-
BurudaniMaswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SEHEMU YA 8
Burudani
Ni mara ngapi wewe hujifurahisha kwa mambo kama vile michezo, muziki, sinema, kutazama televisheni, au michezo ya kompyuta?
□ Mara chache sana
□ Mara moja kwa siku
□ Mara kadhaa kwa siku
Maamuzi yako kuhusu burudani hutegemea nani au nini hasa?
□ Vijana wenzako
□ Mzazi (wazazi) wako
□ Matangazo ya biashara
Tofauti na ilivyokuwa zamani, leo kuna tafrija nyingi zaidi ambazo wewe na vijana wenzako mnaweza kufurahia. Hata hivyo, bado siku zina saa 24 tu. Tafrija unayochagua inaweza kuathiri kufikiri kwako na mtazamo wako. Basi, ni kiasi gani cha wakati kinachofaa kutumiwa katika tafrija? Nawe unaweza kuamuaje tafrija inayofaa? Sura ya 30-33 zitakusaidia kufikiria kwa makini jinsi unavyochagua tafrija.
-
-
Nicheze Michezo ya Kompyuta?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 30
Nicheze Michezo ya Kompyuta?
“MICHEZO ya kompyuta inasisimua na inapendwa sana,” anasema kijana anayeitwa Brian. “Katika michezo hiyo, unafanya mambo ambayo kwa kawaida hungefanya maishani kwa sababu kuyafanya kihalisi kungekuingiza katika matata.” Deborah anasema kwamba yeye pia hupenda kucheza michezo ya kompyuta. Hata hivyo, anaongeza tahadhari hii: “Inaweza kuchukua wakati mwingi, hata kuwa uraibu.”
Bila shaka, michezo ya kompyuta si burudani ya hali ya juu tu. Inahusisha akili yako na huondolea mbali uchovu. Si hayo tu. Michezo ya kompyuta inaweza kukufanya uwe chapuchapu. Mingine inaweza hata kuboresha uwezo wako wa kufanya hesabu na kusoma. Isitoshe, wakati wa mapumziko, karibu kila mwanafunzi huzungumzia michezo ya karibuni zaidi ya kompyuta. Ikiwa umeicheza, utakuwa na jambo la kuchangia katika mazungumzo hayo.
Bila shaka, ukichagua kwa uangalifu, unaweza kupata michezo isiyokiuka kanuni za Kikristo, na wakati uleule yenye kusisimua. Hata hivyo, kwa nini unahitaji kuwa mwangalifu?
Hatari za Michezo ya Kompyuta
Inasikitisha kwamba si michezo yote ya kompyuta inafaa. Michezo mingi ya kompyuta siku hizi inaunga mkono mambo ambayo katika Biblia yanatajwa kuwa “matendo ya mwili,” yaani, mazoea machafu ambayo Mungu anashutumu.—Wagalatia 5:19-21.
Adrian, mwenye umri wa miaka 18, anasema kwamba mchezo unaopendwa na kuuzwa sana umejaa “vita, matumizi ya dawa za kulevya, habari chafu za ngono, lugha chafu, jeuri kali, umwagaji wa damu, na mambo mengine ya kikatili.” Michezo mingine inatukuza kuwasiliana na pepo. Na kila mchezo mpya unaotokea hufanya ile ya zamani ionekane kuwa duni sana. Mingi ya michezo hiyo inaweza kuchezwa pamoja na watu wengine kupitia Intaneti. Kucheza na watu wengine hufanya michezo hiyo ipendeze na kusisimua hata zaidi. James mwenye miaka 19 anasema: “Ukiwa nyumbani, unaweza kucheza na watu wanaoishi katika nchi nyingine za mbali, katika Intaneti.”
Michezo ya Intaneti ambayo kila mchezaji anakuwa mhusika katika mchezo huo, inapendwa na wengi. Katika michezo hiyo, kila mchezaji hubuni mhusika. Mhusika huyo anaweza kuwa mtu, mnyama, au nusu mtu nusu mnyama. Wahusika hao huishi na kutenda katika ulimwengu uliobuniwa wenye maelfu ya wachezaji wengine. Ulimwengu huo uliobuniwa una maduka, magari, nyumba, majumba ya dansi, madanguro, kwa ujumla ni kama ulimwengu halisi. Wachezaji wanaweza kuwasiliana wao kwa wao kwa kutumiana ujumbe mfupi huku wahusika wao waliobuniwa wakiendelea na shughuli zao katika mchezo huo.
Vikundi vya majambazi, wanaume wanaowatongoza makahaba, makahaba, wanyang’anyi, walaghai, na wauaji, ni baadhi tu ya waigizaji katika michezo hiyo. Wachezaji wanaweza kujiingiza katika mambo ambayo hawangeweza kamwe kuyafanya maishani. Kwa kubofya tu kibodi, wahusika hao waliobuniwa wanaweza kuanza kufanya ngono huku wachezaji wenyewe wakizungumzia ngono kwa kutumiana ujumbe mfupi. Michezo fulani huwawezesha wahusika waliobuniwa kufanya ngono na wahusika wengine wanaofanana na watoto. Wachambuzi wanashangazwa kwamba watu wanaweza kutengeneza michezo kutokana na mambo mapotovu hivyo.
Kuchagua Michezo Hiyo Ni Jambo Zito
Wale wanaocheza michezo hiyo yenye jeuri na inayoonyesha ngono waziwazi huenda wakasema: “Hakuna madhara yoyote. Si mambo halisi. Ni mchezo tu.” Lakini usidanganyike!
Biblia inasema: “Kwa matendo yake, mvulana hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” (Methali 20:11) Ikiwa unacheza michezo yenye jeuri na matendo mapotovu, unaweza kuitwa mtu aliye safi na mnyoofu? Uchunguzi umeonyesha tena na tena kwamba kutazama burudani zenye jeuri huwafanya watazamaji wawe wakatili. Wachunguzi fulani wamesema kwamba kwa sababu Intaneti huwawezesha watu kushirikiana, michezo ya kompyuta inaweza kuwa na madhara makubwa kuliko televisheni.
Kuamua kucheza michezo ya kompyuta yenye jeuri au matendo mapotovu ni kama kucheza na vitu vyenye miale hatari. Huenda madhara yasionekane mara moja, lakini muda si muda, athari zake zitaonekana. Jinsi gani? Kuwa mahali penye miale mingi kama hiyo kunaweza kuharibu sehemu ya ndani ya tumbo na hivyo kuruhusu bakteria kwenye utumbo kuingia katika damu na kusababisha ugonjwa. Vivyo hivyo, kucheza kwa muda mrefu michezo inayoonyesha jeuri na ngono waziwazi kunaweza kuharibu ‘ufahamu wako wa maadili’ na kuruhusu tamaa za mwili ziingie na kutawala fikira na matendo yako.—Waefeso 4:19; Wagalatia 6:7, 8.
Nichague Mchezo Gani?
Ikiwa wazazi wako wanakuruhusu ucheze michezo ya kompyuta, utajuaje mchezo unaoweza kuchagua na muda utakaotumia kuucheza? Jiulize maswali yafuatayo:
Uchaguzi wangu utamfanya Yehova anioneje? “Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu, na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia,” yasema Zaburi 11:5. Kuhusu wale wanaojiingiza katika mazoea ya kuwasiliana na pepo, Neno la Mungu linasema: “Kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Ikiwa unataka kuwa rafiki ya Mungu, unahitaji kufuata shauri hili katika Zaburi 97:10: ‘Chukia yaliyo mabaya.’
Mchezo huo utaathiri jinsi gani kufikiri kwangu? Jiulize, ‘Je, kucheza michezo hiyo kutafanya iwe rahisi au vigumu kwangu “[kuukimbia] uasherati”?’ (1 Wakorintho 6:18) Michezo yenye picha au mazungumzo yanayoamsha tamaa ya ngono haiwezi kukusaidia kukazia fikira mambo yaliyo ya uadilifu, safi kiadili, na wema wa adili.—Wafilipi 4:8.
Nitacheza kwa muda gani? Hata mchezo unaofaa unaweza kuchukua muda mwingi sana. Basi weka rekodi ya muda unaotumia kucheza. Je, unapoteza wakati ambao ungetumia kufanya mambo ya maana zaidi? Kuona mahali unapopotezea wakati kutakusaidia kutanguliza mambo yaliyo ya maana zaidi.—Waefeso 5:16.
Ni kweli kwamba Biblia haisemi kwamba utumie wakati wako wote kujifunza na kufanya kazi. Badala yake, inatukumbusha sote kwamba kuna “wakati wa kucheka . . . na wakati wa kurukaruka.” (Mhubiri 3:4) Hata hivyo, kumbuka kwamba neno “kurukaruka” linatia ndani mazoezi ya mwili pia bali si kucheza michezo ya kompyuta tu. Basi, kwa nini usitumie wakati wako kucheza michezo inayohusisha mazoezi ya mwili badala ya kuketi tu na kucheza kwenye kompyuta au televisheni?
Chagua kwa Hekima
Bila shaka, kucheza michezo ya kompyuta kunaweza kukupa raha, hasa ikiwa unajua kuicheza vizuri. Na hiyo ndiyo sababu unapaswa kuchagua michezo hiyo kwa hekima. Jiulize, ‘Mimi hufanya vizuri shuleni katika masomo gani?’ Ni yale unayofurahia zaidi, sivyo? Ni kweli kwamba kadiri unavyofurahia somo fulani, ndivyo unavyolikumbuka zaidi. Sasa jiulize: ‘Ni mchezo gani ninaoufurahia zaidi? Ni mambo gani ninayojifunza kutokana na mchezo huo?’
Badala ya kucheza mchezo fulani kwa sababu tu ndio unaopendwa na rafiki zako, jifanyie uamuzi wa busara. Zaidi ya yote, tumia shauri hili la Biblia: ‘Endelea kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.’—Waefeso 5:10.
Unapenda muziki, na hilo ni jambo la kawaida. Lakini je, wewe ni mtumwa wa muziki?
MAANDIKO MUHIMU
“Enyi mnaompenda Yehova, chukieni yaliyo mabaya.”—Zaburi 97:10.
PENDEKEZO
Andika habari fupi kuhusu kila mchezo unaotaka kucheza, eleza lengo la kila mchezo na jinsi unavyochezwa ili kufikia lengo hilo. Linganisha habari hiyo na kanuni za Biblia zinazotajwa katika sura hii, kisha uamue ikiwa mchezo huo unafaa au haufai.
JE, WAJUA . . .?
Kliniki ya kwanza ulimwenguni ya kutibu watu wenye uraibu wa kucheza michezo ya kompyuta ilianzishwa Amsterdam, Uholanzi, mwaka wa 2006.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Rafiki yangu akiniambia nicheze mchezo wenye jeuri au matendo mapotovu, nitamwambia ․․․․․
Sitapitisha saa ․․․․․ kwa juma moja nikicheza michezo ya kompyuta, nami nitahakikisha nimeshikamana na lengo hilo kwa ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Michezo ya kompyuta inaweza kuathiri kufikiri na mtazamo wa mtu jinsi gani?
● Kwa nini ni muhimu kufikiria viwango vya Yehova kuhusu maadili unapochagua mchezo fulani?
● Unaweza kumsaidia jinsi gani mdogo wako aliye na mazoea ya kucheza mchezo ambao unajua ni mbaya?
[Blabu katika ukurasa wa 249]
‘‘Michezo mingi hukufanya uone vitu kama jeuri, lugha chafu, na matendo mapotovu kuwa mambo ya kawaida na hivyo kufanya iwe rahisi kutumbukia katika vishawishi vingine maishani. Unapaswa kuwa mwangalifu sana kuhusu michezo unayochagua.’’—Amy
[Picha katika ukurasa wa 250]
Kucheza michezo ya kompyuta yenye jeuri au matendo mapotovu ni kama kucheza na vitu vyenye miale hatari. Huenda madhara yasionekane mara moja, lakini muda si muda, athari zake zitaonekana
-
-
Ninaweza Kuwa na Usawaziko Jinsi Gani Kuhusu Muziki?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 31
Ninaweza Kuwa na Usawaziko Jinsi Gani Kuhusu Muziki?
Muziki ni wa maana kwako kadiri gani?
□ Si wa lazima.
□ Siwezi kuishi bila muziki.
Wewe husikiliza muziki wakati gani?
□ Ninaposafiri
□ Ninaposoma
□ Wakati wote
Ni muziki wa aina gani unaopenda sana?
YAELEKEA sote tuliumbwa tukiwa na uwezo wa kufurahia muziki. Na kwa vijana wengi, muziki ni wa lazima. “Siwezi kuishi bila muziki,” anasema Amber mwenye umri wa miaka 21. “Mimi husikiliza muziki karibu kila wakati, ninapofanya usafi, ninapopika, ninapotembea, au hata ninaposoma.”
Hata muziki wenye mdundo wa kawaida tu unaweza kupenya ndani sana na kuchochea hisia zetu. Kama vile “neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” wimbo unaochezwa wakati unaofaa unaweza kuburudisha sana! (Methali 15:23) “Nyakati nyingine unahisi kwamba hakuna mtu anayekuelewa,” anasema Jessica mwenye umri wa miaka 16. “Lakini ninaposikiliza nyimbo za bendi fulani ninayopenda, najihisi kwamba siko peke yangu.”
Je, Muziki Hutokeza Vita au Amani?
Ingawa unapenda muziki, huenda wazazi wako wakawa na maoni tofauti. Kijana mmoja anasema: “Baba yangu husema, ‘Zima hiyo kilele! Inaniumiza masikio!’” Ugomvi unapotokea, huenda ukaona kwamba wazazi wako wanachemka bure. “Ilikuwaje walipokuwa vijana?” anauliza msichana mmoja. “Kwani wazazi wao pia hawakufikiri kwamba muziki walioupenda ulikuwa mbaya?” Ingred mwenye umri wa miaka 16 analalamika: “Watu wazima hawapendi mabadiliko. Ingekuwa afadhali kama wangetambua kwamba kizazi chetu kinapenda muziki tofauti!”
Kuna ukweli fulani katika maneno ya Ingred. Kama ujuavyo, tangu zamani mapendezi ya vijana na ya watu wazima yametofautiana sana. Hata hivyo, haimaanishi kwamba lazima mgombane kwa sababu ya muziki kila siku. Siri ni kujaribu kutafuta maelewano kuhusu muziki. Ikiwa wazazi wako wanaiheshimu Biblia, basi kuna matumaini. Kwa nini? Kwa kuwa Neno la Mungu linaweza kukusaidia wewe na wazazi wako kutambua mambo yanayofaa na yanayotegemea mapendezi ya kibinafsi. Ili kufanya hivyo, unahitaji kuchanganua mambo mawili makuu: (1) ujumbe ulio katika muziki unaosikiliza na (2) muda unaotumia kusikiliza muziki. Kwanza, tufikirie swali hili . . .
Muziki Ninaopenda Una Ujumbe Gani?
Muziki ni kama chakula. Unahitaji aina inayofaa kwa kiasi kinachofaa. Aina mbaya, hata iwe ni kiasi gani, ni hatari. Kwa kusikitisha, katika ulimwengu wa muziki, aina mbaya ya muziki ndiyo inayovutia zaidi. “Kwa nini miziki yote yenye midundo mitamu huwa na maneno machafu hivyo?” alalamika kijana anayeitwa Steve.
Ikiwa unapendezwa na mdundo, kuna haja ya kuzingatia ujumbe uliopo? Ili kujibu swali hilo, jiulize: ‘Ikiwa mtu fulani angetaka ninywe sumu, angetumia mbinu gani ili kunifanya niinywe? Je, angeichovya katika kitu kichungu au katika sukari?’ Yule mwanamume mwaminifu, Ayubu, aliuliza: “Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?” (Ayubu 12:11) Kwa hiyo, badala ya kusikiliza muziki kwa sababu tu unapenda mdundo wake—utamu wake wa kijuujuu—‘pima maneno yake’ kwa kufikiria kichwa cha muziki na maneno yaliyomo. Kwa nini? Kwa sababu maneno yaliyo katika muziki yataathiri kufikiri kwako na mtazamo wako.
Inasikitisha kwamba miziki inayopendwa sana leo ina maneno yanayosifu ngono, jeuri, na matumizi ya dawa za kulevya. Ikiwa huoni kwamba kusikiliza maneno hayo kunaweza kukuathiri, basi “sumu” yake imeanza kukuingia.
Usifuate Upepo
Vijana wenzako wanaweza kukushinikiza usikilize muziki usiofaa. Pia, soko la muziki lina uvutano mkubwa. Kukiwa na redio, Intaneti, na televisheni, muziki umekuwa biashara kubwa. Wataalamu wa mauzo wameajiriwa ili kukuchochea upendezwe na muziki wa aina fulani.
Lakini unapoacha marafiki au vyombo vya habari vikuamulie muziki utakaosikiliza, unapoteza uhuru wako wa kuchagua. Unakuwa mtumwa, mtu asiyetumia akili yake. (Waroma 6:16) Biblia inakuhimiza uepuke uvutano wa ulimwengu katika mambo kama hayo. (Waroma 12:2) Hivyo, unapaswa kuzoeza ‘nguvu zako za ufahamu ili zitofautishe yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Unaweza kutumia jinsi gani nguvu zako za ufahamu unapochagua muziki? Fikiria mapendekezo yanayofuata:
Chunguza picha na maandishi yaliyo kwenye kasha. Mara nyingi unaweza kujua yaliyomo katika kanda kwa kutazama kasha. Unapoona picha zinazoonyesha jeuri, ngono, au kuwasiliana na pepo, tahadhari. Inaelekea muziki wenyewe pia haufai.
Soma maneno ya wimbo. Ni nini kinachosemwa? Je, kweli ungependa kusikiliza maneno hayo tena na tena? Je, ujumbe wa wimbo huo unapatana na sifa na kanuni za Kikristo?—Waefeso 5:3-5.
Chunguza athari zake. Kijana anayeitwa Philip anasema: “Niligundua kwamba muziki na maneno niliyosikiliza yalinifanya nishuke moyo.” Kwa kweli, muziki unaweza kuathiri watu kwa njia mbalimbali. Lakini muziki unaosikiliza unaamsha hisia gani? Jiulize: ‘Je, mimi huwa na mawazo yasiyofaa baada ya kusikiliza muziki au maneno ya muziki fulani? Je, nimeanza kutumia lugha ya mitaani inayotumiwa katika muziki?’—1 Wakorintho 15:33.
Wafikirie wengine. Wazazi wako wana maoni gani kuhusu muziki unaosikiliza? Waulize maoni yao. Pia, fikiria maoni ya Wakristo wenzako. Je, wengine wanaweza kukwazwa? Kubadili mwenendo wako ili usiumize hisia za wengine kunaonyesha kwamba wewe ni mkomavu.—Waroma 15:1, 2.
Kujiuliza maswali yaliyo hapo juu kutakusaidia kuchagua muziki ambao utakuchangamsha moyo pasipo kuangamiza hali yako ya kiroho. Hata hivyo, kuna jambo lingine la kufikiria.
Ni Wakati Gani Muziki Unapita Kiasi?
Muziki unaofaa kama vile chakula kizuri unaweza kuwa wenye faida. Hata hivyo, methali yenye hekima inaonya: “Je, umepata asali? Kula kiasi cha kukutosha, ili usiile kupita kiasi kisha uitapike.” (Methali 25:16) Asali ni dawa. Lakini kitu chochote hata kiwe kizuri kinapopita kiasi kinaweza kukudhuru. Kwa hiyo, vitu vizuri vinapaswa kufurahiwa kwa kiasi.
Hata hivyo, maisha ya vijana fulani hutawaliwa na muziki. Kwa mfano, Jessica aliyetajwa mapema, anakiri: “Mimi husikiliza muziki kila wakati—hata ninapojifunza Biblia. Mimi huwaambia wazazi wangu kwamba muziki hunisaidia kukaza fikira. Lakini hawaniamini.” Je, umewahi kuwa na maoni kama ya Jessica?
Unaweza kujua jinsi gani ikiwa unapita kiasi katika kusikiliza muziki? Jiulize maswali yanayofuata:
Kila siku mimi hutumia saa ngapi kusikiliza muziki? ․․․․․
Ninatumia pesa ngapi kwa muziki kila mwezi? ․․․․․
Je, muziki unaharibu uhusiano kati yangu na wengine katika familia? Ikiwa ndivyo, andika hapa chini jinsi unavyoweza kurekebisha hali hiyo. ․․․․․
Badili Mazoea Yako
Ikiwa muziki unachukua wakati mwingi kupita kiasi, unapaswa kujiwekea mipaka na kuwa na usawaziko kuhusiana na mazoea yako ya kusikiliza muziki. Kwa mfano, huenda ukahitaji kuacha mazoea ya kuweka masikioni vidude vya kusikilizia muziki siku nzima au mazoea ya kuwasha redio mara tu unapofika nyumbani.
Kwa nini usijifunze kufurahia pindi za utulivu, pasipo kelele yoyote? Kufanya hivyo kutakusaidia katika masomo yako. Steve aliyetajwa mapema anasema: “Unaweza kujifunza mambo mengi zaidi ikiwa muziki umezimwa.” Jaribu kusoma bila muziki, na uone iwapo utakazia fikira zaidi mambo unayojifunza.
Pia, utahitaji kupanga wakati wa kusoma na kujifunza Biblia na vitabu vinavyotegemea Biblia. Nyakati nyingine, Yesu Kristo alitafuta mahali patulivu ili kusali na kutafakari. (Marko 1:35) Je, wewe pia hujifunza katika mazingira matulivu, yasiyo na kelele? Ikiwa hufanyi hivyo, huenda unazuia ukuzi wako wa kiroho.
Fanya Uchaguzi Unaofaa
Kwa kweli, muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu, lakini unapaswa kujihadhari usiitumie vibaya. Usiwe kama msichana anayeitwa Marlene, anayesema: “Nina muziki ambao ninajua ninapaswa kuutupilia mbali. Lakini ni mtamu wee.” Fikiria madhara anayosababisha katika akili na moyo wake kwa kusikiliza muziki usiofaa! Usinaswe na mtego huo. Usikubali muziki ukupotoshe au utawale maisha yako. Chagua muziki unaopatana na viwango vya Kikristo. Mwombe Mungu akusaidie. Tafuta marafiki walio na maoni kama yako.
Muziki unaweza kukustarehesha na kukuburudisha. Unaweza kukuondolea hisia za upweke. Hata hivyo, hautatui matatizo yako. Isitoshe, nyimbo haziwezi kulinganishwa na marafiki wa kweli. Kwa hiyo, usiruhusu muziki uwe jambo kuu maishani mwako. Furahia muziki, lakini usikubali ukutawale.
Unahitaji kujiburudisha mara kwa mara. Kanuni za Biblia zinaweza kukusaidia jinsi gani unufaike kutokana na pindi hizo zenye kufurahisha?
MAANDIKO MUHIMU
“Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?”—Ayubu 12:11.
PENDEKEZO
Ikiwa unataka wazazi wako waelewe ni kwa nini unapenda muziki au bendi fulani, kwanza jaribu kupendezwa na baadhi ya miziki wanayofurahia.
JE, WAJUA . . .?
Ikiwa hupendi wazazi wako wasikilize muziki unaopenda sana, basi huenda muziki unaosikiliza una kasoro.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ninaweza kuwa na usawaziko kuelekea muziki niki ․․․․․
Vijana wenzangu wakinishurutisha nisikilize muziki usiofaa, nitawaambia ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini uchaguzi wako wa muziki ni wa maana sana?
● Unaweza kuamua jinsi gani ikiwa wimbo fulani unafaa au haufai?
● Unaweza kufanya nini ili ujifunze kufurahia miziki ya aina nyingine?
[Blabu katika ukurasa wa 259]
‘‘Wakati mwingine mimi hujikuta nikisikiliza muziki usiofaa. Nauzima bila kukawia. Nisipofanya hivyo mara moja, nitaanza kutafuta visababu vya kuusikiliza.’’—Cameron
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 258]
Jifunze Kufurahia Miziki ya Aina Nyingine
Je, unapenda aina nyingi zaidi za chakula leo kuliko ulipokuwa na umri wa miaka mitano? Ikiwa ndivyo, ni kwa sababu umejizoeza kufurahia ladha ya vyakula vipya. Ndivyo ilivyo na muziki. Usisikilize muziki wa aina moja tu. Jifunze kupendezwa na miziki ya aina nyingine.
Njia moja ya kufanya hivyo ni kujifunza kupiga ala fulani ya muziki. Kufanya hivyo kunaweza kukuchangamsha na kukuridhisha na pia kutakufanya upendezwe na aina nyingine ya muziki mbali na ile inayopigiwa debe na wafanyabiashara. Utapata wapi wakati wa kujifunza? Unaweza kupunguza wakati unaotumia kutazama televisheni au kucheza michezo ya kompyuta. Ona yale ambayo vijana hawa wanasema.
“Kupiga ala ya muziki ni raha na kunaweza kuwa njia bora ya kuonyesha hisia zako. Kujifunza kupiga nyimbo mpya kumenisaidia kupenda aina mbalimbali za muziki.”—Brian, mwenye umri wa 18, ambaye hupiga gitaa, ngoma, na piano.
“Unahitaji kufanya mazoezi ikiwa unataka kujifunza kupiga vizuri chombo fulani cha muziki. Na mazoezi hayafurahishi sikuzote. Lakini kuwa stadi wa kupiga muziki fulani ni jambo lenye kufurahisha na kuridhisha kwelikweli.”—Jade, mwenye umri wa miaka 13, ambaye hupiga fidla.
“Ninapokuwa nimechoka au kushuka moyo, kupiga gitaa hunisaidia kustarehe. Kutunga muziki mzuri na wenye kutuliza na kuburudisha ni jambo lisilo na kifani.”—Vanessa, mwenye umri wa miaka 20, hupiga gitaa, piano, na zumari.
“Nilikuwa nikijiambia, ‘Sitawahi kuwa na ustadi kama fulani wa fulani.’ Lakini niliendelea kufanya mazoezi, na sasa ninapata uradhi ninapopiga wimbo fulani vizuri. Sasa, nawavulia kofia wanamuziki wengine stadi.”—Jacob, mwenye umri wa miaka 20, hupiga gitaa.
[Picha katika ukurasa wa 255]
Muziki ni kama chakula. Unahitaji aina inayofaa kwa kiasi kinachofaa. Aina mbaya, hata iwe ni kiasi gani, ni hatari
-
-
Mfano wa Kuigwa—DaudiMaswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
Mfano wa Kuigwa—Daudi
Daudi anapenda muziki. Ni mwimbaji hodari na mtungaji stadi. Hata hujitengenezea vyombo vya muziki. (2 Mambo ya Nyakati 7:6) Daudi ana ustadi mwingi sana hivi kwamba mfalme wa Israeli anamwalika akapige muziki katika makao ya mfalme. (1 Samweli 16:15-23) Daudi anakubali. Hata hivyo, haingiwi na kiburi, wala hakubali maisha yake yatawaliwe na muziki. Badala yake, anatumia vipawa vyake kumsifu Yehova.
Je, unapenda muziki? Huenda usiwe mwanamuziki mwenye kipawa, lakini bado unaweza kuiga mfano wa Daudi. Jinsi gani? Kwa kutokubali muziki utawale maisha yako au kukufanya ufikiri na kutenda kwa njia inayomvunjia Mungu heshima. Badala yake, tumia muziki kufanya maisha yako yawe yenye kufurahisha zaidi. Uwezo wa kutunga na kufurahia muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Yakobo 1:17) Daudi alitumia zawadi hiyo kwa njia zinazompendeza Yehova. Je, utafanya hivyo pia?
-
-
Ninaweza Kujifurahisha Jinsi Gani?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 32
Ninaweza Kujifurahisha Jinsi Gani?
Tia alama maswali yafuatayo kweli au si kweli.
Kulingana na Biblia . . .
Ni kosa kushiriki michezo ya aina yoyote.
□ Kweli □ Si kweli
Sinema zote na vipindi vyote vya televisheni ni vibaya.
□ Kweli □ Si kweli
Dansi zote ni mbaya.
□ Kweli □ Si kweli
UMESOMA kwa bidii juma zima. Mwisho juma umefika. Kazi za nyumbani zimekwisha. Lakini ungali na nguvu—mojawapo ya baraka za kuwa kijana. (Methali 20:29) Sasa, kile ungependa kufanya ni kujifurahisha kidogo.
Huenda vijana wenzako wakahisi kwamba Biblia inashutumu kujifurahisha, na hivyo inakuzuia kufurahia maisha. Lakini, je, hilo ni kweli? Acheni tuchunguze maswali yaliyo katika ukurasa unaotangulia tuone maoni ya Biblia kuhusu kujifurahisha.
● Ni kosa kushiriki michezo ya aina yoyote.
Si kweli. Biblia inasema kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mazoezi” ambalo Paulo alitumia katika mstari huo linamaanisha ‘kujizoeza kama mwanasarakasi.’ Leo kuna michezo mingi—kama vile kuteleza barafuni, kuendesha baiskeli, kukimbia mchakamchaka, tenisi, besiboli, soka, voliboli, na mingine mingi—inayoweza kumsaidia mtu kufanya mazoezi na pia kujifurahisha.
Hata hivyo, kuna haja yoyote ya kuchukua tahadhari? Fikiria muktadha wa mstari ulionukuliwa hapo juu. Akimwandikia kijana Timotheo, mtume Paulo alisema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo; lakini ujitoaji-kimungu ni wenye faida kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” Maneno ya Paulo yanatukumbusha kwamba jambo kuu maishani mwetu ni kumpendeza Mungu. Unaweza kuhakikisha kwamba unatanguliza ujitoaji-kimungu—hata unapochagua mchezo fulani—kwa kujiuliza maswali haya matatu:
1. Kuna hatari yoyote inayohusika katika mchezo huo? Usitegemee tu mambo ya watu au kukubaliana na maoni ya vijana wenzako ambao ni mashabiki wa mchezo huo. Tafuta ukweli wa mambo. Kwa mfano, uliza: Ni watu wangapi wanaoumia katika mchezo huo? Ni tahadhari gani inayochukuliwa wakati wa mchezo huo? Ni mazoezi na vifaa gani vinavyohitajiwa ili kucheza mchezo huo bila kujihatarisha? Ingawa kuna hatari fulani katika karibu kila mchezo, je, lengo kuu la mchezo huo ni kufanya mambo yanayohatarisha uhai?
Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Kulingana na Sheria ya Mungu kwa Waisraeli, hata mtu aliyemuua mwingine bila kukusudia alipata adhabu. (Kutoka 21:29; Hesabu 35:22-25) Hivyo, watu wa Mungu walitiwa moyo kuzingatia sana usalama. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Vivyo hivyo, Wakristo leo wanapaswa kuheshimu uhai.
2. Katika mchezo huo, je, kuna mashirika mazuri? Ikiwa wewe ni mwanariadha hodari, huenda marafiki na walimu wakataka ujiunge na timu ya shule. Huenda ukashawishika kufanya hivyo. Kijana Mkristo, Mark anasema, “Sielewi ni kwa nini wazazi wangu hawataki nijiunge na timu ya shule.” Lakini badala ya kujaribu kuwabembeleza wazazi wako wakubali maoni yako, fikiria mambo yanayofuata: Kwa kawaida mazoezi na michezo hufanywa baada ya saa za kawaida za shule. Ukitia fora, utahitajika kutumia muda mwingi zaidi katika michezo. Usipofaulu, bado utalazimika kutumia muda mwingi zaidi kufanya mazoezi. Pia, timu nyingi hupenda kusherehekea ushindi pamoja au kwenda “kuomboleza” pamoja wanaposhindwa.
Sasa jiulize: ‘Je, kutumia wakati wangu katika mchezo unaoweza kunifanya nijenge urafiki wa karibu na vijana ambao hawaongozwi na viwango kama vyangu, kutanisaidia kiroho?’ (1 Wakorintho 15:33) ‘Nitalazimika kudhabihu mambo gani ili tu nijiunge na timu hiyo?’
3. Mchezo huo utachukua kiasi gani cha wakati na pesa? Biblia inatushauri ‘tuhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Ili kukusaidia kuona jinsi unavyoweza kutumia shauri hilo, jiulize: ‘Je, mchezo huo utakula wakati ambao nimepangia kazi za shule au mambo ya kiroho? Kwa ujumla mchezo huo utanigharimu pesa ngapi? Je, ninaweza kuugharimia?’ Kujibu maswali hayo kutakusaidia kutanguliza mambo yaliyo ya maana zaidi.
● Sinema zote na vipindi vyote vya televisheni ni vibaya.
Si kweli. Biblia inawaamuru Wakristo ‘washike sana yaliyo mazuri’ na ‘wajiepushe na kila namna ya uovu.’ (1 Wathesalonike 5:21, 22) Si sinema zote na vipindi vyote vya televisheni vinavyopingana na kanuni hiyo.a
Bila shaka, kwenda kutazama sinema kunaweza kuwa njia nzuri ya kutumia wakati pamoja na marafiki. Leigh, msichana kutoka Afrika Kusini anasema, “Ninapotaka kutazama sinema fulani, mimi humpigia simu mmoja wa rafiki zangu, kisha tunasambaza habari kwa marafiki wengine.” Kwa kawaida kikundi hicho hutazama sinema hiyo mapema. Baadaye, wao huchukuliwa na wazazi wao na kwenda kula hotelini.
Sinema na televisheni ni uvumbuzi wa karibuni, hata hivyo, ni njia mpya tu ya kufanya jambo lililoanza zamani za kale, yaani usimuliaji wa hadithi. Yesu alikuwa stadi wa kusimulia hadithi zilizochochea mioyo ya watu. Kwa mfano, hadithi yake kuhusu Msamaria mwema huchochea hisia za huruma na kufundisha mambo muhimu.—Luka 10:29-37.
Leo pia, watengenezaji wa sinema hufundisha mambo yanayochochea maoni ya watu. Wao hujaribu kufanya watazamaji wavutiwe na wahusika katika sinema hizo, hata iwe mhusika mkuu ni mhalifu au mkatili. Usipokuwa mwangalifu, huenda ukajikuta ukishabikia mtu mhalifu, na kutetea mwenendo wake mpotovu au wenye ukatili! Unaweza kuepuka mtego huo jinsi gani?
Unapochagua sinema au kipindi cha televisheni, jiulize: ‘Je, kipindi hiki kitanisaidia kuwa mwenye huruma nyororo?’ (Waefeso 4:32) ‘Au kitanifanya niwacheke wengine wanapoumia?’ (Methali 17:5) ‘Kitafanya iwe vigumu kwangu “[kuchukia] yaliyo mabaya”?’ (Zaburi 97:10) ‘Je, ninawaunga mkono “watenda maovu” kwa kutazama kipindi au sinema hiyo?’—Zaburi 26:4, 5.
Uchambuzi na matangazo ya sinema yanaweza kukusaidia kujua yaliyomo katika sinema hiyo. Hata hivyo, ‘usiamini tu kila neno’ kipumbavu. (Methali 14:15) Kwa nini? Uchambuzi wa sinema ni maoni tu ya mtu mwingine. Nayo matangazo huenda yasionyeshe kwamba sinema hiyo ina mandhari zenye kuchukiza. Tineja anayeitwa Connie anasema, “Nimeona kwamba mara nyingi kuwajua wahusika wakuu katika sinema kunasaidia kujua sinema hiyo itakuwaje.”
Vijana wenzako Wakristo ambao pia huongozwa na kanuni za Biblia wanaweza kujua ikiwa sinema fulani inafaa. Lakini kumbuka kwamba mara nyingi watu hueleza mambo waliyofurahia katika sinema. Kwa nini usiulize kile ambacho hawakufurahia? Uliza habari hususa. Kwa mfano, waulize ikiwa kuna sehemu zinazoonyesha jeuri, ngono, au kuwasiliana na pepo. Wazazi wako pia wanaweza kukusaidia. Vanessa anasema: “Mimi huzungumza na wazazi wangu kuhusu sinema. Wakisema inafaa, ninaenda kuitazama.”
Kuchagua sinema au programu ya televisheni ni jambo zito. Kwa nini? Kwa sababu burudani unayochagua inaonyesha kilicho moyoni mwako, inafunua mambo unayoona kuwa muhimu. (Luka 6:45) Uchaguzi wako unaonyesha aina ya watu unaopenda kushirikiana nao, usemi unaofurahia, na mapendezi yako ya kiadili. Kwa hiyo, uwe mteuzi!
● Dansi zote ni mbaya.
Si kweli. Waisraeli walipovuka Bahari Nyekundu na kulikimbia jeshi la Misri, Miriamu aliwaongoza wanawake katika kucheza dansi. (Kutoka 15:20) Pia, katika ule mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, mwana huyo aliporudi watu walishangilia kwa “muziki na dansi.”—Luka 15:25.
Ndivyo ilivyo leo. Katika utamaduni wa nchi nyingi, vijana kwa wazee hucheza dansi familia na marafiki wanapokusanyika pamoja. Hata hivyo, kuna uhitaji wa tahadhari. Ingawa Biblia haishutumu karamu zenye kiasi, inaonya dhidi ya “karamu za kupindukia.” (Wagalatia 5:19-21) Nabii Isaya aliandika: “Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema ili watafute tu kileo, wanaokawia mpaka giza la jioni sana hivi kwamba divai inawawasha! Na kutakuwa na kinubi na kinanda, tari na filimbi, na divai katika karamu zao; lakini hawauangalii utendaji wa Yehova, wala hawakuiona kazi ya mikono yake.”—Isaya 5:11, 12.
Karamu hizo zilitia ndani “kileo” na dansi potovu. Zilianza mapema na kuendelea mpaka jioni. Ona pia kwamba waliokuwa katika karamu hizo walijiendesha kana kwamba hakuna Mungu! Si ajabu Mungu alishutumu karamu za namna hiyo.
Ukialikwa katika karamu ambayo watu watacheza dansi, jiulize: ‘Ni nani watakaokuwako? Wana sifa gani? Imepangwa na nani? Ni nani atakayeisimamia? Wazazi wangu watakubali niende? Kutakuwa na dansi ya aina gani?’ Dansi nyingi hukusudiwa kuamsha tamaa za ngono. Je, kucheza au kutazama tu dansi za aina hiyo kutakusaidia ‘kuukimbia uasherati’?—1 Wakorintho 6:18.
Namna gani ukialikwa kwenda disko? Fikiria maneno ya kijana anayeitwa Shawn ambaye kabla ya kuwa Mkristo alipenda kwenda disko. Anakumbuka: “Kwa kawaida muziki unaochezwa ni mbaya, dansi zinazochezwa ni chafu, na watu wengi huenda huko wakiwa na kusudi fulani.” Kusudi lenyewe ni kutoka huko na mtu wa kufanya ngono naye, anasema Shawn. Baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, Shawn alibadili nia yake. Ana maoni gani sasa? “Klabu hizo haziwafai Wakristo.”
Kwa Nini Uwe Macho?
Unafikiri ni wakati gani askari anaweza kushambuliwa kwa urahisi zaidi—akiwa vitani au anapopumzika na marafiki? Bila shaka ni wakati anapopumzika. Vivyo hivyo unapokuwa shuleni au kazini uko chonjo kiroho. Unaweza kuona hatari zinazoweza kutokea. Lakini, wakati wa starehe pamoja na marafiki wako, ni rahisi zaidi kulegeza viwango vyako na kuvunja msimamo wako wa kiadili.
Huenda vijana wenzako wakakudhihaki kwa sababu ya msimamo wako thabiti wa kiadili hata wakati wa burudani. Unaweza hata kushinikizwa na vijana ambao wamelelewa na wazazi Wakristo. Lakini dhamiri za vijana hao zimekuwa sugu. (1 Timotheo 4:2) Huenda wakadai kuwa huna usawaziko au una maringo. Hata hivyo, badala ya kushindwa na msongo wa marika, jitahidi ‘kuwa na dhamiri njema.’—1 Petro 3:16.
Jambo la maana si jinsi marafiki wako wanavyokuona bali ni jinsi Yehova anavyokuona! Na ikiwa rafiki zako wanakudhihaki kwa sababu ya kufuata dhamiri yako, tafuta marafiki wapya. (Methali 13:20) Kumbuka kwamba wewe tu ndiwe unayeweza kujiamulia jinsi utakavyojiendesha kiadili—hata unapokuwa katika starehe.—Methali 4:23.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 37
Siku hizi ponografia imeenea sana na inaweza kupatikana kwa urahisi. Unaweza kuepuka mtego huo jinsi gani?
[Maelezo ya Chini]
a Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 1, sura ya 36.
MAANDIKO MUHIMU
“Ewe kijana, shangilia katika ujana wako, . . . nawe utembee katika njia za moyo wako na katika mambo ambayo macho yako yameona. Lakini ujue kwamba kwa ajili ya mambo yote hayo, Mungu wa kweli atakuleta hukumuni.”—Mhubiri 11:9.
PENDEKEZO
Waulize wazazi wako ikiwa wanaweza kupanga pindi kadhaa kila mwezi ambapo familia nzima inaweza kufanya mambo fulani yenye kufurahisha badala ya kutazama televisheni tu.
JE, WAJUA . . .?
Muziki na dansi zilikuwa sehemu muhimu katika ibada ya kweli ya Waisraeli.—Zaburi 150:4.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nikiombwa kujiunga na timu ya mchezo fulani baada ya saa za shule, nitasema ․․․․․
Ikiwa sinema ninayotazama pamoja na marafiki wangu haifai, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini Wakristo wanapaswa kujiepusha na michezo hatari?
● Unaweza kuamua jinsi gani ikiwa sinema fulani inafaa?
● Ni dansi ya aina gani inayofaa?
[Blabu katika ukurasa wa 269]
‘‘Ninapenda kucheza dansi, lakini nimeona faida ya kusikiliza mashauri ya wazazi wangu. Sitangulizi dansi maishani mwangu.’’—Tina
[Picha katika ukurasa wa 268]
Kama vile ambavyo askari anaweza kushambuliwa kwa urahisi asipokuwa macho, wewe pia unaweza kulegeza msimamo wako wa maadili unapostarehe
-
-
Kwa Nini Niepuke Ponografia?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 33
Kwa Nini Niepuke Ponografia?
Ni mara ngapi unapoona picha za ponografia bila kukusudia?
□ Sijawahi
□ Mara chache
□ Mara nyingi
Ni wapi hasa inapotukia?
□ Kwenye Intaneti
□ Shuleni
□ Kwenye televisheni
□ Kwingineko
Wewe hufanya nini?
□ Ninaacha mara moja kutazama.
□ Udadisi hunifanya niitazame kwa muda fulani.
□ Mimi huitazama kwa muda mrefu na hata kutafuta picha zaidi.
WAZAZI wako walipokuwa na umri kama wako, mtu aliyetaka ponografia alikuwa akiitafuta. Leo, ponografia inakutafuta. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 19 anasema: “Nyakati nyingine ninapotafuta-tafuta habari au bidhaa fulani katika Intaneti au hata ninapotaka kuona baki kwenye akaunti yangu ya benki kisha ghafula bin vuu—picha za ponografia zinatokea!” Hilo ni jambo la kawaida. Katika uchunguzi mmoja, asilimia 90 ya vijana walio na umri kati ya miaka 8 na 16 walisema kwamba walikumbana na ponografia kwenye Intaneti bila kukusudia, mara nyingi walipokuwa wakifanya migawo ya shule!
Kwa kuwa ponografia imeenea sana, huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli ponografia ni mbaya?’ Ndiyo! Ponografia huwashushia heshima wahusika na wale wanaoitazama, na mara nyingi hiyo huongoza kwenye uasherati. Lakini kuna mengi zaidi.
Kutazama ponografia kunaweza kuwa zoea lenye madhara ya kudumu. Kwa mfano, mfikirie Jeff ambaye hata baada ya miaka 14 kupita tangu alipoacha kutazama ponografia, anasema: “Mimi hupambana kila siku. Ingawa si kama zamani, bado mimi huwa na hamu ya kuitazama. Picha hizo zingali akilini. Laiti singeanza zoea hilo. Mwanzoni sikuona ubaya wowote. Lakini sasa ninajua. Ponografia inadhuru, ni potovu, na inawashushia heshima wote wanaohusika. Hata wale wanaoitetea waseme nini, ponografia haina faida yoyote.”
Chunguza Hali
Unaweza kuepuka jinsi gani kuona picha za ponografia hata bila kukusudia? Kwanza chunguza hali. Je, kuna mambo fulani yanayotokea kila mara kabla ya picha hizo kutokea? Fikiria mifano inayofuata:
Je, wanafunzi wenzako hukutumia ponografia kupitia barua-pepe au simu ya mkononi? Ikiwa ndivyo, ingefaa kufuta ujumbe unaopata kutoka kwao bila hata kuufungua.
Unapotumia Intaneti, je, vituo hivyo hutokea ghafula unapotafuta habari kwa kuandika maneno fulani? Kujua hilo kunaweza kukusaidia kuchagua kwa uangalifu zaidi maneno hususa utakayotumia.
Andika hapa chini njia mbalimbali ambazo umekumbana na ponografia.
․․․․․
Kuna jambo lolote unaloweza kufanya ili kupunguza au kuepuka kabisa ponografia zinazotokea bila kukusudia? Ikiwa ndiyo, andika hapa chini kile unachopanga kufanya.
․․․․․
Ikiwa Tayari Una Zoea Hilo
Kuona ponografia bila kukusudia ni tofauti kabisa na kuitazama kimakusudi. Namna gani ikiwa limeanza kuwa zoea? Usidanganyike, si rahisi kuacha zoea hilo. Tuseme mikono yako imefungwa pamoja kwa uzi mmoja. Huenda ungeweza kujinasua kwa urahisi kwa kuukata uzi huo. Lakini namna gani ikiwa uzi huo ungezungushwa mikononi mwako mara nyingi? Ingekuwa vigumu kujinasua. Ndivyo ilivyo na watu ambao wana mazoea ya kutazama ponografia. Kadiri wanavyoitazama, ndivyo wanavyozidi kunaswa. Ikiwa tayari una mazoea hayo, unaweza kufanya nini?
Tambua mtego wa ponografia. Shetani hutumia ponografia kuvunjia heshima kitu ambacho Yehova aliumba kiheshimike. Kuwa na maoni hayo kutakusaidia ‘kuchukia yaliyo mabaya.’—Zaburi 97:10.
Fikiria madhara. Ponografia huharibu ndoa. Inawashushia heshima wahusika. Inamshushia heshima mtu anayeitazama. Ndiyo sababu Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Andika hapa chini mfano mmoja wa msiba unaoweza kukupata ukiwa na zoea la kutazama ponografia.
․․․․․
Jiwekee azimio. Mwanamume mwaminifu Ayubu alisema: “Nimejifunga rasmi mimi mwenyewe, macho yangu yasimtazame msichana kwa tamaa.” (Ayubu 31:1, BHN) Wewe pia unaweza ‘kujifunga rasmi’ kwa kufanya yafuatayo:
Sitatumia Intaneti kamwe nikiwa peke yangu chumbani.
Nitafunga mara moja kituo chochote kinachoonyesha mambo ya ngono.
Nitazungumza na rafiki mkomavu iwapo nitatumbukia tena katika zoea hilo.
Kuna jambo au mambo mengine yanayoweza kukusaidia kushinda tatizo la kutazama ponografia? Yaandike hapa chini.
․․․․․
Sali kuhusu jambo hilo. Mtunga-zaburi alisali hivi kwa Yehova: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.” (Zaburi 119:37) Yehova Mungu anataka ufaulu, naye anaweza kukupa nguvu za kufanya yaliyo sawa!—Wafilipi 4:13.
Zungumza na mtu. Mara nyingi kuchagua mtu unayeweza kumfunulia moyo wako husaidia sana kushinda zoea hilo. (Methali 17:17) Andika hapa chini jina la mtu mkomavu ambaye unaona ni rahisi kumweleza jambo hilo.
․․․․․
Uwe na hakika kwamba unaweza kushinda zoea la kutazama ponografia. Kwa kweli, kila mara unapoiepuka, ni ushindi mkubwa. Mweleze Yehova kuhusu ushindi huo, na umshukuru kwa kukupa nguvu. Sikuzote kumbuka kwamba kwa kuepuka mtego wa ponografia, unaufanya moyo wa Yehova ushangilie!—Methali 27:11.
MAANDIKO MUHIMU
“Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”—Wakolosai 3:5.
PENDEKEZO
Hakikisha kwamba kompyuta yako imezuiwa kufungua vituo vya ponografia. Pia, epuka kubofya anwani zilizo katika barua-pepe kutoka kwa watu usiowajua.
JE, WAJUA . . .?
Tamaa isiyozuilika ya kutazama ponografia ni kama yale mapendezi mapotovu ya ngono ambayo roho waovu wa siku za Noa walikuwa nayo.—Mwanzo 6:2
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili kujilinda dhidi ya ponografia, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Ni kwa njia gani ponografia inavunjia heshima kitu kinachopaswa kuheshimika?
● Unaweza kumsaidia jinsi gani ndugu au dada yako aliye na tatizo la kutazama ponografia?
[Blabu katika ukurasa wa 278]
‘‘Kabla ya kujifunza Biblia, nilikuwa nimetumia kwa wingi karibu dawa zote za kulevya. Lakini kati ya mazoea yangu yote, ilikuwa vigumu zaidi kuacha kutazama ponografia. Yehova amenisaidia kupambana na tatizo hilo.’’—Jeff
[Picha katika ukurasa wa 276]
Kadiri unavyotazama ponografia ndivyo inavyokuwa vigumu zaidi kuacha zoea hilo
-
-
Daftari—BurudaniMaswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SEHEMU YA 8
Daftari—Burudani
Ni burudani gani unayoipenda sana na kwa nini?
․․․․․
Wazia kwamba unapaswa kumweleza mdogo wako faida ya kuwa na maoni yanayofaa kuhusu burudani. Utamwambia nini?
․․․․․
-