Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Paradiso Yarudishwa!
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • [Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 370]

  • Paradiso Yarudishwa!
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Nchi Yenye Ukiwa Yafurahi

      3. Kulingana na unabii wa Isaya, nchi itageuzwa iweje?

      3 Unabii wa Isaya uliopuliziwa kuhusu Paradiso iliyorudishwa waanza kwa maneno haya: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. Litachanua maua mengi, na kufurahi, naam, kwa shangwe na kuimba; litapewa uzuri wa Lebanoni, utukufu wa Karmeli na Sharoni; watauona utukufu wa BWANA [“Yehova,” “NW”], ukuu wa Mungu wetu.”—Isaya 35:1, 2.

      4. Nchi ya Wayahudi yageuka kuwa kama nyika wakati gani na jinsi gani?

      4 Isaya aandika maneno hayo karibu mwaka wa 732 K.W.K. Miaka ipatayo 125 baadaye, Wababiloni waharibu Yerusalemu na watu wa Yuda wapelekwa uhamishoni. Nchi yao yaachwa ukiwa, bila watu. (2 Wafalme 25:8-11, 21-26) Basi onyo la Yehova kwamba watu wa Israeli wangeenda uhamishoni iwapo wangekosa kuwa waaminifu latimia. (Kumbukumbu la Torati 28:15, 36, 37; 1 Wafalme 9:6-8) Taifa la Waebrania linapokuwa mateka katika nchi ya kigeni, mashamba yao ya matunda yenye kunyunyizwa maji vizuri yaachwa pasipo utunzaji kwa miaka 70 nayo yawa kama nyika.—Isaya 64:10; Yeremia 4:23-27; 9:10-12.

      5. (a) Hali za kiparadiso zarudishwaje nchini? (b) Watu wauonaje “utukufu wa Yehova”?

      5 Hata hivyo, unabii wa Isaya watabiri kuwa nchi haitakaa ukiwa milele. Itarudishwa kuwa paradiso kwelikweli. Itapewa “uzuri wa Lebanoni” na “utukufu wa Karmeli na Sharoni.”a Jinsi gani? Warudipo kutoka uhamishoni, Wayahudi waweza tena kulima na kunyunyiza maji mashamba yao, na nchi yao yaanza kuzaa kwa wingi tena kama hapo awali. Ni Yehova peke yake anayestahili kusifiwa kwa hayo. Wayahudi wapata kufurahia hali hizo zinazofanana na paradiso kwa sababu ya mapenzi, utegemezo, na baraka zake. Watu waweza kuona “utukufu wa Yehova, ukuu wa Mungu [wao]” wanapoona jinsi ambavyo Yehova ameigeuza nchi yao kwa njia ya ajabu.

      6. Watu waona utimizo gani muhimu wa maneno ya Isaya?

      6 Ijapokuwa hivyo, kuna utimizo muhimu zaidi wa maneno ya Isaya katika nchi ya Israeli iliyorudishwa. Kwa miaka mingi, Israeli imekuwa katika hali ya ukame, iliyo kama jangwa kiroho. Wahamishwa walipokuwa huko Babiloni, ibada safi ilizuiwa sana. Hapakuwa na hekalu, wala madhabahu, wala ukuhani uliopangwa. Dhabihu za kila siku zilikuwa zimekoma kwa muda. Isaya sasa atoa unabii wa mabadiliko. Chini ya uongozi wa watu kama vile Zerubabeli, Ezra, na Nehemia, wawakilishi kutoka kwa makabila yote 12 ya Israeli warudi Yerusalemu, wajenga tena hekalu, na kumwabudu Yehova kwa uhuru. (Ezra 2:1, 2) Hiyo ni paradiso ya kiroho kwelikweli!

      Kuwaka Roho

      7, 8. Kwa nini wahamishwa Wayahudi wahitaji kuwa na mtazamo mzuri, na maneno ya Isaya yatoaje kitia-moyo?

      7 Maneno ya Isaya sura ya 35 yana furaha ndani yake. Nabii huyo anatangaza wakati ujao ulio mzuri kwa ajili ya taifa hilo lenye kutubu. Yeye kwa kweli asema akiwa na uhakika na matumaini mema. Karne mbili baadaye, Wayahudi waliohamishwa wahitaji kuwa na uhakika na matumaini mema kama hayo huku kurudishwa kwao kunapokaribia. Kupitia Isaya, Yehova awahimiza kwa kutumia unabii: “Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu, yafanyeni imara magoti yaliyolegea, waambieni walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope; tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi.”—Isaya 35:3, 4.

      8 Mwisho wa uhamisho huo mrefu ni wakati wa utendaji. Mfalme Koreshi wa Uajemi, anayetumiwa kulipiza kisasi cha Yehova dhidi ya Babiloni, ametangaza kuwa ibada ya Yehova yapasa kurudishwa Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23) Maelfu ya familia za Waebrania zahitaji kupangwa ndipo zifunge safari hatari ya kutoka Babiloni hadi Yerusalemu. Watakapofika huko, watahitaji kujenga makao ya kutosha na kujitayarisha kufanya kazi kubwa mno ya kujenga tena hekalu na jiji. Huenda hayo yote yakaonekana kuwa magumu sana kwa Wayahudi fulani huko Babiloni. Hata hivyo, huu sio wakati wa kudhoofika au kuhofu. Wayahudi wapaswa kutiana nguvu na kumtumaini Yehova. Yeye awahakikishia kuwa wataokolewa.

      9. Wayahudi wanaorudi watolewa ahadi gani tukufu?

      9 Wale waliowekwa huru kutoka utekwani Babiloni watakuwa na sababu nzuri ya kufurahi, kwa kuwa wakati ujao mtukufu unawangojea wanaporudi Yerusalemu. Isaya atabiri: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6a.

      10, 11. Ni kwa nini lazima maneno ya Isaya yawe na maana ya kiroho kwa Wayahudi wanaorudi, na maneno hayo yadokeza nini?

      10 Yaonekana Yehova aifikiria hali ya kiroho ya watu wake. Wameadhibiwa kwa kupelekwa uhamishoni kwa miaka 70 kwa sababu ya uasi wao wa awali. Hata hivyo, Yehova ajapowatia watu wake nidhamu, hakuwapiga kwa upofu, uziwi, ulemavu, na ububu. Basi, kurudisha taifa la Israeli hakuhitaji uponyaji wa kasoro za kimwili. Yehova arudisha kile kilichopotea, yaani, afya ya kiroho.

      11 Wayahudi wenye kutubu waponywa kwa kupata tena uwezo wao mbalimbali wa kiroho—uwezo wao wa kuona kiroho na uwezo wao wa kusikia, kutii, na kunena neno la Yehova. Wao watambua uhitaji wao wa kukaa karibu na Yehova. Kupitia mwenendo mzuri, ‘waimba’ kwa furaha ya kumsifu Mungu wao. Aliyekuwa “kilema” hapo awali apata hamu na nguvu ya kuabudu Yehova. “Ataruka-ruka kama kulungu” kitamathali.

      Yehova Awaburudisha Watu Wake

      12. Yehova ataibariki nchi kwa maji kadiri gani?

      12 Ni vigumu kuwazia paradiso isiyo na maji. Paradiso ya kwanza huko Edeni ilikuwa na maji mengi. (Mwanzo 2:10-14) Nchi waliyopewa Israeli pia ilikuwa “nchi yenye vijito vya maji, na chemchemi, na visima, vibubujikavyo.” (Kumbukumbu la Torati 8:7) Kwa kufaa basi, Isaya atoa ahadi hii yenye kuburudisha: “Katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji; katika makao ya mbweha, walipokuwa wamelala, patakuwa na majani, pamoja na mianzi na manyasi.” (Isaya 35:6b, 7) Waisraeli watakapoanza kuitunza nchi tena, sehemu zenye ukiwa ambapo mbweha walikaa wakati fulani zitafunikwa kwa majani tele yanayonawiri na yenye rangi ya kijani. Nchi kame na yenye vumbi itageuzwa kuwa mahali penye “matope” panapoweza kumea mafunjo na mianzi mingine imeayo majini.—Ayubu 8:11.

      13. Taifa lililorudishwa litapewa maji gani mengi ya kiroho?

      13 Ingawa hivyo, jambo la maana zaidi ni yale maji ya kiroho ya ile kweli, ambayo Wayahudi waliorudishwa watapata kwa wingi. Yehova atatoa ujuzi, kitia-moyo, na faraja kupitia Neno lake. Na zaidi, wanaume na wakuu wazee waaminifu watakuwa “kama mito ya maji mahali pakavu.” (Isaya 32:1, 2) Wale wanaoendeleza ibada safi, kama vile Ezra, Hagai, Yoshua, Nehemia, Zekaria, Zerubabeli, kwa kweli watakuwa ushuhuda ulio hai wa utimizo wa unabii wa Isaya.—Ezra 5:1, 2; 7:6, 10; Nehemia 12:47.

      “Njia ya Utakatifu”

      14. Fafanua hali ya usafiri kati ya Babiloni na Yerusalemu.

      14 Hata hivyo, ili Wayahudi hao wahamishwa wafurahie hali hizo za kiparadiso za kimwili na kiroho, watahitaji kufunga safari ndefu na hatari kutoka Babiloni hadi Yerusalemu. Ikiwa wangeenda moja kwa moja wangevuka kilometa 800 katika eneo kame, lisilokalika. Njia iliyo afadhali kidogo ingehusisha kusafiri kilometa 1,600. Kila moja ya safari hizo ingehusisha kusafiri miezi kadhaa katika halihewa kali na hatari ya kukutana na wanyama wa mwituni na pia watu walio kama wanyama. Ijapokuwa hivyo, wale wanaouamini unabii wa Isaya hawahangaiki kupita kiasi. Kwa nini?

      15, 16. (a) Yehova awapa Wayahudi waaminifu ulinzi gani wakiwa safarini kwenda kwao? (b) Yehova awapa Wayahudi njia kuu iliyo salama kwa maana gani nyingine?

      15 Yehova aahidi hivi kupitia Isaya: “Hapo patakuwa na njia kuu, na njia, nayo itaitwa, Njia ya utakatifu; wasio safi hawatapita juu yake; bali itakuwa kwa ajili ya watu hao; wasafirio, wajapokuwa wajinga, hawatapotea katika njia hiyo. Hapo hapatakuwa na simba, wala mnyama mkali hatapanda juu yake; hawataonekana hapo; bali waliokombolewa watakwenda katika njia hiyo.” (Isaya 35:8, 9) Yehova amewakomboa watu wake! Hao ndio watu wake “waliokombolewa,” naye awahakikishia kwamba watasafiri salama salimini warudipo nyumbani. Je, kuna barabara halisi kutoka Babiloni hadi Yerusalemu iliyotengenezwa, kuinuliwa, na kuzungushwa ua? La, bali ulinzi wa Yehova juu ya watu wake wakiwa safarini ni hakika sana hivi kwamba ni kama wako kwenye njia kuu kama hiyo.—Linganisha Zaburi 91:1-16.

      16 Wayahudi walindwa pia kutokana na hatari za kiroho. Njia kuu hiyo ya kitamathali ni “Njia ya utakatifu.” Wale wanaopuuza mambo matakatifu au walio wachafu kiroho hawafai kutembea katika njia hiyo. Hawatakikani katika nchi iliyorudishwa. Waliokubaliwa wana nia nzuri. Hawarudi Yuda na Yerusalemu kwa roho ya kuonea fahari taifa lao au ili kufuatia masilahi ya kibinafsi. Wayahudi wanaozingatia mambo ya kiroho watambua kuwa sababu kuu ya kurudi kwao ni kuanzisha tena ibada safi ya Yehova nchini humo.—Ezra 1:1-3.

      Watu wa Yehova Wafurahi

      17. Unabii wa Isaya wamalizikia kwa masimulizi gani yenye furaha?

      17 Sura ya 35 ya unabii wa Isaya yamalizikia kwa masimulizi yenye furaha: “Hao waliokombolewa na BWANA watarudi, watafika Sayuni wakiimba; na furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao; nao watapata kicheko na furaha, huzuni na kuugua zitakimbia.” (Isaya 35:10) Huenda mateka Wayahudi walioutegemea unabii huo ili kupata faraja na tumaini wakiwa uhamishoni walihangaikia jinsi ambavyo mambo mbalimbali ya unabii yangetimizwa. Labda hawajaelewa mambo mengi yanayotiwa ndani katika unabii huo. Licha ya hayo, imekuwa wazi sana kwamba “watarudi, watafika Sayuni.”

      18. Huzuni na majonzi huko Babiloni zabadilikaje kuwa shangwe na furaha katika nchi iliyorudishwa?

      18 Basi, katika mwaka wa 537 K.W.K., wanaume wapatao 50,000 (ikijumlisha watumwa zaidi ya 7,000) pamoja na wanawake na watoto wafunga safari ya miezi minne kurudi Yerusalemu, wakimtumaini Yehova kabisa. (Ezra 2:64, 65) Miezi michache tu baadaye, madhabahu ya Yehova yajengwa, ambayo ni hatua ya kwanza kuelekea ujenzi kamili wa hekalu. Unabii wa Isaya ambao umedumu miaka 200 watimia. Badala ya huzuni na majonzi ya taifa hilo huko Babiloni, sasa ni shangwe na furaha katika nchi iliyorudishwa. Yehova ametimiza ahadi yake. Paradiso—paradiso halisi na ya kiroho vilevile—imerudishwa!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki