Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • Wasiliana kwa Njia Inayofaa

      Iwe unataka uhuru zaidi au kupunguza tu mkazo unaotokana na sheria ambazo wazazi wako wamekuwekea, siri ya kupata mafanikio ni kuwasiliana nao kwa njia inayofaa. Huenda wengine wakasema: ‘Nimejaribu kuzungumza na wazazi wangu, lakini ni kazi bure!’ Ikiwa ndivyo unavyohisi, jiulize: ‘Je, ninaweza kubadili jinsi ninavyowasiliana nao?’ Mawasiliano ni kifaa muhimu kinachoweza (1) kuwasaidia wengine wakuelewe au (2) kukusaidia kuelewa ni kwa nini mambo unayotaka yamekataliwa. Ikiwa unataka utendewe kama mtu mzima, basi lazima ujifunze kuwasiliana nao kama mtu mzima. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

      Jifunze kuzuia hisia zako. Ili kuwasiliana vizuri, lazima uwe na sifa ya kujizuia. Biblia inasema hivi: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” (Methali 29:11) Hivyo, epuka kunung’unika-nung’unika, kununa-nuna, na kutaka ubembelezwe kama mtoto. Ni kweli kwamba huenda ukataka kubamiza mlango au kupiga-piga miguu chini kwa hasira unapohisi kwamba wazazi wako wanakunyima uhuru. Lakini, kufanya hivyo kutawafanya wakuwekee sheria nyingi hata zaidi.

      Jaribu kuwaelewa wazazi wako. Tracy, msichana Mkristo aliyelelewa na mzazi mmoja, anasema, “Mimi hujiuliza, ‘Mama anataka kunifundisha nini?’” Tracy alikata kauli gani? “Anajaribu kunisaidia niwe na sifa nzuri.” (Methali 3:1, 2) Kuelewa hisia za wazazi wako kwa njia hiyo kunaweza kukusaidia kuwasiliana nao vizuri.

      Kwa mfano, tuseme wazazi wako wanasita kukupa ruhusa ya kwenda kujumuika na vijana wengine. Badala ya kubishana nao, unaweza kuwauliza, “Namna gani ikiwa kutakuwa na mtu mkomavu anayetegemeka?” Huenda bado wazazi wako wakakataa. Hata hivyo, ukielewa hangaiko lao, huenda ukapendekeza jambo ambalo labda litakubalika machoni pao.

      Jiendeshe kwa njia itakayofanya wazazi wako wawe na imani nawe. Wazia mtu amechukua mkopo katika benki. Akiwa na mazoea ya kulipa kwa wakati, benki itamwamini na inaweza kumpa mkopo mkubwa zaidi siku za usoni. Ndivyo ilivyo na nyumbani. Unapaswa kuwatii wazazi wako. Ukifanya hivyo hata katika mambo madogo, wazazi wako watakuamini hata zaidi wakati ujao. Lakini, ukiwatamausha wazazi wako mara kwa mara, usishangae wakikaza kamba au hata kukuzuilia kabisa.

      Unapovunja Sheria

      Haikosi kuna wakati ambapo utavunja sheria fulani. Huenda ukakosa kufanya kazi ulizopewa, ukatumia simu kwa muda mrefu sana, au ukachelewa kurudi nyumbani. (Zaburi 130:3) Katika hali hiyo, utalazimika kuwaeleza ni kwa nini. Unaweza kuzuiaje hali isiwe mbaya zaidi?

      Sema kweli. Usiwape hadithi ndefu. Kufanya hivyo kwaweza kuwafanya wazazi wako wapoteze imani waliyokuwa nayo kukuelekea. Hivyo sema kweli na kutaja mambo waziwazi. (Methali 28:13) Epuka kujitetea au kupunguza uzito wa kosa. Na sikuzote ukumbuke kwamba “jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.”—Methali 15:1.

      Omba msamaha. Kuwaeleza kwamba unasikitika kwa kuwahangaisha, kuwavunja moyo, au kuwaongezea kazi, ni vizuri na kunaweza kukupunguzia adhabu. Hata hivyo, unapaswa kufanya hivyo kutoka moyoni.

      Kubali matokeo. (Wagalatia 6:7) Huenda mwanzoni ukapinga adhabu hiyo, hasa unapoona kwamba unaonewa. Hata hivyo, kukubali makosa na nidhamu huonyesha kwamba wewe ni mkomavu. Jambo la maana ni kujitahidi kuwafanya wazazi wakuamini tena.

  • Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 189]

      Ukurasa wa Mazoezi

      Zungumza na Wazazi Wako!

      Sura mbili zilizotangulia zimezungumzia jinsi unavyoweza kufanya unapolaumiwa na wazazi au unapowekewa sheria. Hata hivyo, utafanya nini ukihisi kwamba wazazi wako wamepita kiasi katika mambo hayo? Unaweza kuanzisha mazungumzo nao jinsi gani?

      ● Chagua wakati ambapo utakuwa umetulia na wazazi wako hawana shughuli nyingi.

      ● Zungumza nao kutoka moyoni, lakini usiropoke tu kwa sababu ya hisia. Wape wazazi wako heshima wanayostahili.

      Ikiwa unahisi kwamba wazazi wako wanakulaumu kupita kiasi, unaweza kuwaambia: “Ninajitahidi kufanya yaliyo sawa, lakini si rahisi ikiwa kila wakati ninalaumiwa. Ningependa tuongee kuhusu jambo hilo.”

      Andika hapa chini jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hilo.

      ․․․․․

      ✔PENDEKEZO: Tumia Sura ya  21 ili kuanzisha mazungumzo. Huenda wazazi wako watapenda kuzungumza nawe mambo yaliyo katika sura hiyo.

      Ikiwa unahisi kwamba wazazi wako hawakupi uhuru wa kutosha, unaweza kuwaambia: “Ni jambo gani ninalopaswa kufanyia kazi ili wakati ujao niwe mwenye kutegemeka zaidi na kustahili kupata uhuru zaidi?”

      Andika hapa chini jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hilo.

      ․․․․․

      ✔PENDEKEZO: Chunguza Sura ya 3 katika Buku la  1 yenye kichwa “Niwafanyeje Wazazi Wangu Wanipe Uhuru Zaidi?” Kisha andika maswali yoyote ambayo huenda ukawa nayo baada ya kusoma sura hiyo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki