-
Je, Umepokea “Roho ya Ile Kweli”?Mnara wa Mlinzi—2002 | Februari 1
-
-
Kuwatendea Mema Ndugu za Kristo
13, 14. (a) Kulingana na mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, wokovu wa kondoo wengine unategemea nini? (b) Katika wakati huu wa mwisho, kondoo wengine wamewaungaje mkono ndugu za Kristo?
13 Yesu alikazia uhusiano wa karibu kati ya kondoo wengine na kundi dogo katika mfano wake wa kondoo na mbuzi, unaotajwa katika unabii wake kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Katika mfano huo, Kristo alionyesha waziwazi kwamba wokovu wa kondoo wengine unategemea sana jinsi wanavyowatendea watiwa-mafuta, ambao aliwaita “ndugu zangu.” Alisema hivi: “Mfalme atawaambia wale walio kwenye mkono wake wa kuume, ‘Njoni, nyinyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, rithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu. . . . Kwa kweli nawaambia nyinyi, Kwa kadiri ambayo mlimfanyia hilo mmoja wa wadogo zaidi sana wa ndugu zangu hawa, mlinifanyia mimi hilo.’”—Mathayo 24:3; 25:31-34, 40.
14 Usemi “kwa kadiri ambayo mlimfanyia” warejezea kuwatendea kwa upendo ndugu za Kristo waliozaliwa kwa roho, ambao ulimwengu wa Shetani umewatendea kama wageni, na hata kutia baadhi yao gerezani. Wamekuwa na uhitaji wa chakula, mavazi ya kutosha, na utunzaji wa afya. (Mathayo 25:35, 36, NW, kielezi-chini) Wakati huu wa mwisho, tangu mwaka wa 1914, watiwa-mafuta wengi wamejikuta katika hali kama hizo. Rekodi ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova yathibitisha kwamba watiwa-mafuta wameungwa mkono na waandamani wao waaminifu, kondoo wengine, ambao wanachochewa na roho.
15, 16. (a) Kondoo wengine wamewasaidia ndugu za Kristo watiwa-mafuta walio duniani katika kazi gani? (b) Watiwa-mafuta wameonyeshaje shukrani zao kwa kondoo wengine?
15 Ndugu za Kristo watiwa-mafuta walio duniani wakati huu wa mwisho hasa wameungwa mkono na kondoo wengine kufanya kazi waliyopewa na Mungu ya ‘kuhubiri habari njema hii ya ufalme katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14; Yohana 14:12) Ingawa idadi ya watiwa-mafuta walio duniani imekuwa ikipungua katika miaka iliyopita, idadi ya kondoo wengine imeongezeka na kufikia milioni kadhaa. Maelfu kati yao wametumikia wakiwa waeneza-evanjeli wa wakati wote—mapainia na mishonari—wakihubiri habari njema za Ufalme hadi “sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8) Wengine hushiriki kazi ya kutoa ushahidi kwa kadiri wawezavyo na kutoa michango yao kwa furaha ili kutegemeza kazi hiyo muhimu.
16 Ndugu za Kristo wanashukuru kama nini kwa msaada huo unaotolewa kwa uaminifu na waandamani wao, kondoo wengine! Maoni yao yalielezwa vyema katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani,” kilichochapishwa na jamii ya mtumwa katika mwaka wa 1986. Kinasema hivi: “Tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili, utimizo wa unabii wa Yesu kwa ‘umalizio wa mfumo wa mambo’ kwa sehemu kubwa ni kwa sababu ya daraka linalotimizwa na ule ‘mkutano mkubwa’ wa ‘kondoo wengine.’ . . . Kwa hiyo shukrani nyingi sana, kwa ule mkutano mkubwa wa kimataifa, wenye kusema lugha nyingi kwa sababu ya sehemu kubwa ambayo umeshiriki katika kutimiza unabii wa [Yesu] yule Bwana-arusi kwenye Mathayo 24:14!”
-
-
Je, Umepokea “Roho ya Ile Kweli”?Mnara wa Mlinzi—2002 | Februari 1
-
-
Kuungana Katika Roho Wakati wa Ukumbusho
19. “Roho ya ile kweli” imewafanyia nini watiwa-mafuta na waandamani wao, nao wataunganaje hasa jioni ya Machi 28?
19 Katika sala yake ya kumalizia usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu alisema: “Nafanya ombi, . . . ili wote wapate kuwa mmoja, kama vile wewe, Baba, umo katika muungano na mimi na mimi nimo katika muungano na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano na sisi, ili ulimwengu upate kuamini kwamba ulinituma mimi.” (Yohana 17:20, 21) Mungu alichochewa na upendo kumtuma Mwana wake atoe uhai wake ili kuokoa watiwa-mafuta na wanadamu watiifu. (1 Yohana 2:2) “Roho ya ile kweli” imeunganisha ndugu za Kristo na waandamani wao. Jioni ya Machi 28, baada ya jua kutua, vikundi vyote viwili vitakutana pamoja ili kukumbuka kifo cha Kristo na kukumbuka yote ambayo Yehova amewafanyia kupitia dhabihu ya Mwana wake mpendwa, Kristo Yesu. Umoja wao na uimarike wanapohudhuria sherehe hiyo muhimu, na waazimie upya kufanya mapenzi ya Mungu, na hivyo kuthibitisha kwamba wanafurahia kuwa miongoni mwa wale wanaopendwa na Yehova.
-