-
Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?
“Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.”—YOHANA 11:25.
1, 2. Kwa nini mwabudu wa Yehova anahitaji kuwa na uhakika katika tumaini la ufufuo?
TUMAINI lako katika ufufuo ni lenye nguvu kadiri gani? Je, hilo hukutia nguvu usihofu kufa na kukufariji upotezapo wapendwa wako katika kifo? (Mathayo 10:28; 1 Wathesalonike 4:13) Je, wewe ni kama watumishi wa Mungu wa zamani, waliovumilia kupigwa mijeledi, kudhihakiwa, kuteswa, kufungwa gerezani, kwa kuimarishwa na imani katika ufufuo?—Waebrania 11:35-38.
2 Naam, mwabudu wa Yehova mwenye moyo mweupe hapaswi kuwa na shaka yoyote kwamba kutakuwa na ufufuo, na uhakika wake wapaswa kuathiri namna anavyoishi. Ni jambo lenye kupendeza kufikiria uhakika wa kwamba katika wakati wa Mungu ufaao, bahari, kifo, na Hadesi vitatoa wafu walio ndani yavyo, nao hao wenye kufufuliwa watakuwa na matazamio ya kuishi milele katika paradiso duniani.—Ufunuo 20:13; 21:4, 5.
Shaka Kuhusu Uhai wa Wakati Ujao
3, 4. Watu wengi bado huamini nini kuhusu uhai baada ya kifo?
3 Jumuiya ya Wakristo imefundisha kwa muda mrefu kwamba kuna uhai baada ya kifo. Makala moja katika gazeti la U.S. Catholic ilisema hivi: “Kwa karne nyingi, Wakristo wamejaribu vile wawezavyo kukubali na kuvumilia kutamauka na mateso yaletwayo na maisha haya, kwa kutazamia kwa hamu maisha mengine, yenye amani na uradhi, yenye kutosheleza na yenye furaha.” Hata ingawa katika nchi kadhaa za Jumuiya ya Wakristo watu wamejitenga na mambo ya dini na kwa njia fulani wanaidharau, wengi bado huhisi kwamba kuna namna fulani ya uhai baada ya kifo. Lakini kuna mambo mengi ambayo hawana uhakika kuyahusu.
4 Makala moja katika gazeti la Time ilisema hivi: “Watu bado huamini katika [uhai wa baadaye]: ni vile tu ufahamu wao juu ya vile uhai huo ulivyo hasa, umetiwa giza zaidi, na ni mara chache sana wao huwasikia mapasta wao wakizungumza kuhusu hilo.” Kwa nini wahudumu wa kidini huzungumza mara chache zaidi kuhusu uhai wa baadaye kuliko walivyokuwa wakifanya? Msomi wa mambo ya kidini, Jeffrey Burton Russell, asema hivi: “Ninafikiri [makasisi] wanataka kuepuka kuzungumzia habari hiyo kwa sababu wao wahisi kwamba watalazimika kukabili kushuku waliko nako watu wengi.”
5. Watu wengi leo wana maoni gani kuhusu fundisho la moto wa helo?
5 Katika makanisa mengi, uhai wa baadaye hutia ndani mbingu na helo yenye moto. Na ikiwa makasisi wanasitasita kuzungumza kuhusu mbingu, watasitasita hata zaidi kuzungumza kuhusu helo. Makala moja ya gazeti la habari ilisema hivi: “Siku hizi hata makanisa yanayoamini katika kuadhibiwa milele katika helo . . . hayakazii fundisho hilo.” Kwa kweli, wanatheolojia wa kisasa hawaamini tena kwamba helo ni mahali halisi pa mateso, kama vile ilivyofundishwa katika Enzi za Kati. Badala yake, wao hupendelea aina ya helo ambayo “si mbaya sana.” Kulingana na watu wengi wenye maoni ya kisasa, watenda-dhambi walio katika helo hawateswi kihalisi, lakini huteseka kwa sababu ya “kutengwa na Mungu kiroho.”
6. Watu fulani hupataje kwamba wamepungukiwa na imani wakabilipo jambo lenye kuhuzunisha?
6 Kufanya mafundisho ya kanisa yasiwe makali sana ili yasiwaudhi watu wa kisasa wenye hisia nyepesi, kwaweza kusaidia kuepuka kuchukiwa kwa mafundisho fulani, lakini jambo hilo huwaacha mamilioni ya waenda-kanisani wenye mioyo myeupe wakijiuliza wataamini nini. Kwa sababu hiyo, wakabilipo kifo, mara nyingi watu hao hupata kwamba hawana imani. Mtazamo wao ni kama wa mwanamke ambaye alipoteza washiriki kadhaa wa familia yake katika aksidenti yenye kuhuzunisha. Alipoulizwa kama imani yake ya kidini ilikuwa imemfariji, alijibu kwa kusitasita, “Nadhani hivyo.” Lakini hata kama angalijibu kwa uhakika kwamba imani yake ya kidini ilikuwa imemsaidia, je, ingekuwa na manufaa gani ya muda mrefu kama imani yake haikuwa na msingi mzuri? Hilo ni jambo la maana kufikiriwa kwa sababu, kwa kweli mambo ambayo makanisa mengi hufundisha juu ya uhai wa wakati ujao ni tofauti sana na yale Biblia hufundisha.
Maoni ya Jumuiya ya Wakristo Kuhusu Uhai Baada ya Kifo
7. (a) Makanisa yaliyo mengi huamini nini? (b) Mwanatheolojia mmoja alifafanuaje fundisho la nafsi isiyoweza kufa?
7 Licha ya tofauti zao nyingi, karibu madhehebu yote ya Jumuiya ya Wakristo hukubali kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuwa hai baada ya kufa kwa mwili. Walio wengi huamini kwamba mtu anapokufa, huenda nafsi yake ikaenda mbinguni. Wengine huhofu kwamba huenda nafsi yao ikaenda helo yenye moto au purgatori. Lakini wazo la nafsi isiyoweza kufa ni jambo kuu katika maoni yao juu ya uhai wa wakati ujao. Mwanatheolojia, Oscar Cullmann, alieleza juu ya hilo katika taarifa yake iliyochapishwa katika kitabu Immortality and Resurrection. Aliandika hivi: “Kama tungeuliza Mkristo wa kawaida leo . . . kulingana na mawazo yake, Agano Jipya hufundisha nini kuhusu kitakachompata mwanadamu baada ya kifo, walio wengi wangejibu hivi: ‘Kutoweza kufa kwa nafsi.’” Hata hivyo, Cullmann aliongeza kusema hivi: “Wazo hilo ambalo limekubaliwa na wengi ni mojawapo ya sababu za kutoelewana kukubwa zaidi kwa Ukristo.” Cullmann alisema kwamba alisababisha mfoko wa ghadhabu aliposema hivyo mara ya kwanza. Hata hivyo, hakukosea.
8. Yehova alimwekea mwanamume na mwanamke wa kwanza taraja gani?
8 Yehova Mungu hakuwaumba wanadamu waende mbinguni baada ya kufa. Awali, hakukusudia wafe kamwe. Adamu na Hawa waliumbwa wakiwa wakamilifu na walipewa fursa ya kuijaza dunia kwa uzao mwadilifu. (Mwanzo 1:28; Kumbukumbu la Torati 32:4) Wazazi wetu wa kwanza waliambiwa kwamba wangekufa iwapo tu wangekosa kumtii Mungu. (Mwanzo 2:17) Kama wangaliendelea kuwa watiifu kwa Baba yao wa kimbingu, wangaliendelea kuishi duniani milele.
9. (a) Ni nini iliyo kweli kuhusu nafsi ya kibinadamu? (b) Ni nini hutukia kwa nafsi inapokufa?
9 Ingawa hivyo, kwa kusikitisha Adamu na Hawa walishindwa kumtii Mungu. (Mwanzo 3:6, 7) Mtume Paulo anayafafanua matokeo yenye kuhuzunisha hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Badala ya kuishi milele duniani, Adamu na Hawa walikufa. Basi, ni nini kilichotukia? Je, walikuwa na nafsi zisizoweza kufa ambazo sasa zingeweza kupelekwa kwenye helo yenye moto kwa sababu ya dhambi yao? Kinyume cha hilo, Biblia husema kwamba, mapema alipoumbwa, Adamu ‘alikuwa nafsi hai.’ (Mwanzo 2:7) Mwanadamu hakupewa nafsi; alikuwa nafsi, mtu anayeishi. (1 Wakorintho 15:45) Kumbe, si Adamu tu aliyekuwa “nafsi hai,” bali kama vile ionyeshwavyo katika Kiebrania ambacho kilitumiwa kuandika kitabu cha Mwanzo, wanyama wa hali ya chini pia walikuwa “nafsi hai”! (Mwanzo 1:24) Adamu na Hawa walipokufa, walikuwa nafsi zilizokufa. Hatimaye, ilitukia kwao kama vile Yehova alikuwa amemwambia Adamu: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”—Mwanzo 3:19.
10, 11. Kichapo New Catholic Encyclopedia hukubali nini kuhusu fundisho la Biblia juu ya nafsi, na hilo hulinganaje na yale Biblia husema?
10 Kichapo New Catholic Encyclopedia hukubaliana kimsingi na jambo hilo. Katika makala yake “Nafsi (katika Biblia),” chasema hivi: “Katika AK [“Agano la Kale,” au Maandiko ya Kiebrania], mwili na nafsi hazigawanywi kuwa sehemu mbili.” Chaongeza kusema kwamba katika Biblia, neno “nafsi” “halimaanishi kamwe kwamba nafsi ni tofauti na mwili au na mtu mwenyewe.” Kwa kweli, nafsi mara nyingi “humaanisha kiumbe chenyewe, kiwe mnyama au kiwe mwanadamu.” Uwazi huo ni wenye kuburudisha, lakini mtu anaweza tu kushangaa ni kwa nini waenda-kanisani kwa ujumla hawajafahamishwa mambo hayo ya hakika.
11 Waenda-kanisani wangaliepushwa na wasiwasi na hofu nyingi kama nini iwapo wangalijua kweli hii sahili ya Biblia: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa,” wala si kuteseka katika moto wa helo! (Ezekieli 18:4, ZSB) Ingawa jambo hilo ni tofauti sana na yale Jumuiya ya Wakristo hufundisha, linapatana kabisa na yale ambayo Solomoni, mwanamume mwenye hekima alipuliziwa kusema: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi la kawaida la wanadamu] uendako wewe.”—Mhubiri 9:5, 10.
12. Jumuiya ya Wakristo ilipata wapi fundisho lake kuhusu nafsi isiyoweza kufa?
12 Kwa nini Jumuiya ya Wakristo hufundisha mambo tofauti na yale Biblia husema? Kichapo New Catholic Encyclopedia, katika makala yake ya “Kutoweza Kufa kwa Nafsi na kwa Binadamu,” chasema kwamba Waandishi wa Kanisa walitegemeza imani yao juu ya nafsi isiyoweza kufa, katika “washairi na wanafalsafa na dhana ya kimapokeo ya Kigiriki wala si katika Biblia . . . Baadaye, wasomi walipendelea kutumia imani ya Plato au kanuni za Aristotle.” Kichapo hicho chataarifu kwamba “uvutano wa dhana ya Uplato na Uplato mpya”—kutia na imani katika nafsi isiyoweza kufa—hatimaye ziliingizwa “katika mambo ya msingi ya theolojia ya Kikristo.”
13, 14. Kwa nini si jambo la akili kutumaini kuelimishwa na wanafalsafa wapagani Wagiriki?
13 Je, wanaodai kuwa Wakristo wangalipaswa kugeukia wanafalsafa wapagani Wagiriki kujifunza jambo la msingi kama vile tumaini la uhai baada ya kifo? Bila shaka la. Paulo alipowaandikia Wakristo walioishi Korintho, Ugiriki, alisema hivi: “Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu; kwa maana imeandikwa: ‘Yeye hunasa wenye hekima katika ujanja wao wenyewe.’ Na tena: ‘Yehova ajua kwamba mawazowazo ya watu wenye hekima ni ya ubatili.’” (1 Wakorintho 3:19, 20) Wagiriki wa kale walikuwa waabudu-sanamu. Hivyo basi, wangeweza kuwaje chanzo cha ile kweli? Paulo aliwauliza Wakorintho hivi: “Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? Kwa maana sisi ni hekalu la Mungu aliye hai; kama vile Mungu alivyosema: ‘Mimi nitakaa miongoni mwao na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.’”—2 Wakorintho 6:16.
14 Ufunuo wa kupata kweli takatifu ulitolewa mara ya kwanza kupitia taifa la Israeli. (Waroma 3:1, 2) Baada ya mwaka wa 33 W.K., ulitolewa kupitia kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta la karne ya kwanza. Akizungumza kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza, Paulo alisema hivi: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua [mambo yaliyotayarishwa kwa ajili ya wale wampendao] kupitia roho yake.” (1 Wakorintho 2:10; ona pia Ufunuo 1:1, 2.) Fundisho la Jumuiya ya Wakristo juu ya kutokufa kwa nafsi limetolewa katika falsafa za Kigiriki. Haikufunuliwa kupitia ufunuo mbalimbali wa Mungu kwa Waisraeli au kupitia kutaniko la karne ya kwanza la Wakristo watiwa-mafuta.
Tumaini Halisi kwa Wafu
15. Kulingana na Yesu, wafu wana tumaini gani halisi?
15 Iwapo hakuna nafsi yoyote isiyoweza kufa, je, kuna tumaini gani halisi kwa wafu? Bila shaka kuna tumaini la ufufuo, ambalo ni fundisho kuu la Biblia, na ahadi ya Mungu ambayo kwa kweli ni ya ajabu. Yesu alimtolea rafiki yake Martha tumaini la ufufuo alipomwambia hivi: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.” (Yohana 11:25) Kumwamini Yesu kwamaanisha kuamini ufufuo, wala si kuamini nafsi isiyoweza kufa.
16. Kwa nini ni jambo la akili kuamini ufufuo?
16 Mapema Yesu alikuwa amezungumza kuhusu ufufuo aliposema kwa Wayahudi fulani hivi: “Msistaajabie hili, kwa sababu saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Kile Yesu anachofafanua hapa ni tofauti sana na kule kubaki hai kwa nafsi isiyoweza kufa baada ya kufa kwa mwili, kisha kwenda moja kwa moja mbinguni. Anafafanua kuhusu ‘kutoka’ kaburini katika wakati ujao kwa watu ambao wamekuwa humo, wengi kwa karne nyingi au hata kwa maelfu ya miaka. Ni nafsi zilizokufa zinazofufuliwa. Je, ni jambo lisilowezekana? Si kwa Mungu “afanyaye wafu kuwa hai na huita mambo yasiyokuwako kama kwamba yamekuwako.” (Waroma 4:17) Wenye kutilia shaka huenda wakadhihaki wazo la watu kurudi kutoka kwa wafu, lakini jambo hilo lapatana kikamili na jambo la hakika kwamba “Mungu ni upendo” na kwamba yeye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—1 Yohana 4:16; Waebrania 11:6.
17. Mungu atatimiza nini kupitia ufufuo?
17 Hata hivyo, Mungu angeweza kuthawabishaje wale waliothibitika kuwa ‘waaminifu hata kufikia kifo’ iwapo angewafufua? (Ufunuo 2:10) Ufufuo pia humwezesha Mungu kutimiza yale mtume Yohana aliyoandika: “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alifanywa dhahiri, yaani, ili avunje-vunje kazi za Ibilisi.” (1 Yohana 3:8) Huko nyuma katika shamba la Edeni, Shetani alipata kuwa muuaji kimakusudi wa jamii yote ya kibinadamu alipowaongoza wazazi wetu wa kwanza kwenye dhambi na kifo. (Mwanzo 3:1-6; Yohana 8:44) Yesu alianza kuvunja-vunja kazi za Shetani alipotoa uhai wake mkamilifu kuwa fidia inayolingana, kufanya hivyo kukiwafungulia wanadamu njia watoke katika utumwa wa dhambi waliorithi, ambao ulitokana na kutotii kimakusudi kwa Adamu. (Waroma 5:18) Ufufuo wa wale ambao hufa kwa sababu ya dhambi ya Adamu utakuwa kuvunjwa-vunjwa zaidi kwa kazi za Ibilisi.
Mwili na Nafsi
18. Wanafalsafa fulani Wagiriki waliitikiaje taarifa ya Paulo ya kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa, na kwa nini?
18 Alipokuwa Athene, mtume Paulo alihubiri habari njema kwa umati uliotia ndani wanafalsafa Wagiriki. Walisikiliza mazungumzo hayo kuhusu Mungu mmoja wa kweli na mwito wake wa toba. Lakini ni nini kilichotukia baadaye? Paulo alimalizia hotuba yake kwa kusema hivi: “[Mungu] ameweka siku ambayo katika hiyo akusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kwa njia ya mwanamume ambaye ameweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” Maneno hayo yalitokeza mvurugo. “Waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine wao wakaanza kudhihaki.” (Matendo 17:22-32) Mwanatheolojia Oscar Cullmann asema hivi: “Kwa Wagiriki walioamini kwamba nafsi haiwezi kufa, huenda lilikuwa jambo gumu zaidi kwao kukubali yale Wakristo waliyohubiri kuhusu ufufuo kuliko ilivyokuwa kwa wengine. . . . Fundisho la Socrates na Plato, waliokuwa wanafalsafa wakuu, haliwezi kwa vyovyote kupatanishwa [kukubaliana] na fundisho la Agano Jipya.”
19. Wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo walijaribu kupatanishaje fundisho la ufufuo na fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa?
19 Ijapokuwa hivyo, kufuatia uasi mkubwa baada ya kifo cha mitume, wanatheolojia walijitahidi kuunganisha fundisho la Wakristo juu ya ufufuo, na imani ya Plato katika nafsi isiyoweza kufa. Baada ya muda, baadhi yao walikubaliana juu ya utatuzi huu mpya: Wakati wa kufa, nafsi hutenganishwa (“huwekwa huru,” kama vile wengine husema) na mwili. Kisha kulingana na kichapo Outlines of the Doctrine of the Resurrection, cha R. J. Cooke, Siku ya Hukumu “kila mwili utaunganishwa tena na nafsi yake wenyewe, na kila nafsi na mwili wake yenyewe.” Kuunganishwa wakati ujao kwa mwili na nafsi yake isiyoweza kufa, kwasemekana kuwa ndio ufufuo.
20, 21. Ni nani ambao wamefundisha kweli kuhusu ufufuo kwa upatano, na hilo limewanufaishaje?
20 Nadharia hiyo bado ni fundisho rasmi la makanisa mashuhuri. Ingawa dhana hiyo yaweza kuonekana kuwa jambo la akili kwa mwanatheolojia, waenda-kanisani wengi hawaifahamu. Wao huamini tu kwamba wataenda mbinguni moja kwa moja watakapokufa. Kwa sababu hiyo, katika makala ya Mei 5, 1995, ya Commonweal, mwandishi John Garvey alidai kwamba: “Imani ya Wakristo walio wengi [kuhusu uhai baada ya kifo] yaonekana yakaribiana zaidi na ile imani ya Uplato mpya kuliko inavyokaribiana na imani yoyote ambayo kwa kweli ni ya Kikristo, na haina msingi wowote wa Biblia.” Kwa kweli, kwa kubadilisha Biblia na imani ya Plato, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walifuta tumaini la Biblia la ufufuo kwa makundi yao.
21 Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova hukataa falsafa ya kipagani na kushikamana na fundisho la Biblia la ufufuo. Wao huliona fundisho hilo kuwa lenye kuelimisha, kuridhisha, na kufariji. Katika makala zinazofuata, tutaona hasa vile mafundisho ya Biblia juu ya ufufuo yalivyo na msingi mzuri, na vile yalivyo mambo ya akili kwa walio na tumaini la kidunia na kwa walio na tazamio la ufufuo wa uhai wa kimbingu. Yakiwa matayarisho kwa ajili ya kuchunguza makala hizo, twapendekeza kwamba usome kwa makini sura ya 15 ya barua ya kwanza kwa Wakorintho.
-
-
“Wafu Watafufuliwa”Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
“Wafu Watafufuliwa”
“Kwa maana hiyo tarumbeta itavuma, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioharibika, nasi tutabadilishwa.”—1 WAKORINTHO 15:52.
1, 2. (a) Ni ahadi gani yenye kufariji iliyotolewa kupitia nabii Hosea? (b) Twajuaje kwamba Mungu yuko tayari kuwafufua wafu?
JE, UMEWAHI kumpoteza mpendwa katika kifo? Basi unajua maumivu ambayo kifo chaweza kuleta. Hata hivyo, Wakristo hupokea faraja katika ahadi ambayo Mungu alitoa kupitia nabii Hosea: “Nitawakomboa na nguvu za kaburi; nitawaokoa na mauti; ewe mauti, ya wapi mapigo yako? ewe kaburi, kuwapi kuharibu kwako?”—Hosea 13:14.
2 Wazo la wafu kufufuliwa laonekana kuwa la kipuuzi na wenye kutilia shaka. Lakini bila shaka Mungu Mweza Yote ana uwezo wa kufanya muujiza kama huo! Suala halisi ni kama Yehova yuko tayari kuwafufua wafu. Yobu mwadilifu, aliuliza hivi: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?” Ndipo akatoa jibu hili lenye kutia moyo: “Wewe ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya [“ungetamani sana,” NW] kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Maneno ‘kutamani sana’ yamaanisha kuwa na hamu nyingi sana au tamaa nyingi mno. (Linganisha Zaburi 84:2, Biblia Habari Njema.) Naam, Yehova hutazamia ufufuo kwa hamu—yeye hutamani sana kuwaona tena watu waaminifu waliokufa, walio hai katika kumbukumbu lake.—Mathayo 22:31, 32.
Yesu Atoa Nuru Juu ya Ufufuo
3, 4. (a) Yesu alitoa nuru gani juu ya tumaini la ufufuo? (b) Kwa nini Yesu alifufuliwa akiwa roho wala si katika mwili?
3 Wanaume wa kale wa imani kama Yobu, walikuwa na uelewevu wa kiasi tu juu ya ufufuo. Yesu Kristo ndiye aliyetoa nuru kikamili juu ya tumaini hilo la ajabu. Alionyesha fungu muhimu ambalo yeye mwenyewe hutimiza aliposema hivi: “Yeye ambaye hudhihirisha imani katika Mwana ana uhai udumuo milele.” (Yohana 3:36) Uhai huo utafurahiwa wapi? Kwa walio wengi ambao hudhihirisha imani, uhai huo utakuwa duniani. (Zaburi 37:11) Hata hivyo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Msiwe na hofu, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa nyinyi ufalme.” (Luka 12:32) Ufalme wa Mungu ni wa kimbingu. Kwa sababu hiyo, ahadi hiyo humaanisha kwamba “kundi dogo” lingepaswa kuwa mbinguni pamoja na Yesu likiwa viumbe wa roho. (Yohana 14:2, 3; 1 Petro 1:3, 4) Ni tazamio lenye utukufu kama nini! Yesu alizidi kumfunulia mtume Yohana kwamba, idadi ya ‘kundi hilo dogo’ ingekuwa watu 144,000 tu.—Ufunuo 14:1.
4 Ingawa hivyo, hao 144,000 wangeingiaje katika utukufu wa kimbingu? Yesu “ametoa nuru juu ya uhai na kutoharibika kupitia habari njema.” Kwa kutumia damu yake, alianzisha “njia mpya na yenye uhai” ya kuingia mbinguni. (2 Timotheo 1:10; Waebrania 10:19, 20) Kwanza, alikufa, kama vile Biblia ilivyotabiri angefanya. (Isaya 53:12) Kisha, kama vile mtume Petro alivyotangaza, “Yesu huyu Mungu alimfufua.” (Matendo 2:32) Ingawa hivyo, Yesu hakufufuliwa akiwa binadamu. Alikuwa amesema hivi: “Mkate ambao nitatoa ni mwili wangu kwa ajili ya uhai wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Kuuchukua mwili wake tena kungebatilisha dhabihu hiyo. Hivyo Yesu ‘aliuawa katika mwili wenye nyama, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.’ (1 Petro 3:18) Hivyo Yesu “[ali]pata ukombozi udumuo milele kwa ajili yetu,” yaani “kundi dogo.” (Waebrania 9:12) Alimtolea Mungu thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ukiwa fidia kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, na wale 144,000 ndio waliokuwa wa kwanza kunufaika na fidia hiyo.
5. Wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walitolewa tumaini gani?
5 Si Yesu pekee ambaye angefufuliwa kwenye uhai wa kimbingu. Paulo aliwaambia Wakristo wenzake katika Roma kwamba walikuwa wametiwa mafuta kwa roho wawe wana wa Mungu na warithi-washirika pamoja na Kristo ikiwa wangethibitisha kutiwa mafuta kwao kwa kuvumilia mpaka mwisho. (Waroma 8:16, 17) Paulo pia alieleza hivi: “Ikiwa tumekuwa wenye kuungana pamoja naye katika ufanani wa kifo chake, hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika ufanani wa ufufuo wake.”—Waroma 6:5.
Kutetea Tumaini la Ufufuo
6. Kwa nini imani katika ufufuo ilishambuliwa katika Korintho, na mtume Paulo aliitikiaje?
6 Ufufuo ni sehemu ya “fundisho la msingi” la Ukristo. (Waebrania 6:1, 2) Hata hivyo, fundisho hilo lilikuwa likishambuliwa huko Korintho. Watu fulani katika kutaniko, waliokuwa kwa wazi wameathiriwa na falsafa za Kigiriki, walikuwa wakisema hivi: “Hakuna ufufuo wa wafu.” (1 Wakorintho 15:12) Wakati ripoti za usemi huo zilipomfikia mtume Paulo, alitetea tumaini la ufufuo, hasa tumaini la Wakristo watiwa-mafuta. Acheni tuchunguze maneno ya Paulo kama yalivyorekodiwa katika 1 Wakorintho sura ya 15. Litakuwa jambo lenye kusaidia ukiwa umesoma hiyo sura yote, kama ambavyo ilipendekezwa katika makala iliyotangulia.
7. (a) Ni suala gani kuu ambalo Paulo alikazia? (b) Ni nani waliomwona Yesu aliyekuwa amefufuliwa?
7 Katika mistari ya kwanza miwili ya 1 Wakorintho sura ya 15, Paulo ataja kichwa cha mazungumzo yake: “Nawajulisha nyinyi, akina ndugu, habari njema niliyowatangazia, mliyoipokea pia, ambayo katika hiyo mwasimama pia, ambayo kupitia hiyo nyinyi pia mnaokolewa, . . . isipokuwa, kwa kweli, mwe mlipata kuwa waamini bila kusudi lolote.” Wakorintho walikuwa wameipokea kweli bure, ikiwa walishindwa kusimama imara katika habari njema. Paulo aliendelea kusema hivi: “Niliwapa nyinyi, miongoni mwa mambo ya kwanza, lile nililolipokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba amefufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alionekana kwa Kefa, kisha kwa wale kumi na wawili. Baada ya hilo alionekana kwa zaidi ya ndugu mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wabaki hadi wakati wa sasa, lakini baadhi yao wamelala usingizi katika kifo. Baada ya hilo alionekana kwa Yakobo, kisha kwa mitume wote; lakini mwisho wa wote alionekana pia kwangu kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.”—1 Wakorintho 15:3-8.
8, 9. (a) Itikadi katika ufufuo ni ya maana kadiri gani? (b) Yaelekea ni wakati gani Yesu alionekana kwa “zaidi ya ndugu mia tano”?
8 Kwa waliokuwa wamepokea habari njema, imani katika ufufuo wa Yesu halikuwa jambo la kuchagua. Kulikuwa na mashahidi wengi waliojionea kwa macho waliothibitisha kwamba “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu” na kwamba alikuwa amefufuliwa. Mmoja wao alikuwa Kefa, au Petro, jina linalojulikana zaidi. Baada ya Petro kumkataa Yesu usiku wa kusalitiwa na kukamatwa kwa Yesu, lazima awe alifarijiwa sana kumwona Yesu. Pia Yesu aliyekuwa amefufuliwa aliwatembelea “wale kumi na wawili,” yaani wale mitume wakiwa kikundi—jambo lililoonwa ambalo bila shaka liliwasaidia kushinda hofu yao na kuwa mashahidi wajasiri wa ufufuo wa Yesu.—Yohana 20:19-23; Matendo 2:32.
9 Kristo pia alionekana kwa kikundi kikubwa zaidi, “ndugu zaidi ya mia tano.” Kwa kuwa ni katika Galilaya tu alikokuwa na idadi kubwa hivyo ya wafuasi, huenda huo ukawa ni ule wakati ambao umeelezwa kwenye Mathayo 28:16-20, Yesu alipotoa amri ya kufanya wanafunzi. Hao watu wangeweza kutoa ushuhuda wenye nguvu kama nini! Baadhi yao walikuwa bado hai mwaka wa 55 W.K. wakati Paulo alipotunga barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Ingawa hivyo, ona kwamba wale waliokuwa wamekufa walitajwa kuwa “wamelala usingizi katika kifo.” Walikuwa bado hawajafufuliwa ili kupokea thawabu yao ya kimbingu.
10. (a) Mkutano wa mwisho wa Yesu pamoja na wanafunzi wake ulikuwa na matokeo gani? (b) Yesu alionekanaje kwa Paulo “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati”?
10 Shahidi mwingine mwenye kutokeza wa ufufuo wa Yesu alikuwa Yakobo, mwana wa Yosefu na Maria, mama yake Yesu. Kabla ya huo ufufuo ni wazi kwamba Yakobo hakuwa amekuwa mwamini. (Yohana 7:5) Lakini baada ya Yesu kuonekana kwake, Yakobo akawa mwamini na labda akatimiza fungu fulani katika kugeuza imani ya ndugu zake. (Matendo 1:13, 14) Katika mkutano wake wa mwisho pamoja na wanafunzi wake, wakati alipopaa kwenda mbinguni, Yesu aliwapa utume wa ‘kuwa mashahidi wake hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.’ (Matendo 1:6-11) Baadaye, alionekana kwa Sauli wa Tarso, aliyekuwa mnyanyasaji wa Wakristo. (Matendo 22:6-8) Yesu alionekana kwa Sauli “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.” Ilikuwa kama kwamba Sauli alikuwa tayari amefufuliwa kwenye uhai wa roho na angeweza kumwona Bwana aliyetukuzwa, karne nyingi kabla ya ufufuo huo kutokea. Jambo hilo lilifanya Sauli aache mara moja upinzani wa hata kuua kimakusudi washiriki wa kutaniko la Kikristo na kufanya badiliko lenye kutokeza. (Matendo 9:3-9, 17-19) Sauli alipata kuwa mtume Paulo, mmojawapo wa watetezi mashuhuri wa imani ya Kikristo.—1 Wakorintho 15:9, 10.
Imani Katika Ufufuo Ni Muhimu
11. Paulo alifichuaje kosa la kusema kwamba “hakuna ufufuo”?
11 Kwa hiyo kufufuliwa kwa Yesu kulikuwa jambo la hakika lililothibitishwa vizuri. “Sasa ikiwa Kristo anahubiriwa kwamba amefufuliwa kutoka kwa wafu,” Paulo atoa hoja, “ni jinsi gani wengine miongoni mwenu husema hakuna ufufuo wa wafu?” (1 Wakorintho 15:12) Watu hao hawakuwa na shaka za kibinafsi au maswali kuhusu ufufuo tu, bali pia walisema waziwazi kwamba hawauamini. Hivyo Paulo afichua kusababu kwao kwenye kosa. Alisema kwamba ikiwa Kristo hakufufuliwa, ule ujumbe wa Kikristo ulikuwa uwongo, na walioshuhudia kufufuliwa kwa Kristo walikuwa “mashahidi wasio wa kweli wa Mungu.” Ikiwa Kristo hakuwa amefufuliwa, Mungu hakuwa amelipwa fidia yoyote; Wakristo walikuwa ‘bado wamo katika dhambi zao.’ (1 Wakorintho 15:13-19; Waroma 3:23, 24; Waebrania 9:11-14) Na Wakristo waliokuwa “wamelala usingizi katika kifo” katika visa vingine wakiwa wafia-imani, walikuwa wameangamia bila tumaini la kweli. Wakristo wangekuwa katika hali yenye kusikitisha kama nini ikiwa uhai huu ndio tu wangeweza kutarajia! Kuteseka kwao kwote hakungekuwa na maana.
12. (a) Ni nini linalodokezwa na kumwita Kristo “matunda ya kwanza katika wale wamelala usingizi katika kifo?” (b) Kristo alifanyaje ufufuo uwezekane?
12 Hata hivyo, hali haikuwa hivyo. Paulo aendelea kusema hivi: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu.” Zaidi ya hayo, yeye ni “matunda ya kwanza kati ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” (1 Wakorintho 15:20) Yehova aliwabariki Waisraeli kwa mavuno makubwa, wakati ambapo walimpa kwa utii matunda ya kwanza ya mazao yao. (Kutoka 22:29, 30; 23:19; Mithali 3:9, 10) Kwa kumwita Kristo “matunda ya kwanza,” Paulo adokeza kwamba mavuno zaidi ya watu wangefufuliwa kutoka kwa wafu wakaishi mbinguni. “Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu,” Paulo asema, “ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, ndivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:21, 22) Yesu alifanya ufufuo uwezekane kwa kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ukiwa fidia, ikiwafungulia wanadamu njia watoke katika utumwa wa dhambi na kifo.—Wagalatia 1:4; 1 Petro 1:18, 19.a
13. (a) Ufufuo wa kimbingu unatukia lini? (b) Inakuwaje kwamba watiwa-mafuta fulani ‘hawalali usingizi katika kifo’?
13 Paulo aendelea kusema hivi: “Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.” (1 Wakorintho 15:23) Kristo alifufuliwa mwaka wa 33 W.K. Hata hivyo, wafuasi wake watiwa-mafuta—“wale walio wa Kristo”—wangelazimika kungoja hadi punde baada ya Yesu kuanza kuwapo kwake kwa kifalme, ambako unabii wa Biblia waonyesha kulitukia mwaka wa 1914. (1 Wathesalonike 4:14-16; Ufunuo 11:18) Namna gani wale ambao wangekuwa hai wakati wa kuwapo kwake? Paulo asema hivi: “Tazama! Nawaambia nyinyi siri takatifu: Hatutalala usingizi katika kifo sisi sote, bali sisi sote tutabadilishwa, kwa dakika, katika kupepeseka kwa jicho, wakati wa tarumbeta ya mwisho. Kwa maana hiyo tarumbeta itavuma, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioharibika, nasi tutabadilishwa.” (1 Wakorintho 15:51, 52) Kwa wazi, si watiwa-mafuta wote ambao hulala kaburini wakingojea ufufuo. Wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo hugeuzwa umbo mara moja.—Ufunuo 14:13.
14. Watiwa-mafuta ‘hubatizwaje kwa kusudi la kuwa wafu’?
14 “Kama sivyo,” Paulo auliza, “watafanya nini wao wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu? Ikiwa wafu hawapaswi kufufuliwa hata kidogo, kwa nini pia wanabatizwa kwa kusudi la kuwa hivyo? Kwa nini sisi pia tumo hatarini kila saa?” (1 Wakorintho 15:29, 30) Paulo hakumaanisha kwamba watu waliokuwa hai walibatizwa kwa niaba ya wafu, kama vile tafsiri nyingine za Biblia hufanya jambo hilo lionekane. Hata hivyo, ubatizo wahusiana na uanafunzi wa Kikristo, na nafsi zilizokufa haziwezi kuwa wanafunzi. (Yohana 4:1) Badala yake, Paulo alikuwa akizungumza juu ya Wakristo waliokuwa hai, ambao wengi wao, kama Paulo mwenyewe, walikuwa “hatarini kila saa.” Wakristo watiwa-mafuta ‘walibatizwa katika kifo cha Kristo.’ (Waroma 6:3) Tangu walipotiwa mafuta, walikuwa ‘wakibatizwa’ kitamathali, na kuingia katika mwendo ambao ungewaongoza kwenye kifo kama kile cha Kristo. (Marko 10:35-40) Wangekufa wakiwa na tumaini la ufufuo mtukufu wa kimbingu.—1 Wakorintho 6:14; Wafilipi 3:10, 11.
15. Huenda Paulo alipatwa na hatari gani, na imani katika ufufuo ilitimizaje fungu katika kuzivumilia?
15 Paulo sasa aeleza kwamba yeye mwenyewe alikuwa amekabili hatari kiasi cha kuweza kusema hivi: “Kila siku nakabili kifo.” Ili wengine wasije wakamshtaki kuwa mwenye kutia chumvi, Paulo aongeza kusema hivi: “Hili nathibitisha kwa mchachawo nilio nao juu yenu, akina ndugu, katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Biblia Habari Njema hutafsiri mstari huu hivi: “Ndugu, mimi ninakabili kifo kila siku! Fahari niliyo nayo juu yenu katika kuungana na Kristo Yesu Bwana wetu inanifanya nitangaze jambo hili.” Ukiwa mfano wa hatari alizokabili, katika mstari wa 32, Paulo asema juu ya ‘kupigana na mahayawani-mwitu katika Efeso.’ Mara nyingi Waroma walifisha wahalifu kwa kuwatupa kwa mahayawani-mwitu katika viwanja vya michezo. Ikiwa Paulo alivumilia pigano na mahayawani-mwitu halisi, angeweza kuwa aliokoka tu kwa msaada wa Yehova. Bila tumaini la ufufuo, kuchagua njia ya maisha iliyomweka katika hatari kama hiyo kwa kweli kungalikuwa kujihatarisha kipumbavu. Bila tumaini la uhai wa wakati ujao, kuvumilia shida na kujidhabihu kulikoambatana na kumtumikia Mungu hakungekuwa na maana. “Ikiwa wafu hawapaswi kufufuliwa,” Paulo asema, “‘acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa.’”—1 Wakorintho 15:31, 32; ona 2 Wakorintho 1:8, 9; 11:23-27.
16. (a) Huenda usemi “acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa” ukawa umetokana na nini? (b) Ni zipi zilizokuwa hatari za kukubali maoni hayo?
16 Huenda ikawa Paulo alinukuu andiko la Isaya 22:13, ambalo lafafanua mtazamo wa nadharia-ajali wa wakazi wa Yerusalemu wasiotii. Au huenda akawa alikuwa akifikiria yale Waepikurea waliyoamini, waliodharau tumaini lolote la uhai baada ya kifo na kuamini raha ya kimwili ndiyo iliyokuwa jambo lenye faida kubwa maishani. Kwa vyovyote vile, “tule na tunywe” ilikuwa falsafa ya kutomwogopa Mungu. Kwa sababu hiyo Paulo aonya hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Kushirikiana na wale ambao walikataa ufufuo kungeweza kuwa jambo lenye sumu. Kushirikiana kama huko kulitimiza fungu fulani katika matatizo ambayo Paulo alikuwa ashughulikie katika kutaniko la Korintho, kama vile ukosefu wa adili katika ngono, migawanyiko, mashtaka ya kisheria, na kutostahi Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Wakorintho 1:11; 5:1; 6:1; 11:20-22.
17. (a) Paulo aliwatolea Wakorintho onyo gani lenye upole? (b) Ni maswali gani yanayobaki kujibiwa?
17 Hivyo Paulo awapa Wakorintho himizo hili lenye upole ambalo lafaa: “Amkeni mwe na utimamu wa akili katika njia ya uadilifu na msizoee dhambi, kwa maana wengine hawana ujuzi juu ya Mungu. Ninasema ili kuwasukuma mwone aibu.” (1 Wakorintho 15:34) Maoni yasiyofaa juu ya ufufuo yaliongoza wengine kuingia katika kuzubaa kiroho, kama kwamba walikuwa wamelewa. Walihitaji kuamka, kuwa timamu kiakili. Hivyohivyo, Wakristo watiwa-mafuta leo wanahitaji kuwa macho kiroho, bila kuathiriwa na maoni yenye kutilia shaka ya ulimwengu. Lazima washikamane kabisa na tumaini lao la ufufuo wa kimbingu. Lakini maswali bado yalibaki—kwa Wakorintho wakati huo na kwetu wakati wa sasa. Kwa kielelezo, wale 144,000 hufufuliwa kwenda mbinguni katika umbo gani? Na namna gani mamilioni ya wengine waliomo kaburini na ambao hawana tumaini la kimbingu? Ufufuo utamaanisha nini kwa watu kama hao? Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza mazungumzo ya Paulo yanayobaki juu ya ufufuo.
-
-
“Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
“Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”
“Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” —1 WAKORINTHO 15:26.
1, 2. (a) Mtume Paulo aliwatolea wafu tumaini gani? (b) Paulo alizungumzia swali gani kuhusu ufufuo?
“NINAAMINI katika . . . ufufuo wa mwili, na uhai udumuo milele.” Hivyo ndivyo isemavyo ile taarifa ya itikadi iitwayo Imani ya Mitume. Wakatoliki na vilevile Waprotestanti huikariri kwa utiifu, wasing’amue kwamba mambo wanayoamini yafanana zaidi na falsafa za Kigiriki kuliko chochote kile ambacho mitume waliwahi kuamini. Hata hivyo, mtume Paulo alikataa falsafa ya Kigiriki na hakuamini kwamba nafsi haiwezi kufa. Hata hivyo, aliamini kwa dhati kuwako kwa uhai wakati ujao na kupuliziwa kuandika hivi: “Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” (1 Wakorintho 15:26) Hilo lamaanisha nini hasa kwa wanadamu wanaokufa?
2 Kwa kujibu, acheni turudi kwenye mazungumzo ya Paulo juu ya ufufuo yaliyorekodiwa katika 1 Wakorintho sura 15. Utakumbuka kwamba katika mistari ya kufungua, Paulo alithibitisha ufufuo kuwa sehemu muhimu ya fundisho la Kikristo. Sasa anazungumzia swali mahususi: “Hata hivyo, mtu fulani atasema: ‘Wafu watafufuliwaje? Ndiyo, wanakuja wakiwa na mwili wa namna gani?’”—1 Wakorintho 15:35.
Mwili wa Aina Gani?
3. Kwa nini watu fulani waliukataa ufufuo?
3 Kwa kuzusha swali hilo, huenda Paulo akawa alinuia kukinza uvutano wa falsafa ya Plato. Plato alifundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo hubaki hai baada ya mwili kufa. Wale waliokua wakiwa na wazo kama hilo, bila shaka fundisho la Kikristo la ufufuo halikuonekana kuwa jambo la lazima. Ikiwa nafsi iliendelea kuwa hai baada ya kifo, ufufuo una maana gani? Na zaidi, yaelekea ufufuo ulionekana kuwa jambo lisilo la akili. Mwili unapooza na kuwa mavumbi, kunaweza kuwaje na ufufuo? Mwelezaji wa Biblia, Heinrich Meyer, asema kwamba ugomvi wa Wakorintho fulani labda ulitegemea “msingi wa falsafa ya kwamba, lilikuwa jambo lisilowezekana kurudisha vitu vinavyoufanyiza mwili.”
4, 5. (a) Kwa nini vipingamizi vya wasio na imani vilikuwa mambo yasiyo ya akili? (b) Eleza kielezi cha Paulo cha “punje tupu.” (c) Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili ya aina gani?
4 Paulo afichua upumbavu wa kusababu kwao: “Wewe mtu asiye na akili! Kile upandacho hakifanywi kuwa hai isipokuwa kwanza kife; na kwa habari ya kile upandacho, wapanda, si mwili utakaositawi, bali punje tupu, huenda ikawa, ya ngano au yoyote moja kati ya zile nyingine; lakini Mungu huipa mwili kama vile imempendeza, na kwa kila moja ya hizo mbegu mwili wayo yenyewe.” (1 Wakorintho 15:36-38) Mungu hangefufua miili ambayo watu walikuwa nayo walipokuwa duniani. Badala yake, kungekuwa na mgeuzo umbo.
5 Paulo alinganisha ufufuo na kumea kwa mbegu. Mbegu ndogo ya ngano huwa haifanani kwa vyovyote na mmea utakaoota kutoka kwake. Kichapo The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Mbegu ianzapo kuota, hufyoza maji mengi sana. Hayo maji husababisha mabadiliko mengi ya kemikali ndani ya hiyo mbegu. Pia husababisha sehemu ya ndani ya mbegu kuvimba na kupasua ngozi ya nje ya mbegu.” Kwa kweli hiyo mbegu hufa ikiwa mbegu na kuwa mmea unaoibuka. “Mungu huipa mwili” kwa kuwa alizipanga sheria za kisayansi zinazoongoza kusitawi kwake, na kila mbegu hupokea mwili kulingana na aina yake. (Mwanzo 1:11) Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta kwanza hufa wakiwa binadamu. Kisha, kwenye wakati wa Mungu uliowekwa, yeye huwafufua katika miili mipya kabisa. Kama vile Paulo alivyowaambia Wafilipi, “Yesu Kristo . . . ataufanya upya mwili wetu uliotwezwa ili upatanishwe na umbo la mwili wake wenye utukufu.” (Wafilipi 3:20, 21; 2 Wakorintho 5:1, 2) Wao hufufuliwa katika miili ya roho na huishi katika makao ya roho.—1 Yohana 3:2.
6. Kwa nini ni jambo la akili kuamini kwamba Mungu aweza kuwapa wenye kufufuliwa miili ifaayo ya roho?
6 Je, jambo hilo ni gumu mno kuamini? La. Paulo anasababu kwamba, wanyama wana miili mingi tofauti. Kwa kuongezea, yeye atofautisha malaika wa kimbingu na wanadamu wenye nyama na damu, akisema: “Kuna miili ya kimbingu, na miili ya kidunia.” Pia kuna tofauti kubwa kati ya uumbaji wa vitu visivyo na uhai. “Nyota hutofautiana na nyota kwa utukufu,” Paulo akasema, muda mrefu kabla sayansi haijagundua nyota kubwa kwa ndogo na zenye rangi tofauti-tofauti. Kwa kufikiria hilo, je, si jambo la akili kwamba Mungu aweza kuandaa miili ya roho ifaayo kwa ajili ya watiwa-mafuta wenye kufufuliwa?—1 Wakorintho 15:39-41.
7. Ni nini maana ya kutoharibika? na ya kutoweza kufa?
7 Kisha Paulo asema hivi: “Ndivyo pia ulivyo ufufuo wa wafu. Hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika.” (1 Wakorintho 15:42) Mwili wa kibinadamu, hata unapokuwa mkamilifu, waweza kuharibika. Waweza kuuawa. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba Yesu aliyefufuliwa “[ali]kusudiwa asirudi tena kwenye uharibifu.” (Matendo 13:34) Hangefufuliwa katika mwili wa kibinadamu wenye kuharibika, hata ingawa ni mkamilifu. Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili isiyoharibika—isiyoweza kufa au kuoza. Paulo aendelea kusema hivi: “Hupandwa katika fedheha, hufufuliwa katika utukufu. Hupandwa katika udhaifu, hufufuliwa katika nguvu. Hupandwa ukiwa mwili wa nyama, hufufuliwa ukiwa mwili wa kiroho.” (1 Wakorintho 15:43, 44) Na zaidi, Paulo asema hivi: “Huu uwezao kufa lazima uvae hali ya kutokufa.” Kutokufa humaanisha uhai wa milele usioweza kuhabiriwa. (1 Wakorintho 15:53; Waebrania 7:16) Katika njia hiyo, wenye kufufuliwa huchukua “mfano wa yule wa kimbingu,” yaani Yesu, aliyewezesha kufufuliwa kwao.—1 Wakorintho 15:45-49.
8. (a) Twajuaje kwamba wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa hai duniani? (b) Ni unabii gani mbalimbali unaotimizwa ufufuo utokeapo?
8 Licha ya mgeuzo umbo huo, wenye kufufuliwa bado watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa. Watafufuliwa na kumbukumbu zilezile na sifa zilezile bora za Kikristo. (Malaki 3:3; Ufunuo 21:10, 18) Katika hilo wanafanana na Yesu Kristo. Umbo lake la roho lilibadilika kuwa la kibinadamu. Kisha akafa na kufufuliwa akiwa roho. Hata hivyo, “Yesu Kristo ni yuleyule jana na leo, na milele.” (Waebrania 13:8) Watiwa-mafuta wana pendeleo lililoje! Paulo asema hivi: “Lakini wakati huu ulio wenye kuharibika uvaapo kutoharibika na huu uwezao kufa uvaapo hali ya kutokufa, ndipo usemi utakapotukia ambao umeandikwa: ‘Kifo kimemezwa milele.’ ‘Kifo, ushindi wako uko wapi? Kifo, kichomeo chako kiko wapi?’”—1 Wakorintho 15:54, 55; Isaya 25:8; Hosea 13:14.
Ufufuo wa Kidunia?
9, 10. (a) Katika muktadha wa 1 Wakorintho 15:24, “mwisho” ni nini, na ni matukio gani yatokeayo kuhusiana na huo? (b) Ni lazima jambo gani litokee ili kifo kifanywe kuwa si kitu?
9 Je, kuna wakati ujao wowote kwa mamilioni yasiyo na tumaini la uhai wa roho usioweza kufa? Kwa kweli kunao! Baada ya kueleza kwamba ufufuo wa kimbingu hutukia wakati wa kuwapo kwa Kristo, Paulo atoa muhtasari wa matukio yanayofuata kuwapo kwa Kristo, akisema: “Halafu, mwisho, wakati amkabidhipo ufalme Mungu wake aliye Baba, wakati akiwa amefanya serikali yote na mamlaka yote na nguvu kuwa si kitu.”—1 Wakorintho 15:23, 24.
10 “Mwisho” ni mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, wakati Yesu amkabidhipo Ufalme Mungu wake aliye Baba, kwa unyenyekevu na kwa uaminifu-mshikamanifu. (Ufunuo 20:4) Kusudi la Mungu “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo” litakuwa limetimizwa. (Waefeso 1:9, 10) Ingawa hivyo, kwanza Kristo atakuwa ameharibu “serikali yote na mamlaka yote” yenye kupinga mapenzi ya Enzi Kuu ya Mungu. Hilo lahusisha mengi zaidi ya uharibifu utakaotekelezwa kwenye Har–Magedoni. (Ufunuo 16:16; 19:11-21) Paulo asema hivi: “Ni lazima [Kristo] atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka maadui wote chini ya miguu yake. Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” (1 Wakorintho 15:25, 26) Naam, alama zote za dhambi na kifo cha Kiadamu zitakuwa zimeondolewa. Basi, kwa sababu ya uhitaji, Mungu atakuwa ameyaacha “makaburi ya ukumbusho” yakiwa tupu kwa kuwafufua wafu.—Yohana 5:28.
11. (a) Twajuaje kwamba Mungu aweza kuumba tena nafsi zilizokufa? (b) Watakaofufuliwa duniani watapewa miili ya aina gani?
11 Hilo lamaanisha kuumba tena nafsi za kibinadamu. Je, ni jambo lisilowezekana? La, kwa kuwa andiko la Zaburi 104:29, 30 latuhakikishia kwamba Mungu aweza kufanya hivyo: “Waiondoa pumzi yao, wanakufa, na kuyarudia mavumbi yao, waipeleka roho yako, wanaumbwa.” Ingawa wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa, hawatahitaji kuwa na miili ileile. Sawa na wale watakaofufuliwa kwenda mbinguni, Mungu atawapa mwili kama vile impendezavyo. Bila shaka miili yao mipya itakuwa yenye afya na kwa kufaa itakuwa sawa na miili yao ya hapo awali, hivi kwamba wapendwa wao wataweza kuwatambua.
12. Ufufuo wa kidunia unatokea lini?
12 Ufufuo wa kidunia utatokea lini? Martha alisema hivi kumhusu ndugu yake Lazaro: “Najua atafufuliwa katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:24) Alijuaje hilo? Ufufuo ulikuwa jambo lenye kubishaniwa katika siku yake, kwa kuwa Mafarisayo waliamini katika ufufuo ilhali Masadukayo hawakuamini katika huo. (Matendo 23:8) Hata hivyo, ni lazima Martha awe aliwajua mashahidi wa kabla ya Ukristo waliotumaini katika ufufuo. (Waebrania 11:35) Pia, angeweza kutambua kutoka katika kitabu cha Danieli 12:13 kwamba ufufuo utatokea siku ya mwisho. Huenda hata akawa alijifunza jambo hilo kutoka kwa Yesu mwenyewe. (Yohana 6:39) “Siku [hiyo] ya mwisho” yasadifiana na Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. (Ufunuo 20:6) Ebu wazia msisimko katika “siku” hiyo wakati ambapo tukio hilo tukufu linaanza!—Linganisha Luka 24:41.
Ni Nani Wanaofufuliwa?
13. Ni ono gani la ufufuo linalorekodiwa kwenye Ufunuo 20:12-14?
13 Ono la Yohana juu ya ufufuo wa kidunia limerekodiwa kwenye Ufunuo 20:12-14 hivi: “Nikaona wafu, wakubwa na wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha ufalme, na hati-kunjo zikafunguliwa. Lakini hati-kunjo nyingine ikafunguliwa; hiyo ndiyo hati-kunjo ya uhai. Na hao wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika hizo hati-kunjo kulingana na vitendo vyao. Nayo bahari ikawatoa hao wafu waliokuwa ndani yayo, na kifo na Hadesi vikawatoa wafu ndani yavyo, nao walihukumiwa mmoja-mmoja kulingana na vitendo vyao. Na kifo na Hadesi vikavurumishwa ndani ya ziwa la moto. Hili humaanisha kifo cha pili, ziwa la moto.”
14. Ni nani watakaokuwa miongoni mwa wale wenye kufufuliwa?
14 Ufufuo utatia ndani “wakubwa na wadogo,” wanadamu mashuhuri na wasio mashuhuri, walioishi na kufa. Naam, hata vitoto vichanga vitakuwa miongoni mwa watakaofufuliwa! (Yeremia 31:15, 16) Kwenye Matendo 24:15, habari nyingine ya maana inafunuliwa: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Watu mashuhuri miongoni mwa “waadilifu” watakuwa wanaume na wanawake waaminifu wa zamani kama vile Abeli, Enoki, Noa, Abrahamu, Sara, na Rahabu. (Waebrania 11:1-40) Ebu wazia kuweza kuongea na mashahidi hao wa kujionea na kupata habari nyingi za matukio ya Biblia ya zamani za kale! “Waadilifu” pia watatia ndani maelfu ya watu wenye kuhofu Mungu ambao wamekufa nyakati za karibuni zaidi na ambao hawakuwa na tumaini la kimbingu. Je, una mshiriki wa familia au mpendwa ambaye huenda akawa miongoni mwao? Inafariji kama nini kujua kwamba unaweza kuwaona tena! Hata hivyo, ni nani hao “wasio waadilifu” ambao watafufuliwa pia? Wanatia ndani mamilioni, labda mabilioni, ambao walikufa bila kuwa na fursa ya kujifunza na kutumia kweli ya Biblia.
15. Yamaanisha nini kusema kwamba wanaofufuliwa “[watahukumiwa] kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika hizo hati-kunjo”?
15 Wenye kufufuliwa “[watahukumiwaje] kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika hizo hati-kunjo kulingana na vitendo vyao”? Hati-kunjo hizo si rekodi ya vitendo vyao vya wakati uliopita; walipokufa, waliondolewa hatia ya dhambi walizofanya maishani mwao. (Waroma 6:7, 23) Hata hivyo, wanadamu wenye kufufuliwa bado watakuwa chini ya dhambi ya Kiadamu. Basi, ni lazima iwe kwamba hati-kunjo hizo zitaeleza kikamili maagizo ya kimungu ambayo wote lazima wafuate ili wanufaike kikamili na dhabihu ya Yesu Kristo. Alama ya mwisho ya dhambi ya Kiadamu inapofutwa, “kifo kitafanywa kuwa si kitu” katika maana kamili. Kufikia mwisho wa miaka elfu, Mungu “[ata]kuwa vitu vyote kwa kila mtu.” (1 Wakorintho 15:28) Mwanadamu hatahitaji tena uingiliaji-kati wa Kuhani wa Cheo cha Juu au Mfidi. Wanadamu wote watarudishwa kwenye hali ya ukamilifu ambayo Adamu alifurahia hapo awali.
Ufufuo Wenye Utaratibu
16. (a) Kwa nini ni jambo la akili kuamini kwamba ufufuo utafanywa kwa utaratibu? (b) Yaelekea ni nani watakaokuwa miongoni mwa watu wa kwanza kufufuliwa?
16 Kwa kuwa ufufuo wa kimbingu ni wenye utaratibu, “kila mmoja katika daraja lake mwenyewe,” ni wazi kwamba ufufuo wa kidunia hautatokeza ongezeko la ghafula la idadi ya watu lisilo na utaratibu. (1 Wakorintho 15:23) Ni jambo lenye kueleweka kwamba, wenye kufufuliwa karibuni watahitaji kutunzwa. (Linganisha Luka 8:55.) Watahitaji riziki ya kimwili na msaada wa kiroho ambao ni wa maana zaidi katika kupata ujuzi wenye kutoa uhai juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Kama wote wangefufuliwa wakati uleule, haingewezekana kuwatunza vya kutosha. Ni jambo la akili kukata kauli kwamba ufufuo utatokea hatua kwa hatua. Wakristo waaminifu waliokufa punde kabla ya mwisho wa mfumo wa Shetani yaelekea watakuwa miongoni mwa wale watakaofufuliwa kwanza. Twaweza pia kutarajia ufufuo wa mapema wa wanaume waaminifu wa zamani watakaotumikia wakiwa “wakuu.”—Zaburi 45:16.
17. Ni masuala gani kuhusiana na ufufuo ambayo Biblia haisemi chochote kuyahusu, na ni kwa nini Wakristo hawapaswi kuhangaika isivyofaa kuhusu mambo hayo?
17 Hata hivyo, hatupaswi kuwalazimisha watu wafuate maoni yetu juu ya mambo hayo. Biblia haisemi chochote juu ya masuala mengi. Haina habari nyingi zilizo wazi juu ya vipi, lini, au mahali ambapo huo ufufuo wa watu utatokea. Haituambii jinsi wanaofufuliwa watakavyopewa makao, chakula, na nguo. Wala hatuwezi kusema kwa uhakika jinsi Yehova atakavyotatua masuala kama vile kulea na kutunza watoto wenye kufufuliwa wala jinsi atakavyoshughulikia hali fulani ambazo huenda zikahusisha marafiki na wapendwa wetu. Ni kweli ni jambo la kawaida kujiuliza maswali kuhusu mambo hayo; lakini halingekuwa jambo la hekima kupoteza wakati ukijaribu kuyajibu maswali ambayo kwa sasa hayawezi kujibiwa. Twapaswa kukaza fikira zetu juu ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu na juu ya kupata uhai udumuo milele. Wakristo watiwa-mafuta huweka tumaini lao katika ufufuo wa kimbingu. (2 Petro 1:10, 11) “Kondoo wengine” hutumaini kupata urithi udumuo milele katika makao ya kidunia ya Ufalme wa Mungu. (Yohana 10:16; Mathayo 25:33, 34) Kuhusu hizo habari nyingi ambazo hazijulikani juu ya ufufuo, tutamtumaini Yehova. Furaha yetu ya wakati ujao iko salama katika mikono ya Yule awezaye ‘kushibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zaburi 145:16; Yeremia 17:7.
18. (a) Paulo akazia ushindi gani? (b) Kwa nini tuko na tumaini hakika katika ufufuo?
18 Paulo amalizia kutoa hoja zake kwa kutangaza hivi: “Shukrani kwa Mungu, kwa maana yeye hutupa sisi ushindi kupitia Bwana wetu Yesu Kristo!” (1 Wakorintho 15:57) Naam, kifo cha Kiadamu hushindwa kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, na watiwa-mafuta na pia “kondoo wengine” hushiriki ushindi huo. Bila shaka, “kondoo wengine” walio hai leo wana tumaini ambalo ni la pekee kwa kizazi hiki. Wakiwa sehemu ya “umati mkubwa,” unaozidi kuongozeka huenda wakaokoka “dhiki kubwa” inayokuja, na kutopatwa kamwe na kifo cha mwili! (Ufunuo 7:9, 14) Hata hivyo, hata wale wanaokufa kwa sababu ya “wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW]” au wakiwa mikononi mwa wawakilishi wa Shetani, wanaweza kuweka uhakika wao katika tumaini la ufufuo.—Mhubiri 9:11.
19. Ni himizo gani lenye bidii ambalo Wakristo wote wapaswa kusikiza leo?
19 Kwa hiyo, twangojea kwa hamu siku hiyo tukufu kifo kitakapofanywa kuwa si kitu. Kutumaini katika ahadi ya Yehova ya ufufuo bila kuyumbayumba hufanya mambo yaonekane halisi. Chochote kitupatacho katika maisha haya—hata ikiwa tutakufa—hakuna chochote kiwezacho kutupokonya thawabu ambayo Yehova ameahidi. Kwa sababu hiyo, himizo lenye bidii la Paulo kwa Wakorintho lafaa leo kama vile lilivyofaa miaka elfu mbili iliyopita: “Kwa sababu hiyo, ndugu zangu wapendwa, iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.
-