-
Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake WaliozeekaMnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
-
-
8. Kwa nini makutaniko yanapaswa kuwahangaikia Wakristo waliozeeka?
8 Vivyo hivyo, Yehova anafurahi wakati makutaniko yanapowasaidia Wakristo waaminifu waliozeeka ambao wana uhitaji lakini hawana washiriki wa familia ambao ni waamini au walio tayari kuwatunza. (1 Tim. 5:3, 5, 9, 10) Kwa kufanya hivyo, washiriki wa kutaniko wanaonyesha kwamba wana ‘hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, na huruma nyororo,’ kuelekea waliozeeka. (1 Pet. 3:8) Paulo anatoa mfano unaoonyesha jinsi kutaniko linavyopaswa kuwahangaikia washiriki wake waliozeeka anaposema kwamba kiungo kimoja cha mwili kikiumia, “viungo vingine vyote huumia pamoja nacho.” (1 Kor. 12:26) Tunapochukua hatua zinazofaa kuwasaidia waliozeeka kwa kuchochewa na huruma, tunaonyesha kwamba tunafuata kanuni ya shauri hili la Paulo: “Endeleeni kubebeana mizigo mizito, na hivyo kuitimiza sheria ya Kristo.”—Gal. 6:2.
9. Mtu aliyezeeka anaweza kubeba mizigo gani mizito?
9 Wakristo waliozeeka wanabeba mizigo gani mizito? Wengi wao wanachoka haraka. Huenda wakashindwa kufanya hata mambo ya kawaida, kama vile, kwenda kumwona daktari, kushughulikia barua, kulipia huduma mbalimbali, kusafisha nyumba, na kupika chakula. Kwa kuwa mara nyingi mtu anapozeeka anapoteza hamu ya kula chakula na kunywa maji, huenda wakafikiri kwamba hawahitaji kula au kunywa maji ingawa wanayahitaji sana. Wanaweza pia kupoteza hamu ya chakula cha kiroho. Kwa sababu ya macho na masikio kuzeeka, kusoma na kusikiliza programu za mambo ya kiroho, na pia kujitayarisha ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunaweza kuchosha. Basi, wengine wanaweza kuwasaidia kwa njia gani Wakristo hao waliozeeka?
Jinsi Unavyoweza Kusaidia
10. Wazee wa kutaniko wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba waliozeeka wanasaidiwa inavyofaa?
10 Katika makutaniko mengi, waliozeeka wanatunzwa kwa njia nzuri sana. Ndugu na dada wenye upendo wanawasaidia kununua vitu, kupika, na kufanya usafi. Wanawasaidia kujifunza, kujitayarisha kwa ajili ya mikutano, na kuwa wa kawaida katika huduma. Mashahidi vijana wanaenda pamoja nao kwenye mikutano na katika huduma na pia wanawasaidia kusafiri. Ikiwa waliozeeka hawawezi kutoka nyumbani, mipango inafanywa ili wasikilize mikutano kupitia simu, au mikutano inarekodiwa kwenye kanda ili wasikilize. Inapowezekana, wazee wa kutaniko wanahakikisha kwamba mipango inayofaa inafanywa ili kuwasaidia washiriki waliozeeka katika kutaniko.c
11. Simulia jinsi familia moja ilivyomsaidia ndugu mmoja aliyezeeka.
11 Mkristo mmoja-mmoja pia anaweza kuwakaribisha na kuwaonyesha ukarimu. Baada ya mke wa ndugu mmoja aliyezeeka kufa, ndugu huyo hangeweza tena kulipa kodi ya nyumba bila malipo ya uzeeni ya mke wake. Yeye na mke wake walikuwa wameifundisha familia moja Biblia, yaani, baba, mama, na binti zao wawili vijana. Familia hiyo ilikuwa na nyumba kubwa, na hivyo ikampa ndugu huyo vyumba viwili ili aishi humo. Kwa miaka 15, walikula pamoja, walikuwa na pindi za furaha, na walimwonyesha upendo wa kindugu. Binti zao vijana walifaidika sana na imani na uzoefu wake wa miaka mingi, naye alifaidika sana na ushirika wao wenye kufurahisha. Ndugu huyo aliyezeeka aliishi nao mpaka alipokufa akiwa na umri wa miaka 89. Familia hiyo bado inamshukuru Mungu kwa sababu ya baraka nyingi walizopata kwa kushirikiana na ndugu huyo. ‘Hawajapoteza thawabu yao’ kwa sababu ya kumsaidia mwanafunzi mwenzao wa Yesu Kristo.—Mt. 10:42.d
12. Unaweza kufanya nini ili kuwaonyesha upendo mwororo ndugu na dada waliozeeka?
12 Huenda usiweze kumsaidia ndugu au dada aliyezeeka kama familia hiyo ilivyofanya, lakini unaweza kuwasaidia waliozeeka kufika kwenye mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani. Unaweza pia kuwaalika nyumbani kwako na kwenda nao katika tafrija. Unaweza kuwatembelea, hasa wanapokuwa wagonjwa au wanaposhindwa kutembea. Zaidi ya hayo, unaweza na unapaswa sikuzote kuwatendea kama watu wazima waliokomaa. Maadamu wanaweza kutumia uwezo wao wa kufikiri, Wakristo waliozeeka wanapaswa kushirikishwa katika kufanya maamuzi yote ambayo yanawahusu. Hata wale ambao wamepoteza uwezo wao wa kufikiri wanatambua ikiwa wanatendewa kwa heshima.
-
-
Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake WaliozeekaMnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
-
-
Lakini matatizo ya magonjwa na uzee yanaweza kuwalemea sana hata wale ambao wanasaidiwa na kutunzwa na washiriki wa familia wenye bidii. Wale wanaowatunza wanaweza pia kuchoka. Kutaniko lina pendeleo na daraka la kuonyesha upendo kwa matendo kwa kuwasaidia wale waliozeeka na wale wanaowatunza. (Gal. 6:10) Tunapowasaidia tunaonyesha kwamba hatuwaambii watu hao waende ‘wajipashe moto na kula vizuri’ bila kuwasaidia kwa njia inayofaa.—Yak. 2:15-17.
-