-
MarafikiMaswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SEHEMU YA 3
Marafiki
Kuna faida gani ya kuwa na marafiki?
□ Hakuna faida
□ Kuna faida fulani
□ Kuna faida kubwa
Je, ni rahisi kupata marafiki?
□ Ndiyo
□ Hapana
Je, una rafiki wa chanda na pete?
□ Ndiyo
□ Hapana
Ni sifa gani ambayo ungependa rafiki yako awe nayo?
Biblia inasema kwamba “rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Huyo ndiye rafiki ambaye wewe unahitaji! Lakini, huenda ikawa vigumu kupata marafiki, na huenda ikawa vigumu hata zaidi kudumisha marafiki. Unaweza kupata marafiki bora na kudumisha urafiki huo jinsi gani? Mashauri yaliyo katika Sura ya 9-12 yanaweza kukusaidia.
-
-
Nifanye Nini Ili Kujiondolea Upweke?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SEHEMU YA 9
Nifanye Nini Ili Kujiondolea Upweke?
Ingawa hali ya hewa ni shwari, huna mipango yoyote. Lakini, marafiki wako wote wana mipango. Wenzako wanakula raha. Kwa mara nyingine tena, hawakukualika! Kutoalikwa huvunja moyo, lakini unaweza kuvunjika moyo hata zaidi unapoanza kufikiria ni kwa nini hukualikwa. Huenda ukawaza, ‘Labda nina kasoro fulani. Kwa nini hakuna mtu anayetaka kuwa pamoja nami?’
LABDA, mara kwa mara, umejikuta katika hali kama ile inayotajwa katika ukurasa unaotangulia. Huenda ukaona kana kwamba kuna pengo kubwa sana kati yako na vijana wenzako. Kila mara unapojaribu kuanzisha mazungumzo pamoja nao, unashikwa na kigugumizi. Unapopata nafasi ya kuchangamana na marafiki, unalemewa na haya. Kwa nini jambo rahisi kama kuchangamana tu na marafiki liwe gumu hivyo?
Badala ya kubaki peke yako ng’ambo moja ya pengo hilo, unaweza kujenga madaraja. Acha tuone jinsi unavyoweza kufanya hivyo.
● Pengo la 1: Kuwa na maoni yasiyofaa juu yako mwenyewe. Vijana fulani hujidharau sikuzote. Wanaamini kwamba hakuna mtu anayependezwa nao na kwamba hawana lolote la kuchangia katika mazungumzo. Je, hivyo ndivyo unavyojiona? Ikiwa ndivyo, maoni hayo yanaweza tu kuzidisha pengo hilo linalokutenganisha na vijana wenzako.
Daraja: Kazia fikira vipawa ulivyo navyo. (2 Wakorintho 11:6) Jiulize, ‘Nina sifa gani nzuri?’ Fikiria vipawa fulani au sifa nzuri ulizo nazo na uziandike hapa chini.
․․․․․
Bila shaka, umepungukiwa katika mambo mengine na ni vizuri kukumbuka hilo. (1 Wakorintho 10:12) Lakini pia, una mengi unayoweza kuchangia. Kujua vipawa ulivyo navyo kunaweza kukupa ujasiri unaohitaji wa kuondolea mbali maoni yasiyofaa kujihusu.
● Pengo la 2: Haya. Ungependa kuanzisha mazungumzo, lakini nafasi inapojitokeza, unakosa la kusema. “Mimi huwa na haya kila wakati,” analalamika Elizabeth mwenye umri wa miaka 19. “Mimi hushindwa kabisa kuzungumza na watu katika mikutano ya Kikristo, nami huvutiwa sana na wale wanaoweza kufanya hivyo!” Ikiwa hali yako inafanana na ya Elizabeth, huenda ukaona ni vigumu kuziba pengo hilo.
Daraja: Pendezwa kikweli na wengine. Usijali—haimaanishi uwe kasuku. Anza kwa kupendezwa na mtu mmoja tu. Kijana anayeitwa Jorge anasema: “Jambo rahisi kama vile kuwajulia watu hali au kuwauliza kuhusu kazi yao kunakuwezesha kuwajua vizuri zaidi.”
Pendekezo: Usizungumze tu na watu wa umri wako. Biblia inataja mifano mbalimbali ya watu waliokuwa na urafiki mkubwa kama vile Ruthu na Naomi, Daudi na Yonathani, na Timotheo na Paulo. (Ruthu 1:16, 17; 1 Samweli 18:1; 1 Wakorintho 4:17) Pia, kumbuka kwamba mazungumzo yanahusisha pande mbili, si upande mmoja tu. Watu hupenda watu wanaowasikiliza. Kwa hiyo, ikiwa wewe ni mwenye haya, kumbuka kwamba huhitaji kutawala mazungumzo!
Andika majina ya watu wazima wawili ambao ungependa kuwajua vizuri zaidi.
․․․․․
Mbona usimfikie mmoja wa watu ulioandika na kuanzisha mazungumzo naye? Kadiri unavyojitahidi kutafuta nafasi za kuzungumza na watu mbalimbali katika “ushirika mzima wa akina ndugu,” ndivyo upweke wako utakavyopungua.—1 Petro 2:17.
● Pengo la 3: Tabia zisizopendeza. Kwa kawaida watu “wajuaji” hupenda kutumia matusi, dhihaka na kuwavunjia wengine heshima. Pia, kuna watu ambao hupenda ubishi na kusisitiza wengine wafuate maoni yao. Kwa kuwa wanajiona kuwa ‘waadilifu kupita kiasi,’ wao humshutumu mtu yeyote asiyefikia viwango vyao. (Mhubiri 7:16) Bila shaka, hungependa kuwa karibu na watu kama hao! Hata hivyo, inawezekana kwamba pengo limetokea kwa sababu hivyo ndivyo ulivyo? Biblia inasema: “Mpumbavu husema maneno mengi,” na pia “katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa.”—Mhubiri 10:14; Methali 10:19.
Daraja: Jifunze kuwa na “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Hata ikiwa hukubaliani na maoni ya mwingine, onyesha subira na umruhusu azungumze. Kazia fikira mambo mnayokubaliana. Ukiona kwamba ni lazima ueleze maoni yako yanayotofautiana na yake, fanya hivyo kwa upole na kwa busara.
Zungumza na wengine vile ambavyo ungependa wazungumze nawe. Biblia inashauri: “Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika na kubishana.” (Wafilipi 2:14) Mambo kama ubishi, utani usiofaa, kuwatusi wengine au kuona hawafai kitu, huzidisha pengo. Watakupenda zaidi ‘maneno yako yakiwa na neema sikuzote.’—Wakolosai 4:6.
Je, Uazimie Kupata Marafiki Hata Iweje?
Baada ya mazungumzo hayo mafupi, na kujichunguza, huenda umeona njia mbalimbali za kujenga madaraja ya kuziba pengo lililopo kati yako na wengine. Bila shaka, unapaswa kuona mambo kihalisi. Usitazamie kupendwa na kila mtu. Yesu alisema kwamba watu fulani hata watawachukia wale wanaotenda mema. (Yohana 15:19) Kwa hiyo, kuazimia kufanya urafiki na kila mtu ni kazi bure.
Hata hivyo, unaweza kujitahidi kuwavutia wengine bila kulegeza viwango vyako vinavyotegemea kanuni za Biblia. Samweli aliyeishi nyakati za Biblia aliazimia kabisa kufanya yale yanayompendeza Mungu. Matokeo? Aliendelea “kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.” (1 Samweli 2:26) Ukitia bidii, hata wewe utafanikiwa!
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 8
Unaweza kupata habari zaidi kwa kutazama DVD ya “Young People Ask—How Can I Make Real Friends?” inayopatikana katika lugha zaidi ya 40
Rafiki yako wa karibu anabadilika ghafula na kuwa adui. Utafanya nini?
MAANDIKO MUHIMU
“Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”—Methali 11:25.
PENDEKEZO
Endeleza mazungumzo. Kwa mfano, mtu akikuuliza kama ulifurahia mwisho-juma, usimjibu tu ndiyo. Eleza ni nini kilichokufurahisha. Kisha mwulize yeye alifanya nini.
JE, WAJUA . . . ?
Biblia inaonyesha kwamba huenda Musa, Yeremia, na Timotheo walikuwa watu wenye haya.—Kutoka 3:11, 13; 4:1, 10; Yeremia 1:6-8; 1 Timotheo 4:12; 2 Timotheo 1:6-8.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Pengo kubwa linalonizuia ni ․․․․․
Nitajitahidi kuziba pengo hilo kwa․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini huenda Wakristo fulani wakawa wapweke?
● Ni nini kinachoweza kukusaidia kuwa na maoni yaliyosawazika kujihusu badala ya kuwa na maoni yasiyofaa nyakati zote?
● Unaweza kumfariji jinsi gani ndugu au dada kijana anayelemewa na upweke?
[Blabu katika ukurasa wa 88]
“Dada mmoja Mkristo alijaribu kufanya urafiki nami, lakini mwanzoni sikutaka. Baadaye tulipoanza urafiki, nilijiona kuwa mpumbavu sana! Mwishowe akawa rafiki yangu wa chanda na pete hata ingawa alikuwa amenizidi umri kwa miaka 25!’’—Marie
[Picha katika ukurasa wa 87]
Unaweza kuziba pengo linalokutenganisha na vijana wenzako kwa kujenga daraja
-
-
Mbona Rafiki Yangu Ananitendea Hivi?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 10
Mbona Rafiki Yangu Ananitendea Hivi?
“Kerry alikuwa rafiki yangu mkubwa. Nilikuwa nikimpitia kila siku baada ya kazi kwa kuwa hakuwa na gari. Hata hivyo, muda si muda nilianza kuona kwamba ananitumia vibaya.
“Alikuwa akijitoma tu ndani ya gari langu huku akizungumza kwenye simu ya mkononi au kutuma ujumbe mfupi. Hakushukuru kamwe kwa kupewa lifti, naye akaacha kuchangia pesa za mafuta. Sikuzote alikuwa akiwachambua-chambua wengine. Nilijuta kwamba nimemvumilia kwa muda mrefu hivyo!
“Siku moja nilimwambia Kerry kwa fadhili kwamba sitampitia tena baada ya kazi. Tangu wakati huo, hakutaka tena kuniona. Naamini kwamba alitaka tu kuwa rafiki yangu kwa sababu ya faida alizopata kutokana na urafiki wetu. Hilo linaniumiza sana!”—Nicole.
INAWEZA kuwa hivyo kwa marafiki wenye uhusiano wa karibu sana. Siku moja ni marafiki wasioachana; siku ya pili hata hawasemezani. Kwa nini urafiki kama huo uvunjike haraka hivyo?
● Katika kisa cha Jeremy, mambo yalibadilika wakati rafiki yake wa karibu alipohamia eneo lililokuwa kilomita 1,600 hivi kutoka kwao. “Alipohama, hakunipigia simu tena,” Jeremy anasema, “na jambo hilo lilinihuzunisha sana.”
● Kerrin alianza kuona utu wa msichana ambaye alikuwa rafiki yake mkubwa kwa miaka mitano ukibadilika. “Nilihangaishwa sana na mtazamo na maneno yake,” anasema Kerrin. “Alianza kuchambua na kudharau mambo niliyoyaona kuwa ya maana. Nilipojaribu kuzungumza naye kuhusu jambo hilo, alisema kwamba ninajifanya mtakatifu, mimi si mwaminifu, na kwamba urafiki wetu hauna maana kwake!”
● Urafiki kati ya Gloria na rafiki yake wa karibu uliisha ghafula na bila mawasiliano yoyote. “Mwanzoni, tulipatana sana,” Gloria anasema, “naye aliniambia kwamba nilikuwa kama dada yake. Kisha, bila sababu yoyote, aliacha kufanya mambo pamoja nami, huku akitoa visingizio.”
● Matatizo kati ya Laura na Daria yalianza wakati Daria alipomnyakua mchumba wa Laura. “Daria alikuwa akizungumza naye kwa simu kwa saa nyingi, hata ingawa alijua kwamba kijana huyo ni mchumba wangu,” anasema Laura. “Nilisalitiwa na rafiki yangu mkubwa na kupoteza mchumba wangu wakati uleule!”
Tatizo Lilikuwa Nini?
Kila mtu hukosea. Kwa hiyo, si ajabu kwamba mara kwa mara rafiki anaweza kusema jambo ambalo linaweza kukuumiza. Huenda hata unakumbuka pindi fulani ambapo wewe mwenyewe uliwaumiza wengine. (Mhubiri 7:22) “Sisi sote hatujakamilika, na mara kwa mara tunaweza kukwaruzana,” anasema msichana anayeitwa Lisa. Kwa kawaida, mazungumzo mafupi yanaweza kuziba pengo ambalo limesababishwa na kutoelewana kidogo.
Hata hivyo, katika visa vingine, pengo katika urafiki halisababishwi na tukio moja tu bali linatokea wakati mnapotambua hatua kwa hatua kwamba mna mapendezi tofauti kinyume na mlivyokuwa mkifikiri. Kumbuka kwamba kadiri unavyokua ndivyo mapendezi yako yanavyobadilika—na ndivyo na ya rafiki yako. Unaweza kufanya nini ukitambua kwamba urafiki wenu umeanza kupoa?
Jinsi ya Kufufua Urafiki
Tuseme nguo unayoipenda sana imeraruka. Utafanya nini? Utaitupa au utaishona? Bila shaka, hatua utakayochukua itategemea nguo hiyo imeraruka kiasi gani na unaithamini kadiri gani. Ikiwa kwa kweli unaipenda sana nguo hiyo, haikosi utatafuta njia za kuirekebisha. Inaweza kuwa hivyo pia kuhusiana na urafiki uliovunjika. Mengi yanategemea tatizo lenyewe na jinsi ambavyo unathamini uhusiano huo.a
Kwa mfano, ikiwa umeambiwa au kutendewa kwa njia isiyo ya fadhili, unaweza kufunika jambo hilo kwa kufuata shauri la Zaburi 4:4: “Semeni moyoni mwenu, kitandani mwenu, na kunyamaza.” Kwa hiyo, kabla ya kuutupilia mbali urafiki huo, fikiri kwa uzito. Je, alitenda hivyo kwa makusudi? Ikiwa huna hakika, kwa nini usichukulie kwamba rafiki yako hakuwa na nia mbaya? Katika visa vingi, unaweza kuacha ‘upendo ufunike dhambi nyingi.’—1 Petro 4:8.
Pia, unaweza kuchunguza ikiwa ulichangia tatizo hilo. Kwa mfano, rafiki akifunua siri uliyomwambia, je, inawezekana kwamba hukutenda kwa hekima kwa kumtwika mzigo mzito hivyo? Unaweza pia kujiuliza ikiwa wewe mwenyewe ulichangia dhihaka unazopata, labda kwa kuongea kupita kiasi au kusema mambo ya kipumbavu. (Methali 15:2) Ikiwa ndivyo, jiulize, ‘Je, ninahitaji kufanya mabadiliko ili rafiki yangu aniheshimu?’
“Ningependa Tuzungumze”
Hata hivyo, namna gani ukiona kwamba huwezi kupuuza jambo lililotokea? Basi, huenda ikafaa kuzungumza na rafiki yako. Lakini uwe mwangalifu usifanye hivyo ukiwa umekasirika. Biblia inasema: “Mtu mwenye ghadhabu huchochea ugomvi, lakini yule ambaye hakasiriki upesi hutuliza mabishano.” (Methali 15:18) Kwa hiyo, kabla ya kujaribu kutatua tatizo hilo, kwanza tulia.
Unapoenda kuzungumza na rafiki yako, kumbuka kwamba kusudi lako si ‘kulipa uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Badala yake, lengo lako ni kutatua tatizo hilo na kurudisha urafiki. (Zaburi 34:14) Kwa hiyo, sema yaliyo moyoni. Unaweza kusema, “Tulikuwa marafiki. Sielewi kilichotokea. Ningependa tuzungumze.” Baada ya kujua kilichosababisha tatizo lenyewe, huenda ikawa rahisi kuwa marafiki tena. Hata rafiki yako asipotaka kuzungumza, angalau unaweza kufarijika kwa kujua kwamba wewe umejaribu kurudisha amani.
Baada ya kufanya yote hayo, kumbuka kwamba “kuna rafiki wanaoelekea kuvunjana vipande-vipande,” hata hivyo, kuna “rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Methali 18:24) Ni kweli kwamba hata marafiki wakubwa wanaweza kukwaruzana mara kwa mara. Hilo likitukia, fanya yote uwezayo kurekebisha uhusiano wenu. Ndiyo, kuwa tayari kutatua hali za kutoelewana zinazotokea, kunaonyesha kwamba unaendelea kukomaa.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 8
Huenda baadhi ya rafiki zako wanatumia saa nyingi wakipiga gumzo katika Intaneti. Ni nini kinachowavutia hivyo?
[Maelezo ya Chini]
a Huenda kusiwe na haja ya kurudisha uhusiano wa karibu na watu fulani, hasa ikiwa hawajiendeshi kwa njia inayomfaa Mkristo.—1 Wakorintho 5:11; 15:33.
MAANDIKO MUHIMU
“Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.
PENDEKEZO
Kabla ya kukata kauli, msikilize kwanza rafiki yako.—Methali 18:13.
JE, WAJUA . . . ?
Rafiki wazuri hutambua kwamba rafiki zao wanahitaji nafasi ya kupumua. (Methali 25:17) Lakini, uhusiano unaweza kuvunjika mtu anapodai rafiki yake atumie muda mwingi kupita kiasi pamoja naye.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nikihitaji kuzungumza na rafiki yangu kwa sababu ameniumiza, nitaanza kwa kusema ․․․․․
Hata ikiwa nimekasirika kwa sababu ya jambo ambalo rafiki yangu ametenda, nitajitahidi kudumisha amani kwa ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini nyakati nyingine pengo hutokea kati ya marafiki?
● Ikiwa rafiki yako amekuumiza, ni mambo gani ambayo unaweza kuamua kusahau badala ya kuzungumza naye, na ni mambo gani ambayo unahitaji kuyatatua kwa kuzungumza naye?
● Ikitokea kwamba umeumizwa na rafiki, ni mambo gani yenye faida unayoweza kujifunza kutokana na hali hiyo?
● Unaweza kufanya nini ili kupunguza uwezekano wa kuumizwa na rafiki?
[Blabu katika ukurasa wa 95]
“Ikiwa ningeweza kuanza upya, singekuwa mwenye kudai mno. Ningemsikiliza zaidi na kumuunga mkono badala ya kukazia fikira kasoro zake. Sasa nimetambua kwamba ili urafiki ufaulu, kinachohitajiwa ni kutatua matatizo na magumu yanayotokea.’’—Keenon
[Picha katika ukurasa wa 94]
Kama vile nguo iliyoraruka inavyoweza kurekebishwa, ndivyo na urafiki uliovunjika
-
-
Mfano wa Kuigwa—LidiaMaswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
Mfano wa Kuigwa—Lidia
Ingawa ni mwamini mpya, Lidia anachukua hatua ya kwanza kumwonyesha ukarimu Paulo na waandamani wake. (Matendo 16:14, 15) Hivyo, anapata pendeleo la pekee la kuwa pamoja na wanafunzi hao. Baada ya Paulo na Sila kuachiliwa kutoka gerezani, wanaenda wapi? Wanarudi moja kwa moja kwenye nyumba ya Lidia!—Matendo 16:40.
Kama Lidia, je, unaweza kuchukua hatua ya kwanza kuwajua wengine? Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Anza polepole. Jitahidi kuzungumza na mtu mmoja-mmoja. Unaweza kuweka mradi wa kuanzisha mazungumzo pamoja na mtu fulani kila mara unapohudhuria mkutano wa Kikristo. Jaribu kutabasamu. Ikiwa hujui la kusema, uliza maswali au useme jambo fulani linalokuhusu. Sikiliza kwa makini. Baada ya muda, huenda ukajisikia huru kusema mengi zaidi. Mara nyingi watu huvutiwa na maneno yanayosemwa kwa unyoofu, yenye fadhili, na yenye kupendeza. (Methali 16:24) Kwa kuwa Lidia alikuwa mwenye urafiki na mkarimu, alibarikiwa kupata marafiki wazuri. Ukimwiga, wewe pia utapata baraka hiyo!
-
-
Kuna Ubaya Kufanya Urafiki Kupitia Intaneti?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 11
Kuna Ubaya Kufanya Urafiki Kupitia Intaneti?
Ni njia gani ya mawasiliano unayopenda?
□ Uso kwa uso
□ Simu
□ Kompyuta
Ni nani ambaye unaona ni rahisi kuwasiliana naye?
□ Wanafunzi wenzako
□ Watu wa familia
□ Wakristo wenzako
Ni wapi hasa unapoona kwamba ni rahisi kuzungumza kwa uhuru?
□ Shuleni
□ Nyumbani
□ Katika mikutano ya kutaniko
UMEJIBUJE swali la kwanza? Je, umejibu kwamba unapendelea kuwasiliana kupitia kompyuta badala ya kuzungumza uso kwa uso? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayependelea kufanya hivyo. Vijana wengi hutumia Intaneti kuanzisha na kuendeleza urafiki. Msichana anayeitwa Elaine anasema: “Inasisimua kujua kwamba unaweza kukutana na watu kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu—watu ambao hungepata kuwajua kamwe.” Tammy, mwenye umri wa miaka 19, anataja jambo lingine linalowavutia watu. “Unaweza kuwafanya watu wakuone vyovyote vile unavyotaka,” anasema. “Unapozungumza na mtu uso kwa uso, asipopendezwa nawe, hakuna lolote unaloweza kufanya.”
Sasa angalia jinsi ulivyojibu swali la pili na la tatu. Usishangae ikiwa ni rahisi zaidi kwako kuzungumza na wanafunzi wenzako kuliko Wakristo wenzako katika mikutano ya Kikristo. “Shuleni, ni rahisi zaidi kupata watu walio katika hali kama yako,” anasema Jasmine mwenye umri wa miaka 18. “Hilo hufanya iwe rahisi zaidi kuzungumza nao.”
Hivyo basi, inaeleweka ni kwa nini ungependa kuwasiliana na wanafunzi wenzako kupitia Intaneti. Tammy anakiri kwamba kwa muda fulani alikuwa akifanya hivyo. Anasema: “Wanafunzi wenzangu wote walikuwa wakiwasiliana katika Intaneti, nami sikutaka kubaki nyuma.”a Natalie, mwenye umri wa miaka 20, alianzisha gombowavu (Web page) katika Intaneti ili kuwasiliana na marafiki. “Tekinolojia imepiga hatua,” anasema. “Kuna njia nyingi mpya za kuwasiliana. Hiyo ni moja kati ya njia hizo, nami naipenda.”
Usipuuze Hatari
Bila shaka, watu fulani huona kwamba ni rahisi zaidi kuanzisha na kuendeleza urafiki katika Intaneti. Kwa mfano, Natalie anasema: “Katika Intaneti unakuwa na ujasiri ambao kwa kawaida hungekuwa nao unapozungumza na mtu uso kwa uso.” Tammy pia ana maoni kama hayo. “Ikiwa wewe ni mtu mwenye haya,” anasema, “unapowasiliana kupitia Intaneti, una nafasi ya kutosha kupanga mambo hususa utakayosema.”
Hata hivyo, kuna hatari za kuwasiliana kupitia Intaneti, na kuzipuuza kungekuwa upumbavu. Kwa mfano: Je, ungefumba macho yako huku ukitembea katika mtaa hatari? Kwa nini basi uzurure-zurure katika Intaneti bila kujali hatari zilizomo?
Fikiria hatari za kujaribu kupata marafiki katika Intaneti. Elaine, ambaye wakati fulani alikuwa na mazoea ya kupiga gumzo na watu asiowajua katika Intaneti, anasema: “Ni rahisi sana kuanzisha mazungumzo na watu wapotovu. Nyakati nyingine hata haichukui muda kabla ya mtu kuanza kusema mambo machafu au kuuliza maswali kama vile: ‘Wewe ni bikira? Wewe hufanya ngono ya kinywa?’ Wengine hata huomba mzungumzie mambo machafu ili kujisisimua kingono.”
Namna gani ikiwa ni mazungumzo tu na rafiki unayemwamini? Bado unahitaji kuwa mwangalifu. “Unaweza kutumia muda mwingi sana ukizungumza na mtu wa jinsia tofauti, hata kama mtu huyo ni ‘rafiki tu,’” Joan anasema. “Kadiri unavyotumia muda mwingi zaidi ukimtumia mtu huyo ujumbe, ndivyo urafiki wenu unavyozidi kukua, nanyi mnaweza kuanza kuzungumzia mambo ya kimahaba.”
“Wale Wanaoficha Jinsi Walivyo”
Mfalme Daudi alijua vizuri faida ya kujihadhari na marafiki wasiofaa. Aliandika: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”—Zaburi 26:4.
Katika Intaneti, je, umewahi kukutana na watu kama hao wanaozungumziwa na Daudi? Katika Intaneti, watu ‘wanaficha jinsi walivyo’ nyakati gani? ․․․․․
Kwa upande mwingine, inawezekana kwamba wewe huficha jinsi ulivyo unapotumia Intaneti? “Nilikuwa nikianza mazungumzo na watu kisha nibadili utu wangu upatane na mazungumzo hayo,” anasema Abigail, ambaye alikuwa na mazoea ya kupiga gumzo kwenye vituo vya Intaneti.
Msichana anayeitwa Leanne alitumia aina nyingine ya udanganyifu. Anasema: “Nilikuwa na mazoea ya kuwasiliana katika Intaneti na mvulana fulani wa kutaniko jirani. Muda si muda tukaanza kuambiana kwamba ‘tunapendana.’ Wazazi walipokuwa wakipita, nilikuwa nikibofya na kuficha nilichokuwa nikifanya kwenye kompyuta, nao hawakujua kamwe kilichokuwa kikiendelea. Hawakufikiri kamwe kwamba binti yao mwenye umri wa miaka 13 alikuwa akimwandikia mvulana mwenye umri wa miaka 14 mashairi ya kimapenzi. Walikuwa gizani kabisa.”
Uwe Mwangalifu
Bila shaka, haimaanishi kwamba mawasiliano yote kwenye Intaneti ni mabaya. Kwa mfano, watu wengi kutia ndani watu wazima hutumia Intaneti ili kuwasiliana na marafiki. Ikiwa ndivyo unavyofanya, je, kuna mambo yoyote unayopaswa kujihadhari nayo? Fikiria mambo yanayofuata.
● Chunguza muda unaotumia katika Intaneti, na usiruhusu Intaneti ikuibie wakati wa kufanya mambo ya maana zaidi, kutia ndani kulala. Kijana fulani anayeitwa Brian anasema: “Vijana fulani shuleni walisema kwamba walitumia Intaneti mpaka usiku wa manane.”—Waefeso 5:15, 16.
● Wasiliana tu na watu unaowajua. Watu wapotovu wana kawaida ya kutumia Intaneti wakitafuta vijana wanaoweza kudanganyika kwa urahisi.—Waroma 16:18.
● Uwe mwangalifu unapofanya mambo ya kibiashara. Uwe mwangalifu sana unapotoa habari zako za kibinafsi. Kosa dogo tu linaweza kufanya upoteze kila kitu.—Mathayo 10:16.
● Unapowatumia marafiki wako picha, jiulize, ‘Je, picha hizi zinamwakilisha mtu anayedai kwamba anamtumikia Mungu?’—Tito 2:7, 8.
● Sawa na mazungumzo ya uso kwa uso, mazungumzo katika Intaneti yakianza kuingilia “mambo yasiyofaa,” yakomeshe.—Waefeso 5:3, 4.
● Unapotumia Intaneti, usiwe mnafiki hata kidogo. Ikiwa unawaficha wazazi wako jinsi ulivyo, basi kuna tatizo. “Simfichi mama yangu chochote,” anasema tineja anayeitwa Kari. “Mimi humwonyesha ninachofanya kwenye Intaneti.”—Waebrania 13:18.
“Mvumilivu Hula Mbivu!”
Ungependa kupata marafiki? Hilo ni jambo la kawaida. Wanadamu waliumbwa wafurahie ushirika wa wengine. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, ikiwa unatamani kupata marafiki, unatenda kulingana na jinsi ulivyoumbwa! Hata hivyo, uwe mwangalifu unapochagua marafiki.
Lakini uwe na hakika kwamba unaweza kupata marafiki wazuri ukitegemea viwango vya Neno la Mungu. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 15 alisema hivi: “Si rahisi kupata marafiki wanaompenda Yehova na wakati huohuo wanakupenda. Hata hivyo, mvumilivu hula mbivu!”
Ati maneno hayawezi kuumiza? Porojo zinaweza kuchoma kama upanga. Unaweza kuzikomesha jinsi gani?
[Maelezo ya Chini]
a Urafiki shuleni utazungumziwa kwa mapana na marefu katika Sura ya 17.
MAANDIKO MUHIMU
“Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”—Zaburi 26:4.
PENDEKEZO
Usipokuwa mwangalifu, unaweza kupoteza wakati mwingi sana kwenye Intaneti! Kwa hiyo, amua kiasi cha wakati utakachotumia na kuhakikisha kwamba hupitishi wakati ulioweka. Ikihitajika, tega saa ambayo italia na kukukumbusha muda wako ukiisha.
JE, WAJUA . . . ?
Mtu mwenye nia mbaya anaweza kukupata kwa urahisi akipata habari chache tu kukuhusu katika Intaneti, kama vile jina lako, shule na namba yako ya simu.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Kila juma ningependa kutumia Intaneti kwa muda wa na ili nifanye hivyo nita ․․․․․
Nikigundua kwamba ninazungumza na mtu nisiyemjua kwenye Intaneti, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kuwasiliana na mtu kwenye Intaneti badala ya uso kwa uso kunaweza kuwa na faida na hatari gani?
● Kwa nini ni rahisi kuficha utu wako unapozungumza kwenye Intaneti?
● Ni nini kinachoweza kukusaidia usipoteze wakati mwingi katika Intaneti?
● Intaneti inaweza kutumiwa kwa ajili ya mawasiliano gani yanayofaa?
[Blabu katika ukurasa wa 103]
Siwasiliani katika Intaneti na watu nisiowajua au wale ambao kwa kawaida singeshirikiana nao.’’—Joan
[Picha katika ukurasa wa 100, 101]
Je, ungefumba macho yako huku ukitembea katika mtaa hatari? Kwa nini basi uwasiliane katika Intaneti bila kujali hatari zilizomo?
-
-
Porojo Ina Ubaya Gani?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 12
Porojo Ina Ubaya Gani?
“Siku moja nilienda katika karamu. Kesho yake kukatokea uvumi kwamba nililala na mvulana fulani huko. Ulikuwa uwongo mtupu!”—Linda.
“Nyakati nyingine mimi husikia uvumi kwamba nina urafiki wa kimapenzi na mtu fulani, mtu ambaye hata simjui! Watu wengi wanaopiga porojo hawatafuti ukweli wa mambo.”—Mike.
POROJO inaweza kufanya maisha yako yaonekane kama sinema. “Karibu kila siku ninasikia porojo kunihusu,” anasema Amber mwenye umri wa miaka 19. “Kulikuwa na uvumi kwamba nina mimba, nimetoa mimba mara kadhaa, mimi ni mlanguzi wa dawa za kulevya, nami hutumia dawa za kulevya. Mbona watu waseme mambo kama hayo kunihusu? Sielewi hata kidogo!”
Mvulana au msichana mwenye nia mbaya anaweza kukuharibia sifa yako akitumia barua-pepe na ujumbe mfupi pasipo hata kufumbua kinywa chake. Uvumi mbaya sana unaweza kuenea haraka kwa kuandika maneno machache tu na kuyasambaza! Katika visa fulani, wengine wameanzisha tovuti (Web site) ili kumwaibisha mtu fulani. Kwa kawaida blogu kwenye Intaneti huwa na porojo chungu nzima ambazo mtu hangeweza kuzisema uso kwa uso.
Lakini je, sikuzote ni vibaya kuongea juu ya wengine? Je, kuna . . .
Porojo Nzuri?
Tia alama taarifa inayofuata, kuonyesha kama ni kweli au si kweli.
Hakuna porojo nzuri. □ Kweli □ Si kweli
Ni jibu gani lililo sahihi? Inategemea unavyoelewa neno “porojo.” Ikiwa ni mazungumzo ya kupisha wakati tu, basi kuna pindi inapofaa. Biblia inatuhimiza ‘tupendezwe na maisha ya wengine.’ (Wafilipi 2:4, New Century Version) Haimaanishi kwamba tujiingize katika mambo ambayo hayatuhusu. (1 Petro 4:15) Hata hivyo, mazungumzo ya kawaida hutusaidia kupata habari, kama vile, ni nani anayeoa au kuolewa, au ni nani aliyepata mtoto. Ukweli ni kwamba hatuwezi kusema tunawajali wengine ikiwa hatuzungumzi kamwe kuwahusu.
Pamoja na hayo, mazungumzo ya kawaida yanaweza kugeuka kwa urahisi na kuwa porojo mbaya. Kwa mfano, mtu akisema “Bob na Sue wanaweza kufaana sana katika ndoa” maneno hayo yanaweza kutiwa chumvi na kuwa “Bob na Sue wanachumbiana,” ijapokuwa Bob na Sue hawana habari hata kidogo. Huenda ukasema, ‘Ah si kitu!’ Lakini, ingekuwaje ikiwa maneno hayo yangesemwa kukuhusu?
Porojo kama hiyo ilienezwa kumhusu Julie, aliye na umri wa miaka 18, naye aliumia sana. Anasema: “Nilikasirika sana na kuanza kumshuku kila mtu.” Jane, mwenye umri wa miaka 19, alikuwa katika hali kama hiyo. “Nilianza kumwepuka mvulana ambaye ilisemekana tunachumbiana,” anasema huku akiongezea, “Sikupaswa kumtendea hivyo, alikuwa rafiki yangu, na kwa maoni yangu tunapaswa kuwa na uhuru wa kuzungumza pasipo mtu yeyote kuanzisha uvumi kutuhusu!”
Endesha Mazungumzo kwa Busara!
Unaweza kuongoza jinsi gani ulimi wako unaposhawishiwa kupiga porojo? Ili kujibu swali hilo, wazia ustadi unaohitajiwa ili kuendesha gari katika barabara yenye magari mengi. Bila kutarajiwa, hali fulani inaweza kukulazimu kutoka upande mmoja wa barabara hadi mwingine, kupisha gari lingine, au kusimama kabisa. Ukiwa macho, utaona kilicho mbele na kuchukua hatua inayohitajika.
Ndivyo ilivyo kuhusiana na mazungumzo pia. Kwa kawaida unaweza kujua iwapo mazungumzo yanaanza kuwa porojo yenye kudhuru. Hilo linapotukia, je, unaweza ‘kutoka upande huo wa barabara’? Usipofanya hivyo, tahadhari, porojo inaweza kutokeza madhara. Mike anaeleza hivi: “Bila kufikiri, nilisema kwamba msichana mmoja anapendezwa sana na wavulana, nazo habari hizo zikamfikia. Sitasahau kamwe uchungu aliokuwa nao alipozungumza nami, jinsi alivyoumizwa na maneno niliyosema. Ingawa tulitatua jambo hilo, ninasikitika ninapokumbuka kwamba nilimuumiza hivyo!”
Hakuna shaka kwamba maneno yanaweza kuumiza. Hata Biblia inasema “kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma.” (Methali 12:18) Ndiyo sababu unapaswa kupima maneno yako! Ni kweli kwamba baada ya mazungumzo kupamba moto ujasiri unahitajika ili kuyakatiza. Ni kama vile tu Carolyn mwenye miaka 17 anavyosema: “Unahitaji kuwa mwangalifu unasema nini. Ikiwa hujasikia jambo kutoka chanzo kinachotegemeka, huenda ukawa unaeneza uwongo.” Kwa hiyo, unaposikia mambo yanayoweza kugeuka na kuwa porojo yenye kudhuru, fuata shauri la Paulo la ‘kufanya iwe shabaha yako kuishi kwa utulivu na kukazia akili mambo yako mwenyewe.’—1 Wathesalonike 4:11.
Ni kwa njia gani unaweza kupendezwa na wengine na wakati uleule kukazia akili mambo yako mwenyewe? Kabla ya kusema jambo fulani juu ya mtu, jiulize: ‘Je, nina habari kamili? Kwa nini ninaeneza habari hiyo? Wengine watanionaje wakijua kwamba ninaeneza porojo?’ Swali hilo la mwisho ni la maana, kwa sababu kujulikana kuwa mweneza porojo kunafunua mengi zaidi kukuhusu wewe kuliko yule anayezungumziwa.
Porojo Ikienezwa Kukuhusu
Unaweza kufanya nini porojo ikienezwa kukuhusu? Andiko la Mhubiri 7:9 linasema hivi: “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako.” Badala yake, jaribu kuzuia hisia zako na kutochukua mambo kwa uzito kupita kiasi. Biblia inasema: “Usiweke moyoni mwako maneno yote ambayo huenda watu wakasema, . . . kwa maana moyo wako mwenyewe unajua vema kwamba hata mara nyingi wewe, naam hata wewe, umewalaani wengine.”—Mhubiri 7:21, 22.
Bila shaka, hakuna udhuru wa kueneza porojo yenye kudhuru. Hata hivyo, kujiachilia uongozwe na hisia kunaweza kukuharibia sifa kuliko porojo yenyewe! Kwa nini usiwe na maoni kama ya Renee? Anasema: “Kwa kawaida mimi huumia mtu anaposema jambo baya kunihusu, hata hivyo mimi hujaribu kudumisha usawaziko. Leo ni mimi, kesho ni mwingine au jambo lingine.”a
Basi, tenda kwa hekima kwa kubadili mazungumzo yanapoanza kuwa porojo yenye kudhuru. Na mambo mabaya yanaposemwa kukuhusu, onyesho ukomavu kwa kutoachilia hisia zikuongoze. Acha ujulikane kwa matendo yako mema. (1 Petro 2:12) Ukifanya hivyo, utadumisha uhusiano mzuri pamoja na wengine na kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Katika hali fulani, huenda likawa jambo la hekima kuzungumza kwa busara na mtu anayeeneza porojo kukuhusu. Hata hivyo, katika visa vingi, hakuna haja kwa sababu “upendo hufunika dhambi nyingi.”—1 Petro 4:8.
MAANDIKO MUHIMU
“Anayelinda kinywa chake anaitunza nafsi yake. Anayefungua wazi midomo yake —yeye atapata uharibifu.”—Methali 13:3.
PENDEKEZO
Mtu akianza kukusimulia porojo, unaweza kumwambia: “Sifurahii mazungumzo haya. Kwanza, hata mhusika mwenyewe hayuko hapa ajitetee.”
JE, WAJUA . . .?
Kusikiliza tu porojo kunaweza kukufanya uwe na hatia kwa kiasi fulani. Kumruhusu mpiga-porojo aendelee kukusimulia ni kama kuongeza kuni kwenye moto.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nikishawishiwa kueneza porojo, nita ․․․․․
Watu wakisema mambo yanayoniumiza, nitashughulikia hali hiyo kwa ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Ni mambo gani yanayofaa tunayoweza kuzungumza kuhusu wengine?
● Je, porojo imewahi kuenezwa juu yako, ikiwa ndivyo, ulijifunza nini kutokana na kisa hicho?
● Kueneza porojo juu ya wengine kunaweza kuharibu jinsi gani sifa yako?
[Blabu katika ukurasa wa 107]
“Nilijuta sana wakati ambapo mtu niliyeeneza porojo kumhusu alipokuja kuzungumza nami. Sikuwa na njia ya kukimbilia! Bila shaka nilijifunza kwamba ni afadhali kuzungumza na mtu moja kwa moja badala ya kumsengenya!’’—Paula
[Picha katika ukurasa wa 108]
Kama silaha hatari, porojo yenye kudhuru inayoweza kumuumiza na kumharibia mtu sifa
-
-
Daftari—MarafikiMaswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SEHEMU YA 3—MARAFIKI
Daftari—Marafiki
Eleza tatizo fulani ambalo umepata hivi karibuni kuhusu urafiki.
․․․․․
Unaweza kutumia jinsi gani habari ambazo umesoma katika sehemu hii kushughulikia tatizo hilo?
․․․․․
-