-
Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Inamaanisha kwamba Mungu anawapenda watoto na vijana. Lakini atawafufua watu wengine pia. Je, Mungu atawafufua watu waliofanya mema tu?— Tunaweza kufikiria hivyo. Lakini, watu wengi hawakujifunza ukweli kumhusu Yehova Mungu na Mwana wake. Kwa hiyo walifanya mabaya kwa sababu walifundishwa mambo yasiyo ya kweli. Unafikiri Yehova atawafufua watu kama hao?—
Biblia inasema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Kwa nini wale ambao hawakuwa waadilifu, au wale ambao hawakufanya mema, wafufuliwe?— Wao watafufuliwa kwa sababu hawakupata nafasi kamwe ya kujifunza kumhusu Yehova na yale anayotaka watu wafanye.
Unafikiri watu watafufuliwa lini?— Fikiria wakati Lazaro alipokufa na ahadi ambayo Yesu alimpa Martha dada yake: “Ndugu yako atafufuka.” Martha akajibu: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:23, 24) Martha alimaanisha nini aliposema Lazaro atafufuka katika “siku ya mwisho”?—
Martha alikuwa amesikia ahadi hii ya Yesu: ‘Wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Kwa hiyo “siku ya mwisho” ni wakati wale wote walio katika kumbukumbu la Mungu watakapofufuliwa. Siku hiyo ya mwisho si siku yenye muda wa saa 24. Itakuwa kipindi cha miaka elfu moja. Biblia inasema kwamba katika siku hiyo ‘Mungu atawahukumu watu wa dunia.’ Watakaohukumiwa watatia ndani wale watakaofufuliwa.—Matendo 17:31; 2 Petro 3:8.
Hebu wazia jinsi itakavyokuwa siku yenye furaha ajabu! Wakati wa kipindi cha hiyo siku ya miaka elfu moja, mamilioni ya watu waliokufa watafufuliwa. Yesu anapaita mahali ambapo watu hao wataishi kuwa Paradiso. Na tuone Paradiso itakuwa wapi na jinsi hali itakavyokuwa.
Karibu saa tatu kabla ya Yesu kufa katika mti wa mateso, anamwambia mtu aliye kwenye mti wa mateso karibu naye kuhusu Paradiso. Mtu huyo anauawa kwa sababu ya uhalifu aliofanya. Lakini mhalifu huyu anapomwona Yesu na kusikia yanayosemwa juu Yake, anaanza kumwamini Yesu. Basi mhalifu huyo anasema: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu anamjibu: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43.
Yesu anamaanisha nini anaposema hivyo? Paradiso iko wapi?— Hebu fikiria. Kwanza kabisa hii Paradiso ilikuwa wapi?— Kumbuka kwamba Mungu aliwapa watu wa kwanza, Adamu na mke wake, paradiso papa hapa duniani ili waishi ndani yake. Iliitwa bustani ya Edeni. Kulikuwa na wanyama katika bustani hiyo, lakini hawakuwa hatari. Kulikuwa na miti yenye matunda mengi matamu, na vilevile mto mkubwa. Palikuwa mahali pazuri ajabu pa kuishi!—Mwanzo 2:8-10.
Tunaposoma kwamba mhalifu huyo atakuwa katika Paradiso, tunapaswa kuona akilini dunia hii ikiwa mahali maridadi pa kuishi. Je, Yesu atakuwa katika Paradiso hapa duniani pamoja na huyo mtu ambaye zamani alikuwa mhalifu?— La. Je, unajua ni kwa nini hatakuwa duniani?—
Ni kwa sababu Yesu atakuwa mbinguni akitawala akiwa Mfalme juu ya dunia Paradiso. Kwa hiyo, Yesu atakuwa pamoja na mtu huyo katika maana ya kwamba Yesu atamfufua na kumtimizia mahitaji yake. Lakini kwa nini Yesu atamruhusu mtu aliyekuwa mhalifu aishi katika Paradiso?— Hebu tuone jibu.
Kabla ya mhalifu huyo kuzungumza na Yesu, je, alijua makusudi ya Mungu?— La. Alifanya mabaya kwa sababu hakujua kweli kumhusu Mungu. Akiwa katika Paradiso atafundishwa makusudi ya Mungu. Kisha atapata nafasi ya kuthibitisha kwamba kwa kweli anampenda Mungu kwa kufanya mapenzi Yake.
-
-
Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Ni wangapi watakaoishi katika dunia Paradiso?— Biblia haisemi. Lakini Mungu aliwaambia Adamu na Hawa walipokuwa katika bustani ya Edeni wazae watoto na kuijaza dunia. Wakakosa kufanya hivyo. Lakini Mungu atahakikisha kwamba kusudi lake la kuijaza dunia watu waadilifu linatimizwa.—Mwanzo 1:28; Isaya 45:18; 55:11.
Hebu wazia tu jinsi itakavyopendeza kuishi katika Paradiso! Dunia yote itakuwa kama bustani. Itakuwa na ndege na wanyama na miti na maua maridadi ya kila aina. Hakuna mtu atakayekuwa na maumivu kwa sababu ya ugonjwa wala hakuna mtu atakayekufa. Watu wote watakuwa marafiki. Ikiwa tunataka kuishi milele katika Paradiso, basi tujitayarishe wakati huu.
-