-
Je, Dini Inachochea Amani?Amkeni!—2011 | Januari
-
-
Je, Dini Inachochea Amani?
KANISA la Kaburi Takatifu huko Yerusalemu ambalo linasemwa kuwa ndilo kanisa takatifu zaidi la dini zinazodai kuwa za Kikristo, linahusianishwa na mizozo na chuki nyingi ya kidini. Inasemekana kwamba kanisa hilo lilijengwa “mahali ambapo Kristo alizikwa na kufufuliwa.” Hata hivyo, vita vingi vikatili vimepiganwa mahali hapo panapoonwa kuwa patakatifu. Watawa na makasisi kutoka dini sita za “Kikristo” wamekuwa na ugomvi kuhusu ni nani atakayelitumia kanisa hilo na wakati gani. Chuki hiyo imeongezeka katika miaka ya hivi karibuni. Imebidi polisi wa kuzuia fujo wenye bunduki waingilie kati na kulidhibiti kanisa hilo kwa muda.
Historia Yenye Jeuri
Matukio katika Kanisa la Kaburi Takatifu ni sehemu ya historia ndefu ya umwagaji wa damu na mauaji makubwa yanayohusianishwa na ushupavu wa kidini. Kitabu Violence in God’s Name kinasema hivi baada ya kuchunguza mapigano ya hivi karibuni katika sehemu mbalimbali duniani: “Kutoka Indonesia hadi Ireland Kaskazini, Mashariki ya Kati hadi Kashmir, India hadi Nigeria, nchi za Balkani hadi Sri Lanka, Wakristo, Wabudha, Wayahudi, Wahindu, Waislamu na Makalasinga wanajitetea kwamba wanatumia jeuri ili kulinda dini zao na masilahi yao.”
Hata hivyo, amani na upatano ni kati ya mafundisho makuu ya dini nyingi. Kwa miaka mingi, kanuni za kuwajali wengine kama vile kumpenda jirani na utakatifu wa uhai wa mwanadamu zimeendelezwa sana na dini. Kwa hiyo, je, dini hazipaswi kuwa mstari wa mbele kuwachochea watu wawe wenye amani? Waabudu wenye mioyo minyoofu wanapaswa kuchunguza swali hilo.
-
-
Kwa Nini Dini Haijawaunganisha Wanadamu?Amkeni!—2011 | Januari
-
-
Kwa Nini Dini Haijawaunganisha Wanadamu?
IKIWA tungesema kwamba dini ndiyo chanzo cha mizozo yote ingemaanisha kwamba iwapo hakungekuwa na dini hakungekuwa na vita vingi. Je, wazo hilo linapatana na akili? Je, tunaweza kumaliza vita kwa kuondoa dini zote? Vyovyote vile utakavyojibu, jambo moja ni hakika: Dini haijawaunganisha wanadamu. Fikiria sababu fulani kwa nini hilo ni kweli.
Kugawanywa na Dini
Wanadamu wamegawanywa na dini, kwa kuwa dini nyingi kuu zimekuwa na chuki ya muda mrefu. Je, kuna sababu ya kuamini kwamba Wabudha, Wahindu, Waislamu, Wakristo, na Wayahudi watawahi kuishi pamoja kwa amani?
Jambo lingine lenye kusikitisha ni kwamba dini hizo kuu zimegawanyika katika vikundi vidogo-vidogo. Kwa mfano, kulingana na kadirio moja, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimegawanyika katika vikundi zaidi ya 30,000. Dini ya Kiislamu pia imegawanywa na mafundisho yanayopingana. Kulingana na shirika moja la habari la Mashariki ya Kati, msomi Mwislamu, Mohsen Hojjat hivi majuzi alikiri kwamba “ukosefu wa umoja kati ya Waislamu ndio unaosababisha matatizo yanayowakabili Waislamu kwa ujumla.” Dini nyingine maarufu kama zile za Wabudha, Wahindu, na Wayahudi zimegawanyika katika madhehebu mengi yanayopingana.
Dini Imejiingiza Katika Siasa
Inaonekana kwamba dini ina uvutano katika karibu kila sehemu ya maisha. Gazeti la habari The Economist linasema kwamba “watu wa kidini wanaeleza waziwazi imani yao katika nyanja zote kutia ndani nyanja ya biashara. Dini pia inaathiri maamuzi ya watu hata katika mambo ya kifedha.” Jambo hilo limewagawanya watu badala ya kuwaunganisha. Lakini uvutano mkubwa zaidi unaoleta madhara unahusiana na historia ndefu ya dini kujiingiza katika siasa.
Katika ripoti ya hivi majuzi iliyotajwa katika habari iliyotangulia, kikundi cha wanahistoria kilisema kwamba “yaelekea dini inaweza kusababisha vita ikiwa dini na serikali zitashirikiana kwa ukaribu au kuungana.” Ukweli wa mambo ni: Dini imekuwa ikijiingiza, na hata sasa bado inajiingiza, katika mashirika ya kisiasa na kijeshi.
Mchanganyiko Unaoweza Kutokeza Madhara
Katika nchi nyingi, dini kubwa zimekuwa njia ya kutambulisha uzalendo au rangi ya mtu. Kwa sababu hiyo, si rahisi kutofautisha chuki ya kitaifa, ubaguzi wa rangi, mizozo ya kikabila, na chuki ya kidini. Mchanganyiko huo unaweza kuharibu kabisa mambo ya ulimwengu huu.
Jambo lenye kupingana ni kwamba dini nyingi hudai kumwakilisha yule Mungu wa Biblia, Muumba. Je, inapatana na akili kwamba Muumba mweza-yote, mwenye hekima yote, na mwenye upendo anaweza kujihusisha kwa njia yoyote na dini zenye kutokeza mgawanyiko na umwagaji wa damu?
[Picha katika ukurasa wa 6]
Maelfu ya Mashahidi wa Yehova wamefungwa kwa sababu ya kuchagua kutounga mkono upande wowote wa kisiasa
-
-
Je, Dini Itawahi Kuleta Amani?Amkeni!—2011 | Januari
-
-
Je, Dini Itawahi Kuleta Amani?
“NA TUFANYE ulimwengu uwe mahali bora. Na tuondoe dini.” Hivyo ndivyo mwanafalsafa Mholanzi, Floris van den Berg, alivyopendekeza katika hotuba yake iliyochapishwa yenye kichwa “Jinsi ya Kuondoa Dini, na kwa Nini.” Ulimwenguni pote, wataalamu katika taaluma mbalimbali wanapendekeza kuondolewa kwa dini.
Mshindi wa Tuzo la Nobeli ambaye pia ni mwanafizikia, Steven Weinberg anasema hivi: “Ulimwengu unahitaji kuamshwa kutoka kwa jinamizi la mafundisho ya kidini.” Wazo la kwamba maovu yanayotendeka ulimwenguni leo yangepungua sana ikiwa dini ingeondolewa limerudiwa mara nyingi katika miaka ya hivi karibuni. Vitabu vinavyopinga dini vimechapishwa kwa wingi na vinapendwa sana.
Wanasayansi maarufu wamekusanyika ili kuzungumzia kile walichosema kuwa uhitaji wa haraka wa kuondolea mbali dini. Kikundi kipya cha watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu kinaeleza waziwazi chuki yao kuhusu dini kupitia vyombo vya habari. Je, sisi sote tunapaswa kufuata maoni hayo ya watu hao wenye kuheshimika?
Je, Kuna Dini ya Kweli?
Ikiwa dini zote zingekuwa za uwongo na hakuna Mungu, basi huenda lingekuwa jambo lenye kupatana na akili kuondoa dini. Lakini, namna gani ikiwa kuna Mungu? Namna gani ikiwa kuna kikundi cha watu duniani kinachomwakilisha Mungu kwa njia inayofaa, yaani, watu wanaofuata dini ya kweli?
Uchunguzi wa historia ya dini unaonyesha kwamba kuna dini moja inayotofautiana kabisa na dini nyingine zote. Ni dini inayofuatwa na watu wachache sana leo. Dini hiyo ilianzishwa na Yesu Kristo na mitume wake. Lakini kwa karne nyingi, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazijajipatanisha na viwango vya dini hiyo.
Kuna tofauti gani kati ya dini zinazodai kuwa za Kikristo na dini iliyoanzishwa na Yesu Kristo? Kuna tofauti nyingi. Hebu tuchunguze tofauti moja.
“Si Sehemu ya Ulimwengu”
Wakristo wa karne ya kwanza hawakujiingiza katika masuala ya kisiasa. Hilo linapatana na msimamo ambao Yesu mwenyewe alichukua. Biblia inasema kwamba katika pindi mbili hivi, Yesu alikataa katakata kuwa kiongozi wa kisiasa. (Mathayo 4:8-10; Yohana 6:15) Yesu hata aliwakemea wanafunzi wake walipotaka kutumia jeuri ili wazuie asikamatwe.—Mathayo 26:51, 52; Luka 22:49-51; Yohana 18:10, 11.
Gavana Mroma wa Yudea alipomwuliza Yesu maswali hususa kuhusu malengo ya kisiasa ambayo ilidaiwa alikuwa nayo, Yesu alifutilia mbali madai hayo ya uwongo kwa kujibu: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Ni wazi kwamba Yesu hakujihusisha na mambo ya kisiasa na ya kijeshi ya siku zake.
Wanafunzi wa Yesu walifuata kielelezo hichohicho. Utafiti uliofanywa na kikundi cha watafiti waliotajwa mwanzoni mwa mfululizo huu ili kuchunguza fungu la dini katika vita ulieleza hivi: “Wakristo wa mapema hawakuunga mkono jeuri. . . . Wakristo wengi walikataa kujiunga na jeshi na kupigana.” Mafundisho ya Yesu na mitume wake yalikazia kumpenda jirani yako, kutia ndani watu usiowajua na wale wa makabila na mataifa mbalimbali. (Matendo 10:34, 35; Yakobo 3:17) Kwa kweli, dini hiyo ilichochea amani.
Hatimaye, mafundisho ya awali ya Kikristo yalichafuliwa na falsafa, tamaduni, na uzalendo wenye kusababisha migawanyiko. Utafiti uliotajwa mapema kuhusu fungu la dini katika vita ulisema: “Kugeuzwa imani kwa [Maliki Mroma] Konstantino kuliwafanya Wakristo wajihusishe katika jeshi—hawakuongozwa tena na mafundisho yenye huruma ya Kristo, bali waliongozwa na malengo ya Maliki ya kupata ushindi wa kisiasa na kupata maeneo. Wakristo, kutia ndani Maliki walilazimika kutafuta sababu za kidini za kujihusisha katika vita.” Kwa njia hiyo, Ukristo bandia ukazaliwa.
Kikundi Kimoja Kilicho “Tofauti”
Je, Ukristo wa awali umepotea kabisa? La, hasha! Kuna kikundi kimoja ambacho kinahitaji kufikiriwa kwa njia ya pekee. Hakuna dini yoyote ambayo huwaiga Wakristo wa karne ya kwanza kama Mashahidi wa Yehova. Hawahusianishwi na dini yoyote kati ya zile zinazodai kuwa za Kikristo. Kitabu The Encyclopedia of Religion kinawafafanua kuwa “tofauti,” kwa sababu mafundisho yao yote yanategemea “mamlaka ya Biblia, badala ya mapokeo.”
Kama Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi katika mizozo ya kisiasa. Jarida moja lililochapishwa na Shirika la Kitaifa la Sayansi la Ukrainia linasema kwamba Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushinda “tofauti za kikabila, kitaifa, kidini, kijamii, na kiuchumi.” Jarida hilo lilieleza kwamba Mashahidi wa Yehova hawajihusishi katika “utendaji wa kupinga serikali” na wao ni “raia wanaotii sheria za nchi yao.”
Profesa Wojciech Modzelewski wa Chuo Kikuu cha Warsaw, Poland, aliandika hivi katika kitabu chake Pacifism and Vicinity: “Mashahidi wa Yehova ndio wanaofanyiza idadi kubwa zaidi leo ya watu wanaopinga vita.” Kwa sababu wao hufuatilia kwa ukaribu kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza, inaweza kusemwa kwamba Mashahidi wa Yehova wamefaulu kurudisha tena ibada ambayo ilianzishwa na Kristo na mitume wake. Ukristo wa aina hiyo kwa kweli huchochea amani.—Ona sanduku kwenye ukurasa unaofuata.
Wakati Ujao Mzuri
Ni kweli kwamba waabudu wengi wanyoofu, kutia ndani viongozi wengi wa kidini, wanachukizwa sana na unafiki wa dini zao wenyewe. Watu wengi wa kidini ambao wanajitahidi kuendeleza amani na upatano ulimwenguni wanastahili pongezi.
Hata hivyo, hata wawe na nia nzuri jinsi gani, wanadamu hawana uwezo wa kutatua matatizo ya ulimwengu huu. Nabii wa kale Yeremia aliandika hivi: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.
Lakini kuna wakati ujao mzuri. Neno la Mungu linafundisha kwamba kutakuwa na jamii mpya ya wanadamu wenye amani duniani. Jamii hiyo mpya itakuwa na undugu wa kweli. Watu wa rangi zote wataishi kwa upatano, na wanadamu hawatagawanywa tena na mipaka, chuki ya kikabila, au mafundisho ya kidini. Wote wataunganishwa pamoja na ibada safi ya Yehova Mungu.
Biblia pia inatabiri kuangamizwa kwa dini ambayo haimheshimu Mungu. Yesu alisema: “Kila ufalme uliogawanyika na kupingana wenyewe unaangamia, na kila jiji au nyumba iliyogawanyika na kupingana yenyewe haitasimama.” (Mathayo 12:25) Kwa wakati wake, Mungu atahakikisha kwamba maneno hayo yanatimia kuhusu dini zote za uwongo.
Biblia ilitabiri zamani sana kwamba Mungu “hakika atafanya hukumu kati ya mataifa na kunyoosha mambo.” Unabii huo pia unasema kwamba watu “watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” (Isaya 2:4) Unabii huo unatimia leo. Tayari dini ya kweli ambayo inafuatwa na Mashahidi wa Yehova inachochea watu wawe wenye amani.
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Mashahidi wa Yehova wameunganishwa na upendo
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Mashahidi wa Yehova ni Tofauti Jinsi Gani?
Watu wengi hushangaa wanapojifunza kwamba Mashahidi wa Yehova ni tofauti sana na dini nyingine zinazodai kumfuata Kristo. Yafuatayo ni baadhi ya mambo yanayowafanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti:
UTARATIBU
● Hawana kikundi cha makasisi.
● Wazee, walimu, na wamishonari wao hawalipwi mishahara.
● Hawatoi fungu la kumi wala hawaombi sadaka katika mahali wanapokutania ambapo huitwa Jumba la Ufalme.
● Utendaji wao wote hutegemezwa na michango ya hiari.
● Hawajihusishi katika siasa.
● Wanahubiri amani na hawashiriki katika vita.
● Wana imani na mafundisho yaleyale ulimwenguni pote.
● Wao hushirikiana pamoja bila ubaguzi wa kijamii, kikabila, na kitaifa.
● Hawana uhusiano na dini nyingine yoyote, iwe ni Wakatoliki, Waothodoksi, au Waprotestanti.
MAFUNDISHO
● Wanaamini kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli ambaye anaitwa Yehova.
● Hawaamini kwamba Yesu Kristo ni Mungu Mweza-Yote, wala hawaamini fundisho la Utatu.
● Wao hufuata mafundisho ya Yesu na wanamheshimu kama Mwana wa Mungu.
● Hawaabudu msalaba, wala hawatumii sanamu katika ibada yao.
● Hawaamini kwamba kuna moto wa mateso ambapo watu wote wabaya wanaenda wanapokufa.
● Wanaamini kwamba Mungu atawabariki wanadamu watiifu kwa kuwapa uzima wa milele ulio mkamilifu katika dunia paradiso.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba wanafuata Ukristo ule uliokuwepo katika karne ya kwanza, Ukristo ambao ulifuatwa na mitume wa Yesu.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Mserbia, Mbosnia, na Mkroatia
-
-
Je, Dini Inapaswa Kulaumiwa?Amkeni!—2011 | Januari
-
-
Je, Dini Inapaswa Kulaumiwa?
MWANDISHI na kasisi wa karne ya 18, Jonathan Swift, aliandika hivi: “Tumejihusisha sana katika dini hivi kwamba tumeanza kuchukiana badala ya kupendana.” Watu wengi wamesema kwamba kwa kweli dini inachochea migawanyiko badala ya umoja. Lakini si kila mtu anayekubaliana na maoni hayo.
Kwa mfano, fikiria mkataa uliofikiwa na kikundi kimoja cha watafiti katika Idara ya Masomo ya Amani katika Chuo Kikuu cha Bradford, Uingereza. Kikundi hicho kilisimamiwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza na kilipaswa kuchunguza ikiwa dini inachochea amani au vita.
Katika ripoti iliyochapishwa, watafiti hao walisema hivi: “Baada ya kupitia uchunguzi wa kihistoria uliofanywa na wataalamu mbalimbali, tunafikia mkataa kwamba kumekuwa na vita vichache sana ambavyo vilisababishwa hasa na dini katika miaka 100 iliyopita.” Kikundi hicho cha watafiti kilieleza kwamba vita fulani ambavyo “mara nyingi vinatajwa na vyombo vya habari na sehemu nyingine kuwa vita kuhusu dini, au vita vinavyosababishwa na tofauti za kidini, kwa kweli ni vita vya kizalendo, vya kukomboa eneo fulani au vya kujilinda.”
Hata hivyo, watu wengine wengi wanasema kwamba viongozi wa kidini, kwa matendo au kwa kukaa kimya, wamekubali au kuunga mkono vita vingi kama inavyoonyeshwa na manukuu yafuatayo:
● “Ni kana kwamba dini imejihusisha na jeuri kila mahali. . . . Katika miaka ya hivi karibuni, jeuri ya kidini imetokea kati ya Wakristo wenye msimamo mkali nchini Marekani, Waislamu na Wayahudi wenye hasira huko Mashariki ya Kati, Wahindu wanaozozana na Waislamu huko Asia Kusini, na pia kati ya watu wa dini za kiasili huko Afrika na Indonesia. . . . Watu wanaohusika katika visa hivyo wameacha dini iwaamulie mambo ya kisiasa na iendeleze mawazo yao ya kulipiza kisasi.”—Terror in the Mind of God—The Global Rise of Religious Violence.
● “Kinyume na inavyotazamiwa, mara nyingi mataifa yaliyo na ushupavu wa kidini ndiyo yaliyo na matendo maovu zaidi ya kijamii. . . . Kuwepo kwa dini nyingi hakujazuia kuongezeka sana kwa uhalifu. . . . Uthibitisho wa wazi unaonyesha hivi: Ili uweze kuishi mahali ambapo ni salama, penye utaratibu, na penye ‘ustaarabu,’ epuka maeneo yaliyo na watu wengi wanaoshikilia sana mambo ya kidini.”—Holy Hatred.
● “Wabaptisti wanajulikana zaidi kwa kupigana badala ya kufanya amani. . . . Suala la utumwa [nchini Marekani] na mambo mengine yalipogawanya makanisa na taifa lote katika karne ya 19, Wabaptisti wa Kaskazini na Kusini waliunga mkono harakati ya vita na kusema vilikuwa vita vya uadilifu na kudai kwamba Mungu alikuwa upande wao. Wabaptisti pia waliunga mkono jitihada za kitaifa za kupigana na Uingereza (1812), Mexico (1845), na Hispania (1898), wakijitetea kwamba walihusika katika vita dhidi ya [Mexico na Hispania] ‘ili kuwakomboa kidini watu waliokandamizwa na kufungua maeneo mapya kwa ajili ya kazi ya umishonari.’ Jambo kuu si kwamba Wabaptisti walipenda vita badala ya amani, lakini ni kwamba, kwa sehemu kubwa, vita vilipotokea, Wabaptisti waliviunga mkono na kushiriki.”—Review and Expositor—A Baptist Theological Journal.
● “Wanahistoria wamegundua kwamba uchochezi wa kidini katika vita umekuwepo kwa vizazi vingi na miongoni mwa watu mbalimbali na tamaduni zote za ulimwengu, na mara nyingi uchochezi huo unakuwa pande zote zinazopigana. Maneno haya ‘miungu iko upande wetu’ ni mojawapo ya maneno yaliyoanza kutumiwa zamani sana kuwachochea watu kwa ajili ya vita.”—The Age of Wars of Religion, 1000-1650—An Encyclopedia of Global Warfare and Civilization.
● “Viongozi wa kidini . . . wanapaswa kufikiria kwa uzito kwa nini wameshindwa kutoa uongozi unaofaa na kuendeleza viwango vya msingi vya imani yao. . . . Ni kweli kwamba dini zote hutaka kuwe na amani lakini haionekani kama dini imewahi kutimiza daraka hilo.”—Violence in God’s Name—Religion in an Age of Conflict.
Muda wote wa historia, viongozi wa kidini wa dini zote kuu zinazodai kuwa za Kikristo (Wakatoliki, Waothodoksi, na Waprotestanti) wa pande zote zinazopigana, wamewatuma makasisi kwenda kuwachochea wanajeshi na kusali kwa ajili ya waliokufa na waliokuwa wakielekea kufa. Kwa kufanya hivyo, wameunga mkono umwagikaji wa damu na kubariki wanajeshi wote.
Huenda wengine bado wakapinga kwamba dini haipaswi kulaumiwa kwa sababu ya vita. Lakini swali ni, Je, dini imefaulu katika jitihada zake za kuwaunganisha wanadamu?
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
“Padri Dakt. Charles A. Eaton, kasisi wa Kanisa la Madison Avenue Baptist, jana alitangaza kutoka jukwaani kwamba nyumba ya parokia iliyojengwa kwenye uwanja wa kanisa itageuzwa kuwa kituo cha kuwaandikisha wanaume wanaotaka kujiunga na jeshi la nchi kavu au la majini.
“Yeye ni kasisi mmoja kati ya zaidi ya kumi katika jiji hilo ambao huhubiri kuhusu vita mara kwa mara wakati wa ibada ya asubuhi ya Jumapili (Siku ya Yenga) na kuwahimiza wanaume na wanawake waonyeshe ushikamanifu wao kwa taifa na demokrasia kwa kutoa huduma zao vitani haraka iwezekanavyo. Bendera zilipeperushwa katika makanisa mengi.”—“The New York Times,” Aprili 16, 1917 (16/4/1917).
-