Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Vita Si Yenu Bali Ni ya Mungu”
    Amkeni!—2000 | Aprili 22
    • Pambano la Quebec

      Ingawa sasa uhuru wa kidini wa Mashahidi wa Yehova uliheshimiwa katika sehemu nyingi za Kanada, sehemu moja ilikuwa tofauti—jimbo la Kikatoliki la Kifaransa la Quebec. Jimbo hilo lilidhibitiwa moja kwa moja kwa zaidi ya miaka 300 na Kanisa Katoliki. Shule, hospitali, na huduma nyingi za umma ama ziliendeshwa na makasisi au kudhibitiwa nao. Hata kulikuwa na kiti cha kadinali wa Katoliki kando ya kiti cha spika katika bunge la Quebec!

      Waziri mkuu na mkuu wa sheria wa Quebec, Maurice Duplessis, alitumia mabavu, na kulingana na mwanahistoria wa Quebec Gérard Pelletier, alitesa jimbo hilo kwa “utawala wa miaka ishirini wa uwongo, ukosefu wa haki, ufisadi, uonevu wa hatua kwa hatua, kuwapotosha watu wenye akili finyu na kutukuza upumbavu.” Duplessis aliimarisha utawala wake wa kisiasa kwa kushirikiana bega kwa bega na Kadinali Mkatoliki Villeneuve.

      Mwanzoni mwa miaka ya 1940, kulikuwa na Mashahidi 300 katika Quebec. Wengi wao, kutia ndani ndugu yangu Joe, walikuwa mapainia kutoka sehemu nyingine za Kanada. Kazi ya kuhubiri ilipopamba moto katika Quebec, polisi wa jimbo hilo wakishinikizwa na makasisi, waliwasumbua Mashahidi kwa kuwakamata mara nyingi na kutumia vibaya sheria ndogo za kibiashara kwa utendaji wetu wa kidini.

      Nilikuwa nikisafiri kati ya Toronto na Quebec mara nyingi sana hivi kwamba hatimaye nilipewa mgawo wa kuhamia Quebec ili niwasaidie wanasheria wasio Mashahidi waliowakilisha ndugu na dada zetu Wakristo. Kila siku kazi yangu ya kwanza ilikuwa kujua ni wangapi waliokamatwa siku iliyotangulia na kwenda haraka mahakamani ili kushughulikia dhamana. Kwa uzuri, Frank Roncarelli, Shahidi aliyekuwa tajiri, alitoa dhamana katika kesi nyingi.

      Toka mwaka wa 1944 hadi 1946, idadi ya walioshtakiwa kwa tuhuma za kukiuka sheria za jimbo iliongezeka kutoka 40 hadi 800! Mbali na mamlaka za serikali kuwashika na kuwanyanyasa Mashahidi bila kukoma, vikundi vya wafanya-ghasia wafidhuli waliwashambulia pia, huku wakichochewa na makasisi Wakatoliki.

      Katika Novemba 2 na 3, mwaka wa 1946, mkutano wa pekee wa kushughulikia tatizo hilo ulifanywa huko Montreal. Ndugu Knorr alitoa hotuba ya mwisho, yenye kichwa “Tutafanya Nini?” Wahudhuriaji wote walifurahia jibu lake—alisoma kwa sauti ile trakti ya kihistoria ya Quebec’s Burning Hate for God and Christ and Freedom Is the Shame of All Canada. Ilikuwa trakti moto-moto yenye kurasa nne—ilitaja waziwazi majina, tarehe, na mahali pa ghasia zilizochochewa na makasisi, ukatili wa polisi, visa vya kutiwa mbaroni, na jeuri ya wafanya-ghasia dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Quebec. Ilisambazwa Kanada yote siku 12 tu baadaye.

      Baada ya siku chache, Duplessis alitangaza hadharani “vita isiyo na huruma” dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Lakini pasipo kujua alitusaidia. Jinsi gani? Kwa kuelekeza kwamba yeyote anayesambaza trakti ya Quebec’s Burning Hate ashtakiwe kwa kosa la uchochezi—kosa zito sana ambalo lingetufikisha kwenye Mahakama Kuu Zaidi ya Kanada kutoka kwa mahakama za Quebec. Duplessis mwenye hasira kali alipuuza tu matokeo hayo. Kisha yeye binafsi akaamuru leseni ya kuuza divai ya Frank Roncarelli ambaye alikuwa mdhamini wetu mkuu, ifutiliwe mbali. Mkahawa wenye faida wa Ndugu Roncarelli katika Montreal ulifungwa baada ya miezi michache kwa sababu ya ukosefu wa divai, naye akafilisika.

      Wengi walitiwa mbaroni. Idadi ya walioshtakiwa iliongezeka upesi kutoka 800 hadi 1,600. Wanasheria wengi na mahakimu walilalamika kwamba kesi za Mashahidi wa Yehova zilijaza mahakama za Quebec. Katika kujibu, tulidokeza utatuzi sahili: Acheni polisi washike wahalifu badala ya Wakristo. Kufanya hivyo kutatatua tatizo hilo!

      Wanasheria wawili Wayahudi walio jasiri, A. L. Stein wa Montreal na Sam S. Bard wa Quebec City, walitusaidia kwa kututetea katika kesi nyingi, hasa kabla sijapata kibali cha kuwa mshiriki wa baraza la wanasheria katika Quebec mnamo 1949. Pierre Elliott Trudeau, ambaye alikuja kuwa waziri mkuu wa Kanada baadaye, aliandika kwamba Mashahidi wa Yehova katika Quebec walikuwa “wamedhihakiwa, wamenyanyaswa, na kuchukiwa na jamii yetu yote, lakini wamefaulu kupambana kisheria na Kanisa, serikali, taifa, polisi, na maoni ya umma.”

      Mtazamo wa mahakama za Quebec ulidhihirishwa na jinsi ambavyo walimtendea ndugu yangu, Joe. Alishtakiwa kwa kosa la kuvuruga amani. Hakimu wa manispaa Jean Mercier alimhukumu Joe kifungo kikali cha siku 60 gerezani. Kisha, akashindwa kabisa kujizuia, akapaaza sauti akiwa kitini ya kwamba angeliweza angelimfunga Joe kifungo cha maisha gerezani!

      Gazeti moja lilisema kwamba Mercier aliwaamuru polisi wa Quebec “wamtie mbaroni mara moja kila Shahidi aliyejulikana au kutuhumiwa.” Zoea hilo lilithibitisha tu ukweli wa mashtaka yaliyokuwa katika trakti yetu ya Quebec’s Burning Hate. Vifuatavyo ni baadhi ya vichwa vilivyokuwa vya kawaida katika magazeti ya sehemu nyingine za Kanada mbali na Quebec: “Enzi za Giza Zarejea Quebec” (The Toronto Star), “Kurudi kwa Mabaraza ya Kuhukumu Wazushi” (The Globe and Mail, Toronto), “Kuzuka Tena kwa Ufashisti Mwovu” (The Gazette, Glace Bay, Nova Scotia).

      Kujitetea Dhidi ya Shtaka la Uchochezi

      Mnamo 1947, nilimsaidia Bw. Stein katika kesi yetu ya kwanza ya uchochezi, ya Aimé Boucher. Aimé alikuwa amesambaza trakti kadhaa ujiranini. Wakati wa kesi ya Aimé tulithibitisha kwamba trakti ya Quebec’s Burning Hate haikuwa na uwongo wowote bali ililaumu kwa maneno makali ukatili dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Tulisema kwamba wale waliotenda ukatili huo hawakushtakiwa. Aimé alipatikana na hatia kwa ajili tu ya kutangaza hadharani ukatili huo. Alishtakiwa kwa kosa moja tu: Kusema kweli lilikuwa kosa la jinai!

      Mahakama za Quebec zilitegemea ufasili usio yakini wa miaka 350 iliyopita wa “uchochezi,” ambao ulidokeza kwamba mtu yeyote anayechambua serikali aweza kushtakiwa kwa kosa la jinai. Duplessis pia alitegemea ufasili huo ili kukandamiza wachambuzi wa uongozi wake. Lakini katika mwaka wa 1950 Mahakama Kuu Zaidi ya Kanada ilikubali hoja yetu ya kwamba katika demokrasia ya kisasa, “uchochezi” huhusisha kuchochea jeuri au uasi dhidi ya serikali. Trakti ya Quebec’s Burning Hate haikuwa na uchochezi wa aina hiyo na kwa hiyo ilikuwa njia halali ya kujieleza kwa uhuru. Kwa uamuzi mmoja muhimu, kesi zote 123 za uchochezi zilifutiliwa mbali! Nilijionea binafsi jinsi ambavyo Yehova alitupatia ushindi.

      Kupambana na Ukaguzi wa Vichapo

      Quebec City lilikuwa na sheria iliyoharamisha usambazaji wa vichapo pasipo kibali cha mkuu wa polisi. Huu ulikuwa ukaguzi wa moja kwa moja na kwa hiyo ulikiuka uhuru wa kidini. Laurier Saumur, aliyekuwa mwangalizi asafiriye wakati huo, alikuwa amefungwa gerezani kwa miezi mitatu na alikabili mashtaka mengine kwa mujibu wa sheria hiyo.

      Mnamo mwaka wa 1947 kesi ya madai ilifunguliwa kwa jina la Ndugu Saumur ili kuzuia Quebec City kutumia sheria yake dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Mahakama za Quebec City ziliamua dhidi yetu, na tukakata rufani tena katika Mahakama Kuu Zaidi ya Kanada. Katika Oktoba 1953, baada ya siku saba za kusikizwa kwa kesi mbele ya mahakimu tisa wa Mahakama hiyo, ombi letu la amri ya kuzuia Quebec lilikubaliwa. Mahakama ilitambua kwamba kusambazwa hadharani kwa vichapo vya Biblia ni sehemu muhimu ya ibada ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova na hivyo vimelindwa kisheria dhidi ya ukaguzi.

      Kwa hiyo, uamuzi wa kesi ya Boucher ulionyesha kwamba mambo waliyosema Mashahidi wa Yehova yalifaa kisheria; lakini uamuzi wa kesi ya Saumur ulidhihirisha namna na mahali yanapopasa kusemwa. Ushindi katika kesi ya Saumur ulifanya kesi 1,100 za mashtaka ya sheria ya Quebec zifutiliwe mbali. Zaidi ya kesi 500 huko Montreal pia zilifutiliwa mbali kwa sababu ya kukosekana kabisa kwa ushahidi. Muda si muda mashtaka yote yalifutiliwa mbali—hakukuwa na mshtakiwa yeyote katika Quebec!

      Shambulizi la Mwisho la Duplessis

      Duplessis alipokosa sheria yoyote ya kutumia dhidi ya Mashahidi wa Yehova, alitunga sheria mpya bungeni mapema Januari mwaka wa 1954, Mswada nambari 38, ulioitwa na vyombo vya habari ‘sheria dhidi ya Mashahidi wa Yehova.’ Ilitaarifu kwamba yeyote aliyeshuku kwamba mtu fulani alinuia kusema jambo lenye “matusi au lenye kuudhi” angeweza kuwasilisha lalamiko lake bila uthibitisho. Akiwa mkuu wa sheria, Duplessis angeweza kupokea idhini ya kumzuia mshtakiwa kutoa taarifa yoyote hadharani. Mara baada ya kumwekea vikwazo mtu mmoja, washiriki wote wa kanisa analoshirikiana nalo wangezuiwa pia kusema hadharani. Isitoshe, Biblia zote na vichapo vya kidini vya kanisa hilo vingechukuliwa na kuharibiwa, na sehemu zote za ibada zingefungwa hadi kesi hiyo ilipoamuliwa, labda baada ya miaka mingi.

      Mswada nambari 38 ulifanana na sheria iliyotungwa katika karne ya 15 wakati wa Baraza la Hispania la Kuhukumu Wazushi chini ya Torquemada. Mshtakiwa na washiriki wake wote walinyimwa haki zote za raia pasipo uthibitisho wa kosa. Kuhusu Mswada nambari 38, vyombo vya habari vilitangaza kwamba polisi wa jimbo hilo walikuwa wameamriwa wafunge Majumba yote ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova na kukusanya na kuharibu Biblia zao na vichapo vingine. Wakikabili tisho hilo la kuogofya, Mashahidi wa Yehova walihamisha vichapo vyao vya kidini vyote kutoka katika jimbo hilo. Hata hivyo, waliendelea na kazi yao ya kuhubiri peupe lakini walitumia nakala zao binafsi za Biblia tu.

      Mswada huo ukawa sheria katika Januari 28, 1954. Katika Januari 29, saa tatu asubuhi, nilifika mahakamani ili nifungue madai kwa niaba ya Mashahidi wa Yehova katika jimbo la Quebec, na kuomba mahakama itoe amri ya kukomesha kabisa hiyo sheria kabla Duplessis hajaitekeleza. Hakimu hakutoa amri ya kuikomesha kwa muda kwa sababu Mswada nambari 38 haukuwa umetekelezwa bado. Lakini alisema kwamba endapo serikali itajaribu kuutumia, ningeweza kumfikia ili nipate ulinzi. Kwa hiyo uamuzi wa hakimu huyo ulikomesha sheria hiyo kwa muda, kwa kuwa Duplessis angezuiwa mara moja kujaribu kutumia sheria hiyo!

      Juma lililofuata, tulisubiri kuona iwapo polisi wangetekeleza sheria hiyo mpya. Hawakuchukua hatua yoyote! Ili kujua sababu, nilipanga kuwajaribu. Mapainia wawili, Victoria Dougaluk (baadaye aliitwa Steele) na Helen Dougaluk (baadaye aliitwa Simcox), walienda nyumba kwa nyumba wakiwa na vichapo huko Trois-Rivières, alikozaliwa Duplessis. Kwa mara nyingine polisi hawakufanya lolote. Dada hao walipokuwa wakihubiri, nilimtuma Laurier Saumur awapigie simu polisi wa jimbo. Pasipo kujitambulisha, alilalamika kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakihubiri na kwamba polisi hawakuwa wakitekeleza sheria mpya ya Duplessis.

      Kwa aibu, ofisa huyo msimamizi akasema: “Naam, twajua kwamba sheria hiyo ilipitishwa; lakini siku iliyofuata Mashahidi wa Yehova waliomba mahakama ituzuie kuitekeleza, kwa hiyo hatuwezi kufanya lolote.” Mara moja, tulirejesha vichapo vyetu kwenye jimbo, na katika miaka kumi ya kusikizwa kwa rufani ya kesi yetu, kazi yetu ya kuhubiri iliendelea kwa mafanikio.

      Pamoja na kuomba amri ya kukomesha sheria hiyo, tuliomba pia Mswada nambari 38 utangazwe kuwa kinyume cha katiba. Ili kuthibitisha kwamba sheria hiyo ilitungwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova hasa, tuliamua kuchukua hatua madhubuti—tulimtumia Duplessis hati ya kumwita mahakamani, iliyombidi ahudhurie na kutoa ushahidi wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo. Nilimhoji kwa saa mbili na nusu. Mara kwa mara nilimwuliza kuhusu tangazo lake la hadharani la “vita isiyo na huruma dhidi ya Mashahidi wa Yehova” na taarifa yake ya kwamba Mswada nambari 38 ungewakomesha Mashahidi wa Yehova katika Quebec. Kwa hasira kali, alinishambulia: “Wewe ni kijana mfidhuli sana!”

      “Bw. Duplessis,” nikamjibu, “kama tungekuwa tunazungumzia sifa za watu, singesema mengi kuhusu utu wako. Lakini kwa kuwa tunashughulikia mambo mazito sana, waweza kueleza mahakama kwa nini hukujibu swali la mwisho nililokuuliza.”

      Mnamo mwaka wa 1964, niliwasilisha Mswada nambari 38 mbele ya Mahakama Kuu Zaidi ya Kanada. Lakini walikataa kuamua kuhusu kuwa kwake kinyume cha katiba kwa sababu sheria hiyo haikuwahi kutumiwa. Hata hivyo, wakati huo Duplessis alikuwa amekufa, na hakuna mtu aliyejali tena Mswada nambari 38. Haukuwahi kutumiwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova wala mtu mwingine yeyote.

      Muda mfupi kabla ya kifo chake mnamo 1959, Duplessis aliamriwa na Mahakama Kuu Zaidi ya Kanada amlipe ridhaa Ndugu Roncarelli kwa sababu ya kufuta kwa njia isiyo halali leseni yake ya kuuza divai. Tangu wakati huo wengi wa wakazi wa Quebec wamekuwa na urafiki mno. Kulingana na hesabu ya serikali, idadi ya Mashahidi huko imeongezeka toka 300 mwaka wa 1943 hadi zaidi ya 33,000 leo. Sasa Mashahidi wa Yehova wameorodheshwa kuwa kikundi cha nne cha kidini kwa ukubwa katika jimbo hilo. Mimi sioni ushindi huo wa kisheria au mafanikio ya huduma ya Mashahidi wa Yehova kuwa ushindi wa mwanadamu yeyote. Badala yake, umenithibitishia kwamba Yehova hutoa ushindi, kwa kuwa vita si yetu bali ni yake.—2 Mambo ya Nyakati 20:15.

  • “Vita Si Yenu Bali Ni ya Mungu”
    Amkeni!—2000 | Aprili 22
    • Pierre Elliott Trudeau, ambaye alikuja kuwa waziri mkuu wa Kanada baadaye, aliandika kwamba Mashahidi wa Yehova katika Quebec walikuwa “wamedhihakiwa, wamenyanyaswa, na kuchukiwa na jamii yetu yote, lakini wamefaulu kupambana kisheria na Kanisa, serikali, taifa, polisi, na maoni ya umma.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki