-
Matokeo ya MsibaAmkeni!—1996 | Agosti 22
-
-
Matokeo ya Msiba
HALI huwaje unapokuwa mkimbizi? Jaribu kuwazia unaishi kwa amani, lakini kwa ghafula ulimwengu wako wabadilika. Kwa ghafula, majirani wako wawa maadui. Wanajeshi waja ambao watapora na kuchoma makao yako. Una dakika kumi kufunganya na kutoroka ili kuokoa uhai wako. Unaweza kuchukua mfuko mmoja mdogo tu, kwa kuwa utahitajika kuubeba kwa kilometa nyingi. Utaweka nini ndani yao?
Waondoka katikati ya sauti za milipuko ya risasi na mizinga. Unajiunga na wengine ambao wanatoroka pia. Siku nyingi zapita; waburuta miguu ukiwa na njaa, kiu, na ukiwa umechoka mno. Ili kusalimika, ni lazima uulazimishe mwili wako kuendelea hata ingawa umechoka. Walala chini. Watafuta chakula mashambani.
Wakaribia nchi salama, lakini walinzi wa mpakani hawakuruhusu kuvuka. Wanapekua-pekua mfuko wako na kuchukua kila kitu chenye thamani. Wapata kizuizi kingine na wavuka mpaka. Wawekwa katika kambi chafu ya wakimbizi, iliyo na ua wa seng’enge. Ingawa umezungukwa na wengine ambao wako katika hali kama yako, wahisi ukiwa peke yako na ukiwa umevurugika.
Wakosa uandamani wa familia yako na marafiki. Wajipata ukitegemea kabisa msaada kutoka nje. Hakuna kazi ya kufanya wala chochote cha kufanya. Wapigana na hisia za kuwa bure, kukata tumaini, na hasira. Wahangaika juu ya wakati wako ujao, ukijua kwamba kukaa kwako katika kambi hiyo yaelekea kutakuwa kwa muda tu. Kwa vyovyote, kambi hiyo si nyumbani—ni kama chumba cha kungojea au bohari la watu ambao hawatakikani na mtu yeyote. Wajiuliza ikiwa utarudishwa kwa lazima kule ulikotoka.
Hii ndiyo hali ya mamilioni leo. Kulingana na Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi (UNHCR), watu milioni 27 ulimwenguni pote wamekimbia vita au mnyanyaso. Watu wengine milioni 23 wamehamishwa katika nchi zao wenyewe. Yote yakiwa yamefikiriwa, mtu 1 kati ya watu 115 duniani amelazimishwa kukimbia. Walio wengi ni wanawake na watoto. Wakiwa matokeo ya vita na taabu, wakimbizi huachwa wahurumiwe na hali katika ulimwengu huu usiowataka, ulimwengu ambao huwakataa, si kwa sababu wao ni nani, bali kwa sababu ya kile walicho.
Kuwapo kwao ni ishara ya vurugu kubwa mno ulimwenguni pote. Lataarifu UNHCR: “Wakimbizi ni dalili ya hatimaye ya mvunjiko wa kijamii. Wao ni kiunganishi cha mwisho, cha wazi zaidi, katika visababishi vingi na athari zifafanuazo kiwango cha mvunjiko wa kijamii na wa kisiasa wa nchi fulani. Wakitazamwa na watu duniani kote, wao ni ishara ya hali ya wakati huu ya ustaarabu wa kibinadamu.”
Wataalamu husema kwamba kiwango cha tatizo hilo hakina kifani na kinaongozeka bila dalili ya kwamba kitakoma. Ni nini ambacho kimeongoza kwa hali hiyo? Je, kuna suluhisho lolote? Makala zifuatazo zitachunguza maswali haya.
-
-
Idadi Yenye Kuongezeka ya WakimbiziAmkeni!—1996 | Agosti 22
-
-
Idadi Yenye Kuongezeka ya Wakimbizi
SEHEMU kubwa ya historia ya mwanadamu imeharibiwa na vita, njaa kuu, na mnyanyaso. Likiwa tokeo, sikuzote kumekuwa na watu wanaohitaji mahali pa kimbilio. Katika nyakati zilizopita, mataifa na watu wamepatia wale wenye uhitaji mahali pa kimbilio.
Sheria zenye kuandaa kimbilio ziliheshimiwa na Waazteki wa kale, Waashuru, Wagiriki, Waebrania, Waislamu, na wengineo. Plato, mwanafalsafa Mgiriki, aliandika hivi zaidi ya karne 23 zilizopita: “Mgeni, akiwa ametengwa kutoka watu wa nchi yake na familia yake, apasa kuonyeshwa upendo mwingi na wanadamu na miungu. Kwa hiyo uangalifu wapasa kutolewa ili wageni wasitendewe mabaya.”
Katika karne ya 20, idadi ya wakimbizi imeongezeka kwa kutazamisha. Katika jitihada ya kutunza wakimbizi milioni 1.5 waliobakia baada ya Vita ya Ulimwengu 2, Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi (UNHCR) ilianzishwa katika 1951. Ilifikiriwa kwamba tume hiyo ingedumu kwa miaka mitatu, kutegemea wazo kwamba muda si muda wakimbizi waliokuwapo wangechangamana katika jamii waliyopata kimbilio. Ilifikiriwa kwamba baada ya hilo, shirika hilo lingekomeshwa.
Hata hivyo, kwa kipindi cha miongo mingi, idadi ya wakimbizi iliongezeka sana. Kufikia 1975 idadi yao ilikuwa imefika milioni 2.4. Katika 1985 tarakimu hiyo ilikuwa milioni 10.5. Kufikia 1995 idadi ya watu wenye kupokea ulinzi na msaada kutoka kwa UNHCR ilikuwa imeongozeka kwa kutazamisha hadi milioni 27.4!
Wengi walitumaini kwamba enzi ya baada ya Vita Baridi ingefungua njia ya kutatua tatizo la duniani pote la wakimbizi; haikulitatua. Badala ya hivyo, mataifa yamegawanyika kwa kufuata historia na ukabila, ikitokeza mapambano. Vita vilipokuwa vikiwaka, watu walitoroka, wakijua kwamba serikali zao hazingeweza kuwalinda. Kwa kielelezo katika 1991, karibu Wairaki milioni mbili walitoroka kwa idadi kubwa kuingia katika nchi za ujirani. Tangu wakati huo, wakimbizi wakadiriwao kuwa 735,000 wametoroka ile iliyokuwa Yugoslavia. Kisha, katika 1994 vita ya wenyewe kwa wenyewe katika Rwanda ikalazimisha zaidi ya nusu ya watu wa nchi hiyo milioni 7.3 kutoroka makao yao. Warwanda milioni 2.1 hivi walitafuta kimbilio katika nchi za karibu za Afrika.
Kwa Nini Tatizo Hilo Lazidi Kuwa Baya?
Kuna sababu kadhaa ambazo zachangia idadi yenye kuongezeka ya wakimbizi. Katika mahali fulani, kama vile Afghanistan na Somalia, serikali za kitaifa zimeporomoka. Hilo limeacha mambo mikononi mwa wanamgambo wenye silaha ambao hupora nchi bila kuzuiwa, wakisababisha wasiwasi na kufanya watu watoroke.
Mahali penginepo, mapambano husababishwa na tofauti tata sana za kikabila na kidini, kusudi kuu la vikundi vyenye kupigana likiwa kuondosha raia. Kuhusu vita katika ile iliyokuwa Yugoslavia, mwakilishi wa UM aliomboleza hivi katikati mwa 1995: “Kwa watu wengi ni vigumu sana kufahamu visababishi vya vita hii: ni nani anayepigana, sababu za kupigana. Watu wengi mno wanatoka upande mmoja na kisha majuma matatu baadaye watu wengi wanatoka upande ule mwingine. Ni vigumu sana kufahamu hata kwa watu ambao eti wanafahamu.”
Silaha za kisasa haribifu mno—roketi zenye kurushwa kwa mfuatano, makombora, mizinga, na silaha kama hizo—huongezea machinjo na kupanua mweneo wa mapambano. Tokeo: wakimbizi wengi hata zaidi. Katika nyakati za hivi majuzi asilimia 80 hivi ya wakimbizi wa ulimwenguni imetoroka kutoka nchi zenye kuendelea hadi nchi za ujirani ambazo zinaendelea pia na zisizo na vifaa vya kutunza wale wanaotafuta kimbilio.
Katika mapambano mengi ukosefu wa chakula huchangia tatizo hilo. Watu wanapokufa njaa, labda kwa sababu msafara wa ugavi wa kutuliza wazuiwa, watu walazimika kuhama. Gazeti The New York Times lataja: “Katika mahali kama vile Pembe ya Afrika, ukame na vilevile vita vimeharibu bara hilo hivi kwamba haliwezi kuandaa riziki tena. Iwe hayo mamia ya maelfu yanatoroka kufa njaa au vita si jambo la maana.”
Mamilioni Yasiyotakikana
Ingawa lile wazo la kimbilio linaheshimiwa kikanuni, idadi kubwa ya wakimbizi hutamausha mataifa. Hali hiyo yapatana na ile ya Misri ya kale. Wakati Yakobo na familia yake walipokimbilia Misri ili kutoroka baa la njaa kuu ya miaka saba, walikaribishwa. Farao aliwapa “palipo pema pa nchi” ili waishi hapo.—Mwanzo 47:1-6.
Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, Waisraeli wakawa wengi, “ile nchi ilikuwa imejawa na wao.” Sasa Wamisri wakaanza kuitikia kwa ukali, lakini “kadiri [Wamisri] walivyowatesa ndivyo [Waisraeli] walivyoongezeka na kuzidi kuenea. Nao walichuki[z]wa kwa sababu ya wana wa Israeli.”—Kutoka 1:7, 12.
Vivyo hivyo, mataifa leo ‘huchukizwa’ kadiri idadi ya wakimbizi iendeleavyo kuongezeka. Sababu kubwa ya hangaiko lao ni ya kiuchumi. Hugharimu fedha nyingi kulisha, kuvisha, kulipia makao, na kulinda mamilioni ya wakimbizi. Kati ya 1984 na 1993, utumizi wa kila mwaka wa UNHCR ulipanda kutoka dola milioni 444 hadi dola bilioni 1.3. Nyingi za fedha hizo huchangwa na mataifa yaliyo tajiri zaidi, baadhi yayo yakiwa yanang’ang’ana na matatizo yayo yenyewe ya kiuchumi. Mataifa yenye kusaidia nyakati nyingine hulalamika: ‘Tunang’ang’ana kusaidia wasio na makao katika mitaa yetu wenyewe. Twaweza kuwaje na daraka kwa wasio na makao wa dunia nzima, hasa wakati ambapo tatizo laelekea kuongezeka badala ya kupungua?’
Ni Nini Kifanyacho Mambo Yawe Magumu?
Wale wakimbizi ambao hufika kwenye nchi tajiri mara kwa mara hupata kwamba hali yao imekuwa ngumu kwa sababu ya maelfu mengi ya watu ambayo yamehamia nchi iyohiyo kwa sababu za kiuchumi. Wahamaji hawa wa kiuchumi si wakimbizi wanaotoroka vita au mnyanyaso au njaa kuu. Badala ya hivyo, wanakuja wakitafuta maisha bora zaidi—maisha yasiyo na umaskini. Kwa sababu mara nyingi wao hujifanya kuwa wakimbizi, wakitaabisha mashirika ya kutoa kimbilio kwa madai yasiyo ya kweli, wanafanya iwe vigumu zaidi kwa wakimbizi wa kweli kupata kusikiwa kwa haki.a
Kuingia kwa wakimbizi wengi na wahamiaji kumefananishwa na mito miwili ambayo imetiririka kando kwa kando ikiingia katika nchi tajiri kwa miaka mingi. Hata hivyo, sheria za uhamiaji zenye kuzidi kuwa ngumu zimezuia mto wa wahamaji wa kiuchumi. Hivyo, wamekuja kuwa sehemu ya mto wa wakimbizi, na mto huu umefurika kupita kiasi.
Wakijua kwamba huenda ikachukua miaka kadhaa kuchunguza maombi yao ya kimbilio, wahamaji wa kiuchumi husababu kwamba wako katika hali itakayowaboresha licha ya matokeo ya maombi yao ya kimbilio. Maombi yao ya kimbilio yakikubaliwa, wanaboresha hali yao, kwa kuwa wanabaki katika mazingira yenye ufanisi zaidi kiuchumi. Maombi yao yakikataliwa, wanaboresha hali yao pia, kwa kuwa watakuwa wamepata fedha na kujifunza stadi fulani za kwenda nazo kwenye nchi ya kwao.
Huku idadi yenye kuongezeka ya wakimbizi, pamoja na wakimbizi wasio wa kweli, ikitiririka katika nchi nyinginezo, nchi nyingi hazikaribishi wala kukubali tena wakimbizi. Nyingine zimefungia wale wanaotoroka mipaka yao. Nchi nyinginezo zimeanzisha sheria na taratibu ambazo hukataa kuingia kwa wakimbizi. Na bado nchi nyingine zimewarudisha wakimbizi kwa lazima hadi kwenye nchi walikotoka. Kichapo kimoja cha UNHCR chataja hivi: “Ongezeko lisilokoma katika idadi—ya wakimbizi wa kweli na wahamaji wa kiuchumi—limeweka mkazo mbaya juu ya desturi ya uandaaji wa kimbilio ambayo imefuatwa kwa miaka 3,500, likifanya ikaribie kuporomoka.”
Chuki na Hofu
Kuongezea matatizo hayo ya wakimbizi ni hali yenye kusumbua ya xenophobia—kuhofu na kuchukia wageni. Katika nchi nyinginezo watu huamini kwamba watu kutoka nje hutisha utambulisho wao wa kitaifa, utamaduni, na kazi. Nyakati fulani hofu hizo husababisha jeuri. Gazeti Refugees lasema: “Kontinenti ya Ulaya hupatwa na shambulio moja la kijamii kwa kila dakika tatu—na makao ya muda kwa wanaotafuta kimbilio mara nyingi sana ndiyo shabaha.”
Bango moja katika Ulaya ya kati huonyesha uhasama wenye kina, uhasama ambao unaendelea kuonekana katika mabara mengi ya dunia. Ujumbe walo wenye nia ovu humlenga mgeni: “Wao ni jipu lichukizalo na lenye maumivu kwenye mwili wa taifa letu. Kikundi cha kikabila kisicho na utamaduni, viwango vya kiadili au kidini, kikundi cha watu wenye kuhama-hama chenye kunyang’anya na kuiba tu. Wakiwa wachafu, waliojaa chawa, wao hukaa barabarani na kwenye vituo vya gari-moshi. Na wakusanye matambara yao machafu na kuondoka milele!”
Bila shaka wakimbizi wengi wangetaka sana “kuondoka milele.” Wao wanatamani kwenda nyumbani. Mioyo yao yatamani kwa maumivu kuishi maisha yenye amani, ya kawaida pamoja na familia na marafiki. Lakini hawana nyumbani pa kwenda.
[Maelezo ya Chini]
a Katika 1993, serikali za Ulaya Magharibi pekee zilitumia dola bilioni 11.6 kuwashughulikia na kuwapokea wanaotafuta kimbilio.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
Hali Mbaya ya Wakimbizi
“Je, ulijua kwamba mamia ya maelfu ya watoto wakimbizi hulala njaa kila usiku? Au kwamba ni mtoto mmoja wa mkimbizi kati ya wanane ambaye amepata kwenda shuleni? Wengi wa watoto hawa hawajapata kamwe kwenda sinemani, au bustanini, acha kwenda hata kwenye jumba la hifadhi ya vitu vya kale. Wengi hukua katika kambi zilizozingirwa kwa seng’enge au katika kambi zilizotengwa. Hawajapata kamwe kuona ng’ombe au mbwa. Watoto wengi sana wa wakimbizi hufikiri kwamba nyasi za kijani kibichi ni kitu cha kula, si kitu cha kuruka-ruka na kukimbia juu yacho. Watoto wa wakimbizi ndio sehemu yenye kuhuzunisha zaidi ya kazi yangu.”—Sadako Ogata, Kamishna Mkuu wa Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi.
[Hisani]
Picha ya U.S. Navy
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
Yesu Alikuwa Mkimbizi
Yusufu na Mariamu walikaa Bethlehemu pamoja na mwana wao, Yesu. Wanajimu kutoka Mashariki walikuja na zawadi za dhahabu, manukato, na manemane (NW). Baada ya wao kuondoka malaika alimtokea Yusufu, akisema: “Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize.”—Mathayo 2:13.
Haraka hao watatu wakakimbilia nchi ya kigeni—wakawa wakimbizi. Herode alikasirika kwamba wale wanajimu hawakumripotia mahali pa Yule aliyetabiriwa kuwa mfalme wa Wayahudi. Katika jaribio la kumuua Yesu lisilokuwa na matokeo, yeye aliamuru wanaume wake wawaue wavulana wote wachanga katika Bethlehemu na viunga vyao.
Yusufu na familia yake walibaki Misri hadi malaika wa Mungu alipomtokea tena Yusufu katika ndoto. Malaika huyo alisema hivi: “Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto.”—Mathayo 2:20.
Inaonekana kwamba Yusufu alinuia kukaa katika Yudea, ambapo walikuwa wakiishi kabla ya kukimbilia Misri. Lakini alionywa katika ndoto kwamba ingekuwa hatari kufanya hivyo. Hivyo tisho la jeuri liliathiri maisha yao tena. Yusufu, Mariamu, na Yesu walisafiri kaskazini hadi Galilaya na kukaa katika mji wa Nazareti.
-
-
Kigezo cha Jinsi ya Kuwatendea WakimbiziAmkeni!—1996 | Agosti 22
-
-
Kigezo cha Jinsi ya Kuwatendea Wakimbizi
KATIKA ile Sheria ambayo Yehova Mungu alipatia taifa la Israeli, Waisraeli walikumbushwa juu ya hali yao wakiwa wakimbizi katika Misri. (Kutoka 22:21; 23:9; Kumbukumbu la Torati 10:19) Kwa hiyo waliagizwa wawatendee kwa fadhili wakazi wa kigeni waliokuwa miongoni mwao, kwa hakika kama ndugu.
Sheria ya Mungu ilitaarifu hivi: “Na mgeni [ambaye mara nyingi alikuwa mkimbizi] akikaa pamoja nawe katika nchi yako, usimdhulumu. Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri.”—Mambo ya Walawi 19:33, 34.
Akitambua kwamba wakazi wa kigeni mara nyingi wangeweza kupatwa kwa urahisi na hatari na kwamba hawakuhisi usalama, Yehova alitoa sheria hususa kwa hali-njema yao na ulinzi. Fikiria haki zifuatazo walizopewa.
HAKI YA KUFANYIWA KESI KWA HAKI: “Mtakuwa na sheria moja tu, kwa huyo aliye mgeni, na kwa mzalia.” “Usipotoshe hukumu ya mgeni.”—Mambo ya Walawi 24:22; Kumbukumbu la Torati 24:17.
HAKI YA KUSHIRIKI SEHEMU YA KUMI: “Kila mwaka wa tatu, mwisho wake, toa fungu la kumi lote la maongeo yako ya mwaka huo, uliweke ndani ya malango yako; na Mlawi kwa kuwa hana fungu wala urithi pamoja nawe, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio ndani ya malango yako, na waje wale na kushiba.”—Kumbukumbu la Torati 14:28, 29.
HAKI YA KUPATA MSHAHARA UFAAO: “Usimwonee mtumishi mwenye ujira aliye maskini na uhitaji, kama ni wa nduguzo, au kama ni wageni wako mmojawapo walio katika nchi yako, ndani ya malango yako.”—Kumbukumbu la Torati 24:14.
HAKI YA MUUAJI ASIYEKUSUDIA KUPATA KIMBILIO: “Miji hiyo sita itakuwa miji ya makimbilio kwa ajili ya wana wa Israeli, na kwa ajili ya mgeni, na kwa ajili ya huyo aketiye kati yao hali ya ugeni; ili kila amwuaye mtu, naye hakukusudia kumwua, apate kukimbilia huko.”—Hesabu 35:15.
HAKI YA KUSAZA: “Na mtakapovuna mavuno ya nchi yenu, usivune kabisa kabisa pembe za shamba lako, wala usiyakusanye masazo ya mavuno yako; wala usiyakusanye masazo ya mizabibu yako, wala usiyaokote matunda ya mizabibu yako yaliyopukutika; uyaache kwa ajili ya maskini na mgeni. Mimi ndimi BWANA, Mungu wenu.”—Mambo ya Walawi 19:9, 10.
Kwa hakika, Muumba wetu, Yehova Mungu, ana huruma kwa wakimbizi, naye ni lazima anafurahi tunapokuwa na huruma pia. “Mfuateni [“Iweni waigaji wa,” NW] Mungu,” akaandika mtume Mkristo Paulo, “mkaenende katika upendo.”—Waefeso 5:1, 2.
-
-
Suluhisho Ni Nini?Amkeni!—1996 | Agosti 22
-
-
Suluhisho Ni Nini?
HALI ya wakimbizi si yenye kukosa tumaini kabisa. Kotekote ulimwenguni, mashirika ya ubinadamu hujitahidi kusaidia wale waliohamishwa na vita na matatizo mengineyo. Njia kuu wanayosaidia nayo ni kwa kuwasaidia wakimbizi kurudi katika nchi zao za uzaliwa.
Wakimbizi huacha nyumba, jamii, na nchi kwa sababu huhofu watauawa kimakusudi, kuteswa, kubakwa, kufungwa gerezani, kufanywa watumwa, kunyang’anywa vitu, au kufanywa wafe kwa njaa. Kwa hiyo kabla ya wakimbizi kurudi nyumbani kwa usalama, matatizo yaliyowafanya watoroke ni lazima yatatuliwe. Hata wakati mapambano ya kisilaha yakomapo hatimaye, kutokuwa na sheria na utengamano mara nyingi huzuia watu kwenda nyumbani. Akasema Agnes, mkimbizi Mrwanda aliye mama wa watoto sita: “Kutupeleka [kuturudisha] Rwanda kutakuwa kama kutupeleka kwenye makaburi yetu.”
Hata hivyo, tangu 1989, zaidi ya wakimbizi milioni tisa wamerudi nyumbani kwao. Milioni 3.6 hivi wamerudi Afghanistan kutoka Iran na Pakistan. Wakimbizi wengine milioni 1.6 katika nchi sita wamerudi Msumbiji, taifa lililoharibiwa kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe ya miaka 16.
Kurudi si rahisi. Mara nyingi nchi ambazo wakimbizi hurudi ni vifusi—vijiji vikiwa vimeporomoka, madaraja kuharibiwa, na barabara na viwanja kujawa na mabomu ya kutegwa ardhini. Hivyo, wakimbizi wanaorudi ni lazima waanze marekebisho tangu mwanzo si kwa maisha yao tu bali pia kwa nyumba, shule, kliniki za afya, na kila kitu chao kingine.
Hata hivyo, hata wakati mapambano yakomapo mahali pamoja, yakiruhusu wakimbizi kurudi, hayo huanza mahali pengine, yakisababisha mitiririko mipya ya wakimbizi. Kwa hiyo kusuluhisha tatizo la wakimbizi, kwamaanisha kusuluhisha tatizo la vita, ukandamizaji, chuki, mnyanyaso, na visababishi vingine ambavyo hufanya watu watoroke ili kuokoa uhai.
Gazeti The State of the World’s Refugees 1995 hukiri hivi: “Kweli halisi . . . ni kwamba masuluhisho [kwa tatizo la wakimbizi] yategemea hasa mambo ya kisiasa, kijeshi na kiuchumi ambayo hayawezi kusuluhishwa na shirika lolote la ubinadamu.” Kulingana na Biblia, masuluhisho pia hayawezi kufikiwa na shirika lolote la kidunia, la ubinadamu au jinginelo.
Ulimwengu Usio na Wakimbizi
Hata hivyo, kuna suluhisho. Biblia huonyesha kwamba Yehova Mungu hujali wale ambao wametenganishwa na nyumba zao na familia zao. Tofauti na serikali za dunia, yeye ana uwezo na hekima ya kusuluhisha matatizo yote magumu yanayokabili jamii ya kibinadamu. Atafanya hivyo kupitia Ufalme wake—serikali ya kimbingu ambayo karibuni itadhibiti mambo ya dunia.
Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu. Badala ya kuwa na serikali nyingi duniani, kama tulizo nazo sasa, kutakuwa na serikali moja tu, ambayo itatawala juu ya sayari yote. Biblia hutabiri: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Huenda unafahamu ile sala ya kiolezo ipatikanayo katika Biblia kwenye Mathayo 6:9-13. Sehemu ya sala hiyo husema: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni.” Kupatana na sala hiyo, Ufalme wa Mungu karibuni ‘utakuja’ na kutimiza kusudi la Mungu kwa dunia.
Chini ya utawala huo wenye upendo wa Ufalme wa Mungu, kutakuwako amani na usalama wa ulimwengu wote mzima. Hakutakuwa tena na chuki na mapigano kati ya vikundi vya watu na mataifa ya dunia. (Zaburi 46:9) Hakutakuwa kamwe na mamilioni ya wakimbizi wanaotoroka ili kuokoa uhai wao au wanaonyong’onyea katika kambi.
Neno la Mungu laahidi kwamba Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Kristo Yesu, “atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”—Zaburi 72:12-14.
-