Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Familia za Kikristo—‘Kaeni Macho’
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Mei 15
    • Familia za Kikristo—‘Kaeni Macho’

      “Na tukae macho na kutunza akili zetu.”—1 THE. 5:6.

      1, 2. Ni nini kinachohitajiwa ili familia iweze kukaa macho kiroho?

      KUHUSU “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha,” mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Thesalonike: “Akina ndugu, hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi, kwa maana ninyi nyote ni wana wa nuru na wana wa mchana. Sisi si wa usiku wala si wa giza.” Paulo aliongezea hivi: “Kwa hiyo, basi, na tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali na tukae macho na kutunza akili zetu.”—Yoe. 2:31; 1 The. 5:4-6.

      2 Shauri la Paulo kwa Wathesalonike linawafaa kabisa hasa Wakristo wanaoishi “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4) Kadiri mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unavyozidi kukaribia, ndivyo Shetani anavyoazimia kuwageuza waabudu wengi iwezekanavyo wa kweli ili waache kumtumikia Mungu. Kwa hiyo, tunatenda kwa hekima tunapochukua kwa uzito himizo au shauri la Paulo la kuendelea kukaa macho kiroho. Ili familia ya Kikristo iweze kukaa macho, ni jambo la maana kwa kila mshiriki kutimiza daraka lake la Kimaandiko. Basi, waume, wake, na watoto wanatimiza daraka gani katika kuzisaidia familia zao ‘kukaa macho’?

      Waume—Mwigeni “Mchungaji Mwema”

      3. Kulingana na andiko la 1 Timotheo 5:8, daraka la mwanamume akiwa kichwa cha familia linatia ndani nini?

      3 Biblia inasema “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Kor. 11:3) Daraka la mwanamume akiwa kichwa cha familia linatia ndani nini? Maandiko yanasema hivi kuhusu daraka moja la kichwa cha familia: “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Tim. 5:8) Kwa kweli, mwanamume anapaswa kuiandalia familia yake mahitaji ya kimwili. Hata hivyo, ili aisaidie familia yake kukaa macho kiroho, ni lazima afanye mengi zaidi kuliko tu kuwapa mahitaji ya kimwili. Anahitaji kuijenga familia yake kiroho, na kuwasaidia washiriki wote wa familia kutia nguvu uhusiano wao pamoja na Mungu. (Met. 24:3, 4) Anaweza kufanya hivyo jinsi gani?

      4. Ni nini kinachoweza kumsaidia mwanamume afanikiwe kuijenga familia yake kiroho?

      4 Kwa kuwa “mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko,” mwanamume aliyeoa anapaswa kuchunguza na kuiga ukichwa wa Yesu juu ya kutaniko. (Efe. 5:23) Fikiria jinsi Yesu alivyoeleza kuhusu uhusiano wake pamoja na wafuasi wake. (Soma Yohana 10:14, 15.) Ni ufunguo gani ambao unaweza kumsaidia mwanamume ambaye anataka kuijenga familia yake kiroho apate matokeo mazuri? Huu ndio ufunguo: Jifunze mambo ambayo Yesu alisema na kutenda akiwa “mchungaji mwema,” na ‘ufuate hatua zake kwa ukaribu.’—1 Pet. 2:21.

      5. Yule Mchungaji Mwema ana ujuzi gani kuhusu kutaniko?

      5 Kwa njia ya mfano, uhusiano kati ya mchungaji na kondoo wake unategemea ujuzi na kuaminiana. Mchungaji anajua kila jambo kuhusu kondoo wake, na kondoo wanamjua na kumwamini mchungaji wao. Wanatambua na kutii sauti yake. Yesu alisema hivi: “Ninawajua kondoo wangu na kondoo wangu wananijua.” Yesu hana ujuzi wa kijuu-juu tu kuhusu kutaniko. Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa ‘kujua’ linamaanisha “ujuzi wa ndani sana kumhusu mtu binafsi.” Ndiyo, yule Mchungaji Mwema anawajua kondoo wake kibinafsi. Anajua mahitaji, udhaifu, na sifa nzuri za kila mmoja wao. Yesu ambaye ni Kielelezo chetu anaona kila jambo linalowahusu kondoo wake. Na kondoo hao wanamjua vizuri kabisa mchungaji wao na wanaamini uongozi wake.

      6. Waume wanaweza kumwiga jinsi gani yule Mchungaji Mwema?

      6 Ili mume amwige Kristo katika kutumia ukichwa wake, ni lazima ajifunze kufikiria hali yake akiwa mchungaji na kuwafikiria wale ambao anawatunza kama kondoo. Anapaswa kujitahidi kuwa na ujuzi wa ndani kuhusu familia yake. Je, kweli mume anaweza kuwa na ujuzi wa aina hiyo? Ndiyo, anaweza kwa kuzungumza au kuwasiliana vizuri na washiriki wote wa familia yake, kusikiliza mahangaiko yao, kuongoza katika utendaji wa familia, na kujitahidi kabisa kufanya maamuzi mazuri kuhusu mambo kama vile ibada ya familia, kuhudhuria mikutano, utumishi wa shambani, tafrija, na vitumbuizo. Mume Mkristo anapoongoza akiwa na ujuzi si wa Neno la Mungu tu bali pia ujuzi kuhusu wale ambao amepewa daraka la kuwatunza, inaelekea sana kwamba washiriki wa familia yake watakuwa na uhakika katika ukichwa wake naye atafurahi kuona wakiendelea kutumika pamoja katika ibada ya kweli.

      7, 8. Mume anaweza kumwiga yule Mchungaji Mwema jinsi gani katika kuwaonyesha upendo wale walio chini ya utunzaji wake?

      7 Mchungaji mzuri anawapenda pia kondoo wake. Tunapojifunza masimulizi ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu, moyo wetu unatuchochea kuthamini upendo ambao Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake. Hata ‘aliitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.’ Waume wanapaswa kumwiga Yesu kwa kuwaonyesha upendo wale walio chini ya utunzaji wao. Badala ya kumtawala mke wake kwa ukali, mume ambaye anatamani kupata kibali cha Mungu anaendelea kumpenda mke wake “kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko.” (Efe. 5:25) Mume anapaswa kumwambia mke wake maneno yenye fadhili na ya ufikirio, kwa sababu mke anastahili heshima.—1 Pet. 3:7.

      8 Kichwa cha familia anapowazoeza watoto wake, anapaswa kushikamana kabisa na kanuni za kimungu. Hata hivyo, hapaswi kamwe kukosa kuwaonyesha watoto wake upendo. Anapaswa kuwatia nidhamu kwa upendo inapohitajika. Watoto fulani wanaweza kuchukua muda mrefu zaidi kuelewa maagizo ya wazazi kuliko watoto wengine. Baba anapaswa kuwa mwenye subira zaidi anaposhughulika na watoto kama hao. Wanaume wanapoendelea kufuata sikuzote mfano wa Yesu, wanatokeza hali yenye amani na usalama nyumbani. Familia zao zinafurahia usalama wa kiroho ambao mtunga-zaburi aliimba kuuhusu.—Soma Zaburi 23:1-6.

      9. Kama Noa, aliyekuwa mzee wa ukoo, wanaume Wakristo wana daraka gani, na ni nini kitakachowasaidia kubeba daraka hilo?

      9 Noa, aliyekuwa mzee wa ukoo, aliishi katika kipindi cha mwisho cha ulimwengu wa siku zake. Lakini Yehova alimlinda “akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Pet. 2:5) Noa alikuwa na daraka la kuisaidia familia yake kuokoka Gharika. Wanaume Wakristo ambao ni vichwa vya familia wanakabili hali kama hiyo katika siku hizi za mwisho. (Mt. 24:37) Ni jambo la maana kama nini kwamba wajifunze mfano wa yule “mchungaji mwema” na kujitahidi kumwiga!

      Wake—‘Mjenge Nyumba Zenu’

      10. Inamaanisha nini mke kujitiisha chini ya mume wake?

      10 Mtume Paulo aliandika hivi: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana.” (Efe. 5:22) Maneno hayo hayaonyeshi kwa njia yoyote kwamba cheo cha wake si cha heshima. Kabla ya kumuumba Hawa, mwanamke wa kwanza, Mungu wa kweli alitangaza hivi: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” (Mwa. 2:18) Daraka la “msaidizi” na “kikamilisho,” yaani, kumuunga mkono mume wake anapotimiza madaraka yake katika familia, ni daraka lenye heshima kwelikweli.

      11. Mke ambaye ni mfano mzuri ‘anaijenga nyumba yake’ jinsi gani?

      11 Mke ambaye ni mfano mzuri anajitahidi kuijenga familia yake. (Soma Methali 14:1.) Tofauti na mwanamke mpumbavu ambaye haheshimu mpango wa ukichwa, mwanamke mwenye hekima anaheshimu sana mpango huo. Badala ya kuonyesha mtazamo wa ulimwengu wa kutotii na kujitegemea, mwanamke mwenye hekima anajitiisha chini ya mume wake. (Efe. 2:2) Mke ambaye ni mpumbavu haogopi kusema mabaya kumhusu mume wake, lakini mwanamke mwenye hekima anajitahidi kuongeza heshima ambayo mume wake anapata kutoka kwa watoto wake na watu wengine. Mke kama huyo anajitahidi sana kutodharau ukichwa wa mume wake kwa kumsumbua-sumbua au kubishana naye. Pia, anajitahidi kutumia pesa vizuri. Inaelekea kwamba mwanamke mpumbavu anatumia vibaya pesa ambazo familia yake inapata kwa shida. Mwanamke anayemuunga mkono mume wake hayuko hivyo. Anashirikiana na mume wake katika mambo ya kifedha. Anafanya mambo kwa busara na kutumia pesa kwa uangalifu. Hamsukumi mume wake afanye kazi nyingine ya ziada.

      12. Mke anaweza kufanya nini ili kuisaidia familia yake ‘kukaa macho’?

      12 Mke ambaye ni mfano mzuri anaisaidia familia ‘kukaa macho’ kwa kumsaidia mume wake katika kuwafundisha watoto mambo ya kiroho. (Met. 1:8) Anaunga mkono kwa bidii programu ya Ibada ya Familia. Zaidi ya hayo, anamuunga mkono mume wake anapowashauri na kuwatia nidhamu watoto wao. Yuko tofauti kabisa na mwanamke ambaye hashirikiani na mume wake, na hivyo watoto wake wanateseka kimwili na kiroho!

      13. Kwa nini ni jambo la maana kwa mke kumuunga mkono mume wake anaposhiriki kwa bidii katika shughuli za kiroho?

      13 Mke anayemuunga mkono mume wake anahisi jinsi gani anapomwona akitimiza madaraka yake kwa bidii katika kutaniko la Kikristo? Anakuwa na shangwe kwelikweli! Iwe mume wake ni mtumishi wa huduma, mzee, au labda mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali au Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa, mke huyo anafurahia pendeleo la mume wake. Bila shaka, atahitaji kujidhabihu ili amuunge mkono kwa bidii mume wake kupitia maneno na matendo yake. Lakini anajua kwamba mume wake anaposhiriki kwa bidii katika shughuli za kiroho anaisaidia familia yote kukaa macho kiroho.

      14. (a) Ni hali gani inayoweza kuwa ngumu kwa mke anayemuunga mkono mume wake, naye anaweza kukabiliana jinsi gani na hali hiyo? (b) Mke anaweza kusaidia jinsi gani ili familia nzima iwe na hali njema?

      14 Si rahisi kwa mke kuweka mfano mzuri katika kumuunga mkono mume wake wakati anapofanya uamuzi ambao mke hakubaliani nao. Hata wakati huo, mke anaonyesha “roho ya utulivu na ya upole” na kushirikiana naye ili uamuzi wake ufanikiwe. (1 Pet. 3:4) Mke mwema anajaribu kuiga mifano mizuri ya wanawake waliomwogopa Mungu nyakati za kale, kama vile, Sara, Ruthu, Abigaili, na Maria, mama ya Yesu. (1 Pet. 3:5, 6) Pia, anawaiga wanawake wenye umri mkubwa leo “wenye tabia ya kumhofu Mungu.” (Tito 2:3, 4) Kwa kumpenda na kumheshimu mume wake, mwanamke ambaye ni mfano mzuri anasaidia sana katika kufanikisha ndoa yao na kuchangia hali njema ya familia nzima. Nyumba yake ni mahali salama na penye kustarehesha. Mwanamume wa kiroho anamthamini sana mke anayemuunga mkono!—Met. 18:22.

      Vijana—‘Endeleeni Kukaza Macho Yenu Juu ya Vitu Visivyoonekana’

      15. Vijana wanaweza kushirikiana jinsi gani na wazazi wao ili familia ‘ikae macho’?

      15 Ninyi vijana mnaweza jinsi gani kushirikiana na wazazi wenu ili familia yenu ‘ikae macho’ kiroho? Fikirieni zawadi ambayo Yehova ameweka mbele yenu. Labda tangu mlipokuwa watoto, wazazi wenu waliwaonyesha picha zinazoonyesha jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso. Mlipoendelea kukua, inaelekea kwamba walitumia Biblia na vichapo vya Kikristo kuwasaidia kuwazia katika akili zenu jinsi uzima wa milele utakavyokuwa katika ulimwengu mpya. Kukazia macho yenu utumishi wa Yehova na kupanga maisha yenu vizuri kutawasaidia ‘kukaa macho.’

      16, 17. Vijana wanaweza kufanya nini ili wafanikiwe kukimbia mbio ya uzima?

      16 Chukueni kwa uzito maneno ya mtume Paulo yaliyo katika andiko la 1 Wakorintho 9:24. (Soma.) Kimbieni mbio ya uzima mkiwa na kusudi moja tu la kushinda. Chagueni maisha ambayo yatawasaidia kupata zawadi ya uzima wa milele. Vijana wengi wameruhusu kufuatia vitu vya kimwili kuwakengeushe na hivyo wameacha kukazia macho yao ile zawadi. Hilo ni jambo la upumbavu kama nini! Kupanga kutumia maisha yetu kutafuta utajiri hakuleti furaha ya kweli. Vitu ambavyo vinaweza kununuliwa kwa pesa ni vya muda tu. Hata hivyo, endeleeni kukaza macho yenu juu ya “vitu visivyoonekana.” Kwa nini? Kwa sababu “vitu visivyoonekana ni vya milele.”—2 Kor. 4:18.

      17 “Vitu visivyoonekana” vinatia ndani baraka za Ufalme. Panga kuishi maisha yako kwa njia ambayo itakuwezesha kupata baraka hizo. Furaha ya kweli inatokana na kutumia maisha yako katika utumishi wa Yehova. Tunapomtumikia Mungu wa kweli tunapata nafasi za kujitahidi kufikia miradi ya muda mfupi na pia miradi ya muda mrefu.a Kujiwekea miradi ya kiroho unayoweza kutimiza kunaweza kukusaidia kukazia macho kumtumikia Mungu ukiwa na kusudi la kupata zawadi ya uzima wa milele.—1 Yoh. 2:17.

      18, 19. Kijana anaweza kujua namna gani ikiwa amefanya kweli iwe mali yake mwenyewe?

      18 Enyi vijana, hatua ya kwanza katika barabara ya uzima ni kufanya kweli iwe mali yenu. Je, umechukua hatua hiyo? Jiulize hivi: ‘Je, mimi ni mtu wa kiroho, au ninashiriki katika utendaji wa kiroho kwa sababu tu ya wazazi wangu? Je, ninasitawisha sifa ambazo zinafanya nimpendeze Mungu? Je, ninajitahidi kuwa na programu ya kawaida ya kushiriki katika utendaji unaohusiana na ibada ya kweli, kama vile kusali kwa ukawaida, kujifunza, kuhudhuria mikutano, na kushiriki katika utumishi wa shambani? Je, ninamkaribia Mungu kwa kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja naye?’—Yak. 4:8.

      19 Tafakari kuhusu mfano wa Musa. Hata ingawa alifundishwa utamaduni wa kigeni, alichagua kutambuliwa kuwa mwabudu wa Yehova badala ya kuitwa mwana wa binti ya Farao. (Soma Waebrania 11:24-27.) Enyi vijana Wakristo, ninyi pia mnahitaji kuazimia kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Mkifanya hivyo, mtapata furaha ya kweli, maisha mazuri kabisa sasa, na tumaini la ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli.’—1 Tim. 6:19.

      20. Katika mbio ya uzima, ni nani wanaopokea zawadi?

      20 Katika michezo ya zamani, mkimbiaji mmoja tu ndiye aliyeshinda mashindano ya mbio. Hali ni tofauti katika mbio ya uzima. Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Watu wengi walioishi kabla yako wamekimbia kwa mafanikio, na wengi wanaendelea kukimbia pamoja nawe. (Ebr. 12:1, 2) Wote ambao hawachoki watapata zawadi. Kwa hiyo, azimia kushinda!

      21. Habari inayofuata itazungumzia nini?

      21 Hatuwezi kuepuka “kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.” (Mal. 4:5) Siku hiyo haipaswi kuzipata familia za Kikristo kwa ghafula. Ni jambo la maana kwa wote katika familia kubeba daraka lao la Kimaandiko. Ni nini kingine unachoweza kufanya ili uendelee kukaa macho kiroho na kutia nguvu uhusiano wako pamoja na Mungu? Habari inayofuata itazungumzia mambo matatu ambayo yanaweza kuisaidia familia nzima iwe na hali njema ya kiroho.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 15, 2010 (15/11/2010), ukurasa wa 12-16; Julai 15, 2004, ukurasa wa 21-23.

  • Familia za Kikristo—“Endeleeni Kuwa Tayari”
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Mei 15
    • Familia za Kikristo—“Endeleeni Kuwa Tayari”

      “Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyoitazamia.”—LUKA 12:40.

      1, 2. Kwa nini tunapaswa kuchukua kwa uzito himizo la Yesu la ‘kuendelea kuwa tayari’?

      “WAKATI Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake” na kuwatenganisha “watu, mmoja kutoka kwa mwenzake,” ni nini kitakachotukia kwako wewe na kwa familia yako? (Mt. 25:31, 32) Kwa kuwa jambo hilo litatukia katika saa tusiyotazamia, ni jambo la maana kama nini kwetu kuchukua kwa uzito himizo au shauri la Yesu la ‘kuendelea kuwa tayari’!—Luka 12:40.

      2 Habari iliyotangulia ilizungumzia jinsi kila mshiriki wa familia anavyoweza kuisaidia familia nzima kuendelea kukaa macho kiroho kwa kuchukua kwa uzito daraka lake. Acheni tuzungumzie njia nyingine ambazo tunaweza kuisaidia familia yetu kuwa na hali nzuri ya kiroho.

      Endelea Kuwa na Jicho “Rahisi”

      3, 4. (a) Familia za Kikristo zinapaswa kujilinda kutokana na nini? (b) Ni nini maana ya kuwa na jicho “rahisi”?

      3 Ili washiriki wa familia wawe tayari wakati ambapo Kristo atakuja, ni lazima wawe makini kutokengeushwa kutoka kwa mambo yanayohusu ibada ya kweli. Wanahitaji kujilinda ili wasipotoshwe na mambo yanayokengeusha fikira. Kwa kuwa kufuatia vitu vya kimwili ni mtego ambao umenasa familia nyingi, fikirieni yale ambayo Yesu alisema kuhusu kudumisha jicho “rahisi.” (Soma Mathayo 6:22, 23.) Kama vile tu ambavyo taa inaweza kuangaza njia yetu na kutuwezesha kutembea bila kuanguka, vivyo hivyo mambo tunayotazama kwa ‘macho ya mfano ya moyo wetu’ yanaweza kuangaza njia yetu na kutusaidia kutembea bila kujikwaa.—Efe. 1:18.

      4 Ili jicho halisi lione waziwazi, ni lazima lifanye kazi vizuri na kuweza kukazia kitu ambacho linatazama. Ndivyo ilivyo na macho ya moyo. Kuwa na jicho rahisi la mfano kunamaanisha kwamba tunakazia fikira kusudi moja. Badala ya kuishi maisha ambayo yanakazia fikira vitu vya kimwili na kuhangaika kupita kiasi kuhusu kutosheleza mahitaji ya kimwili ya familia yetu, jicho letu linakazia mambo ya kiroho. (Mt. 6:33) Hilo linamaanisha kwamba tunatosheka na mahitaji yetu ya lazima ambayo Mungu anatusaidia kupata na kutanguliza utumishi wake katika maisha yetu.—Ebr. 13:5.

      5. Msichana fulani tineja alionyesha jinsi gani kwamba “jicho” lake lilikazia kumtumikia Mungu?

      5 Matokeo yanaweza kuwa mazuri kama nini watoto wakizoezwa kuendelea kuwa na jicho rahisi! Fikiria mfano wa msichana mmoja tineja katika nchi ya Ethiopia. Alifanya vizuri sana shuleni hivi kwamba alipomaliza masomo yake ya msingi, alipewa nafasi ya kulipiwa masomo ili apate elimu zaidi. Hata hivyo, kwa sababu jicho lake lilikazia kumtumikia Yehova, alikataa nafasi hiyo. Baada ya muda mfupi, alipewa nafasi ya kufanya kazi ambayo angelipwa mshahara wa dola za Marekani 4,200 kwa mwezi, pesa nyingi sana zikilinganishwa na mishahara ambayo watu wengi wanapata katika nchi yake. Lakini “jicho” la msichana huyo lilikazia utumishi wa painia. Hakuhitaji kuzungumza na wazazi wake kabla ya kukataa kazi hiyo. Wazazi wake walihisi namna gani waliposikia kuhusu jambo ambalo binti yao alifanya? Kwa kweli, walifurahi pamoja naye na kumwambia jinsi walivyojivunia yeye kuwa binti yao!

      6, 7. Tunapaswa ‘kuendelea kufungua macho yetu’ ili tuone hatari gani?

      6 Katika andiko la Mathayo 6:22, 23, Yesu anatoa onyo lisilo la moja kwa moja kuhusu pupa. Yesu hakusema kwamba kinyume cha jicho “rahisi” ni jicho “linalokazia mambo mengi,” badala yake alisema kinyume chake ni jicho “bovu.” ‘Jicho bovu’ ni jicho baya; lenye wivu, yaani, lina pupa au linatamani. (Mt. 6:23) Yehova anahisi namna gani kuhusu kutamani au pupa? Biblia inasema: “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa [au, kutamani] visitajwe hata kidogo katikati yenu.”—Efe. 5:3.

      7 Ingawa inaweza kuwa rahisi kugundua kwamba wengine wana pupa, ni vigumu zaidi kugundua kwamba sisi wenyewe tuna pupa. Hivyo, ni jambo la hekima kwetu kutii shauri hili la Yesu: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa.” (Luka 12:15) Ili tufanye hivyo ni lazima tujichunguze na kuona tunakazia nini katika mioyo yetu. Familia za Kikristo zinapaswa kufikiria kwa uzito wakati na pesa ambazo wanatumia katika vitumbuizo, tafrija, na kununua vitu vya kimwili.

      8. Inapohusu kununua vitu, tunaweza jinsi gani ‘kuendelea kufungua macho yetu’?

      8 Kabla ya kununua kitu, unapaswa kufikiria mambo mengi zaidi kuliko tu kuamua ikiwa unaweza kukinunua au huwezi. Fikiria mambo kama haya: ‘Je, nitakuwa na wakati wa kutumia kitu hicho kwa ukawaida na kukitunza? Nitahitaji muda mrefu kadiri gani kujifunza kukitumia vizuri?’ Enyi vijana, msiamini mambo yote ambayo matangazo ya kibiashara ulimwenguni yanasema kuhusu vitu vinavyouzwa na kuwafanya mnunue mitindo ya mavazi ya bei ghali na vitu vingine ambavyo si vya lazima. Mjizuie. Pia, fikiria ikiwa kupata kitu fulani kutaisaidia familia yako kujitayarisha kwa ajili ya kuja kwa Mwana wa binadamu. Uwe na imani katika ahadi hii ya Yehova: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—Ebr. 13:5.

      Fuatia Miradi ya Kiroho

      9. Kufuatia miradi ya kiroho kunaweza kuisaidia familia jinsi gani?

      9 Njia nyingine ambayo washiriki wa familia wanaweza kutia nguvu imani yao na kuisaidia familia nzima kuwa na hali nzuri ya kiroho ni kujiwekea miradi ya kiroho na kuifuatia. Kufanya hivyo kunaweza kuzisaidia familia kutambua maendeleo wanayofanya katika kutimiza kusudi lao la kumpendeza Yehova na pia kuamua ikiwa utendaji fulani ni wa maana au si wa maana sana.—Soma Wafilipi 1:10.

      10, 11. Mnafuatia miradi gani ya kiroho mkiwa familia, na mngependa kujiwekea miradi gani ya wakati ujao?

      10 Hata mnaweza kupata baraka nyingi mkijiwekea miradi midogo inayofaa ambayo karibu kila mshiriki wa familia anaweza kuifikia. Kwa mfano, fikiria mradi wa kuzungumzia andiko la siku kila siku. Maelezo yanayotolewa na washiriki wa familia yanaweza kumsaidia kichwa cha familia kutambua kiwango cha hali yao ya kiroho. Mradi wa kusoma Biblia pamoja kwa ukawaida mkiwa familia unawapa watoto nafasi nzuri sana ya kuboresha uwezo wao wa kusoma na pia kuelewa vizuri zaidi ujumbe wa Biblia. (Zab. 1:1, 2) Na je, hatupaswi kujiwekea mradi wa kuboresha sala zetu? Kusitawisha kwa kadiri kubwa zaidi sifa za tunda la roho kunaweza pia kuwa mradi mzuri sana wa kufuatia. (Gal. 5:22, 23) Au je, mnaweza kutafuta njia za kuwatendea kwa huruma watu mnaokutana nao katika huduma? Kujitahidi kufanya hivyo mkiwa familia kunaweza kuwasaidia watoto kujifunza kuwa wenye huruma, na inaelekea sana kwamba watakuza tamaa ya kutumika wakiwa mapainia wa kawaida au wamishonari.

      11 Kwa nini usifikirie miradi fulani ambayo wewe na familia yako mnaweza kufuatia? Je, familia yako inaweza kujiwekea mradi wa kutumia muda zaidi katika huduma? Je, mnaweza kujiwekea mradi wa kuwa na ujasiri wa kutoa ushahidi barabarani, katika maeneo ya kibiashara, au kwa kutumia simu? Je, mnaweza kwenda kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme? Je, mshiriki mmoja wa familia yenu anaweza kujifunza lugha ya kigeni ili awahubirie habari njema watu wa nchi nyingine?

      12. Vichwa vya familia wanaweza kufanya nini ili kuzisaidia familia zao kukua kiroho?

      12 Ukiwa kichwa cha familia, angalia mambo ambayo familia yako inaweza kutimiza ili ifanye maendeleo kiroho. Kisha, mjiwekee miradi hususa yenye kujenga ya kuwasaidia kutimiza kusudi hilo. Miradi ambayo mnajiwekea mkiwa familia inapaswa kuwa inayofaa na ambayo mnaweza kuifikia kulingana na uwezo na hali zenu. (Met. 13:12) Bila shaka, muda unahitajika ili kujitahidi kufikia mradi fulani wa maana. Kwa hiyo, nunueni wakati ambao mnatumia kutazama televisheni na kuutumia kufuatia mambo ya kiroho. (Efe. 5:15, 16) Ujitahidi kufikia miradi ambayo unaiwekea familia yako. (Gal. 6:9) Familia ambayo inafuatia miradi ya kiroho itafanya maendeleo yake “yawe wazi kwa watu wote.”—1 Tim. 4:15.

      Endeleeni Kuwa na Jioni ya Ibada ya Familia

      13. Ni badiliko gani ambalo lilifanywa katika ratiba ya kila juma ya mikutano ya kutaniko, na ni maswali au maulizo gani tunayopaswa kutafakari?

      13 Badiliko kubwa ambalo lilifanywa kuanzia Januari 1, 2009 (1/1/2009) katika ratiba au programu ya kila juma ya mikutano ni mpango mzuri zaidi wa kuzisaidia familia ‘kuendelea kuwa tayari’ kwa ajili ya kuja kwa Mwana wa binadamu. Hatuhitaji tena kukutana pamoja katika siku tofauti kwa ajili ya mkutano ambao ulikuwa ukiitwa Funzo la Kitabu la Kutaniko kwa sababu mkutano huo uliunganishwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Badiliko hilo lilifanywa ili familia za Kikristo zipate nafasi ya kujenga hali yao ya kiroho kwa kutenga jioni moja kila juma ili kuwa na ibada ya familia. Sasa kwa kuwa muda fulani umepita tangu badiliko hilo lilipofanywa, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninatumia vizuri wakati ambao umetengwa ili kuwa na jioni ya Ibada ya Familia au kuwa na funzo la kibinafsi? Je, nimefanikiwa kutimiza kusudi la mpango huo?’

      14. (a) Ni nini kusudi kuu la kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia au funzo la kibinafsi? (b) Kwa nini ni jambo la maana kutenga jioni moja kwa ajili ya kujifunza?

      14 Kusudi kuu la kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia au wakati wa funzo la kibinafsi ni kumkaribia Mungu zaidi. (Yak. 4:8) Tunapotumia wakati kujifunza Biblia kwa ukawaida na kuongeza ujuzi wetu kumhusu Muumba, uhusiano wetu pamoja naye unatiwa nguvu. Kadiri tunavyozidi kumkaribia Yehova, ndivyo tunavyochochewa zaidi kumpenda ‘kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote, kwa akili yetu yote, na kwa nguvu zetu zote.’ (Marko 12:30) Bila shaka, tunatamani kumtii Mungu na kumwiga. (Efe. 5:1) Basi, kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia kwa ukawaida, ni jambo la maana linalowasaidia washiriki wote wa familia yetu ‘kuendelea kuwa tayari’ kiroho tunapongojea “dhiki kuu” iliyotabiriwa. (Mt. 24:21) Hilo ni jambo la maana ili tuokolewe.

      15. Jioni ya Ibada ya Familia inaweza kuwasaidia washiriki wa familia wawe na hisia gani kuelekea washiriki wenzao wa familia?

      15 Mpango wa Ibada ya Familia unatimiza pia kusudi lingine—kuwasaidia washiriki wa familia kuwa na uhusiano wa karibu kati yao. Kutumia wakati pamoja kuzungumzia mambo ya kiroho kila juma kunaboresha sana jinsi washiriki wa familia wanavyohisi kuhusu wengine katika familia. Wenzi wa ndoa wanakuwa na uhusiano wa karibu sana wanaposikia mwenzi wao akishangilia wanapopata wakiwa pamoja hazina ya kiroho katika funzo! (Soma Mhubiri 4:12.) Inaelekea kwamba wazazi na watoto wanaoabudu pamoja wanaunganishwa na upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Kol. 3:14.

      16. Simulia jinsi dada watatu kiroho wanavyofaidika kwa kutenga jioni moja ya kujifunza Biblia.

      16 Fikiria jinsi ambavyo dada watatu wa kiroho wamefaidika kupitia mpango wa kutenga jioni moja kwa ajili ya funzo la Biblia. Ingawa dada hao hawana uhusiano wa kiukoo, wajane hao watatu waliozeeka wanaishi katika mji mmoja na wamekuwa marafiki wa karibu kwa miaka mingi. Kwa kuwa walitaka sana kushirikiana zaidi pamoja na wakati huohuo kufaidika kiroho badala ya kufurahia ushirika tu wa kirafiki, waliamua kutenga jioni moja ili wakutane na kujifunza Biblia. Walianza kujifunza wakitumia kitabu “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu. Mmoja wao anasema hivi: “Tunafurahia sana wakati huo hivi kwamba kwa kawaida tunajifunza kwa zaidi ya saa nzima. Tunajaribu kuwazia akilini hali za ndugu zetu wa karne ya kwanza, na tunazungumzia jinsi ambavyo tungetenda katika hali kama hizo. Kisha tunajaribu kutumia katika huduma mambo tuliyojifunza kutokana na mazungumzo yetu. Hilo limefanya kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi iwe yenye kufurahisha zaidi na yenye matokeo zaidi kuliko mwanzoni.” Mpango huo umewajenga kiroho marafiki hao watatu na zaidi ya hilo umewasaidia kuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi. Wanasema hivi: “Tunathamini sana mpango huo.”

      17. Ni mambo gani yanayosaidia jioni ya Ibada ya Familia iwe yenye matokeo mazuri?

      17 Namna gani wewe? Unafaidika jinsi gani kwa kutenga jioni ya kuwa na ibada ya familia au funzo la kibinafsi? Mpango huo usipofuatwa kwa ukawaida, hauwezi kutimiza kusudi lake. Kila mshiriki wa familia anapaswa kuwa tayari kujifunza wakati uliowekwa. Mambo madogo-madogo hayapaswi kuruhusiwa kuvuruga jioni hiyo. Zaidi ya hayo, mnapaswa kuchagua mambo ya kujifunza ambayo yanafanya pindi hiyo iwe yenye kujenga familia yenu. Mnaweza kufanya nini ili vipindi hivyo vya kujifunza viwe vyenye kufurahisha? Tumieni njia mbalimbali za kujifunza zenye matokeo mazuri, na mdumishe mazingira matulivu na yenye heshima.—Yak. 3:18.a

      ‘Kaa Macho’ na ‘Uendelee Kuwa Tayari’

      18, 19. Kujua kwamba Mwana wa binadamu yuko karibu kuja kunapaswa kukuchochea jinsi gani wewe na familia yako?

      18 Hali za ulimwengu ambazo zinazidi kuwa mbaya katika siku zetu zinaonyesha waziwazi kwamba tangu mwaka wa 1914, ulimwengu mwovu wa Shetani uliingia katika siku zake za mwisho. Mawingu ya dhoruba ya Har–Magedoni yako karibu sana. Hivi karibuni Mwana wa binadamu atakuja kutekeleza hukumu ya Yehova juu ya watu waovu. (Zab. 37:10; Met. 2:21, 22) Je, kujua hivyo hakupaswi kukuchochea wewe na familia yako?

      19 Je, unatii shauri la Yesu la kuendelea kuwa na jicho “rahisi”? Ingawa huenda watu wa ulimwengu huu wakajitahidi kupata utajiri, umashuhuri, au mamlaka, je, familia yako inafuatia miradi ya kiroho? Je, mpango wa jioni ya Ibada ya Familia au wakati wa funzo la kibinafsi unakusaidia? Je, unatimiza vizuri makusudi ya mpango huo? Kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, je, unatimiza madaraka yako ya Kimaandiko ukiwa mume, mke, au mtoto, na hivyo kuisaidia familia nzima ‘kukaa macho’? (1 The. 5:6) Ikiwa unafanya hivyo, ‘utaendelea kuwa tayari’ kwa ajili ya kuja kwa Mwana wa binadamu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ili kupata mapendekezo kuhusu mambo ya kujifunza na jinsi ya kufanya jioni za Ibada ya Familia ziwe zenye faida na zenye kufurahisha, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Oktoba 15, 2009, ukurasa wa 29-31.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki