-
Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha KwakoMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 15
-
-
Upendo na Staha kwa Wale Wanaofundishwa
12. Mtazamo wa Yesu kuelekea wanafunzi wake ulikuwa nini?
12 Sifa nyingine muhimu ni mtazamo unaofaa kuelekea wale unaofundisha. Mafarisayo waliwadharau wale waliomsikiliza Yesu. “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa,” wakasema. (Yohana 7:49) Lakini Yesu alikuwa na upendo wenye kina kirefu na pia staha kwa wanafunzi wake. Yeye alisema: “Siwaiti nyinyi tena watumwa, kwa sababu mtumwa hayajui yale afanyayo bwana-mkubwa wake. Lakini nimewaita nyinyi marafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha nyinyi.” (Yohana 15:15) Hilo lilionyesha namna ambavyo wanafunzi wa Yesu wanapaswa kuendesha utendaji wao wa kufundisha.
-
-
Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha KwakoMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 15
-
-
15. Twaweza kuonyeshaje staha kwa wanafunzi wetu wa Biblia?
15 Staha kwa wanafunzi wetu yahusisha kuepuka kujaribu kudhibiti maisha yao ya kibinafsi. (1 Wathesalonike 4:11) Kwa mfano, twaweza kuwa tunajifunza na mwanamke ambaye anaishi na mwanamume ambaye hajafunga ndoa naye. Labda wamezaa watoto pamoja. Mwanamke huyo ataka kurekebisha mambo ili ajipatanishe na viwango vya Yehova kwa kuwa amepata ujuzi sahihi juu ya Mungu. (Waebrania 13:4) Je, apaswa kuolewa na mwanamume huyo au kutengana naye? Labda twahisi kwa dhati kwamba kuolewa na mwanamume ambaye hapendezwi sana na mambo ya kiroho kungezuia maendeleo yake ya baadaye. Kwa upande mwingine, huenda tukahofia hali njema ya watoto wake na kufikiria kwamba ingekuwa afadhali aolewe na huyo mwanamume. Kwa vyovyote vile, itakuwa kukosa kuonyesha staha na upendo kuingilia maisha ya mwanafunzi na kujaribu kumlazimisha akubali maoni yetu katika mambo kama hayo. Kwani, ni huyo mwanamke ambaye ni lazima aishi na matokeo ya uamuzi wake. Basi, je, haingekuwa bora kumzoeza mwanafunzi wa aina hiyo kutumia ‘nguvu zake mwenyewe za ufahamu’ na kujiamulia yale anayopaswa kufanya?—Waebrania 5:14.
-