-
‘Wafarijini Watu Wangu’Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Mungu Mwenye Nguvu Anayetunza Kondoo Zake kwa Wororo
12, 13. (a) Kwa nini ahadi ya kurudishwa yaweza kutumainiwa? (b) Kuna habari gani njema kwa wahamishwa Wayahudi, na kwa nini wanaweza kuwa na uhakika?
12 Isaya atoa sababu ya pili ya kuitumaini ahadi ya kurudishwa. Anayeahidi ni Mungu mwenye nguvu anayewatunza watu wake kwa wororo. Isaya aendelea: “Wewe uuhubiriye Sayuni habari njema, panda juu ya mlima mrefu; wewe uuhubiriye Yerusalemu habari njema, paza sauti kwa nguvu; paza sauti yako, usiogope; iambie miji ya Yuda, Tazameni, Mungu wenu. Tazameni, Bwana Mungu atakuja kama shujaa [“na nguvu,” “NW,” kielezi-chini], na mkono wake ndio utakaomtawalia; tazameni, thawabu yake i pamoja naye, na ijara yake i mbele zake. Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake, nao wanyonyeshao atawaongoza polepole.”—Isaya 40:9-11, chapa ya 1989.
13 Katika nyakati za Biblia, wanawake walikuwa na desturi ya kusherehekea ushindi, wakipaza sauti au wakiimba habari njema za mapigano waliyoshinda au za kitulizo kinachokuja. (1 Samweli 18:6, 7; Zaburi 68:11) Isaya aonyesha kwa unabii kwamba kuna habari njema kwa wahamishwa Wayahudi, habari zinazoweza kutangazwa kwa sauti kubwa bila hofu, hata kwenye vilele vya milima—Yehova atawaongoza watu wake kurudi kwenye jiji wanalolipenda, Yerusalemu! Wanaweza kuwa na uhakika, kwa kuwa Yehova atakuja “na nguvu.” Basi hakuna kiwezacho kumzuia asitimize ahadi yake.
14. (a) Isaya atoaje kielezi cha jinsi ambavyo Yehova atawaongoza watu wake kwa wororo? (b) Ni kielelezo gani kinachoonyesha jinsi ambavyo wachungaji hutunza kondoo zao kwa wororo? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 405.)
14 Hata hivyo, Mungu huyu mwenye nguvu ana sifa ya wororo. Isaya aeleza kwa uchangamfu jinsi Yehova atakavyowaongoza watu wake kurudi nchini kwao. Yehova ni kama mchungaji mwenye upendo anayewakusanya pamoja wana-kondoo wake na kuwabeba “kifuani” mwake. Yaonekana neno hili “kifua” larejezea mikunjo ya juu ya vazi. Nyakati nyingine wachungaji hubebea kifuani wana-kondoo waliozaliwa hivi karibuni ambao hawauwezi mwendo wa kundi. (2 Samweli 12:3) Onyesho kama hilo lenye kuvutia linalotokana na maisha ya uchungaji hapana shaka lawapa tena watu wa Yehova waliohamishwa uhakikishio wa utunzaji wake wenye upendo kwao. Kwa hakika Mungu huyo mwenye nguvu lakini mwenye wororo aweza kutumainiwa atimize yale ambayo amewaahidi!
-
-
‘Wafarijini Watu Wangu’Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Mwenye Nguvu Zote, Mwenye Hekima Yote
17, 18. (a) Kwa nini wahamishwa Wayahudi waweza kuitumaini ahadi ya kurudishwa? (b) Isaya auliza maswali gani yenye kutia hofu?
17 Wahamishwa Wayahudi waweza kuitumaini ahadi ya kurudishwa kwa sababu Mungu ni mwenye nguvu zote na mwenye hekima yote. Isaya asema: “Ni nani aliyeyapima maji kwa konzi ya mkono wake, na kuzikadiri mbingu kwa shubiri, na kuyashika mavumbi ya dunia katika pishi, na kuipima milima kwa uzani, na vilima kama kwa mizani? Ni nani aliyemwongoza roho ya BWANA, na kumfundisha kwa kuwa mshauri wake? Alifanya shauri na nani, ni nani aliyemwelimisha na kumfunza njia ya hukumu, na kumfunza maarifa, na kumwonyesha njia ya fahamu?”—Isaya 40:12-14.
18 Hayo ni maswali yanayotia hofu ambayo wahamishwa Wayahudi wapaswa kuyatafakari. Je, wanadamu duni waweza kuyazuia mawimbi yenye nguvu ya bahari? Haiwezekani hata kidogo! Na bado, kwa maoni ya Yehova, bahari zinazoifunika dunia ni kama tone la maji katika kiganja cha mkono wake.b Je, wanadamu duni waweza kuzipima mbingu kubwa mno, zenye kujaa nyota au kupima milima na vilima vya dunia? La. Ingawa hivyo, Yehova huzipima mbingu kwa urahisi kama vile mwanadamu awezavyo kupima kitu fulani kwa shubiri, yaani, urefu wa kutoka mwisho wa kidole gumba hadi ncha ya kidole cha mwisho wakati mkono umenyoshwa. Ni kana kwamba Mungu aweza kuipima milima na vilima kwa mizani. Je, hata wanadamu wenye akili zaidi waweza kumshauri Mungu kuhusu mambo ya kufanya sasa au kumwambia yale ya kufanya wakati ujao? La, hasha!
19, 20. Ili kukazia ukuu wa Yehova, Isaya atumia vielezi gani?
19 Namna gani mataifa yenye nguvu duniani—je, yaweza kumpinga Mungu atimizapo neno lake la ahadi? Isaya ajibu kwa kuyafafanua mataifa ifuatavyo: “Tazama, mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani; tazama, yeye huvinyanyua visiwa kama ni kitu kidogo sana. Lebanoni nayo hautoshi kwa kuni, wala wanyama wake hawatoshi kwa kafara. Mataifa yote huwa kama si kitu mbele zake; huhesabiwa kwake kuwa duni ya si kitu, na ubatili.”—Isaya 40:15-17.
20 Kwa maoni ya Yehova, mataifa yote ni kama tone la maji linaloanguka kutoka katika ndoo. Ni kama tu mavumbi membamba sana yaliyo kwenye mizani, yasiyo na uzito wowote.c Tuseme kwamba mtu fulani angejenga madhabahu kubwa mno na kutumia kuni zote zinazofunika milima ya Lebanoni kwenye madhabahu hiyo. Kisha atoe dhabihu ya wanyama wote walio katika milima hiyo. Hata matoleo hayo yote hayangemfaa Yehova. Kana kwamba mfano uliotumiwa hadi sasa hautoshi, Isaya atoa taarifa yenye nguvu hata zaidi—mataifa yote “si kitu” machoni pa Yehova.—Isaya 40:17.
21, 22. (a) Isaya akaziaje kwamba Yehova hana kifani? (b) Ufafanuzi ulio waziwazi wa Isaya watuongoza kwenye mkataa gani? (c) Nabii Isaya aandika taarifa gani ambayo ni sahihi kisayansi? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 412.)
21 Ili kukazia zaidi kwamba Yehova hawezi kulinganishwa, Isaya aanza kuonyesha upumbavu wa wale wanaotengeneza sanamu kutokana na dhahabu, fedha, au miti. Ni upumbavu kama nini kufikiri kuwa sanamu hizo zaweza kuwa mfano unaofaa wa ‘Yeye anayeketi juu ya duara ya dunia’ na ambaye huwatawala wakazi wake!—Soma Isaya 40:18-24.
22 Ufafanuzi wote huo ulio waziwazi hutuongoza kwenye mkataa mmoja—hakuna kiwezacho kumzuia Yehova aliye mwenye nguvu zote, mwenye hekima yote, na asiye na kifani, asiitimize ahadi yake. Maneno ya Isaya yaliwafariji na kuwaimarisha kama nini wahamishwa Wayahudi huko Babiloni waliotamani kurudi nchini kwao! Leo sisi pia twaweza kuwa na uhakika kwamba ahadi za Yehova kwa ajili ya wakati wetu ujao zitatimia.
“Ni Nani Aliyeziumba Hizi”?
23. Sababu gani wahamishwa Wayahudi waweza kutiwa moyo, na sasa Yehova akazia jambo gani kujihusu mwenyewe?
23 Bado kuna sababu nyingine inayowatia moyo wahamishwa Wayahudi. Yeye anayeahidi ukombozi ni Muumba wa vitu vyote na Chanzo cha nishati yenye msukumo. Ili kukazia uwezo wake wa ajabu, Yehova akazia uwezo wake unaoonekana katika uumbaji: “Mtanifananisha na nani, basi, nipate kuwa sawa naye? asema yeye aliye Mtakatifu. Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake [“nishati yake yenye msukumo,” “NW”], na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—Isaya 40:25, 26.
24. Huku akijisemea mwenyewe, Yehova aonyeshaje kwamba hakuna anayelingana naye?
24 Mtakatifu wa Israeli anajisemea mwenyewe. Ili kuonyesha kwamba hakuna anayelingana naye, Yehova aelekeza fikira kwenye nyota za mbinguni. Kama vile kamanda wa kijeshi anayeongoza majeshi yake, ndivyo Yehova anavyoongoza nyota. Iwapo angezikusanya, ‘hapana moja isingekuwapo mahali pake.’ Ingawa idadi ya nyota ni kubwa, yeye huziita kila moja kwa jina, kwa kutumia jina la kibinafsi au mtajo ulio kama jina. Kama vile wanajeshi watiifu, nyota hukaa mahali pake na kufuata utaratibu ufaao, kwa kuwa Kiongozi wao ana wingi wa “nishati yenye msukumo” naye ni “hodari kwa nguvu.” Kwa hiyo, wahamishwa Wayahudi wana sababu ya kuwa na tumaini. Muumba, anayeziongoza nyota, ana nguvu za kuwategemeza watumishi wake.
25. Twaweza kuitikiaje mwaliko wa Mungu ulioandikwa kwenye Isaya 40:26, na kukiwa na matokeo gani?
25 Ni nani kati yetu awezaye kuukataa mwaliko wa Mungu ulioandikwa kwenye Isaya 40:26: “Inueni macho yenu juu, mkaone”? Uvumbuzi mbalimbali wa waastronomia wa leo umeonyesha kuwa mbingu zilizojaa nyota ni za ajabu hata zaidi kuliko zilivyoonekana katika siku ya Isaya. Waastronomia wanaotazama mbinguni wakitumia darubini kali wanakadiria kuwa ulimwengu unaoonekana una makundi ya nyota yapatayo bilioni 125. Lahaula, kwa makadirio fulani, mojawapo la makundi hayo liitwalo Kilimia, lina nyota zaidi ya bilioni 100! Kujua hayo kwapaswa kutuchochea tumstahi Muumba wetu kutoka moyoni na kulitumaini kabisa neno lake la ahadi.
26, 27. Fikira za wahamishwa huko Babiloni zafafanuliwaje, nao wapaswa kujua mambo gani?
26 Akitambua kwamba kuishi utekwani kwa miaka mingi kutapunguza ari ya wahamishwa Wayahudi, Yehova ampulizia Isaya kuandika mapema maneno haya yenye kitia-moyo: “Mbona unasema, Ee Yakobo, mbona unanena, Ee Israeli, Njia yangu imefichwa, BWANA asiione, na hukumu yangu imempita Mungu wangu asiiangalie? Je! wewe hukujua? hukusikia? Yeye Mungu wa milele, BWANA, Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki; akili zake hazichunguziki.”—Isaya 40:27, 28.
27 Isaya aandika maneno ya Yehova yanayoeleza fikira za wahamishwa huko Babiloni, mamia ya kilometa kutoka nchini kwao. Wengine waona kwamba Mungu wao haioni au haijui “njia” yao, yaani, mwendo mgumu wa maisha yao. Wanafikiri kwamba Yehova hajali ukosefu wa haki unaowapata. Wanakumbushwa mambo wanayopaswa kujua kwa kujionea, la sivyo, kwa kusikia. Yehova ana uwezo na nia ya kuwakomboa watu wake. Yeye ni Mungu wa milele na Muumba wa dunia nzima. Kwa hiyo, bado ana nguvu alizoonyesha wakati wa uumbaji, na hata Babiloni yenye nguvu haiwezi kulingana naye. Mungu wa namna hiyo hawezi kuchoka wala kuwatamausha watu wake. Hawapaswi kutarajia kuyaelewa kikamilifu matendo ya Yehova, kwa maana uelewevu wake—au ufahamu wenye kina, na utambuzi—unazidi uwezo wao wa ufahamu.
28, 29. (a) Yehova awakumbushaje watu wake kwamba atawasaidia wenye kuzimia? (b) Ni kielezi gani kimetumiwa ili kuonyesha jinsi ambavyo Yehova huwapa watumishi wake nguvu?
28 Kupitia Isaya, Yehova aendelea kuwatia moyo wahamishwa walioshuka moyo: “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”—Isaya 40:29-31.
29 Azungumziapo uhitaji wa kumpa nguvu mwenye kuzimia, huenda Yehova azingatia safari yenye kuchosha sana ambayo itabidi wahamishwa wafunge ili kurudi nyumbani. Yehova awakumbusha watu wake kwamba yeye ana zoea la kuwasaidia watu wanaozimia na ambao humtegemea. Hata wanadamu wenye nguvu zaidi—“vijana” na “wanaume vijana”—huenda wakazimia na kuanguka kwa sababu ya uchovu. Ingawa hivyo, Yehova aahidi kuwapa wale wanaomtumaini nguvu, nguvu kamili za kukimbia na kutembea. Kielezi cha tai, ndege mwenye nguvu awezaye kupaa kwa saa kadhaa pasipo kutua kana kwamba hatumii nguvu, kimetumiwa kuonyesha jinsi Yehova anavyowapa watumishi wake nguvu.d Huku wakiwa na matarajio hayo ya kutegemezwa na Mungu, wahamishwa Wayahudi hawana sababu ya kufa moyo.
-