-
Msiba Watokea GhafulaMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
Msiba Watokea Ghafula
OWEN, mvulana mwenye umri wa miaka miwili na nusu, alikuwa akicheza katika bafu nyumbani kwao. Alipanda na kuifikia kabati ya dawa ambayo wazazi wake walifikiri hawezi kuifikia. Owen aliona chupa iliyomvutia kati ya vitu vilivyokuwa ndani ya kabati hiyo. Alipoifungua na kunywa umajimaji uliokuwa ndani, msiba ulitokea.
Chupa hiyo ilikuwa na asidi kali, na kwa kusikitisha, Owen alikufa. Wazazi wake walihuzunika sana. Percy, baba yake, alienda kwa kasisi wa kanisa lake ili kufarijiwa. Alimwuliza, “Kwa nini jambo hili lilitukia?” Kasisi huyo akamjibu, “Mungu alitaka malaika mwingine mdogo mbinguni.” Mzazi huyo mwenye huzuni nyingi alihisi kwamba Mungu hakutenda haki hata kidogo. Je, kweli Mungu alitaka msiba huo utokee? Kwa kukata tamaa, Percy aliamua kuliacha kanisa hilo.
Alipofikiria yaliyotokea, Percy alijiuliza: ‘Je, mtoto wangu bado anateseka? Je, nitamwona tena?’
Huenda hata wewe hujui ni nini hutokea mtu anapokufa, na ikiwa wakati ujao itawezekana kuungana na wapendwa wetu waliokufa. Neno la Mungu, Biblia, hujibu maswali hayo. Biblia ina majibu yaliyo wazi na yenye kuwafariji wote waliofiwa. Isitoshe, inafunua tumaini tukufu ambalo Mungu ameahidi, yaani, ufufuo.
Tafadhali soma makala inayofuata ili upate kujua mengi zaidi kuhusu tumaini hilo zuri.
-
-
Tumaini Tukufu la UfufuoMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
Tumaini Tukufu la Ufufuo
WATU wengi wanaamini ufufuo. Kitabu kitakatifu cha Waislamu, Kurani, kina sura nzima inayozungumzia ufufuo. Sehemu fulani ya Sura ya 75 inasema: “Naapa kwa siku ya Kiama . . . Anadhani mtu ya kuwa sisi hatutaikusanya mifupa yake? . . . Anauliza: ‘Itakuwa lini hiyo siku ya Kiama?’ . . . Je! Hakuwa Huyo ni Muweza wa kuhuisha wafu?”—Sura 75:1-6, 40.
Kulingana na kitabu The New Encyclopædia Britannica, dini ya Zoroaster “hufundisha kwamba Uovu utashindwa kabisa, kutakuwa na ufufuo wa watu kwa ujumla, Hukumu ya Mwisho, na kusafishwa kwa ulimwengu kwa ajili ya waadilifu.”
Kitabu Encyclopaedia Judaica hufafanua ufufuo kuwa “imani kwamba hatimaye wafu watafufuliwa na kuishi tena duniani.” Kitabu hichohicho kinasema pia kwamba fundisho lililokubaliwa rasmi katika Dini ya Kiyahudi kuwa mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa linatatanisha. Kinakiri hivi: “Imani katika ufufuo inapingana na imani katika nafsi isiyoweza kufa.”
Wahindu hufundisha kwamba mwanadamu huzaliwa upya katika mwili mwingine tena na tena. Kwa hiyo, lazima mwanadamu awe na nafsi inayoendelea kuishi baada ya kifo ili aweze kuzaliwa upya. Kitabu kitakatifu cha Wahindu, Bhagavad Gita, kinasema: “Nafsi iliyo katika kila sehemu ya mwili haiwezi kuharibiwa. Hakuna anayeweza kuharibu nafsi isiyoweza kuharibiwa.”
Wabudha hutofautiana na Wahindu kwa kufundisha kwamba nafsi inaweza kufa. Hata hivyo, leo Wabudha wengi katika Mashariki ya Mbali wanaamini kwamba nafsi haifi bali huhama na kuingia katika mwili mwingine.a
Wachanganyikiwa Kuhusu Fundisho la Ufufuo
Mara nyingi dini zinazojidai kuwa za Kikristo hutaja ufufuo na pia nafsi inayoendelea kuishi baada ya kifo katika ibada zao za mazishi. Kwa mfano, ni kawaida kwa kasisi Mwanglikana kukariri maneno haya: ‘Kwa kuwa imempendeza Mungu Mweza-Yote katika rehema zake nyingi kuichukua nafsi ya ndugu yetu mpendwa ambaye ametuacha, basi tunaurudisha mwili wake kwenye ardhi; udongo urudi kwenye udongo, majivu yarudi kwenye majivu, na mavumbi yarudi kwenye mavumbi; tukitumaini kabisa kwamba Bwana wetu Yesu Kristo atamfufua aishi milele.’—The Book of Common Prayer.
Maneno hayo yanaweza kumtatanisha mtu asijue kama Biblia hufundisha kuhusu ufufuo au nafsi isiyoweza kufa. Hata hivyo, ona maneno yaliyoandikwa na Oscar Cullmann, ambaye ni Profesa Mprotestanti nchini Ufaransa. Anaandika hivi katika kitabu chake, Immortality of the Soul or Resurrection of the Dead?: “Kuna tofauti kubwa kati ya imani ya Wakristo katika ufufuo wa wafu na imani ya Wagiriki katika nafsi isiyoweza kufa. . . . Ingawa baadaye Ukristo ulionyesha kwamba imani hizi mbili zinahusiana, na leo Mkristo wa kawaida amechanganyikiwa kuhusu imani hizo, sioni sababu ya kuficha kile ambacho mimi na wasomi wengi hukiona kuwa kweli. . . . Imani katika ufufuo ndilo fundisho muhimu katika Agano Jipya. . . . Mwanadamu aliyekufa kabisa hufufuliwa kupitia tendo jipya la uumbaji.”
Haishangazi kwamba watu kwa ujumla wamechanganyikiwa kuhusu kifo na ufufuo. Ili kutatua tatizo hilo, tunahitaji kuitegemea Biblia ambayo ina kweli zilizofunuliwa na Muumba wa mwanadamu, Yehova Mungu. Biblia imetaja visa kadhaa vya ufufuo. Acheni tuchunguze visa vinne na tuone mambo ambayo vinafunua kuhusu ufufuo.
“Wanawake Waliwapokea Wafu Wao kwa Ufufuo”
Katika barua yake kwa Wayahudi waliokuwa Wakristo, mtume Paulo alisema kwamba wanawake wenye imani “waliwapokea wafu wao kwa ufufuo.” (Waebrania 11:35) Mmoja wao aliishi Sarefathi, mji wa Foinike uliokuwa karibu na Sidoni kwenye Pwani ya Mediterania. Mwanamke huyo alikuwa mjane, naye alimkaribisha Eliya nabii wa Mungu na hata kumpa chakula wakati wa njaa kali. Kwa kusikitisha, mwana wa mwanamke huyo alishikwa na ugonjwa na kufa. Eliya alimpeleka mvulana huyo moja kwa moja kwenye chumba cha darini, ambako nabii huyo alikuwa akikaa, kisha akamwomba Yehova amfufue. Muujiza ulitokea, na kijana huyo “akawa hai.” Eliya alimrudisha kwa mama yake na kusema: “Tazama, mwana wako yuko hai.” Mwanamke huyo alifanyaje? Alisema hivi kwa furaha: “Kwa kweli sasa najua kwamba wewe ni mtu wa Mungu na kwamba neno la Yehova kinywani mwako ni la kweli.”—1 Wafalme 17:22-24.
Elisha aliyekuwa nabii baada ya Eliya, alitunzwa na mtu mmoja na mkewe ambao waliishi umbali wa kilometa 100 hivi kusini ya Sarefathi. Mke wa mtu huyo alikuwa mashuhuri katika kijiji cha kwao cha Shunemu. Yeye na mumewe walikubali Elisha akae katika chumba cha darini nyumbani kwao. Walikuwa na huzuni kwa sababu hawakuwa na watoto, lakini walifurahi mwanamke huyo alipozaa mtoto wa kiume. Mvulana huyo alipoendelea kukua, mara nyingi alikuwa akienda shambani kujiunga na wavunaji na babake. Siku moja, msiba ulitokea. Mvulana huyo alisema kwamba anaumwa na kichwa. Mtumishi mmoja alimpeleka nyumbani haraka ambako mamake alimweka kwenye mapaja yake. Lakini mtoto huyo akafa. Mama huyo mwenye huzuni aliamua kumwita Elisha amsaidie. Huku akiandamana na mtumishi fulani, mama huyo alisafiri kuelekea Mlima Karmeli, upande wa kaskazini-magharibi, ambako Elisha alikuwa akikaa.
Nabii huyo alimtuma Gehazi, mtumishi wake, atangulie, naye akakuta kwamba kwa hakika mvulana huyo alikuwa amekufa. Elisha na mwanamke huyo walikuja baadaye, lakini ni nini kilichotukia walipofika Shunemu? Andiko la 2 Wafalme 4:32-37 linasema: “Mwishowe Elisha akaingia katika hiyo nyumba, na, tazama, huyo mvulana alikuwa amekufa, amelazwa juu ya kitanda chake. Ndipo akaingia ndani, akafunga mlango nyuma yao wawili, akaanza kusali kwa Yehova. Mwishowe akaenda juu, akajilaza juu ya yule mtoto, akakitia kinywa chake juu ya kinywa chake, na macho yake juu ya macho yake, na mikono yake juu ya mikono yake, akaendelea kuinama juu yake, na hatua kwa hatua mwili wa mtoto ukawa na joto. Kisha akaanza kutembea tena ndani ya nyumba, mara moja huku mara moja kule, halafu akaenda juu, akainama juu yake. Na yule mvulana akaanza kupiga chafya mara saba, kisha mvulana huyo akafungua macho yake. Sasa akamwita Gehazi na kusema: ‘Mwite huyo mwanamke Mshunamu.’ Basi akamwita, naye akaingia kwake. Kisha akasema: ‘Mchukue mwana wako.’ Naye akaingia, akaanguka miguuni pake, akamwinamia mpaka chini, kisha akamchukua mwana wake, akatoka nje.”
Kama yule mjane wa Sarefathi, mwanamke huyo wa Shunemu alijua kwamba mtoto wake alifufuliwa kwa nguvu za Mungu. Wanawake hao wawili walipata shangwe kubwa Mungu alipowafufua watoto wao wapendwa.
Ufufuo Wakati wa Huduma ya Yesu
Miaka 900 hivi baadaye, ufufuo ulitokea kaskazini ya Shunemu, nje ya kijiji cha Naini ambacho hakikuwa mbali na Shunemu. Yesu Kristo na wanafunzi wake waliposafiri kutoka Kapernaumu na kukaribia lango la Naini, walikutana na msafara wa mazishi, na Yesu akamwona mjane aliyekuwa amefiwa na mwanawe wa pekee. Yesu alimwambia aache kulia. Luka, ambaye alikuwa daktari, anaeleza kilichotukia: “Ndipo [Yesu] akakaribia na kuligusa sanduku, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Kijana, ninakuambia, Inuka!’ Na huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake.” (Luka 7:14, 15) Wale walioona muujiza huo walimtukuza Mungu. Habari kuhusu ufufuo huo zilienea upande wa kusini hadi Yudea na wilaya ya karibu. Wanafunzi wa Yohana Mbatizaji walisikia habari hizo, nao wakamweleza Yohana kuhusu muujiza huo. Yohana naye akawatuma kumtafuta Yesu na kumuuliza kama Yeye ndiye Masihi anayetarajiwa. Yesu aliwaambia: “Nendeni, mkamwambie Yohana yale mliyoona na kusikia: vipofu wanaona, vilema wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa na viziwi wanasikia, na wafu wanafufuliwa, maskini wanaambiwa ile habari njema.”—Luka 7:22.
Muujiza ambao Yesu alifanya alipomfufua rafiki yake Lazaro ndio maarufu zaidi kati ya miujiza yake ya ufufuo. Katika kisa hiki kuhusu kifo cha Lazaro, Yesu hakwenda nyumbani kwa akina Lazaro moja kwa moja. Hatimaye, Yesu alipofika Bethania, Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne. Yesu alipoagiza kwamba jiwe lililokuwa kwenye mlango wa kaburi liondolewe, Martha alikataa na kusema hivi: “Bwana, kufikia sasa lazima awe ananuka, kwa maana ni siku nne.” (Yohana 11:39) Hata hivyo, Lazaro alifufuliwa licha ya kuharibika kwa mwili wake. Kwa amri ya Yesu, “huyo mtu aliyekuwa mfu akatoka miguu na mikono yake ikiwa imefungwa vitambaa, na uso wake ulikuwa umefungwa-fungwa kwa kitambaa.” Matendo ya adui za Yesu baadaye yanathibitisha pasipo shaka kwamba Lazaro alifufuliwa.—Yohana 11:43, 44; 12:1, 9-11.
Tunafikia mkataa gani kutokana na visa hivyo vinne vya ufufuo? Kila aliyefufuliwa alikuwa mtu yuleyule aliyekufa. Wote walitambuliwa na watu, kutia ndani jamaa zao wa karibu. Hakuna yeyote kati yao aliyeeleza kilichotukia katika kipindi kifupi alipokuwa mfu. Hakuna yeyote aliyetaja kwamba alisafiri kwenda katika ulimwengu mwingine. Yaonekana wote walifufuliwa wakiwa na afya nzuri. Kama Yesu alivyodokeza, ni kana kwamba walikuwa wamelala usingizi kwa muda mfupi, kisha wakaamka. (Yohana 11:11) Hata hivyo, wote walikufa baadaye.
Tazamio Tukufu la Kuwaona Tena Wapendwa Wetu
Muda mfupi baada ya kifo chenye kuhuzunisha cha Owen, aliyetajwa katika makala inayotangulia, babake alimtembelea jirani. Akiwa huko, aliona juu ya meza kikaratasi cha kuwakaribisha watu kwenye hotuba ya watu wote iliyopangwa na Mashahidi wa Yehova. Kichwa cha hotuba hiyo, “Wafu Wako Wapi?,” kilimvutia. Alikuwa anajiuliza swali hilohilo. Alienda kusikiliza hotuba hiyo naye akapata faraja ya kweli kutoka katika Biblia. Alijifunza kwamba wafu hawateseki. Badala ya kuteseka motoni au kuchukuliwa na Mungu ili wawe malaika mbinguni, wafu, kutia ndani Owen, wanangojea kaburini hadi watakapoamshwa katika ufufuo.—Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4.
Je, familia yako imepatwa na msiba? Je, kama vile babake Owen, wewe unataka kujua mahali walipo wapendwa wako waliokufa na kama inawezekana kuwaona tena? Basi tunakualika uchunguze mafundisho zaidi ya Biblia kuhusu ufufuo. Labda unajiuliza: ‘Ufufuo utakuwa lini? Ni nani hasa watakaofufuliwa?’ Tafadhali soma makala zinazofuata ambazo zitazungumzia maswali hayo na mengineyo.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, ukurasa wa 150-154, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Fundisho la Ufufuo LinakuhusuMnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
Fundisho la Ufufuo Linakuhusu
“Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—MATENDO 24:15.
1. Ufufuo ulipataje kuwa suala la kujadiliwa mbele ya Sanhedrini?
MTUME Paulo alikuwa Yerusalemu mwishoni mwa safari yake ya tatu ya umishonari mwaka wa 56 W.K. Baada ya kukamatwa na Waroma, aliruhusiwa kwenda mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi. (Matendo 22:29, 30) Paulo alipowatazama washiriki wa mahakama hiyo, aliona Masadukayo na Mafarisayo. Kulikuwa na tofauti moja kubwa sana kati ya vikundi hivyo viwili. Mafarisayo waliamini kuna ufufuo, nao Masadukayo walisema hakuna ufufuo. Ili kuonyesha msimamo wake kuhusu suala hilo, Paulo alisema: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo, mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa juu ya tumaini la ufufuo wa wafu.” Maneno hayo ya Paulo yalisababisha mvurugo katika mahakama hiyo!—Matendo 23:6-9.
2. Kwa nini Paulo alikuwa tayari kutetea imani yake kuhusu ufufuo?
2 Miaka kadhaa awali, alipokuwa njiani kwenda Damasko, Paulo aliona maono na kusikia sauti ya Yesu. Paulo hata alimuuliza Yesu: “Nitafanya nini, Bwana?” Yesu akamjibu: “Simama, ondoka uende Damasko, na huko utaambiwa kila kitu ambacho umewekewa kufanya.” Paulo alipofika Damasko, Anania, mwanafunzi Mkristo mwenye kujali, alimtafuta Paulo na kumweleza hivi: “Mungu wa mababu zetu amekuchagua upate kujua mapenzi yake na kumwona yule Aliye mwadilifu [Yesu aliyefufuliwa] na kuisikia sauti ya kinywa chake.” (Matendo 22:6-16) Basi, haishangazi kwamba Paulo alikuwa tayari kutetea imani yake kuhusu ufufuo.—1 Petro 3:15.
Atangaza Waziwazi Tumaini la Ufufuo
3, 4. Paulo aliliteteaje fundisho la ufufuo kwa uthabiti, na mfano wake unaweza kutufunza nini?
3 Baadaye, Paulo alipelekwa mbele ya Gavana Feliksi. Pindi hiyo, Tertulo, “msemaji wa hadharani” aliyewasilisha kesi ya Wayahudi dhidi ya Paulo, alimshtaki kuwa mchochezi wa uasi na kiongozi wa madhehebu fulani. Kwa kujibu, Paulo alitangaza hivi waziwazi: “Ninakiri jambo hili kwako, kwamba, kulingana na ile njia wanayoiita ‘madhehebu,’ kwa namna hii mimi ninatoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zangu.” Kisha akaeleza suala kuu lililohusika kwa kusema: “Nina tumaini kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanalo, kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 23:23, 24; 24:1-8, 14, 15.
4 Miaka miwili hivi baadaye, Porkio Festo, aliyekuwa Gavana baada ya Feliksi, alimwalika Mfalme Herode Agripa ajiunge naye kumhoji Paulo, aliyekuwa mfungwa. Festo alieleza kwamba wale waliomshtaki Paulo walikataa dai lake kwamba “mtu fulani anayeitwa Yesu aliyekuwa amekufa . . . alikuwa hai.” Paulo alijitetea kwa kuuliza hivi: “Kwa nini mnaamua kwamba ni jambo lisiloaminika kwamba Mungu hufufua wafu?” Kisha akasema: “Kwa sababu nimeupata msaada kutoka kwa Mungu ninaendelea mpaka leo kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia, lakini bila kusema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia, kwamba Kristo angeteseka na, akiwa wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu, angetangaza nuru kwa watu hawa na pia kwa mataifa.” (Matendo 24:27; 25:13-22; 26:8, 22, 23) Paulo alikuwa mteteaji thabiti sana wa tumaini la ufufuo. Kama Paulo, sisi pia tunaweza kutangaza kwa uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo. Lakini tunaweza kutazamia watu waitikieje? Yaelekea itikio litakuwa sawa na lile ambalo Paulo alipata.
5, 6. (a) Watu waliitikiaje mitume walipotetea tumaini la ufufuo? (b) Tunapoendelea kuwaeleza watu kuhusu tumaini letu katika ufufuo, ni jambo gani lililo muhimu?
5 Fikiria mambo yaliyotukia mapema katika safari ya pili ya Paulo ya umishonari (yapata mwaka wa 49-52 W.K.) alipotembelea jiji la Athene. Alijadiliana na watu walioamini katika miungu mingi na kuwahimiza wafikirie kusudi la Mungu la kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye Amemweka rasmi. Mwanamume huyo ni Yesu. Paulo alieleza kwamba Mungu alitoa uhakikisho wa jambo hilo kwa kumfufua Yesu. Watu waliitikiaje? Tunasoma hivi: “Basi, waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine kati yao wakaanza kudhihaki, huku wengine wakisema: ‘Tutakusikiliza tena juu ya jambo hili wakati mwingine.’”—Matendo 17:29-32.
6 Watu hao waliitikia kama wale waliowasikiliza Petro na Yohana muda mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K. Kwa mara nyingine tena, Masadukayo walihusika sana katika ubishi huo. Andiko la Matendo 4:1-4 linaeleza kilichotukia: “Sasa hao wawili walipokuwa wakisema na watu, wakuu wa makuhani na kapteni wa hekalu na Masadukayo wakawajia, wakiwa wameudhika kwa sababu walikuwa wakiwafundisha watu na walikuwa wakiutangaza waziwazi ufufuo kutoka kwa wafu kwa kisa cha Yesu.” Hata hivyo, wengine waliitikia vizuri. “Wengi kati ya wale waliokuwa wamesikiliza maneno hayo wakaamini, na hesabu ya wanaume ikawa karibu elfu tano.” Tunaweza kutazamia watu waitikie kwa njia tofauti-tofauti tunapowaeleza kuhusu tumaini la ufufuo. Kwa hiyo, ni muhimu tuimarishe imani yetu katika fundisho hilo.
Imani na Ufufuo
7, 8. (a) Kama inavyoonyeshwa katika barua iliyoandikiwa kutaniko la Korintho katika karne ya kwanza, imani inawezaje kuwa bure? (b) Kulielewa tumaini la ufufuo kwa usahihi hutofautishaje Wakristo wa kweli na wa uwongo?
7 Si Wakristo wote katika karne ya kwanza W.K. waliokubali kwa urahisi tumaini la ufufuo. Baadhi ya Wakristo hao walikuwa katika kutaniko la Korintho. Paulo aliwaandikia hivi: “Niliwapa ninyi, kati ya mambo ya kwanza, yale niliyopokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.” Kisha Paulo akathibitisha jambo hilo kwa kusema kwamba Kristo aliyefufuliwa “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano,” naye akaongeza kwamba wengi wao bado walikuwa hai. (1 Wakorintho 15:3-8) Paulo pia alitoa hoja hii: “Ikiwa Kristo anahubiriwa kwamba amefufuliwa kutoka kwa wafu, kwa nini wengine kati yenu wanasema hakuna ufufuo wa wafu? Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, basi Kristo hakufufuliwa. Lakini ikiwa Kristo hakufufuliwa, hakika kuhubiri kwetu ni bure, na imani yetu ni bure.”—1 Wakorintho 15:12-14.
8 Kwa kweli, fundisho la ufufuo ni muhimu sana hivi kwamba imani ya Kikristo ni bure ikiwa ufufuo haukubaliwi kuwa jambo halisi. Naam, kuuelewa ufufuo kwa usahihi hutofautisha Wakristo wa kweli na wa uwongo. (Mwanzo 3:4; Ezekieli 18:4) Kwa hiyo, Paulo anataja ufufuo kuwa sehemu ya “fundisho la msingi” la Ukristo. Na tuazimie ‘kusonga mbele kuelekea ukomavu.’ Paulo anatuhimiza hivi: “Na hili tutalifanya, ikiwa kwa kweli Mungu ataruhusu.”—Waebrania 6:1-3.
Tumaini la Ufufuo
9, 10. Biblia inamaanisha nini inapotaja ufufuo?
9 Ili kuimarisha imani yetu katika ufufuo, acheni tuchunguze maswali haya: Biblia inamaanisha nini inapotaja ufufuo? Fundisho la ufufuo huonyeshaje kwamba Yehova ana upendo mwingi sana? Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kuwafundisha wengine na pia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.—2 Timotheo 2:2; Yakobo 4:8.
10 “Ufufuo” ni tafsiri ya neno la Kigiriki ambalo kihalisi linamaanisha “kusimama tena.” Neno hilo linahusisha nini? Kulingana na Biblia, tumaini la ufufuo ni usadikisho kwamba mtu aliyekufa anaweza kuishi tena. Pia Biblia inaonyesha kwamba mtu hufufuliwa akiwa na mwili wa kibinadamu ikiwa ana tumaini la kuishi duniani, au mwili wa roho ikiwa ana tumaini la kuishi mbinguni. Tunavutiwa na upendo, hekima, na nguvu ambazo Yehova anaonyesha katika tumaini hili zuri la ufufuo.
11. Watumishi wa Mungu watiwa-mafuta wanaweza kutazamia nini kuhusiana na ufufuo?
11 Kama vile Yesu, ndugu zake watiwa-mafuta hupewa mwili wa roho wanapofufuliwa ambao unafaa kwa utumishi wao mbinguni. (1 Wakorintho 15:35-38, 42-53) Yesu na ndugu zake watiwa-mafuta watatawala katika Ufalme wa Kimasihi ambao utaifanya dunia kuwa Paradiso. Watiwa-mafuta wanakuwa ukuhani wa kifalme chini ya Yesu, Kuhani Mkuu. Watatumia faida za dhabihu yake ya fidia kwa ajili ya wanadamu katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Waebrania 7:25, 26; 9:24; 1 Petro 2:9; Ufunuo 22:1, 2) Sasa Wakristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani wanatamani kuendelea kuwa na kibali cha Mungu. Wanapokufa, wanapokea “thawabu” yao kwa kufufuliwa ili waishi mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. (2 Wakorintho 5:1-3, 6-8, 10; 1 Wakorintho 15:51, 52; Ufunuo 14:13) Paulo aliandika: “Ikiwa tumeungana pamoja naye katika mfano wa kifo chake, hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika mfano wa ufufuo wake.” (Waroma 6:5) Lakini vipi wale ambao watafufuliwa kuishi tena duniani wakiwa wanadamu? Tumaini la ufufuo linawezaje kuwasaidia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu? Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wa Abrahamu.
Ufufuo na Urafiki Pamoja na Yehova
12, 13. Abrahamu alikuwa na sababu gani nzuri sana ya kuamini katika ufufuo?
12 Abrahamu, anayetajwa kuwa “rafiki ya Yehova,” alikuwa na imani ya pekee. (Yakobo 2:23) Paulo alitaja imani ya Abrahamu mara tatu alipowataja wanaume na wanawake wenye imani katika sura ya 11 ya kitabu cha Waebrania. (Waebrania 11:8, 9, 17) Anapomtaja Abrahamu mara ya tatu anakazia imani ambayo Abrahamu alionyesha wakati ambapo, kwa utii, alimtayarisha mwanawe Isaka ili amtoe akiwa dhabihu. Abrahamu alisadiki kwamba Yehova hangekosa kutimiza ahadi yake ya kumpa uzao kupitia Isaka. Hata kama Isaka angekufa kwa kutolewa akiwa dhabihu, Abrahamu “alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua hata kutoka kwa wafu.”
13 Hivyo, Yehova alipoona imani yenye nguvu ya Abrahamu, aliandaa mnyama atolewe akiwa dhabihu badala ya Isaka. Hata hivyo, kisa cha Isaka kinatoa mfano wa ufufuo, kama Paulo alivyoeleza: “Kutoka huko [Abrahamu] alimpokea [Isaka] pia kwa njia ya mfano.” (Waebrania 11:19) Isitoshe, tayari Abrahamu alikuwa na sababu nzuri sana ya kuamini ufufuo. Je, Yehova hakurudisha nguvu za uzazi za Abrahamu wakati yeye na mke wake Sara walipompata mwana wao Isaka wakiwa wazee?—Mwanzo 18:10-14; 21:1-3; Waroma 4:19-21.
14. (a) Kulingana na Waebrania 11:9, 10, Abrahamu alingojea nini? (b) Ni jambo gani ambalo ni lazima litukie kwa Abrahamu ili apate baraka za Ufalme katika ulimwengu mpya? (c) Tunawezaje kupata baraka za Ufalme?
14 Paulo alitaja kwamba Abrahamu alikuwa mkaaji mgeni, aliyeishi katika mahema “akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Waebrania 11:9, 10) Hilo ni jiji la mfano, wala si jiji halisi kama Yerusalemu, ambako hekalu la Mungu lilikuwa. Jiji hilo ni Ufalme wa mbinguni wa Mungu ambao mtawala wake ni Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000. Wanapokuwa katika utukufu wao mbinguni, watawala hao 144,000 pia wanaitwa “jiji takatifu, Yerusalemu Jipya,” “bibi-arusi” wa Kristo. (Ufunuo 21:2) Katika mwaka wa 1914, Yehova alimtawaza Yesu kuwa Mfalme wa Kimasihi wa Ufalme wa mbinguni na kumwamuru atawale katikati ya adui zake. (Zaburi 110:1, 2; Ufunuo 11:15) Ili kupata baraka za utawala wa Ufalme, lazima Abrahamu, “rafiki ya Yehova,” aishi tena. Vivyo hivyo, ili tupate baraka za Ufalme, lazima tuwe hai katika ulimwengu mpya wa Mungu tukiwa sehemu ya umati mkubwa utakaookoka Har–Magedoni au wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu. (Ufunuo 7:9, 14) Lakini ni nini msingi wa tumaini la ufufuo?
Upendo wa Mungu Ndio Msingi wa Tumaini la Ufufuo
15, 16. (a) Unabii wa kwanza katika Biblia hutuwekeaje msingi wa kuwa na tumaini la ufufuo? (b) Imani katika ufufuo hutuwezeshaje kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?
15 Kwa sababu ya uhusiano wetu wa karibu pamoja na Baba yetu mwenye upendo wa mbinguni, imani yetu yenye nguvu kama ile ya Abrahamu, na utii wetu kwa amri za Mungu, Yehova hututangaza kuwa waadilifu na kutuona kuwa rafiki zake. Hilo hutuwezesha kunufaika na utawala wa Ufalme. Naam, unabii wa kwanza kabisa kuandikwa katika Neno la Mungu, kwenye Mwanzo 3:15, hutuwekea msingi wa kuwa na tumaini la ufufuo na urafiki pamoja na Mungu. Unabii huo unataja kupondwa kwa kichwa cha Shetani na pia kutiwa jeraha kwa kisigino cha Uzao wa mwanamke wa Mungu. Yesu alitiwa jeraha kwa njia ya mfano alipokufa kwenye mti wa mateso. Ufufuo wake katika siku ya tatu uliponya kidonda hicho na kumwezesha kuchukua hatua madhubuti dhidi ya “yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.”—Waebrania 2:14.
16 Paulo anatukumbusha kwamba “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Waroma 5:8) Kuthamini fadhili hizo zisizostahiliwa hutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yesu na Baba yetu wenye upendo wa mbinguni.—2 Wakorintho 5:14, 15.
17. (a) Ayubu alikuwa na tumaini gani? (b) Andiko la Ayubu 14:15 linafunua nini kumhusu Yehova, na jambo hilo linakufanya uhisije?
17 Ayubu, mtu mwaminifu aliyeishi kabla ya Ukristo, alitarajia kufufuliwa pia. Shetani alimtesa sana. Ayubu alikuwa tofauti na rafiki zake wa uwongo ambao hawakutaja ufufuo kamwe. Alifarijiwa na tumaini hilo la ufufuo na kuuliza: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Akijibu swali lake mwenyewe, Ayubu alisema: “Mimi nitangojea siku zote za kazi yangu ya kulazimishwa, mpaka kitulizo changu kije.” Alipozungumza na Mungu wake Yehova, Ayubu alisema hivi: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.” Kuhusu hisia za Muumba wetu mwenye upendo, Ayubu alisema: “Utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Naam, Yehova anatazamia kwa hamu wakati ambapo waaminifu watakuwa hai tena kupitia ufufuo. Kwa kweli, jambo hilo hutuvuta kwake tunapotafakari kuhusu upendo na fadhili zisizostahiliwa ambazo yeye hutuonyesha ingawa sisi si wakamilifu!—Waroma 5:21; Yakobo 4:8.
18, 19. (a) Danieli ana tazamio gani la kuishi tena? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?
18 Nabii Danieli, ambaye alitajwa na malaika wa Mungu kuwa “mtu mwenye kutamanika sana,” alimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa muda mrefu. (Danieli 10:11, 19) Alidumisha utimilifu wake kwa Yehova tangu apelekwe uhamishoni mwaka wa 617 K.W.K., hadi alipokufa muda fulani baada ya kupata maono mwaka wa 536 K.W.K., ambao ulikuwa mwaka wa tatu wa utawala wa Koreshi, mfalme wa Uajemi. (Danieli 1:1; 10:1) Wakati fulani katika mwaka huo wa tatu wa utawala wa Koreshi, Danieli aliona maono kuhusu mfuatano wa serikali za ulimwengu ambao utakoma wakati wa dhiki kuu inayokuja. (Danieli 11:1–12:13) Kwa kuwa hakuweza kuelewa maono hayo kikamili, Danieli alimuuliza hivi malaika aliyetumwa kumwonyesha maono hayo: “Ee bwana wangu, mwisho wa mambo hayo utakuwa nini?” Malaika huyo alimjibu kwa kutaja “wakati wa mwisho” ambapo “wale walio na ufahamu wataelewa.” Danieli mwenyewe alikuwa na tazamio gani? Malaika huyo alimwambia: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” (Danieli 12:8-10, 13) Danieli atarudi “katika ufufuo wa walio waadilifu,” wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo.—Luka 14:14.
19 Tunaishi katika umalizio wa wakati wa mwisho na sasa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo uko karibu zaidi kuanza kutawala kuliko wakati tulipoanza kuamini. Kwa hiyo, lazima tujiulize, ‘Je, nitakuwapo katika dunia mpya ili kuungana na Abrahamu, Ayubu, Danieli, na wanaume na wanawake wengine waaminifu?’ Tutakuwapo ikiwa tutaendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kutii amri zake. Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza tumaini la ufufuo kwa undani zaidi ili tupate kujua ni nani watakaofufuliwa.
-
-
Ni Nani Watakaofufuliwa?Mnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
Ni Nani Watakaofufuliwa?
“Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” —YOHANA 5:28, 29.
1. Ni maneno gani ya ajabu ambayo Musa alisikia kwenye mti wa miiba uliokuwa ukiwaka moto, na ni nani aliyeyarudia baadaye?
JAMBO fulani la ajabu sana lilitukia miaka zaidi ya 3,500 iliyopita. Musa alikuwa akichunga kondoo za Yethro, mzee wa ukoo, karibu na Mlima Horebu, wakati malaika wa Yehova alipomtokea katika mwali wa moto katikati ya mti wa miiba. Kitabu cha Kutoka kinasema: “Alipoendelea kuangalia, tazama, ule mti wa miiba ulikuwa ukiwaka moto lakini haukuwa ukiteketea.” Kisha sauti ikamwita kutoka kwenye mti huo na kumwambia: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.” (Kutoka 3:1-6) Baadaye katika karne ya kwanza W.K., maneno hayo yalirudiwa na Yesu, Mwana wa Mungu.
2, 3. (a) Abrahamu, Isaka, na Yakobo wanangojea thawabu gani? (b) Ni maswali gani yanayotokea?
2 Yesu alikuwa akizungumza na Masadukayo fulani ambao hawakuamini ufufuo. Yesu alisema: “Hata Musa alifunua kwamba wafu watafufuliwa, katika masimulizi juu ya ule mti wa miiba, anapomwita Yehova ‘Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, hao wote wako hai.” (Luka 20:27, 37, 38) Kwa kusema hivyo, Yesu alithibitisha kwamba kulingana na maoni ya Mungu, bado Abrahamu, Isaka, na Yakobo, waliokufa zamani, wako hai katika kumbukumbu ya Mungu. Kama Ayubu, wanangojea ‘kazi yao ya kulazimishwa’ iishe, yaani, kulala usingizi katika kifo. (Ayubu 14:14) Watafufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.
3 Lakini, itakuwaje kwa mabilioni ya watu ambao wamekufa katika historia yote ya mwanadamu? Je, wao pia watafufuliwa? Kabla ya kujibu swali hilo kwa njia yenye kuridhisha, na tuone kulingana na Neno la Mungu watu huenda wapi wanapokufa.
Wafu Wako Wapi?
4. (a) Watu huenda wapi wanapokufa? (b) Sheoli ni nini?
4 Biblia inasema kwamba wafu “hawajui lolote kamwe.” Baada ya kifo, wanadamu hawateswi katika moto wala hawangoji kwa muda mrefu chini ya hali ngumu katika Ahera, bali wao hurudi mavumbini. Kwa hiyo, Neno la Mungu linawashauri hivi walio hai: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi [“Sheoli,” maelezo ya chini], mahali unapokwenda.” (Mhubiri 9:5, 10; Mwanzo 3:19) Hapa neno “Kaburi” ni tafsiri ya neno la Kiebrania “Sheoli.” Dini nyingi hufundisha kwamba wafu bado wako hai, lakini kama vile Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linavyoonyesha, wale walio katika Sheoli wamekufa, hawana fahamu yoyote. Sheoli ni kaburi.
5, 6. Yakobo alienda wapi alipokufa, naye alijiunga na nani huko?
5 Katika Biblia, neno “Sheoli” linapatikana kwa mara ya kwanza katika Mwanzo 37:35. Baada ya kufikiri kwamba mwanawe mpendwa Yosefu alikuwa amekufa, mzee wa ukoo Yakobo alikataa kufarijiwa na kusema: “Nitashuka kuingia katika [Sheoli] nikimwombolezea mwanangu!” Kwa kuamini kwamba mwanawe alikuwa amekufa, Yakobo alitamani kufa na kwenda katika Sheoli. Baadaye, wana tisa wa Yakobo, waliokuwa na umri mkubwa, walitaka kwenda na mwanawe mdogo, Benyamini, huko Misri ili kutafuta chakula kwa sababu ya njaa. Hata hivyo, Yakobo alikataa na kusema: “Mwanangu hatashuka kwenda nanyi, kwa sababu ndugu yake amekufa naye amebaki peke yake. Tukio lenye kufisha likimpata katika njia mtakayoiendea, basi bila shaka mtazishusha mvi zangu kwa huzuni mpaka katika [Sheoli].” (Mwanzo 42:36, 38) Maandiko hayo mawili yanahusianisha kifo na Sheoli, bali si hali ya kuendelea kuishi baada ya kufa.
6 Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yanaonyesha kwamba Yosefu alikuwa msimamizi wa chakula huko Misri. Hivyo, Yakobo alienda huko ili akaungane kwa furaha na Yosefu. Baadaye, Yakobo aliishi katika nchi hiyo hadi alipokufa akiwa na umri mkubwa wa miaka 147. Kulingana na mapendekezo yake kabla ya kufa, wanawe waliusafirisha mwili wake na kuuzika katika pango la Makpela katika nchi ya Kanaani. (Mwanzo 47:28; 49:29-31; 50:12, 13) Kwa hiyo, Yakobo alijiunga na Isaka baba yake, na Abrahamu babu yake.
‘Walikusanywa kwa Mababu Zao’
7, 8. (a) Abrahamu alienda wapi alipokufa? Eleza. (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba wengine walienda katika Sheoli walipokufa?
7 Awali, Yehova alipohalalisha agano lake na Abrahamu na kumwahidi kwamba uzao wake ungekuwa mwingi, alimweleza jambo ambalo lingempata. Yehova alimwambia hivi: “Lakini wewe, utaenda kwa mababu zako kwa amani; utazikwa katika uzee mwema.” (Mwanzo 15:15) Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Andiko la Mwanzo 25:8 linasema: “Kisha Abrahamu akakata pumzi, akafa katika umri mwema wa uzee, akiwa mzee na mwenye kutosheka, naye akakusanywa kwa watu wake.” Hao ni akina nani? Andiko la Mwanzo 11:10-26 linataja mababu zake wote kuanzia Shemu, mwana wa Noa. Kwa hiyo alipokufa, Abrahamu alikusanywa na kujiunga na watu hao ambao tayari walikuwa wanalala katika Sheoli.
8 Maneno ‘kukusanywa kwa watu wake’ yametajwa mara nyingi katika Maandiko ya Kiebrania. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Ishmaeli, mwana wa Abrahamu, na Haruni, ndugu ya Musa, walienda katika Sheoli walipokufa, nao wanangojea ufufuo wakiwa huko. (Mwanzo 25:17; Hesabu 20:23-29) Musa pia alienda katika Sheoli, ingawa hakuna mtu aliyejua mahali kaburi lake lilipokuwa. (Hesabu 27:13; Kumbukumbu la Torati 34:5, 6) Vivyo hivyo, Yoshua, ambaye alikuwa kiongozi wa Waisraeli baada ya Musa, pamoja na kizazi kizima cha watu, walienda katika Sheoli walipokufa.—Waamuzi 2:8-10.
9. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba neno la Kiebrania “Sheoli” na neno la Kigiriki “Hadesi” hurejelea mahali palepale? (b) Kuna tazamio gani kwa wale walio katika Sheoli, au Hadesi?
9 Karne kadhaa baadaye, Daudi akawa mfalme wa makabila 12 ya Israeli. Alipokufa, ‘alilala na mababu zake.’ (1 Wafalme 2:10) Je, yeye pia alikuwa katika Sheoli? Katika siku ya Pentekoste 33 W.K., mtume Petro alitaja kifo cha Daudi na kunukuu andiko la Zaburi 16:10, linalosema: “Hutaiacha nafsi yangu katika [Sheoli].” Baada ya kutaja kwamba Daudi bado alikuwa katika kaburi lake, Petro alitumia maneno hayohayo kumhusu Yesu, naye akasema kwamba Daudi “aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika [“Hadesi,” maelezo ya chini] wala mwili wake haukuona uharibifu. Yesu huyo Mungu alimfufua, uhakika ambao sisi sote ni mashahidi.” (Matendo 2:29-32) Hapa Petro alitumia neno la Kigiriki “Hadesi,” ambalo lina maana sawa na neno la Kiebrania “Sheoli.” Hivyo, hali ya wale wanaosemwa kwamba wako katika Hadesi ni sawa na ya wale wanaosemwa kwamba wako katika Sheoli. Wanalala huku wakingojea ufufuo.
Je, Kuna Watu Wasio Waadilifu Katika Sheoli?
10, 11. Kwa nini tunaweza kusema kwamba watu fulani wasio waadilifu huenda katika Sheoli, au Hadesi, wanapokufa?
10 Baada ya Musa kuliongoza taifa la Israeli kutoka Misri, kulitokea uasi nyikani. Musa aliwaambia watu wajitenge na Kora, Dathani, na Abiramu, viongozi wa uasi huo. Watu hao wangekufa ghafula na kwa uchungu mwingi. Musa alieleza: “Ikiwa watu hawa watakufa kifo cha wanadamu wote na kwamba adhabu iletwe juu yao kulingana na adhabu ya wanadamu wote, basi si Yehova aliyenituma mimi. Lakini ikiwa ni kitu fulani kilichoumbwa ambacho Yehova ataumba, nayo nchi ifungue kinywa chake na kuwameza na kila kitu kilicho chao, nao washuke chini wakiwa hai mpaka katika [Sheoli], ndipo hakika mtajua kwamba watu hawa wamemtendea Yehova bila heshima.” (Hesabu 16:29, 30) Hivyo, wawe walimezwa na dunia iliyofunguka au wawe waliteketezwa kwa moto, kama ilivyokuwa katika kisa cha Kora na Walawi 250 waliomuunga mkono, waasi hao wote walienda katika Sheoli, au Hadesi.—Hesabu 26:10.
11 Shimei, ambaye alimlaani Mfalme Daudi, aliadhibiwa na Sulemani aliyekuwa Mfalme baada ya Daudi. Daudi aliamuru: “Usimwache bila adhabu, kwa maana wewe ni mtu mwenye hekima na unajua vema jinsi unavyopaswa kumtendea, nawe lazima ushushe katika [Sheoli] mvi zake kwa damu.” Sulemani alimwagiza Benaya atekeleze hukumu hiyo. (1 Wafalme 2:8, 9, 44-46) Mtu mwingine aliyeuawa na Benaya ni Yoabu, aliyekuwa mkuu wa jeshi la Israeli. Mvi zake ‘hazikushuka kwa amani katika Sheoli.’ (1 Wafalme 2:5, 6, 28-34) Mifano hiyo miwili inaonyesha kwamba wimbo ambao Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuimba ni wa kweli: “Watu waovu watarudi katika [Sheoli], naam, mataifa yote yanayomsahau Mungu.”—Zaburi 9:17.
12. Ahithofeli alikuwa nani, naye alienda wapi alipokufa?
12 Ahithofeli alikuwa mshauri wa kibinafsi wa Daudi. Shauri lake lilionwa kuwa muhimu, kana kwamba lilitoka kwa Yehova mwenyewe. (2 Samweli 16:23) Kwa kusikitisha, mtumishi huyo mwenye kutegemewa alimsaliti Daudi na alihusika katika mapinduzi yaliyoongozwa na Absalomu, mwana wa Daudi. Yaonekana Daudi aliurejelea usaliti huo alipoandika: “Sikushutumiwa na adui; kama ndivyo ningaliweza kuvumilia hilo. Si mtu anayenichukia vikali aliyejivuna sana dhidi yangu; kama ndivyo ningaliweza kujificha kutoka kwake.” Daudi aliongeza: “Ukiwa na uwe juu yao! Na washuke katika [Sheoli] wakiwa hai; kwa maana wakati wao wa kukaa ugenini mambo mabaya yamekuwa ndani yao.” (Zaburi 55:12-15) Walipokufa, Ahithofeli na wenzake walienda katika Sheoli.
Ni Nani Walio Katika Gehena?
13. Kwa nini Yuda anaitwa “mwana wa maangamizi”?
13 Linganisha hali ya Daudi na ile iliyompata Daudi Mkuu, Yesu. Kama Ahithofeli, Yuda Iskariote, mmoja kati ya mitume 12 wa Kristo, alibadilika akawa msaliti. Usaliti wake ulikuwa mbaya kuliko ule wa Ahithofeli. Yuda alimsaliti Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Aliposali mwishoni mwa huduma yake duniani, Mwana wa Mungu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Nilipokuwa pamoja nao nilikuwa nikiwalinda kwa sababu ya jina lako ambalo umenipa; nami nimewatunza, na hata mmoja wao hakuangamizwa ila yule mwana wa maangamizi, ili andiko lipate kutimizwa.” (Yohana 17:12) Kwa kutaja kwamba Yuda alikuwa “mwana wa maangamizi,” Yesu alionyesha kwamba Yuda alipokufa, hakuwa na tumaini lolote la kufufuliwa. Hakubaki katika kumbukumbu ya Mungu. Hivyo, hakuenda katika Sheoli, bali alienda katika Gehena. Gehena ni nini?
14. Gehena inafananisha nini?
14 Yesu aliwashutumu viongozi wa dini wa siku zake kwa sababu walimfanya kila mmoja wa wanafunzi wao “astahili Gehena.” (Mathayo 23:15) Wakati huo, watu walilijua Bonde la Hinomu, lililotumiwa kama mahali pa kutupia takataka ambako pia watu walitupa miili ya wahalifu waliouawa ambao walionwa kuwa hawastahili mazishi yanayofaa. Awali, Yesu mwenyewe alikuwa ametaja Gehena katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 5:29, 30) Wasikilizaji wake walielewa maana ya mfano ya Gehena. Hiyo inafananisha kuharibiwa kabisa bila tumaini la ufufuo. Mbali na Yuda Iskariote wa siku za Yesu, je, kuna wengine ambao, baada ya kufa, wameenda katika Gehena badala ya kwenda katika Sheoli, au Hadesi?
15, 16. Ni nani walioenda katika Gehena walipokufa, na kwa nini walienda huko?
15 Wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, waliumbwa wakiwa wakamilifu. Walifanya dhambi kimakusudi. Wangeweza kuchagua uzima wa milele au kifo. Lakini wakamwasi Mungu na kumuunga mkono Shetani. Walipokufa, hawakuwa na tazamio lolote la kufaidika na dhabihu ya fidia ya Kristo. Hivyo, walienda katika Gehena.
16 Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu, alimuua ndugu yake Abeli na baadaye akawa mkimbizi. Mtume Yohana alimtaja Kaini kuwa mtu “aliyetokana na yule mwovu.” (1 Yohana 3:12) Ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Kaini alienda katika Gehena alipokufa, sawa na wazazi wake. (Mathayo 23:33, 35) Hali hiyo ni tofauti sana na ya Abeli mwadilifu. Paulo alieleza: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu, Mungu akitoa ushahidi kuhusu zawadi zake.” Kisha akaongeza: “Na kupitia hiyo yeye, ijapokuwa alikufa, bado anasema.” (Waebrania 11:4) Naam, kwa sasa Abeli yuko katika Sheoli akingojea ufufuo.
Ufufuo wa “Kwanza” na Ufufuo “Ulio Bora”
17. (a) Ni nani wanaoenda katika Sheoli ‘wakati huu wa mwisho’? (b) Kuna matazamio gani kwa wale walio katika Sheoli na wale walio katika Gehena?
17 Wengi watakaosoma makala hii watataka kujua kuhusu hali ya wale wanaokufa ‘wakati huu wa mwisho.’ (Danieli 8:19) Sura ya 6 ya kitabu cha Ufunuo inaeleza kuhusu wapanda-farasi wanne wanaoendesha farasi wakati huu. Mpanda-farasi wa mwisho anaitwa Kifo, naye anafuatwa na Hadesi. Hivyo, wengi wanaokufa mapema kwa sababu ya matukio na hali zinazofananishwa na wapanda-farasi wanaotangulia, wanaingia katika Hadesi. Huko wanangojea ufufuo katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufunuo 6:8) Hivyo basi, kuna matazamio gani kwa wale walio katika Sheoli (Hadesi) na wale walio katika Gehena? Kwa ufupi, kuna tazamio la ufufuo kwa wale walio katika Sheoli (Hadesi), lakini kwa wale walio katika Gehena kuna tazamio la uharibifu wa milele, yaani, kutokuwapo tena.
18. Wale wanaofufuliwa katika “ufufuo wa kwanza” wana tazamio gani?
18 Mtume Yohana aliandika: “Mwenye furaha na mtakatifu ni yeyote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; kifo cha pili hakina mamlaka juu ya hao, bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” Wale watakaotawala pamoja na Kristo wanafufuliwa katika “ufufuo wa kwanza.” Lakini wanadamu wengine wana tazamio gani?—Ufunuo 20:6.
19. Wengine hunufaikaje na “ufufuo ulio bora”?
19 Tangu siku za watumishi wa Mungu, Eliya na Elisha, muujiza wa ufufuo uliwawezesha watu kuwa hai tena. Paulo aliandika hivi: “Wanawake waliwapokea wafu wao kwa ufufuo; lakini watu wengine waliteswa kwa sababu hawakukubali kuachiliwa huru kupitia fidia fulani, ili waupate ufufuo ulio bora.” Naam, watu hao waaminifu waliodumisha utimilifu walitazamia ufufuo ambao ungewawezesha kuishi milele, wala si kuishi kwa miaka kadhaa kisha wafe tena! Kwa kweli, huo utakuwa “ufufuo ulio bora.”—Waebrania 11:35.
20. Makala inayofuata itazungumzia nini?
20 Iwapo tutakufa tukiwa waaminifu kabla ya Yehova kuangamiza mfumo huu mwovu, tuna tumaini hakika la kupata “ufufuo ulio bora,” katika maana ya kwamba tukifufuliwa tutakuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. Yesu aliahidi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Makala inayofuata itazungumzia zaidi kusudi la ufufuo. Itaonyesha jinsi ambavyo tumaini la ufufuo hutuimarisha ili kudumisha utimilifu wetu na kutusaidia kusitawisha roho ya kujitolea.
-
-
Tumaini la Ufufuo Linamaanisha Nini Kwako?Mnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
-
-
Tumaini la Ufufuo Linamaanisha Nini Kwako?
“Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” —Zaburi 145:16.
1-3. Wengine wana tumaini gani la wakati ujao? Eleza.
SIKU moja asubuhi, Christopher mwenye umri wa miaka tisa na ndugu yake, binamu zao wawili, pamoja na mjomba na shangazi yao, walienda kuhubiri nyumba kwa nyumba karibu na mji wa Manchester, huko Uingereza. Gazeti letu la Amkeni! linaeleza yaliyotukia. “Alasiri, walisafiri pamoja kwenda kutazama mandhari huko Blackpool, eneo la watalii lililo karibu na kwao. Wote 6 walikuwa kati ya watu 12 waliokufa papo hapo kwenye msiba wa barabarani, ambao ulifafanuliwa na polisi kuwa ‘maafa makubwa.’”
2 Usiku uliotangulia msiba huo, familia ya akina Christopher ilikuwa imehudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko, ambako kifo kilizungumziwa. Babake alisema: “Christopher alikuwa mvulana mwenye kutafakari sana. Usiku huo alizungumza waziwazi kuhusu ulimwengu mpya na tumaini lake la wakati ujao. Mazungumzo yalipokuwa yakiendelea, Christopher alisema hivi kwa ghafula: ‘Faida ya kuwa Shahidi wa Yehova ni kwamba ingawa kifo huumiza, tunajua kwamba siku moja tutaonana tena duniani.’ Hatukutambua kwamba maneno hayo yangetugusa moyo sana baadaye.”a
3 Katika mwaka wa 1940, Shahidi mmoja wa Austria anayeitwa Franz alijua kwamba angekatwa kichwa kwa sababu ya ushikamanifu wake kwa Yehova. Franz alimwandikia mamake hivi kutoka gerezani huko Berlin: “Kwa yale niliyojua, ikiwa ningalikula kiapo [cha kijeshi], ningalitenda dhambi inayostahili kifo. Huo ungekuwa uovu kwangu. Nisingepata ufufuo. . . . Na sasa, Mama yangu mpendwa na ndugu na dada zangu wote, leo niliambiwa hukumu yangu, na msiogopeshwe, ni kifo, nami nitauawa kesho asubuhi. Nina nguvu yangu kutoka kwa Mungu, sawa na ilivyokuwa sikuzote kwa Wakristo wote wa kweli huko nyuma. . . . Ikiwa mtasimama imara hadi kifo, tutaonana tena kwenye ufufuo. . . . Hadi tutakapoonana tena.”b
4. Unahisije baada ya kusoma visa vilivyosimuliwa hapa, na tutazungumzia nini?
4 Tumaini la ufufuo lilikuwa na maana kubwa kwa Christopher na Franz. Ufufuo ulikuwa halisi kwao. Bila shaka, masimulizi hayo yanatugusa moyo! Ili tuwe na uthamini mkubwa zaidi kwa Yehova na kuimarisha tumaini letu katika ufufuo, acheni tuone kwa nini kutakuwa na ufufuo na jinsi jambo hilo linavyoweza kumchochea kila mmoja wetu.
Maono Kuhusu Ufufuo wa Watakaoishi Duniani
5, 6. Maono ambayo mtume Yohana aliandika kwenye Ufunuo 20:12, 13 yanafunua nini?
5 Katika maono kuhusu mambo yatakayotukia wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo Yesu, mtume Yohana aliona ufufuo wa wale watakaoishi duniani. ‘Niliwaona wafu, wakubwa kwa wadogo,’ akasema. “Na bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na [Hadesi] vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake.” (Ufunuo 20:12, 13) Hata wawe wa cheo gani, wawe “wakubwa” au “wadogo,” wote ambao ni mateka katika Hadesi (Sheoli), yaani, kaburi, wataachiliwa. Pia wale waliofia baharini watakuwa hai tena wakati huo. Tukio hilo zuri ni sehemu ya kusudi la Yehova.
6 Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo utakapoanza, Shetani atafungwa na kutupwa katika abiso. Hakuna yeyote kati ya wale watakaofufuliwa au watakaookoka dhiki kuu atakayepotoshwa na Shetani wakati wa utawala huo, kwa kuwa hatakuwa anatenda. (Ufunuo 20:1-3) Huenda ukafikiri kwamba miaka elfu ni muda mrefu, lakini Yehova huiona “kama siku moja.”—2 Petro 3:8.
7. Hukumu itategemea nini wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo?
7 Kulingana na maono hayo, Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo utakuwa wakati wa hukumu. Mtume Yohana aliandika: ‘Niliwaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme, na vitabu vya kukunjwa vikafunguliwa. Lakini kitabu kingine cha kukunjwa kikafunguliwa; hicho ni kitabu cha uzima. Na wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao. Nao walihukumiwa kila mmoja kulingana na matendo yake.’ (Ufunuo 20:12, 13) Ona kwamba hukumu hiyo haitategemea mambo ambayo watu hao walitenda kabla ya kufa. (Waroma 6:7) Badala yake, inahusiana na “vitabu vya kukunjwa” vitakavyofunguliwa. Kuandikwa kwa jina la mtu katika “kitabu cha kukunjwa cha uzima” kutategemea jinsi atakavyotenda baada ya kujifunza mambo yaliyo katika vitabu hivyo.
“Ufufuo wa Uzima” au “Ufufuo wa Hukumu”
8. Wale watakaofufuliwa watapata mojawapo ya mambo gani mawili?
8 Mapema katika maono ya Yohana, Yesu anatajwa kuwa na “funguo za kifo na za [Hadesi].” (Ufunuo 1:18) Yeye ndiye ‘Wakili Mkuu wa Yehova wa uzima,’ ambaye amepewa mamlaka ya kuhukumu “walio hai na wafu.” (Matendo 3:15; 2 Timotheo 4:1) Atafanyaje hivyo? Kwa kuwafufua wale waliolala usingizi katika kifo. Yesu aliuambia hivi umati ambao aliuhubiria: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” Kisha akaongeza: “Wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28-30) Kwa hiyo, wanaume na wanawake waaminifu wa kale wana tazamio gani la wakati ujao?
9. (a) Wengi watajifunza nini baada ya kufufuliwa? (b) Ni kazi gani kubwa ya kuelimisha itakayoanza?
9 Wakati watu hao waaminifu wa kale watakapofufuliwa, watatambua upesi kwamba ahadi walizotumaini zimetimia. Watatamani sana kujua Uzao wa mwanamke wa Mungu anayetajwa katika unabii wa kwanza wa Biblia kwenye Mwanzo 3:15! Watafurahi kama nini kusikia kwamba Yesu, Masihi huyo aliyeahidiwa, alikuwa mwaminifu hadi kifo, na hivyo kutoa uhai wake ukiwa dhabihu ya fidia! (Mathayo 20:28) Wale watakaowakaribisha baada ya kufufuliwa watafurahia sana kuwasaidia waelewe kwamba fidia hiyo ni wonyesho wa rehema na fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Bila shaka, wale watakaofufuliwa watamsifu Yehova sana watakapotambua yale ambayo Ufalme wa Mungu unafanya ili kutimiza kusudi lake kuihusu dunia. Watakuwa na nafasi ya kutosha kuonyesha ushikamanifu wao kwa Baba yao mpendwa wa mbinguni na Mwana wake. Wakati huo, kila mtu atafurahia kazi kubwa ya kuwaelimisha mabilioni ya watu watakaofufuliwa, ambao pia watahitaji kukubali maandalizi ya Mungu ya fidia.
10, 11. (a) Ile Miaka Elfu itawaandalia nafasi gani wote watakaokuwa duniani? (b) Hilo linapaswa kutuchochea kufanya nini?
10 Abrahamu atakapofufuliwa atafarijiwa sana na jinsi maisha yatakavyokuwa katika utawala wa “jiji” alilotazamia. (Waebrania 11:10) Ayubu mwaminifu aliyeishi zamani atafurahi sana kujua kwamba maisha yake yaliwaimarisha watumishi wengine wa Yehova ambao utimilifu wao ulijaribiwa! Naye Danieli atatamani sana kujua ikiwa unabii ambao roho ya Mungu ilimwongoza kuandika ulitimia!
11 Naam, wote watakaopata uhai katika ulimwengu mpya wenye uadilifu, iwe ni kupitia ufufuo au kuokoka dhiki kuu, watajifunza mengi juu ya kusudi la Yehova kuihusu dunia na wakaaji wake. Bila shaka, tazamio la kuishi milele na kumsifu Yehova milele na milele litafanya programu ya elimu ya Miaka Elfu iwe yenye kufurahisha sana. Hata hivyo, jambo la maana zaidi ni matendo yetu binafsi baada ya kujifunza mambo yaliyo katika vitabu vya kukunjwa. Je, matendo yetu yatapatana na yale tutakayojifunza? Je, tutatafakari na kutenda kupatana na habari muhimu ambazo zitatuimarisha kushinda jaribu la mwisho la Shetani la kutukengeusha kutoka katika kweli?
12. Ni nini kitakachomsaidia kila mmoja kushiriki kikamili katika kazi ya kuwaelimisha watu na kuigeuza dunia kuwa paradiso?
12 Hatupaswi kupuuza baraka zitakazotokana na kutumia faida za dhabihu ya fidia ya Kristo. Wale watakaofufuliwa hawatakuwa na ulemavu au magonjwa yanayowapata watu leo. (Isaya 33:24) Kwa sababu watakuwa na mwili wenye afya na tazamio la kuwa na afya kamilifu, wakaaji wote wa ulimwengu mpya wataweza kushiriki kikamili katika kazi ya kuwaelimisha mabilioni ya watu watakaofufuliwa kuhusu njia ya uzima. Pia wakaaji hao watashiriki katika kazi kubwa zaidi kuwahi kufanywa duniani, yaani, kuigeuza dunia yote kuwa paradiso na kumletea Yehova sifa.
13, 14. Shetani ataachiliwa kwa kusudi gani wakati wa lile jaribu la mwisho, na huenda mtu mmoja-mmoja akapatwa na nini?
13 Shetani atakapoachiliwa kutoka katika abiso kwa ajili ya jaribu la mwisho, atajaribu kuwapotosha wanadamu tena. Kulingana na Ufunuo 20:7-9, mataifa yote au vikundi vya watu ‘watakaopotoshwa’ kwa kuvutwa na ushawishi mwovu wa Shetani, watahukumiwa uharibifu: ‘Moto utashuka kutoka mbinguni na kuwateketeza.’ Kwa habari ya wale watakaofufuliwa wakati wa kipindi cha ile Miaka Elfu, uharibifu huo utafanya ufufuo wao uwe wa hukumu. Tofauti na hao, wale watakaodumisha utimilifu baada ya ufufuo watapokea zawadi ya uzima wa milele. Kwa kweli, ufufuo wao utakuwa “ufufuo wa uzima.”—Yohana 5:29.
14 Tumaini la ufufuo linawezaje kutufariji hata sasa? Naam, tunapaswa kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tutanufaika na ufufuo wakati ujao?
Mambo ya Kutilia Maanani Sasa
15. Imani katika ufufuo inawezaje kutusaidia sasa?
15 Huenda umefiwa na mpendwa wako hivi majuzi, na huenda unakabiliana na mabadiliko makubwa yanayosababishwa na hali hiyo. Tumaini la ufufuo linakusaidia kupata amani ya akili na nguvu ambazo wale wasiojua kweli hawapati. Paulo aliwafariji hivi Wathesalonike: “Hatutaki mkose kujua kuhusu wale walalao usingizi katika kifo; ili msiwe na huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.” (1 Wathesalonike 4:13) Je, unajiona ukiwa katika ulimwengu mpya, ukishuhudia ufufuo? Pata faraja sasa kwa kutafakari juu ya tazamio la kukutana tena na wapendwa wako.
16. Huenda utahisije ufufuo utakapotokea?
16 Huenda kwa sasa wewe ni mgonjwa kwa sababu ya matokeo ya kuasi kwa Adamu. Usiruhusu huzuni inayotokana na hali hiyo ikufanye usahau tazamio lenye kufurahisha la kufufuliwa na kuishi tena ukiwa na afya nzuri na nguvu katika ulimwengu mpya. Bila shaka, utakapofungua macho na kuona watu wenye furaha na hamu ya kushangilia pamoja nawe ufufuo wako, utamshukuru Mungu kwa fadhili zake zenye upendo.
17, 18. Ni mambo gani mawili tunayopaswa kutilia maanani?
17 Kwa sasa, fikiria mambo mawili ambayo tunapaswa kutilia maanani. Jambo la kwanza ni umuhimu wa kumtumikia Yehova kwa nafsi yote sasa. Kwa kumwiga Bwana wetu, Kristo Yesu, maisha yetu ya kujitolea huonyesha tunampenda Yehova na jirani zetu. Upinzani au mateso yakitukosesha riziki au uhuru, sisi huazimia kuendelea kuwa na imani thabiti hata tupatwe na majaribu ya aina gani. Wapinzani wakitisha kutuua, tumaini la ufufuo hutufariji na kutuimarisha kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na Ufalme wake. Naam, kuhubiri na kufanya wanafunzi kwa bidii hutupa tazamio la kupata baraka za milele ambazo Yehova atawapa waadilifu.
18 Jambo la pili linahusiana na jinsi tunavyoweza kukabili majaribu yanayosababishwa na mwili wenye dhambi. Kujua tumaini la ufufuo na kuthamini fadhili zisizostahiliwa za Yehova huimarisha azimio letu la kudumisha imani thabiti. Mtume Yohana alionya: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Vitu vya kimwili ambavyo ulimwengu hutumia kutushawishi havitakuwa vyenye kuvutia sana tunapovilinganisha na “uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:17-19) Tukishawishiwa kufanya jambo fulani chafu kiadili, tutakataa katakata. Tunajua kwamba tukiendelea kufanya mambo yasiyompendeza Yehova kisha tufe kabla ya Har–Magedoni, tunaweza kupoteza tazamio la ufufuo.
19. Ni pendeleo gani kubwa tusilopaswa kupuuza?
19 Zaidi ya yote, hatupaswi kupuuza pendeleo kubwa sana la kuufanya moyo wa Yehova ushangilie, sasa na milele. (Methali 27:11) Uaminifu wetu hadi kifo au kudumisha utimilifu wetu hadi mwisho wa mfumo huu mwovu humwonyesha Yehova tuko upande gani kuhusiana na suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Itakuwa shangwe iliyoje kuishi katika dunia Paradiso kwa kuokoka dhiki kuu au kupitia muujiza wa ufufuo!
Kutosheleza Tamaa Zetu
20, 21. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa waaminifu hata ingawa kuna maswali ambayo hayajajibiwa kuhusu ufufuo? Eleza.
20 Mazungumzo yetu kuhusu ufufuo hayakujibu maswali yote. Yehova anakusudia nini kwa ajili ya wale waliokuwa wameoana kabla ya kufa? (Luka 20:34, 35) Je, ufufuo utatukia mahali ambapo watu walifia? Je, watafufuliwa karibu na mahali ambapo watu wa familia zao wanaishi? Kuna maswali mengi ambayo hayajajibiwa kuhusu mambo yanayohusiana na ufufuo. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka maneno haya ya Yeremia: “Yehova ni mwema kwa yule anayemtumaini, kwa nafsi inayoendelea kumtafuta. Ni jambo jema kwa mtu kuungojea, ndiyo, kimyakimya, wokovu wa Yehova.” (Maombolezo 3:25, 26) Katika wakati wa Yehova unaofaa, maswali yetu yote yatajibiwa kwa njia yenye kuridhisha kabisa. Kwa nini tuna uhakika kuhusu jambo hilo?
21 Tafakari maneno ya mtunga-zaburi yaliyoongozwa na roho ya Mungu alipoimba hivi kumhusu Yehova: “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zaburi 145:16) Umri unapozidi kusonga, mapendezi yetu hubadilika. Hatutamani tena mambo tuliyoyapenda tulipokuwa watoto. Maoni yetu kuhusu maisha huathiriwa na matumaini yetu na pia mambo yanayotupata. Hata hivyo, katika ulimwengu mpya, bila shaka Yehova atatosheleza tamaa zetu zote zinazofaa.
22. Kwa nini tuna sababu nzuri ya kumsifu Yehova?
22 Jambo la maana sasa ni kwamba kila mmoja wetu awe mwaminifu. “Kinachoangaliwa katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.” (1 Wakorintho 4:2) Sisi ni wasimamizi-nyumba wa habari njema tukufu za Ufalme wa Mungu. Bidii yetu ya kuwahubiria habari njema wote tunaokutana nao hutusaidia kudumu katika barabara inayoelekea kwenye uzima wa milele. Usisahau kamwe kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11) Ili kukabiliana na wasiwasi wowote usio wa lazima unaosababishwa na kuhangaikia mambo yanayoweza kutokea maishani, dumisha imani yenye nguvu katika tumaini tukufu la ufufuo. Hata kama inaonekana kwamba utakufa kabla ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo kuanza, unaweza kufarijiwa na uhakika wa kwamba kitulizo kitakuja. Katika wakati wa Yehova unaofaa, utaweza kurudia maneno haya ya Ayubu, ambayo alimwambia Muumba: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.” Na tumsifu Yehova, ambaye hutamani kuwafufua wale wote walio katika kumbukumbu yake!—Ayubu 14:15.
[Maelezo ya Chini]
a Ona gazeti la Amkeni! la Julai 8, 1988, ukurasa wa 10, (la Kiingereza au Kifaransa) lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 662, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-