze kutumia muhtasari, unahitaji kupanga mambo unayotaka kuzungumzia. Hiyo haimaanishi kuchagua maneno ambayo unapanga kutumia. Inamaanisha tu kufikiri kabla ya kuzungumza.
Kwa kawaida, mtu ambaye huzungumza bila kufikiri hushtukia amesema mambo ambayo baadaye anajutia. Mwingine naye anaweza kuzungumza bila mpango, akitangatanga kutoka jambo moja hadi jingine. Unaweza kusuluhisha matatizo hayo vizuri kwa kutua na kupanga kwa ufupi mawazo yako akilini kabla ya kuzungumza. Kwanza kumbuka kusudi lako, kisha chagua mambo ambayo unahitaji kufanya ili kutimiza kusudi hilo, kisha uzungumze.
-
-
Kutumia MuhtasariFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Muhtasari Wako Uwe Rahisi. Je, muhtasari wako ni wa kutoa hotuba? Muhtasari huo uwe na habari gani?
Kumbuka kwamba kusudi la muhtasari ni kukusaidia kukumbuka mawazo unayotaka kuwasilisha. Labda ungependa kuandika utangulizi wenye sentensi chache. Lakini baada ya hapo kazia akili mawazo unayotaka kuwasilisha na wala si maneno unayotaka kutumia. Tumia sentensi fupi-fupi unapoandika mawazo hayo. Mambo makuu machache ambayo unapanga kutumia yawe dhahiri katika muhtasari wako. Unaweza kuyafanya yawe dhahiri kwa kuyaandika kwa herufi kubwa, kuyapiga mstari, au kuyatia alama kwa rangi tofauti. Chini ya kila jambo kuu, orodhesha mambo ambayo unataka kutumia ili kulifafanua jambo kuu. Andika maandiko ambayo unapanga kusoma. Mara nyingi ni afadhali kusoma maandiko hayo katika Biblia. Andika mifano ambayo unataka kutumia. Pia unaweza kuwa na mnukuo mzuri uliopata katika vichapo vya kilimwengu ambao unafaa kutumiwa. Maandishi yako yawe na mambo hususa unayotaka kutaja. Ni rahisi zaidi kutumia muhtasari nadhifu.
Wengine hutumia mihtasari ambayo ina mambo machache kabisa. Muhtasari unaweza kuwa na maneno machache makuu, maandiko ambayo msemaji atayanukuu kutoka akilini, na michoro au picha zinazomwezesha kukumbuka mambo anayotaka kusema. Kwa maandishi hayo tu, msemaji anaweza kutoa hotuba inayofuatana vizuri na kwa njia ya mazungumzo. Na hilo ndilo lengo la somo hili.
Kuna mazungumzo yanayohusu “Kutayarisha Muhtasari” katika ukurasa wa 39 hadi 42 wa kitabu hiki. Kuna faida kubwa ya kusoma habari hiyo unaposhughulikia somo hili la “Kutumia Muhtasari.”
Jinsi ya Kutumia Muhtasari. Wakati huu kusudi lako si kutayarisha muhtasari wa hotuba, bali ni kuutumia muhtasari vizuri.
Hatua ya kwanza ya kutumia muhtasari ni matayarisho ya kuutoa. Chunguza kichwa kikuu, soma kila jambo kuu, na utambue uhusiano uliopo kati ya mambo hayo makuu na kichwa kikuu. Tazama muda ambao unaweza kutumia kwa kila jambo kuu. Kisha chunguza jambo kuu la kwanza. Pitia sababu zinazoonyeshwa, maandiko, na mifano ambayo unataka kutumia katika sehemu hiyo. Pitia sehemu hiyo mara kadhaa mpaka uielewe vizuri. Fanya hivyo na kila mojawapo ya mambo mengine makuu. Fikiria mambo ambayo unaweza kukosa kutaja hali ikikulazimu ili umalize kwa wakati. Kisha pitia hotuba yote. Kazia mambo makuu, na wala si maneno. Usikariri hotuba hiyo.
Unapotoa hotuba, unapaswa kuwatazama wasikilizaji kwa njia nzuri. Mara nyingi baada ya kusoma andiko, unapaswa kusababu juu ya andiko hilo ukitumia Biblia bila kurudia maandishi yako. Vilevile ukitoa mfano, uutoe kama ambavyo ungewaeleza marafiki wako badala ya kusoma mfano huo katika maandishi yako. Unapozungumza, usitazame-tazame maandishi yako na kusoma kila sentensi. Zungumza kwa hisia, nawe utagusa mioyo ya wale wanaokusikiliza.
Utakapokuwa stadi wa kutoa hotuba ukitumia muhtasari, utakuwa umepiga hatua kubwa ya kuwa msemaji mzuri unapohutubia watu.
-