-
Kutumia Vizuri VielelezoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 47
Kutumia Vizuri Vielelezo
KWA NINI utumie vielelezo unapofundisha? Kwa sababu vielelezo hufanya uwe mwalimu bora. Yehova Mungu na Yesu Kristo walitumia vielelezo nasi tunaweza kuwaiga. Vielelezo vinapotumiwa pamoja na maelezo, akili hupokea habari kwa njia mbili. Vielelezo vinaweza kuvuta usikivu wa wasikilizaji na kufanya wakumbuke jambo hilo. Unawezaje kutumia vielelezo unapohubiri habari njema? Unawezaje kuwa na hakika kwamba unatumia vizuri vielelezo?
Jinsi Ambavyo Walimu Wakuu Walitumia Vielelezo. Yehova alifundisha mambo muhimu sana kupitia vielelezo vilivyo rahisi kukumbuka. Siku moja alimleta Abrahamu nje, akasema: “Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. . . . Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.” (Mwa. 15:5) Hata ingawa kwa maoni ya binadamu ahadi hiyo ilionekana kuwa haiwezi kutimizwa, Abrahamu aliguswa moyo sana akaweka imani katika Yehova. Pindi nyingine, Yehova alimtuma Yeremia kwa mfinyanzi akamwambia aingie kwenye karakana yake akatazame jinsi mfinyanzi anavyofinyanga udongo. Hilo ni somo lililoje kuhusu mamlaka ya Muumba juu ya wanadamu! (Yer. 18:1-6) Na, je, kweli Yona angesahau somo la rehema ambalo Yehova alimfundisha kupitia mtango? (Yona 4:6-11) Yehova hata aliwaambia manabii wake waigize ujumbe wake wa unabii wakitumia vitu fulani. (1 Fal. 11:29-32; Yer. 27:1-8; Eze. 4:1-17) Sehemu za hema la kukutania na hekalu ni mifano inayotusaidia kuelewa mambo halisi ya mbinguni. (Ebr. 9:9, 23, 24) Pia Mungu alitumia sana maono ili kutangaza ujumbe muhimu.—Eze. 1:4-28; 8:2-18; Mdo. 10:9-16; 16:9, 10; Ufu. 1:1.
Yesu alitumiaje vielelezo? Mafarisayo na wafuasi wa chama cha Herode walipojaribu kumtega Yesu kwa maneno, aliomba sarafu ya dinari na kuwaonyesha picha ya Kaisari. Akawaeleza kwamba Kaisari apewe vitu vyake na Mungu apewe vitu vyake. (Mt. 22:19-21) Yesu alifundisha somo la kumheshimu Mungu kwa vyote tulivyo navyo kwa kumrejelea mjane mmoja maskini kwenye hekalu ambaye alitoa mchango wa sarafu mbili ndogo, riziki yake yote. (Luka 21:1-4) Pindi nyingine alitumia mtoto mdogo kuwa mfano wa unyenyekevu na wa kutotamani makuu. (Mt. 18:2-6) Alionyesha pia maana ya kuwa mnyenyekevu, kwa kuosha miguu ya wanafunzi wake.—Yn. 13:14.
-
-
Kutumia Vizuri VielelezoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Kutumia Vielelezo Mbele ya Watu Wengi. Vielelezo vikitayarishwa vizuri na kuonyeshwa vizuri vinaweza kusaidia sana kufundisha watu wengi. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara huandaa aina kadhaa za vielelezo kama hivyo.
Kwa kawaida, somo la Mnara wa Mlinzi hutia ndani vielelezo kama vile picha ambazo kiongozi anaweza kutumia kukazia mambo muhimu. Ndivyo ilivyo na vichapo vinavyotumiwa kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko.
Hotuba fulani za watu wote zinaweza kutolewa kwa urahisi kwa kutumia vielelezo vinavyokazia mambo makuu. Lakini utakuwa na matokeo zaidi ukikazia akili mambo yaliyo katika Biblia kwa kuwa wasikilizaji wengi wana Biblia. Ikiwa pindi moja unahitaji kutumia picha au mchoro fulani wa mambo makuu ili kufafanua jambo moja au mambo kadhaa makuu ya hotuba, chunguza mapema uone kama kielelezo hicho kinaweza kuonwa (au kusomwa) na wale ambao wameketi nyuma kwenye jumba. Vielelezo kama hivyo vitumiwe mara chache sana.
Kusudi la vielelezo si kutumbuiza watu tunapozungumza na kufundisha. Tunapotumia vielelezo vinavyofaa, kusudi linapaswa kuwa kukazia mawazo yanayostahili kukaziwa kwa njia ya pekee. Vielelezo hivyo hufaa sana vinaposaidia kufafanua jambo na kufanya lieleweke kwa urahisi, au vinapotumiwa kuthibitisha jambo kabisa. Ukitumia vizuri kielelezo, kinaweza kukazia jambo kabisa hivi kwamba wasikilizaji watakumbuka kielelezo hicho na jambo hilo kwa miaka mingi.
Uwezo wa kusikia na kuona hutusaidia sana kujifunza. Kumbuka jinsi Walimu wakuu wametumia hali ya kusikia na kuona, na ujaribu kuwaiga unapofundisha wengine.
-