Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
    • JINSI YEHOVA ALIVYOANDAA FIDIA

      9. Ni fidia ya aina gani iliyohitajiwa?

      9 Kwa kuwa uhai mkamilifu wa kibinadamu ulipotea, hakuna mwanadamu yeyote asiye mkamilifu angeweza kuurudisha. (Zaburi 49:7, 8) Kilichohitajiwa ni fidia yenye thamani inayolingana na kilichopotezwa. Hilo linapatana na kanuni hii ya haki kamilifu inayopatikana katika Neno la Mungu: “Nafsi itakuwa kwa nafsi.” (Kumbukumbu la Torati 19:21) Kwa hiyo, ni nini kingeweza kulipia thamani ya nafsi au uhai mkamilifu wa kibinadamu uliopotezwa na Adamu? Kilichohitajiwa ni “fidia inayolingana” ya uhai mwingine mkamilifu wa kibinadamu. —1 Timotheo 2:6.

      10. Yehova aliandaaje fidia?

      10 Yehova aliandaaje fidia? Alimtuma mmoja kati ya wana wake wakamilifu wa kiroho aje duniani. Lakini Yehova hakutuma kiumbe yeyote tu wa roho. Alimtuma yule aliyempenda sana, Mwana wake mzaliwa-pekee. (1 Yohana 4:9, 10) Mwana huyo alikubali kwa hiari kuacha makao yake mbinguni. (Wafilipi 2:7) Kama tulivyojifunza katika Sura ya 4 ya kitabu hiki, Yehova alifanya muujiza alipohamisha uhai wa Mwana huyo na kuutia katika tumbo la Maria. Kupitia roho takatifu ya Mungu, Yesu alizaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu wala hakuwa chini ya laana ya dhambi.—Luka 1:35.

      Yesu ametundikwa juu ya mti wa mateso akifa kifo chenye maumivu makali

      Yehova alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee awe fidia kwa ajili yetu

      11. Mtu mmoja angewezaje kuwa fidia kwa ajili ya mamilioni ya watu?

      11 Mtu mmoja angewezaje kuwa fidia kwa ajili ya watu wengi, mamilioni ya wanadamu? Kwanza, mamilioni hayo ya wanadamu walipataje kuwa wenye dhambi? Kumbuka kwamba kwa kufanya dhambi Adamu alipoteza uhai mkamilifu wa kibinadamu wenye thamani sana. Kwa hiyo, hangeweza kuwapitishia wazao wake uhai huo mkamilifu. Badala yake aliwapitishia dhambi na kifo tu. Yesu, ambaye Biblia inamwita “Adamu wa mwisho,” alikuwa na uhai mkamilifu wa kibinadamu wala hakufanya dhambi kamwe. (1 Wakorintho 15:45) Hivyo, Yesu alichukua mahali pa Adamu ili atuokoe. Yesu alilipia dhambi ya Adamu kwa kudhabihu uhai wake mkamilifu na kumtii Mungu kikamili. Hivyo, Yesu akawapa wazao wa Adamu tumaini.—Waroma 5:19; 1 Wakorintho 15:21, 22.

      12. Kuteseka kwa Yesu kulithibitisha nini?

      12 Biblia inaeleza kinaganaga kuhusu mateso ambayo Yesu alivumilia kabla ya kufa. Alipigwa mijeledi, akatundikwa kikatili, na kufa kwa maumivu makali juu ya mti wa mateso. (Yohana 19:1, 16-18, 30; Nyongeza “Kwa Nini Wakristo wa Kweli Hawatumii Msalaba Katika Ibada?”) Kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke sana hivyo? Baadaye tutaona kwamba Shetani alitilia shaka ikiwa Yehova ana watumishi wa kibinadamu wanaoweza kumtumikia kwa uaminifu chini ya majaribu. Kwa kuvumilia kwa uaminifu licha ya mateso makali, Yesu alijibu madai ya Shetani kwa njia bora zaidi. Yesu alithibitisha kwamba mwanadamu mkamilifu aliye na uhuru wa kuchagua anaweza kumtii Mungu kikamili hata Ibilisi afanye nini. Haikosi kwamba Yehova alifurahishwa sana na uaminifu wa Mwana wake mpendwa!—Methali 27:11.

      13. Fidia ililipwaje?

      13 Fidia ililipwaje? Mungu aliruhusu Mwana wake mkamilifu asiye na dhambi auawe katika siku ya 14 ya mwezi wa Kiyahudi unaoitwa Nisani, mwaka wa 33 W.K. Hivyo, Yesu alidhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu “mara moja kwa wakati wote.” (Waebrania 10:10) Siku ya tatu baada ya Yesu kufa, Yehova alimfufua na kumrudisha kwenye uhai wa roho. Akiwa mbinguni, Yesu alimpa Mungu thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uliotolewa dhabihu kama fidia kwa ajili ya wazao wa Adamu. (Waebrania 9:24) Yehova alikubali thamani ya dhabihu ya Yesu kama fidia ya kuwakomboa wanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo.—Waroma 3:23, 24.

  • Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki