Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nuru kwa Mataifa
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • [Sanduku katika ukurasa wa 409]

      Zawadi Zilizotiwa Mafuta za Kumpa Yehova Kutoka Katika Mataifa Yote

      Mwaka wa 1920, Juan Muñiz aliondoka Marekani kwenda Hispania kisha akasonga mbele na safari yake hadi Argentina, ambako aliyapanga kitengenezo makutaniko ya watiwa-mafuta. Kuanzia mwaka wa 1923 na kuendelea, nuru ya kweli iling’aa juu ya wenye mioyo minyoofu katika Afrika Magharibi wakati mishonari William R. Brown (ambaye mara nyingi aliitwa Bible Brown) aliposhika njia kwenda kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika sehemu kama vile Sierra Leone, Ghana, Liberia, Gambia, na Nigeria. Mwaka huo huo George Young wa Kanada aliteremka Brazil, kisha akasonga mbele kwenda Argentina, Costa Rica, Panama, Venezuela, na hata Muungano wa Sovieti. Karibu na wakati huo huo, Edwin Skinner alisafiri baharini kutoka Uingereza hadi India, na huko akajikakamua muda wa miaka mingi katika kazi ya mavuno.

      [Picha katika ukurasa wa 411]

      Wayahudi fulani waliokuwa kwenye Pentekoste walikuwa ‘ndugu kutoka mataifa yote’

      [Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 413]

  • Nuru kwa Mataifa
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • 9. Yehova anatangaza habari njema zipi?

      9 Je, kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. kunamaanisha kwamba Yehova hatakuwa tena na mashahidi duniani? Sivyo. Watu walio na uaminifu-maadili wenye kutokeza, kama vile Danieli na waandamani wake watatu, wataendelea kumtumikia Yehova hata wakiwa wahamishwa Babiloni. (Danieli 1:6, 7) Naam, ule mfuatano wa mashahidi wengi waaminifu wa Yehova utabaki hivyo hivyo, na mwishoni mwa miaka 70, wanaume na wanawake waaminifu wataondoka Babiloni kurudi Yuda ili kuirudisha ibada safi huko. Hilo ndilo jambo ambalo sasa Yehova anagusia: “Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa.”—Isaya 66:19.

      10. (a) Wayahudi waaminifu waliokombolewa Babiloni watakuwaje ishara? (b) Ni nani leo wanaokuwa ishara?

      10 Kundi la wanaume na wanawake waaminifu wanaorudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. litatumika likiwa ishara ya kugutusha, ushuhuda wa kwamba Yehova amewakomboa watu wake. Ni nani angaliwaza kwamba siku moja Wayahudi mateka wangekuwa huru ili kufuatia ibada safi kwenye hekalu la Yehova? Hali kadhalika, katika karne ya kwanza Wakristo watiwa-mafuta ndio waliokuwa “ishara na ajabu,” nao walimiminikiwa na watu watiifu waliotaka kumtumikia Yehova. (Isaya 8:18; Waebrania 2:13) Leo Wakristo watiwa-mafuta, wanaopata ufanisi katika nchi yao iliyorudishiwa hali nzuri, wanakuwa kama ishara ya kugutusha duniani. (Isaya 66:8) Wao ni ushuhuda halisi wa kuonyesha kwamba roho ya Yehova ina nguvu za kuvuta watu watiifu wanaosukumwa na mioyo yao kumtumikia Yehova.

      11. (a) Baada ya kurudishwa, itakuwaje kwamba watu wa mataifa watakuja kujifunza habari za Yehova? (b) Andiko la Zekaria 8:23 lilitimizwaje mara ya kwanza?

      11 Lakini, baada ya kurudishwa mwaka wa 537 K.W.K., watu wa mataifa ambao hawajawahi kuisikia habari za Yehova watamjuaje? Si Wayahudi wote waaminifu watakaorudi Yerusalemu mwishoni mwa utekwa wa Kibabiloni. Wengine, kama vile Danieli, watabaki Babiloni. Na wengine zaidi watatawanyika hadi pembe nne za dunia. Kufikia karne ya tano K.W.K., sehemu zote za Milki ya Uajemi zilikuwa na Wayahudi. (Esta 1:1; 3:8) Bila shaka wengine wao waliwaeleza majirani zao wapagani habari za Yehova, kwa maana wengi kutoka mataifa hayo walikuja kuwa waongofu Wayahudi. Inaonekana hata yule towashi Mwethiopia aliyehubiriwa na Filipo mwanafunzi Mkristo katika karne ya kwanza alikuwa mwongofu. (Matendo 8:26-40) Yote hayo yalitukia yakiwa utimizo wa kwanza wa maneno ya nabii Zekaria: “Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Kwa kweli, Yehova aliyapelekea mataifa nuru!—Zaburi 43:3.

      ‘Kumletea Yehova Zawadi’

      12, 13. Kuanzia mwaka wa 537 K.W.K., “ndugu” wataletwa Yerusalemu kwa njia gani?

      12 Baada ya Yerusalemu kujengwa upya, Wayahudi waliotawanyika mbali sana na nchi yao wataelekeza fikira na mtazamo wao kwenye jiji hilo pamoja na ukuhani wake uliorudishwa likiwa kituo cha ibada safi. Wengi wao watasafiri mbali kuhudhuria sherehe za kila mwaka huko. Isaya anaandika hivi kwa kupuliziwa: “Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka [“zawadi,” “NW”] kwa BWANA, juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema BWANA; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka [“zawadi,” “NW”] yao nyumbani kwa BWANA katika chombo safi. Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi.”—Isaya 66:20, 21.

      13 Wengine wa hao ‘ndugu kutoka mataifa yote’ walikuwako siku ya Pentekoste wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi wa Yesu. Masimulizi hayo yanasema hivi: “Kulikuwa na Wayahudi wakikaa katika Yerusalemu, wanaume wenye kumhofu Mungu, kutoka kila taifa la yale yaliyo chini ya mbingu.” (Matendo 2:5) Walikuja Yerusalemu kuabudu kulingana na desturi ya Kiyahudi, lakini walipozisikia habari njema juu ya Yesu Kristo, wengi walionyesha wazi kwamba wanamwamini kisha wakabatizwa.

      14, 15. (a) Wakristo watiwa-mafuta waliwakusanyaje wengi wa “ndugu” zao wa kiroho baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, nao waliletwaje kwa Yehova wakiwa ‘zawadi katika chombo safi’? (b) Yehova ‘alitwaa baadhi ya hao kuwa makuhani’ jinsi gani? (c) Ni akina nani waliokuwa baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta waliohusika katika kukusanya ndugu zao wa kiroho? (Ona sanduku katika ukurasa huu.)

      14 Je, unabii huu una utimizo wa kisasa? Tena sana. Baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walitambua kutokana na Maandiko kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa umeanzishwa mbinguni mwaka wa 1914. Kupitia funzo la uangalifu la Biblia, walijifunza kwamba warithi wa ziada wa Ufalme, au akina “ndugu,” walipasa kukusanywa. Wahudumu hodari walisafiri “hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia,” wakitumia usafiri wa kila namna ili kuwatafuta wale waliotazamiwa kuwa washirika wa mabaki-watiwa mafuta, wengi wao wakitoka kwenye makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Walipopatikana, waliletwa wawe zawadi kwa Yehova.—Matendo 1:8.

      15 Watiwa-mafuta waliokusanywa miaka ya mapema hawakumtazamia Yehova awakubali wakiwa na hali waliyokuwa nayo kabla ya kuujua ukweli wa Biblia. Walichukua hatua za kujisafisha uchafu wa kiroho na wa kiadili ili waweze kutolewa wawe ‘zawadi katika chombo safi,’ au kama ilivyotajwa na mtume Paulo, wawe “bikira safi kiadili kwa Kristo.” (2 Wakorintho 11:2) Zaidi ya kukataa kosa la kimafundisho, watiwa-mafuta walilazimika kujifunza jinsi ya kudumisha msimamo wa kutokuwamo kabisa katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu. Mwaka wa 1931, watumishi wake walipokuwa wamesafishwa kwa kiasi kinachofaa, Yehova aliwaonyesha neema kwa kuwapa pendeleo la kubeba jina lake wakiwa Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10-12) Ingawa hivyo, Yehova ‘aliwatwaa baadhi yao kuwa makuhani’ jinsi gani? Wakiwa kikundi, watiwa-mafuta hawa wanakuwa sehemu ya “ukuhani wa kifalme, taifa takatifu,” wakimtolea Mungu dhabihu za sifa.—1 Petro 2:9; Isaya 54:1; Waebrania 13:15.

      Ukusanyaji Waendelea

      16, 17. Ni nani wale wanaoitwa “uzao wenu” baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu?

      16 Idadi kamili ya huo “ukuhani wa kifalme” ni 144,000, na baada ya muda, kazi ya kuwakusanya ilimalizika. (Ufunuo 7:1-8; 14:1) Je, huo ulikuwa mwisho wa kazi ya kukusanya? Sivyo. Unabii wa Isaya unaendelea kusema hivi: “Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.” (Isaya 66:22) Katika utimizo wa kwanza wa maneno hayo, Wayahudi wanaorudi kutoka kwenye utekwa wa Babiloni wataanza kulea watoto. Kwa njia hiyo, mabaki ya Wayahudi waliorudishwa, yaani ile “dunia mpya,” wakiwa chini ya usimamizi mpya wa Kiyahudi, yaani “mbingu mpya,” wataimarika sana. Hata hivyo, unabii huo umekuwa na utimizo wenye kutokeza sana katika siku zetu.

      17 “Uzao” ambao taifa la ndugu za kiroho wanautokeza ni “umati mkubwa,” walio na tumaini la uhai wa milele duniani. Wao ‘hutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,’ na husimama “mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.” “Wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:9-14; 22:17) Leo wale walio “umati mkubwa” wanaepuka giza la kiroho na kuja kwenye nuru ambayo Yehova huandaa. Wanaonyesha imani katika Yesu Kristo, na wanajitahidi kubaki wakiwa safi kiroho na kiadili kama ndugu na dada zao watiwa-mafuta. Wakiwa kikundi, wanaendelea kutumikia chini ya mwelekezo wa Kristo na ‘watakaa’ milele!—Zaburi 37:11, 29.

      18. (a) Washirika wa umati mkubwa wameenenda kama ndugu zao watiwa-mafuta jinsi gani? (b) Watiwa-mafuta na waandamani wao humwabudu Yehova “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato” jinsi gani?

      18 Wanaume na wanawake hawa wenye bidii walio na tumaini la kidunia wanajua kwamba ingawa ni muhimu kubaki safi kiadili na kiroho, mengi zaidi yanahusika ili kumfurahisha Yehova. Kazi ya ukusanyaji inavuma, nao wanataka kuishiriki. Kitabu cha Ufunuo kinatoa unabii huu kuwahusu: “Wako mbele ya hicho kiti cha ufalme cha Mungu; nao wanamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufunuo 7:15) Maneno hayo yanatukumbusha mstari wa pili kutoka mwisho wa unabii wa Isaya: “Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema BWANA.” (Isaya 66:23) Jambo hilo linatendeka leo. “Mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato,” yaani, kwa ukawaida, kila juma la kila mwezi, Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, yaani ule umati mkubwa, hukutanika kumwabudu Yehova. Njia mojawapo ambayo wanafanya hivyo ni kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki katika huduma ya peupe. Je, wewe ni mmoja wa wale ‘wanaokuja kuabudu mbele za Yehova’? Watu wa Yehova wanapata shangwe kubwa wanapofanya hivyo, na wale wa umati mkubwa wanautazamia wakati ambao “wanadamu wote,” watamtumikia Yehova “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato” kwa umilele wote.

      Mwisho Kamili wa Adui za Mungu

      19, 20. Gehena ilitumika kwa kusudi gani nyakati za Biblia, na inafananisha nini?

      19 Mstari mmoja unabaki katika funzo letu la unabii wa Isaya. Kitabu kinafikia mwisho kwa kusema hivi: “Watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.” (Isaya 66:24) Inaelekea kwamba Yesu Kristo alikuwa akiufikiria unabii huu alipowahimiza wanafunzi wake kurahisisha maisha yao na kuweka masilahi ya Ufalme kwanza. Alisema hivi: “Ikiwa jicho lako lakufanya ukwazike, litupilie mbali; ni bora zaidi kwako kuingia katika ufalme wa Mungu ukiwa na jicho moja kuliko kutupwa ndani ya Gehena ukiwa na macho mawili, mahali ambapo funza wao hafi na ule moto hauzimwi.”—Marko 9:47, 48; Mathayo 5:29, 30; 6:33.

      20 Ni mahali gani hapa panapoitwa Gehena? Karne nyingi zilizopita, msomi Myahudi David Kimhi aliandika hivi: “Hapo ni mahali . . . ambapo pamepakana na Yerusalemu, tena ni mahali pa kuchukiza sana, na watu hutupa humo vitu vichafu na mizoga. Vilevile, humo mlikuwa na moto ulioendelea kuwaka ili kuchoma vitu vichafu na mifupa ya mizoga. Kwa hiyo, hukumu ya waovu huitwa Gehinnom kwa njia ya mfano.” Ikiwa, kama vile msomi huyu Myahudi anavyodokeza, Gehena ilitumiwa kama mahali pa kutupia takataka na mizoga ya wale walioonwa hawastahili kuzikwa, basi moto ungekuwa kitu kinachofaa cha kumaliza takataka hizo. Kisichoteketezwa na moto, kingeliwa na funza. Hiyo inaonyesha vizuri kama nini mwisho kamili utakaowapata adui za Mungu!b

      21. Kitabu cha Isaya kinafikia mwisho mzuri kuhusiana na akina nani, na kwa nini?

      21 Kwa sababu ya kutaja maiti, moto, na funza, je, si kweli kwamba unabii wenye kusisimua wa Isaya unamalizika kwa njia ya kutisha? Hakuna shaka kwamba maadui sugu wa Mungu watafikiri hivyo. Lakini uharibifu wa milele wa waovu ni kitia-moyo kweli kweli kwa marafiki wa Mungu. Watu wa Yehova wanahitaji uhakikisho huo kwamba sasa adui zao hawatawaweza tena. Maadui hao, ambao wamewatesa sana watu wa Mungu na kuliletea jina lake suto kubwa, wataharibiwa milele. Halafu, “mateso hayatainuka mara ya pili.”—Nahumu 1:9.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki