Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Wewe Huizungumzia Dini?
    Amkeni!—1999 | Februari 22
    • Je, Wewe Huizungumzia Dini?

      “Tafadhali, acha tubadilishe mazungumzo. Kunayo mambo mawili ambayo siyazungumzii kamwe—dini na siasa!”

      “Mimi humwachia mke wangu na watoto wangu dini.”

      “Sitaki kuizungumzia dini sasa. Nimetoka tu kanisani.”

      JE, WEWE husikia maelezo kama hayo kwa ukawaida? Watu fulani hawapendelei kuizungumzia dini kwa sababu wanaiona kuwa jambo la kibinafsi, yaani kati yao na Mungu. Yesu alisema hivi: “Usalipo ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye katika siri; ndipo Baba yako atazamaye katika siri atakurudishia wewe.”—Mathayo 6:6.

      Kwa upande mwingine, Yesu na wanafunzi wake hawakuona kwamba kila jambo linalohusu dini lapaswa kuwa la kibinafsi. Waliongea kwa uhuru na kusema waziwazi juu ya masuala mengi ya kiroho, na tokeo likawa kwamba mafundisho yao yalienezwa ulimwenguni pote. (Matendo 1:8; Wakolosai 1:23) Bila shaka, si kila mtu aliyetaka kuzungumza nao, na baadhi ya watu waliozungumza nao waliendelea kutilia shaka.

      Leo pia, mtazamo wa watu mmoja-mmoja na tamaduni mbalimbali kuelekea kuizungumzia dini hutofautiana. Kwa mfano, katika nchi nyingi za Magharibi, watu wana mwelekeo wa kuhangaikia sana mambo ya kilimwengu—elimu, kazi ya kuajiriwa, michezo, televisheni, kompyuta, na kadhalika. Katika tamaduni nyinginezo, watu wako tayari kuzungumzia imani zao. Na bado, bila kujali hali za watu, kuna mambo fulani yanayotukia katika maisha yao ambayo huwafanya baadhi ya watu ambao hapo mwanzoni hawakupendezwa na dini wachunguze upya uhitaji wao wa kiroho.

      Kutovumiliana Huwavunja Wengi moyo

      Wale wanaokataa kuizungumzia dini huenda waliona au kuhusika katika mazungumzo yaliyotokeza hasira kali na kugeuka kuwa mabishano makali. “Tofauti za kidini hutokeza ugomvi mwingi zaidi kuliko tofauti za kisiasa,” akasema mhutubu mmoja mwenye kujulikana sana. Pia, Richard M. Johnson, aliyekuwa makamu wa rais wa Marekani, alionelea hivi: “Ushupavu wa kidini hutokeza chuki mbaya sana isiyo na sababu katika akili ya mwanadamu; na, unapokuwa umepotoka, ushupavu huo huamsha hisia kali, zilizo mbaya sana za asili yetu huku kukiwa na kisingizio cha kwamba tunamtumikia Mungu.”

      Je, haikushangazi kwamba mafundisho ya Biblia, ambayo yana uwezo wa kuadilisha na kukuza hadhi, yanatumiwa vibaya ili kuendeleza kutovumiliana, kung’ang’ania imani, na chuki? Kwa kweli, si mafundisho ya Biblia yanayowafanya wengi waikatae dini. Badala yake, ni kule kuyapotosha. Kwa mfano, fikiria Ukristo.

      Kupitia neno na kielelezo, Mwanzilishi wa Ukristo, Yesu Kristo, alitia moyo kupenda Mungu na kupenda jirani, wala si kutovumiliana na ushupavu. Kristo na wafuasi wake walitumia mbinu za kusababu na kushawishi katika huduma yao. (Mathayo 22:41-46; Matendo 17:2; 19:8) Nao waliwaombea maadui na wanyanyasi wao.— Mathayo 5:44; Matendo 7:59, 60.

      Kupitia neno na kielelezo, Mwanzilishi wa Ukristo, Yesu Kristo, alitia moyo kupenda Mungu na kupenda jirani, wala si kutovumiliana na ushupavu. Kristo na wafuasi wake walitumia mbinu za kusababu na kushawishi katika huduma yao. (Mathayo 22:41-46; Matendo 17:2; 19:8) Nao waliwaombea maadui na wanyanyasi wao.—Mathayo 5:44; Matendo 7:59, 60.

      Dini ya kweli huelimisha akili na moyo, na huwaunganisha watu. Kwa hiyo, kama tutakavyoona, mazungumzo yenye heshima yanayohusu dini yaweza kuleta matokeo mazuri sana kwa wale wanaotafuta kweli kwa moyo mweupe.

      [Sanduku katika ukurasa wa 3]

      Yale Ambayo Watu Mashuhuri Wamesema

      “Ikiwa Yesu ndiye njia iongozayo kwa Mungu, ni lazima wafuasi wa Yesu washiriki na wengine habari hiyo.”—Ben Johnson, profesa wa somo la kueneza evanjeli katika Seminari ya Theolojia ya Co­lum­bia.

      “Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kuwapelekea watu gospeli. Hilo Agizo Kuu latuamuru kwenda katika ulimwengu wote. Bwana aliwaamuru wafuasi wake waende kotekote.”—Kenneth S. Hemphill, mkurugenzi wa Southern Baptist Center for Church Growth.

      “Isipokuwa tuwe mashahidi, hatuwezi kuwa Wakristo halisi. . . . Kila Mkristo anahitajiwa awe mishonari na shahidi.”—Papa John Paul wa Pili.

      Wahubiri wengi sana . . . wanapendezwa zaidi kujenga makutaniko makubwa na miradi ya ujenzi wa makanisa na mgawo wao wa uchungaji unaofuata kuliko vile wanavyopendezwa kuhubiri ujumbe usioridhiana na usiopendeza ulio katika Gospeli.”—Cal Thomas, mtungaji na mwandishi wa safu za gazeti.

      “Ni lazima tubishe milango . . . Kama wafanyavyo Mashahidi (wa Yehova) na baadhi ya watu wengine, ni lazima twende na kutangaza Gospeli ya Yesu Kristo.”—Thomas V. Daily, askofu Mkatoliki.

  • Kwa Nini Izungumziwe
    Amkeni!—1999 | Februari 22
    • Kwa Nini Izungumziwe

      “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.”—Mithali 27:17, Biblia.

      MABAPA hayanolewi kwa kugonganishwa. Kunoa ni utaratibu mwanana. Vivyo hivyo, kunazo njia nzuri na mbaya za kunoa akili kupitia mazungumzo, hasa yanapohusu masuala yanayohitaji utumie busara kama vile dini.

      Kwanza kabisa, ni lazima tuheshimu hadhi ya mtu tunayezungumza naye na tuonyeshe heshima hiyo kwa maneno na kwa mwenendo wetu. “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi,” Biblia yasema. (Wakolosai 4:6) Usemi unaotolewa kwa upendezi na uliokolezwa haulazimishi kwa namna yake ya sauti, hata wakati ambapo msemaji amesadiki kwamba yeye yuko sahihi na mwenzake amekosea.

      Jinsi tunavyosikiliza hudhihirisha upendezi wetu pia. Ikiwa twakatisha mazungumzo au hatusikilizi kwa makini kwa sababu tunatayarisha bishano linalofuata, haiwezekani kuwa tunasikiliza kwa upendezi. Kuna uwezekano mkubwa kwamba yule anayesema atatambua hali yetu iliyo wazi ya kutopendezwa na maoni yake na labda atakatisha mazungumzo. Tena, tusimlazimishe au kumwogopesha kamwe mtu ili abadili maoni yake. Hii ni kwa sababu ‘Mungu ndiye huikuza mbegu ya ile kweli’ katika moyo wa msikilizaji mwenye kuitikia kwa njia nzuri.—1 Wakorintho 3:6.

      Mtume Paulo ni kielelezo kizuri kwetu, kwa kuwa alitumia “kutoa sababu” na “ushawishi” katika huduma yake. (Matendo 17:17; 28:23, 24) Paulo aliizungumzia dini pamoja na watu popote alipowapata, kama vile mahali pa soko na katika nyumba zao. (Matendo 17:2, 3; 20:20) Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuiga mfano huo kwa kwenda popote ambapo huenda pana watu na kusababu nao kwa kutumia Maandiko.

      Epuka Kutoelewana

      Taifa la Israeli lilikuwa tu limetulia katika Bara Lililoahidiwa punde tu kulipotokea hali fulani ya kutoelewana iliyohusu madhabahu, ambayo ilikaribia kusababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe. Watu walioishi mashariki ya Mto Yordani walijenga madhabahu, ingawa yale makabila mengine yalifikiri kimakosa kwamba ilikuwa madhabahu ya ibada isiyo ya kweli. Kwa hiyo, wakapanga kuchukua hatua ya kijeshi wapate kuwaadhibu ndugu zao. Lakini wakatumia busara. Wale waliopanga kuchukua hatua ya uchokozi walituma ujumbe kwanza ili kuulizia kusudi la madhabahu hiyo. Waliambiwa kwamba hiyo ilikuwa tu nguzo ya ukumbusho—“ushahidi”—kuyakumbusha makabila yote juu ya umoja wao mbele za Yehova Mungu, na hilo likatokeza kitulizo kwao. Mazungumzo yalizuia vita—na uhai wa wengi ukaokolewa!—Yoshua 22:9-34.

      Vivyo hivyo leo, hali za kutoelewana mara nyingi hutokeza uadui na hata chuki isiyo na sababu. Kwa mfano, watu fulani wamewaona Mashahidi wa Yehova kuwa ni washupavu wa kidini kwa sababu ya ripoti zinazohusu msimamo wao wa kukataa kutiwa damu mishipani. Lakini wale ambao wamechukua hatua ya kibinafsi ya kuulizia kutoka kwa Mashahidi kuhusu suala hilo mara nyingi wamefurahia kujua kwamba kunao msingi wa Kibiblia wa kuunga mkono msimamo wao na kwamba kuna matibabu ya badala yaliyo salama, na yenye matokeo mazuri. (Mambo ya Walawi 17:13, 14; Matendo 15:28, 29) Kwa kweli, mwandishi mmoja wa safu za gazeti alisema hivi, kuhusu matatizo ya kutiwa damu mishipani: “Mungu asifiwe kwa sababu Mashahidi wa Yehova wanaongoza katika utafiti wa vibadala vya kutumia damu katika tiba.”

      Hali kadhalika, baadhi ya watu wamekataa kuongea na Mashahidi kwa sababu wameambiwa kwamba Mashahidi wa Yehova hawamwamini Yesu Kristo. Jambo hilo si la kweli hata kidogo! Kwa kweli, Mashahidi hukazia daraka la Yesu katika wokovu wetu, wakieleza kwamba yeye ni Mwana wa Mungu, ambaye Mungu alimtuma duniani ili kufidi wanadamu kutoka kwenye dhambi na kifo. Watu wanaposema na Mashahidi kuhusu suala hilo, kutoelewana kunaondolewa.—Mathayo 16:16; 20:28; Yohana 3:16; 14:28; 1 Yohana 4:15.

      Kweli—Inapendwa na Wengi au Haipendwi na Wengi?

      Labda jambo linalowashangaza wengi ni kwamba inapohusu dini, mara nyingi njia inayopendwa na wengi kwa kawaida ndiyo njia yenye kosa. Yesu Kristo mwenyewe alifundisha hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.

      Ni watu wanane tu waliosema kweli ya kiroho katika siku ya Noa—Noa, mke wake, wana wake watatu, na wake za wanaye. Yaonekana ujumbe wao wa kutoa onyo na kazi ya kujenga safina viliwafanya wawe vitu vya kudhihakiwa, na hata kutendwa vibaya. Na bado Noa na familia yake hawakuogopeshwa; waliendelea kuhubiri na kujenga. (Mwanzo 6:13, 14; 7:21-24; 2 Petro 2:5) Vivyo hivyo, ni watu watatu tu waliotii maagizo ya Mungu na hivyo wakaokoka kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora.—Mwanzo 19:12-29; Luka 17:28-30.

      Vipi wakati wetu? Mwenye nyumba mmoja aliwaambia Mashahidi wa Yehova hivi: “Ikiwa Kristo angerudi katika mwili wenye nyama leo, yaelekea watu wangemwua tena.” Mtu huyu alionelea kwamba mafundisho na viwango vya juu vya adili vya Yesu havingependwa na wengi leo kama vile havikupendwa na wengi miaka 2000 iliyopita. Je, unakubaliana na hilo?

      Ikiwa wajibu ndiyo, uko sahihi, kwa kuwa Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Mtakuwa vitu vya kuchukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu”—utabiri ambao umethibitika kuwa kweli. (Mathayo 24:9) Viongozi wa Kiyahudi mjini Roma walimwambia mtume Paulo hivi kuhusu Ukristo: “Kwa habari ya farakano hili . . . kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Hata hivyo, wafuasi wa Kristo hawakuacha kuwaeleza wengine imani zao kwa sababu Ukristo haukupendwa na wengi. Wala hilo halikuwazuia watu wenye mioyo minyofu wasiongee na Wakristo.—Matendo 13:43-49.

      Leo ujumbe wa Yesu una umuhimu kuliko wakati mwingine wowote. Kwa nini? Kwa sababu hali za ulimwengu zaonyesha kwamba sasa tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu na kwamba mwisho wa siku hizi utakuwa kuondolewa kwa utendaji wa makosa kutoka kwenye dunia. Yesu aliulinganisha wakati wetu na siku za Noa. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:37-39) Sasa, huu sio wakati wa kuzishikilia imani zetu bila kuzichunguza, kwa kuwa ni wale tu wanaomjua Mungu na ‘wanaomwabudu kwa roho na kweli’ watakaopewa uhai wa milele.—Yohana 4:24; 2 Wathesalonike 1:6-9.

      Jinsi ya Kupata Njia ya Kweli

      Francis Bacon, ambaye alikuwa mwanafalsafa Mwingereza, mwandishi wa insha, mwana-sheria, na mtawala mwenye busara wa karne ya 17, aliwashauri wenye kutafuta kweli “wafikirie kwa makini na kutafakari.” Naye rais wa zamani wa Marekani, Thomas Jefferson, alisema hivi: “Kusababu na kuulizia waziwazi ndivyo vyombo pekee vyenye matokeo vinavyoshinda kosa. . . . [Vyombo] hivyo ndivyo maadui wa kosa.” Kwa hiyo ikiwa sisi tunatafuta kweli kwa moyo mweupe, “tutafikiria kwa makini na kutafakari” na tufuatilie “kusababu na kuulizia waziwazi.”

      Akifafanua umuhimu wa mfikio huo, mwanasayansi Mwingereza Sir Hermann Bondi alisema: “Kwa kuwa ni imani moja tu inayoweza kuwa ya kweli, tokeo ni kwamba kuna uwezekano mkubwa sana wa binadamu kuwa na imani yenye uthabiti na unyofu katika kitu kisicho cha kweli kwa mambo yahusuyo dini iliyofunuliwa. Mtu angetarajia kwamba uhakika huu ulio wazi ungewafanya watu wawe wanyenyekevu kwa kiasi fulani, wawe na fikira ya kwamba hata ingawa huenda mtu akawa na imani yenye nguvu, yawezekana amekosea.”

      Basi, mtu aweza kutambuaje ikiwa kwa kweli yupo kwenye ‘barabara inayoongoza kwenye uhai’? Yesu alifundisha kwamba ni lazima Mungu aabudiwe ‘kwa kweli.’ Hivyo, kufikiri kuzuri kunamfanya mtu aamue kwamba ikiwa mafundisho mawili yanapingana, yote mawili hayawezi kuwa kweli. Kwa mfano, ama wanadamu wana nafsi isiyokufa ama hawana. Ama Mungu ataingilia kati shughuli za binadamu ama hataingilia. Ama Mungu ni Utatu ama si Utatu. Watu wanaotafuta kweli wanataka majibu yenye uhakika kuhusu maswali haya muhimu. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Mungu ametupa majibu katika Neno lake, Biblia.a

      Kwa kuwa “Andiko lote limepuliziwa na Mungu,” njia kuu ya kuyapima mafundisho mbalimbali ni kwa kuyalinganisha na Biblia. (2 Timotheo 3:16) Ukifanya hivyo, ‘utajithibitishia mwenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Waroma 12:2) Je, unaweza ‘kujithibitishia mwenyewe’ kwamba Biblia ndiyo msingi wa imani yako? Ni jambo la muhimu ufanye hivyo kwa sababu Mungu hataki uongozwe vibaya pamoja na “dunia nzima inayokaliwa.”—Ufunuo 12:9.

      Je, Walimu Wanahitajiwa?

      Yesu hakuwapa wanafunzi wake hati-kunjo chache na kuwaambia: “Majibu ya maswali yenu yamo humo. Nendeni nyumbani mkajitafutie wenyewe.” Badala yake, aliwafunza neno la Mungu kwa saburi na kwa fadhili. Halafu, wale waliokubali mafundisho yake waliwafunza wengine zaidi kwa kufuata mbinu zake. Fikiria mfano wa mwanafunzi Filipo. Alizungumza na ofisa mmoja Mwethiopia mwenye moyo mnyofu, ambaye hapo mapema alikuwa ameyafahamu Maandiko kupitia uhusiano wake na Wayahudi. Lakini mwanamume huyo alihitaji msaada. Hivyo Filipo—mwakilishi wa kutaniko la Kikristo—alielekezwa ili amsaidie. Ikiwa ofisa huyu angekataa kuizungumzia dini, hangejifunza juu ya daraka la Yesu katika kusudi la Mungu. Huyu Mwethiopia aliweka kielelezo kizuri kama nini kwa wote wanaotafuta kweli!—Matendo 8:26-39.

      Je, wewe uko tayari kuzizungumzia imani zako na kuuliza maswali kama huyu Mwethiopia alivyofanya? Kwa hakika unaweza kupata faida nyingi ukifanya hivyo. Mashahidi wa Yehova hufurahia kuizungumzia Biblia pamoja na watu wanaotaka kikweli kujua yale ambayo Biblia inasema. Mashahidi hawatoi maoni yao wenyewe. Bali, wao hujitahidi kuwaonyesha watu yale ambayo Biblia yenyewe husema.

      Huyo ofisa Mwethiopia alijifunza mambo fulani yenye kutokeza kuhusu Yesu Kristo, kama vile ambavyo angetumiwa na Mungu kuhusiana na wokovu wetu. Leo, utimizo wa kusudi la Mungu unakaribia sana kukamilika. Mambo ya ajabu, yenye kutia hofu yako karibu kutukia papa hapa duniani. Makala inayofuata itaonyesha kwamba kila mtu duniani ataathiriwa. Bila shaka, mtazamo na mwendo tunaofuata vitaamua jinsi tutakavyoathiriwa.

  • Tumaini Linalotolewa na Dini ya Kweli
    Amkeni!—1999 | Februari 22
    • Tumaini Linalotolewa na Dini ya Kweli

      KWA asili sisi hupenda kusema juu ya mambo yanayotuhangaisha au yanayosisimua hisia zetu. Hii ni sababu moja inayowafanya Mashahidi wa Yehova wafurahie kushiriki na wengine ujumbe mzuri ajabu wa Biblia. Ujumbe huo, unaokazia Ufalme wa Mungu, unatoa majibu kwa mambo yanayowahangaisha watu kikweli leo, kama vile wakati ujao, usalama, afya, na furaha.—Luka 4:43.

      Lakini kwanza, Ufalme wa Mungu ni nini?

      Tumaini Lenye Kusisimua

      Ufalme wa Mungu ni serikali ya Mungu, na Mwana wake, “Mfalme wa amani,” ndiye mtawala. Biblia yasema hivi kumhusu: “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake . . . Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.”—Isaya 9:6, 7.

      Unabii mwingine wa Biblia, ukitabiri mambo ambayo yangetokea baadaye kabisa, naam, wakati wa historia yetu wenyewe na watawala wake, ulisema hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

      Huu Ufalme wa Mungu, unaotawaliwa na Kristo, Mfalme wa Amani, utatimiza ile sala ambayo Yesu aliwafunza wafuasi wake kusali, yaani: “Baba yetu uliye katika mbingu . . . , acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:9, 10) Itakuwaje kwetu na kwa dunia Ufalme wa Mungu utakapokuja? Fikiria ahadi zilizotolewa na Yehova Mungu mwenyewe, kama zilivyorekodiwa katika Biblia. Baadhi ya ahadi hizo zimeonyeshwa katika kurasa hizi.

      Ujumbe Kutoka kwa Mungu

      Ahadi nzuri ajabu zinazopatikana katika Neno la Mungu hazipasi kufichwa, na jambo hili laturudisha kwenye lile suala la kuizungumzia dini. Yesu alitabiri kwamba kabla ya mwisho wa mfumo wa mambo uliopo, wafuasi wake wangechukua hatua ya kwanza ya kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 1:8.

      Ujumbe huu unaohusu Ufalme wa Mungu ndio ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova wanatangaza ulimwenguni kote. Gazeti jenzi, Mnara wa Mlinzi, sasa linachapishwa katika lugha 130, na juu ya jalada la kila moja ya nakala zaidi ya milioni 22 za kila toleo zinazochapishwa kuna maneno “Unaotangaza Ufalme wa Yehova.”

      Ikiwa wewe ni mtu mwenye hekima, unahitaji kufanya maamuzi yanayotegemea ujuzi kuhusu uhai wako. (Mithali 18:13) Basi, twakutolea mwaliko wa kujifunza mengi yanayohusu Ufalme wa Mungu wenye utukufu na yale ambayo unaweza kumaanisha kwako. Ili uyafahamu hayo, usikatae kuizungumzia Biblia. Hakuna mazungumzo yoyote yanayoweza kuelimisha, kupendeza, na kuwa yenye umuhimu kuliko yale ya Biblia.—Yohana 17:3.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki