-
Msifuni Mfalme wa Umilele!Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
Kazi Zenye Uweza Hata Zaidi
17. ‘Wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo’ wamtukuzaje Yehova?
17 Katika miaka elfu sita iliyopita, Mfalme wa umilele ameanzisha kazi zenye uweza hata zaidi. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, kwenye Ufunuo 15:3, 4 (NW) twasoma juu ya wale walio mbinguni ambao wamepata ushindi dhidi ya maadui walio roho waovu: “Wanaimba wimbo wa Musa mtumwa wa Mungu na wimbo wa Mwana-Kondoo, wakisema: ‘Ni kubwa na za ajabu sana kazi zako, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Ni za uadilifu na za kweli njia zako, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuhofu wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu? Kwa maana mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele yako, kwa sababu maagizo yako ya uadilifu yamefanywa kuwa dhahiri.’” Kwa nini huo waitwa ‘wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo’? Acheni tuone.
18. Ni kazi gani yenye uweza inayokumbukwa katika wimbo ulio katika Kutoka sura 15?
18 Miaka ipatayo 3,500 iliyopita, wakati jeshi la Farao lenye uweza lilipoangamia katika Bahari Nyekundu, Waisraeli walimsifu Yehova kwa shukrani katika wimbo. Twasoma hivi kwenye Kutoka 15:1, 18 (NW): “Wakati huo Musa na wana wa Israeli walianza kuimba wimbo huu kwa Yehova na kusema yafuatayo: ‘Acha nimwimbie Yehova wimbo, kwa maana ametukuka sana. Farasi na mpanda-farasi wake yeye ametumbukiza baharini. Yehova atatawala akiwa mfalme kwa wakati usiodhahiri, hata milele.’” Amri za uadilifu za huyu Mfalme wa umilele zilidhihirika katika kuhukumu na kuangamiza kwake maadui waliokaidi enzi kuu yake.
19, 20. (a) Kwa nini Yehova alifanyiza taifa la Israeli? (b) Mwana-kondoo na wengine wamejibuje ushindani wa Shetani?
19 Kwa nini hilo lilikuja kuhitajiwa? Ni katika bustani ya Edeni yule nyoka mwenye hila aliwaongoza wazazi wetu wa kwanza watende dhambi. Tokeo la hilo likawa kupitishwa kwa hali ya kutokamilika yenye dhambi kwa wanadamu wote. Hata hivyo, kwa kupatana na kusudi lake la kwanza, Mfalme wa umilele alichukua hatua mara iyo hiyo, ambazo zingeongoza kwenye kuondolea mbali maadui wake wote kutoka kwenye makao ya dunia na kurudisha hali za kiparadiso. Mfalme wa umilele alifanyiza taifa la Israeli na kuandaa Sheria yake ili kuonyesha kimbele jinsi ambavyo angetimiza hilo.—Wagalatia 3:24.
20 Lakini, baada ya wakati fulani, Israeli lenyewe lilididimia katika hali ya kutokuwa jaminifu, na hali hiyo yenye kuhuzunisha ilifikia upeo wakati watawala walo walipokabidhi Waroma Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu ili ateswe vibaya sana na kuuawa. (Matendo 10:39; Wafilipi 2:8) Hata hivyo, uaminifu-maadili wa Yesu hadi kifo, akiwa “Mwana-Kondoo wa Mungu” aliyedhabihiwa, ulijibu kwa njia yenye kutokeza lile suala lililotolewa na Mpinzani wa kale wa Mungu, Shetani—kwamba hakuna mtu duniani ambaye angeendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu akiwa chini ya jaribu kali sana. (Yohana 1:29, 36; Ayubu 1:9-12; 27:5) Ingawa wamerithi kutokamilika kwa Adamu, mamilioni ya wanadamu wengine wamhofuo Mungu wamefuata hatua za Yesu kwa kushika uaminifu-maadili wakabiliwapo na mashambulio ya kishetani.—1 Petro 1:18, 19; 2:19, 21.
21. Kwa kupatana na Matendo 17:29-31, ni nini litakalofuata kuzungumzwa?
21 Sasa siku imewasili kwa Yehova kuthawabisha waaminifu hao na kuhukumu maadui wote wa kweli na uadilifu. (Matendo 17:29-31) Hilo litatendekaje? Makala yetu ifuatayo itaeleza.
-
-
“Msifuni Yah, Enyi Watu!”Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
1, 2. (a) Ni kwa kadiri gani Ukristo wa kweli ulisitawi katika karne ya kwanza? (b) Mitume walitoa onyo gani la kimbele? (c) Uasi-imani ulisitawije?
YESU aliwapanga kitengenezo wanafunzi wake kuwa kutaniko la Kikristo, lililositawi katika karne ya kwanza. Ujapokuwa upinzani mkali, ‘habari njema ilihubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23, NW) Lakini baada ya kifo cha mitume wa Yesu Kristo, Shetani alichochea kwa hila ukuzi wa uasi-imani.
2 Mitume walikuwa wametoa onyo la kimbele juu ya uasi-imani huo. Kwa kielelezo, Paulo aliwaeleza wazee kutoka Efeso: “Kazieni uangalifu kwenu wenyewe na kwa kundi lote, ambalo miongoni mwalo roho takatifu imewaweka nyinyi rasmi kuwa waangalizi, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe. Mimi najua kwamba baada ya kwenda zangu mbwa-mwitu wenye kuonea wataingia miongoni mwenu na hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka miongoni mwenu nyinyi wenyewe watu watainuka na kusema mambo yaliyopotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:28-30, NW; ona pia 2 Petro 2:1-3; 1 Yohana 2:18, 19.) Hivyo, katika karne ya nne, Ukristo wenye kuasi imani ulianza kujiunga na Milki ya Roma. Karne kadhaa baadaye, Milki Takatifu ya Roma, kwa ushirikiano na papa wa Roma, ilikuja kutawala sehemu kubwa ya wanadamu. Baada ya wakati fulani, Warekebishaji wa Kidini wa Kiprotestanti waliasi dhidi ya mambo maovu yenye kupita kiasi ya Kanisa Katoliki, lakini wakashindwa kurudisha Ukristo wa kweli.
3. (a) Ni lini na jinsi gani habari njema ilihubiriwa kwa viumbe vyote? (b) Ni matazamio gani yenye kutegemea Biblia yaliyotimizwa katika 1914?
3 Hata hivyo, mwisho wa karne ya 19 ulipokuwa ukikaribia, kikundi chenye moyo mweupe cha wanafunzi wa Biblia kilikuwa chenye shughuli tena kikihubiri na kueneza kwa ‘viumbe vyote chini ya mbingu tumaini la habari njema.’ Kwa msingi wa funzo la unabii wa Biblia, kikundi hiki kilielekeza mbele kwenye miaka zaidi ya 30 hadi 1914 kuwa mwaka wenye kutia alama mwisho wa “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa,” kipindi cha “nyakati saba,” au miaka 2,520, kilichoanza na kufanywa ukiwa kwa Yerusalemu katika 607 K.W.K. (Luka 21:24, NW; Danieli 4:16) Kwa utimizo wa matazamio yao, 1914 ulithibitika kuwa mwaka wenye kuleta badiliko la maana katika mambo ya wanadamu duniani. Mbinguni pia, mambo ya maana kihistoria yalitendeka. Ndio wakati Mfalme wa umilele alipomweka Mfalme-Mshirika wake, Yesu Kristo, juu ya kiti cha utawala cha kimbingu, kwa utayarishaji wa kufagilia mbali uovu wote kutoka kwenye uso wa dunia hii na kuanzisha Paradiso tena.—Zaburi 2:6, 8, 9; 110:1, 2, 5.
Tazama Mfalme wa Kimesiya!
4. Yesu alijipatanishaje na maana ya jina lake Mikaeli?
4 Katika 1914 Mfalme huyu wa Kimesiya, Yesu, alianza kuchukua hatua. Katika Biblia yeye huitwa pia Mikaeli, kumaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?,” kwa maana amenuia kutetea enzi kuu ya Yehova. Kama ilivyorekodiwa kwenye Ufunuo 12:7-12, mtume Yohana alifafanua katika ono kile ambacho kingetendeka: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.” Ni anguko kubwa kwelikweli!
5, 6. (a) Baada ya 1914, ni mbiu gani yenye kusisimua iliyotangazwa kutoka mbinguni? (b) Mathayo 24:3-13 yaambatanaje na hiyo?
5 Ndipo sauti kuu sana mbinguni ikapiga mbiu hivi: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. Nao [Wakristo waaminifu] wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo [Kristo Yesu], na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.” Hilo lamaanisha ukombozi kwa washika uaminifu-maadili, ambao wamedhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu yenye thamani.—Mithali 10:2; 2 Petro 2:9.
6 Hiyo sauti kuu mbinguni ikaendelea kutangaza hivi: “Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Huo “ole” uliotabiriwa hivyo kwa dunia hii umekuwa dhahiri katika vita vya ulimwengu, njaa kali, magonjwa ya kuambukiza, matetemeko ya dunia, na uasi-sheria ambao umeikumba dunia katika karne hii. Kama vile Mathayo 24:3-13 (NW) husimulia, Yesu alitabiri kwamba hayo yangekuwa sehemu ya ‘ishara ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ Kwa utimizo wa unabii huo, tangu 1914 wanadamu wamepatwa na ole duniani usio na kifani katika historia yote ya kibinadamu iliyotangulia.
7. Kwa nini Mashahidi wa Yehova huhubiri kwa uharaka?
7 Katika enzi hii ya ole wa kishetani, je, wanadamu waweza kupata tumaini kwa wakati ujao? Ndiyo, kwa kuwa Mathayo 12:21 husema hivi juu ya Yesu: “Na jina lake Mataifa watalitumainia”! Hali zenye kufadhaisha zilizo miongoni mwa mataifa hazionyeshi tu ‘ishara ya umalizio wa mfumo wa mambo’ bali pia zaonyesha ‘ishara ya kuwako kwa Yesu’ akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimesiya. Kuhusu Ufalme huo, Yesu asema zaidi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Ni kikundi kipi kimoja cha watu duniani leo kinachohubiri tumaini tukufu la utawala wa Ufalme wa Mungu? Mashahidi wa Yehova! Kwa uharaka, wao hupiga mbiu nyumba kwa nyumba kwamba Ufalme wa Mungu wenye uadilifu na amani uko karibu kutwaa usimamizi wa mambo ya dunia. Je, wewe unashiriki katika huduma hiyo? Huwezi kupata pendeleo kubwa kuliko hili!—2 Timotheo 4:2, 5.
“Mwisho” Unakujaje?
8, 9. (a) Hukumu ilianzaje “katika nyumba ya Mungu”? (b) Jumuiya ya Wakristo imekiukaje Neno la Mungu?
8 Wanadamu wameingia katika kipindi cha hukumu. Tunajulishwa kwenye 1 Petro 4:17 kwamba hukumu ilianza “katika nyumba ya Mungu”—hukumu juu ya matengenezo yanayodai eti kuwa ya Kikristo ambayo imeonekana wazi tangu “siku za mwisho” zilipoanza kwa machinjo ya Vita ya Ulimwengu 1 katika kipindi cha 1914-1918. Jumuiya ya Wakristo imehukumiwaje katika hukumu hiyo? Naam, fikiria msimamo wa makanisa katika kutegemeza vita tangu 1914. Je, makasisi hawajatiwa “alama za damu za nafsi maskini zisizo na hatia” ambazo walizihimiza ziende vitani?—Yeremia 2:34, NW.
9 Kulingana na Mathayo 26:52, Yesu alisema: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” Hilo limekuwa kweli kama nini katika vita vya karne hii! Makasisi wamehimiza vijana wachinje vijana wengine, hata wale wa dini yao—Mkatoliki akimuua Mkatoliki na Mprotestanti akimuua Mprotestanti. Utukuzo wa taifa umekuzwa juu ya Mungu na Kristo. Majuzi, katika baadhi ya mataifa ya Afrika, mahusiano ya kikabila yametangulizwa mbele ya kanuni za Biblia. Katika Rwanda, ambako idadi kubwa ya watu ni Wakatoliki, angalau watu nusu milioni walichinjwa ovyo-ovyo katika ujeuri wa kikabila. Papa alikiri hivi katika gazeti la habari la Vatikani L’Osservatore Romano: “Haya ni maangamizi ya moja kwa moja ya kabila zima, ambayo inasikitisha kwamba hata Wakatoliki wameshiriki.”—Linganisha Isaya 59:2, 3; Mika 4:3, 5.
10. Ni hukumu gani ambayo Yehova atatekeleza juu ya dini bandia?
10 Mfalme wa umilele huzionaje dini zinazotia watu moyo wachinjane au zinazosimama kando tu huku washiriki wa kundi lazo wakiua washiriki wengine? Kuhusu Babiloni Mkubwa, mfumo wa ulimwenguni pote wa dini bandia, Ufunuo 18:21, 24 (NW) hutuambia hivi: “Malaika mwenye nguvu akainua jiwe kama jiwe kubwa la kusagia na kulivurumisha ndani ya bahari, akisema: ‘Hivyo kwa mtupo wa kasi sana atavurumishwa chini Babiloni lile jiji kubwa, na hatapatikana tena kamwe. Ndiyo, katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wote wale ambao wamechinjwa juu ya dunia.’”
11. Ni mambo gani yenye kuchukiza ambayo yamekuwa yakitendeka katika Jumuiya ya Wakristo?
11 Kwa utimizo wa unabii wa Biblia, mambo yenye kuchukiza yamekuwa yakitendeka katika Jumuiya ya Wakristo. (Linganisha Yeremia 5:30, 31; 23:14.) Kwa sababu hasa ya mtazamo wenye uendekevu wa makasisi, makundi yao yamejawa ukosefu wa adili. Katika Marekani, linaloonwa kuwa taifa la Kikristo, karibu nusu ya ndoa zote huishia kwenye talaka. Mimba za matineja na ugoni-jinsia-moja umepita kiasi miongoni mwa washiriki wa kanisa. Mapadri wanawatenda vibaya kingono watoto wachanga—na si katika visa vichache tu. Imesemwa kwamba malipo ya mahakamani yanayohusiana na kesi hizo yanaweza kugharimu Kanisa Katoliki katika Marekani dola bilioni moja katika mwongo mmoja. Jumuiya ya Wakristo imepuuza onyo la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10 (NW): “Ama! Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawatarithi ufalme wa Mungu? Msiongozwe vibaya. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.”
12. (a) Mfalme wa umilele atachukuaje hatua dhidi ya Babiloni Mkubwa? (b) Tofauti na Jumuiya ya Wakristo, ni kwa sababu gani watu wa Mungu wataimba korasi za “Haleluya”?
12 Hivi karibuni, Mfalme wa umilele, Yehova, akitenda kupitia Amiri Mkuu wa kimbingu, Kristo Yesu, ataanzisha dhiki kubwa. Kwanza, Jumuiya ya Wakristo na sehemu nyinginezo za Babiloni Mkubwa zitapatwa na utekelezaji wa hukumu ya Yehova. (Ufunuo 17:16, 17) Wamejionyesha kutostahili wokovu ambao Yehova ameandaa kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu. Wamedharau jina takatifu la Mungu. (Linganisha Ezekieli 39:7.) Ni dhihaka iliyoje kwamba wanaimba korasi za “Haleluya” katika majengo yao ya kidini yenye kuvutia! Wanaondoa jina la Yehova lenye thamani kutoka tafsiri zao za Biblia lakini inaonekana hawajui kamwe jambo la kwamba “Haleluya” humaanisha “Msifuni Yah”—“Yah” ikiwa ni ufupisho wa “Yehova.” Kwa kufaa, Ufunuo 19:1-6 hurekodi korasi za “Haleluya” zitakazoimbwa karibuni katika sherehe ya utekelezaji wa hukumu ya Mungu juu ya Babiloni Mkubwa.
13, 14. (a) Ni matukio gani makubwa yatakayofuata kutukia? (b) Ni yapi matokeo yenye furaha ya wanadamu wenye kumhofu Mungu?
13 Jambo linalofuata kutukia ni ‘kuwasili’ kwa Yesu ili kutangaza na kutekeleza hukumu juu ya mataifa na watu. Yeye mwenyewe alitoa unabii hivi: “Wakati Mwana wa binadamu [Kristo Yesu] awasilipo katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake [cha hukumu] cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote [duniani] yatakusanywa mbele yake, naye atatenganisha watu, kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto. Ndipo mfalme atakapowaambia wale walio kwenye mkono wake wa kuume, ‘Njoni, nyinyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, rithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu ulimwengu kuwekwa msingi.’” (Mathayo 25:31-34, NW) Mt 25 Mstari wa 46 (NW) waendelea kusimulia kwamba jamii ya mbuzi “wataondoka kuingia katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele, lakini waadilifu kuingia katika uhai udumuo milele.”
14 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chaendelea kufafanua jinsi ‘Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,’ Bwana wetu wa kimbingu, Yesu Kristo, atakavyoendesha farasi kuingia katika pigano kwenye Har–Magedoni, akiharibu sehemu ya kisiasa na ya kibiashara ya mfumo wa Shetani. Hivyo Kristo atakuwa ameimwaga “ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi” juu ya makao yote ya kidunia ya Shetani. Mambo haya ‘ya kwanza yapitapo,’ wanadamu wenye kumhofu Mungu wataingizwa katika ulimwengu mpya wenye utukufu ambamo Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao.”—Ufunuo 19:11-16; 21:3-5.
-