Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mimi Nipo Pamoja Nanyi”
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 15
    • “Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

      “Mjumbe wa Yehova akaendelea kuwaambia: . . . ‘“Mimi nipo pamoja nanyi,” asema Yehova.’”—HAGAI 1:13.

      1. Yesu alizungumzia unabii gani unaohusu nyakati zetu?

      TUNAISHI wakati muhimu katika historia. Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tangu mwaka wa 1914 tumekuwa katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Huenda umejifunza unabii mbalimbali kuhusu “siku [hiyo] ya Bwana.” Hivyo, unajua kwamba Yesu alisema “siku za Mwana wa binadamu” katika mamlaka ya Ufalme ni kama “siku za Noa” na “siku za Loti.” (Luka 17:26, 28) Biblia inaonyesha kwamba mambo yaliyotukia siku za Noa na za Loti ni unabii unaohusu nyakati zetu. Hata hivyo, kuna unabii mwingine kuhusu nyakati zetu ambao tunapaswa kufikiria kwa uzito.

      2. Yehova aliwapa Hagai na Zekaria kazi gani?

      2 Acheni tuzungumzie hali fulani iliyokuwapo katika siku za manabii Waebrania, Hagai na Zekaria. Manabii hao wawili waaminifu walikuwa na ujumbe gani ambao unahusu watu wa Yehova wa siku zetu? Hagai na Zekaria walikuwa ‘wajumbe wa Yehova’ kwa Wayahudi waliorudi kutoka utekwani Babiloni. Walipewa utume wa kuwahakikishia Waisraeli kwamba Mungu angewategemeza katika kazi ya kujenga upya hekalu. (Hagai 1:13; Zekaria 4:8, 9) Ingawa vitabu ambavyo Hagai na Zekaria waliandika ni vifupi, vitabu hivyo ni sehemu ya “andiko lote [ambalo] limeongozwa na roho ya Mungu [na] lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”—2 Timotheo 3:16.

      Tunapaswa Kukazia Fikira Unabii Huo

      3, 4. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na ujumbe wa Hagai na Zekaria?

      3 Bila shaka, ujumbe wa Hagai na Zekaria uliwafaidi Wayahudi wa siku zao, na unabii wao ulitimizwa kwa kiasi fulani wakati huo. Hata hivyo, tunawezaje kuwa na hakika kwamba vitabu hivyo viwili vinatuhusu leo? Andiko la Waebrania 12:26-29 linatusaidia kupata jibu. Hapo mtume Paulo ananukuu andiko la Hagai 2:6 linalosema kwamba Mungu ‘anatikisa mbingu na dunia.’ Mwishowe, kutikisa huko ‘kutakipindua kiti cha falme na kuangamiza nguvu za falme za mataifa.’—Hagai 2:22.

      4 Anaponukuu Hagai, Paulo anaeleza kile kitakachopata “falme za mataifa” na anakazia ukuu wa Ufalme usiotikisika ambao Wakristo watiwa-mafuta watapokea. (Waebrania 12:28) Basi, maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba unabii wa Hagai na Zekaria unahusu kipindi cha baadaye, baada ya kitabu cha Waebrania kuandikwa katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida. Bado kungali na mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta duniani leo, ambao watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa Kimasihi. Hivyo, unabii wa Hagai na Zekaria unahusu nyakati zetu.

      5, 6. Ni mambo gani yaliyotukia kabla ya unabii wa Hagai na Zekaria?

      5 Kitabu cha Ezra kinaeleza mambo yaliyotukia kabla ya unabii wa Hagai na Zekaria. Baada ya Wayahudi kurudi kutoka utekwani Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua (au Yeshua) walisimamia kuwekwa kwa msingi wa hekalu jipya mwaka wa 536 K.W.K. (Ezra 3:8-13; 5:1) Ingawa tukio hilo lilipaswa kutokeza shangwe nyingi, baada ya muda Wayahudi walianza kuogopa. Andiko la Ezra 4:4 linasema kwamba adui, au ‘watu wa nchi walizidi kuilegeza mikono ya watu wa Yuda na kuwavunja moyo wasijenge.’ Adui hao, hasa Wasamaria, walitoa madai ya uwongo dhidi ya Wayahudi. Wapinzani hao walimchochea mfalme wa Uajemi apige marufuku ujenzi wa hekalu.—Ezra 4:10-21.

      6 Bidii ya kazi ya ujenzi ilididimia. Wayahudi wakafuatia mambo ya kibinafsi. Hata hivyo, mwaka wa 520 K.W.K., miaka 16 baada ya kuwekwa kwa msingi wa hekalu, Yehova aliwatuma Hagai na Zekaria ili wawahimize watu waanze tena kulijenga hekalu. (Hagai 1:1; Zekaria 1:1) Kwa kuwa Wayahudi walichochewa na wajumbe wa Mungu na kuthibitishiwa kwamba Yehova angewasaidia, walianza tena kazi ya kujenga hekalu, nao wakalimaliza mwaka wa 515 K.W.K.—Ezra 6:14, 15.

      7. Hali katika siku za Hagai na Zekaria zinalinganaje na hali za leo?

      7 Je, unajua mambo yote hayo yanatuhusuje? Tuna kazi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Kazi hiyo ilitiliwa maanani zaidi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kama vile Wayahudi wa kale walivyowekwa huru kutoka utekwani Babiloni, watu wa Yehova wa leo waliwekwa huru kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini za uwongo. Watiwa-mafuta wa Mungu walifanya kwa bidii kazi ya kuhubiri, kufundisha, na kuelekeza watu kwenye ibada ya kweli. Kazi hiyo inaendelea leo kwa kadiri kubwa hata zaidi, na huenda unaifanya. Huu ndio wakati wa kuifanya kwa kuwa mwisho wa mfumo huu mbovu uko karibu! Lazima kazi hiyo tuliyopewa na Mungu iendelee mpaka aingilie kati shughuli za wanadamu wakati wa “dhiki kuu.” (Mathayo 24:21) Wakati huo uovu utakomeshwa, na hilo litawezesha ibada ya kweli kusitawi kila mahali duniani.

      8. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatusaidia katika kazi yetu?

      8 Kama vile unabii wa Hagai na Zekaria unavyoonyesha, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia na kutubariki tunapoendelea kufanya kazi hiyo kwa moyo wote. Licha ya jitihada za wengine za kuwazuia watumishi wa Mungu au kupiga marufuku kazi waliyopewa, hakuna serikali ambayo imefaulu kukomesha kazi ya kuhubiri. Fikiria jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi ya Ufalme kwa kuleta ongezeko kwa miaka mingi tangu Vita vya Kwanza vya Ulimwengu mpaka wakati huu. Lakini, bado kuna mengi ya kufanya.

      9. Tunapaswa kufikiria hali gani iliyotukia kale, na kwa nini?

      9 Mambo tunayojifunza katika unabii wa Hagai na Zekaria yanaweza kutuchocheaje hata zaidi kutii amri ya Mungu ya kuhubiri na kufundisha? Acheni tuone mambo kadhaa ambayo tunaweza kujifunza kutokana na vitabu hivyo viwili vya Biblia. Kwa mfano, fikiria mambo machache kuhusiana na kazi ya ujenzi wa hekalu ambayo Wayahudi waliorudishwa walipaswa kufanya. Kama ilivyotajwa, Wayahudi waliorudi Yerusalemu kutoka Babiloni hawakuendelea kufanya kazi ya ujenzi wa hekalu. Baada ya kuweka msingi wa hekalu, bidii yao ilididimia. Walianza kuwa na maoni gani yasiyofaa? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

      Maoni Yanayofaa Kuhusu Mali

      10. Wayahudi walisitawisha maoni gani yasiyofaa, na matokeo yakawaje?

      10 Wayahudi waliorudishwa walikuwa wakisema: “Wakati haujaja.” (Hagai 1:2) Walipoanza kazi ya kujenga hekalu, kwa kuweka msingi mwaka wa 536 K.W.K., hawakusema “wakati haujaja.” Lakini, baada ya muda usio mrefu waliruhusu upinzani kutoka kwa majirani na serikali uwaathiri. Wayahudi walianza kuhangaikia nyumba zao na starehe zao wenyewe. Kwa kuwa nyumba zao zilizofunikwa kwa mbao bora zilikuwa tofauti sana zikilinganishwa na hekalu ambalo halikuwa limemalizika, Yehova aliuliza hivi: “Je, huu ni wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenu zilizofunikwa kwa mbao, huku nyumba hii ikiwa imeharibika?”—Hagai 1:4.

      11. Kwa nini Yehova aliwashauri Wayahudi wa siku za Hagai?

      11 Naam, Wayahudi walibadili maoni yao kuhusu mambo yaliyo muhimu. Badala ya kutanguliza kusudi la Yehova la kujenga hekalu, watu wa Mungu walijihangaikia wenyewe na nyumba zao. Walipuuza ujenzi wa nyumba ya Mungu ya ibada. Neno la Yehova kwenye Hagai 1:5 liliwahimiza Wayahudi ‘waweke moyo wao juu ya njia zao.’ Yehova alitaka watafakari mambo waliyokuwa wakifanya na kufikiria hasara walizokuwa wakipata kwa sababu ya kutotanguliza ujenzi wa hekalu maishani mwao.

      12, 13. Andiko la Hagai 1:6 linaelezaje hali ya Wayahudi, na mstari huo unamaanisha nini?

      12 Kwa kuwa Wayahudi walitanguliza mambo yasiyofaa, walipata hasara wao wenyewe. Ona maoni ya Mungu kwenye Hagai 1:6: “Mmepanda mbegu nyingi, lakini mavuno ni kidogo. Mnakula chakula, lakini hamshibi. Mnakunywa, lakini hamlewi. Mnavaa nguo, lakini hakuna yeyote anayepata joto; na yeye anayeajiriwa, anaajiriwa kwa ajili ya mfuko wenye matundu.”

      13 Ingawa Wayahudi walikuwa katika nchi ambayo Mungu alikuwa amewapa, haikutokeza mazao kama walivyotazamia. Yehova hakuwabariki, kama alivyokuwa ameonya mapema. (Kumbukumbu la Torati 28:38-48) Bila msaada wake, Wayahudi walipanda mbegu lakini wakapata mavuno kidogo, naam, chakula kidogo ambacho hakikuwashibisha. Bila baraka zake, hawangeweza kujivika nguo zenye joto. Ni kana kwamba pesa walizochuma zilitiwa katika mfuko uliojaa matundu, kwa kuwa hazikuwafaidi wale waliozichuma. Namna gani maneno haya: “Mnakunywa, lakini hamlewi”? Kwa kuwa Mungu anashutumu ulevi, maneno hayo hayamaanishi kwamba kulewa kungeonyesha baraka zake. (1 Samweli 25:36; Methali 23:29-35) Badala yake, maneno hayo yanakazia tena jinsi Wayahudi walivyokosa baraka za Mungu. Kiasi chochote cha divai ambacho wangetengeneza kingekuwa kidogo, kisichoweza kulewesha. Biblia Habari Njema hutafsiri Hagai 1:6 hivi: “Mnakunywa divai, lakini hamtosheki.”

      14, 15. Tunajifunza nini katika Hagai 1:6?

      14 Mambo tunayojifunza kuhusu nyumba za Wayahudi, hayatufundishi kupamba nyumba. Muda mrefu kabla ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni, nabii Amosi aliwakemea matajiri katika Israeli kwa sababu ya “nyumba [zao] za pembe za tembo” na jinsi ‘walivyojilaza katika vitanda vya pembe za tembo.’ (Amosi 3:15; 6:4) Nyumba hizo zenye madoido na vyombo vya mbao vilivyopambwa hazikudumu. Vitu hivyo vyote viliporwa na maadui waliowashinda. Hata hivyo, miaka mingi baadaye, baada ya kuwa uhamishoni kwa miaka 70, wengi kati ya watu wa Mungu hawakuwa wamejifunza kutokana na matukio hayo. Je, sisi tutajifunza? Inafaa kila mmoja wetu ajiulize: ‘Mimi huhangaikia nyumba yangu na mapambo yake kwa kadiri gani? Namna gani kupata elimu ya ziada ili kupandishwa cheo kazini ingawa jambo hilo litanichukua miaka mingi na kunizuia nisifanye mambo muhimu ya kiroho?’—Luka 12:20, 21; 1 Timotheo 6:17-19.

      15 Mambo tunayoyasoma kwenye Hagai 1:6 yanapaswa kutuonyesha kwamba tunahitaji baraka za Mungu maishani mwetu. Wayahudi hao wa kale walikosa baraka hizo, nao wakaumia. Iwe tuna mali nyingi au la, tukikosa baraka za Yehova, hakuna shaka kwamba tutaathiriwa kiroho. (Mathayo 25:34-40; 2 Wakorintho 9:8-12) Lakini, tunaweza kupataje baraka hizo?

      Yehova Hutoa Msaada Kupitia Roho Yake

      16-18. Andiko la Zekaria 4:6 lilimaanisha nini kwa Wayahudi wa kale?

      16 Zekaria, aliyekuwa nabii kama Hagai, alichochewa kukazia njia ambayo Yehova alitumia kuwachochea na kuwabariki watu waliojitoa kwake wakati huo. Jambo hilo linaonyesha jinsi atakavyokubariki pia. Tunasoma hivi: “‘Si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho yangu,’ Yehova wa majeshi amesema.” (Zekaria 4:6) Huenda umesikia andiko hilo likinukuliwa mara nyingi, lakini lilimaanisha nini kwa Wayahudi wa siku za Hagai na Zekaria, nalo lina umuhimu gani kwako?

      17 Kumbuka kwamba maneno ya Hagai na Zekaria yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yalikuwa na matokeo mazuri wakati huo. Mambo ambayo manabii hao wawili walisema yaliwaimarisha Wayahudi waaminifu. Hagai alianza kutoa unabii katika mwezi wa sita, mwaka wa 520 K.W.K. Zekaria alianza kutoa unabii katika mwezi wa nane mwaka huohuo. (Zekaria 1:1) Kulingana na Hagai 2:18, kazi ya kuweka msingi ilianza tena kwa bidii katika mwezi wa tisa. Kwa hiyo, Wayahudi walichochewa kutenda, nao walimtii Yehova wakiwa na hakika kwamba angewategemeza. Naam, maneno ya Zekaria 4:6 yanazungumzia msaada wa Mungu.

      18 Wayahudi waliporudi katika nchi yao mwaka wa 537 K.W.K., hawakuwa na jeshi. Hata hivyo, Yehova aliwalinda na kuwaongoza walipokuwa safarini kutoka Babiloni. Isitoshe, roho yake ilikuwa ikielekeza mambo walipoanza ujenzi wa hekalu muda mfupi baadaye. Ikiwa wangerudia kazi hiyo kwa bidii tena, angewasaidia kupitia roho yake takatifu.

      19. Roho ya Mungu ilishinda uvutano gani wenye nguvu?

      19 Kupitia mfululizo wa maono manane, Zekaria alihakikishiwa kwamba Yehova angekuwa pamoja na watu wake ambao wangeendelea kwa uaminifu kufanya kazi ya kujenga hekalu na kuimaliza. Maono ya nne, yaliyoandikwa katika sura ya 3, yanaonyesha kwamba Shetani alikuwa anajitahidi kuzuia jitihada za Wayahudi za kumaliza kujenga hekalu. (Zekaria 3:1) Bila shaka, Shetani hangefurahi kumwona Kuhani Mkuu Yoshua akiwatumikia watu kwenye hekalu jipya. Ingawa Ibilisi alijitahidi kuwazuia Wayahudi wasijenge hekalu, roho ya Yehova ilitimiza sehemu muhimu katika kuondoa vizuizi na kuwaimarisha Wayahudi waendelee na kumaliza ujenzi wa hekalu.

      20. Roho takatifu iliwasaidiaje Wayahudi kufanya mapenzi ya Mungu?

      20 Kulikuwa na upinzani mwingi uliokuwa kama mlima kutoka kwa maofisa wa serikali ambao walipiga marufuku kazi ya ujenzi. Hata hivyo, Yehova aliahidi kwamba “mlima” huo ungeondolewa na kuwa “nchi tambarare.” (Zekaria 4:7) Hivyo ndivyo ilivyokuwa! Mfalme Dario wa Kwanza alifanya uchunguzi, naye akagundua hati ya Koreshi ya kumbukumbu, ambayo iliwaruhusu Wayahudi kujenga upya hekalu. Basi, Dario akaondoa marufuku hayo, naye akaamuru kwamba Wayahudi wapewe pesa kutoka katika hazina ya kifalme ili kulipia gharama za ujenzi. Hilo lilikuwa badiliko lililoje! Je, roho ya Mungu ilihusika? Bila shaka. Ujenzi wa hekalu ulikamilishwa mwaka wa 515 K.W.K., katika mwaka wa sita wa utawala wa Dario wa Kwanza. —Ezra 6:1, 15.

      21. (a) Katika nyakati za kale, Mungu ‘alitikisaje mataifa yote,’ na “vitu vyenye kutamanika” vilitokaje? (b) Unabii huo umetimiaje leo?

      21 Kwenye Hagai 2:5, nabii huyo aliwakumbusha Wayahudi agano ambalo Mungu alikuwa amefanya pamoja nao katika Mlima Sinai wakati “mlima wote ulikuwa ukitetemeka sana.” (Kutoka 19:18) Katika siku za Hagai na Zekaria, Yehova alikusudia kutikisa mambo tena, kama mstari wa 6 na 7 unavyoonyesha. Milki ya Uajemi ingekumbwa na misukosuko, lakini kazi ya ujenzi wa hekalu ingesonga mbele mpaka ikamilike. Watu fulani ambao hawakuwa Wayahudi, yaani, vile “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote,” wangejiunga na Wayahudi kumtukuza Mungu katika mahali hapo pa ibada. Leo, kwa njia kubwa, Mungu ‘ametikisa mataifa’ kupitia kazi yetu ya kuhubiri, na “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” vimeingia kumwabudu Mungu pamoja na mabaki ya watiwa-mafuta. Naam, sasa watiwa-mafuta na kondoo wengine wanaijaza nyumba ya Yehova utukufu. Waabudu hao wa kweli wanatazamia kwa imani wakati ambapo Yehova ‘atatikisa mbingu na dunia’ katika njia nyingine. Hilo litafanywa ili kupindua na kuangamiza nguvu za falme za mataifa. —Hagai 2:22.

      22. Mataifa ‘yanatikiswaje,’ na matokeo ni nini, na ni mambo gani yatakayotukia wakati ujao?

      22 Unabii huo unatukumbusha misukosuko ambayo imetokea katika sehemu mbalimbali zinazofananishwa na “mbingu na dunia na bahari na nchi kavu.” Kwanza, Shetani Ibilisi na roho waovu wake walitupwa duniani. (Ufunuo 12:7-12) Isitoshe, kazi ya kuhubiri inayoongozwa na watiwa-mafuta wa Mungu imetikisa sehemu za kidunia za mfumo huu wa mambo. (Ufunuo 11:18) Licha ya hayo yote, “umati mkubwa” wa vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote umejiunga na Waisraeli wa kiroho katika kumtumikia Yehova. (Ufunuo 7:9, 10) Umati huo mkubwa unashirikiana na Wakristo watiwa-mafuta katika kuhubiri habari njema kwamba hivi karibuni Mungu atayatikisa mataifa kwenye Har–Magedoni. Tukio hilo litawezesha ibada ya kweli ifanywe kuwa kamilifu duniani pote.

  • Mikono Yenu na Iwe na Nguvu
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 15
    • Mikono Yenu na Iwe na Nguvu

      “Mikono yenu na iwe na nguvu, ninyi ambao siku hizi mnayasikia maneno haya kutoka katika kinywa cha manabii.”—ZEKARIA 8:9.

      1, 2. Kwa nini tunapaswa kuchunguza vitabu vya Hagai na Zekaria?

      INGAWA unabii wa Hagai na Zekaria uliandikwa yapata miaka 2,500 iliyopita, bado una mafunzo muhimu kwetu. Masimulizi ya Biblia yaliyo katika vitabu hivyo viwili si historia tu. Masimulizi hayo ni sehemu ya “mambo yote yaliyoandikwa zamani . . . ili kutufundisha sisi.” (Waroma 15:4) Mambo mengi yaliyo katika vitabu hivyo hutufanya tufikirie hali halisi ambazo zimekuwa zikitukia tangu Ufalme uliposimamishwa mbinguni mwaka wa 1914.

      2 Akirejelea matukio na hali zilizowapata watu wa Mungu wa kale, mtume Paulo alisema hivi: “Basi mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (1 Wakorintho 10:11) Huenda basi ukauliza, ‘Vitabu vya Hagai na Zekaria vinatufunza mambo gani muhimu?’

      3. Hagai na Zekaria walikazia nini?

      3 Kama vile makala iliyotangulia ilivyosema, unabii wa Hagai na Zekaria ulihusu wakati ambapo Wayahudi walirudi katika nchi waliyopewa na Mungu baada ya kuachiliwa huru kutoka utekwani huko Babiloni. Manabii hao wawili walikazia kujengwa upya kwa hekalu. Wayahudi waliweka msingi wa hekalu mwaka wa 536 K.W.K. Ingawa Wayahudi fulani wazee walikumbuka hekalu la zamani, kwa ujumla, watu ‘walipaaza sauti kwa shangwe.’ Hata hivyo, jambo muhimu hata zaidi limetukia katika siku zetu. Jambo gani?—Ezra 3:3-13.

      4. Ni nini kilichotokea muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu?

      4 Muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, watiwa-mafuta wa Yehova waliachiliwa huru kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa. Jambo hilo lilionyesha wazi kwamba Yehova anawategemeza. Mwanzoni ilidhaniwa kwamba viongozi wa kidini na washiriki wao wa kisiasa walikuwa wamekomesha kazi ya kuhubiri na ya kufundisha ya Wanafunzi wa Biblia. (Ezra 4:8, 13, 21-24) Lakini, Yehova Mungu aliondoa mambo yaliyozuia kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Kwa makumi ya miaka tangu 1919, kazi ya Ufalme imeongezeka na hakuna kitu ambacho kimeweza kuikomesha.

      5, 6. Andiko la Zekaria 4:7 linatabiri utimizo wa jambo gani muhimu?

      5 Tuna uhakika kwamba kazi ya kuhubiri na kufundisha inayofanywa na watumishi wa Yehova watiifu wa wakati wetu itaendelea kwa msaada wake. Tunasoma hivi kwenye Zekaria 4:7: “Ataleta jiwe la juu kabisa. Nalo litapaaziwa sauti: ‘Linavutia kama nini! Linavutia kama nini!’” Unabii huo unahusu jambo gani muhimu ambalo limetimizwa katika siku zetu?

      6 Andiko la Zekaria 4:7 linatabiri wakati ambapo ibada ya kweli ya Bwana Mwenye Enzi Kuu ingefanywa kuwa kamilifu katika ua wa kidunia wa hekalu lake la kiroho. Hekalu hilo ni mpango wa Yehova wa kumfikia katika ibada kwa msingi wa dhabihu ya upatanisho ya Kristo Yesu. Ni kweli kwamba hekalu hilo kubwa la kiroho limekuwapo tangu karne ya kwanza W.K. Hata hivyo, bado ibada ya kweli duniani haijafanywa kuwa kamilifu. Sasa mamilioni ya waabudu wanatumikia katika ua wa kidunia wa hekalu hilo la kiroho. Watu hao pamoja na umati wa wale watakaofufuliwa watafanywa kuwa wakamilifu wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo. Mwishoni mwa hiyo miaka elfu, ni waabudu wa kweli wa Mungu tu ndio watakaobaki katika dunia iliyosafishwa.

      7. Yesu ana jukumu gani katika kufanya ibada ya kweli iwe kamilifu katika siku zetu, na kwa nini hilo linatutia moyo?

      7 Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua waliona ujenzi wa hekalu ukikamilishwa mwaka wa 515 K.W.K. Vivyo hivyo, andiko la Zekaria 6:12, 13 lilitabiri jukumu la Yesu la kufanya ibada ya kweli ifikie hali yake kamilifu: “Yehova wa majeshi amesema hivi: ‘Tazama, mtu ambaye jina lake ni Chipukizi. Naye atachipuka kutoka mahali pake mwenyewe, naye atalijenga hekalu la Yehova. Naye . . . atachukua heshima; ataketi na kutawala juu ya kiti chake cha ufalme, naye atakuwa kuhani juu ya kiti chake cha ufalme.’” Kwa kuwa Yesu, aliye mbinguni na anayesababisha wafalme wa ukoo wa Daudi kuchipuka, anategemeza kazi ya Ufalme kwenye hekalu la kiroho, je, kuna mtu yeyote anayeweza kuizuia kazi hiyo? La hasha! Je, hilo halipaswi kututia moyo tuendelee na utumishi wetu, bila kukengeushwa na mahangaiko ya kila siku?

      Mambo ya Kutanguliza

      8. Kwa nini ni lazima tutangulize kazi inayofanywa katika hekalu la kiroho?

      8 Ili tupate msaada na baraka za Yehova, lazima tuendelee kutanguliza kazi inayofanywa katika hekalu la kiroho. Tofauti na Wayahudi waliosema, “Wakati haujaja,” tunapaswa kukumbuka kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (Hagai 1:2; 2 Timotheo 3:1) Yesu alitabiri kwamba wanafunzi wake washikamanifu wangehubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. Tunapaswa kuwa waangalifu tusipuuze huduma yetu ya pekee. Kazi ya kuhubiri na kufundisha iliyokuwa imekomeshwa kwa muda mfupi kwa sababu ya upinzani kutoka kwa ulimwengu ilianza tena mwaka wa 1919, lakini bado haijakamilishwa. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba kazi hiyo itakamilishwa!

      9, 10. Baraka za Yehova zinategemea nini, na hilo linatuhusuje?

      9 Kadiri tunavyofanya kazi hiyo kwa bidii, ndivyo tutakavyobarikiwa, tukiwa kikundi na tukiwa mtu mmoja-mmoja. Ona ahadi ya Yehova inayotupa uhakikisho. Wayahudi waliporudia ibada safi kwa nafsi yote na kuanza tena kujenga msingi wa hekalu kwa bidii, Yehova alisema hivi: “Kuanzia leo hii nitatoa baraka.” (Hagai 2:19) Wayahudi wangepata tena kibali cha Yehova kwa ukamili. Sasa ona baraka zinazotajwa katika ahadi hii ya Mungu: “Kutakuwa na mbegu ya amani; mzabibu utazaa matunda yake, na dunia itatoa mazao yake, na mbingu zitatoa umande wake; nami nitawafanya mabaki ya watu hawa warithi vitu hivyo vyote.”—Zekaria 8:9-13.

      10 Kama vile Yehova alivyowabariki Wayahudi hao kiroho na kimwili, ndivyo atakavyotubariki tukifanya kazi aliyotupa kwa bidii na kwa mioyo yenye furaha. Baraka hizo zinatia ndani amani kati yetu wenyewe, usalama, ufanisi, na ukuzi wa kiroho. Lakini Mungu ataendelea kutubariki maadamu tunaendelea kufanya kazi katika hekalu la kiroho jinsi anavyotaka tuifanye.

      11. Tunaweza kujichunguzaje?

      11 Sasa ndio wakati wa ‘kuweka moyo wetu juu ya njia zetu.’ (Hagai 1:5, 7) Tunapaswa kuchanganua mambo tunayotanguliza maishani. Baraka ambazo Yehova anatupa leo zinategemea jinsi tunavyolitukuza jina lake na kuendelea kufanya kazi yetu katika hekalu lake la kiroho. Unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, nimeacha kutanguliza mambo niliyoyatanguliza zamani? Je, bidii yangu kwa ajili ya Yehova, kweli yake, na kazi yake ni sawa na bidii niliyokuwa nayo nilipobatizwa? Je, tamaa ya kuishi maisha ya starehe inaathiri maoni yangu kuhusu Yehova na Ufalme wake? Je, ninakosa kumtukuza Yehova kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu au kuhangaikia maoni yao?’—Ufunuo 2:2-4.

      12. Andiko la Hagai 1:6, 9 linazungumzia hali gani iliyokuwapo miongoni mwa Wayahudi?

      12 Hatutaki kukosa baraka za Mungu kwa sababu ya kupuuza kazi ya kulitukuza jina lake. Kumbuka kwamba baada ya kuanza kazi kwa bidii, Wayahudi waliorudishwa walikuwa “mbioni, kila mmoja kwa ajili ya nyumba yake mwenyewe,” kama andiko la Hagai 1:9 linavyosema. Walijishughulisha tu na mahitaji yao na maisha yao. Hivyo, kukawa na ‘mavuno kidogo,’ uhaba wa chakula kizuri na vinywaji, na ukosefu wa nguo za kuwapasha joto. (Hagai 1:6) Yehova aliacha kuwabariki. Je, kuna mambo tunayojifunza kutokana na hali hiyo?

      13, 14. Tunaweza kutumiaje jambo tunalojifunza katika Hagai 1:6, 9, na kwa nini hilo ni muhimu?

      13 Naam, ili tuendelee kupata baraka za Yehova, ni lazima tuepuke kuhangaikia masilahi yetu wenyewe huku tukipuuza kumtukuza Yehova. Tunahitaji kuepuka kufanya hivyo iwe tunakengeushwa na kutafuta pesa, miradi ya kujitajirisha upesi, miradi ya kufuatia elimu ya juu ili kuwa na kazi nzuri katika mfumo huu, au miradi ya kujitakia makuu.

      14 Mambo hayo si dhambi. Hata hivyo, unapofikiria uzima wa milele, je, huoni kwamba hayo ni “matendo yaliyokufa”? (Waebrania 9:14) Kwa njia gani? Yamekufa kiroho, ni ya ubatili, na hayana faida yoyote. Mtu akiendelea kuyafuatilia, matendo hayo yatamfanya afe kiroho. Ndivyo ilivyokuwa kwa Wakristo fulani watiwa-mafuta katika siku za mitume. (Wafilipi 3:17-19) Hali hiyo pia imewapata wengine katika siku zetu. Huenda unajua baadhi ya watu ambao walikengeushwa pole kwa pole kutoka kwenye utendaji wa Kikristo na kutoka kutanikoni na sasa hawaonyeshi kwamba wangependa kurudia utumishi wa Yehova. Ni matumaini yetu kwamba watu hao watamrudia Yehova, lakini ukweli ni kwamba kufuatia “matendo yaliyokufa” kunaweza kumfanya mtu apoteze kibali na baraka za Yehova. Hilo ni jambo lenye kusikitisha sana. Linamfanya mtu apoteze shangwe na amani inayotokana na roho ya Mungu. Isitoshe, hebu wazia kile ambacho mtu hupoteza asiposhirikiana na undugu wa Kikristo wenye upendo!—Wagalatia 1:6; 5:7, 13, 22-24.

      15. Andiko la Hagai 2:14 linaonyeshaje uzito wa ibada yetu?

      15 Hilo ni jambo zito sana. Ona kwenye Hagai 2:14 jinsi Yehova alivyowaona Wayahudi ambao waliipuuza nyumba yake ya ibada ili wajenge nyumba zao wenyewe, kihalisi au kwa njia ya mfano. “‘Hivyo ndivyo kikundi hiki cha watu kilivyo, na hivyo ndivyo taifa hili lilivyo mbele zangu,’ asema Yehova, ‘na hivyo ndivyo kazi yote ya mikono yao ilivyo, na chochote wanachotoa huko, ni najisi.’” Dhabihu zozote ambazo Wayahudi walitoa kwa moyo nusu-nusu kwenye madhabahu ya muda huko Yerusalemu hazingekubaliwa ikiwa wangeendelea kupuuza ibada ya kweli.—Ezra 3:3.

      Uhakikisho wa Kupata Msaada

      16. Wayahudi walipata uhakikisho gani kutokana na maono ambayo Zekaria alipokea?

      16 Kupitia maono manane ambayo Zekaria aliona, Mungu aliwahakikishia Wayahudi watiifu ambao walifanya kazi ya kujenga upya hekalu kwamba angewategemeza. Maono ya kwanza yalitoa uhakikisho wa kwamba hekalu lingekamilishwa na Yerusalemu na Yuda zingebarikiwa ikiwa Wayahudi wangeendelea kuwa watiifu na kufanya kazi waliyopewa. (Zekaria 1:8-17) Maono ya pili yalionyesha mwisho wa serikali zote zinazoipinga ibada ya kweli. (Zekaria 1:18-21) Maono mengine yaliwahakikishia kwamba Mungu angewalinda wakati wa ujenzi wa hekalu, kwamba watu wa mataifa mengi wangemiminika kwenye nyumba ya Yehova ya ibada iliyokamilishwa, kwamba kungekuwa na amani na usalama wa kweli, kwamba vizuizi vikubwa vya kazi ya ujenzi iliyoagizwa na Mungu vingeondolewa, kwamba uovu ungeondolewa, na kwamba malaika wangesimamia mambo na kuandaa ulinzi. (Zekaria 2:5, 11; 3:10; 4:7; 5:6-11; 6:1-8) Kwa sababu ya uhakikisho huo wa kwamba Mungu angewategemeza, unaweza kutambua sababu iliyofanya watu watiifu warekebishe maisha yao na kutilia maanani kazi ambayo Mungu alitaka waifanye alipowakomboa.

      17. Kwa kuwa tumepewa uhakikisho, tunapaswa kujiuliza maswali gani?

      17 Vivyo hivyo, kwa kuwa tumehakikishiwa kwamba mwishowe ibada ya kweli itashinda, tunapaswa kuchochewa kutenda na kuifikiria kwa uzito nyumba ya Yehova ya ibada. Jiulize hivi: ‘Ikiwa ninasadiki kwamba huu ndio wakati wa kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi, je, miradi yangu na maisha yangu yanapatana na usadikisho huo? Je, ninatenga wakati wa kutosha ili kujifunza Neno la Mungu la kinabii, kulitanguliza maishani mwangu, na kuzungumza juu yake pamoja na Wakristo wenzangu na vilevile wale ninaowahubiria?’

      18. Kulingana na Zekaria sura ya 14, ni mambo gani yatakayotukia wakati ujao?

      18 Zekaria alirejelea uharibifu wa Babiloni Mkubwa unaofuatiwa na vita vya Har–Magedoni. Tunasoma hivi: “Itakuwa siku moja inayojulikana kuwa ni ya Yehova. Haitakuwa mchana, wala haitakuwa usiku; na itatukia kwamba wakati wa jioni kutakuwa na nuru.” Naam, siku ya Yehova itakuwa yenye giza kwelikweli, siku isiyopendeza kwa adui zake duniani! Lakini itakuwa siku nzuri na yenye nuru kwa waabudu waaminifu wa Yehova. Zekaria pia alieleza jinsi kila kitu katika ulimwengu mpya kitakavyoutangaza utakatifu wa Yehova. Ibada ya kweli kwenye hekalu kubwa la kiroho la Mungu ndiyo itakayokuwa ibada pekee duniani. (Zekaria 14:7, 16-19) Huo ni uhakikisho ulioje! Tutaona utimizo wa mambo yaliyotabiriwa, nasi tutaona pia enzi kuu ya Yehova ikitetewa. Kwelikweli, hiyo itakuwa siku ya Yehova isiyo na kifani!

      Baraka za Kudumu

      19, 20. Ni nini kinachokutia moyo katika andiko la Zekaria 14:8, 9?

      19 Baada ya utimizo huo mkuu, Shetani na roho wake waovu watawekwa katika hali ya kutotenda, ambayo inafananishwa na abiso. (Ufunuo 20:1-3, 7) Kisha, baraka zitamiminika wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu. Andiko la Zekaria 14:8, 9 linasema hivi: “Itatukia siku hiyo kwamba maji yaliyo hai yatatoka katika Yerusalemu, nusu yake kuelekea upande wa bahari ya mashariki na nusu yake kuelekea upande wa bahari ya magharibi. Itakuwa hivi wakati wa kiangazi na wa majira ya baridi kali. Na Yehova atakuwa mfalme juu ya dunia yote. Katika siku hiyo Yehova atakuwa mmoja, na jina lake litakuwa moja.”

      20 “Maji yaliyo hai,” au “mto wa maji ya uzima,” yanayowakilisha maandalizi ya Yehova ya uzima, yataendelea kutiririka kutoka kwenye kiti cha Ufalme wa Kimasihi. (Ufunuo 22:1, 2) Umati mkubwa wa waabudu wa Yehova ambao wataokoka Har–Magedoni, watafaidika kwa kuwekwa huru kutokana na laana ya kifo kilichotokana na Adamu. Hata wafu watafaidika kupitia ufufuo. Huo utakuwa mwanzo wa kipindi kipya cha utawala wa Yehova juu ya dunia. Wanadamu wote duniani watamtambua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote na kwamba ni yeye pekee anayepaswa kuabudiwa.

      21. Tunapaswa kuwa na usadikisho gani?

      21 Kutokana na mambo yote ambayo Hagai na Zekaria walitabiri na yote ambayo yametimizwa, tuna sababu nzuri za kuendelea kufanya kazi ambayo Mungu ametupa katika ua wa kidunia wa hekalu lake la kiroho. Hadi wakati ambapo ibada ya kweli itafanywa kuwa kamilifu, acheni sote tujitahidi sana kutanguliza mambo ya Ufalme. Andiko la Zekaria 8:9 linatuhimiza hivi: “Mikono yenu na iwe na nguvu, ninyi ambao siku hizi mnayasikia maneno haya kutoka katika kinywa cha manabii.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki