-
Kwa Nini Tupo Hapa?Amkeni!—2008 | Desemba
-
-
Kwa Nini Tupo Hapa?
Ni nini kusudi la uhai?
MARA nyingi watu wamejiuliza maswali yaliyo hapo juu. Pia wao hujiuliza: Je, kuna kusudi lingine isipokuwa kuishi kwa miaka 70 au 80 kisha tufe?—Zaburi 90:9, 10.
Huenda tukajiuliza maswali kama hayo hasa tunapotambua kwamba maisha yetu ni mafupi sana. Bila shaka, si lazima tuwe tunakabili hatari maishani ili kujiuliza kwa nini tupo hapa. Kukata tamaa pia kunaweza kutufanya tujiulize swali hilo. Na watu wengine hujiuliza swali hilo wanapotafakari juu ya maisha yao.
Dave alikuwa na kazi yenye mshahara mnono, nyumba nzuri, na alifurahia kuwa pamoja na marafiki wake. Anasema hivi: “Usiku mmoja nilikuwa nikirudi nyumbani kutoka kwenye sherehe nilipojiuliza swali hili, ‘Je, hili ndilo kusudi la uhai?—Je, nitaishi kwa muda mfupi tu kisha nife? Au je, kuna kusudi lingine?’ Jambo lililonisumbua ni kugundua sikuwa na kusudi maishani wakati huo.”
Katika kitabu chake Man’s Search for Meaning, Viktor Frankl alisema kwamba baada ya kuachiliwa kutoka katika kambi za mateso, baadhi ya waokokaji wenzake wa yale Maangamizi Makubwa waliuliza swali kama hilo. Waliporudi nyumbani, baadhi yao walikuta kwamba wapendwa wao walikuwa wameangamia. Frankl aliandika hivi: “Ole wake yule ambaye siku ya kuachiliwa, alikuta maisha yakiwa tofauti sana kuliko alivyotarajia!”
Watu Wanaouliza Swali Hilo
Swali kuhusiana na kusudi la uhai limeulizwa na watu katika vizazi vyote. Biblia inatuambia kuhusu watu waliotaka kujua maisha yana kusudi gani. Ayubu aliuliza hivi baada ya kupoteza mali na watoto wake na alipougua ugonjwa mbaya: “Kwa nini sikufa tokea tumbo la uzazi? Kwa nini sikutoka tumboni kisha nikate pumzi?”—Ayubu 3:11.
Nabii Eliya alihisi vivyo hivyo. Huku akihisi kwamba yeye ndiye mwabudu pekee wa Mungu, alilalamika hivi: “Inatosha! Sasa, Ee Yehova, iondoe nafsi yangu.” (1 Wafalme 19:4) Watu wengi sana wamehisi hivyo. Kwa kweli, Biblia inamfafanua Eliya kuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.”—Yakobo 5:17.
Safari Yenye Mafanikio Maishani
Maisha hulinganishwa na safari. Kama vile unavyoweza kuanza safari bila kufikiria utafika wapi, unaweza kuishi bila kutambua kusudi halisi la maisha. Ukifanya hivyo, utakuwa kama watu ambao mwandishi anayejulikana Stephen R. Covey anasema wanatafuta kusudi kwa kufanya maisha yawe yenye shughuli nyingi sana. Aliandika kuhusu wale ambao “wanapata mafanikio yasiyo na maana, mafanikio ambayo wamepata kwa kupoteza vitu ambavyo ghafula wanatambua vilikuwa vya muhimu zaidi kwao.”
Je, hukubali kwamba kuongeza mwendo katika safari ni bure ikiwa hatuelekei upande unaofaa? Vivyo hivyo, kutafuta kusudi maishani kwa kuwa na shughuli nyingi hakutaleta uradhi wa kweli.
Tamaa ya kujua kwa nini tupo hapa ni kawaida kwa watu wa utamaduni na umri mbalimbali. Inatokana na uhitaji muhimu ambao sote tunao, uhitaji wa kiroho ambao hauwezi kutoshelezwa hata baada ya mahitaji yetu ya kimwili kutimizwa. Hebu ona jinsi wengine wamejaribu kutosheleza uhitaji huo wanapotafuta kusudi la maisha.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Kutafuta kusudi maishani kwa kuwa na shughuli nyingi hakutaleta uradhi wa kweli
[Picha katika ukurasa wa 3]
Ayubu aliuliza kwa nini alizaliwa
[Picha katika ukurasa wa 4]
Eliya alikuwa na “hisia kama zetu”
-
-
Unaweza Kupata Wapi Majibu?Amkeni!—2008 | Desemba
-
-
Unaweza Kupata Wapi Majibu?
LENGO moja la dini ni kufundisha kuhusu kusudi la uhai. Hata hivyo, watu wengi wametambua kwamba mahitaji yao ya kiroho hayajatoshelezwa na mafundisho ya dini zao. Denise aliyelelewa na wazazi Wakatoliki, anakumbuka: “Katekisimu ya Baltimore inatia ndani swali hili, ‘Kwa nini Mungu alituumba?’ na inajibu hivi, ‘Mungu alituumba ili kuonyesha wema Wake na kushiriki nasi furaha Yake ya milele mbinguni.’
“Hilo halikunieleza ni kwa nini nipo hapa,” Denise anaendelea. “Ikiwa ninangojea tu kwenda mbinguni, ninapaswa kuwa nikifanya nini sasa?” Watu wengi wana mawazo kama ya Denise. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 66 hivi ya wale waliohojiwa wanaamini kwamba kanisa na masinagogi mengi hayawasaidii watu kupata kusudi maishani.
Kwa sababu hiyo, wanatafuta majibu kwingineko, iwe ni kupitia sayansi au falsafa za aina mbalimbali. Kwa nini watu wanaendelea kutafuta majibu, ingawa ni wachache tu wanaoonekana kupata uradhi?
Tuna Uhitaji wa Kiroho
Dakt. Kevin S. Seybold anasema kwamba kuna “mwelekeo wa wanadamu ulimwenguni pote wa kuabudu kitu fulani.” Katika miaka ya karibuni wanasayansi kadhaa wamefikia mkataa wa kwamba wanadamu wamezaliwa na mwelekeo wa kutafuta kusudi halisi maishani. Watu fulani wanaamini kwamba chembe za urithi na utendaji wa wanadamu unaonyesha kwamba wanadamu wana uhitaji wa asili wa kuwa na uhusiano na nguvu zisizo za kawaida.
Ingawa wasomi wanatilia shaka wazo la kwamba wanadamu wana uhitaji wa kiroho, watu wengi hawahitaji uchunguzi wa kisayansi ili waamini jambo hilo. Ni uhitaji huo wa kiroho ambao hufanya tujiulize yale ambayo watu fulani wameyaita maswali muhimu zaidi: Kwa nini tupo hapa? Tunapaswa kufanya nini na maisha yetu? Je, tunawajibika kwa Muumba Mweza-Yote?
Ukitenga wakati kuchunguza ulimwengu wa asili, utapata baadhi ya majibu ya maswali hayo. Kwa mfano, fikiria vitu vya asili vyenye kutatanisha, kuanzia viumbe vyenye chembe moja hadi makundi ya nyota yaliyo mbali sana angani. Je, havituonyeshi kwamba kuna Mbuni, au Muumba mwenye akili? Biblia inasema hivi: “Kwa maana sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.”—Waroma 1:20.
Tosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho
Biblia inasema hivi kuhusiana na jinsi Mungu alivyowaumba wanadamu: “Ameweka milele vilevile ndani ya mioyo yao.” (Mhubiri 3:11, Zaire Swahili Bible) Tumezaliwa na tamaa ya kuishi, si kufa. Tuna tamaa ya kupata kusudi la maisha, kujua majibu ya maswali.
Kwa hiyo, ni kawaida kwa wanadamu kuuliza maswali. Baada ya kutaja kuhusu maendeleo ya kisayansi na kitekinolojia, mhariri wa jarida The Wall Street Journal aliandika: “Bado tunajiuliza sisi ni nani na kwa nini tupo hapa na tunaelekea wapi.” Kwa hekima, tutatafuta majibu kutoka chanzo bora zaidi. Biblia inasema hivi kuhusu Chanzo hicho: “[Mungu] ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.”—Zaburi 100:3.
Je, haipatani na akili kumtazamia Yule aliyefanya miujiza kama ile ya uumbaji atosheleze uhitaji wetu wa kiroho? Yesu Kristo alipendekeza kwamba tufanye hivyo. Alitambua kwamba Muumba wetu ambaye ndiye Chanzo pekee cha uhai, anaweza kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho.—Zaburi 36:5, 9; Mathayo 5:3, 6.
Kwa kweli, kupata jibu linalotegemeka la swali hili, Kwa nini tupo hapa? ni muhimu ili kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho. Tafadhali fikiria maoni yenye kupendeza ya Muumba wetu kuhusu jambo hilo.
-
-
Sababu Tupo HapaAmkeni!—2008 | Desemba
-
-
Sababu Tupo Hapa
BIBLIA inaonyesha kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu, hatendi bila kusudi. Kwa mfano, fikiria uumbaji wake wa mzunguko wa maji unaoendeleza uhai duniani. Biblia inaufafanua hivi kwa usahihi: “Mito yote hutiririkia baharini, lakini bahari kamwe haijai; huko ambako mito hutiririkia ndiko huko inakotoka tena.”—Mhubiri 1:7, Biblia Habari Njema.
Biblia inalinganisha kutegemeka kwa ahadi za Mungu na mzunguko ambao umefafanuliwa. Kama tunavyojua leo, nguvu za jua hufanya maji yavukizwe kutoka katika bahari na maziwa, na baadaye yanarudi duniani kama mvua. Yehova anaelekeza fikira kwenye mzunguko huo na kueleza: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:10, 11.
Maji safi hurudi duniani kutoka kwenye mawingu ili kuendeleza uhai duniani. Vivyo hivyo, ‘neno linalotoka katika kinywa cha Mungu’ linaweza kuendeleza maisha yetu ya kiroho. Ni kama Yesu Kristo alivyoeleza: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.
Kula chakula cha kiroho kinachotoka kwa Mungu hutuwezesha kupatanisha maisha yetu na kusudi lake. Lakini, kabla ya kufanya hivyo, tunahitaji kuelewa kusudi la Mungu ni nini. Kwa mfano, kwa nini Mungu aliumba dunia? Na kusudi lake kwa dunia linatuhusu jinsi gani? Acheni tuone.
Kusudi la Mungu kwa Dunia
Kwa sababu Mungu anataka wanadamu wawe na maisha bora, alimweka mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, katika Edeni, bustani iliyokuwa paradiso. Kisha akawaagiza wazae, akiwaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”—Mwanzo 1:26-28; 2:8, 9, 15.
Tunaweza kukata kauli gani kutokana na maagizo hayo? Je, si wazi kwamba Mungu alitaka dunia yote igeuzwe kuwa paradiso kwa ajili ya wanadamu? Neno lake linasema: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.”—Zaburi 115:16.
Hata hivyo, ili wanadamu wapate utimizo wa kusudi la Mungu la kuishi duniani milele kwa furaha, wangehitaji kumheshimu Yehova kwa kumtii. Lakini je, Adamu alifanya hivyo? La, alifanya dhambi kwa kutomtii Mungu. Hilo lilikuwa na matokeo gani? Wazao wote wa Adamu, kutia ndani sisi sote leo, tumerithi dhambi na kifo, kama vile Biblia inavyosema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.
Kwa sababu hiyo, wanadamu wote wanakufa na dunia haijageuzwa kuwa paradiso. Basi, je, inawezekana kwamba kusudi la Mungu kwa dunia limebadilika?
La, kwa sababu Mungu alisema: “Neno langu linalotoka katika kinywa changu . . . halitarudi kwangu bila matokeo” bali “litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” Isitoshe, Mungu aliahidi: “Kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.” (Isaya 45:18; 46:10; 55:11) Na ni mapenzi ya Mungu, naam, ni kusudi lake, kwamba dunia yote iwe paradiso iliyojaa wanadamu wanaomtumikia milele kwa furaha, kama alivyokusudia mwanzoni.—Zaburi 37:29; Isaya 35:5, 6; 65:21-24; Ufunuo 21:3, 4.
Kusudi la Mungu Litatimia Jinsi Gani?
Yehova alionyesha hekima na upendo wake usio na kifani kwa kufanya maandalizi ili wanadamu wawekwe huru kutoka kwa dhambi waliyorithi na matokeo yake ambayo ni kutokamilika na kifo. Alifanya hivyo kwa kufanya mwana azaliwe ambaye hangerithi dhambi ambayo wote wamerithi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Uandalizi huo unaitwa fidia ambayo ilitolewa ili wanadamu wanaostahili wapate uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Waefeso 1:7; 1 Timotheo 2:5, 6) Fidia ilitolewa jinsi gani?
Malaika wa Yehova, Gabrieli, alimwambia mwanamke bikira aliyeitwa Maria kwamba angezaa mtoto kimuujiza, akamfafanulia jinsi angemzaa mtoto huyo hata ingawa ‘hakuwa akilala na mwanamume.’ Muujiza ambao Mungu alifanya ulikuwa kuhamisha uhai wa Mwana wake mzaliwa wa kwanza kutoka mbinguni hadi katika yai lililo katika tumbo la uzazi la Maria. Hivyo, akachukua mimba kupitia utendaji wa roho takatifu ya Mungu.—Luka 1:26-35.
Yesu alizaliwa miezi tisa hivi baadaye akiwa mwanadamu mkamilifu, kama tu mwanadamu wa kwanza, Adamu. Baada ya kuwa mtu mzima, alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu katika kifo cha kidhabihu. Kwa kufanya hivyo, Yesu alikuwa ‘Adamu wa pili’ na hivyo akaweka msingi kwa ajili ya wote ambao ni waaminifu kwa Mungu waweze kukombolewa kutoka kwa dhambi na kifo.—1 Wakorintho 15:45, 47.
Kwa kweli tunapaswa kuchochewa na upendo mwingi ambao Mungu ametuonyesha! Biblia inasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Swali ni, Tutaonyesha jinsi gani kwamba tunathamini upendo wa Mungu? Je, hatupaswi kuthamini zawadi yake? Fikiria mifano ya watu ambao wameonyesha uthamini wao.
Furahia Maisha Yenye Kusudi
Denise, aliyetajwa katika makala inayotangulia, aliona kwamba kuheshimu Mungu kwa kufuata sheria na maagizo yake kulifanya maisha yake yawe na kusudi. Anasema hivi: “Nilijifunza kutoka kwa Biblia kwamba licha ya kuwa na kusudi kwa ajili ya wanadamu litakalotimizwa wakati ujao, Mungu anataka waabudu wake wafanye kazi fulani hususa. Siwezi kuwazia maisha yenye kuridhisha kuliko kutumia uhuru wa kuchagua ambao amenipa ili nimtukuze kwa kuishi kulingana na kusudi lake.”
Tunaweza kufanya hivyo kwa kujifunza mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Ni kweli, hatujapata manufaa kamili za dhabihu ya fidia ambayo itatuwezesha tufurahie ukamilifu wa kibinadamu katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. Lakini kwa sasa, ni muhimu tutosheleze tamaa yetu ya kiroho ambayo Mungu ameweka ndani ya kila mmoja wetu.
Njaa ya kiroho ya Dave, aliyetajwa katika makala ya kwanza, ilitoshelezwa. Alipata majibu ya maswali yake kuhusu kusudi la uhai. “Nikitazama nyuma,” anasema, “ninaona kwamba maisha yangu kabla ya kujifunza kusudi la Mungu yalikuwa yamejaa jitihada zisizo na mafanikio. Wakati huo sikujua kwamba kukosa uradhi kulitokana na uhitaji wangu mwingi wa kiroho. Sasa sijihisi hivyo tena. Ninaelewa kwa nini nipo hapa na ninachopaswa kufanya maishani.”
Naam, tofauti na mawazo ya wanadamu wasio wakamilifu, maoni ya Mungu kuhusu kusudi la uhai kama yalivyoandikwa katika Biblia yanaridhisha kwelikweli. Tupo hapa kwa sababu ya kusudi la Yehova la kutuumba, yaani, tulitukuze jina lake, tuwe na uhusiano mzuri naye, na hivyo tutosheleze uhitaji wetu wa kiroho. Leo na kwa umilele wote, tunaweza kufurahia kutimizwa kwa maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zaburi 144:15.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
TATIZO LA KUTESEKA
Kuteseka kumesemwa kuwa ndilo tatizo kubwa zaidi linalofanya tusielewe kwa nini tupo hapa. Viktor Frankl alisema: “Ikiwa kuna kusudi la uhai, basi lazima kuwe na sababu inayotufanya tuteseke. Kuteseka ni sehemu ya maisha isiyoweza kuondolewa, kama tu majaliwa na kifo visivyoweza kuondolewa.”
Biblia inaeleza sababu inayotufanya tuteseke na kufa. Hatupaswi kumlaumu Mungu. Badala yake, tunapatwa na hali hizo kwa sababu ya uamuzi mbaya ambao wenzi wawili wa kwanza walifanya kwa kutomtegemea Muumba wao. Wazao wao wote wamerithi mwelekeo huo wa kufanya dhambi na ndiyo sababu wanadamu wanateseka.
Ingawa kuelewa kwa nini tupo hapa hakusuluhishi matatizo yote tunayokabili maishani, kunatupa msingi wa kukabiliana nayo. Pia, tunapata tumaini kwa ajili ya wakati ujao, wakati ambapo Mungu ataondoa kuteseka na kifo milele.
[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 7]
Biblia inalinganisha kutegemeka kwa ahadi za Mungu na mzunguko wa maji wenye kustaajabisha
[Mchoro]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mvua
Uvukizaji
Uvukizaji
Maziwa, Mto
Bahari
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba hatimaye dunia itakuwa paradiso iliyojaa watu wenye furaha na afya?
[Picha katika ukurasa wa 9]
‘Siwezi kuwazia maisha yenye kuridhisha kuliko kutumia uhuru wangu wa kuchagua kumtumikia Mungu.’—Denise
-