Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Usimamizi wa Kutimiza Kusudi la Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Februari 15
    • Usimamizi wa Kutimiza Kusudi la Mungu

      ‘Mungu anatenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.’—WAEFESO 1:11.

      1. Kwa nini makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova yatakutanika Aprili 12, 2006?

      SIKU ya Jumatano, Aprili 12, 2006, watu milioni 16 hivi watakusanyika kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Kwenye sehemu zote ambako watakutanikia, kutakuwa na meza yenye mkate usiotiwa chachu ambao unawakilisha mwili wa Kristo, na divai nyekundu inayowakilisha damu yake iliyomwagwa. Mwishoni mwa hotuba inayozungumzia umuhimu wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu, mifano hiyo itapitishwa kwa wale watakaohudhuria. Mkate utapitishwa kwanza, kisha divai. Katika makutaniko machache ya Mashahidi wa Yehova, mtu mmoja au zaidi kati ya wale watakaohudhuria atashiriki kula mkate huo na kunywa divai hiyo. Hata hivyo, katika makutaniko mengi hakuna atakayeshiriki kula mkate na kunywa divai. Kwa nini ni Wakristo wachache tu, wale walio na tumaini la kuishi mbinguni, ndio wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai huku wengi, walio na tumaini la kuishi milele duniani, hawashiriki?

      2, 3. (a) Yehova alifanyaje kazi ya uumbaji kupatana na kusudi lake? (b) Yehova aliumba dunia na wanadamu kwa kusudi gani?

      2 Yehova ni Mungu mwenye kusudi. Katika kutimiza kusudi lake, yeye ‘hutenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.’ (Waefeso 1:11) Kwanza, alimuumba Mwana wake mzaliwa-pekee. (Yohana 1:1, 14; Ufunuo 3:14) Halafu, kupitia Mwana huyo Yehova aliumba familia ya wana wa roho, kisha akaumba ulimwengu unaoonekana kutia ndani dunia na wanadamu.—Ayubu 38:4, 7; Zaburi 103:19-21; Yohana 1:2, 3; Wakolosai 1:15, 16.

      3 Yehova hakuiumba dunia iwe mahali pa kuwajaribu wanadamu ili kuona ikiwa wanastahili kuwa wana wa roho huko mbinguni kama vile dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo zinavyofundisha. Aliiumba dunia akiwa na kusudi hususa, kwamba “ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mungu aliiumba dunia kwa ajili ya mwanadamu na alimuumba mwanadamu kwa ajili ya dunia. (Zaburi 115:16) Dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa wanadamu waadilifu ambao wangeilima na kuitunza. Wanadamu wawili wa kwanza hawakuwa kamwe na tumaini la kwenda mbinguni.—Mwanzo 1:26-28; 2:7, 8, 15.

      Kusudi la Yehova Latiliwa Shaka

      4. Njia ya Yehova ya kutawala ilitiliwaje shaka mwanzoni mwa historia ya wanadamu?

      4 Mmoja wa wana wa roho wa Mungu aliasi na akaazimia kuharibu kusudi la Yehova huku akitumia vibaya zawadi aliyopewa na Mungu ya uhuru wa kuchagua. Aliharibu amani ya wale wote wanaojitiisha kwa upendo chini ya utawala wa Yehova. Shetani aliwaongoza wanadamu wa kwanza waanze kujitegemea badala ya kumtegemea Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Hakutilia shaka nguvu za Yehova, bali alitilia shaka njia ya Yehova ya kutawala, yaani, haki ya Yehova ya kutawala. Hivyo, suala kuu kuhusu haki ya Yehova ya kutawala lilizushwa hapa duniani, mwanzoni mwa historia ya wanadamu.

      5. Ni suala gani la pili lililozushwa, nalo lilihusisha nani?

      5 Katika siku za Ayubu, Shetani alizusha suala lingine linalohusiana sana na suala hilo kuu la haki ya Yehova ya kutawala. Shetani alitilia shaka nia ya viumbe wa Yehova ya kujitiisha kwa Yehova na kumtumikia. Shetani alidokeza kwamba walikuwa wanafanya hivyo kwa sababu za ubinafsi na kwamba ikiwa wangejaribiwa, wangemwasi Mungu. (Ayubu 1:7-11; 2:4, 5) Ingawa dai hilo lilizushwa dhidi ya mtumishi wa Yehova aliye mwanadamu, lilihusisha pia wana wa roho wa Mungu, hata Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova.

      6. Yehova alikuwaje mwaminifu kwa kusudi lake na kwa jina lake?

      6 Kwa kuwa yeye ni mwaminifu kwa kusudi lake na kwa maana ya jina lake, Yehova alijifanya kuwa Nabii na Mwokozi.a Alimwambia Shetani hivi: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwanzo 3:15) Kupitia Uzao wa “mwanamke” wake, au sehemu ya mbinguni ya tengenezo lake, Yehova angejibu dai la Shetani na kuwapa wazao wa Adamu tumaini la kupata ukombozi na uzima.—Waroma 5:21; Wagalatia 4:26, 31.

      “Siri Takatifu ya Mapenzi Yake”

      7. Yehova alifunua kusudi gani kupitia mtume Paulo?

      7 Katika barua aliyowaandikia Wakristo huko Efeso, mtume Paulo alieleza vizuri sana jinsi Yehova anavyosimamia mambo ili kutimiza kusudi lake. Paulo aliandika hivi: “Alitujulisha siri takatifu ya mapenzi yake. Ni kulingana na upendezi wake mwema alioukusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi, yaani, kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:9, 10) Kusudi tukufu la Yehova ni kufanyiza ulimwengu wenye umoja ulio na viumbe wanaojitiisha kwa upendo chini ya utawala wake. (Ufunuo 4:11) Kwa kufanya hivyo, jina lake litatakaswa, Shetani atathibitishwa kuwa mwongo, na mapenzi ya Mungu yatatendeka “duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10.

      8. Ni nini maana ya neno linalotafsiriwa kuwa “usimamizi”?

      8 ‘Upendezi mwema’ wa Yehova, au kusudi lake, litatimizwa kupitia “usimamizi” fulani. Paulo alitumia neno ambalo, linapotafsiriwa moja kwa moja humaanisha “usimamizi wa nyumba.” Halirejelei serikali, kama vile Ufalme wa Kimasihi, bali linarejelea njia ya kusimamia mambo.b Njia bora ambayo Yehova angetumia kusimamia mambo ili kutimiza kusudi lake ilihusisha “siri takatifu” ambayo ingefunuliwa hatua kwa hatua kadiri wakati ulivyopita.—Waefeso 1:10; 3:9, maelezo ya chini katika Reference Bible.

      9. Yehova alifunuaje hatua kwa hatua siri takatifu ya mapenzi yake?

      9 Kupitia maagano mbalimbali yaliyofuatana, Yehova alifunua hatua kwa hatua jinsi ambavyo kusudi lake kuhusiana na Uzao ulioahidiwa huko Edeni lingetimizwa. Agano lake na Abrahamu lilifunua kwamba Uzao ulioahidiwa ungekuja duniani katika ukoo wa Abrahamu, na kupitia Uzao huo “mataifa yote ya dunia” yangejibariki. Agano hilo pia lilidokeza kwamba wengine wangeshirikiana na sehemu ya msingi ya uzao huo. (Mwanzo 22:17, 18) Agano la Sheria lililofanywa pamoja na taifa la Israeli la asili lilifunua kusudi la Yehova la kuwa na “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:5, 6) Agano lililofanywa pamoja na Daudi lilionyesha kwamba Uzao huo ungekuwa Kichwa cha Ufalme mpaka wakati usio na kipimo. (2 Samweli 7:12, 13; Zaburi 89:3, 4) Baada ya agano la Sheria kuwaongoza Wayahudi kwa Masihi, Yehova alifunua mambo mengine kuhusu utimizo wa kusudi lake. (Wagalatia 3:19, 24) Wanadamu ambao wangeshirikiana na sehemu ya msingi ya uzao ndio wangefanyiza “ufalme wa makuhani” uliotabiriwa, nao wangeingizwa katika “agano jipya” wakiwa “Israeli” jipya, taifa la kiroho.—Yeremia 31:31-34; Waebrania 8:7-9.c

      10, 11. (a) Yehova alifunuaje Uzao uliotabiriwa? (b) Kwa nini Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuja duniani?

      10 Kupatana na usimamizi wa kusudi la Mungu, wakati ulifika ili Uzao uliotabiriwa utokee duniani. Yehova alimtuma malaika Gabrieli amwambie Maria kwamba angemzaa mwana ambaye angeitwa Yesu. Malaika huyo alimwambia Maria hivi: “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Hivyo, Uzao ulioahidiwa ulitambulishwa waziwazi.—Wagalatia 3:16; 4:4.

      11 Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova angekuja duniani na kujaribiwa hadi kifo. Maisha ya Yesu ndiyo yangetoa jibu kamili kwa dai la Shetani. Je, angebaki mwaminifu kwa Baba yake? Jambo hilo lilihusisha siri takatifu. Baadaye, mtume Paulo alieleza daraka la Yesu alipoandika hivi: “Ni jambo lenye kukubalika kwamba siri takatifu ya huu ujitoaji-kimungu ni kubwa: ‘Yeye alifunuliwa katika mwili, alitangazwa kuwa mwadilifu katika roho, alionekana kwa malaika, alihubiriwa kati ya mataifa, aliaminiwa katika ulimwengu, alipokewa juu katika utukufu.’” (1 Timotheo 3:16) Naam, kupitia utimilifu wake hadi kifo, Yesu alitoa jibu kamili kwa dai la Shetani. Lakini mambo mengine kuhusu siri takatifu yangefunuliwa baadaye.

      “Siri Takatifu ya Ufalme wa Mungu”

      12, 13. (a) Ni nini sehemu moja ya “siri takatifu ya ufalme wa Mungu”? (b) Ni nini kilichohusika Yehova alipochagua idadi ndogo ya wanadamu waende mbinguni?

      12 Katika mojawapo ya ziara zake za kuhubiri huko Galilaya, Yesu alionyesha kwamba siri takatifu ilihusiana sana na serikali yake ya Ufalme wa Kimasihi. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu za ufalme wa mbinguni [“ufalme wa Mungu,” Marko 4:11].” (Mathayo 13:11) Sehemu moja ya siri hiyo inahusiana na jinsi ambavyo Yehova angechagua “kundi dogo” la wanadamu 144,000 ili washirikiane na Mwana wake wakiwa sehemu ya ule uzao na kutawala pamoja naye mbinguni.—Luka 12:32; Ufunuo 14:1, 4.

      13 Kwa kuwa wanadamu waliumbwa waishi duniani, ilibidi Yehova atokeze “kiumbe kipya” ili wanadamu fulani waende mbinguni. (2 Wakorintho 5:17) Akiwa mmoja wa wale waliochaguliwa kupata tumaini hilo la pekee la kwenda mbinguni, mtume Petro aliandika hivi: “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenye urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu.”—1 Petro 1:3, 4.

      14. (a) Wasio Wayahudi walihusikaje katika “siri takatifu ya ufalme wa Mungu”? (b) Kwa nini tunaweza kuelewa haya “mambo mazito ya Mungu”?

      14 Sehemu nyingine ya siri takatifu inayohusiana na serikali ya wakati ujao ya Ufalme ni mapenzi ya Mungu ya kuwatia ndani wasio Wayahudi katika idadi ndogo ya wanadamu ambao wangepata mwito wa kutawala na Kristo mbinguni. Paulo alieleza jambo hilo kuhusu “usimamizi” wa Yehova au njia ya kusimamia utimizo wa kusudi lake alipoandika hivi: “Katika vizazi vingine siri hii haikujulishwa kwa wana wa binadamu kama vile ambavyo imefunuliwa sasa kwa mitume wake watakatifu na manabii kupitia roho, yaani, kwamba watu wa mataifa wawe warithi wa pamoja na viungo vyenzi vya mwili na washiriki pamoja nasi wa ahadi katika muungano na Kristo Yesu kupitia habari njema.” (Waefeso 3:5, 6) ‘Mitume watakatifu’ walifunuliwa sehemu hiyo ya siri takatifu. Vivyo hivyo leo, hatungeweza kuelewa haya “mambo mazito ya Mungu” bila msaada wa roho takatifu.—1 Wakorintho 2:10; 4:1; Wakolosai 1:26, 27.

      15, 16. Kwa nini Yehova alichagua wale watakaoshiriki kutawala pamoja na Kristo kutoka kati ya wanadamu?

      15 “Wale 144,000” ambao wanaonekana wakisimama pamoja na “Mwana-Kondoo” juu ya Mlima Sayuni wa mbinguni wanasemwa kuwa “wamenunuliwa kutoka duniani,” naam, “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo,” Kristo Yesu. (Ufunuo 14:1-4) Yehova alichagua mwana wa kwanza kati ya wana wake wa mbinguni kuwa sehemu ya msingi ya uzao ulioahidiwa huko Edeni, lakini kwa nini alichagua washirika wa Kristo kutoka kati ya wanadamu? Mtume Paulo anaeleza kwamba idadi hiyo ndogo ‘iliitwa kulingana na kusudi lake Yehova,’ “kulingana na upendezi mwema wa mapenzi yake.”—Waroma 8:17, 28-30; Waefeso 1:5, 11; 2 Timotheo 1:9.

      16 Kusudi la Yehova ni kutakasa jina lake kuu lililo takatifu na kutetea enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima. Kupitia “usimamizi” wake, au njia yake ya kusimamia mambo inayoonyesha hekima yake isiyo na kifani, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza duniani, ambapo alijaribiwa hadi kifo. Isitoshe, Yehova aliamua kwamba serikali ya Ufalme wa Kimasihi ya Mwana wake ingetia ndani wanadamu ambao pia walikuwa wameunga mkono enzi kuu Yake hadi kifo.—Waefeso 1:8-12; Ufunuo 2:10, 11.

      17. Kwa nini tunaweza kufurahi kwamba Kristo na wale watakaotawala pamoja naye walikuwa wanadamu wakati fulani?

      17 Yehova alionyesha kwamba anawapenda sana wazao wa Adamu kwa kumtuma Mwana wake duniani na kuchagua kutoka kati ya wanadamu wale watakaokuwa warithi-washirika pamoja na Mwana wake katika serikali ya Ufalme. Jambo hilo linaweza kuwafaidije wengine ambao wamekuwa waaminifu kwa Yehova, kuanzia Abeli na kuendelea? Kwa kuwa wamezaliwa wakiwa watumwa wa dhambi na kifo, wanadamu wasio wakamilifu wanahitaji kuponywa kiroho na kimwili na kufanywa wawe wakamilifu, kupatana na kusudi la awali la Yehova kwa ajili ya wanadamu. (Waroma 5:12) Inafariji kama nini kwa wale wote wanaotazamia uzima wa milele duniani kujua kwamba Mfalme wao atawatendea kwa upendo na kwa fadhili kama vile alivyowatendea wanafunzi wake wakati wa huduma yake duniani! (Mathayo 11:28, 29; Waebrania 2:17, 18; 4:15; 7:25, 26) Isitoshe, wanafarijika kama nini wanapotambua kwamba wale watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni wakati mmoja walikuwa wanaume na wanawake wenye imani ambao walikabili udhaifu mbalimbali na matatizo ya maisha, kama sisi!—Waroma 7:21-25.

      Kusudi la Yehova Lisiloweza Kushindwa

      18, 19. Kwa nini tunaelewa wazi zaidi maneno ya Paulo kwenye Waefeso 1:8-11, na tutachunguza nini katika makala inayofuata?

      18 Sasa tunaweza kuelewa vizuri maana ya maneno ya Paulo kwa Wakristo watiwa-mafuta yanayopatikana katika Waefeso 1:8-11. Paulo alisema kwamba Yehova alikuwa amewajulisha “siri takatifu ya mapenzi yake,” kwamba walikuwa ‘wamehesabiwa kuwa warithi’ pamoja na Kristo, na kwamba walikuwa ‘wameagizwa kimbele kulingana na kusudi lake yeye anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.’ Tunatambua kwamba jambo hilo linapatana kabisa na “usimamizi” bora wa Yehova wa kutimiza kusudi lake. Pia, hilo linatusaidia kuelewa kwa nini ni Wakristo wachache tu kati ya wale wanaohudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana ndio wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai.

      19 Katika makala inayofuata, tutaona umuhimu wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo kwa Wakristo walio na tumaini la kwenda mbinguni. Pia, tutajifunza ni kwa nini mamilioni ya watu walio na tumaini la kuishi milele duniani wanapaswa kupendezwa sana na maana ya Ukumbusho.

  • Kukusanya Vitu Vilivyo Mbinguni na Vitu Vilivyo Duniani
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Februari 15
    • Kukusanya Vitu Vilivyo Mbinguni na Vitu Vilivyo Duniani

      “Ni kulingana na upendezi wake mwema . . . kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.”—WAEFESO 1:9, 10.

      1. Yehova ana ‘upendezi gani mwema’ kwa ajili ya mbingu na dunia?

      AMANI KILA MAHALI! Hilo ndilo kusudi tukufu la Yehova, “Mungu wa amani.” (Waebrania 13:20) Alimwongoza mtume Paulo kuandika kwamba “upendezi [Wake] mwema” ni “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:9, 10) Ni nini kinachomaanishwa na kitenzi kinachotafsiriwa kuwa “kukusanya tena pamoja” katika mstari huo? Msomi wa Biblia J. B. Lightfoot anasema hivi: “Maneno hayo yanarejelea upatano wote wa ulimwengu, ambao hautakuwa tena na vitu vigeni vinavyosababisha mgawanyiko, lakini sehemu zake zote zitaunganishwa pamoja katika Kristo. Hakutakuwapo tena na dhambi, kifo, huzuni, kutofanikiwa, na mateso.”

      “Vitu Vilivyo Mbinguni”

      2. “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo vinahitaji kukusanywa ni akina nani?

      2 Mtume Petro alieleza vizuri tumaini bora la Wakristo wa kweli alipoandika hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) “Mbingu mpya” zinazoahidiwa hapa zinamaanisha serikali mpya, yaani, Ufalme wa Kimasihi. “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo Paulo alitaja katika barua yake kwa Waefeso vitakusanywa “katika Kristo.” Vitu hivyo ni wale wanadamu wachache ambao wamechaguliwa kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (1 Petro 1:3, 4) Wakristo hao 144,000 waliotiwa mafuta “wamenunuliwa kutoka duniani,” ‘wamenunuliwa kutoka kati ya wanadamu,’ wawe warithi-washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni.—Ufunuo 5:9, 10; 14:3, 4; 2 Wakorintho 1:21; Waefeso 1:11; 3:6.

      3. Ni kwa njia gani watiwa-mafuta ‘wameketishwa katika mahali pa kimbingu’ hata wakiwa bado duniani?

      3 Wakristo watiwa-mafuta wanazaliwa tena kwa roho takatifu ili wawe wana wa roho wa Yehova. (Yohana 1:12, 13; 3:5-7) Kwa kuwa Yehova amewafanya kuwa “wana,” wao ni ndugu za Yesu. (Waroma 8:15; Waefeso 1:5) Hivyo, hata wakiwa bado duniani, wanasemwa kuwa ‘wameinuliwa na kuketishwa pamoja katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo Yesu.’ (Waefeso 1:3; 2:6) Wana cheo hicho cha juu cha kiroho kwa sababu ‘wametiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa, ambayo ni rehani ya kimbele ya urithi wao’ ambao wamewekewa akiba mbinguni. (Waefeso 1:13, 14; Wakolosai 1:5) Basi, wao ndio “vitu vilivyo mbinguni,” ambao idadi yao kamili iliyoagizwa kimbele na Yehova ilihitaji kukusanywa.

      Kukusanywa Kunaanza

      4. Kukusanywa kwa “vitu vilivyo mbinguni” kulianza wakati gani na jinsi gani?

      4 Kupatana na “usimamizi” wa Yehova, au njia yake ya kusimamia mambo, kukusanywa kwa “vitu vilivyo mbinguni” kulipaswa kuanze “kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi.” (Waefeso 1:10) Wakati huo ulifika siku ya Pentekoste 33 W.K. Siku hiyo, roho takatifu ilimiminwa juu ya mitume na kikundi cha wanafunzi cha wanaume na wanawake. (Matendo 1:13-15; 2:1-4) Hilo lilithibitisha kwamba agano jipya lilikuwa limeanza, na huo ulikuwa mwanzo wa kutaniko la Kikristo na taifa jipya la Israeli wa kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16; Waebrania 9:15; 12:23, 24.

      5. Kwa nini Yehova aliumba “taifa” jipya lichukue mahali pa taifa la Israeli la asili?

      5 Agano la Sheria lililofanywa pamoja na taifa la Israeli la asili halikutokeza “ufalme wa makuhani na taifa takatifu” ambalo lingetumika milele mbinguni. (Kutoka 19:5, 6) Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini Wayahudi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mathayo 21:43) Taifa hilo, Israeli wa kiroho, limefanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta walio katika agano jipya. Mtume Petro aliwaandikia hivi Wakristo hao: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu. Kwa kuwa wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu.” (1 Petro 2:9, 10) Waisraeli wa asili hawakuwa tena watu wa Yehova wa agano. (Waebrania 8:7-13) Kama Yesu alivyotabiri, walinyang’anywa pendeleo la kuwa sehemu ya Ufalme wa Kimasihi, na badala yao, washirika 144,000 wa Israeli wa kiroho wakapewa pendeleo hilo.—Ufunuo 7:4-8.

      Kuingizwa Katika Agano la Ufalme

      6, 7. Ni agano gani la pekee ambalo Yesu alifanya pamoja na ndugu zake waliozaliwa kwa roho, nalo linamaanisha nini kwao?

      6 Usiku ambao Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.” (Luka 22:28-30) Katika andiko hilo, Yesu alizungumzia agano la pekee ambalo alifanya pamoja na ndugu zake 144,000 waliozaliwa kwa roho, ambao wangebaki ‘waaminifu hata kufikia kifo’ na kujithibitisha kuwa ‘washindi.’—Ufunuo 2:10; 3:21.

      7 Wale wa kikundi hicho kidogo huacha kuwa na matumaini yoyote ya kuishi milele duniani wakiwa wanadamu wenye mwili wa nyama na damu. Watatawala pamoja na Kristo mbinguni huku wakiwa wameketi juu ya viti vya ufalme ili kuwahukumu wanadamu. (Ufunuo 20:4, 6) Acheni sasa tuchunguze maandiko mengine ambayo yanawahusu tu hao watiwa-mafuta na ambayo yanaonyesha kwa nini wale wa “kondoo wengine” hawashiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho.—Yohana 10:16.

      8. Watiwa-mafuta huonyesha nini kwa kushiriki kula mkate? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 23.)

      8 Watiwa-mafuta wanashiriki mateso ya Kristo na wako tayari kufa kama yeye. Akiwa mmoja wa watiwa-mafuta, Paulo alisema kwamba alikuwa tayari kutoa dhabihu yoyote kusudi aweze “kumpata Kristo . . . ili kumjua yeye na nguvu za ufufuo wake na kushiriki katika mateso yake.” Naam, Paulo alikuwa tayari kupatwa na “kifo kama chake.” (Wafilipi 3:8, 10) Wakristo wengi watiwa-mafuta wamevumilia katika miili yao ya kibinadamu “matendo yenye kuleta kifo ambayo Yesu alitendewa.”—2 Wakorintho 4:10.

      9. Ni mwili gani unaowakilishwa na mkate wa Ukumbusho?

      9 Alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, Yesu alisema hivi: “Huu unamaanisha mwili wangu.” (Marko 14:22) Alikuwa akizungumza kuhusu mwili wake halisi, ambao ulikuwa karibu kupigwa na kupata madoa ya damu. Mkate usio na chachu ulifananisha vizuri mwili huo. Kwa nini? Kwa sababu katika Biblia, chachu inaweza kufananisha dhambi au uovu. (Mathayo 16:4, 11, 12; 1 Wakorintho 5:6-8) Yesu alikuwa mkamilifu, na mwili wake wa kibinadamu haukuwa na dhambi. Angetoa mwili huo mkamilifu kuwa dhabihu ya upatanisho. (Waebrania 7:26; 1 Yohana 2:2) Kufanya hivyo kungewafaidi Wakristo wote waaminifu, iwe wanatumaini kuishi mbinguni au kupata uzima wa milele katika dunia iliyo paradiso.—Yohana 6:51.

      10. Ni kwa njia gani wale wanaoshiriki kunywa divai ya Ukumbusho ‘hushiriki katika damu ya Kristo’?

      10 Paulo aliandika hivi kuhusu divai ambayo Wakristo watiwa-mafuta hushiriki kunywa wakati wa Ukumbusho: “Kikombe cha baraka ambacho tunabariki, je, hicho si kushiriki katika damu ya Kristo?” (1 Wakorintho 10:16) Ni kwa njia gani wale wanaoshiriki kunywa divai ‘hushiriki katika damu ya Kristo’? Bila shaka, hawashiriki kutoa dhabihu ya fidia, kwa kuwa wao wenyewe wanahitaji ukombozi. Kupitia imani yao katika nguvu za ukombozi za damu ya Kristo, dhambi zao husamehewa, nao wanatangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima huko mbinguni. (Waroma 5:8, 9; Tito 3:4-7) Ni kupitia damu ya Kristo iliyomwagwa kwamba wale warithi-washirika wa Kristo 144,000 ‘wanatakaswa,’ wanawekwa kando, na kusafishwa kutokana na dhambi ili wawe “watakatifu.” (Waebrania 10:29; Danieli 7:18, 27; Waefeso 2:19) Naam, kupitia damu yake iliyomwagwa, Kristo ‘alimnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa, naye akawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10.

      11. Watiwa-mafuta huonyesha nini kwa kunywa divai ya Ukumbusho?

      11 Yesu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwapa mitume wake waaminifu kikombe cha divai na kusema: “Kinyweeni, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.” (Mathayo 26:27, 28) Kama vile damu ya ng’ombe-dume na mbuzi ilivyohalalisha agano la Sheria kati ya Mungu na taifa la Israeli, damu ya Yesu ilihalalisha agano jipya ambalo Yehova angefanya pamoja na taifa la Israeli wa kiroho, kuanzia siku ya Pentekoste 33 W.K. (Kutoka 24:5-8; Luka 22:20; Waebrania 9:14, 15) Kwa kunywa divai ambayo inafananisha ‘damu ya agano,’ watiwa-mafuta wanaonyesha kwamba wameingizwa katika agano jipya na kwamba wanapata faida zake.

      12. Watiwa-mafuta hubatizwaje katika kifo cha Kristo?

      12 Watiwa-mafuta wanakumbushwa jambo lingine. Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake waaminifu: “Kikombe ninachokunywa mtakunywa, na ubatizo ninaobatizwa mtabatizwa.” (Marko 10:38, 39) Baadaye, mtume Paulo alisema kwamba Wakristo ‘wamebatizwa katika kifo cha Kristo.’ (Waroma 6:3) Watiwa-mafuta hudhabihu maisha yao. Kifo chao ni cha kidhabihu kwa sababu wanatupilia mbali tumaini lolote la kupata uzima wa milele duniani. Ubatizo wa Wakristo hao watiwa-mafuta katika kifo cha Kristo unamalizika wakati ambapo, baada ya kufa wakiwa waaminifu, wanafufuliwa wakiwa viumbe wa roho ili ‘watawale wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo mbinguni.—2 Timotheo 2:10-12; Waroma 6:5; 1 Wakorintho 15:42-44, 50.

      Kushiriki Kula Mkate na Kunywa Divai

      13. Kwa nini wale walio na tumaini la kuishi duniani hawashiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho, lakini kwa nini wanahudhuria Ukumbusho?

      13 Kwa kuwa kushiriki kula mkate na kunywa divai inayopitishwa wakati wa Ukumbusho kunahusisha mambo yote hayo, ni wazi kwamba haifai kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani kushiriki kula mkate na kunywa divai. Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanatambua kwamba wao si washiriki waliotiwa mafuta wa mwili wa Kristo, wala hawako katika agano jipya ambalo Yehova alifanya pamoja na wale watakaotawala na Yesu Kristo. Kwa kuwa “kikombe” kinawakilisha agano jipya, ni wale tu walio katika agano jipya wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho. Wale wanaotazamia kupata uzima wa milele wakiwa wanadamu wakamilifu duniani chini ya Ufalme, hawabatizwi katika kifo cha Yesu wala hawapati mwito wa kutawala pamoja naye mbinguni. Ikiwa wangekula mkate na kunywa divai hiyo, basi wangekuwa wanafanya jambo lisilofaa. Kwa hiyo, ingawa wanahudhuria Ukumbusho wakiwa watazamaji wenye heshima, hawashiriki kula mkate na kunywa divai. Wanathamini mambo yote ambayo Yehova amewafanyia kupitia Mwana wake, kutia ndani kuwasamehe kwa msingi wa damu ya Kristo iliyomwagwa.

      14. Watiwa-mafuta wanaimarishwaje kiroho kwa kushiriki kula mkate na kunywa divai?

      14 Kutiwa muhuri kwa mwisho kwa idadi ndogo ya Wakristo walio na mwito wa kutawala pamoja na Kristo mbinguni kunakaribia kumalizika. Hadi mwisho wa maisha yao hapa duniani ambayo wanayadhabihu, watiwa-mafuta huimarishwa kiroho wanaposhiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho. Wanahisi wameunganishwa pamoja na ndugu na dada zao waliotiwa mafuta, wakiwa washiriki wa mwili wa Kristo. Kushiriki kula mkate na kunywa divai huwakumbusha kwamba wana wajibu wa kuwa waaminifu hadi kifo.—2 Petro 1:10, 11.

      Kukusanya “Vitu Vilivyo Duniani”

      15. Ni nani ambao wamekusanywa upande wa Wakristo watiwa-mafuta?

      15 Tangu katikati ya miaka ya 1930, idadi inayoongezeka ya “kondoo wengine,” ambao si sehemu ya “kundi dogo” na ambao wana tumaini la kupata uzima wa milele duniani, wamewaunga mkono watiwa-mafuta. (Yohana 10:16; Luka 12:32; Zekaria 8:23) Wamekuwa waandamani washikamanifu wa ndugu za Kristo, wakiwasaidia sana kuhubiri “habari njema ya ufalme” ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote. (Mathayo 24:14; 25:40) Hivyo, wana nafasi nzuri ya kuhukumiwa na Kristo kuwa “kondoo” zake na kuwekwa kwenye “mkono wake wa kuume” wa kibali wakati atakapokuja kuyahukumu mataifa. (Mathayo 25:33-36, 46) Kupitia imani yao katika damu ya Kristo, watafanyiza “umati mkubwa” ambao utaokoka “dhiki kuu.”—Ufunuo 7:9-14.

      16. “Vitu vilivyo duniani” vitatia ndani akina nani, na ni kwa njia gani wote hao watakuwa na nafasi ya kuwa “watoto wa Mungu”?

      16 Kutiwa muhuri kwa mwisho kwa mabaki ya wale 144,000 kutakapomalizika, zile “pepo” za uharibifu zitaachiliwa juu ya mfumo mbovu wa mambo wa Shetani duniani. (Ufunuo 7:1-4) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo pamoja na wafalme na makuhani wenzake, umati mkubwa utaunganishwa na idadi kubwa sana ya watu watakaofufuliwa. (Ufunuo 20:12, 13) Watakuwa na nafasi ya kuwa raia wa kidunia wa Mfalme wa Kimasihi, Kristo Yesu, milele. Mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu, ‘vitu vyote hivyo vilivyo duniani’ vitakabili jaribu la mwisho. Wale watakaokuwa waaminifu watafanywa kuwa “watoto wa Mungu” duniani.—Waefeso 1:10; Waroma 8:21; Ufunuo 20:7, 8.

      17. Kusudi la Yehova litatimiaje?

      17 Hivyo, kupitia “usimamizi” wake wenye hekima isiyo na kifani au njia yake ya kusimamia mambo, Yehova atakuwa ametimiza kusudi lake la “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” Viumbe wote wenye akili mbinguni na duniani watakuwa wamekusanywa pamoja wakifurahia amani kila mahali, nao watajitiisha kwa shangwe chini ya utawala wenye uadilifu wa yule Mkusudiaji Mkuu, Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki