-
“Ninyi Ni Rafiki Zangu”Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 15
-
-
“Ninyi Ni Rafiki Zangu”
“Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.”—YOH. 15:14.
1, 2. (a) Marafiki wa Yesu walitoka katika malezi gani mbalimbali? (b) Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuwa marafiki wa Yesu?
WANAUME wanaoketi na Yesu kwenye chumba cha juu walitoka katika malezi mbalimbali. Petro na Andrea ambao ni ndugu wa kimwili walikuwa wavuvi. Zamani, Mathayo alikuwa mkusanya-kodi, kazi ambayo ilidharauliwa na Wayahudi. Wengine wao, kama vile Yakobo na Yohana, inaelekea walimjua Yesu tangu alipokuwa mvulana mdogo. Na wengine, kama vile Nathanaeli, huenda walikuwa wamemjua kwa miaka michache tu. (Yoh. 1:43-50) Hata hivyo, wote waliokuwepo usiku huo wakati wa Pasaka hiyo ya pekee huko Yerusalemu walisadiki kwamba Yesu alikuwa ndiye yule Masihi aliyeahidiwa, Mwana wa Mungu aliye hai. (Yoh. 6:68, 69) Bila shaka, walitiwa moyo sana walipomsikia Yesu akiwaambia: “Nimewaita ninyi rafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha ninyi.”—Yoh. 15:15.
2 Maneno hayo ambayo Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu yanawahusu kimsingi Wakristo wote watiwa-mafuta leo, na kwa kuongezea yanawahusu waandamani wao wa “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Hata iwe tumetoka katika malezi gani, tunaweza kuwa na pendeleo la kuwa marafiki wa Yesu. Urafiki wetu pamoja naye ni wa maana sana kwa sababu tunapokuwa marafiki wake tunakuwa pia marafiki wa Yehova. Kwa kweli, hatuwezi kumkaribia Yehova bila kumkaribia kwanza Kristo. (Soma Yohana 14:6, 21.) Hivyo basi, ni lazima tufanye nini ili tuwe marafiki wa Yesu na kudumisha urafiki huo? Kabla ya kuzungumzia habari hiyo ya maana sana, acheni tuchunguze mfano wa Yesu akiwa rafiki mzuri na tuone jambo tunaloweza kujifunza kutokana na jinsi wanafunzi wake walivyohisi kuhusu urafiki huo.
Mfano wa Yesu Akiwa Rafiki Mzuri
3. Yesu alijulikana kwa sababu gani?
3 Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Tajiri ana rafiki wengi.” (Met. 14:20) Maneno hayo yanaonyesha mwelekeo wa wanadamu wasio wakamilifu, wa kufanya urafiki kwa msingi wa kile wanachoweza kupata badala ya kile wanachoweza kutoa. Yesu hakuwa na udhaifu huo. Hakushawishiwa kufanya urafiki na mtu kwa sababu ya uwezo wa mtu huyo wa kiuchumi au cheo chake katika jamii. Ni kweli kwamba Yesu alimpenda mtawala mmoja kijana na akamwalika amfuate ili awe mfuasi wake. Hata hivyo, Yesu alimwambia mwanamume huyo auze vitu alivyokuwa navyo na kuwapa maskini. (Marko 10:17-22; Luka 18:18, 23) Yesu alijulikana kwa sababu alikuwa rafiki ya watu wa hali ya chini na waliodharauliwa, bali si kwa sababu alishirikiana na watu matajiri na mashuhuri.—Mt. 11:19.
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba marafiki wa Yesu walikuwa watu wasio wakamilifu?
4 Bila shaka, marafiki wa Yesu walikuwa watu wasio wakamilifu. Pindi moja Petro alikosa kuona mambo kwa njia ya kiroho. (Mt. 16:21-23) Yakobo na Yohana walionyesha roho ya kujitakia makuu walipomwomba Yesu awape vyeo vikubwa katika Ufalme. Tendo lao liliwakasirisha mitume wengine, na suala hilo la kutafuta ukubwa lilifanya wagombane mara kwa mara. Hata hivyo, Yesu alijitahidi kwa subira kurekebisha mawazo ya marafiki wake naye hakuwa mwepesi kukasirika.—Mt. 20:20-28.
5, 6. (a) Kwa nini Yesu alidumisha urafiki na wengi kati ya mitume wake? (b) Kwa nini Yesu alikomesha urafiki wake pamoja na Yuda?
5 Yesu hakudumisha urafiki na watu hao wasio wakamilifu kwa kupuuza tu au kuachilia udhaifu wao. Badala yake, aliamua kukazia fikira nia yao nzuri na sifa zao nzuri. Kwa mfano, Petro, Yakobo, na Yohana walilala usingizi badala ya kumtegemeza Yesu alipokabili wakati mgumu zaidi. Yesu alivunjwa moyo na jambo hilo. Hata hivyo, aliona kwamba nia yao ilikuwa nzuri, akasema hivi: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.”—Mt. 26:41.
6 Kinyume chake, Yesu alikomesha urafiki wake na Yuda Iskariote. Hata ingawa kwa nje Yuda alionekana kuwa rafiki mzuri, Yesu aligundua kwamba rafiki huyo wa zamani alikuwa ameruhusu moyo wake upotoshwe. Kwa sababu Yuda alikuwa sasa rafiki ya ulimwengu, alijifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu. (Yak. 4:4) Kwa hiyo, Yesu alikuwa tayari amemfukuza Yuda wakati alipotangaza urafiki Wake pamoja na mitume wake waaminifu 11 waliobaki.—Yoh. 13:21-35.
7, 8. Yesu alionyesha jinsi gani upendo wake kwa marafiki wake?
7 Yesu hakukazia fikira makosa ya marafiki wake washikamanifu bali alichukua hatua ya kuwasaidia. Kwa mfano, alisali ili Baba yake awalinde wakati wa majaribu. (Soma Yohana 17:11.) Yesu alitilia maanani udhaifu wao wa kimwili. (Marko 6:30-32) Na hakupendezwa tu kuwaeleza yale aliyofikiri bali pia alisikiliza na kuelewa yale waliyofikiri na kuhisi.—Mt. 16:13-16; 17:24-26.
8 Yesu aliishi na kufa kwa ajili ya marafiki wake. Kwa kweli, alijua kwamba kulingana na sheria ilikuwa lazima atoe uhai wake ili kutimiza kiwango cha haki cha Baba yake. (Mt. 26:27, 28; Ebr. 9:22, 28) Lakini Yesu alionyesha upendo kwa kutoa uhai wake. Alisema hivi: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.”—Yoh. 15:13.
Wanafunzi Walihisi Jinsi Gani Kuhusu Urafiki wa Yesu?
9, 10. Watu waliitikia jinsi gani ukarimu wa Yesu?
9 Yesu alikuwa mkarimu katika kutumia wakati wake, kuonyesha upendo, na kutoa vitu vya kimwili. Kwa sababu hiyo, watu walijihisi huru kumkaribia na walifurahi pia kumpa vitu. (Luka 8:1-3) Kutokana na mambo aliyojionea mwenyewe, Yesu alisema hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwagia katika mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.”—Luka 6:38.
10 Bila shaka, watu wengine walijaribu kushirikiana na Yesu kwa sababu tu ya vitu ambavyo wangepata kutoka kwake. Marafiki hao wa uwongo walimwacha Yesu walipoelewa kimakosa jambo fulani alilosema. Badala ya kumwamini Yesu wakati walipokosa kuelewa alilosema, walifanya haraka kukata kauli yenye kosa na kuacha kumfuata. Lakini mitume walikuwa washikamanifu. Mara nyingi, urafiki wao pamoja na Kristo ulijaribiwa, lakini walifanya yote waliyoweza ili kumtegemeza katika nyakati nzuri na mbaya pia. (Soma Yohana 6:26, 56, 60, 66-68.) Katika usiku wake wa mwisho duniani akiwa mwanadamu, Yesu alieleza jinsi alivyowathamini sana marafiki wake kwa kusema hivi: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu.”—Luka 22:28.
11, 12. Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake nini, nao waliitikia namna gani?
11 Muda mfupi baada ya Yesu kuwapongeza wanafunzi wake kwa sababu ya ushikamanifu wao, walimwacha. Kwa muda mfupi, waliruhusu woga wa wanadamu ushinde upendo wao kwa Kristo. Kwa mara nyingine tena, Yesu aliwasamehe. Baada ya kufa na kufufuliwa, aliwatokea na kuwahakikishia tena urafiki wake. Zaidi ya hilo, aliwakabidhi kazi takatifu, yaani, kufanya wanafunzi kutoka kwa “watu wa mataifa yote” na kuwa mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mt. 28:19; Mdo. 1:8) Wanafunzi hao waliitikia jinsi gani?
12 Wanafunzi hao walijitoa kwa moyo na nafsi yao yote kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, walijaza Yerusalemu mafundisho yao baada ya muda mfupi. (Mdo. 5:27-29) Hata vitisho vya kuwaua havingeweza kuwazuia wasitii amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi. Makumi machache tu ya miaka baada ya Yesu kuwapa amri hiyo, mtume Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa imehubiriwa “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Bila shaka, wanafunzi hao walithibitisha kwamba walithamini urafiki wao pamoja na Yesu!
13. Wanafunzi wa Yesu waliruhusu mafundisho yake yabadili maisha yao katika njia gani?
13 Pia, wale waliogeuka na kuwa wanafunzi waliruhusu mafundisho ya Yesu yabadili maisha yao. Kwa wengi, hilo lilimaanisha kufanya mabadiliko makubwa katika mwenendo na utu wao. Kabla ya hapo, wanafunzi fulani wapya walikuwa walawiti, wazinzi, walevi, au wezi. (1 Kor. 6:9-11) Wengine walihitaji kubadili mtazamo wao kuelekea watu wa jamii nyingine. (Mdo. 10:25-28) Hata hivyo, walimtii Yesu. Walivua utu wao wa zamani na kuvaa utu mpya. (Efe. 4:20-24) Walipata kujua “akili ya Kristo,” wakaelewa na kuiga njia yake ya kufikiri na kutenda.—1 Kor. 2:16.
Urafiki Pamoja na Kristo Leo
14. Yesu aliahidi kufanya nini wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo”?
14 Wengi kati ya Wakristo hao wa karne ya kwanza walimjua Yesu kibinafsi au walimwona baada ya ufufuo wake. Kwa wazi, sisi hatuna pendeleo hilo. Basi, tunaweza kuwa marafiki wa Kristo jinsi gani? Njia moja ni kutii mwongozo unaotolewa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, ambayo inafanyizwa na ndugu watiwa-mafuta wa Yesu ambao wangali hai duniani. Yesu aliahidi kwamba wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” atamweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:3, 45-47) Leo, wengi wa wale ambao wanataka kuwa marafiki wa Kristo si washiriki wa jamii hiyo ya mtumwa. Kukubali kwao mwongozo wanaopata kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu kuna uvutano gani juu ya urafiki wao pamoja na Kristo?
15. Ni nini kitakachoamua ikiwa mtu atawekwa upande wa kondoo au wa mbuzi?
15 Soma Mathayo 25:31-40. Yesu aliwaita wale ambao wangefanyiza jamii ya mtumwa mwaminifu kuwa ndugu zake. Katika mfano unaohusu kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi, Yesu anasema waziwazi kwamba jinsi watu wanavyowatendea ndugu zake ni kana kwamba wanamtendea yeye binafsi. Kwa kweli, alisema kwamba jambo kuu ambalo lingetofautisha kondoo na mbuzi ni jinsi ambavyo mtu angemtendea hata yule aliye ‘mdogo zaidi wa ndugu zake.’ Kwa hiyo, njia kuu ambayo wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaonyesha tamaa yao ya kuwa marafiki wa Kristo ni kwa kuiunga mkono jamii ya mtumwa mwaminifu.
16, 17. Tunaweza kuonyesha jinsi gani urafiki wetu kuwaelekea ndugu za Kristo?
16 Ikiwa unatumaini kuishi duniani chini ya Ufalme wa Mungu, unaweza kuonyesha jinsi gani urafiki wako kuwaelekea ndugu za Kristo? Acheni tuchunguze njia tatu tu. Kwanza, kwa kushiriki kwa moyo wote katika kazi ya kuhubiri. Kristo aliwaamuru ndugu zake wahubiri habari njema ulimwenguni pote. (Mt. 24:14) Hata hivyo, ingekuwa vigumu sana kwa mabaki ya ndugu za Kristo walio duniani leo kutimiza daraka hilo bila msaada wa waandamani wao wa kondoo wengine. Kwa kweli, kila mara washiriki wa jamii ya kondoo wengine wanaposhiriki katika kazi ya kuhubiri, wanawasaidia ndugu za Kristo kutimiza kazi yao takatifu. Kristo na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara wanathamini sana tendo hilo la urafiki.
17 Njia ya pili ambayo wale wa jamii ya kondoo wengine wanaweza kuwasaidia ndugu za Kristo ni kwa kutegemeza kifedha kazi ya kuhubiri. Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wajifanyie marafiki na “mali zisizo za uadilifu.” (Luka 16:9) Si kwamba tunaweza kununua kwa pesa urafiki wa Yesu au Yehova. Badala yake, tunapotumia vitu vyetu vya kimwili ili kutegemeza kazi ya Ufalme, tunathibitisha urafiki na upendo wetu, si kwa maneno tu, bali pia “kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:16-18) Tunatoa utegemezo huo wa kifedha kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri, kwa kutoa michango ya pesa ili kujenga na kutunza mahali petu pa ibada, na pia wakati tunapotoa michango ya pesa kwa ajili ya kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote. Iwe kiasi cha pesa tunachotoa ni kidogo au ni kikubwa, bila shaka Yehova na Yesu wanathamini tunapotoa kwa uchangamfu.—2 Kor. 9:7.
18. Kwa nini tunapaswa kutii mwongozo unaotegemea Biblia ambao unatolewa na wazee wa kutaniko?
18 Njia ya tatu ambayo sote tunaweza kuthibitisha kwamba sisi ni marafiki wa Kristo ni kwa kutii mwongozo unaotolewa na wazee wa kutaniko. Wanaume hao wamewekwa rasmi na roho takatifu chini ya mwongozo wa Kristo. (Efe. 5:23) Mtume Paulo aliandika hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee.” (Ebr. 13:17) Nyakati nyingine, huenda tukaliona kuwa jambo gumu kutii mwongozo unaotegemea Biblia ambao tunapewa na wazee wa kutaniko letu. Inaelekea tunajua udhaifu wao, na huenda hilo likapotosha maoni yetu kuhusu mashauri yao. Hata hivyo, bado Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko, anapendezwa kuwatumia wanaume hao wasio wakamilifu. Kwa hiyo, urafiki wetu pamoja na Kristo unahusiana moja kwa moja na jinsi tunavyoitikia mamlaka yao. Tunapofuata mwongozo wa wazee kwa furaha badala ya kukazia fikira makosa yao, tunathibitisha kwamba tunampenda Kristo.
Tunaweza Kupata Wapi Marafiki Wazuri?
19, 20. Tunaweza kupata nini katika kutaniko, na tutachunguza nini katika habari inayofuata?
19 Yesu anaendelea kututunza si kupitia tu usimamizi wa wachungaji wenye upendo, bali pia kupitia mama, ndugu, na dada wa kiroho katika kutaniko. (Soma Marko 10:29, 30.) Ulipoanza kwa mara ya kwanza kushirikiana na tengenezo la Yehova, watu wako wa ukoo waliitikia jinsi gani? Labda, walikuunga mkono katika jitihada zako za kumkaribia Mungu na Kristo. Lakini Yesu alionya kwamba wakati fulani “adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mt. 10:36) Inafariji kama nini kujua kwamba katika kutaniko, tunaweza kupata wale ambao watashikamana nasi kwa ukaribu kuliko ndugu zetu wa kimwili!—Met. 18:24.
20 Kama inavyoonyeshwa na salamu za Paulo mwenyewe mwishoni mwa barua yake kwa kutaniko la Roma, alianzisha urafiki wa karibu sana na watu wengi. (Rom. 16:8-16) Mtume Yohana alimalizia barua yake ya tatu kwa maneno haya: “Wape rafiki salamu zangu kwa jina.” (3 Yoh. 14) Ni wazi kwamba yeye pia alianzisha urafiki wa kudumu na watu wengi. Tunaweza kuiga jinsi gani mfano wa Yesu na wanafunzi wa mapema kwa kuanzisha na kudumisha urafiki mzuri na ndugu na dada zetu wa kiroho? Tutachunguza jibu la swali hilo katika habari inayofuata.
-
-
Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na UpendoMnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 15
-
-
Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo
“Mambo haya ninawaamuru ninyi, kwamba mpendane.”—YOH. 15:17.
1. Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walihitaji kuendelea kuwa marafiki wa karibu?
KATIKA usiku wake wa mwisho duniani, Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake washikamanifu waendelee kuwa marafiki. Mapema jioni hiyo, alisema kwamba upendo ambao wangeonyeshana ungewatambulisha kuwa wafuasi wake. (Yoh. 13:35) Mitume walihitaji kuendelea kuwa marafiki wa karibu ikiwa wangevumilia majaribu ambayo yalikuwa mbele yao na kutimiza kazi ambayo Yesu angewakabidhi baada ya muda mfupi. Kwa kweli, Wakristo wa karne ya kwanza walijulikana kwa sababu ya ujitoaji wao wa moyo wote kwa Mungu na kwa waamini wenzao.
2. (a) Tumeazimia kufanya nini, na kwa nini? (b) Tutachunguza maswali gani?
2 Leo, inafurahisha kama nini kushirikiana na tengenezo la ulimwenguni pote ambalo washiriki wake wanafuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza! Tumeazimia kutii amri ya Yesu ya kuonyeshana upendo wa kweli. Hata hivyo, katika siku hizi za mwisho, watu kwa ujumla si washikamanifu na hawaonyeshi upendo wa asili. (2 Tim. 3:1-3) Mara nyingi urafiki wao ni wa kijuu-juu tu na wa kichoyo. Ili tuendelee kutambuliwa kuwa Wakristo wa kweli, ni lazima tuepuke mitazamo kama hiyo. Acheni basi tuchunguze maswali yafuatayo: Ni nini msingi wa urafiki mzuri? Tunaweza kupata jinsi gani marafiki wazuri? Ni wakati gani tunapohitaji kukomesha urafiki? Na tunaweza kudumisha jinsi gani urafiki wenye kujenga?
Ni Nini Msingi wa Urafiki Mzuri?
3, 4. Ni nini msingi wa urafiki wenye nguvu zaidi, na kwa nini?
3 Urafiki wenye nguvu zaidi unajengwa juu ya msingi wa upendo kwa Yehova. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.” (Mhu. 4:12) Yehova anapokuwa uzi wa tatu katika urafiki, urafiki huo utadumu.
4 Ni kweli kwamba wale wasiompenda Yehova wanaweza pia kuanzisha urafiki mzuri. Lakini watu wanapokuwa marafiki kwa sababu wote wawili wanampenda Mungu, urafiki wao utakuwa imara kabisa. Wanapokosa kuelewana, marafiki wa kweli wanatendeana kwa njia ambayo inampendeza Yehova. Ikiwa wapinzani wa Mungu wanajaribu kusababisha migawanyiko, maadui hao wanagundua kwamba urafiki kati ya Wakristo wa kweli hauwezi kuvunjwa. Katika historia yote, watumishi wa Yehova wamethibitisha kwamba wako tayari kufa badala ya kuwasaliti waabudu wenzao.—Soma 1 Yohana 3:16.
5. Kwa nini urafiki kati ya Ruthu na Naomi ulikuwa wenye kudumu?
5 Bila shaka, tunaweza kufurahia urafiki ulio mzuri zaidi pamoja tu na wale ambao wanampenda Yehova. Fikiria mfano wa Ruthu na Naomi. Wanawake hao walijenga urafiki ambao ni kati ya urafiki wenye kuvutia zaidi katika Biblia. Kwa nini urafiki wao ulikuwa wenye nguvu na wenye kudumu? Ruthu alifunua sababu alipomwambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. . . . Yehova na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.” (Rut. 1:16, 17) Ni wazi kwamba Ruthu na Naomi wote wawili walimpenda sana Mungu, na waliacha upendo huo uongoze jinsi walivyotendeana. Kwa sababu hiyo, wanawake hao wawili walibarikiwa na Yehova.
Jinsi ya Kupata Marafiki Wazuri
6-8. (a) Urafiki wenye kudumu unategemea nini? (b) Unaweza kuchukua jinsi gani hatua ya kwanza ili upate marafiki?
6 Mfano wa Ruthu na Naomi unaonyesha kwamba urafiki mzuri haujitokezi wenyewe tu. Msingi wa kweli wa urafiki ni kwamba marafiki wote wawili wanapaswa kumpenda Yehova. Lakini ni lazima tujitahidi sana na kujidhabihu ili tuwe na urafiki wenye kudumu. Hata ndugu na dada wa kimwili wanaomwabudu Yehova katika familia za Kikristo wanahitaji kujitahidi sana ili kuwa marafiki wa karibu. Hivyo basi, unaweza kuanzisha jinsi gani urafiki mzuri?
7 Chukua hatua ya kwanza. Mtume Paulo aliwatia moyo marafiki wake katika kutaniko la Roma ‘wafuate mwendo wa ukaribishaji-wageni.’ (Rom. 12:13) Kufuata kihalisi njia fulani kunatia ndani kupiga hatua mbalimbali, moja baada ya nyingine. Vivyo hivyo, kuwa mkaribishaji-wageni kunatia ndani kuchukua hatua fulani ndogo-ndogo, kwa ukawaida. Hakuna mtu mwingine anayeweza kufuata njia au mwendo wa ukaribishaji-wageni kwa niaba yako. (Soma Methali 3:27.) Njia moja ya kuwa mkaribishaji-wageni ni kuwaalika watu mbalimbali katika kutaniko ili wale chakula chepesi pamoja nawe. Je, unaweza kufanya ukaribishaji-wageni uwe zoea lako kwa kuwaalika washiriki wa kutaniko lenu?
8 Njia nyingine ambayo unaweza kutumia ili kupata marafiki ni kuwaalika watu mbalimbali washiriki pamoja nawe katika kazi ya kuhubiri. Unaposimama kwenye mlango wa mwenye nyumba na kumsikia yule ambaye unahubiri naye akizungumza kutoka moyoni kuhusu upendo wake kwa Yehova, utachochewa kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na mtu huyo.
9, 10. Paulo alituwekea mfano gani, na tunaweza kumwiga namna gani?
9 Panuka katika upendo wako. (Soma 2 Wakorintho 6:12, 13.) Je, umewahi kuhisi kwamba hakuna mtu yeyote katika kutaniko lenu anayeweza kuwa rafiki yako? Ikiwa ndivyo, je, inaweza kuwa kwamba una matakwa makali kuhusu ni nani anayeweza kuwa rafiki yako? Mtume Paulo aliweka mfano mzuri wa kupanuka katika upendo. Pindi moja, hangewazia kamwe kuwa na urafiki wa karibu na watu wasio Wayahudi. Hata hivyo, alikuja kuwa “mtume kwa mataifa.”—Rom. 11:13.
10 Zaidi ya hayo, Paulo hakuanzisha urafiki na watu wa umri wake tu. Kwa mfano, yeye na Timotheo walikuja kuwa marafiki wa karibu ingawa walikuwa na umri na malezi tofauti. Leo, vijana wengi wanathamini sana kuanzisha urafiki na washiriki wenye umri mkubwa kutanikoni. Vanessa, mwenye umri wa miaka 20 na kitu, anasema hivi: “Nina rafiki mpendwa sana ambaye ana umri wa miaka zaidi ya 50. Ninaweza kumweleza kila jambo ambalo ninaweza kumweleza rafiki wa umri wangu. Ananijali sana.” Walianzisha urafiki huo jinsi gani? Vanessa anasema: “Nilijitahidi sana kuanzisha urafiki huo, sikungoja urafiki huo ujianzishe tu.” Je, uko tayari kuanzisha urafiki pamoja na watu wasio wa umri wako? Bila shaka, Yehova atakuthawabisha kwa sababu ya jitihada zako.
11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yonathani na Daudi?
11 Uwe mshikamanifu. Sulemani aliandika hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Met. 17:17) Alipokuwa akiandika maneno hayo, huenda Sulemani alikuwa akifikiria urafiki ambao baba yake, Daudi, alikuwa nao pamoja na Yonathani. (1 Sam. 18:1) Mfalme Sauli alitaka mwana wake Yonathani awe mrithi wa kiti cha ufalme wa Israeli. Lakini Yonathani alikubali uhakika wa kwamba Yehova alimchagua Daudi kwa ajili ya pendeleo hilo. Tofauti na Sauli, Yonathani hakumwonea wivu Daudi. Hakuchukizwa na pongezi ambazo Daudi alipewa, wala hakuamini uchongezi ambao Sauli alieneza kumhusu Daudi. (1 Sam. 20:24-34) Je, sisi ni kama Yonathani? Marafiki wetu wanapopata mapendeleo, je, tunafurahi pamoja nao? Wanapopatwa na matatizo, je, tunawafariji na kuwategemeza? Tukisikia porojo zenye kuumiza zikienezwa kumhusu rafiki yetu, je, tunafanya haraka kuziamini? Au, kama Yonathani, tunamtetea rafiki yetu kwa ushikamanifu?
Wakati Urafiki Unapohitaji Kukomeshwa
12-14. Ni tatizo gani ambalo wanafunzi fulani wa Biblia wanakabili, na tunaweza kuwasaidia jinsi gani?
12 Mwanafunzi wa Biblia anapoanza kufanya mabadiliko katika maisha yake, anaweza kukabili matatizo kuhusiana na marafiki. Anaweza kuwa na marafiki ambao anafurahia kushirikiana nao lakini ambao hawaishi kulingana na viwango vya Biblia vya maadili. Zamani, huenda alishirikiana nao kwa ukawaida. Lakini, sasa anaona kwamba mambo ambayo wanafanya yanaweza kuwa na uvutano mbaya juu yake, na anahisi kwamba anahitaji kupunguza wakati ambao anashirikiana na marafiki kama hao. (1 Kor. 15:33) Hata hivyo, huenda akahisi kwamba asiposhirikiana nao, ataonekana si mshikamanifu.
13 Ikiwa wewe ni mwanafunzi wa Biblia ambaye anakabili tatizo hilo, kumbuka kwamba rafiki wa kweli atafurahi kuona kuwa unajitahidi kuboresha maisha yako. Huenda akataka kujiunga nawe katika kujifunza kumhusu Yehova. Kwa upande mwingine, marafiki wa uwongo ‘watakutukana’ kwa sababu huendi nao kwenye “dimbwi lilelile la chini la upotovu.” (1 Pet. 4:3, 4) Kwa kweli, marafiki hao ndio wasio washikamanifu kwako, bali si wewe.
14 Wanafunzi wa Biblia wanapoachwa na marafiki wao wa zamani ambao hawampendi Mungu, washiriki wa kutaniko wanaweza kujaza pengo hilo. (Gal. 6:10) Je, unawajua kibinafsi wale wanaohudhuria mikutano yenu ambao wanajifunza Biblia? Je, unaweza pindi fulani kuwa na ushirika wenye kujenga pamoja nao?
15, 16. (a) Tunapaswa kutenda jinsi gani rafiki yetu akiacha kumtumikia Yehova? (b) Tunaweza kuthibitisha jinsi gani kwamba tunampenda Mungu?
15 Namna gani ikiwa rafiki yako katika kutaniko anaamua kumwacha Yehova, na labda anatengwa na ushirika? Hali hiyo inaweza kuwa yenye kufadhaisha sana. Dada mmoja alisema hivi kuhusu alivyohisi wakati rafiki yake wa karibu alipoacha kumtumikia Yehova: “Nilihisi ni kana kwamba sehemu fulani ya mwili wangu ilikuwa imekufa. Nilifikiri kwamba rafiki yangu alikuwa imara katika kweli, lakini hakuwa imara. Nilijiuliza ikiwa alikuwa akimtumikia Yehova ili aifurahishe tu familia yake. Kisha nikaanza kuchunguza nia yangu. Je, nilikuwa nikimtumikia Yehova kwa sababu zinazofaa?” Dada huyo alikabiliana jinsi gani na hali hiyo? Anasema hivi: “Nilimtupia Yehova mzigo wangu. Nimeazimia kumwonyesha Yehova kwamba ninampenda kwa sababu ya sifa zake, bali si kwa sababu ananipa marafiki katika tengenezo lake.”
16 Hatuwezi kutazamia kwamba tutaendelea kuwa marafiki wa Mungu ikiwa tunawaunga mkono wale ambao wanachagua kuwa marafiki wa ulimwengu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Yak. 4:4) Tunaweza kuthibitisha kwamba tunampenda Mungu kwa kutumaini kwamba ikiwa sisi ni washikamanifu kwake, atatusaidia kukabiliana na uchungu wa kupoteza rafiki. (Soma Zaburi 18:25.) Dada aliyetajwa mapema anasema hivi kwa ufupi: “Nilijifunza kwamba hatuwezi kumfanya mtu ampende Yehova au kutupenda sisi. Kwa wazi, ni uamuzi wa mtu binafsi.” Hivyo basi, tunaweza kufanya nini ili kudumisha urafiki wenye kujenga pamoja na wale wanaobaki katika kutaniko?
Kudumisha Urafiki Mzuri
17. Marafiki wazuri wanazungumza jinsi gani?
17 Mawasiliano mazuri yanadumisha uhusiano wa karibu kati ya marafiki. Unaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu Ruthu na Naomi, Daudi na Yonathani, na Paulo na Timotheo, utaona kwamba marafiki wazuri wanazungumza kwa uhuru lakini kwa heshima. Kuhusu jinsi tunavyopaswa kuzungumza na wengine, Paulo aliandika hivi: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.” Paulo alikuwa akisema hasa kuhusu jinsi tunavyopaswa kuzungumza na wale “walio nje,” yaani, wale ambao si ndugu zetu Wakristo. (Kol. 4:5, 6) Bila shaka, ikiwa tunapaswa kuwaheshimu watu wasio waamini tunapozungumza nao, tunapaswa kuwaheshimu hata zaidi marafiki wetu katika kutaniko!
18, 19. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu shauri lolote tunalopewa na rafiki yetu Mkristo, na wazee wa Efeso walituwekea mfano gani?
18 Marafiki wazuri wanathamini maoni ya mmoja na mwingine, hivyo mawasiliano kati yao yanapaswa kuwa yenye adabu na yaliyo wazi. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Mafuta na uvumba ndivyo huufanya moyo ushangilie, ndivyo pia utamu wa rafiki ya mtu kwa sababu ya shauri la nafsi.” (Met. 27:9) Je, hivyo ndivyo unavyoona shauri lolote ambalo unapewa na rafiki yako? (Soma Zaburi 141:5.) Ikiwa rafiki yako anaonyesha hangaiko kuhusu mambo fulani unayofanya, wewe unaitikia jinsi gani? Je, unaona maelezo yake kuwa tendo la fadhili zisizostahiliwa, au unamkasirikia?
19 Mtume Paulo alifurahia uhusiano wa karibu pamoja na wazee wa kutaniko la Efeso. Inaelekea kwamba aliwafahamu wanaume fulani kati yao wakati walipogeuka na kuwa waamini. Hata hivyo, wakati wa mkutano wake wa mwisho pamoja nao, aliwapa mashauri ya waziwazi. Waliitikia jinsi gani? Marafiki wa Paulo hawakukasirika. Badala yake, walithamini jinsi alivyopendezwa nao, na hata walilia aliposema kwamba hawatamwona tena.—Mdo. 20:17, 29, 30, 36-38.
20. Rafiki mwenye upendo atafanya nini?
20 Marafiki wazuri hawakubali tu mashauri mazuri lakini pia wanayatoa. Bila shaka, tunahitaji kutambua wakati wa ‘kukazia akili mambo yetu wenyewe.’ (1 The. 4:11) Na tunapaswa pia kutambua kwamba kila mmoja wetu “atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Rom. 14:12) Lakini inapohitajika, rafiki mwenye upendo atamkumbusha rafiki yake viwango vya Yehova kwa fadhili. (1 Kor. 7:39) Kwa mfano, utafanya nini ikiwa unatambua kwamba rafiki yako ambaye hajafunga ndoa anaanza kuwa na uhusiano wa karibu sana na mtu ambaye si mwamini? Je, utasitasita kumweleza mahangaiko yako kwa sababu unaogopa kuumiza hisia zake? Au utafanya nini ikiwa rafiki yako anapuuza mashauri yako? Rafiki mzuri ni yule anayetafuta msaada wa wachungaji wenye upendo ili kumsaidia rafiki ambaye amejikwaa katika kosa fulani. Kuchukua hatua kama hiyo kunahitaji ujasiri. Hata hivyo, hakuna madhara yoyote ya kudumu ambayo yataharibu urafiki unaotegemea upendo kwa Yehova.
21. Nyakati nyingine sote tutafanya nini, lakini kwa nini ni jambo la maana kudumisha urafiki wenye nguvu katika kutaniko?
21 Soma Wakolosai 3:13, 14. Nyakati nyingine, tutafanya mambo ambayo yatawafanya marafiki wetu wawe na “sababu ya kulalamika” juu yetu, nao pia watatenda au kusema mambo ambayo yatatukasirisha. Yakobo aliandika hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2) Hata hivyo, kinachoamua ikiwa sisi ni marafiki wa kweli si mara ambazo tunatendeana makosa, bali ni ikiwa tunasameheana kabisa makosa hayo. Ni jambo la maana kama nini kwetu kujenga urafiki wenye nguvu kwa kuzungumza waziwazi na kusameheana kwa hiari! Tukionyesha upendo kama huo, utakuwa “kifungo kikamilifu cha muungano.”
-