-
Tuna Sababu ya Kulia kwa ShangweMnara wa Mlinzi—1996 | Februari 15
-
-
Tuna Sababu ya Kulia kwa Shangwe
“Wao watapata mchachawo na kushangilia, na huzuni na kupiga kite lazima zikimbie mbali.”—ISAYA 35:10, NW.
1. Ni nani leo walio na sababu ya shangwe hasa?
YAELEKEA umeona kwamba ni watu wachache walio na shangwe halisi siku hizi. Lakini, wakiwa Wakristo wa kweli, Mashahidi wa Yehova wana shangwe. Na taraja la kupata shangwe iyo hiyo tayari lapatikana kwa mamilioni mengine ya wale ambao hawajabatizwa bado, vijana kwa wazee, wanaoshirikiana na Mashahidi. Jambo la kwamba wewe sasa unasoma maneno haya katika gazeti hili laonyesha kwamba shangwe hii ni yako tayari au waweza kuipata kwa urahisi.
2. Shangwe ya Mkristo hutofautianaje na hali ya kawaida ya watu walio wengi?
2 Watu walio wengi huhisi kwamba maisha zao zinakosa jambo fulani. Namna gani wewe? Ni kweli, huenda usiwe na kila kitu cha kimwili ambacho ungeweza kutumia, kwa hakika huna vyote ambavyo matajiri na watu wenye nguvu wa leo walivyo navyo. Na huenda ukapenda kuwa na mengi zaidi kwa habari ya afya nzuri na nguvu. Hata hivyo, yaweza kusemwa bila kusita kwamba kwa habari ya shangwe, wewe ni tajiri zaidi na mwenye afya zaidi kuliko walio wengi wa mabilioni ya watu wa dunia. Namna gani?
3. Ni maneno gani yenye maana yanayostahili uangalifu wetu, na kwa nini?
3 Kumbuka maneno haya ya Yesu: “Mambo hayo nimewaambia, ili shangwe yangu ipate kuwa katika nyinyi na shangwe yenu ipate kufanywa yenye kujaa.” (Yohana 15:11, NW) “Shangwe yenu ipate kufanywa yenye kujaa.” Huo ni ufafanuzi ulioje! Funzo la kindani juu ya njia ya kuishi ya Kikristo lingefunua sababu nyingi za kujaa kwa shangwe yetu. Lakini sasa hivi, ona maneno yenye maana kwenye Isaya 35:10 (NW). Haya ni yenye maana kwa sababu yanahusiana sana nasi leo. Twasoma hivi: “Wale wenyewe waliokombolewa na Yehova watarudi na kwa hakika watakuja Zayoni kwa kilio chenye shangwe; na kushangilia hadi wakati usio dhahiri kutakuwa juu ya kichwa chao. Wao watapata mchachawo na kushangilia, na huzuni na kupiga kite lazima zikimbie mbali.”
4. Ni shangwe ya namna gani inayotajwa kwenye Isaya 35:10, na kwa nini tukazie jambo hilo uangalifu?
4 “Kushangilia hadi wakati usio dhahiri.” Fungu la maneno “hadi wakati usio dhahiri” ni ufasiri sahihi wa kile ambacho Isaya aliandika katika Kiebrania. Lakini, kama vile imeonyeshwa katika maandiko mengine, maana yalo katika mstari huu ni “milele.” (Zaburi 45:6; 90:2; Isaya 40:28) Kwa hiyo kushangilia huko kutakuwa bila kikomo, katika hali zitakazoruhusu—ndiyo, zitakazothibitisha—kushangilia kudumuko milele. Je, hilo halisikiki kuwa jambo lenye kupendeza? Lakini, labda mstari huo waonekana kwako kuwa simulizi juu ya hali ya kuwaziwa tu, likikufanya uhisi: ‘Hilo kwa kweli halinihusu mimi kadiri ambavyo matatizo na mahangaiko yangu ya kila siku hunihusu.’ Lakini, mambo ya hakika huonyesha vingine. Ahadi ya kiunabii kwenye Isaya 35:10 ina maana kwako leo. Ili kupata kujua ni jinsi gani, acheni tuchunguze sura hii nzuri, Isaya 35, tukiangalia kila sehemu kulingana na muktadha. Uwe na uhakika kwamba utafurahia kile tutakachopata.
Watu Waliohitaji Kushangilia
5. Unabii katika Isaya sura ya 35 umo katika kikao kipi cha kiunabii?
5 Ukiwa msaada, acheni tuangalie habari ya msingi, na kikao cha kihistoria, cha unabii huu wenye kusisimua. Nabii Mwebrania Isaya aliuandika wakati fulani karibu na 732 K.W.K. Hiyo ilikuwa miongo kadhaa kabla ya majeshi ya Babiloni kuharibu Yerusalemu. Kama vile Isaya 34:1, 2 lionyeshavyo, Mungu alikuwa ametabiri kwamba atalipiza kisasi mataifa, kama vile Edomu, lililotajwa kwenye Isaya 34:6. Kwa wazi yeye alitumia Wababiloni wa kale ili kufanya hivyo. Vivyo hivyo, Mungu alitumia Wababiloni wafanye Yuda ukiwa kwa sababu Wayahudi hawakuwa waaminifu. Tokeo likawa nini? Watu wa Mungu walichukuliwa mateka, na bara lao likawa ukiwa kwa miaka 70.—2 Mambo ya Nyakati 36:15-21.
6. Kuna tofauti gani kati ya kile ambacho kingepata Waedomu na kile ambacho kingepata Wayahudi?
6 Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya Waedomu na Wayahudi. Adhabu ya kimungu juu ya Waedomu ilikuwa yenye kudumu; hatimaye wao walitoweka wakiwa kikundi cha watu. Ndiyo, waweza bado kuyazuru yale magofu matupu yaliyo katika eneo ambapo Waedomu walikuwa wakiishi, kama yale mabaki ya Petra yajulikanayo ulimwenguni pote. Lakini leo, hakuna taifa wala kikundi cha watu kiwezacho kuthibitishwa kuwa ‘Waedomu.’ Kwa upande mwingine, je, ule ukiwa wa Yuda uliosababishwa na Babiloni ungedumu milele, ukiacha bara hilo bila shangwe milele?
7. Wayahudi waliotekwa Babiloni huenda wakawa waliitikiaje Isaya sura ya 35?
7 Hapa huo unabii mzuri ajabu katika Isaya sura ya 35 una maana yenye kusisimua. Huo waweza kuitwa unabii wa kurudishwa, kwa maana ulikuwa na utimizo wao wa kwanza wakati Wayahudi waliporudi bara lao katika 537 K.W.K. Waisraeli waliokuwa wametekwa Babiloni walipewa uhuru wa kurudi bara lao. (Ezra 1:1-11) Hata hivyo, mpaka hilo lilipotendeka Wayahudi waliotekwa Babiloni waliofikiria unabii huo wa kimungu huenda wakawa walijiuliza ni hali za namna gani wangepata waliporudi bara lao la kitaifa, Yuda. Nao wenyewe wangekuwa katika hali gani? Majibu yanahusiana moja kwa moja na sababu kwa nini sisi kwa kweli tuna sababu ya kulia kwa shangwe. Acheni tuone.
8. Wayahudi walipata hali zipi waliporudi kutoka Babiloni? (Linganisha Ezekieli 19:3-6; Hosea 13:8.)
8 Kwa hakika hali isingeonekana kuwa nzuri kwa Wayahudi hata waliposikia kwamba waliweza kurudi bara lao. Bara lao lilikuwa limekuwa ukiwa kwa miongo saba, muda wa maisha ya mtu. Bara hilo lilikuwa limepatwa na nini? Mashamba yoyote yaliyokuwa yamelimwa, ya mizabibu, au ya miti yenye matunda yangalikuwa yamekuwa nyika. Bustani au nyanja zenye kunyunyizwa maji zingezorota kuwa bara kavu lililo tupu au jangwa. (Isaya 24:1, 4; 33:9; Ezekieli 6:14) Fikiria pia, wanyama wa pori ambao wangekuwa wengi. Hao wangetia ndani wale walao nyama, kama vile simba na chui. (1 Wafalme 13:24-28; 2 Wafalme 17:25, 26; Wimbo Ulio Bora 4:8) Wala hawangeweza kupuuza dubu, waliokuwa na uwezo wa kumpiga kwa nguvu mwanamume, mwanamke, au mtoto. (1 Samweli 17:34-37; 2 Wafalme 2:24; Mithali 17:12) Na hata hatuhitaji kutaja wale nyoka-vipiri na nyoka wengine wenye sumu, wala nge. (Mwanzo 49:17; Kumbukumbu la Torati 32:33; Ayubu 20:16; Zaburi 58:4; 140:3; Luka 10:19) Kama ungalikuwa pamoja na wale Wayahudi wenye kurudi kutoka Babiloni katika 537 K.W.K., labda ungalisita kutembea huku na huku katika eneo hilo. Hilo halikuwa paradiso walipowasili.
9. Ni kwa sababu gani wale wenye kurudi walikuwa na msingi wa kuwa na tumaini na uhakika?
9 Bado, Yehova mwenyewe alikuwa amewaongoza waabudu wake hadi nyumbani, naye ana uwezo wa kugeuza kabisa hali ya ukiwa. Je, huamini hivyo kuhusu Muumba? (Ayubu 42:2; Yeremia 32:17, 21, 27, 37, 41) Kwa hiyo yeye angewafanyia nini—yeye aliwafanyia nini—wale Wayahudi wenye kurudi na bara lao? Hilo linaathirije watu wa Mungu katika nyakati za kisasa na linaathirije hali yako—sasa na wakati ujao? Kwanza acheni tuone ni nini kilichotendeka wakati huo wa nyuma.
Wenye Shangwe Juu ya Hali Iliyobadilika
10. Isaya 35:1, 2 lilitabiri badiliko jipi?
10 Ni nini kingetendeka wakati Sairasi (Koreshi) alipowaruhusu Wayahudi warudi bara hilo lenye kutia hofu? Soma ule unabii wenye kusisimua kwenye Isaya 35:1, 2, NW: “Nyika na mkoa usio na maji utachachawa, na uwanda wa jangwa utakuwa wenye shangwe na kuchanua maua kama waridi. Hautakosa kuchanua maua, nao utakuwa wenye shangwe kwelikweli kwa kushangilia na kwa kulia kwa furaha. Lazima upewe utukufu wa Lebanoni wenyewe, uzuri wa Karmeli na wa Sharoni. Kutakuwa na wale watakaoona utukufu wa Yehova, uzuri wa Mungu wetu.”
11. Isaya alitumia ujuzi upi juu ya bara?
11 Katika nyakati za Biblia, Lebanoni, Karmeli, na Sharoni zilijulikana kwa uzuri wazo wa mimea mibichi. (1 Mambo ya Nyakati 5:16; 27:29; 2 Mambo ya Nyakati 26:10; Wimbo Ulio Bora 2:1; 4:15; Hosea 14:5-7) Isaya alitumia vielezi hivyo ili kufafanua jinsi ambavyo lile bara lililogeuzwa lingekuwa, kwa msaada wa Mungu. Lakini je, hilo lilipaswa liwe tokeo juu ya udongo pekee? Bila shaka la!
12. Kwa nini twaweza kusema kwamba unabii katika Isaya sura ya 35 unakazia fikira watu?
12 Isaya 35:2, (NW), husema juu ya bara kuwa ‘lenye shangwe kwa kushangilia na kwa kulia kwa furaha.’ Twajua kwamba udongo na mimea haikuwa ‘yenye shangwe kwa kushangilia,’ kihalisi. Hata hivyo, kugeuzwa kwayo kuwa yenye rutuba na yenye kuzaa kungefanya watu wahisi hivyo. (Mambo ya Walawi 23:37-40; Kumbukumbu la Torati 16:15; Zaburi 126:5, 6; Isaya 16:10; Yeremia 25:30; 48:33) Mabadiliko halisi katika bara lenyewe yangelingana na mabadiliko katika watu, kwa kuwa watu ndio wanaokaziwa fikira katika unabii huu. Kwa hiyo tuna sababu ya kuyaelewa maneno ya Isaya kuwa yanakazia fikira hasa mabadiliko katika Wayahudi wenye kurudi, hasa hali yao ya kushangilia.
13, 14. Isaya 35:3, 4 lilitabiri badiliko gani katika watu?
13 Kwa hiyo, acheni tuchunguze zaidi unabii huu wenye kusisimua tuone jinsi ilivyotimizwa baada ya kuwekwa huru kwa Wayahudi na kurudi kwao kutoka Babiloni. Katika mstari wa 3 na wa 4, Isaya asema juu ya mabadiliko mengine katika wale wenye kurudi: “Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu, yafanyeni imara magoti yaliyolegea, Waambieni walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope; tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi.”
14 Je, haitii nguvu kufikiri kwamba Mungu wetu, ambaye aliweza kugeuza hali ya ardhi yenye ukiwa, hupendezwa sana na waabudu wake? Yeye hakutaka Wayahudi waliotekwa wahisi udhaifu, kuvunjika moyo, au kuhangaikia wakati ujao. (Waebrania 12:12) Fikiria hali ya mateka hao Wayahudi. Kando ya lile tumaini ambalo waliweza kupata kutoka katika unabii mbalimbali wa Mungu juu ya wakati ujao wao, ingalikuwa vigumu kwao kuwa wenye matazamio mazuri. Ilikuwa kana kwamba walikuwa ndani ya gereza la chini ya ardhi lenye giza, bila uhuru wa kwenda huku na huku na kuwa wenye bidii katika kumtumikia Yehova. Kwa hakika ingalionekana kwao kana kwamba hakukuwa na nuru huko mbele.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 28:29; Isaya 59:10.
15, 16. (a) Twaweza kukata maneno kwamba Yehova aliwafanyia nini wale wenye kurudi? (b) Kwa nini wale wenye kurudi wasingalitazamia maponyo ya kimwili ya kimuujiza, lakini Mungu alifanya nini kulingana na Isaya 35:5, 6?
15 Lakini, hilo lilibadilika kama nini, wakati Yehova alipomfanya Sairasi awaachilie ili warudi nyumbani! Hakuna uthibitisho wa Kibiblia kwamba Mungu alifumbua kimuujiza macho yoyote mapofu ya Wayahudi wenye kurudi huko, akazibua masikio ya wowote waliokuwa viziwi, au kuponya viungo vyovyote vilivyolemaa au vilivyokosekana. Hata hivyo, kwa kweli yeye alifanya jambo lililo tukufu zaidi. Aliwarudisha kwenye nuru na uhuru wa bara lao walilopenda!
16 Hakuna jambo lionyeshalo kwamba wale wenye kurudi walimtazamia Yehova afanye maponyo hayo ya kimwili ya kimuujiza. Ni lazima iwe waling’amua kwamba Mungu hakuwa amefanya hivyo na Isaka, Samsoni, au Eli. (Mwanzo 27:1; Waamuzi 16:21, 26-30; 1 Samweli 3:2-8; 4:15) Lakini ikiwa walitazamia kugeuzwa kwa hali yao kitamathali kwa njia ya kimungu, hawakukatishwa tamaa. Kwa hakika, mstari wa 5 na wa 6 ulikuwa na utimizo kabisa katika maana ya kitamathali. Isaya alitabiri hivi kwa usahihi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”
Kufanya Bara Liwe Kama Paradiso
17. Yehova alifanya mabadiliko gani ya halisi hatimaye?
17 Wale wenye kurudi kwa hakika wangalikuwa na sababu ya kulia kwa furaha juu ya hali kama zile ambazo Isaya aliendelea kufafanua: “Maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji; katika makao ya mbweha, walipokuwa wamelala, patakuwa na majani, pamoja na mianzi na manyasi.” (Isaya 35:6b, 7) Ingawa huenda tusione hali hiyo katika mkoa huo wote leo, uthibitisho hudokeza kwamba wakati mmoja eneo lililokuwa Yuda lilikuwa “paradiso ya kimalisho.”a
18. Yaelekea Wayahudi wenye kurudi wangaliitikiaje baraka za Mungu?
18 Kwa habari ya visababishi vya shangwe, fikiria jinsi ambavyo mabaki ya Wayahudi lazima yawe yalihisi yaliporudishwa kwenye Bara Lililoahidiwa! Yalikuwa na fursa ya kuchukua lile bara kavu, lililokaliwa na mbweha na wanyama wengine wa jinsi hiyo, na kuligeuza. Je, wewe usingalipata shangwe katika kufanya kazi hiyo ya kurudisha hali nzuri, hasa ikiwa ulijua kwamba Mungu alikuwa akibariki jitihada zako?
19. Kurudi kutoka utekwa wa Kibabiloni kulikuwa na masharti katika maana gani?
19 Hata hivyo, si kwamba Wayahudi wote waliotekwa Babiloni waliweza kurudi au walirudi ili kushiriki katika mgeuzo huo wa hali wenye shangwe. Mungu aliweka masharti. Hakuna yeyote aliyechafuliwa na mazoea ya kidini ya kipagani, yaliyo ya Kibabiloni aliyekuwa na haki ya kurudi. (Danieli 5:1, 4, 22, 23; Isaya 52:11) Wala hakuna yeyote aliweza kurudi aliyejitia kwa upumbavu katika mwendo usio wenye hekima. Watu wote kama hao hawakustahili. Kwa upande mwingine, wale waliotimiza viwango vya Mungu, ambao aliwaona kuwa watakatifu kwa kadiri fulani, wangeweza kurudi Yuda. Wangeweza kusafiri kana kwamba wakiwa katika Njia ya Utakatifu. Isaya alielewesha hilo wazi katika mstari wa 8, NW: “Kwa hakika kutakuja kuwa na njia kuu huko, hata njia; na hiyo itaitwa Njia ya Utakatifu. Na yule asiye safi hataipitia. Nayo itakuwa kwa ajili ya yule atembeaye katika njia hiyo, na wapumbavu wowote hawatazurura juu yayo.”
20. Wayahudi hawakuhitaji kuhofu nini walipokuwa wakirudi, hilo likitokeza nini?
20 Wayahudi wenye kurudi hawakuhitaji kuhofu shambulio lolote kutoka kwa watu walio kama hayawani au kwa magenge ya watekaji. Kwa nini? Kwa sababu Yehova asingeruhusu hao wawe katika Njia hiyo pamoja na watu wake walionunuliwa tena. Kwa hiyo waliweza kusafiri wakiwa na matazamio mazuri yenye shangwe, wakiwa na mataraja yenye furaha. Ona jinsi Isaya alivyofafanua hilo katika kumalizia unabii huo: “Hakuna simba atakayethibitika kuwa huko, na aina ya hayawani-mwitu wakali hawataiingia. Hakuna watakaopatikana huko; na wale walionunuliwa tena lazima watembee humo. Na wale wenyewe waliokombolewa na Yehova watarudi na kwa hakika watakuja Zayoni kwa kilio chenye shangwe; na kushangilia hadi wakati usio dhahiri kutakuwa juu ya kichwa chao. Wao watapata mchachawo na kushangilia, na huzuni na kupiga kite lazima zikimbie mbali.”—Isaya 35:9, 10, NW.
21. Sisi leo twapaswa kuonaje utimizo wa Isaya sura ya 35 ambao umetukia tayari?
21 Tuna maelezo ya kiunabii yaliyoje hapa! Lakini, hatupaswi kuyaona haya kuwa yakishughulika na historia tu iliyopita, kana kwamba yalikuwa masimulizi yenye kupendeza yasiyohusu sana hali yetu au wakati wetu ujao. Jambo la hakika ni kwamba unabii huu una utimizo wa ajabu leo miongoni mwa watu wa Mungu, kwa hiyo kwa kweli unaathiri kila mmoja wetu. Huo watuandalia sababu timamu za kulia kwa shangwe. Sehemu hizi zinazohusu maisha yako sasa na katika wakati ujao zinashughulikiwa katika makala inayofuata.
-
-
Wenye Shangwe Sasa na MileleMnara wa Mlinzi—1996 | Februari 15
-
-
Wenye Shangwe Sasa na Milele
“Mchachawe, enyi watu, na mwe na shangwe milele katika kile ninachoumba. Kwa sababu ninaumbia Yerusalemu chanzo cha shangwe na watu wayo chanzo cha mchachawo.”—ISAYA 65:18, NW.
1. Ibada ya kweli imeathirije watu mmoja-mmoja muda wa karne ambazo zimepita?
MUDA wa karne ambazo zimepita, idadi ya watu isiyohesabika wamepata shangwe nyingi katika kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova. Daudi alikuwa mmoja wao aliyekuwa mwenye shangwe katika ibada ya kweli. Biblia husimulia kwamba wakati sanduku la agano lilipoletwa Yerusalemu, “Daudi na nyumba yote ya Israeli wakalileta sanduku la BWANA kwa shangwe.” (2 Samweli 6:15) Shangwe hiyo katika kumtumikia Yehova si jambo la wakati uliopita tu. Wewe waweza kushiriki katika hiyo. Na hata sehemu mpya za shangwe zaweza kuwa zako karibuni!
2. Zaidi ya utimizo wa kwanza wa Isaya sura ya 35 kwa Wayahudi wenye kurudi, ni nani leo wanaohusika katika utimizo mwingine?
2 Katika makala inayotangulia, tulichunguza utimizo wa kwanza wa unabii wenye kusisimua uliorekodiwa katika Isaya sura ya 35. Twaweza kwa kufaa kuuita huo unabii wa kurudisha kwa sababu ndivyo ulivyokuja kuwa kwa Wayahudi wa zamani. Huo una utimizo uo huo katika wakati wetu. Jinsi gani? Kuanzia na mitume wa Yesu na wengine wakati wa Pentekoste 33 W.K., Yehova amekuwa akishughulika na Waisraeli wa kiroho. Hawa ni wanadamu waliotiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu wanaokuwa sehemu ya lile ambalo mtume Paulo huita “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Warumi 8:15-17) Kumbuka pia, kwamba kwenye 1 Petro 2:9, (NW) Wakristo hawa wanaitwa “jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, kikundi cha watu kwa ajili ya miliki ya pekee.” Petro aendelea kutambulisha mgawo wanaopewa Israeli wa kiroho: ‘Mnapaswa kutangaza kotekote sifa bora kabisa za yeye aliyewaita nyinyi kutoka gizani kuingia katika nuru yake ya ajabu.’
Utimizo Katika Wakati Wetu
3, 4. Hali ilikuwa nini wakati Isaya sura ya 34 ilipotimizwa katika nyakati za kisasa?
3 Kulikuwa na wakati mapema katika karne hii ambapo mabaki ya Israeli wa kiroho duniani hawakuwa wenye kutenda kwa uthabiti sikuzote katika kutangaza ujumbe huo. Hawakuwa wakishangilia kikamili katika nuru ya Mungu ya ajabu. Kwa kweli, walikuwa gizani sana. Hiyo ilikuwa lini? Na Yehova Mungu alifanya nini juu ya hilo?
4 Ilikuwa katika kipindi cha Vita ya Ulimwengu 1, upesi baada ya Ufalme wa Mungu wa Kimesiya kusimamishwa mbinguni mwaka 1914. Mataifa, kwa kuungwa mkono na makasisi wa makanisa katika nchi mbalimbali, yalikuwa yameghadhabikiana. (Ufunuo 11:17, 18) Bila shaka, Mungu alikuwa amepinga Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi pamoja na jamii yayo ya makasisi iliyokwezwa kama vile alivyokuwa amepinga lile taifa la Edomu lenye kiburi. Kwa hiyo, Jumuiya ya Wakristo, lile Edomu la mfano, karibu itapatwa na utimizo wa unabii wa siku ya kisasa ya Isaya sura ya 34. Utimizo huo kupitia uangamizo wenye kudumu ni wa hakika kama vile utimizo wa kwanza dhidi ya Edomu la kale ulivyokuwa.—Ufunuo 18:4-8, 19-21.
5. Isaya sura ya 35 imekuwa na utimizo wa namna gani katika wakati wetu?
5 Namna gani sura ya 35 ya unabii wa Isaya, inayokazia shangwe? Huo pia umetimizwa katika wakati wetu. Namna gani? Umetimizwa katika kule kurudishwa kwa Israeli wa kiroho kutoka katika aina fulani ya mateka. Acheni tuchunguze mambo ya hakika katika ile ambayo kwa kweli ni historia ya kitheokrasi ya hivi majuzi, yaliyotendeka katika muda wa maisha ya wengi walio hai bado.
6. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba mabaki ya Israeli wa kiroho waliingia katika hali ya mateka?
6 Kwa muda mfupi kwa kulinganisha katika kipindi cha Vita ya Ulimwengu 1, mabaki ya Israeli wa kiroho hawakuwa wamejiweka safi kikamili na kupatanishwa na mapenzi ya Mungu. Baadhi yao walikuwa wametiwa mawaa kwa mafundisho bandia na kuacha msimamo wao kwa kutochukua msimamo wa wazi kwenye upande wa Yehova walipowekwa chini ya msongo wa kuunga mkono mataifa yenye kupiga vita. Katika miaka hiyo ya vita, walipatwa na namna zote za minyanyaso, hata fasihi zao za Biblia zikipigwa marufuku katika mahali pengi. Hatimaye, baadhi ya ndugu wenye umashuhuri zaidi walihukumiwa na kufungwa gerezani kwa mashtaka bandia. Kwa kufikiria yaliyotokea si vigumu kuona kwamba, kwa maana fulani, watu wa Mungu walikuwa katika hali ya mateka, badala ya kuwa huru. (Linganisha Yohana 8:31, 32.) Walikuwa na utovu mkubwa wa mwono wa kiroho. (Waefeso 1:16-18) Walionyesha hali ya kuwa bubu kwa kadiri fulani kwa habari ya kumsifu Mungu, kukiwa na tokeo la kwamba hawakuwa wenye kuzaa matunda kiroho. (Isaya 32:3, 4; Warumi 14:11; Wafilipi 2:11) Je, waona jinsi hii inavyolingana na hali ya Wayahudi wa kale katika hali ya mateka Babiloni?
7, 8. Mabaki wa siku ya kisasa waliona kurudishwa kwa aina gani?
7 Lakini je, Mungu angewaacha watumishi wake wa siku ya kisasa wakiwa katika hali hiyo? La, yeye aliazimia kuwarudisha, kwa kupatana na yale yaliyotabiriwa kupitia Isaya. Hivyo unabii uo huo katika sura ya 35 wapata utimizo dhahiri katika wakati wetu, kwa kule kurudishwa kwa mabaki ya Israeli wa kiroho kwenye ufanisi na afya katika paradiso ya kiroho. Kwenye Waebrania 12:12, Paulo alitumia Isaya 35:3 katika maana ya kitamathali, akiunga mkono usahihi wa kufanya kwetu matumizi ya kiroho kwa sehemu hii ya unabii wa Isaya.
8 Katika kipindi cha baada ya vita, ilikuwa kana kwamba wale wanaobaki wa watiwa-mafuta wa Israeli wa kiroho walitoka katika hali ya mateka. Yehova Mungu alimtumia Yesu Kristo, yule Sairasi Mkubwa, kuwaweka huru. Hivyo, hawa mabaki waliweza kufanya kazi ya kujenga upya, iliyofanana na kazi ya mabaki ya Wayahudi wa kale, ambao walirudi bara lao ili kujenga upya hekalu halisi Yerusalemu. Zaidi ya hayo, Waisraeli hawa wa kiroho katika nyakati za kisasa waliweza kuanza kusitawisha na kutokeza paradiso ya kiroho yenye mimea mibichi, bustani ya Edeni ya kitamathali.
9. Jambo fulani kama lile lililofafanuliwa kwenye Isaya 35:1, 2, 5-7 lilisitawikaje katika wakati wetu?
9 Kwa kuyafikiria yaliyo juu, acheni tuchunguze mara nyingine tena Isaya sura ya 35, na tutazame kwanza mstari wa 1 na wa 2. Mahali palipoonekana kuwa mkoa usio na maji kwa kweli palianza kuchanua maua na kuwa penye kutokeza matunda kama vile nyanda za kale za Sharoni. Kisha, angalia mstari wa 5 hadi wa 7. Wale mabaki, ambao baadhi yao bado wako hai na wenye kutenda katika utumishi wa Yehova, walifunguliwa macho ya uelewevu. Waliweza kuona vizuri zaidi maana ya yale yaliyokuwa yametendeka mwaka 1914 na baadaye. Hilo limekuwa pia na uvutano juu ya wengi wetu tufanyizao “umati mkubwa,” unaotumikia sasa pamoja na mabaki.—Ufunuo 7:9, NW.
Je, Wewe Ni Sehemu ya Huo Utimizo?
10, 11. (a) Umehusikaje katika utimizo wa Isaya 35:5-7? (b) Wewe binafsi unahisije kuhusu mabadiliko hayo?
10 Kwa kielelezo jifikirie mwenyewe. Kabla ya kukutana na Mashahidi wa Yehova, je, ulisoma Biblia kwa ukawaida? Ikiwa ulifanya hivyo, ulikuwa na uelewevu kiasi gani? Mathalani, sasa wajua kweli kuhusu hali ya wafu. Labda ungeweza kumrejeza mtu fulani mwenye kupendezwa na jambo hilo kwenye maandiko yanayohusu hilo katika Mwanzo sura ya 2, Mhubiri sura ya 9, na Ezekieli sura ya 18, na pia kwenye mafungu mengine mengi. Ndiyo, yaelekea waelewa yale ambayo Biblia hufundisha juu ya mambo au masuala mengi. Kwa kusema kwa usahili, Biblia ina maana kwako, nawe waweza kuwaeleza wengine mengi juu yayo, kama vile bila shaka umefanya.
11 Lakini, kila mmoja wetu angefanya vema kuuliza hivi, ‘Nilijifunzaje yote ninayojua kuhusu kweli ya Biblia? Kabla ya kujifunza pamoja na watu wa Yehova, je, nilikuwa nimeyapata mafungu hayo yote ambayo yametoka tu kutajwa? Je, nilikuwa nimeelewa maana yayo na kufikia mikataa iliyo sawa juu ya maana yayo?’ Jibu la unyoofu kwa maswali hayo laelekea ni la. Hakuna mtu apaswaye kuudhika na maneno hayo, lakini yaweza kusemwa kwamba kwa msingi ulikuwa kipofu kwa habari ya maandiko hayo na maana yayo. Sivyo? Yalikuwa humo katika Biblia, lakini hukuweza kuyafahamu, wala kuelewa umaana wayo. Kwa hiyo, macho yako yalifunguliwaje kiroho? Ilikuwa ni kwa lile ambalo Yehova amefanya katika kutimiza Isaya 35:5 juu ya mabaki watiwa-mafuta. Kisha umefunguliwa macho yako. Humo tena katika giza la kiroho. Wewe waweza kuona.—Linganisha Ufunuo 3:17, 18.
12. (a) Kwa nini twaweza kusema kwamba huu si wakati wa uponyaji wa kimwili wa kimuujiza? (b) Hali ya Ndugu F. W. Franz ilionyeshaje njia ambayo Isaya 35:5 linatimizwa katika wakati wetu?
12 Wanafunzi wenye bidii wa Biblia na wa shughuli za Mungu katika muda wote wa karne ambazo zimepita wanajua kwamba hiki si kipindi katika historia cha miujiza ya uponyaji wa kimwili. (1 Wakorintho 13:8-10) Kwa hiyo hatumtazamii Yesu Kristo kuwa akifumbua macho yaliyopofuka katika kuthibitisha kwamba yeye ndiye Mesiya, Nabii wa Mungu. (Yohana 9:1-7, 30-33) Wala yeye hawawezeshi viziwi wote wasikie tena. Frederick W. Franz, mmoja wa watiwa-mafuta na msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, alipokaribia umri wa miaka 100, alikuwa karibu kipofu na alihitaji kutumia kifaa cha kumsaidia asikie. Kwa miaka kadhaa yeye hakuweza kuona tena ili kusoma; hata hivyo, ni nani ambaye angemwona kuwa kipofu au kiziwi katika maana ya Isaya 35:5? Mwono wake mkali wa kiroho ulikuwa baraka kwa watu wa Mungu duniani pote.
13. Watu wa Mungu wa siku ya kisasa waliona kugeuzwa au kurudishwa kupi kwa hali?
13 Au namna gani ulimi wako? Huenda ikawa watiwa-mafuta wa Mungu walikuwa bubu wakati wa hali yao ya mateka ya kiroho. Lakini mara Mungu alipogeuza hali hiyo, ndimi zao zilianza kulia kwa furaha juu ya yale waliyojua kuhusu Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na ahadi zake kwa wakati ujao. Huenda ikawa wamekusaidia uufungue ulimi wako pia. Ulisema na wengine juu ya kweli ya Biblia kwa kadiri gani katika wakati uliopita? Labda kwa hatua fulani ulifikiri, ‘Nafurahia kujifunza, lakini sitaenda kamwe kuongea na watu nisiowajua?’ Hata hivyo, je, si kweli kwamba “ulimi wake aliye bubu” sasa ‘unaimba kwa furaha’?—Isaya 35:6.
14, 15. Wengi wametembeaje katika “Njia ya Utakatifu” katika wakati wetu?
14 Wayahudi wa kale waliowekwa huru kutoka Babiloni walikuwa na safari ndefu ya kurudi bara lao. Hilo linalingana na nini katika wakati wetu? Angalia Isaya 35:8, (NW): “Kwa hakika kutakuja kuwa na njia kuu huko, hata njia; na hiyo itaitwa Njia ya Utakatifu. Na yule asiye safi hataipitia.”
15 Tangu kuachiliwa kwao kutoka katika hali ya mateka ya kiroho, mabaki ya watiwa-mafuta, wanaoandamana sasa na mamilioni ya kondoo wengine, wametoka Babiloni Mkubwa katika njia kuu ya kitamathali, njia safi ya utakatifu imwongozayo mtu kwenye paradiso ya kiroho. Tunajitahidi kwa kila njia kustahili kuwa katika hii Njia ya Utakatifu na kuendelea kuwa katika hiyo. Jifikirie mwenyewe. Je, viwango vyako vya kiadili na kanuni unazoshikamana nazo si za juu zaidi sasa kuliko wakati ulipokuwa ulimwenguni? Je, wewe hujitahidi zaidi sana ili kupatanisha kufikiri kwako na mwenendo wako na wa Mungu?—Warumi 8:12, 13; Waefeso 4:22-24.
16. Twaweza kufurahia hali zipi tutembeapo kwenye Njia ya Utakatifu?
16 Uendeleapo katika hii Njia ya Utakatifu, kwa msingi wewe huna wasiwasi juu ya wanadamu wa kihayawani. Ni kweli, ulimwenguni unahitaji kuwa macho kwamba watu wenye pupa au wenye chuki hawakunyafui kitamathali. Watu wengi sana ni wakali katika njia wanayoshughulika na wengine. Ni tofauti kama nini miongoni mwa watu wa Mungu! Humo umo katika mazingira yenye ulinzi. Bila shaka, Wakristo wenzako si wakamilifu; nyakati nyingine mmoja hukosea au huudhi. Lakini wajua kwamba ndugu zako hawana nia ya kukuumiza au kukunyafua. (Zaburi 57:4; Ezekieli 22:25; Luka 20:45-47; Matendo 20:29; 2 Wakorintho 11:19, 20; Wagalatia 5:15) Badala ya hivyo, wao huonyesha kupendezwa nawe; wamekusaidia; wanataka kutumikia pamoja nawe.
17, 18. Ni katika maana gani kwamba paradiso iko sasa, na hilo lina tokeo gani juu yetu?
17 Kwa hiyo twaweza kuangalia Isaya sura ya 35, tukifikiria utimizo wa wakati huu wa mstari wa 1 hadi wa 8. Je, si wazi kwamba tumepata ile ambayo huitwa kwa kufaa paradiso ya kiroho? La, haijakamilika—bado. Lakini kwa kweli ni paradiso, kwa maana, hapa twaweza tayari ‘kuona utukufu wa Yehova, uzuri wa Mungu wetu,’ kama vile isemwavyo katika mstari wa 2, (NW). Na tokeo ni nini? Mstari wa 10 (NW) wasema hivi: “Wale wenyewe waliokombolewa na Yehova watarudi na kwa hakika watakuja Zayoni kwa kilio chenye shangwe; na kushangilia hadi wakati usio dhahiri kutakuwa juu ya kichwa chao. Wao watapata mchachawo na kushangilia, na huzuni na kupiga kite lazima zikimbie mbali.” Kwa kweli, kule kutoka kwetu katika dini bandia na kufuatia kwetu ibada ya kweli chini ya upendeleo wa Mungu ni jambo lenye kuchochea shangwe.
18 Shangwe inayohusiana na ibada ya kweli huzidi kuongezeka, sivyo? Waona wale wenye kupendezwa karibuni wakifanya mabadiliko na kuwa imara katika kweli ya Biblia. Waona vijana wakikua na kufanya maendeleo ya kiroho kutanikoni. Kuna ubatizo, ambapo waona wale unaowajua wakibatizwa. Je, hizo si sababu za shangwe, za shangwe nyingi, leo? Ndiyo, ni shangwe iliyoje kwa wengine kuungana nasi katika uhuru wetu wa kiroho na hali za paradiso!
Utimizo Ulio Mbele Bado!
19. Isaya sura ya 35 inatujaza tazamio gani lenye tumaini?
19 Kufikia sasa tumechunguza Isaya sura ya 35 kwa habari ya utimizo wayo wa kwanza wa kurudi kwa Wayahudi na kwa habari ya utimizo wa kiroho unaoendelea leo. Lakini huo sio mwisho. Kuna mengi zaidi. Unahusiana na uhakikishio wa Kibiblia wa kurudisha kunakokuja kwa hali za paradiso halisi duniani.—Zaburi 37:10, 11; Ufunuo 21:4, 5.
20, 21. Kwa nini ni jambo la kiakili na la Kimaandiko kuamini kwamba kutakuwa bado na utimizo mwingine wa Isaya sura ya 35?
20 Lisingekuwa jambo la kupatana kwa Yehova kuandaa mafafanuzi ya wazi kuhusu paradiso kisha azuie utimizo huo mbalimbali kwa mambo ya kiroho pekee. Bila shaka, hilo si kusema kwamba utimizo mbalimbali wa kiroho si wa maana. Hata ikiwa paradiso halisi ingesimamishwa, hiyo isingeturidhisha ikiwa miongoni mwa mandhari nzuri na wanyama wenye amani tungezungukwa na watu walio wafisadi kiroho, wanadamu wenye kutenda kama hayawani wakali. (Linganisha Tito 1:12.) Ndiyo, lazima utimizo wa kiroho uje kwanza, kwani ni wa maana zaidi.
21 Hata hivyo, Paradiso inayokuja haifiki mwisho kwenye hali za kiroho tunazofurahia sasa na ambazo tutafurahia hata zaidi wakati ujao. Tuna sababu nzuri ya kutazamia utimizo halisi wa unabii mbalimbali kama vile Isaya sura ya 35. Kwa nini? Katika sura ya 65 (NW) Isaya alitabiri “mbingu mpya na dunia mpya.” Mtume Petro alitumia andiko hilo alipofafanua yale yanayofuata siku ya Yehova. (Isaya 65:17, 18; 2 Petro 3:10-13) Petro alikuwa akionyesha kwamba mambo ambayo Isaya alifafanua yangekuwako kwa kweli wakati “dunia mpya” inapokuwa uhalisi. Hilo latia ndani mafafanuzi ambayo huenda ukayafahamu—kujenga nyumba na kukaa ndani yazo; kupanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yayo; mtu kufurahia kwa muda mrefu kazi ya mikono yake; mbwa-mwitu na mwana-kondoo wakikaa pamoja; na hakuna madhara yatokeayo duniani pote. Yaani, maisha marefu, makao yaliyo salama, chakula kingi, kazi yenye kuridhisha, na amani miongoni mwa wanyama na kati ya wanyama na wanadamu.
22, 23. Kutakuwa na msingi gani wa shangwe katika utimizo wa wakati ujao wa Isaya sura ya 35?
22 Je, taraja hilo halikujazi shangwe? Lapaswa kufanya hivyo, kwa maana hivyo ndivyo Mungu alivyotuumba tuishi. (Mwanzo 2:7-9) Kwa hiyo, yamaanisha nini kwa habari ya unabii katika Isaya sura ya 35 tunayochunguza? Yamaanisha kwamba tuna sababu zaidi ya kulia kwa shangwe. Majangwa halisi na mikoa isiyo na maji itachanua maua, ikitufanya tushangilie. Ndipo watu wenye macho ya buluu, au ya kahawia, au ya rangi nyingine yenye kupendeza, lakini ambao ni vipofu sasa, wataweza kuona. Wakristo wenzetu walio viziwi, au hata wale kati yetu tulio na ugumu wa kusikia, tutaweza kusikia kwa wazi. Ni shangwe kama nini kutumia uwezo huo ili kusikia Neno la Mungu likisomwa na kuelezwa, na pia kusikiliza sauti za upepo ukiwa mitini, za kicheko cha mtoto, za wimbo wa ndege!
23 Itamaanisha pia kwamba walemavu, kutia na wale wanaoathiriwa na ugonjwa wa yabisi kavu sasa, watatembea huku na huku bila maumivu yoyote. Ni kitulizo kilichoje! Wakati huo mabubujiko halisi ya maji yatapitia majangwa kwa kishindo. Tutayaona maji hayo yenye mawimbi na pia kusikia sauti ya kububujika. Tutaweza kutembea hapo na kugusa nyasi mbichi na mimea ya mafunjo. Kwa kweli itakuwa Paradiso iliyorudishwa. Namna gani ile shangwe ya kuwa karibu na simba au mnyama mwingine wa jinsi hiyo bila hofu? Hatuhitaji kuanza kufafanua hilo, kwani tayari sisi sote tumewazia na kufurahia mandhari hiyo.
24. Kwa nini waweza kukubaliana na usemi katika Isaya 35:10 (NW)?
24 Isaya atuhakikishia hivi: “Wale wenyewe waliokombolewa na Yehova watarudi na kwa hakika watakuja Zayoni kwa kilio chenye shangwe; na kushangilia hadi wakati usio dhahiri kutakuwa juu ya kichwa chao.” Kwa hiyo twaweza kukubali kwamba tuna sababu ya kulia kwa shangwe. Shangwe juu ya yale ambayo tayari Yehova anawafanyia watu wake katika paradiso yetu ya kiroho, na shangwe juu ya yale tuwezayo kutazamia katika ile Paradiso halisi iliyo karibu. Kuhusu wale wenye shangwe—kuhusu sisi—Isaya aandika hivi: “Wao watapata mchachawo na kushangilia, na huzuni na kupiga kite lazima zikimbie mbali.”—Isaya 35:10, NW.
-