Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuzungumza kwa njia ya kawaida
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 14

      Kuzungumza kwa njia ya kawaida

      Unahitaji kufanya nini?

      Uwe kama kawaida yako—kwa maongezi na unyofu bila kuiga wengine.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Ikiwa una wasiwasi, ikiwa hujatulia, au ikiwa huzungumzi kwa njia ya kawaida kwa sababu ya kujifikiria sana, wengine wanaweza kukengeushwa wasikusikilize.

      KUONGEA kwa njia ya kawaida hufanya wengine wakuamini. Je, unaweza kuamini maneno ya mtu ambaye amefunika uso wake kwa kitu fulani? Na je, ungeamini maneno yake kama kitu hicho kinavutia kuliko sura yake halisi? Hapana. Basi uwe jinsi ulivyo kwa kawaida badala ya kuiga usemi mwingine.

      Kuzungumza kwa njia ya kawaida si uzembe. Kutotumia lugha sanifu, kutamka maneno vibaya, na kutosema maneno yanayosikika wazi hakufai. Tuepuke lugha ya mtaani. Nyakati zote maneno yetu na tabia zetu ziwe na adabu. Mtu ambaye anaongea kwa njia ya kawaida haongei kwa njia rasmi kupita kiasi wala hafikirii tu kuvutia watu.

  • Kuzungumza kwa njia ya kawaida
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • Jukwaani. Unapohutubia watu, njia bora ni kuzungumza kwa njia ya kawaida na ya maongezi. Bila shaka unahitaji kuinua sauti ikiwa wasikilizaji ni wengi. Ukiona unajaribu kukariri hotuba yako au kama una maandishi mengi mno, labda sababu ni kwamba unaogopa kukosea. Ni muhimu kutumia maneno yanayofaa, lakini maneno hayo yakizingatiwa kupita kiasi, hotuba haitapendeza wala kuvutia. Haitatokea kwa njia ya kawaida. Unapaswa kufikiria mapema kwa makini mambo ambayo utasema, lakini zingatia zaidi mawazo yako badala ya kufikiria maneno hususa utakayotumia.

      Na ndivyo ilivyo unapohojiwa mkutanoni. Jitayarishe vizuri, lakini usisome wala kukariri majibu yako. Zungumza kwa njia ya kawaida ili maelezo yako yatoke moyoni na kuvutia.

      Hata sifa nzuri zinaweza kuonwa na wasikilizaji kuwa si za kawaida zikitumiwa kupita kiasi. Kwa mfano, unapaswa kuzungumza kwa njia inayoeleweka wazi na kutamka maneno vizuri, au kwa njia ya kawaida. Hotuba yako inaweza kuchangamsha ukitumia vizuri ishara za kutia mkazo au za ufafanuzi, lakini ishara zinazolazimishwa au zenye kupita kiasi hukengeusha wasikilizaji. Zungumza kwa kiasi kinachofaa cha sauti lakini si kwa sauti kubwa kupita kiasi. Inafaa kuwa na shauku mara kwa mara katika hotuba, lakini epuka kuongea kwa majivuno. Ubadilifu wa sauti, shauku, na hisia zinapasa kuonyeshwa kwa njia ambayo haifanyi mtu ajielekezee fikira au kufanya wasikilizaji wawe na wasiwasi.

      Watu wengine wana njia zao za kawaida za kuongea, hata wakati hawatoi hotuba. Wengine hutoa hotuba kwa njia ya maongezi zaidi. Jambo muhimu ni kuzungumza kwa njia nzuri kila siku na kujiendesha kwa njia ya Kikristo. Kisha unapotoa hotuba jukwaani, itakuwa rahisi kuongea na kutenda kwa njia ya kawaida inayopendeza.

  • Kuzungumza kwa njia ya kawaida
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • JINSI YA KUFAULU

      • Zungumza kama unavyofanya kila siku. Badala ya kujifikiria, mfikirie Yehova na ukumbuke kwamba watu wake wanahitaji kujifunza juu yake.

      • Unapotayarisha hotuba, zingatia zaidi mawazo, na wala si maneno hususa utakayotumia.

      • Unapotoa hotuba na unapoongea kama kawaida, jaribu kuepuka kuzungumza kwa njia ya kizembe na pia jaribu kuepuka kutumia sifa za usemi zinazofanya ujielekezee fikira.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki