Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Dini ya Kweli Je, Ni Moja Tu?
    Amkeni!—2008 | Machi
    • Dini ya Kweli Je, Ni Moja Tu?

      Watu fulani huchukizwa na swali hilo. Kwa kuwa kuna dini nyingi ulimwenguni, wao hufikiri kwamba yeyote anayedai kwamba yeye tu ndiye aliye na ukweli lazima awe na akili finyu au hata kiburi. Wao huona kwamba inapatana na akili kufikiri kuna jambo fulani zuri katika dini zote au nyingi kati ya hizo. Je, una maoni kama hayo?

      BILA shaka, kuna pindi ambapo lingekuwa jambo la busara kuwa na maoni mbalimbali. Kwa mfano, mtu anaweza kuamini vyakula fulani vinaweza kumfanya awe na afya bora. Lakini je, anapaswa kuwalazimisha watu wale vyakula hivyo kana kwamba hiyo ndiyo njia pekee ya kuwa na afya nzuri? Kwa kweli, ungekuwa ni unyenyekevu na hekima kuona kwamba huenda vyakula ambavyo mtu mwingine anachagua ni vyenye afya zaidi angalau kwa mtu huyo.

      Je, tunaweza kusema hivyo kuhusu dini? Je, kuna njia mbalimbali zinazokubalika ambazo mtu anaweza kuchagua ikitegemea malezi au jinsi mtu anavyoelewa mambo? Au je, kuna imani moja tu ya kweli ya kidini inayopaswa kufuatwa na wanadamu wote? Acheni tuchunguze maoni ya Biblia. Kwanza tutachunguza ikiwa watu wanaweza kupata kweli. Ikiwa haiwezi kupatikana, basi hakuna haja ya kutafuta dini moja ya kweli.

      Je, Kweli ya Kidini Inaweza Kupatikana?

      Muda mfupi kabla ya kuuawa, Yesu Kristo alimwambia hivi Gavana Mroma Pontio Pilato aliyekuwa akimhoji: “Kila mtu aliye upande wa ile kweli huisikiliza sauti yangu.” Huenda Pilato alikuwa na shaka alipomwuliza: “Kweli ni nini?” (Yohana 18:37, 38) Kwa upande mwingine, Yesu alisema kwa ujasiri kuhusu kweli. Hakuwa na shaka kwamba kuna kweli. Kwa mfano, fikiria mambo manne ambayo Yesu aliwaambia watu tofauti.

      “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.”—Yohana 18:37.

      “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.”—Yohana 14:6.

      “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.

      “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—Yohana 8:31, 32.

      Kwa kuwa Yesu alizungumza kwa uhakika kuhusu kweli na kwamba tunaweza kujifunza kweli, je, hatupaswi kuchunguza uwezekano wa kwamba kuna kweli ya kidini na kwamba inaweza kupatikana?

      Je, Kuna Kweli?

      Bila shaka utakubali kwamba kuna mambo fulani ambayo tunaweza kuwa na uhakika kwamba yapo. Una hakika kwamba wewe upo na kwamba vitu vinavyokuzunguka ni halisi. Miti, milima, mawingu, jua, na mwezi, yaani, ulimwengu halisi, si vitu vya kuwaziwa tu. Kwa kweli kuna watu wachache ambao wanaweza kujaribu kukusadikisha kwamba uhalisi wa vitu hivyo unatiliwa shaka. Lakini wewe hukubaliani na wazo hilo la ajabu, sivyo?

      Pia kuna sheria za asili. Tuna hakika vilevile kwamba sheria hizo zipo. Kwa mfano, ukiruka kutoka kwenye jabali kubwa utaanguka; ukikataa kula utasikia njaa; na ukikosa kula kwa muda mrefu utakufa. Una hakika kwamba sheria hizo za asili haziwaathiri watu wachache tu na kutowaathiri wengine. Zinawaathiri wanadamu wote na hivyo zinatumika ulimwenguni pote.

      Biblia inataja sheria moja inayotumika ulimwenguni pote inapouliza hivi: “Je, mtu anaweza kukusanya moto kifuani pake na mavazi yake yasiungue?” Kwa kweli maneno hayo yalipoandikwa, ilijulikana ulimwenguni pote kwamba nguo zinaweza kuteketea zikiguswa na moto. Hata hivyo, methali hiyo ya Biblia ilikuwa ikitaja jambo muhimu zaidi, yaani, “yule anayelala na mke wa mwenzake” atapata madhara makubwa.—Methali 6:27, 29.

      Je, tunaweza kuwa na hakika kwamba maneno hayo ni kweli kabisa? Huenda watu fulani wakakataa. Wanaweza kudai kwamba viwango vya maadili hutofautiana kati ya watu, na kwamba vinategemea malezi, imani, na hali za mtu. Lakini fikiria sheria chache za Mungu kuhusu maadili zinazopatikana katika Biblia. Je, sheria hizo hazikubaliwi kuwa kweli ulimwenguni pote?

      Biblia hushutumu uzinzi. (1 Wakorintho 6:9, 10) Watu fulani hawaoni fundisho hilo la Biblia kuwa kweli, na hivyo wao hufanya uzinzi. Hata hivyo, hata wao hupatwa na madhara machungu yanayotia ndani dhamiri mbaya, talaka, na majeraha ya kihisia yanayowaathiri wote wanaohusika.

      Mungu pia anashutumu ulevi. (Methali 23:20; Waefeso 5:18) Ni nini hutukia watu wanapolewa? Katika visa vingi wao hupoteza kazi, afya yao huzorota, na familia zao huvunjika na kuumia kihisia. (Methali 23:29-35) Madhara hayo huwapata hata wale ambao hawaamini kwamba ulevi ni mbaya. Je, ukweli kuhusu viwango hivyo vya maadili vinategemea imani au jinsi mtu anavyoona mambo?

      Pia kuna amri za Biblia ambazo zinatuchochea kufanya mema kama vile amri ya mume kumpenda mke wake, mke kumheshimu mume wake, na kuwafanyia wengine mema. (Mathayo 7:12; Waefeso 5:33) Kutii amri hizo huleta faida. Je, ungesema kwamba amri hizo zinawanufaisha watu fulani tu na haziwanufaishi wengine?

      Iwe sheria za Biblia zinafuatwa au hazifuatwi matokeo huonekana. Jambo hilo linaonyesha kwamba sheria hizo si maoni mbalimbali ambayo mtu anachagua kufuata. Badala yake, sheria hizo ni kweli. Uthibitisho umeonyesha kwamba sheria za Biblia zinapofuatwa kunakuwa na matokeo mazuri, lakini zisipofuatwa kunakuwa na matokeo mabaya.

      Hebu fikiria: Ikiwa viwango vya maadili vya Biblia ni vya kweli kwa wanadamu wote, vipi kuhusu viwango vya Neno la Mungu kuhusu ibada? Vipi kuhusu kile ambacho Biblia inasema juu ya hali ya wafu na tumaini letu la kuishi milele? Ni jambo linalopatana na akili kwamba mafundisho hayo ya Biblia ni kweli ambazo zimetolewa kwa ajili ya wanadamu wote. Faida na madhara hayawapati tu wale wanaoamini kweli hizo.

      Inawezekana kupata kweli. Yesu alisema kwamba Neno la Mungu, Biblia ni kweli. (Yohana 17:17) Hata hivyo, huenda ikaonekana kwamba kweli haiwezi kupatikana. Kwa nini? Kwa sababu dini nyingi zinadai kufundisha yale ambayo Biblia inasema. Ni dini gani inayofundisha kweli ya Neno la Mungu? Je, ni dini moja tu? Je, kweli yote au sehemu yake inaweza kupatikana katika dini mbalimbali?

      [Blabu katika ukurasa wa 4]

      Madhara ya kukumbatia moto yanahusianaje na kutotii amri za Mungu?

  • Ni Nani Anayepaswa Kuamua Dini ya Kweli?
    Amkeni!—2008 | Machi
    • Ni Nani Anayepaswa Kuamua Dini ya Kweli?

      YESU alionyesha wazi kwamba si dini zote zinazokubaliwa na Mungu. Alizungumza kuhusu “manabii wa uwongo,” akiwalinganisha na mti unaozaa matunda yasiyofaa ambao “hukatwa na kutupwa ndani ya moto.” Pia alisema: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 7:15-22.

      Kwa kweli, Yesu alisema hivi kuhusu watu fulani ambao wangedai kumfuata: “Nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mathayo 7:23) Isitoshe, akizungumza na viongozi wa kidini wa siku zake, Yesu alitumia maneno yaleyale ambayo Mungu aliwaambia Waisraeli waasi-imani. Alisema hivi kuwahusu: “Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.”—Marko 7:6, 7.

      Ni wazi kwamba Mungu au Mwana wake hawakubali ibada ya aina zote. Hivyo, si dini zote za kweli. Je, hilo linamaanisha kwamba ni dini moja tu inayofundisha kweli? Je, haiwezekani kwamba Mungu anatumia dini kadhaa na kukataa nyingine? Au je, inawezekana kwamba Mungu anakubali au kukataa ibada ya mtu mmoja-mmoja walio katika dini mbalimbali licha ya yale ambayo dini zao hufundisha?

      Mtume Paulo aliandika hivi akiongozwa na roho ya Mungu: “Sasa nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.” (1 Wakorintho 1:10) Biblia pia inawahimiza Wakristo wawe na ‘akili ileile na wawe na upendo uleule, waunganishwe pamoja katika nafsi, wakishika wazo moja akilini.’—Wafilipi 2:2.

      Bila shaka, kunapokuwa na umoja kama huo, kunakuwa na dini moja. Kupatana na hilo, Biblia inasema kwamba kuna “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.”—Waefeso 4:4, 5.

      Biblia Inafunua Nini?

      Biblia inaunga mkono wazo hilo. Kwa kuichunguza Biblia utaona kwamba Mungu alishughulika na watu wake kupitia mfumo mmoja wa ibada. Mapema katika historia ya wanadamu, Mungu alitumia wazee wa ukoo kuwa wawakilishi wake. Wazee fulani maarufu kati yao ni Noa, Abramu (Abrahamu), Isaka, na Yakobo.—Mwanzo 8:18-20; 12:1-3; 26:1-4; 28:10-15.

      Wazao wa Yakobo walikuwa watumwa nchini Misri. Wakiwa huko, ingawa walikandamizwa waliongezeka na kuwa mamilioni. Mungu aliwakomboa kutoka utumwani na kuwapitisha kimuujiza katika Bahari Nyekundu. Kisha akawafanya wawe watu wake, na akawapa sheria kupitia mpatanishi ambaye ni Musa. Hivyo wakawa taifa la kale la Israeli, taifa la Mungu.—Kutoka 14:21-28; 19:1-6; 20:1-17.

      Mungu hakukubali ibada ya mataifa yaliyozunguka Israeli. Kwa kweli, aliwaadhibu watu wake walipoacha sheria zake na kufuata ibada ya mataifa hayo.—Mambo ya Walawi 18:21-30; Kumbukumbu la Torati 18:9-12.

      Namna gani watu mmojammoja kutoka mataifa mengine waliotaka kumwabudu Mungu wa kweli? Walihitaji kwanza kuacha ibada yao ya uwongo na kisha kujiunga na Waisraeli katika kumwabudu Yehova Mungu. Wengi wao walipata kibali cha Mungu na kuwa watumishi wake washikamanifu. Watu hao walitia ndani wanawake kama Rahabu Mkanaani na Ruthu Mmoabu; na wanaume kama vile Uria Mhiti na Ebed-meleki Mwethiopia; na vikundi vya watu kama vile Wagibeoni. Mfalme Sulemani wa Israeli alisali kutoka moyoni kwa niaba ya watu wote waliojiunga katika ibada ya kweli pamoja na watu wa Mungu.a—2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33.

      Baada ya Yesu Kuja Duniani

      Baadaye Yesu alipokuja duniani, ibada ya kweli ilianzishwa kwa kutegemea mafundisho yake, na kusudi la Mungu lilifafanuliwa kwa njia kubwa. Baada ya muda, waabudu wa kweli waliitwa “Wakristo.” (Matendo 11:26) Hivyo, Wayahudi waliotaka kibali cha Mungu walihitaji kuacha ibada yao ya zamani. Hawakupaswa kuchagua mifumo miwili ya ibada au kuabudu wakiwa mtu mmojammoja. Kama vile tumeona katika Neno la Mungu, waabudu wa kweli waliunganishwa katika “imani moja.”—Waefeso 4:4, 5.

      Leo huenda wazo la kwamba Mungu anashughulika na wanadamu kupitia dini moja tu halivutii watu fulani. Hata hivyo, hivyo ndivyo Biblia inakata maneno. Nyakati za zamani, watu wengi walioabudu kwa njia zao wenyewe walitambua ukweli huo. Walijiunga na waabudu wa kweli wa Yehova, na ingawa mwanzoni walikuwa na mashaka, yote yaligeuzwa yakawa baraka nyingi na furaha. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba baada ya mwanamume Mwethiopia kukubali Ukristo na kubatizwa “aliendelea kwenda zake akishangilia.”—Matendo 8:39.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki