-
Je, Utakuwepo Katika Ulimwengu Mpya?Mnara wa Mlinzi—2000 | Aprili 15
-
-
4, 5. Ni unabii gani mbalimbali wa Biblia tuliochunguza tayari ambao waweza kuimarisha tumaini letu juu ya mambo yatakayotukia wakati ujao?
4 Fikiria mambo ambayo makala iliyotangulia ilithibitisha kuhusu ahadi za Biblia juu ya mbingu mpya na dunia mpya. Isaya alitabiri mfumo huo mpya, na unabii wake ulitimizwa Wayahudi waliporudi katika nchi yao na kuanzisha tena ibada ya kweli. (Ezra 1:1-3; 2:1, 2; 3:12, 13) Hata hivyo, je, unabii wa Isaya ulirejezea tukio hilo tu? Bila shaka la! Mambo aliyotabiri yangetimizwa pia katika njia kubwa zaidi muda mrefu baadaye. Kwa nini tukate kauli hiyo? Kwa sababu ya mambo tusomayo katika 2 Petro 3:13 na Ufunuo 21:1-5. Maandiko hayo yarejezea mbingu mpya na dunia mpya zitakazowanufaisha Wakristo ulimwenguni pote.
-
-
Je, Utakuwepo Katika Ulimwengu Mpya?Mnara wa Mlinzi—2000 | Aprili 15
-
-
6. Unabii wa nne unaotaja “mbingu mpya na dunia mpya” watabiri nini?
6 Sasa na tuchunguze usemi unaosalia wa “mbingu mpya na dunia mpya,” kwenye Isaya 66:22-24: “Kama vile mbingu mpya na nchi [“dunia,”NW] mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa. Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema BWANA. Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.”
7. Kwa nini tufikie mkataa wa kwamba andiko la Isaya 66:22-24 litatimizwa wakati ujao?
7 Unabii huo ulitimizwa miongoni mwa Wayahudi waliorudishwa katika nchi yao, lakini kungekuwa na utimizo mwingine. Lazima utimizo huo ungetokea baadaye sana, baada ya barua ya pili ya Petro na Ufunuo kuandikwa, kwa kuwa barua hizo zataja ‘mbingu na dunia mpya’ za wakati ujao. Twaweza kutarajia utimizo huo mkubwa na ulio kamili katika mfumo mpya. Fikiria baadhi ya mambo tuwezayo kutazamia kufurahia.
8, 9. (a) Ni katika maana gani watu wa Mungu wataendelea ‘kukaa’? (b) Ni nini maana ya unabii kwamba watumishi wa Yehova wataabudu “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato”?
8 Andiko la Ufunuo 21:4 laonyesha kwamba kifo hakitakuwapo tena kamwe. Maneno ya Isaya sura ya 66 yakubaliana na ahadi hiyo. Twaweza kuona kuanzia mstari wa 22 kwamba Yehova anajua ya kwamba mbingu mpya na dunia mpya hazitakuwa za muda mfupi tu. Isitoshe, watu wake watadumu; wataendelea ‘kukaa’ mbele zake. Yale ambayo tayari Mungu amewafanyia wateule wake yatupa uhakika. Wakristo wa kweli wamekabili mnyanyaso mkali, hata wamekabili jitihada za kishupavu za kuwaangamiza. (Yohana 16:2; Matendo 8:1) Lakini, hata maadui wenye nguvu sana wa watu wa Mungu, kama vile Maliki Nero wa Roma na Adolf Hitler, hawajaweza kuwaondolea mbali waaminifu-washikamanifu wa Mungu, wanaoitwa kwa jina lake. Yehova amehifadhi kutaniko la watu wake, nasi tuna hakika kwamba anaweza kuendelea kulifanya likae hata milele.
9 Vivyo hivyo, wakiwa mtu mmoja-mmoja, wale walio waaminifu kwa Mungu, wakiwa sehemu ya dunia mpya, jamii ya waabudu wa kweli katika ulimwengu mpya, watakaa daima kwa kuwa watakuwa wakimtolea Muumba wa vitu vyote ibada safi. Ibada hiyo haitakuwa ya pindi kwa pindi au isiyo na utaratibu. Sheria ya Mungu, ambayo Waisraeli walipewa kupitia Musa, ilitaka matendo fulani ya ibada yafanywe kila mwezi, uliotiwa alama na mwezi mpya, na kila juma, lililotiwa alama na siku ya Sabato. (Mambo ya Walawi 24:5-9; Hesabu 10:10; 28:9, 10; 2 Mambo ya Nyakati 2:4) Kwa hiyo, Isaya 66:23 lataja ibada ya kawaida na yenye kuendelea ya Mungu, juma baada ya juma, mwezi baada ya mwezi. Kutoamini kuwepo kwa Mungu na unafiki wa kidini hazitakuwako wakati huo. “Wanadamu wote watakuja kuabudu mbele” za Yehova.
10. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba ulimwengu mpya hautaharibiwa daima na waovu?
10 Isaya 66:24 latuhakikishia kwamba amani na uadilifu za dunia mpya hazitakuwa hatarini kamwe. Waovu hawataiharibu dunia kamwe. Kumbuka kwamba andiko la 2 Petro 3:7 lasema kwamba tunangojea “siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.” Watakaoharibiwa ni watu wasiomwogopa Mungu. Hakuna madhara yatakayowapata wasio na hatia, tofauti na vile itukiavyo mara nyingi katika vita vya wanadamu, ambapo majeruhi walio raia huwa wengi kuliko askari. Hakimu Mkuu atuhakikishia kwamba siku yake itakuwa ya kuangamiza watu wasiomwogopa Mungu.
11. Isaya anaonyesha ni nini kitampata yeyote anayekataa Mungu na ibada yake?
11 Waokokaji waadilifu wataona kwamba neno la Mungu la kiunabii ni la kweli. Mstari wa 24 hutabiri kwamba ‘mizoga ya watu waliomwasi’ Yehova itakuwa uthibitisho wa hukumu yake. Huenda maneno ya waziwazi ambayo Isaya alitumia yakawa yenye kushtua. Hata hivyo, yanapatana na jambo hakika la kihistoria. Nje ya kuta za Yerusalemu la kale kulikuweko mahali mbalimbali pa kutupa takataka na, pindi kwa pindi, mizoga ya wahalifu walioonekana kuwa hawastahili mazishi ya heshima.a Huko funza na moto mkali zingemaliza upesi takataka hizo na mizoga hiyo. Kwa wazi, mfano wa Isaya waonyesha mfano wa hukumu ya Yehova dhidi ya waasi ambayo haiwezi kubadilishwa.
-