-
Ndoa Inaweza Kufanikiwa Katika Ulimwengu wa LeoMnara wa Mlinzi—2005 | Machi 1
-
-
Ndoa Inaweza Kufanikiwa Katika Ulimwengu wa Leo
“Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—WAKOLOSAI 3:14.
1, 2. (a) Ni jambo gani linalotia moyo kuhusiana na kutaniko la Kikristo? (b) Ndoa yenye mafaniko ni ipi?
TUNAPOTAZAMA washiriki mbalimbali wa kutaniko la Kikristo, je, haichangamshi moyo kuona watu wengi waliofunga ndoa ambao wamekuwa washikamanifu kwa wenzi wao kwa miaka 10, 20, 30, au hata kwa muda mrefu zaidi? Wamekuwa washikamanifu kwa wenzi wao kwa heri na kwa shari.—Mwanzo 2:24.
2 Wengi wao watakubali kwamba wamekuwa na matatizo katika ndoa zao. Mchunguzi mmoja aliandika hivi: “Ndoa zenye furaha hazikosi mahangaiko na matatizo. Kuna nyakati zenye furaha na nyakati za matatizo . . . Lakini . . . ndoa hizo zimedumu licha ya msukosuko wa maisha ya kisasa.” Wenzi ambao wamefanikiwa wamejifunza kukabiliana na misukosuko na misiba isiyoepukika ambayo husababishwa na mikazo ya maisha, hasa ikiwa wamelea watoto. Kutokana na mambo ambayo wamejionea, wenzi hao wamejifunza kwamba upendo wa kweli “haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:8.
3. Takwimu zinaonyesha nini kuhusu ndoa na talaka, na hilo linatokeza maswali gani?
3 Tofauti na hilo, ndoa nyingi zimevunjika. Ripoti moja inasema hivi: “Nusu ya ndoa zote huko Marekani leo zinatarajiwa kuishia katika talaka. Na nusu ya [talaka] hizo zitatokea katika miaka 7.8 ya kwanza ya ndoa . . . Kati ya asilimia 75 ya wale wanaofunga ndoa tena, asilimia 60 watatalikiana tena.” Talaka zimeongezeka hata katika nchi ambazo hapo awali zilikuwa na idadi ya chini ya talaka. Kwa mfano, huko Japani, idadi ya talaka imeongezeka karibu maradufu katika miaka ya hivi karibuni. Ni mikazo gani imechangia hali hiyo, mikazo ambayo nyakati nyingine huwaathiri hata washiriki wa kutaniko la Kikristo? Ni nini kinachohitajiwa ili ndoa ifanikiwe licha ya jitihada za Shetani za kudhoofisha mpango huo?
Mitego ya Kuepukwa
4. Ni baadhi ya mambo gani ambayo yanaweza kudhoofisha ndoa?
4 Neno la Mungu hutusaidia kuelewa baadhi ya mambo yanayoweza kudhoofisha ndoa. Kwa mfano, fikiria yale ambayo mtume Paulo alisema kuhusu hali ambazo zingekuwapo katika siku hizi za mwisho: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake; nawe geukia mbali kutoka kwa hao.”—2 Timotheo 3:1-5.
5. Kwa nini mtu ‘anayejipenda mwenyewe’ anahatarisha ndoa yake, nayo Biblia inatoa shauri gani kuhusiana na hilo?
5 Tunapochunguza maneno ya Paulo, tunaona kwamba mambo mengi aliyoorodhesha yanaweza kuharibu mahusiano ya ndoa. Kwa mfano, watu “wenye kujipenda wenyewe” wana ubinafsi na hawawafikirii wengine. Waume au wake wanaojipenda wenyewe hutaka tu kutimiza makusudi yao. Hawako tayari kubadilika. Je, mtazamo kama huo unaweza kuchangia furaha katika ndoa? Sivyo kabisa. Kwa hekima, mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo, kutia ndani wenzi wa ndoa: “[Hampaswi] kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi, mkiendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.”—Wafilipi 2:3, 4.
6. Kupenda pesa kunaweza kudhoofishaje uhusiano wa ndoa?
6 Kupenda pesa kunaweza kusababisha mgawanyiko kati ya mume na mke. Paulo alionya hivi: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Kwa kusikitisha, maneno hayo ya Paulo yametimia katika ndoa nyingi leo. Katika kufuatia mali, watu wengi wamepuuza mahitaji ya wenzi wao kutia ndani uhitaji wa kutegemezwa kihisia na kuwa na urafiki mchangamfu wenye kudumu.
7. Katika visa fulani, ni mwenendo gani umesababisha ukosefu wa ushikamanifu katika ndoa?
7 Paulo alisema pia kwamba katika siku hizi za mwisho watu fulani wangekuwa “wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote.” Nadhiri ya ndoa ni ahadi nzito ambayo inapaswa kuongoza kwenye kifungo chenye kudumu, haipaswi kuvunjwa kwa hila. (Malaki 2:14-16) Hata hivyo, wengine wamependezwa kimapenzi na watu ambao si wenzi wao wa ndoa. Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 30 na kitu, ambaye mume wake alimwacha anasema kwamba hata kabla ya kumwacha, mume wake alikuwa na uhusiano wa karibu na wanawake wengine naye aliwapenda sana. Alikosa kutambua kwamba alikuwa akijihusisha na mwenendo usiomfaa mwanamume aliyeoa. Aliumia sana alipoona jambo hilo likitukia, na kwa busara alijaribu kumwonya mume wake kwamba alikuwa akijihusisha na mwenendo hatari. Hata hivyo, mume wake alifanya uzinzi. Hata ingawa alionywa kwa fadhili, mwenzi huyo hakutaka kusikiliza. Alitumbukia kwenye mtego.—Methali 6:27-29.
8. Ni jambo gani linaloweza kuongoza kwenye uzinzi?
8 Biblia inaonya waziwazi kuhusu uzinzi. “Yeyote anayefanya uzinzi na mwanamke amepungukiwa moyoni; yule anayefanya hivyo anaiangamiza nafsi yake mwenyewe.” (Methali 6:32) Kwa kawaida, uzinzi si tendo linalofanywa ghafula bila kufikiriwa. Kama Yakobo, mwandikaji wa Biblia alivyoonyesha, kwa kawaida dhambi kama vile uzinzi hutukia baada tu ya wazo hilo kutungwa akilini na kufikiriwa kwa muda. (Yakobo 1:14, 15) Pole kwa pole, mwenzi anayezini huacha kuwa mshikamanifu kwa mwenzi wake ambaye aliapa atakuwa mwaminifu kwake katika maisha yake yote. Yesu alisema: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:27, 28.
9. Tunapata shauri gani lenye hekima kwenye Methali 5:18-20?
9 Kwa hiyo, mwenendo wenye hekima na mshikamanifu ni ule unaotajwa katika kitabu cha Methali: “Chemchemi yako ya maji na ibarikiwe, na ushangilie pamoja na mke wa ujana wako, paa mwenye kupendeka na mbuzi wa milimani mwenye kuvutia. Na maziwa yake yakuleweshe nyakati zote. Upendo wake na ukufurahishe sikuzote. Basi mwanangu, kwa nini umfurahie mwanamke mgeni au kukumbatia kifua cha mwanamke wa kigeni?”—Methali 5:18-20.
Usikimbilie Ndoa
10. Kwa nini ni jambo la hekima kuchukua wakati kumjua yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa?
10 Huenda matatizo yakatokea katika ndoa wenzi wa ndoa wanapoingia kwenye mpango huo haraka-haraka bila kufikiri. Huenda wakawa wachanga mno na wasio na uzoefu. Au labda hawachukui wakati kujuana, yaani, kujua mapendezi yao, miradi yao maishani, na malezi yao. Ni jambo la hekima kuwa na subira na kuchukua wakati kumjua yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa. Mfikirie Yakobo, mwana wa Isaka. Ilibidi kumfanyia kazi kwa miaka saba yule aliyetazamia kuwa baba-mkwe wake ili akubaliwe kumwoa Raheli. Alikuwa tayari kufanya hivyo kwa sababu hisia zake zilitegemea upendo wa kweli, na si kuvutiwa tu na urembo wa nje.—Mwanzo 29:20-30.
11. (a) Kifungo cha ndoa huunganisha nini? (b) Kwa nini ni muhimu kutumia usemi unaofaa katika ndoa?
11 Ndoa inahusisha mengi zaidi ya uhusiano wa kimapenzi. Kifungo cha ndoa huwaunganisha watu wawili kutoka malezi tofauti na wenye nyutu, hisia, na mara nyingi elimu tofauti. Mara nyingine kinaunganisha tamaduni mbili, na hata lugha mbili. Hata kama kifungo hicho hakiwaunganishi watu katika njia zilizotajwa, kinawaunganisha watu wawili wanaoweza kuwa na maoni tofauti. Watu hao wenye maoni tofauti ndio hufanyiza kifungo cha ndoa. Wanaweza kuwa wachambuzi na walalamikaji daima au wanaweza kuwa wenye kutia moyo na kujenga. Naam, maneno yetu yanaweza kuumiza au kuponya mwenzi wetu. Usemi usiodhibitiwa unaweza kutokeza mkazo mkubwa katika ndoa.—Methali 12:18; 15:1, 2; 16:24; 21:9; 31:26.
12, 13. Tunatiwa moyo tuwe na maoni gani halisi kuhusu ndoa?
12 Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuchukua wakati kumjua vizuri yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa. Dada mmoja Mkristo ambaye ameolewa kwa muda mrefu alisema hivi pindi moja: “Unapomchunguza yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa, fikiria sifa kumi hivi muhimu ambazo ungependa awe nazo. Ikiwa mtu huyo ana sifa saba tu, jiulize, ‘Je, niko tayari kupuuza zile sifa tatu ambazo hana? Je, kila siku nitavumilia upungufu huo?’ Ikiwa una shaka yoyote, tua na ufikirie tena.” Bila shaka, unapaswa kuona mambo kihalisi. Ukitaka kufunga ndoa, kumbuka kwamba hutapata kamwe mwenzi mkamilifu. Hata hivyo, yule ambaye utafunga naye ndoa hatapata mwenzi mkamilifu pia!—Luka 6:41.
13 Ndoa hutia ndani kujidhabihu. Paulo alikazia jambo hilo aliposema: “Nataka ninyi msiwe na mahangaiko. Mwanamume ambaye hajaoa huhangaikia mambo ya Bwana, jinsi anavyoweza kupata kibali cha Bwana. Lakini mwanamume aliyeoa huhangaikia mambo ya ulimwengu, jinsi anavyoweza kupata kibali cha mke wake, naye amegawanyika. Zaidi ya hayo, mwanamke mseja, na bikira, huhangaikia mambo ya Bwana, ili awe mtakatifu katika mwili wake na pia katika roho yake. Hata hivyo, mwanamke aliyeolewa huhangaikia mambo ya ulimwengu, jinsi anavyoweza kupata kibali cha mume wake.”—1 Wakorintho 7:32-34.
Kwa Nini Ndoa Fulani Hazifanikiwi?
14, 15. Ni nini kinachoweza kuchangia kudhoofika kwa kifungo cha ndoa?
14 Mwanamke mmoja Mkristo alipatwa na mfadhaiko wa talaka mume wake alipomwacha baada ya miaka 12 ya ndoa na kuanza urafiki na mwanamke mwingine. Je, aliona dalili zozote mbaya kabla ya ndoa yao kuvunjika? Anaeleza hivi: “Ilifikia wakati mume wangu hakuwa akisali tena. Alitoa visababu vya kukosa mikutano ya Kikristo na kwenda kuhubiri. Alidai kwamba alikuwa na shughuli nyingi mno au alikuwa amechoka sana hivi kwamba hakuwa na wakati wa kuwa pamoja nami. Alikataa kuzungumza nami. Hakuzungumza nami mambo ya kiroho. Inasikitisha kwamba alibadilika sana. Hakuwa tena yule mwanamume niliyefunga naye ndoa.”
15 Wengine wamesema kwamba wameona dalili hizohizo, kutia ndani kupuuzwa kwa funzo la kibinafsi la Biblia, sala, au kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Yaani, watu wengi ambao mwishowe waliwaacha wenzi wao waliruhusu uhusiano wao na Yehova udhoofike. Waliacha kukazia fikira mambo ya kiroho. Hawakumwona tena Yehova kuwa Mungu aliye hai. Ulimwengu mpya wa uadilifu unaoahidiwa haukuwa tena halisi kwao. Katika visa fulani, hali ya kiroho ilidhoofika hata kabla mwenzi aliyezini kuwa na uhusiano nje ya ndoa.—Waebrania 10:38, 39; 11:6; 2 Petro 3:13, 14.
16. Ni nini huimarisha ndoa?
16 Tofauti na hilo, mume na mke fulani ambao wana furaha sana katika ndoa yao wanasema kwamba ndoa yao imefanikiwa kwa sababu wana uhusiano wa kiroho wenye nguvu. Wao husali na kujifunza pamoja. Mume huyo anasema hivi: “Sisi husoma Biblia pamoja. Tunahubiri pamoja. Sisi hufurahia kufanya mambo pamoja.” Somo liko wazi: Kudumisha uhusiano mzuri na Yehova kutachangia sana kuimarisha ndoa.
Oneni Mambo Kihalisi na Mwasiliane
17. (a) Ni mambo gani mawili ambayo huchangia kufanikiwa kwa ndoa? (b) Paulo anafafanuaje upendo wa Kikristo?
17 Mambo mengine mawili ambayo huchangia kufanikiwa kwa ndoa ni: upendo wa Kikristo na kuwasiliana. Watu wawili wanapopendana, kila mmoja huwa na mwelekeo wa kupuuza kasoro za mwenzake. Huenda wenzi hao wakaingia katika ndoa wakitarajia mambo mengi kwa sababu ya yale wanayosoma katika vitabu vya mahaba au wanayoona katika sinema. Hata hivyo, mwishowe wenzi hao watalazimika kuona mambo kihalisi. Wakati huo, huenda kasoro ndogo-ndogo au tabia zenye kuudhi zikasababisha matatizo makubwa. Hali hiyo ikitokea, Wakristo wanahitaji kuonyesha matunda ya roho, mojawapo likiwa upendo. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa kweli, upendo wa Kikristo, na si upendo wa kimahaba, una nguvu sana. Paulo alifafanua upendo huo wa Kikristo aliposema hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” (1 Wakorintho 13:4-7) Kwa wazi, upendo wa kweli huvumilia udhaifu wa kibinadamu. Huona mambo kihalisi, kwa hiyo hautarajii ukamilifu.—Methali 10:12.
18. Mawasiliano yanawezaje kuimarisha ndoa?
18 Mawasiliano pia ni muhimu. Hata wenzi wa ndoa wawe wameoana kwa muda mrefu kadiri gani, wanapaswa kuzungumziana na kila mmoja amsikilize mwenzake kikweli. Mume mmoja anasema hivi: “Sisi huonyeshana wazi hisia zetu lakini kwa njia ya kirafiki.” Baada ya kukaa pamoja kwa muda mrefu, mume au mke hujifunza si kusikiliza tu yale yanayosemwa bali pia kusikiliza mambo ambayo hayajasemwa. Yaani, kadiri miaka inavyopita, wenzi wa ndoa wenye furaha hujifunza kutambua mawazo ambayo hayajasemwa au hisia ambazo hazijaonyeshwa. Wake fulani wamesema kwamba waume zao hawawasikilizi kikweli. Waume fulani wamelalamika kwamba wake zao hutaka kuzungumza nyakati zisizofaa. Mawasiliano hutia ndani kuwa na huruma na kuwafikiria wengine. Mawasiliano mazuri humfaidi mume na mke.—Yakobo 1:19.
19. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kuomba msamaha? (b) Ni nini kitakachotuchochea kuomba msamaha?
19 Nyakati nyingine, mawasiliano hutia ndani kuomba msamaha. Si rahisi sikuzote kufanya hivyo. Mtu anahitaji kuwa mnyenyekevu ili akubali makosa yake. Lakini jambo hilo linaweza kuimarisha sana ndoa. Kuomba msamaha kwa unyoofu kunaweza kuondoa hali ambayo inaweza kusababisha ugomvi wakati ujao na kufanya iwe rahisi kusamehe kikweli na kusuluhisha tatizo hilo. Paulo alisema hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:13, 14.
20. Mkristo anapaswa kumtendeaje mwenzi wake wa ndoa wakiwa faraghani na mbele za watu?
20 Pia kutegemezana ni muhimu katika ndoa. Mume na mke Mkristo wanapaswa kuaminiana na kutegemezana. Hawapaswi kuharibiana sifa au kwa njia fulani kumfanya mwingine ahisi kuwa hafai. Tukiwa Wakristo waliofunga ndoa, sisi huwapongeza wenzi wetu kwa upendo na hatuwachambui vikali. (Methali 31:28b) Bila shaka, hatuwashushii heshima kwa kuwafanyia mizaha ya kipumbavu. (Wakolosai 4:6) Kutegemezana huko huimarishwa kwa kuonyeshana upendo kwa ukawaida. Mguso au neno fulani linaweza kumwonyesha mwenzi wako kwamba bado unampenda na unafurahia kuwa naye. Hayo ni baadhi ya mambo yanayoweza kusaidia uhusiano na kufanya ndoa ifanikiwe katika ulimwengu wa leo. Kuna mambo mengine, na makala inayofuata itatoa mwongozo zaidi wa Kimaandiko kuhusu jinsi ya kufanikisha ndoa.a
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona kichapo Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa NdoaMnara wa Mlinzi—2005 | Machi 1
-
-
Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa
“Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana. Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu.”—WAEFESO 5:22, 25.
1. Ni maoni gani yanayofaa kuhusu ndoa?
YESU alisema kwamba ndoa ni kuunganishwa kwa mwanamume na mwanamke na Mungu ili wawe “mwili mmoja.” (Mathayo 19:5, 6) Inahusisha watu wawili wenye nyutu mbalimbali ambao wanajifunza kuwa na mapendezi yaleyale na kushirikiana kufikia miradi ileile. Ndoa ni kifungo cha maisha, si mkataba unaoweza kuvunjwa kwa urahisi. Katika nchi nyingi, ni rahisi kupata talaka, lakini Mkristo huiona ndoa kuwa takatifu. Inaweza kuvunjwa tu kukiwa na sababu muhimu.—Mathayo 19:9.
2. (a) Wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada gani? (b) Kwa nini ni muhimu kujitahidi kufanikisha ndoa?
2 Mshauri mmoja wa ndoa alisema hivi: “Ndoa nzuri hubadilika-badilika daima inapotokeza masuala mapya, inaposhughulika na matatizo yanayotokea, na kutumia maandalizi yaliyopo katika kila hatua ya maisha.” Kwa wenzi wa ndoa Wakristo, maandalizi hayo yanatia ndani shauri lenye hekima kutoka katika Biblia, msaada kutoka kwa Wakristo wenzao, na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova kupitia sala. Ndoa yenye mafanikio hudumu, nayo huletea mume na mke furaha na uradhi kadiri miaka inavyopita. Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba humletea heshima Yehova Mungu, ambaye ndiye Mwanzilishi wa ndoa.—Mwanzo 2:18, 21-24; 1 Wakorintho 10:31; Waefeso 3:15; 1 Wathesalonike 5:17.
Igeni Yesu na Kutaniko Lake
3. (a) Taja mambo makuu katika shauri la Paulo kwa wenzi wa ndoa. (b) Yesu alituwekea kielelezo gani kizuri?
3 Miaka 2,000 iliyopita, mtume Paulo aliwapa wenzi Wakristo shauri hili lenye hekima alipoandika: “Kama vile kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote. Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Waefeso 5:24, 25) Huo ni ulinganisho mzuri sana. Wake Wakristo wanaojitiisha kwa unyenyekevu kwa waume zao huliiga kutaniko katika kutambua na kutii kanuni ya ukichwa. Waume wanaoamini ambao huendelea kuwapenda wake zao katika nyakati nzuri au katika nyakati ngumu, huonyesha kwamba wanafuata kwa ukaribu kielelezo cha Kristo cha kulipenda na kulitunza kutaniko.
4. Waume wanawezaje kufuata kielelezo cha Yesu?
4 Waume Wakristo ni vichwa vya familia zao, lakini wao pia wana kichwa ambaye ni Yesu. (1 Wakorintho 11:3) Hivyo, kama vile Yesu alivyolitunza kutaniko lake, ndivyo waume hutunza familia zao kwa upendo kwa njia ya kiroho na kimwili, hata kama atalazimika kujidhabihu ili kufanya hivyo. Wao hutanguliza masilahi ya familia zao badala ya tamaa na mapendezi yao. Yesu alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kanuni hiyo inatumika hasa katika ndoa. Paulo alionyesha hilo aliposema: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. . . . Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo.” (Waefeso 5:28, 29) Mwanamume anapaswa kumlisha na kumtunza mke wake kwa bidii kama anavyojilisha na kujitunza mwenyewe.
5. Wake wanawezaje kuiga kutaniko la Kikristo?
5 Wake wanaomwabudu Mungu huiga kielelezo cha kutaniko la Kikristo. Yesu alipokuwa duniani, wafuasi wake waliacha kwa hiari mambo waliyofuatilia hapo awali na kumfuata. Baada ya kifo chake, waliendelea kujitiisha kwake, na kwa miaka zaidi ya 2,000 hivi iliyopita, kutaniko la Kikristo la kweli limeendelea kujitiisha kwa Yesu na kufuata uongozi wake katika mambo yote. Vivyo hivyo, wake Wakristo hawadharau waume zao au kupuuza mpango wa Kimaandiko wa ukichwa katika ndoa. Badala yake, wao huwasaidia waume zao na kujitiisha kwao, wakishirikiana nao, na hivyo kuwatia moyo. Mume na mke wanapotenda kwa njia hiyo ya upendo, ndoa yao itafanikiwa na wote watapata shangwe katika uhusiano huo.
Endeleeni Kukaa Nao
6. Petro aliwapa waume shauri gani, na kwa nini shauri hilo ni muhimu?
6 Mtume Petro pia aliwashauri wenzi wa ndoa, na shauri lake kwa waume lilikuwa la moja kwa moja. Alisema: “Endeleeni kukaa [na wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa ninyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Petro 3:7) Uzito wa shauri la Petro unaelezwa katika maneno ya mwisho ya mstari huo. Mume asipomheshimu mke wake, uhusiano wake pamoja na Yehova utaathiriwa. Sala zake zitazuiwa.
7. Mume anapaswa kumheshimu mke wake jinsi gani?
7 Basi, waume wanaweza kuwaonyeshaje wake zao heshima? Kumheshimu mke wako kunamaanisha kumtendea kwa upendo, staha, na hadhi. Wengi wangeona kumtendea mke kwa fadhili kuwa jambo lisilo la kawaida. Msomi mmoja Mgiriki anaandika hivi: “Chini ya sheria ya Waroma, mwanamke hakuwa na haki zozote. Kulingana na sheria, haki zake zilikuwa sawa na za mtoto. . . . Alitiishwa kabisa chini ya mume wake, naye alitawaliwa kabisa na mumewe.” Hilo lilikuwa tofauti sana na mafundisho ya Kikristo. Mume Mkristo alimheshimu mke wake. Alishughulika naye kulingana na kanuni za Kikristo, wala si kulingana na hisia zake za ghafula. Isitoshe, alimtendea kwa ufikirio “kulingana na ujuzi,” akikumbuka kwamba mke ni chombo dhaifu zaidi.
“Chombo Dhaifu Zaidi” Katika Njia Gani?
8, 9. Wanawake ni sawa na wanaume katika njia zipi?
8 Kwa kusema kwamba mwanamke ni “chombo dhaifu zaidi,” Petro hakumaanisha kwamba wanawake ni dhaifu zaidi kiakili au kiroho kuliko wanaume. Ni kweli kwamba wanaume wengi Wakristo wana mapendeleo kutanikoni ambayo wanawake hawatarajii kuwa nayo, na katika familia wanawake hujitiisha kwa waume zao. (1 Wakorintho 14:35; 1 Timotheo 2:12) Hata hivyo, wote, wanaume kwa wanawake, wanapaswa kuwa na imani, uvumilivu, na viwango vilevile vya juu vya maadili. Na kama Petro alivyosema, wote wawili, mume na mke ni “warithi . . . wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima.” Kwa habari ya wokovu, wote wana msimamo sawa mbele za Yehova Mungu. (Wagalatia 3:28) Petro alikuwa akiwaandikia Wakristo watiwa-mafuta wa karne ya kwanza. Kwa hiyo, maneno yake yaliwakumbusha waume Wakristo kwamba wakiwa “warithi pamoja na Kristo,” wao pamoja na wake zao walikuwa na tumaini lilelile la kimbingu. (Waroma 8:17) Siku moja, wote watakuwa makuhani na wafalme katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu!—Ufunuo 5:10.
9 Bila shaka, wake Wakristo waliotiwa mafuta hawakuwa duni kwa kulinganishwa na waume zao Wakristo waliotiwa mafuta. Na kanuni hiyohiyo inatumika kwa wale walio na tumaini la kidunia. Wote, wanaume na wanawake wa “umati mkubwa” wanafua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Wote, wanaume na wanawake wanashiriki katika kumtolea Yehova sifa “mchana na usiku” ulimwenguni pote. (Ufunuo 7:9, 10, 14, 15) Wote, wanaume na wanawake wanatazamia kupata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu,” watakapofurahia “uzima ulio wa kweli.” (Waroma 8:21; 1 Timotheo 6:19) Wawe ni watiwa-mafuta au wale wa kondoo wengine, Wakristo wote humtumikia Yehova pamoja wakiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Hiyo ni sababu yenye kusadikisha sana kwa waume na wake Wakristo kuheshimiana.
10. Wanawake ni ‘vyombo dhaifu zaidi’ katika maana gani?
10 Basi, wanawake ni ‘vyombo dhaifu zaidi’ katika njia gani? Huenda Petro alikuwa akirejelea ukweli wa kwamba, kwa ujumla, wanawake ni wadogo zaidi kimwili na hawana nguvu nyingi kama wanaume. Zaidi ya hayo, kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, pendeleo la pekee la kuzaa watoto huathiri afya ya wanawake. Huenda wanawake wenye umri wa kuweza kuzaa wakawa na maumivu ya mwili mara kwa mara. Kwa kweli wanahitaji utunzaji na ufikirio wa pekee wanapokuwa na maumivu hayo au uchovu unaosababishwa na kuwa mja-mzito na kujifungua. Mume anayemheshimu mke wake akitambua kwamba anahitaji kutegemezwa kihisia, atachangia sana kufanikiwa kwa ndoa.
Katika Nyumba Iliyogawanyika Kidini
11. Ni katika maana gani ndoa inaweza kufanikiwa hata kama mume na mke ni wa dini tofauti?
11 Hata hivyo, namna gani ikiwa wenzi wa ndoa wana maoni tofauti ya kidini kwa sababu mmoja alikubali kweli ya Kikristo muda fulani baada ya kufunga ndoa na yule mwingine hakuikubali? Je, ndoa hiyo inaweza kufanikiwa? Ndoa nyingi kama hizo zimefanikiwa. Mume na mke ambao wana maoni tofauti ya kidini bado wanaweza kuwa na ndoa yenye mafanikio katika maana ya kwamba wanaweza kuwa na ndoa inayodumu na yenye furaha. Mbali na hilo, bado ndoa hiyo ni halali machoni pa Yehova; bado wao ni “mwili mmoja.” Kwa hiyo, wenzi wa ndoa Wakristo wanashauriwa wakae na mwenzi asiyeamini iwapo mwenzi huyo anakubali. Ikiwa kuna watoto, wananufaika na uaminifu wa mzazi aliye Mkristo.—1 Wakorintho 7:12-14.
12, 13. Kwa kufuata shauri la Petro, wake Wakristo wanaweza kuwasaidiaje waume wasioamini?
12 Petro anatoa shauri lenye fadhili kwa wanawake Wakristo wanaoishi katika nyumba zilizogawanyika kidini. Maneno yake yanaweza kuwahusu pia waume Wakristo walio katika hali kama hiyo. Petro anaandika hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Petro 3:1, 2.
13 Ikiwa mke anaweza kumweleza mume wake imani yake kwa busara, hilo ni jambo la kusifiwa. Lakini, namna gani ikiwa hataki kusikiliza? Huo ni uamuzi wake. Hata hivyo, bado kuna tumaini, kwa kuwa mwenendo wa Kikristo pia hutoa ushahidi wenye nguvu. Waume wengi ambao hapo mwanzoni hawakupendezwa au hata walipinga imani ya wake zao baadaye walikuwa na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” baada ya kuona mwenendo mzuri wa wake zao. (Matendo 13:48) Hata kama mume hatakubali kweli ya Kikristo, huenda bado akavutiwa na mwenendo wa mke wake, na hilo linaweza kuimarisha kifungo cha ndoa. Mume mmoja ambaye mke wake ni Shahidi wa Yehova alikiri kwamba hawezi kuishi kupatana na viwango vya juu vya Mashahidi wa Yehova. Lakini bado alisema kwamba “alifurahi kuwa mume wa mke mwenye kuvutia” na akamsifu kwa unyoofu mke wake pamoja na Mashahidi wenzake katika barua aliyoandikia gazeti moja.
14. Waume wanaweza kuwasaidiaje wake wasioamini?
14 Vivyo hivyo, waume Wakristo ambao wamefuata kanuni zinazopatikana katika maneno ya Petro wamewavuta wake zao kupitia mwenendo wao. Wake wasioamini wameona waume zao wakichukua madaraka yao kwa uzito, wakiacha kupoteza pesa kwa kuvuta sigara, kunywa pombe, na kucheza kamari, na kuacha kutumia lugha chafu. Baadhi ya wake hao wasioamini wamefahamiana na washiriki wa kutaniko la Kikristo. Walivutiwa na undugu wa Kikristo wenye upendo, na yale waliyoona kati ya akina ndugu yaliwavuta kwa Yehova.—Yohana 13:34, 35.
“Yule Mtu wa Siri wa Moyoni”
15, 16. Mke Mkristo anaweza kumvuta mume asiyeamini kwa mwenendo wa aina gani?
15 Ni mwenendo wa aina gani unaoweza kumvuta mume? Kwa kweli, ni mwenendo ambao kwa kawaida husitawishwa na wanawake Wakristo. Petro anasema: “Kujipamba kwenu kusiwe kule kusuka nywele kwa nje na kule kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu. Kwa maana, pia, ndivyo walivyokuwa wakijipamba wale wanawake watakatifu hapo zamani, waliokuwa wakimtumaini Mungu, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe, kama Sara alivyokuwa akimtii Abrahamu, akimwita ‘bwana.’ Nanyi mmekuwa watoto wake, mradi tu mnaendelea kutenda mema na kutokuwa na woga kwa sababu ya kitisho chochote.”—1 Petro 3:3-6.
16 Petro anamshauri mwanamke Mkristo asitegemee sura ya nje. Badala yake, anapaswa kuacha mume wake aone jinsi mafundisho ya Biblia yanavyobadili utu wake wa ndani. Anapaswa kuacha mume wake aone jinsi anavyovaa utu mpya. Labda ataulinganisha na ule utu wa zamani ambao mke wake alikuwa nao. (Waefeso 4:22-24) Bila shaka, ataona “roho ya utulivu na ya upole” ya mke wake kuwa yenye kuburudisha na kuvutia. Roho hiyo haimpendezi tu mume wake bali pia ni “ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—Wakolosai 3:12.
17. Sara ni kielelezo kizuri kwa wake Wakristo jinsi gani?
17 Sara anatajwa kuwa kielelezo, naye ni mfano mzuri wa kuigwa na wake Wakristo iwe waume zao ni waamini au la. Bila shaka, Sara alimwona Abrahamu kuwa kichwa chake. Hata moyoni mwake, alimwita “bwana” wake. (Mwanzo 18:12) Hata hivyo, hilo halikumfanya kuwa duni. Ni wazi kwamba alikuwa mwanamke mwenye nguvu kiroho aliyekuwa na imani thabiti katika Yehova. Kwa kweli, yeye ni sehemu ya ‘wingu kubwa la mashahidi’ ambao kielelezo chao cha imani kinapaswa kutuchochea “tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 11:11; 12:1) Kwa hiyo mke Mkristo hawi duni anapomwiga Sara.
18. Ni kanuni gani zinazopaswa kufuatwa katika nyumba iliyogawanyika kidini?
18 Katika nyumba iliyogawanyika kidini, bado mume ndiye kichwa. Ikiwa yeye ni mwamini, atafikiria imani ya mke wake huku akishikilia imani yake. Ikiwa mke ndiye mwamini, yeye pia atashikilia imani yake. (Matendo 5:29) Hata hivyo, hatapinga ukichwa wa mume wake. Ataheshimu cheo chake na kuendelea kuwa chini ya “sheria ya mume wake.”—Waroma 7:2.
Mwongozo wa Biblia Wenye Hekima
19. Ni mambo gani ambayo huleta mkazo katika kifungo cha ndoa, lakini yanaweza kushindwaje?
19 Leo, kuna mambo mengi yanayoweza kusababisha mkazo katika kifungo cha ndoa. Wanaume fulani hukosa kutimiza madaraka yao. Wanawake fulani hukataa kukubali ukichwa wa waume zao. Katika ndoa fulani, mwenzi mmoja hutendewa vibaya na yule mwingine. Mikazo ya kiuchumi, kutokamilika kwa kibinadamu, na roho ya ulimwengu pamoja na ukosefu wa maadili na viwango vyake vilivyopotoka vinaweza kujaribu ushikamanifu wa Wakristo. Hata hivyo, wanaume na wanawake Wakristo wanaofuata kanuni za Biblia hata hali zao ziweje, hubarikiwa na Yehova. Hata kama mwenzi mmoja tu katika ndoa ndiye anayefuata kanuni za Biblia, hali huwa bora zaidi kuliko wote wawili wanapokosa kuzifuata. Zaidi ya hayo, Yehova huwapenda na kuwasaidia watumishi wake wanaoendelea kuwa waaminifu kwa nadhiri zao za ndoa hata chini ya hali ngumu. Yeye hasahau ushikamanifu wao.—Zaburi 18:25; Waebrania 6:10; 1 Petro 3:12.
20. Petro anatoa shauri gani kwa Wakristo wote?
20 Baada ya kuwashauri wanaume na wanawake waliofunga ndoa, mtume Petro alimalizia kwa maneno machangamfu na yenye kutia moyo. Alisema: “Mwishowe, ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili, msilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano, bali, kinyume chake, mkitoa baraka, kwa sababu mliitwa kwenye mwendo huu, ili mrithi baraka.” (1 Petro 3:8, 9) Hilo ni shauri zuri sana kwa wote, hasa kwa wenzi wa ndoa.
-