Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’
    Mkaribie Yehova
  • Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’
    Mkaribie Yehova
    • Kuwafufua Wafu

      17, 18. (a) Kwa nini Yesu aliwashutumu Masadukayo? (b) Ni tukio gani lililomfanya Eliya amwombe Yehova amfufue mfu?

      17 Katika karne ya kwanza W.K., viongozi fulani wa kidini, wanaoitwa Masadukayo, hawakuamini ufufuo. Yesu aliwashutumu hivi: “Mwakosea, kwa sababu hamjui wala Maandiko wala nguvu ya Mungu.” (Mathayo 22:29) Naam, Maandiko yanafunua kwamba Yehova ana nguvu za kufufua. Jinsi gani?

      18 Hebu wazia jambo lililotukia siku za Eliya. Mjane mmoja alikuwa amebeba mwili wa mwanaye pekee. Mvulana huyo alikuwa mfu. Haikosi jambo hilo lilimshtua nabii Eliya, aliyekuwa ameishi katika nyumba ya mjane huyo kwa muda fulani. Mapema, alimwokoa mtoto huyo asife njaa. Yaelekea Eliya alimpenda sana mvulana huyo. Mamaye alihuzunika sana. Mvulana huyo pekee ndiye aliyemfanya amkumbuke mume wake aliyekuwa amekufa. Huenda alitumaini kwamba mwanaye angemtunza akizeeka. Mjane huyo aliyefadhaika alidhani kwamba labda alikuwa akiadhibiwa kwa sababu ya dhambi fulani aliyotenda zamani. Eliya hakuweza kuvumilia msiba huo wenye kusikitisha sana. Alitwaa huyo mfu kwa upole kutoka katika kifua cha mamaye, akampeleka katika chumba chake orofani, kisha akamwomba Yehova Mungu arudishe nafsi au uhai, wa mtoto huyo.—1 Wafalme 17:8-21.

      19, 20. (a) Abrahamu alionyeshaje imani kwamba Yehova anaweza kufufua, na imani hiyo ilitegemea nini? (b) Yehova alimthawabishaje Eliya kwa sababu ya imani yake?

      19 Eliya hakuwa mtu wa kwanza kuamini ufufuo. Miaka mingi mapema, Abrahamu aliamini kwamba Yehova ana uwezo wa kufufua. Na alikuwa na sababu nzuri ya kuamini hivyo. Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 100 na Sara miaka 90, Yehova alirudisha uwezo wao wa kuzaa, na Sara akamzaa mwana kimuujiza. (Mwanzo 17:17; 21:2, 3) Baadaye, kijana huyo alipokuwa mtu mzima, Yehova alimwamuru Abrahamu amtoe kuwa dhabihu. Abrahamu alikuwa na imani, alitambua kwamba Yehova angeweza kumfufua Isaka mwanaye mpendwa. (Waebrania 11:17-19) Yaonekana imani hiyo thabiti ndiyo iliyomfanya Abrahamu, kabla ya kukwea mlimani kumtoa mwanaye, awahakikishie watumishi wake kwamba yeye na Isaka wangerudi pamoja.—Mwanzo 22:5.

      Mjane akimpokea kwa furaha mwana wake aliyefufuliwa na nabii Eliya

      “Tazama, mwanao yu hai”!

      20 Yehova aliingilia na Isaka hakuuawa, hivyo ufufuo haukuhitajiwa wakati huo. Hata hivyo, katika kisa cha Eliya, mwana wa mjane tayari alikuwa amekufa—lakini si kwa muda mrefu. Yehova alimthawabisha nabii huyo mwenye imani kwa kumfufua mwana huyo! Kisha Eliya akamrudisha mvulana huyo kwa mamaye, akanena maneno haya yasiyoweza kusahaulika: “Tazama, mwanao yu hai”!—1 Wafalme 17:22-24.

      21, 22. (a) Ufufuo mbalimbali unaosimuliwa katika Maandiko ulikuwa na kusudi gani? (b) Ni watu wangapi watakaofufuliwa katika Paradiso, na ni nani atakayewafufua?

      21 Hivyo basi, kwa mara ya kwanza kabisa katika Biblia, twaona Yehova akitumia uwezo wake wa kuwafufua wanadamu. Baadaye, Yehova pia aliwapa Elisha, Yesu, Paulo, na Petro uwezo wa kufufua wafu. Bila shaka, wale waliofufuliwa walikufa hatimaye. Hata hivyo, matukio hayo ya Biblia yanatuonyesha mambo mazuri yatakayotukia wakati ujao.

      22 Katika Paradiso, Yesu atakuwa “ufufuo na uhai.” (Yohana 11:25) Atafufua mamilioni ya wafu, na kuwapa fursa ya kuishi milele katika Paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29) Hebu wazia jinsi marafiki wapendwa na watu wa jamaa waliotenganishwa na kifo watakavyokumbatiana kwa shangwe kubwa ajabu! Wanadamu wote watamsifu Yehova kwa ajili ya uwezo wake wa kufufua.

      23. Ni tukio gani lililokuwa uthibitisho mkuu zaidi wa uwezo wa Yehova, na hilo linatuhakikishia jinsi gani tumaini letu la wakati ujao?

      23 Yehova ametuhakikishia kabisa kwamba tumaini hilo ni hakika. Yehova alithibitisha uwezo wake kwa njia kuu kupita zote alipomfufua Mwanaye, Yesu, akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo, na kumpa cheo cha pili katika ulimwengu mzima. Mamia ya watu walimwona Yesu aliyefufuliwa. (1 Wakorintho 15:5, 6) Ushahidi huo unatosha kuwasadikisha wale wanaotilia shaka jambo hilo. Yehova ana uwezo wa kufufua.

      24. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atafufua wafu, na sote tunaweza kuthamini tumaini gani?

      24 Si kwamba tu Yehova ana uwezo wa kufufua wafu bali pia ana tamaa ya kufanya hivyo. Mwanamume mwaminifu Yobu alipuliziwa kusema kwamba kwa kweli Yehova ana tamaa ya kuwafufua wafu. (Ayubu 14:15) Je, wewe huvutiwa na Mungu wetu, ambaye anatamani kutumia kwa upendo uwezo wake wa kufufua? Kumbuka kwamba ufufuo ni sehemu moja tu ya kazi kubwa ambayo Yehova atafanya wakati ujao ya kufanya mambo kuwa mapya. Kadiri unavyomkaribia zaidi, endelea kuthamini tumaini la pekee sana la kwamba huenda ukawapo Yehova ‘atakapofanya vitu vyote kuwa vipya.’—Ufunuo 21:5.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki