Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tunastaajabishwa na Ulimwengu!
    Amkeni!—2009 | Desemba
    • Tunastaajabishwa na Ulimwengu!

      UTAFITI wa wanasayansi umetuwezesha kufahamu mambo mengi kuhusu jinsi ulimwengu unavyofanya kazi. Sasa wanadamu wanaweza kuuelewa vizuri zaidi, kuanzia chembe zake ndogo sana hadi anga lake kubwa. Hata hivyo, bado kuna mambo mengi sana ambayo kufikia sasa hatujayaelewa.

      Dunia yetu ni ndogo sana inapolinganishwa na ulimwengu wote. Hata hivyo, tunastaajabishwa na utata na umaridadi wa vitu vya asili vilivyo duniani kama vile ua lenye kupendeza, mandhari yenye kuvutia, manyoya ya ndege yenye rangi nzuri, mabawa ya kipepeo, machweo yenye rangi nyekundu, au tabasamu ya mtu tunayempenda.

      Watu wengi wamepata uthibitisho wa kutosha katika ulimwengu unaowafanya waamini kwamba kuna mtu mwenye akili ambaye ndiye Mwanzilishi wa vitu vyote. Wanasema kwamba inaonekana ni kama sheria za fizikia zimepimwa kwa usahihi ili ziweze kutegemeza uhai. Ikiwa vipimo hivyo vingetofautiana hata kwa kiasi kidogo tu, hakungeweza kuwa na uhai. Lakini tumezungukwa na unamna-namna mwingi sana wa uhai ambao ni maridadi sana.

      Mtaalamu wa anga, Paul Davies anaandika hivi: “Ulimwengu unaposonga na kubadilika ni kana kwamba unafuata mpangilio fulani . . . Ulimwengu haukutokezwa na matukio yaliyotokea bila mpango bali ulitokezwa na sheria za hisabati ambazo zinapatana kwa ustadi.” Wanasayansi fulani wanakubaliana na Davies. Wengine hawakubaliani naye.

      Kwa mfano, mtaalamu wa fizikia aliye pia mshindi wa Tuzo la Nobeli Steven Weinberg, aliandika hivi: “Kadiri ulimwengu uonekanavyo kuwa wenye kueleweka zaidi, ndivyo inavyozidi kuonekana kuwa vigumu kuelewa ni kwa nini upo.” Ingawa hivyo, Weinberg pia alisema kwamba “nyakati nyingine ni kana kwamba vitu fulani katika ulimwengu vipo tu kwa sababu ya umaridadi na si kwamba ni lazima viwepo. . . . Tunalazimika kufikia mkataa kwamba umaridadi huo wote ulitokezwa kwa faida yetu.”

      Una maoni gani? Ikiwa kuna vipimo sahihi, si bila shaka lazima kuwe pia na Mpimaji Mkuu—Mbuni, Muumba—aliye na kusudi? Je, kuna kusudi la kuwepo kwa uhai na ulimwengu wetu? Au je, tupo hapa kwa sababu ya matukio fulani yaliyotokea bila mpango au mwelekezo wowote? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.

  • Je, Ulibuniwa kwa Kusudi au Ulijitokeza Wenyewe?
    Amkeni!—2009 | Desemba
    • Je, Ulibuniwa kwa Kusudi au Ulijitokeza Wenyewe?

      Mnamo 1802, William Paley, kasisi Mwingereza ambaye pia ni mwanatheolojia, alieleza ni kwa nini aliamini kwamba kuna Muumba. Alisema kwamba ikiwa angepata jiwe porini, huenda angekata kauli kwamba lilitokezwa na utendaji fulani wa kiasili. Lakini ikiwa angepata saa ya mkononi, hangekuwa na maoni kama hayo. Kwa nini? Kwa sababu kuna uthibitisho wa kutosha kuonyesha kwamba saa hiyo ilibuniwa na mtu fulani na kwa kusudi fulani.

      HOJA hiyo ya Paley ilikuwa na uvutano mkubwa kwa Mwingereza Charles Darwin, ambaye alichunguza vitu vya asili. Hata hivyo, kinyume na hoja ya Paley inayopatana na akili, baadaye Darwin alitoa hoja ya kwamba ubuni unaoonekana katika viumbe hai ulitokana na utendaji aliouita “uteuzi wa kiasili.” Wengi waliona kuwa nadharia ya Darwin ya mageuzi inathibitisha kwamba ni vitu vya asili havikubuniwa.

      Habari nyingi zimeandikwa kuhusu suala hilo tangu siku za Paley na Darwin. Hoja zinazounga mkono ubuni na zile zinazounga mkono uteuzi wa kiasili zimeboreshwa, kuelezwa kwa undani, na kuandikwa upya. Na hoja hizo zimeathiri sana maoni ya watu kuhusu ikiwa ulimwengu huu ulitokezwa kwa kusudi fulani au la. Maoni yako kuhusu jambo hilo yanaweza kuathiri kusudi lako maishani. Jinsi gani?

      Madhara ya Nadharia ya Darwin

      Nadharia ya Darwin imewafanya watu wengi wanyoofu waamini kwamba maisha yao hayana kusudi. Ikiwa ulimwengu na kila kitu kilicho ndani yake kilitokezwa ghafula baada ya ule mlipuko mkubwa wa kwanza, basi uhai hauna kusudi halisi. Jacques Monod, mwanabiolojia aliyeshinda Tuzo la Nobeli alisema hivi: “Hatimaye mwanadamu anajua kwamba yuko peke yake katika ulimwengu usio na kitu, na ambako yeye alitokea tu kwa nasibu. Wakati wake ujao na majukumu yake hayajaandikwa mahali popote.”

      Peter William Atkins, profesa wa kemia katika chuo kikuu cha Oxford anaeleza wazo kama hilo anaposema: “Kwa maoni yangu ulimwengu huu usio na kifani ni kitu chenye kushangaza, kustaajabisha, na chenye fahari. Unaning’inia ukiwa na utukufu wake na ukiwa kamili lakini bila kusudi lolote.”

      Si wanasayansi wote wanaokubaliana na maneno hayo na wana sababu nzuri.

      Je, Vipimo Sahihi Vinathibitisha Ulimwengu Ulibuniwa kwa Kusudi Fulani?

      Wanapochunguza sheria za asili, wachunguzi wengi hawakubaliani na wazo la kwamba ulimwengu hauna kusudi. Kwa mfano, wanavutiwa na kani za msingi zinazoongoza ulimwengu. Inaonekana kwamba sheria zinazoongoza kani hizo zimepimwa kwa usahihi kabisa ili kutokeza ulimwengu unaoweza kutegemeza uhai. “Kubadili sheria hizi kidogo tu kunaweza kusababisha madhara makubwa,” anasema mtaalamu wa anga, Paul Davies. Kwa mfano, ikiwa protoni zingekuwa nzito kidogo tu kuliko nutroni, badala ya kuwa nyepesi kama zilivyo, basi protoni zote zilizotokezwa zingekuwa nutroni. Je, hilo lingetokeza madhara makubwa? “Kama hakungekuwa na protoni zinatokeza umeme,” anaeleza Davies, “atomu hazingekuwapo.”

      Kani ya sumaku-umeme huvuta protoni kwenye elektroni na kuwezesha molekuli kufanyizwa. Kama kani hiyo ingalikuwa dhaifu kidogo tu, elektroni hazingaliweza kukusanywa kuzunguka kiini cha atomu na molekuli hazingefanyizwa. Kwa upande mwingine, kama kani hiyo ingalikuwa yenye nguvu zaidi, elektroni zingenaswa katika kiini cha atomu. Hakungalikuwa na utendaji wowote kati ya atomu mbalimbali na pia hakungekuwa na uhai.

      Ikiwa kani za sumaku-umeme zingebadilika kidogo tu zingeathiri jua na nguvu zake zinazofika duniani. Badiliko hilo lingefanya iwe vigumu sana au hata isiwezekane kuwa na usanidimwanga (njia ya mimea kujifanyizia chakula). Kwa hiyo, kipimo sahihi kabisa cha kani za sumaku-umeme huamua kama tutaishi au hatutaishi.a

      Kitabu Science & Christianity—Four Views kinaeleza kwa njia yenye kupendeza jinsi kani za msingi zinazoongoza ulimwengu na vitu vilivyomo vimesawazishwa kwa njia ya ajabu. Mwandishi wa kitabu hicho anawaomba wasomaji wawazie mtu akiingia kwenye “chumba kilicho na mitambo ya kuongoza ulimwengu wote.” Mtu huyo anaona geji nyingi sana zenye mishale inayoweza kusogezwa kwenye kipimo chochote, na anagundua kwamba mshale wa kila geji umewekwa kwenye kipimo hususa kabisa ili uhai uwepo. Geji moja inapima kiasi cha nguvu za uvutano, nyingine inapima nguvu za sumaku-umeme, na nyingine inapima uwiano kati ya uzito wa nutroni na protoni, na kadhalika. Mtu huyo anapochunguza geji hizo nyingi, anaona kwamba huenda zingeweza kuwekwa katika vipimo tofauti. Pia anagundua kwamba vipimo hivyo vimefanyiwa hesabu kwa uangalifu hivi kwamba ikiwa vingesogezwa hata kidogo tu, hilo lingebadili sana muundo wa ulimwengu hivi kwamba haungeweza kutegemeza tena uhai. Kila geji imewekwa katika kipimo kinachofaa kabisa ili ulimwengu uendelee kutenda kazi na kutegemeza uhai. Mtu huyo atakata kauli gani anapoona jinsi vipimo vya geji hizo vimewekwa?

      Mtaalamu wa nyota George Greenstein, anasema hivi: “Tunapochunguza uthibitisho uliopo, kila mara tunapata wazo la kwamba lazima kitu fulani kilicho na nguvu zisizo za kawaida—au, Mtu fulani alihusika. Inawezekana kwamba kwa ghafula, bila kutarajia, tumepata uthibitisho wa kisayansi kwamba kuna Mtu Mkuu Kuliko Wote?”

      Una maoni gani? Ni nadharia gani inayoeleza vizuri vipimo sahihi vinavyoonekana ulimwenguni? Je, vilibuniwa kwa kusudi au vilijitokeza vyenyewe?

      ‘Tupo Hapa—Hakuna la Ziada’

      Bila shaka, watu ambao wanaamini kwamba hakuna Mungu wana hoja zao zinazopinga kuwapo kwake. Wengine hupuuza vipimo sahihi ulimwenguni, wakisema: ‘Bila shaka ulimwengu unaoonekana unaweza kutegemeza uhai wa wanadamu. Ikiwa haungeweza, hatungekuwa hai na hivyo hatungehangaishwa na jambo hilo. Kwa hiyo, hakuna jambo la ajabu sana. Tupo hapa, na hakuna la ziada.’ Lakini je, unaona hilo kuwa jibu lenye kuridhisha linaloeleza kwa nini tupo hapa?

      Hoja nyingine wanayotoa ni kwamba siku moja itathibitishwa kwamba kuna nambari fulani tu ambazo zinaweza kuelezea sheria za msingi za nguvu za asili. Yaani, ilibidi geji tulizotaja ziwekwe katika vipimo sahihi ili ulimwengu uwepo. Wengine husema, ‘Iko hivyo kwa sababu ilipaswa kuwa hivyo!’ Hata kama hoja hizo ni za kweli, bado hazielezi vizuri kwa nini tupo hapa. Kwa ufupi, je, ulimwengu huu unaoweza kutegemeza uhai ulijitokeza tu bila mpango?

      Ili kujaribu kueleza kwamba ubuni na vipimo sahihi vinavyoonekana ulimwenguni ni matokeo ya utendaji wa kiasili, wengine wamesema kwamba kuna zaidi ya ulimwengu mmoja tu. Kulingana na nadharia hiyo, huenda tunaishi katika moja kati ya mamia yasiyohesabika ya ulimwengu ambayo yanatofautiana, lakini hakuna ulimwengu wowote ulio na kusudi au ubuni. Kulingana na maoni hayo na sheria ya uwezekano, ikiwa kuna mamia ya ulimwengu, basi lazima kuwe na moja inayoweza kutegemeza uhai. Hata hivyo, hakuna uthibitisho wowote wa kisayansi unaounga mkono nadharia hiyo ya kwamba kuna ulimwengu zaidi ya mmoja. Hayo ni mambo ya kuwaziwa tu.

      Baada ya kueleza kwamba haungi mkono wazo hilo, Christian de Duve, mwanabiokemia aliyeshinda Tuzo la Nobeli alisema hivi: “Kwa maoni yangu, iwe kuna ulimwengu zaidi ya mmoja ambao unaweza au hauwezi kutokeza uhai na akili ya mwanadamu, uhai na akili ya mwanadamu ni vitu vya pekee sana, na kwa hiyo lazima viwe muhimu. Ingawa watu wanasema kwamba kuna ulimwengu mwingine mbali na wetu, hilo halipunguzi umuhimu wa ulimwengu wetu ulio na sifa za pekee ambazo zinadokeza kwamba ulibuniwa.”

      Uwezo wa Mwanadamu wa Kufahamu Mambo

      Inastaajabisha kwamba tunaweza kutunga nadharia zinazoeleza kuwepo kwa ulimwengu. Ikiwa ulimwengu hauna kusudi, basi uwezo huo ungekuwa umejitokeza tu wenyewe. Kwa maoni yako, je, hilo linapatana na akili?

      Ubongo wa mwanadamu umefafanuliwa kuwa “ndicho kitu chenye kustaajabisha na tata zaidi katika ulimwengu wote.” Hakuna nyanja yoyote ya fizikia na kemia inayoweza kuelezea vizuri uwezo wa mwanadamu wa kufikiri na jitihada zetu za kupata kusudi maishani.

      Ama akili ya mwanadamu na jitihada zake za kuelewa mambo ilitokezwa na mtu mwenye akili sana, ama ilijitokeza yenyewe. Kati ya mambo hayo mawili, unaona ni lipi linalopatana na akili?

      Je, Kuna Wazo Lingine?

      Kwa kweli, sayansi imetueleza mengi kuhusu jinsi ambavyo ulimwengu na viumbe hai vinatenda kazi. Watu fulani wanaona kwamba kadiri wanavyozidi kupata habari nyingi kutoka kwa wanasayansi, “ndivyo inavyozidi kuwa vigumu kuelewa ni kwa nini tupo hapa.” Inakuwa vigumu kuelewa kwa nini tupo hapa ikiwa nadharia ya mageuzi ni ya kweli. Hata hivyo, tukinukuu maneno ya mwandishi wa mambo ya kisayansi John Horgan, “kila kitu kinachotuzunguka kinaonekana kimebuniwa kwa ustadi sana na, inaonekana kwamba haiwezekani kuwa ulimwengu ulitokea tu.” Mwanafizikia Freeman Dyson alisema hivi: “Kadiri ninavyouchunguza ulimwengu na kujifunza mambo hususa kuhusu muundo wake, ndivyo ninavyopata uthibitisho zaidi kwamba ulimwengu ulijua tutaishi ndani yake.”

      Unapochunguza uthibitisho uliopo—utata wa vitu hai, vipimo sahihi, ubuni unaoonekana wazi, na uwezo wa mwanadamu wa kufahamu mambo—je, halingekuwa jambo linalopatana na akili angalau kuchunguza uwezekano wa kuwepo kwa Muumba? Kuna sababu nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa Muumba atatueleza jinsi ambavyo uhai ulitokea na kama uhai una kusudi—maswali ambayo sayansi imeshindwa kujibu.

      Maswali hayo yanajibiwa katika kitabu kinachoitwa Biblia, au Maandiko Matakatifu, ambacho waandikaji wake wanadai kwamba waliongozwa na Muumba kukiandika. Mbona usichunguze yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo?

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi, ona ukurasa wa 10-26 katika kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      Je, ubongo wa mwanadamu ulijitokeza wenyewe tu?

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      Ni Nini Ambacho Kinawawezesha Wanasayansi Kufanya Utafiti?

      Utafiti wa kisayansi unawezekana kwa sababu ulimwengu una utaratibu na kwa sababu nguvu na vitu vilivyomo hutenda kwa njia inayoweza kujulikana mapema, vinapokuwa katika hali fulani. Utaratibu huo unaweza kuelezewa kwa usahihi kulingana na sheria za msingi za hisabati, fizikia, kemia na kadhalika. Bila utaratibu huo, hakungekuwa na utafiti wa kisayansi, teknolojia na hata uhai wenyewe.

      Swali ni: Sheria za asili zilitoka wapi? Na kwa nini zinafanya kazi kwa njia hiyo? Wengi huamini kwamba kuna Mtu Mwenye Akili Nyingi Sana aliyepanga mambo hayo. Wewe una maoni gani?

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      Je, Ilitokea Yenyewe Tu?

      Molekuli za DNA au Deoksiribonyukilia Asidi (chembe za urithi) kwenye kila chembe ya kiumbe hai zina habari muhimu kwa ajili ya ukuzi na maendeleo ya kiumbe hicho. Ingawa DNA ni tata sana, inaweza kulinganishwa na habari za kielektroniki zilizohifadhiwa kwenye diski ya DVD. Inapochezeshwa, habari zilizomo ndani ya DVD hiyo zinamwezesha mtu kuona picha za video au kusikiliza muziki. Vivyo hivyo, molekuli za DNA ambazo zinaonekana kama ngazi ya kamba iliyosokotwa, zina habari yote muhimu inayowezesha viumbe hai kutofautiana—ndizi kutofautiana na maharagwe, pundamilia atofautiane na sisimizi, na mwanadamu atofautiane na nyangumi.

      Bila shaka, hakuna yeyote anayeweza kusema kwamba habari zilizomo katika DVD zilijitokeza tu. Je, inapatana na akili kufikiria kwamba habari tata sana zilizomo kwenye DNA zilitokea zenyewe tu?

      [Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]

      Sombrero Galaxy: NASA and The Hubble Heritage Team (STScI/AURA)

  • Kwa Nini Tupo Hapa?
    Amkeni!—2009 | Desemba
    • Kwa Nini Tupo Hapa?

      KULINGANA na Biblia, Mungu ambaye jina lake ni Yehova ana akili nyingi sana. Yeye ndiye Chanzo cha nguvu zote ulimwenguni na Muumba wa ulimwengu. (Zaburi 83:18; 92:5) Sura ya kwanza ya Biblia inasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Baadaye, Mungu alimfanya mtu kwa “mfano” wake, yaani, akiwa na sifa kama zake—na Mungu akamwambia mwanadamu azae na kuijaza dunia.—Mwanzo 1:1, 26, 28.

      Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu aliuumba ulimwengu, kutia ndani dunia pamoja na wanyama na mimea mingi iliyomo kwa ajili tu ya wanadamu? Na je, tupo hapa ili tu tufurahie maisha kwa miaka michache, tule, tunywe, na kuzaa?

      Kwa Nini Mungu Alituumba?

      Yehova Mungu alimuumba mwanadamu ili kuonyesha upendo wake—alitaka kushiriki uhai na furaha yake pamoja na wanadamu. Bila shaka, Mungu alifurahia sana kutokeza uumbaji wa aina mbalimbali ili mwanadamu azungukwe na viumbe wengi maridadi. Jambo muhimu zaidi ni kwamba wanadamu waliumbwa wawe na uhusiano wa karibu na Muumba wao, wamfahamu, na kuwasiliana naye. Waliumbwa waishi milele chini ya hali kamilifu na zenye amani.—Mwanzo 3:8, 9; Zaburi 37:11, 29.

      Yehova pia aliwapa wanadamu kazi muhimu na yenye kuridhisha. Mungu aliwaambia hivi wanadamu wa kwanza: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.” (Mwanzo 1:28) Naam, wanadamu wawili wa kwanza na watoto wao wangeifanya dunia yote kuwa paradiso yenye kupendeza.

      Lakini mambo hayakutukia kama Yehova alivyokuwa amekusudia.a Hata hivyo, kusudi la kwanza la Mungu kwa ajili ya mwanadamu litatimia.—Isaya 46:9-11; 55:11.

      Kwa sasa, jitihada za mwanadamu za kutafuta kusudi zinaonyesha kwamba anatamani na anahitaji kumfahamu Mungu na kuwa na uhusiano naye. Mwanadamu aliumbwa akiwa kiumbe mwenye akili aliye na tamaa ya kuchunguza na kuelewa mambo. Na Biblia inasema kwamba mwanadamu ataendelea kutafuta habari zenye kuridhisha kumhusu Mungu na uumbaji wake milele.

      Mwandikaji mmoja wa Biblia anaeleza kusudi la mwanadamu kwa njia hii: “Nimeona shughuli ambayo Mungu amewapa wana wa binadamu wajishughulishe nayo. Amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho. Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.” (Mhubiri 3:10-13) Kwa hiyo, mwanadamu hatafikia mwisho wa kujifunza kumhusu Yehova na uumbaji wake.

      Jifunze Kumhusu Mungu

      Unaweza kujifunza kumhusu Yehova kwa kuchunguza uumbaji wake. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema kwamba “sifa zake [Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Naam, uumbaji unafunua upendo, hekima, na nguvu za Yehova.

      Njia nyingine muhimu ya kujifunza kumhusu Mungu ni Biblia. Kitabu hicho kilichoongozwa na roho ya Mungu kinatueleza mambo mengi zaidi kumhusu Yehova kuliko yale tunayoweza kujifunza kutokana na uumbaji wake. Kinatueleza maoni yake, sifa zake, na kusudi lake.

      Biblia inasema hivi kuhusu kusudi la Mungu: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.” (Zaburi 115:16) Inaonekana kwamba dunia ndiyo mahali panapofaa zaidi kwa mwanadamu kuishi, nayo iliumbwa hasa kwa kusudi hilo.

      Vipi kuhusu ulimwengu wetu mkubwa? Je, nyota hizo zote zinazotuzunguka ziliumbwa ili tu kudumisha usawaziko kamili katika mfumo wetu wa jua ili kuendeleza uhai duniani? Je, jua, nyota, na sayari nyingine ziliumbwa ili tu kurembesha anga letu usiku? Tunapaswa kutambua kwamba bado kuna mambo mengi sana ambayo hatujui. Lakini hilo ni jambo zuri! Kwa nini?

      Hata mwanadamu aishi milele, hataweza kuelewa yote ambayo Mungu amefanya na anayokusudia kufanya. Mungu anataka wakati wetu ujao uwe wakati wa kuvumbua mambo na kuwa na shangwe isiyo na mwisho. Kuishi milele kwa furaha hapa duniani kutawapa wanadamu watiifu nafasi tele ya kuvumbua mambo mengi sana kuhusu ulimwengu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Uovu na kuteseka kunawazuia watu wengi kuamini kwamba kuna Muumba mwenye upendo. Kwa habari zaidi kuhusu jambo hilo, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki