Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Imani ya Kikristo Itajaribiwa
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Mei 15
    • Imani Yajaribiwa Kuhusiana na Mwaka wa 1914

      11. Mwaka wa 1914 ulikuwaje wenye maana kwa C. T. Russell na washiriki wake?

      11 Miaka mingi kabla ya kuzuka kwa vita ya ulimwengu ya kwanza, mabaki watiwa-mafuta walikuwa wakipiga mbiu kwamba, mwaka wa 1914 ungekuwa tarehe yenye maana katika unabii wa Biblia. Hata hivyo, baadhi ya matarajio yao yalikuwa ya kabla ya wakati, na maoni yao juu ya yale ambayo yangetukia hayakuwa sahihi kabisa. Kwa kielelezo, C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, na washiriki wake, wangeweza kuona kwamba kazi kubwa mno ya kuhubiri ilihitajika. Walisoma hivi: “Gospeli ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, King James Version) Ingawa hivyo, ni jinsi gani hesabu yao iliyokuwa ndogo kwa kulinganishwa, ingeweza kwa vyovyote kufanya hivyo?

      12. Mmoja wa washiriki wa Russell aliitikiaje kweli ya Biblia?

      12 Fikiria jinsi jambo hilo lilivyomwathiri A. H. Macmillan, mshiriki wa Russell. Macmillan, aliyezaliwa Kanada, hakuwa amefikia umri wa miaka 20 alipopata kitabu cha Russell kiitwacho The Plan of the Ages (1886). (Kitabu hicho ambacho pia kiliitwa The Divine Plan of the Ages, kilipata kuwa Buku la 1 la seti iitwayo Studies in the Scriptures, iliyogawanywa kwa wingi mno. Buku la 2 liitwalo, The Time Is at Hand [1889], lilionyesha mwaka wa 1914 kuwa mwisho wa “nyakati za Wasio Wayahudi.” [Luka 21:24, KJ]) Usiku uleule Macmillan alipoanza kukisoma, aliwaza hivi: “Hiyo yasikika kuwa kweli!” Katika kiangazi cha mwaka wa 1900, alikutana na Russell kwenye mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Punde si punde, Macmillan akabatizwa na kuanza kufanya kazi pamoja na Ndugu Russell kwenye makao makuu ya Sosaiti huko New York.

      13. Macmillan na wengineo waliona tatizo gani kuhusiana na utimizo wa Mathayo 24:14?

      13 Kwa kutegemea usomaji wao wa Biblia, hao Wakristo watiwa-mafuta walionyesha mwaka wa 1914 kuwa wakati wa badiliko la maana katika kusudi la Mungu. Lakini Macmillan na wengineo walijiuliza jinsi ambavyo huko kuyahubiri mataifa kulikotabiriwa kwenye Mathayo 24:14 kungeweza kutimizwa katika wakati mfupi uliobaki. Baadaye alisema hivi: “Nakumbuka nikizungumzia jambo hilo pamoja na Ndugu Russell mara nyingi, na alikuwa akisema, ‘Ndugu, hapahapa katika New York tuna Wayahudi wengi zaidi kuliko walioko Yerusalemu. Tuna watu wengi zaidi kutoka Ireland kuliko walioko Dublin. Na tuna Waitalia wengi zaidi kuliko walioko Roma. Sasa ikiwa tutawafikia wakiwa hapa, hiyo itakuwa kuufikia ulimwengu kwa ule ujumbe.’ Lakini hilo halikuelekea kutosheleza akili zetu. Kwa hiyo basi, tukafikiria kutokeza ‘Photo-Drama’ [Drama-Picha].”

      14. Ni mradi gani wenye kutokeza ambao ulianzishwa kabla ya mwaka wa 1914?

      14 Hiyo “Photo-Drama of Creation” (Drama-Picha ya Uumbaji) ilikuwa jambo lenye kutokeza kama nini! Ilikuwa ni muunganisho wa sinema na slaidi za rangi, ambazo ziliambatanishwa na hotuba za Biblia na muziki uliochezwa kwa kutumia sahani za santuri. Mwaka wa 1913, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema hivi kuhusu mkusanyiko uliokuwa Arkansas, Marekani: “Iliamuliwa kwa kauli moja kwamba, wakati umefika wa kutumia sinema katika kuifundisha kweli ya Biblia. . . [Russell] alieleza kwamba alikuwa akishughulikia mpango huohuo kwa miaka mitatu na sasa alikuwa na mamia ya picha nzuri zilizokuwa zinakaribia kuwa tayari, ambazo bila shaka zingevutia umati mkubwa na kuitangaza Gospeli, na kusaidia umma kurudisha imani yao katika Mungu.”

      15. Ile “Photo-Drama” ilikuwa na matokeo ya aina gani?

      15 Ile “Photo-Drama” ilitimiza jambo hilohilo baada ya kuonyeshwa mara ya kwanza katika Januari 1914. Zifuatazo ni ripoti kutoka katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1914 (la Kiingereza):

      Aprili 1: “Baada ya kutazama sehemu mbili, kasisi mmoja alisema hivi: ‘Nimetazama sehemu moja na nusu tu ya PHOTO-DRAMA OF CREATION, lakini kutoka kwayo, tayari nimejifunza mambo mengi zaidi kuhusu Biblia kushinda yale niliyojifunza katika mtaala wangu wa miaka mitatu katika seminari ya theolojia.’ Baada ya kuitazama, Myahudi mmoja alisema, ‘Naenda zangu nikiwa Myahudi bora zaidi ya vile nilivyokuwa nilipoingia.’ Makasisi na watawa wa kike kadhaa wamekuja kuitazama hiyo DRAMA na wameonyesha uthamini mkubwa. . . . Ni seti kumi na mbili tu za hiyo DRAMA ambazo zimekamilika . . . Hata hivyo tayari tumeyafikia na tunayatumikia majiji thelathini na moja . . . Watu zaidi ya thelathini na tano elfu kwa siku, wanatazama, kusikia, kushangilia, na kufikiri, nao wanabarikiwa.”

      Juni 15: “Hizo picha zimenifanya niwe na bidii zaidi kuieneza Kweli, na imeongeza upendo wangu kwa Baba wa Kimbingu na Ndugu yetu Mkubwa mpendwa, Yesu. Mimi husali kila siku ili Mungu abariki sana hiyo PHOTO-DRAMA OF CREATION na wote wanaoshiriki kuionyesha. . . . Ni mimi mtumishi wenu katika Yeye, F. W. KNOCHE.—Iowa.”

      Julai 15: “Twapendezwa kuona uvutio mzuri ajabu ambao hizo picha zimekuwa nao katika jiji hili, na tumepata uhakikisho wa kwamba, ushahidi huo unaotolewa ulimwengu pia unatumiwa kukusanya wengi wanaothibitika kuwa vito vyenye kuchaguliwa na Bwana. Twajua juu ya hesabu kubwa ya wanafunzi wa Biblia ambao sasa wanashirikiana na Darasa hapa kwa sababu ya hiyo kazi ya Photo-Drama. . . . Dada yenu katika Bwana, EMMA L. BRICKER.”

      Novemba 15: “Tuna hakika kwamba mtaterema kusikia juu ya ushahidi mzuri ambao unatolewa kupitia PHOTO-DRAMA OF CREATION kwenye jumba liitwalo The London Opera House, Kingsway. Mkono wenye kuongoza wa Bwana umedhihirishwa vizuri ajabu katika kila shughuli ya maonyesho hayo hivi kwamba, ndugu wanashangilia sana . . . Watazamaji wetu walikuwa watu wa matabaka yote na aina zote; tumewaona makasisi wengi kati ya wahudhuriaji. Kasisi mmoja . . . aliomba apewe tikiti ili yeye na mke wake waweze kuja na kuiona tena. Kasisi fulani wa Kanisa la Uingereza, ameitazama hiyo DRAMA mara kadhaa, na . . . amewaleta rafiki zake wengi ili kuishuhudia. Maaskofu wawili wamekuwapo, na watu kadhaa wenye vyeo.”

      Desemba 1: “Mke wangu nami twamshukuru Baba yetu wa Kimbingu kwa kweli, kwa sababu ya baraka kubwa na yenye thamani sana ambayo imetujia kupitia kwako. Tuliielewa na kuikubali Kweli kwa sababu ya PHOTO-DRAMA yenu nzuri . . . Tuna mabuku yako sita ya STUDIES IN THE SCRIPTURES. Yanatusaidia sana.”

      Kuitikia Majaribu Wakati Huo

      16. Kwa nini mwaka wa 1914 ulileta majaribu ya imani?

      16 Ingawa hivyo, ilikuwaje wakati ambapo hao Wakristo wenye moyo mweupe na wenye kujitoa waligundua kwamba tarajio lao la kujiunga pamoja na Bwana mwaka wa 1914 halikutimizwa? Watiwa-mafuta hao walipatwa na kipindi chenye majaribu yasiyo na kifani. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1914, (la Kiingereza) lilitangaza hivi: “Na tukumbuke kwamba tuko katika majira ya majaribu.” Juu ya hilo, kitabu Mashahidi wa Yehova Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu (1997) chataarifu hivi: “Miaka ya kutoka 1914 hadi 1918, ilithibitika kwelikweli kuwa ‘majira ya kutahini [kujaribiwa]’ kwa Wanafunzi wa Biblia.” Je, wangeruhusu imani yao itakaswe na kufikiri kwao kurekebishwe ili waweze kuchukua daraka la kufanya kazi kubwa iliyokuwa mbele yao?

      17. Watiwa-mafuta waaminifu waliitikiaje kubaki duniani baada ya mwaka wa 1914?

      17 Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1916, (la Kiingereza) lilisema hivi: “Tuliwaza kwamba kazi ya Uvunaji ya kukusanya Kanisa [watiwa-mafuta], ingetimizwa kabla ya mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi; lakini Biblia haikusema jambo lolote kama hilo. . . . Je, tunajuta kwamba kazi ya Uvunaji inaendelea? . . . Ndugu wapendwa, mtazamo wetu wa sasa wapaswa kuwa wa kuonyesha shukrani kubwa kwa Mungu, wa kuonyesha uthamini wenye kuongezeka wa Kweli nzuri ambayo Ametupa pendeleo la kuielewa na kutambulishwa kwayo, na wa kuwa na bidii yenye kuongezeka katika kusaidia kupelekea wengine ujuzi wa hiyo Kweli.” Imani yao ilikuwa imejaribiwa, hata hivyo walikabili jaribu hilo kwa mafanikio. Lakini yatupasa sisi Wakristo tujue kwamba, majaribu ya imani yaweza kuwa mengi na ya aina mbalimbali.

      18, 19. Baada ya kifo cha Ndugu Russell, ni majaribu gani mengine ya imani yaliyofuata kwa watu wa Mungu?

      18 Kwa kielelezo, punde baada ya Ndugu Charles T. Russell kufa, aina nyingine ya jaribu iliwapata mabaki. Hilo lilikuwa jaribu la uaminifu-mshikamanifu wao na imani yao. Ni nani ‘aliyekuwa mtumwa mwaminifu’ wa Mathayo 24:45? Baadhi yao walihisi kwamba huyo mtumwa mwaminifu alikuwa Ndugu Russell mwenyewe, nao walisita kushirikiana na mipango mipya ya kitengenezo. Ikiwa alikuwa amekuwa huyo mtumwa, ndugu wangefanya nini kwa kuwa sasa alikuwa amekufa? Je, iliwapasa wafuate mtu fulani aliyechaguliwa karibuni, au sasa ulikuwa wakati wa kutambua kwamba Yehova alikuwa akitumia, si mtu mmoja tu, bali kikundi chote cha Wakristo kikiwa mtumishi, au jamii ya mtumwa?

      19 Jaribu la ziada liliwapata Wakristo wa kweli mwaka wa 1918, wakati ambapo wenye mamlaka wa kilimwengu, wakichochewa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, ‘walitunga madhara kwa njia ya sheria’ dhidi ya tengenezo la Yehova. (Zaburi 94:20, KJ) Mnyanyaso wenye jeuri ulioongezeka ulianzishwa dhidi ya Wanafunzi wa Biblia katika Amerika Kaskazini na Ulaya. Upinzani uliochochewa na makasisi ulifikia upeo katika Mei 7, 1918, wakati ambapo waranti za serikali ya muungano ya Marekani zilitolewa ili kumkamata J. F. Rutherford na washiriki kadhaa wa karibu, kutia na A. H. Macmillan. Walishtakiwa isivyo kweli kuwa wachochezi, na wenye mamlaka walipuuza maombi yao ya kutokuwa na hatia.

      20, 21. Kama ilivyotabiriwa kwenye Malaki 3:1-3, ni kazi gani iliyofanywa miongoni mwa watiwa-mafuta?

      20 Ingawa haikutambuliwa hivyo wakati huo, kazi ya kutakasa ilikuwa ikiendelea, kama ifafanuliwavyo kwenye Malaki 3:1-3: “Ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye [mjumbe wa agano] ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo; naye ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa, naye atawatakasa wana wa Lawi, atawasafisha kama dhahabu na fedha; nao watamtolea BWANA dhabihu katika haki.”

      21 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipokaribia kwisha, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walikabili jaribu jingine la imani—kama wangedumisha kutokuwamo kabisa kuhusiana na mambo ya kijeshi ya kilimwengu. (Yohana 17:16; 18:36) Baadhi yao hawakufanya hivyo. Kwa hiyo mwaka wa 1918, Yehova alimtuma “mjumbe wa agano,” Kristo Yesu, kwenye mpango Wake wa hekalu la kiroho ili kukitakasa kikundi kidogo cha waabudu Wake kisiwe na mawaa ya kilimwengu. Waliokubali wajibu wa kuonyesha imani ya kweli walijifunza kutokana na jambo hilo lililowapata na kusonga mbele, wakiendelea kuhubiri kwa bidii.

      22. Kuhusiana na majaribu ya imani, ni mambo gani ambayo yabaki kuchunguzwa?

      22 Yale ambayo tumechunguza si mambo yenye upendezi wa kijuujuu tu wa kihistoria. Yanahusika moja kwa moja na hali ya kiroho ya sasa ya kutaniko la ulimwenguni pote la Yehova. Lakini acheni tuchunguze katika makala inayofuata baadhi ya majaribu ya imani ambayo watu wa Mungu leo wanakabili, na tuone jinsi tuwezavyo kuyashinda kwa mafanikio.

  • Ubora wa Imani Yako—Wajaribiwa Sasa
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Mei 15
    • 4. Ndugu mmoja alihisije juu ya majaribu ambayo yeye na Wakristo wengine watiwa-mafuta walipatwa nayo?

      4 Katika makala iliyotangulia, tulichunguza majaribu ambayo mabaki watiwa-mafuta walikabili kuanzia mwaka wa 1914 na kuendelea. Je, hayo yalikuwa msingi wa kuwa na shangwe? A. H. Macmillan alitoa maoni haya kwa kukumbuka wakati uliopita: “Nimeona majaribu makali yakilipata tengenezo na majaribu ya imani ya wale waliomo ndani yake. Kwa msaada wa roho ya Mungu, tengenezo liliokoka na kuendelea kusitawi. Nimeona hekima ya kumngojea Yehova kwa subira ili aboreshe uelewevu wetu wa mambo ya Kimaandiko, badala ya kukasirika kwa sababu ya wazo jipya. . . . Hata iwe pindi kwa pindi tutalazimika kufanya marekebisho gani katika maoni yetu, jambo hilo halingebadili maandalizi yenye rehema ya fidia na ahadi ya Mungu ya uhai wa milele. Kwa hiyo hakukuwa na uhitaji wa kuruhusu imani yetu idhoofishwe na matarajio ambayo hayakutimizwa au mabadiliko katika maoni.”—Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1966, ukurasa wa 504 (la Kiingereza).

      5. (a) Ni manufaa zipi zilizotokezwa na kupatwa na majaribu kwa mabaki? (b) Kwa nini jambo hilo la kujaribiwa litupendeze sasa?

      5 Wakristo watiwa-mafuta waliookoka kipindi cha majaribu cha 1914-1919 waliwekwa huru na uvutano wenye kudhibiti wa ulimwengu, na mazoea ya kidini ya Kibabiloni. Mabaki walisonga mbele wakiwa watu waliosafishwa na kutakaswa, wakitoa kwa utayari dhabihu za sifa kwa Mungu na wakiwa na uhakikisho kwamba, walikuwa kikundi cha watu waliokubalika kwake. (Isaya 52:11; 2 Wakorintho 6:14-18) Hukumu ilikuwa imeanza na nyumba ya Mungu, lakini haingekamilishwa katika kipindi kimoja kilichowekwa. Kujaribiwa na kupepetwa kwa watu wa Mungu kwaendelea. Imani ya wale watumainio kuokoka “dhiki kubwa” inayokaribia, inajaribiwa pia. (Ufunuo 7:9, 14) Inajaribiwa katika njia sawa na vile imani ya watiwa-mafuta ilivyojaribiwa, na vilevile katika njia nyinginezo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki