-
Fundisho la Ufufuo LinakuhusuMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
Ufufuo na Urafiki Pamoja na Yehova
12, 13. Abrahamu alikuwa na sababu gani nzuri sana ya kuamini katika ufufuo?
12 Abrahamu, anayetajwa kuwa “rafiki ya Yehova,” alikuwa na imani ya pekee. (Yakobo 2:23) Paulo alitaja imani ya Abrahamu mara tatu alipowataja wanaume na wanawake wenye imani katika sura ya 11 ya kitabu cha Waebrania. (Waebrania 11:8, 9, 17) Anapomtaja Abrahamu mara ya tatu anakazia imani ambayo Abrahamu alionyesha wakati ambapo, kwa utii, alimtayarisha mwanawe Isaka ili amtoe akiwa dhabihu. Abrahamu alisadiki kwamba Yehova hangekosa kutimiza ahadi yake ya kumpa uzao kupitia Isaka. Hata kama Isaka angekufa kwa kutolewa akiwa dhabihu, Abrahamu “alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua hata kutoka kwa wafu.”
13 Hivyo, Yehova alipoona imani yenye nguvu ya Abrahamu, aliandaa mnyama atolewe akiwa dhabihu badala ya Isaka. Hata hivyo, kisa cha Isaka kinatoa mfano wa ufufuo, kama Paulo alivyoeleza: “Kutoka huko [Abrahamu] alimpokea [Isaka] pia kwa njia ya mfano.” (Waebrania 11:19) Isitoshe, tayari Abrahamu alikuwa na sababu nzuri sana ya kuamini ufufuo. Je, Yehova hakurudisha nguvu za uzazi za Abrahamu wakati yeye na mke wake Sara walipompata mwana wao Isaka wakiwa wazee?—Mwanzo 18:10-14; 21:1-3; Waroma 4:19-21.
14. (a) Kulingana na Waebrania 11:9, 10, Abrahamu alingojea nini? (b) Ni jambo gani ambalo ni lazima litukie kwa Abrahamu ili apate baraka za Ufalme katika ulimwengu mpya? (c) Tunawezaje kupata baraka za Ufalme?
14 Paulo alitaja kwamba Abrahamu alikuwa mkaaji mgeni, aliyeishi katika mahema “akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Waebrania 11:9, 10) Hilo ni jiji la mfano, wala si jiji halisi kama Yerusalemu, ambako hekalu la Mungu lilikuwa. Jiji hilo ni Ufalme wa mbinguni wa Mungu ambao mtawala wake ni Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000. Wanapokuwa katika utukufu wao mbinguni, watawala hao 144,000 pia wanaitwa “jiji takatifu, Yerusalemu Jipya,” “bibi-arusi” wa Kristo. (Ufunuo 21:2) Katika mwaka wa 1914, Yehova alimtawaza Yesu kuwa Mfalme wa Kimasihi wa Ufalme wa mbinguni na kumwamuru atawale katikati ya adui zake. (Zaburi 110:1, 2; Ufunuo 11:15) Ili kupata baraka za utawala wa Ufalme, lazima Abrahamu, “rafiki ya Yehova,” aishi tena. Vivyo hivyo, ili tupate baraka za Ufalme, lazima tuwe hai katika ulimwengu mpya wa Mungu tukiwa sehemu ya umati mkubwa utakaookoka Har–Magedoni au wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu. (Ufunuo 7:9, 14) Lakini ni nini msingi wa tumaini la ufufuo?
-
-
Fundisho la Ufufuo LinakuhusuMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
17. (a) Ayubu alikuwa na tumaini gani? (b) Andiko la Ayubu 14:15 linafunua nini kumhusu Yehova, na jambo hilo linakufanya uhisije?
17 Ayubu, mtu mwaminifu aliyeishi kabla ya Ukristo, alitarajia kufufuliwa pia. Shetani alimtesa sana. Ayubu alikuwa tofauti na rafiki zake wa uwongo ambao hawakutaja ufufuo kamwe. Alifarijiwa na tumaini hilo la ufufuo na kuuliza: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Akijibu swali lake mwenyewe, Ayubu alisema: “Mimi nitangojea siku zote za kazi yangu ya kulazimishwa, mpaka kitulizo changu kije.” Alipozungumza na Mungu wake Yehova, Ayubu alisema hivi: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.” Kuhusu hisia za Muumba wetu mwenye upendo, Ayubu alisema: “Utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Naam, Yehova anatazamia kwa hamu wakati ambapo waaminifu watakuwa hai tena kupitia ufufuo. Kwa kweli, jambo hilo hutuvuta kwake tunapotafakari kuhusu upendo na fadhili zisizostahiliwa ambazo yeye hutuonyesha ingawa sisi si wakamilifu!—Waroma 5:21; Yakobo 4:8.
18, 19. (a) Danieli ana tazamio gani la kuishi tena? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?
18 Nabii Danieli, ambaye alitajwa na malaika wa Mungu kuwa “mtu mwenye kutamanika sana,” alimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa muda mrefu. (Danieli 10:11, 19) Alidumisha utimilifu wake kwa Yehova tangu apelekwe uhamishoni mwaka wa 617 K.W.K., hadi alipokufa muda fulani baada ya kupata maono mwaka wa 536 K.W.K., ambao ulikuwa mwaka wa tatu wa utawala wa Koreshi, mfalme wa Uajemi. (Danieli 1:1; 10:1) Wakati fulani katika mwaka huo wa tatu wa utawala wa Koreshi, Danieli aliona maono kuhusu mfuatano wa serikali za ulimwengu ambao utakoma wakati wa dhiki kuu inayokuja. (Danieli 11:1–12:13) Kwa kuwa hakuweza kuelewa maono hayo kikamili, Danieli alimuuliza hivi malaika aliyetumwa kumwonyesha maono hayo: “Ee bwana wangu, mwisho wa mambo hayo utakuwa nini?” Malaika huyo alimjibu kwa kutaja “wakati wa mwisho” ambapo “wale walio na ufahamu wataelewa.” Danieli mwenyewe alikuwa na tazamio gani? Malaika huyo alimwambia: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” (Danieli 12:8-10, 13) Danieli atarudi “katika ufufuo wa walio waadilifu,” wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo.—Luka 14:14.
-
-
Ni Nani Watakaofufuliwa?Mnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
2, 3. (a) Abrahamu, Isaka, na Yakobo wanangojea thawabu gani? (b) Ni maswali gani yanayotokea?
2 Yesu alikuwa akizungumza na Masadukayo fulani ambao hawakuamini ufufuo. Yesu alisema: “Hata Musa alifunua kwamba wafu watafufuliwa, katika masimulizi juu ya ule mti wa miiba, anapomwita Yehova ‘Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, hao wote wako hai.” (Luka 20:27, 37, 38) Kwa kusema hivyo, Yesu alithibitisha kwamba kulingana na maoni ya Mungu, bado Abrahamu, Isaka, na Yakobo, waliokufa zamani, wako hai katika kumbukumbu ya Mungu. Kama Ayubu, wanangojea ‘kazi yao ya kulazimishwa’ iishe, yaani, kulala usingizi katika kifo. (Ayubu 14:14) Watafufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.
-