Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa nini kuna sheria nyingi sana?
    Amkeni!—2006 | Desemba
    • Mawasiliano Yenye Matokeo

      Ikiwa unataka kuwa na uhuru zaidi au ikiwa una uhuru wa kutosha lakini kuna matatizo yanayoambatana nao, ni muhimu kuwa na mawasiliano mazuri. Huenda wengine wakasema, ‘Nimejaribu kuzungumza na wazazi wangu lakini hakuna matokeo!’ Ikiwa unahisi hivyo, jiulize, ‘Je, ninaweza kuboresha njia yangu ya kuwasiliana?’ Mawasiliano ni muhimu ili kukusaidia (1) upate unachotaka au (2) uelewe vizuri zaidi kwa nini hauruhusiwi kufanya unachotaka. Kwa kweli, ukitaka kuonwa kuwa mtu mzima, ni muhimu ujue kuwasiliana kwa njia nzuri.

      ◼ Jifunze kudhibiti hisia zako. Biblia inasema: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” (Methali 29:11) Mawasiliano mazuri si kulalamika tu. Ukifanya hivyo wazazi wako watakutia nidhamu tena! Kwa hiyo epuka kulialia, kununa, na tabia za kitoto. Kwa hiyo, ukihisi kwamba unataka kuufunga mlango kwa nguvu au kutembea-tembea kwa kishindo ndani ya nyumba wazazi wanapokuzuia usitoke nje, kumbuka kwamba tabia kama hiyo itafanya tu waweke sheria nyingine, si kukupa uhuru zaidi.

      ◼ Jaribu kuelewa maoni ya wazazi wako. Tracy, kijana Mkristo ambaye amelelewa katika familia yenye mzazi mmoja, ameona hilo kuwa jambo lenye faida. Anasema: “Mimi hujiuliza, ‘Mama anajaribu kutimiza nini kwa kuweka sheria?’ Anajaribu kunisaidia kuwa mtu bora.” (Methali 3:1, 2) Kuelewa hisia zao kunaweza kukusaidia kuwaelewa wazazi wako. Kwa mfano, huenda wakawa hawataki kukuruhusu uhudhurie kikusanyiko fulani. Badala ya kubishana, unaweza kuuliza, “Vipi ikiwa nitaandamana na rafiki mkomavu na mwenye kutumainika?” Huenda wazazi wako wasikubali sikuzote kile unachotaka, lakini ikiwa unaelewa mambo yanayowahangaisha, unaweza kutoa mapendekezo mazuri ambayo watayakubali.

      ◼ Wafanye wazazi wako wakuamini zaidi. Kuaminiwa na wazazi wako ni kama kuweka pesa katika akaunti ya benki. Unaweza kutoa tu kile ambacho tayari umeweka. Ukitoa zaidi ya ulichoweka utatozwa faini, na ukifanya hivyo mara kadhaa akaunti yako inaweza kufungwa. Kupata uhuru zaidi ni kama kutoa pesa benki; utaupata ikiwa tu umeweka rekodi nzuri ya kuwa na tabia yenye kuheshimika.

      ◼ Usitazamie mengi kupita kiasi. Wazazi wako wana daraka la kudhibiti kwa kadiri fulani matendo yako. Hivyo, Biblia huzungumza kuhusu “amri ya baba yako” na “sheria ya mama yako.” (Methali 6:20) Isitoshe, hupaswi kuhisi kwamba sheria za nyumbani zitaharibu maisha yako. Ukijitiisha kwa mamlaka ya wazazi wako, Yehova anaahidi kwamba mwishowe, mambo ‘yatakuendea vema’!—Waefeso 6:1-3.

  • Kwa nini kuna sheria nyingi sana?
    Amkeni!—2006 | Desemba
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

      Sheria Inapovunjwa

      Huenda umejikuta katika hali kama hii: Umefika nyumbani baada ya wakati ambao wazazi wanataka, hujafanya kazi zako, au umetumia wakati mwingi kuliko inavyoruhusika kwenye simu. Sasa unakabiliana na wazazi wako! Unaweza kuzuiaje hali isiwe mbaya zaidi?

      ◼ Sema ukweli. Huo si wakati wa kujifanya mjanja; sema kweli na utoe habari hususa. (Methali 28:13) Kutunga hadithi kunaweza kuwafanya wazazi waache kukuamini kabisa. Epuka kujitetea au kupunguza uzito wa jambo lililotendeka. Sikuzote kumbuka kwamba “jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.”—Methali 15:1.

      ◼ Omba msamaha. Inafaa kuomba msamaha kwa sababu ya kuwafanya wazazi wawe na wasiwasi, kuwakatisha tamaa, au kuwafanyisha kazi ya ziada. Huenda kufanya hivyo kukapunguza adhabu uliyopaswa kupewa. (1 Samweli 25:24) Hata hivyo, unapaswa kuwa mnyoofu.

      ◼ Kubali matokeo. Huenda ukaitikia kwanza kwa kupinga adhabu uliyopewa, hasa ikionekana kuwa si ya haki. (Methali 20:3) Hata hivyo, ni ishara ya ukomavu kukubali daraka kwa ajili ya mambo uliyofanya. (Wagalatia 6:7) Jambo bora zaidi unaloweza kufanya ni kujitahidi kuaminiwa tena na wazazi wako.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki