-
Mwige Mfanya-wanafunzi MkuuMnara wa Mlinzi—2007 | Novemba 15
-
-
Yesu Aliwatia Wengine Moyo Wazungumze
4. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa msikilizaji mzuri?
4 Tangu akiwa mtoto, Yesu alikuwa na desturi ya kuwasikiliza watu na kuwatia moyo watoe maoni yao. Kwa mfano, alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake walimkuta katikati ya walimu hekaluni, “akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” (Luka 2:46) Yesu hakwenda hekaluni ili kuwaaibisha walimu kwa ujuzi wake. Alienda huko ili kusikiliza, ingawa pia aliuliza maswali. Mwelekeo wake wa kusikiliza vizuri huenda ni moja ya sifa zilizomfanya apate kibali cha Mungu na wanadamu.—Luka 2:52.
5, 6. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu aliwasikiliza wale ambao aliwafundisha?
5 Baada ya kubatizwa na kutiwa mafuta awe Masihi, Yesu aliendelea kuwasikiliza watu. Hakuwa mwenye shughuli nyingi sana za kuwafundisha watu hivi kwamba akawasahau wale waliokuja kumsikiliza. Mara nyingi, alitua kidogo, aliwauliza maoni yao, na kusikiliza majibu yao. (Mathayo 16:13-15) Kwa mfano, baada ya kifo cha Lazaro, ndugu ya Martha, Yesu alimwambia Martha hivi: “Kila mtu aliye hai na ananiamini hatakufa kamwe.” Kisha akamuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Na bila shaka Yesu alisikiliza Martha alipomjibu hivi: “Ndiyo, Bwana; nimeamini kwamba wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu.” (Yohana 11:26, 27) Ilipendeza kama nini kumsikia Martha akieleza imani yake kwa njia hiyo!
6 Wanafunzi wengi walipomwacha Yesu, yeye alitaka kujua maoni ya mitume wake. Hivyo aliuliza hivi: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Simoni Petro akamjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.” (Yohana 6:66-69) Maneno hayo yalimfurahisha Yesu kama nini! Bila shaka, maneno kama hayo ya imani kutoka kwa mwanafunzi wa Biblia yatakufurahisha wewe pia.
Yesu Alisikiliza kwa Heshima
7. Kwa nini Wasamaria wengi walimwamini Yesu?
7 Sababu nyingine iliyomfanya Yesu awe na matokeo mazuri katika kazi ya kufanya wanafunzi ni kwamba aliwajali watu na kuwasikiliza kwa heshima. Kwa mfano, pindi moja Yesu alimhubiria mwanamke Msamaria karibu na chemchemi ya Yakobo huko Sikari. Wakati wa mazungumzo hayo, Yesu hakuzungumza tu; alimsikiliza mwanamke huyo. Alipokuwa akimsikiliza, Yesu alitambua kwamba alipendezwa na ibada na akamwambia kwamba Mungu alikuwa akitafuta watu ambao wangemwabudu kwa roho na kweli. Yesu alimheshimu na kumhangaikia mwanamke huyo, na hivyo mwanamke huyo akawaambia wengine kumhusu Yesu, na “wengi wa Wasamaria kutoka jiji hilo walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke.”—Yohana 4:5-29, 39-42.
8. Mwelekeo wa watu wa kutaka kutoa maoni yao unaweza kukusaidia jinsi gani kuanzisha mazungumzo katika huduma?
8 Kwa kawaida, watu wanafurahia kutoa maoni yao. Kwa mfano, wakaaji wa kale wa Athene walifurahia kutoa maoni yao na kusikiliza mambo mapya. Hilo lilimwongoza mtume Paulo kutoa hotuba iliyokuwa na matokeo mazuri kwenye Areopago katika jiji hilo. (Matendo 17:18-34) Unapoanza mazungumzo pamoja na mwenye nyumba katika huduma yako leo, unaweza kusema, “Ninakutembelea kwa sababu ningependa kujua maoni yako kuhusu [habari fulani].” Sikiliza maoni ya mtu huyo, na useme jambo fulani kuhusu maoni yake, au uliza swali kuhusu maoni hayo. Kisha, kwa fadhili mwonyeshe yale ambayo Biblia inasema juu ya habari hiyo.
Yesu Alijua Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo
9. Yesu alifanya nini kabla ya ‘kuwafungulia Maandiko’ Kleopa na msafiri mwenzake?
9 Yesu hakukosa kamwe jambo la kusema. Zaidi ya kuwa msikilizaji mzuri, mara nyingi Yesu alijua yale ambayo watu walikuwa wakifikiri, na alijua ni nini hasa alipaswa kusema. (Mathayo 9:4; 12:22-30; Luka 9:46, 47) Kwa mfano: Muda mfupi baada ya ufufuo wa Yesu, wanafunzi wawili walikuwa wakisafiri kwa miguu kutoka Yerusalemu kwenda Emau. Simulizi la Injili linasema hivi: “Walipokuwa wakiongea na kujadiliana, Yesu akakaribia, akaanza kutembea pamoja nao; lakini macho yao yalizuiwa wasiweze kumtambua. Akawaambia: ‘Ni mambo gani haya ambayo mnajadiliana kati yenu wenyewe mnapotembea?’ Nao wakasimama tuli wakiwa na nyuso zenye huzuni. Yule aliyeitwa Kleopa akajibu, akamwambia: ‘Je, wewe unakaa peke yako kama mgeni katika Yerusalemu na kwa hiyo huyajui mambo ambayo yametukia humo siku hizi?’ Naye akawaambia: ‘Mambo gani?’” Mwalimu Mkuu aliwasikiliza walipokuwa wakieleza kwamba Yesu Mnazareti aliwafundisha watu, alifanya miujiza, na aliuawa. Sasa watu wengine walikuwa wakisema kwamba alifufuliwa kutoka kwa wafu. Yesu alimwacha Kleopa na msafiri mwenzake wajieleze. Kisha, akawaeleza mambo waliyohitaji kujua, ‘akawafungulia Maandiko.’—Luka 24:13-27, 32.
10. Unaweza kujua jinsi gani maoni ya kidini ya mtu unayekutana naye katika huduma yako?
10 Huenda usijue jambo lolote kuhusu maoni ya kidini ya mwenye nyumba fulani. Ili kujua maoni yake, labda unaweza kusema kwamba ungependa kusikia yale ambayo watu wanafikiri kuhusu sala. Kisha unaweza kuuliza, “Je, unafikiri kweli kuna yeyote anayesikiliza sala?” Huenda jibu utakalopewa litafunua mengi kuhusu maoni ya mtu huyo na malezi yake ya kidini. Ikiwa anapendezwa na mambo ya kidini, huenda ukajua mengi zaidi kuhusu maoni yake kwa kuuliza, “Je, unafikiri Mungu anasikiliza sala zote, au huenda kuna sala nyingine ambazo hasikilizi?” Maswali kama hayo yanaweza kuongoza kwenye mazungumzo mazuri. Ikiwa inafaa kumwonyesha yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo, utahitaji kufanya hivyo kwa busara, lakini hupaswi kushambulia imani ya mtu huyo. Ikiwa anafurahia kukusikiliza, huenda akataka umrudie. Lakini namna gani akiuliza swali ambalo huwezi kujibu? Unaweza kufanya utafiti fulani na kurudi ukiwa tayari kumtolea ‘sababu ya tumaini lililo ndani yako, lakini ukifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.’—1 Petro 3:15.
-
-
Mwige Mfanya-wanafunzi MkuuMnara wa Mlinzi—2007 | Novemba 15
-
-
13. Ni nini kinachoweza kukusaidia kutambua maoni ya mtu kuhusu Biblia?
13 Unaweza jinsi gani kuwatia watu moyo wakueleze maoni yao kuhusu Neno la Mungu? Katika maeneo fulani, swali hili linafaa, “Je, unaona ni vigumu kuielewa Biblia?” Mara nyingi, jibu la swali hilo linafunua mtazamo wa mtu kuelekea mambo ya kiroho. Njia nyingine ni kusoma andiko na kuuliza, “Una maoni gani kuhusu hilo?” Kama Yesu, unaweza kutimiza mengi katika huduma yako kwa kutumia maswali vizuri. Hata hivyo, ni vizuri kuwa mwangalifu.
Yesu Alitumia Maswali Vizuri
14. Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unapendezwa na maoni ya watu bila kuwahoji?
14 Pendezwa na maoni ya wengine bila kuwaaibisha. Iga njia za Yesu. Hakuuliza maswali bila busara, lakini aliuliza maswali ambayo yalichochea fikira. Pia, Yesu alikuwa msikilizaji mwenye fadhili ambaye aliwaburudisha watu wanyoofu na kuwafanya wastarehe. (Mathayo 11:28) Watu wa aina zote walijihisi huru kuzungumza naye kuhusu matatizo yao. (Marko 1:40; 5:35, 36; 10:13, 17, 46, 47) Ukitaka watu wajisikie huru kukueleza maoni yao kuhusu Biblia na mafundisho yake, unapaswa kuepuka kuwahoji.
15, 16. Unaweza kuanzisha jinsi gani mazungumzo na watu kuhusu mambo ya kidini?
15 Zaidi ya kutumia maswali vizuri, unaweza kumtia mtu moyo azungumze kwa kusema jambo fulani lenye kupendeza na kisha kusikiliza itikio lake. Kwa mfano, Yesu alimwambia Nikodemo hivi: “Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Maneno hayo yalikuwa yenye kuvutia sana hivi kwamba Nikodemo hangejizuia kuitikia na kumsikiliza Yesu. (Yohana 3:4-20) Wewe pia unaweza kuanzisha mazungumzo na watu kwa njia kama hiyo.
16 Leo, kutokea kwa dini nyingi mpya ni habari inayowavutia watu wengi barani Afrika, Ulaya Mashariki, na Amerika ya Latini. Katika maeneo kama hayo, mara nyingi unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema hivi: “Sielewi kwa nini kuna dini nyingi mno. Lakini ninatumaini kuona hivi karibuni watu kutoka katika mataifa yote wakiunganishwa katika ibada ya kweli. Je, ungependa kuona jambo hilo likitukia?” Kwa kusema jambo fulani lenye kushangaza kuhusu tumaini lako, unaweza kuwachochea watu watoe maoni yao. Ni rahisi watu kujibu maswali wanapopewa nafasi ya kuchagua kati ya majibu mawili. (Mathayo 17:25) Baada ya mwenye nyumba kujibu swali lako, jibu swali hilo kwa kutumia andiko moja au mawili. (Isaya 11:9; Sefania 3:9) Ukimsikiliza kwa makini na kufikiria jibu lake, unaweza kujua yale mtakayozungumzia utakaporudi.
-