Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yesu Angejibuje?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Yesu Angejibuje?

      Leo, watu wanaodai kumwogopa Mungu wanahisi kwamba dini inapaswa kujihusisha na siasa. Wanaamini kwamba dini inaweza kusaidia katika kutatua matatizo ya wanadamu. Hata hivyo, waamini wengine wanyoofu wanafikiri kwamba dini na siasa hazipaswi kuchanganywa. Wewe binafsi unafikiri dini inatimiza fungu gani katika siasa? Je, dini inapaswa kushirikiana na siasa?

      YESU KRISTO ametajwa kuwa “mtu mwenye uvutano mkubwa zaidi katika historia ya kidini ya wanadamu.” Fikiria kama tungeweza kumuuliza Yesu swali hili, Je, dini inapaswa kujihusisha na siasa? Yesu angejibuje? Alipokuwa duniani, alijibu swali hilo kupitia maneno na matendo yake. Kwa mfano, katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alitoa miongozo inayoweza kuwasaidia wafuasi wake kutambua jukumu wanalopaswa kutimiza katika jamii. Acha tuchunguze mambo fulani katika mahubiri hayo yanayojulikana sana.

      Jinsi Wakristo Wanavyoweza Kuwasaidia Wengine

      Yesu alieleza mtazamo ambao wafuasi wake wanapaswa kuwa nao kuelekea watu ulimwenguni. Alisema hivi: “Ninyi ndio chumvi ya dunia; lakini chumvi ikipoteza nguvu zake, ladha yake itarudishwaje? Haitumiki tena kwa kitu chochote bali ni ya kutupwa nje ili ikanyagwe-kanyagwe na watu. Ninyi ndio nuru ya ulimwengu. . . . Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:13-16) Kwa nini Yesu alisema wafuasi wake ni kama chumvi na nuru?

      Maneno ya Yesu yanadokeza kwamba wafuasi wake ni kama chumvi kwa wanadamu wote, bali si kwa kikundi fulani kidogo. Wao ni kama nuru, si kwa watu wachache, bali kwa watu wote wanaotaka kuona vizuri. Kwa kutumia maneno hayo ya mfano, Yesu alionyesha waziwazi kwamba hakutaka wafuasi wake wajitenge na jamii. Kwa nini?

      Fikiria mambo yafuatayo: Chumvi haiwezi kuhifadhi chakula ikiwa haitachanganywa na chakula chenyewe. Taa haiwezi kuangaza chumbani ikiwa haitawekwa ndani ya chumba hicho. Hivyo, ni rahisi kuelewa ni kwa nini Yesu hakuwaamuru wanafunzi wake wajitenge na kwenda katika sehemu fulani ya dunia ili kuanzisha jamii za waamini. Wala hakuwaambia wafuasi wake wajitenge na watu ulimwenguni na waishi katika mashirika ya kidini. Badala yake, kama vile chumvi inavyopaswa kugusa chakula na pia nuru inavyopaswa kuangaza gizani, ndivyo Wakristo wanavyopaswa kuwasaidia watu wengine kuboresha maisha yao.

      “Si Sehemu ya Ulimwengu”

      Hata hivyo, maagizo ya Yesu kwamba wafuasi wake wanapaswa kushirikiana na watu wengine yanatokeza swali muhimu kuhusu mtazamo wa Wakristo kuelekea siasa. Kwa nini? Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisali hivi kwa Mungu kwa ajili ya wafuasi wake: “Ninakuomba, si kwamba uwatoe ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Hivyo basi, Wakristo wanawezaje kutokuwa sehemu ya ulimwengu, na wakati uleule, wajihusishe na jamii yao? Ili kujua jambo hilo, acheni tuchunguze maswali mengine matatu:

      • Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu siasa?

      • Wakristo wanapaswa kufanya nini leo?

      • Mafundisho ya Kikristo yanasaidiaje jamii?

      [Blabu katika ukurasa wa 4]

      Yesu alionyesha waziwazi kwamba hakutaka wafuasi wake wajitenge na jamii

  • Yesu Alikuwa na Maoni Gani Kuhusu Siasa?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Yesu Alikuwa na Maoni Gani Kuhusu Siasa?

      WAANDIKAJI wa Vitabu vya Injili wanataja matukio kadhaa katika huduma ya Yesu ambayo yalifanya akabiliane moja kwa moja na siasa. Kwa mfano, muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa akiwa na umri wa miaka 30 hivi, Ibilisi alitaka kumpa cheo cha kuwa mtawala wa ulimwengu. Kisha, katika huduma yake, umati ulitaka kumfanya kuwa mfalme. Pia baadaye, watu walijaribu kumlazimisha kuwa mwanasiasa. Yesu alitendaje? Acha tuchunguze matukio hayo.

      Mtawala wa Ulimwengu. Vitabu vya Injili vinataja kwamba Ibilisi alitaka kumpa Yesu utawala juu ya “falme zote za ulimwengu.” Fikiria mambo ambayo Yesu angefanya ili kuwaondolea wanadamu mateso ikiwa angetumia mamlaka ya mtawala wa ulimwengu! Bila shaka, mtu anayeamini kwamba siasa ndiyo inayoweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu na anatamani kuyaondoa, hangekataa cheo kama hicho. Lakini Yesu alikataa.​—Mathayo 4:8-11.

      Mfalme. Watu wengi walioishi wakati wa Yesu walitamani sana kuwa na mtawala ambaye angeweza kutatua matatizo yao ya kiuchumi na kisiasa. Kwa sababu walipendezwa na uwezo wa Yesu, walitaka ajihusishe na siasa. Yesu alitendaje? Yohana, mwandikaji wa Injili anasema: “Yesu, akijua walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme, akaondoka tena kwenda mlimani akiwa peke yake.” (Yohana 6:10-15) Ni wazi kwamba Yesu alikataa kujihusisha na siasa.

      Mwanasiasa. Ona kilichotokea siku kadhaa kabla ya kifo cha Yesu. Wanafunzi wa Mafarisayo, ambao walitaka kupata uhuru kutoka kwa Milki ya Roma, wakishirikiana na Waherode ambao walikuwa wafuasi wa chama cha kisiasa kilichounga mkono Waroma, walienda kuzungumza na Yesu. Walitaka kumlazimisha aonyeshe msimamo wake kisiasa. Walimuuliza ikiwa Wayahudi walipaswa kulipa kodi kwa Waroma.

      Marko aliandika jibu hili la Yesu: “‘Kwa nini mnanijaribu? Nileteeni dinari niitazame.’ Wakaleta moja. Naye akawaambia: ‘Sanamu hii na mwandiko huu ni za nani?’ Wakamwambia: ‘Ni za Kaisari.’ Ndipo Yesu akasema: ‘Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.’” (Marko 12:13-17) Kitabu Church and State​—The Story of Two Kingdoms kinasema hivi kuhusu jibu la Yesu: “Alikataa kutenda kama masihi wa kisiasa na kwa busara akaweka mipaka kati ya Kaisari na Mungu.”

      Hata hivyo, Yesu alisikitishwa na matatizo yaliyowapata wanadamu kama vile umaskini, ufisadi, na ukosefu wa haki. Hata Biblia inaonyesha kwamba aliguswa sana na hali yenye kuhuzunisha ya watu waliomzunguka. (Marko 6:33, 34) Lakini Yesu hakuanzisha kampeni ya kuondoa ukosefu wa haki duniani, ingawa watu fulani walijaribu kumshawishi ajiingize katika siasa.

      Kama vile mifano hiyo inavyoonyesha, ni wazi kwamba Yesu alikataa kujihusisha na mambo ya kisiasa. Lakini vipi kuhusu Wakristo leo? Wanapaswa kufanya nini?

  • Wakristo Wanapaswa Kufanya Nini Leo?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Wakristo Wanapaswa Kufanya Nini Leo?

      WAKRISTO wa kweli leo hawashiriki katika siasa. Kwa nini? Kwa sababu wanaiga mfano wa Yesu. Alisema hivi kujihusu: “Mimi si sehemu ya ulimwengu.” Na akasema hivi kuwahusu wafuasi wake: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:14) Fikiria sababu kadhaa kwa nini Wakristo hawapaswi kujiingiza katika siasa.

      1. Wanadamu hawana uwezo kamili. Biblia inasema kwamba wanadamu hawana uwezo wala haki ya kujitawala. Nabii Yeremia aliandika: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”​—Yeremia 10:23.

      Kama vile ambavyo wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kupaa angani kwa nguvu zao wenyewe, vilevile hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kujitawala wenyewe kwa mafanikio. Akionyesha kwamba serikali hazina uwezo kamili, mwanahistoria David Fromkin alisema hivi: “Serikali hufanyizwa na wanadamu; hivyo basi mara nyingi hazifaulu na wakati wao ujao haujulikani. Zina nguvu kwa kiasi fulani, lakini si kikamili.” (The Question of Government) Ndiyo sababu Biblia inatuonya tusiwategemee wanadamu!​—Zaburi 146:3.

      2. Roho waovu wanaongoza wanadamu. Shetani alipotaka kumpa Yesu utawala wa dunia, Yesu hakusema kwamba Ibilisi hakuwa na mamlaka ya kumpa falme zote za ulimwengu. Baadaye, hata Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” Miaka kadhaa baadaye mtume Paulo alisema kwamba Shetani ni “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4) Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Roho waovu ndio wanaotawala ulimwengu ingawa watu wengi hawafahamu hivyo. Jambo hilo linapaswa kufanya tuwe na maoni gani kuhusu siasa?

      Fikiria ulinganisho huu: Kama vile mashua ndogo zinavyoweza kusukumwa na upepo wa baharini, ndivyo mifumo ya kisiasa ya wanadamu inavyoongozwa na nguvu za roho waovu. Na kama vile mabaharia katika mashua hizo wasivyoweza kubadili upepo huo wenye nguvu, ndivyo pia wanasiasa wasivyoweza kubadili nguvu za roho hao waovu. Roho hao waovu wameazimia kuwapotosha wanadamu kabisa na kusababisha ‘ole kwa dunia.’ (Ufunuo 12:12) Kwa hiyo, badiliko la kweli linaweza kuletwa tu na mtu mwenye nguvu kuliko Shetani na mashetani wake. Mtu huyo ni Yehova Mungu.​—Zaburi 83:18; Yeremia 10:7, 10.

      3. Wakristo wa kweli wanaunga mkono Ufalme wa Mungu peke yake. Yesu na wanafunzi wake walijua kwamba Mungu alikuwa amepanga wakati ambao atasimamisha serikali mbinguni itakayotawala dunia nzima. Biblia inasema serikali hiyo ni Ufalme wa Mungu na inafunua kwamba Yesu Kristo ndiye aliyechaguliwa kuwa Mfalme. (Ufunuo 11:15) Kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu kilikuwa “habari njema ya ufalme wa Mungu,” kwa sababu alijua kwamba Ufalme huo unawahusu wanadamu wote. (Luka 4:43) Pia, aliwafundisha wanafunzi wake kusali: “Ufalme wako na uje.” Kwa nini? Kwa sababu chini ya ufalme huo, bila shaka, mapenzi ya Mungu yatatimia mbinguni na duniani.​—Mathayo 6:9, 10.

      Hivyo basi, serikali za wanadamu zitapatwa na nini? Biblia inajibu kwamba serikali za “dunia nzima inayokaliwa,” zitaharibiwa. (Ufunuo 16:14; 19:19-21) Ikiwa kwa kweli mtu anaamini kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za wanadamu, basi itakuwa jambo la busara kutounga mkono mifumo ya kisiasa. Zaidi ya hayo, ikiwa mtu ataunga mkono serikali za wanadamu ambazo zitaharibiwa, basi atakuwa akimpinga Mungu.

      Kwa sababu Wakristo wa kweli hawashiriki katika siasa, je, hilo linamaanisha kwamba hawataki kabisa kujaribu kusaidia watu wengine wawe na maisha bora? Ona jibu linalotolewa katika makala inayofuata.

      [Blabu katika ukurasa wa 7]

      Mashahidi wa Yehova wanajishughulisha katika kuunga mkono Ufalme wa Mungu, wala si mabadiliko ya kisiasa

  • Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?

      MAKALA zilizotangulia zimeeleza kwa nini Wakristo wa kweli hawashiriki katika siasa. Hata hivyo, Wakristo wanaweza kuonyeshaje kwamba wanataka kuwasaidia watu katika jamii wawe na maisha bora? Njia moja ni kwa kutii amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”​—Mathayo 28:19, 20.

      Kutii amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi’ kunahusiana na kufuata mashauri yake ya kuwa kama chumvi na nuru kwa ulimwengu. (Mathayo 5:13, 14) Mambo hayo yanahusianaje? Na kazi hiyo inaweza kuwasaidiaje watu?

      Ujumbe wa Kristo Unaelimisha na Kulinda

      Chumvi hutumiwa kuhifadhi vitu visiharibike. Vivyo hivyo, ujumbe ambao Yesu aliwaamuru wafuasi wake wawapelekee watu wa mataifa yote unaweza kuwahifadhi. Watu wanaokubali na kuishi kulingana na mafundisho ya Yesu wanajilinda kutokana na maadili mapotovu ambayo yameenea sana leo. Hilo linawezekanaje? Wanajifunza jinsi ya kuepuka mazoea ambayo yanaweza kuwadhuru kiafya, kwa mfano kuvuta sigara, na wanasitawisha sifa kama vile upendo, amani, ustahimilivu, fadhili, na wema. (Wagalatia 5:22, 23) Sifa kama hizo zinafanya wawe watu wazuri katika jamii. Wakristo wanaoshiriki pamoja na jirani zao ujumbe huo wenye kuhifadhi, wanasaidia sana jamii zao.

      Vipi kuhusu mfano wa nuru? Kama vile tu mwezi unavyoangaza nuru kutoka kwenye jua, ndivyo wafuasi wa Kristo wanavyoangaza “nuru” kutoka kwa Yehova Mungu. Wanaangaza nuru hiyo kupitia ujumbe wenye kuelimisha wanaohubiri na pia kupitia matendo yao mazuri.​—1 Petro 2:12.

      Zaidi ya hayo, Yesu alieleza uhusiano uliopo kati ya kuwa nuru na kuwa mwanafunzi aliposema: “Watu huwasha taa na kuiweka, si chini ya kikapu cha kupimia, bali juu ya kinara cha taa, nayo huangazia watu wote waliomo ndani ya nyumba. Vivyo hivyo acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu.” Taa inayong’aa ambayo imewekwa juu ya kinara inaonekana na watu wote wanaoizunguka. Vilevile, kazi ya kuhubiri na matendo mengine mazuri ambayo Wakristo wa kweli wanatenda yanapaswa kuonekana waziwazi na watu wanaowazunguka. Kwa nini? Yesu alisema kwamba wale wanaoona matendo hayo mazuri watamtukuza Mungu bali si Wakristo.​—Mathayo 5:14-16.

      Daraka la Wakristo Wote

      Yesu aliposema, “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu” na “acheni nuru yenu iangaze,” alikuwa akiwaagiza wanafunzi wake wote. Amri ambayo Yesu alitoa haiwezi kutimizwa na watu wachache waliotawanyika katika dini mbalimbali. Badala yake, waamini wote ni “nuru.” Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi ambao wanaishi katika nchi zaidi ya 235, wanaamini kwamba wana jukumu la kuwatembelea jirani zao na kuwaeleza kuhusu ujumbe ambao Kristo anataka wafuasi wake watangaze.

      Kichwa kikuu cha ujumbe wa Mashahidi wa Yehova ni nini? Yesu alipotoa amri ya kuhubiri, hakuwaagiza wafuasi wake wahubiri kuhusu mabadiliko ya kijamii au kisiasa, muungano wa Kanisa na Serikali, au sera nyingine za wanadamu. Badala yake, alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hivyo, Wakristo wa kweli leo wanatii maagizo ya Yesu kwa kuendelea kuongea na jirani zao kuhusu Ufalme wa Mungu ambao ni serikali pekee iliyo na uwezo wa kukomesha mfumo mwovu wa Shetani na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu.

      Unaposoma masimulizi ya Injili, utaona mambo mawili makuu kuhusu huduma ya Yesu ambayo yanaongoza matendo ya Wakristo wa kweli leo. Mambo hayo mawili yanazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Jinsi ya Kuwa Mkristo Mnyoofu na Raia Mwema
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Jinsi ya Kuwa Mkristo Mnyoofu na Raia Mwema

      NI MAMBO gani mawili yanayojitokeza wazi katika huduma ya Yesu? Kwanza, Yesu alijitahidi kubadili mioyo ya watu, wala si mashirika ya kisiasa. Kwa mfano, ona jambo ambalo Yesu alikazia katika Mahubiri yake ya Mlimani. Kabla tu ya kuongea kuhusu umuhimu wa kuwa kama chumvi na nuru, aliwaambia wasikilizaji wake kwamba watu wenye furaha ya kweli ni wale “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” Kisha akaongezea: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, . . . walio safi moyoni, . . . wanaofanya amani.” (Mathayo 5:1-11) Yesu aliwasaidia wafuasi wake waone umuhimu wa kubadili maoni na hisia zao kuelekea viwango vya Mungu vinavyohusu mema na mabaya na umuhimu wa kumtumikia Mungu kwa moyo wote.

      Pili, Yesu alipowaona wanadamu wakiteseka, huruma ilimchochea kuwapunguzia mateso yao. Hata hivyo, hakufanya lengo lake kuu liwe kuondoa mateso yote. (Mathayo 20:30-34) Aliponya wagonjwa, lakini hakuondoa magonjwa. (Luka 6:17-19) Alileta kitulizo kwa watu waliokuwa wakikandamizwa, lakini bado ukosefu wa haki uliendelea kuwepo. Aliwalisha watu waliokuwa na njaa, lakini bado wanadamu waliendelea kukumbwa na janga la njaa.​—Marko 6:41-44.

      Kuwachochea Watu Wabadili Maisha Yao na Kupunguza Mateso

      Kwa nini Yesu alikazia fikira kubadili mioyo ya watu na kupunguza mateso lakini si kubadili mashirika au kuondoa kuteseka? Yesu alijua kwamba Mungu amepanga kutumia Ufalme Wake wakati ujao ili kukomesha serikali zote za wanadamu na kuondoa mambo yanayosababisha kuteseka. (Luka 4:43; 8:1) Ndiyo sababu, wakati fulani wanafunzi walipomhimiza Yesu aendelee kuponya wagonjwa, aliwaambia hivi: “Twendeni mahali pengine, katika miji ya vijiji iliyo karibu, ili nipate kuhubiri huko pia, kwa maana nilitoka kwa kusudi hilo.” (Marko 1:32-38) Yesu alipunguza mateso yaliyokuwa yanawapata watu wengi, lakini alitanguliza kuhubiri na kufundisha neno la Mungu.

      Leo, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kumwiga Yesu wanapofanya kazi yao ya kuhubiri. Wanachochewa kupunguza mateso yanayowapata watu kwa kuwapa msaada wanaohitaji. Lakini Mashahidi hawajitahidi kuondoa ukosefu wa haki ulio duniani. Wanaamini kwamba Ufalme wa Mungu utaondoa mambo yanayosababisha kuteseka. (Mathayo 6:10) Kama Yesu, wanajitahidi kubadili mioyo ya watu bali si mashirika ya kisiasa. Mtazamo huo ni mzuri kwa sababu matatizo makuu ya mwanadamu, si ya kisiasa, bali ni ya kiadili.

      Raia Wema

      Wakati uleule, Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba wakiwa Wakristo wana wajibu wa kuwa raia wema. Hivyo, wanaheshimu na kutii mamlaka za kiserikali. Kupitia machapisho yao na kazi yao ya kuhubiri, wanawatia moyo jirani zao watii sheria. Hata hivyo, serikali inapotaka wafanye jambo linalopingana moja kwa moja na sheria za Mungu, Mashahidi hawakubali. ‘Wanamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’​—Matendo 5:29; Waroma 13:1-7.

      Mashahidi wa Yehova wanawatembelea watu wote katika jamii zao na kuwafundisha Biblia bila malipo. Kupitia mafundisho hayo, mamilioni ya watu wamebadili mioyo yao. Kila mwaka, watu wengi wanasaidiwa kuacha mazoea yenye kudhuru kama vile kuvuta sigara, ulevi, kutumia dawa za kulevya, kucheza kamari, na maadili mapotovu kingono. Wamekuwa raia wenye maadili safi na wanaowajibika kwa sababu wamejifunza kuishi kulingana na kanuni za Biblia.—Ona makala yenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha,” kwenye ukurasa wa 18 wa gazeti hili.

      Zaidi ya hayo, elimu ya Biblia inasaidia watu wa familia waheshimiane hata zaidi na kuboresha mawasiliano kati yao, yaani, kati ya wenzi wa ndoa, vilevile kati ya wazazi na watoto, na hata kati ya watoto wenyewe. Hayo ni mambo yanayoboresha uhusiano katika familia. Familia zilizo na uhusiano mzuri zinafanyiza jamii zenye uhusiano mzuri.

      Baada ya kuchunguza mambo yaliyozungumziwa katika makala hizi, una maoni gani: Je, Biblia inakubali dini ijihusishe na siasa? Jibu ni wazi; haikubali. Lakini, je, Wakristo wa kweli wanapaswa kuwa raia wema? Ndiyo wanapaswa. Wanawezaje kufanya hivyo? Ni kwa kufuata amri ya Yesu ya kuwa kama chumvi na nuru katika ulimwengu.

      Wale wanaojitahidi kutumia maagizo ya Kristo wanafaidika wao wenyewe na hata familia zao na vilevile jamii zao. Mashahidi wa Yehova walio katika eneo unaloishi watafurahi kukueleza mambo mengi zaidi kuhusu programu ya elimu ya Biblia ambayo inaendelea katika jamii yako.a

      [Maelezo ya Chini]

      a Ikiwa unataka unaweza kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova kupitia Tovuti ya www.watchtower.org

      [Blabu katika ukurasa wa 10]

      Yesu alijitahidi kubadili mioyo ya watu, wala si mashirika ya kisiasa

      [Blabu katika ukurasa wa 11]

      Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba wana wajibu wa kuwa raia wema

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki