-
Jiji Kubwa LateketezwaUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 36
Jiji Kubwa Lateketezwa
Njozi ya 12—Ufunuo 18:1–19:10
Habari: Anguko na uharibifu wa Babuloni Mkubwa; ndoa ya Mwana-Kondoo yatangazwa
Wakati wa utimizo: Kutoka 1919 mpaka baada ya ile dhiki kubwa
1. Ni nini kitakachotia alama mwanzo wa dhiki kubwa?
CHA GHAFULA, chenye kugutusha, chenye kuteketeza—ndivyo kitakuwa kifo cha Babuloni Mkubwa! Kitakuwa mojapo matukio yenye msiba mkuu zaidi sana katika historia yote, kikifanyiza mwanzo wa “dhiki kubwa kama ambayo haijapata kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.”—Mathayo 24:21, NW.
2. Ingawa milki za kisiasa zimeinuka na zikaanguka, ni milki ya aina gani ambayo imedumu?
2 Dini bandia imekuwapo kwa muda mrefu. Imekuwapo bila kikomo tangu siku za Nimrodi mwenye kiu cha damu ambaye alipinga Yehova na akaanzisha watu kujenga Mnara wa Babeli. Yehova alipovuruga ndimi za waasi hao na kuwatawanya juu ya dunia, dini bandia ya Babuloni ilienda pamoja nao. (Mwanzo 10:8-10; 11:4-9) Tangu hapo, milki za kisiasa zimeinuka na zikaanguka, lakini dini ya Kibabuloni imedumu. Imechukua sura na maumbo mengi, ikiwa milki ya ulimwengu ya dini bandia, Babuloni Mkubwa aliyetolewa unabii. Sehemu yake yenye kutokeza zaidi sana ni Jumuiya ya Wakristo, ambayo ilikua kutokana na mchanganyo wa mafundisho ya Kibabuloni ya mapema zaidi na mafundisho ya “Ukristo” ulioasi imani. Kwa sababu ya historia ndefu, ndefu mno ya Babuloni Mkubwa, watu wengi wanaliona kuwa jambo gumu kuitikadi kwamba itaangamizwa wakati wowote.
3. Ufunuo unathibitishaje hukumu ya maangamizi ya dini bandia?
3 Kwa hiyo inafaa kwamba yaupasa Ufunuo uthibitishe hukumu ya uangamivu wa dini bandia kwa kutupatia maelezo mawili yenye mambo mengi ya kuanguka kwake na matukio yanayofuata yakiongoza kwenye kufanywa ukiwa wake mkubwa. Sisi tumekwisha kumwona yeye akiwa ndiye “kahaba mkubwa” ambaye mwishowe anateketezwa na wale ambao hapo zamani walikuwa wapenzi wake wa milki ya kisiasa. (Ufunuo 17:1, 15, 16, NW) Sasa, katika njozi nyingine bado, sisi tutamwona akiwa jiji, kifananisho cha kidini cha Babuloni wa kale.
Babuloni Mkubwa Aanguka
4. (a) Yohana anafuata kuona njozi gani? (b) Sisi tunaweza kumtambuaje malaika, na ni kwa nini inamfaa yeye atangaze anguko la Babuloni Mkubwa?
4 Yohana aendelea na simulizi, akituambia: “Baada ya vitu hivi mimi nikaona malaika mwingine akishuka kutoka katika mbingu, akiwa na mamlaka kubwa; na dunia ilinururishwa kutokana na utukufu wake. Na yeye akalia kwa sauti imara, kusema: ‘Yeye ameanguka! Babuloni Mkubwa ameanguka.’” (Ufunuo 18:1, 2a, NW) Hii ni mara ya pili kwa Yohana kusikia tangazo hilo la kimalaika. (Ona Ufunuo 14:8.) Hata hivyo, wakati huu umaana walo umekaziwa na utukufu wa huyo malaika wa kimbingu, kwa kuwa utukufu wake unanururisha dunia kwa ujumla! Yeye anaweza kuwa nani? Karne nyingi mapema nabii Ezekieli, akiripoti juu ya njozi ya kimbingu, alitaarifu kwamba “dunia yenyewe iling’aa kwa sababu ya utukufu [wa Yehova].” (Ezekieli 43:2, NW) Malaika pekee wa kung’aa kwa utukufu unaolinganika na wa Yehova angekuwa Bwana Yesu, ambaye ni “ule mrudisho wa utukufu [wa Mungu] na uwakilisho barabara wa kuwako kwake kwenyewe.” (Waebrania 1:3, NW) Katika 1914, Yesu alipata kuwa Mfalme mbinguni, na tangu wakati huo amekuwa akitumia mamlaka juu ya dunia akiwa Mfalme na Hakimu mshirika wa Yehova. Inafaa, basi, kwamba imempasa yeye atangaze kuanguka kwa Babuloni Mkubwa.
5. (a) Malaika huyo anatumia nani kutoa habari ya anguko la Babuloni Mkubwa? (b) Hukumu ilipoanza juu ya wale wenye kudai kuwa “nyumba ya Mungu,” Jumuiya ya Wakristo ilikuwa hali gani?
5 Malaika huyu mwenye mamlaka kubwa anatumia nani katika kutoa habari kama hizo zenye kushangaza mbele ya aina ya binadamu? Kwani, ni wale watu wenyewe ambao wanaachiliwa likiwa tokeo la anguko hilo, wale wapakwa-mafuta wabakio duniani, jamii ya Yohana. Kutoka 1914 mpaka 1918, hao waliteseka sana mikononi mwa Babuloni Mkubwa, lakini katika 1918 Bwana Yehova na “mjumbe wa agano [la Kiabrahamu]” wake, Yesu Kristo, alianza hukumu pamoja na “nyumba ya Mungu,” wale wenye kudai kuwa Wakristo. Hivyo Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani ililetwa kwenye jaribio. (Malaki 3:1; 1 Petro 4:17, NW) Hatia ya damu yayo kubwa mno iliyopata wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, ushiriki wayo katika kunyanyasa mashahidi waaminifu wa Yehova, na itikadi zayo za Kibabuloni havikuisaidia katika wakati wa hukumu yayo; wala hapana sehemu nyingine yoyote ya Babuloni Mkubwa iliyostahili kibali cha Mungu.—Linga Isaya 13:1-9.
6. Inaweza kusemwaje kwamba Babuloni Mkubwa alikuwa ameanguka kufikia 1919?
6 Hivyo kufikia 1919 Babuloni Mkubwa alikuwa ameanguka, kufungulia njia watu wa Mungu waachiliwe na warudishwe, kana kwamba kwa siku moja, kwenye bara lao la ufanisi wa kiroho. (Isaya 66:8) Kufikia mwaka huo, Yehova Mungu na Yesu Kristo, Dario Mkubwa Zaidi na Sairasi Mkubwa Zaidi, walikuwa wameongoza mambo kwa werevu ili kwamba dini bandia isiweze tena kuwashikilia watu wa Yehova. Haingeweza tena kuwazuia wasimtumikie Yehova na kujulisha kwa wote ambao yamkini kusikia kwamba Babuloni Mkubwa aliye kama kahaba amehukumiwa uangamivu na kwamba kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kumekaribia karibu.—Isaya 45:1-4; Danieli 5:30, 31.
7. (a) Ingawa Babuloni Mkubwa hakuharibiwa katika 1919, Yehova alimwonaje? (b) Babuloni Mkubwa alipoanguka katika 1919, tokeo lilikuwa nini kwa watu wa Yehova?
7 Ni kweli, Babuloni Mkubwa hakuangamizwa katika 1919—kama vile jiji la Babuloni la kale halikuangamizwa katika 539 K.W.K. wakati lilipoanguka mikononi mwa majeshi ya Sairasi Mwajemi. Lakini kwa maoni ya Yehova, tengenezo hilo lilikuwa limeanguka. Yeye alikuwa amepata hukumu mbaya ya kimahakama, akingojea kufishwa; kwa hiyo dini bandia haingeweza kushikilia tena watu wa Yehova katika utekwa. (Linga Luka 9:59, 60.) Hao waliachiliwa wakatumikie wakiwa mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu wa Bwana-Mkubwa wakitoa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Wao walikuwa wamepokea hukumu ya ‘Mmefanya vema’ nao walipewa utume wajishughulishe tena na kazi ya Yehova.—Mathayo 24:45-47; 25:21, 23; Matendo 1:8, NW.
8. Ni tukio gani ambalo mlinzi wa Isaya 21:8, 9 hupigia mbiu, na ni nani leo anayetolewa kivuli na mlinzi huyo?
8 Mileani nyingi zilizopita Yehova alitumia manabii wengine watabiri tukio hili kubwa lenye kuanzisha muda maalumu. Isaya alisema juu ya mlinzi ambaye “aliendelea kuita kwa sauti kubwa kama simba: ‘Juu ya mnara wa lindo, O Yehova, mimi ninasimama daima mchana, na kwenye kilindio changu mimi nimewekwa mausiku yote.’” Na ni tukio gani analotambua mlinzi huyo na kupiga mbiu kwa ujasiri kama wa simba? Hili: “Yeye ameanguka! Babuloni ameanguka, na mifano yote ya kuchongwa ya miungu yake [Yehova] amevunja hadi kwenye dunia!” (Isaya 21:8, 9, NW) Mlinzi huyu anatolea kivuli vizuri jamii ya Yohana leo ambayo ni yenye kuamka kabisa, inapotumia gazeti Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya kitheokrasi kuvumisha kotekote habari za kwamba Babuloni ameanguka.
Mshuko wa Babuloni Mkubwa
9, 10. (a) Uvutano wa dini ya Kibabuloni umepatwa na mpunguo gani tangu Vita ya Ulimwengu 1? (b) Malaika mwenye nguvu anaelezaje hali ya kuanguka ya Babuloni Mkubwa?
9 Anguko la Babuloni wa kale katika 539 K.W.K. lilikuwa mwanzo wa mshuko mrefu ambao ulimalizikia katika ukiwa wake. Hali kadhalika, tangu vita ya kwanza ya ulimwengu, uvutano wa dini ya Kibabuloni umeshuka sana kwa kadiri ya tufe lote. Kufuata vita ya ulimwengu ya pili, ibada ya Shinto ya maliki ilikatazwa katika Japani. Katika China, serikali ya Kikomunisti hudhibiti uwekwaji rasmi na utendaji wote wa kidini. Katika Ulaya kaskazini ya Kiprotestanti, watu walio wengi wamekuwa wasiopendezwa na dini. Na hivi majuzi Kanisa Katoliki la Roma limedhoofishwa na mifarakano na kutopatana kwa ndani katika milki yalo ya tufe lote.—Linga Marko 3:24-26.
10 Pasipo shaka miendo hii yote ni sehemu ya ‘kukauka kwa mto Eufrati’ katika kutayarishia shambulio linalokuja la kivita juu ya Babuloni Mkubwa. ‘Kukauka’ huku kunaonyeshwa, vilevile, katika tangazo la papa la Oktoba 1986 kwamba lazima kanisa ‘liwe mwomba-ombaji tena’—kwa sababu ya upungufu mkubwa mno. (Ufunuo 16:12) Hususa tangu 1919 Babuloni Mkubwa amekuwa akifichuliwa atazamwe na wote kuwa yeye ni bara-tupu la kiroho, kama malaika mwenye nguvu anavyotangaza hapa: “Na yeye amekuwa mahali pa kukaa roho waovu na mahali pa kujibanza kila pumzi isiyo safi na mahali pa kujibanza kila ndege asiye safi na mwenye kuchukiwa!” (Ufunuo 18:2b, NW) Karibuni atakuwa bara-tupu kama hilo kihalisi, akiwa ukiwa kama magofu ya Babuloni katika Iraki ya leo.—Ona pia Yeremia 50:25-28.
11. Ni katika maana gani Babuloni Mkubwa amekuwa “mahali pa kukaa roho waovu” na ‘mahali pa kujibanza pumzi zisizo safi na pa ndege wasio safi’?
11 Neno “roho waovu” hapa inaelekea ni mrudisho wa neno “roho waovu wenye umbo-mbuzi” (se‘i·rimʹ) linalopatikana katika elezo la Isaya kuhusu Babuloni aliyeanguka: “Na huko mizuka ya mikoa isiyo na maji kwa hakika italala chini, na nyumba zayo lazima zijawe na tai-bundi. Na huko mbuni lazima wakae, na roho waovu wenye umbo-mbuzi wenyewe wataenda wakirukaruka huko.” (Isaya 13:21, NW) Huenda isirejezee roho waovu halisi bali wanyama wakaa-jangwani wenye nywele za matimutimu ambao mwonekano wao ulifanya watazamaji wafikirie roho waovu. Katika magofu ya Babuloni Mkubwa, kuwako kitamathali kwa wanyama kama hao, pamoja na hewa tuli (“pumzi isiyo safi”) yenye sumu, na ndege wasio safi, huashiria hali yake ya kiroho iliyokufa. Yeye hatolei aina ya binadamu mataraja yoyote ya uhai.—Linga Waefeso 2:1, 2.
12. Hali ya Babuloni Mkubwa hulandaje unabii wa Yeremia katika sura ya 50?
12 Hali yake hulanda pia unabii wa Yeremia: “‘Kuna upanga dhidi ya Wakaldayo,’ ni tamko la Yehova, ‘na dhidi ya wakaaji wa Babuloni na dhidi ya wana-wafalme wake na dhidi ya wenye hekima wake. . . . Kuna mteketezo juu ya maji yake, na ni lazima yakaushwe kabisa. Kwa maana ni bara la mifano ya kuchongwa, na kwa sababu ya njozi zao zenye kujaa kikuli wao huendelea kutenda kikichaa. Kwa hiyo mizuka ya mikoa isiyo na maji itakaa pamoja na wanyama wenye kulia, na ndani yake yeye lazima mbuni wakae; naye hatakaliwa tena kamwe milele, wala yeye hatakaa kizazi baada ya kizazi.’” Ibada ya sanamu na kuimbwa kwa sala za kurudiwarudiwa hakuwezi kumwokoa Babuloni Mkubwa asipatwe na lipo linaloshabihi kuangushwa kwa Sodoma na Gomora na Mungu.—Yeremia 50:35-40, NW.
Divai Yenye Kuamsha Harara
13. (a) Malaika mwenye nguvu avutaje uangalifu kwenye mweneo mpana wa ukahaba wa Babuloni Mkubwa? (b) Ni utovu wa adili gani ulioenea sana katika Babuloni wa kale unaopatikana pia katika Babuloni Mkubwa?
13 Kisha malaika mwenye nguvu anaelekeza uangalifu kwenye mweneo mpana wa ukahaba wa Babuloni Mkubwa, akipiga mbiu hivi: “Kwa sababu ya divai yenye kuamsha harara ya uasheratia wake mataifa yote yameanguka yakiwa majeruhi, na wafalme wa dunia walifanya uasherati na yeye, na wauza-bidhaa wasafiri wa dunia wakawa na utajiri kwa sababu ya nguvu za anasa yake isiyo ya aibu.” (Ufunuo 18:3, NW) Yeye amefundisha mataifa yote ya aina ya binadamu katika njia zake zisizo safi za kidini. Katika Babuloni wa kale, kulingana na mwanahistoria Herodoto, kila mwanamwali alitakwa aufanyize uasherati ubikira wake katika ibada ya hekalu. Kufikia leo hii ufisadi wa kingono wenye kukirihisha unaonyeshwa kitaswira katika sanamu-choro zilizoharibiwa na vita kwenye Angkor Wat katika Kampuchea na katika mahekalu katika Khajuraho, India, ambazo huonyesha mungu wa Kihindu Vishnu akizungukwa na mandhari za kimahaba zenye kunyarafisha. Katika United States, mafumbuo ya utovu wa adili ambayo yalitetemesha ulimwengu wa waevanjeli wa TV katika 1987, na tena katika 1988, pamoja na ufunuo wa zoea lenye kuenea pote la ugoni-jinsia-moja wa wahudumu wa kidini, hutoa kielezi kwamba hata Jumuiya ya Wakristo huvumilia mazidio yenye kugutusha ya uasherati halisi. Hata hivyo, mataifa yote yamekuwa majeruhi ya aina ya uasherati mbaya hata zaidi.
14-16. (a) Ni uhusiano gani usio halali wa dini-siasa uliotukia katika Italia ya Ufashisti? (b) Wakati Italia ilipovamia Abisinia, ni taarifa gani walizotoa maaskofu wa Kanisa Katoliki la Roma?
14 Sisi tumekwisha pitia uhusiano haramu wa dini-siasa uliomweka Hitla katika mamlaka katika Ujeremani ya Nazi. Mataifa mengine pia yalitaabika kwa sababu ya dini kujidukiza katika mambo ya kiserikali. Mathalani, Katika Italia ya Ufashisti, katika Februari 11, 1929, Mwafaka wa Laterani ulitiwa sahihi na Mussolini na Kardinali Gasparri, ukifanya Jiji la Vatikani kuwa dola lenye enzi. Papa Pius 11 alidai kwamba yeye alikuwa ‘ameirudisha Italia kwa Mungu, na Mungu akamrudisha kwa Italia.’ Je! huo ulikuwa ni ukweli? Fikiria yaliyotokea miaka sita baadaye. Katika Oktoba 3, 1935, Italia ilivamia Abisinia, ikidai kwamba lilikuwa “bara la kishenzi ambalo lilikuwa lingali linazoea utumwa.” Ni nani, kwa kweli, aliyekuwa wa kishenzi? Je! Kanisa Katoliki lililaumu vikali ushenzi wa Mussolini? Ingawa papa alitoa taarifa zisizoeleweka, maaskofu wake walisema wazi kabisa katika kubariki majeshi yenye silaha ya Italia “bara-baba” lao. Katika kitabu The Vatican in the Age of the Dictators, Anthony Rhodes huripoti hivi:
15 “Katika Barua ya Uchungaji yake ya Oktoba 19 [1935], Askofu wa Udine [Italia] aliandika, ‘Si la wakati unaofaa wala lenye kufaa kwa sisi kutamka yanayofaa na yasiyofaa ya kisa hiki. Wajibu wetu tukiwa Waitalia, na hata hivyo zaidi tukiwa Wakristo ni kuchangia fanikio la silaha zetu.’ Askofu wa Padua aliandika katika Oktoba 21, ‘katika hizi saa ngumu ambazo sisi tunazipitia, sisi tunawaomba nyinyi mwe na imani katika watawala wetu na majeshi yenye silaha.’ Oktoba 24, Askofu wa Kremona aliweka wakfu bendera kadhaa za kijeshi na akasema: ‘Baraka ya Mungu na iwe juu ya askari-jeshi hawa ambao, juu ya udongo wa Kiafrika, watashinda mabara mapya na yenye rutuba kwa ajili ya ubunifu wa Italia, na hivyo kuwaletea utamaduni wa Kiroma na Kikristo. Italia na isimame kwa mara nyingine tena ikiwa mshauri wa ulimwengu kwa ujumla.’”
16 Abisinia ikatwaliwa kinguvu, kwa baraka ya makasisi wa Katoliki ya Roma. Je! yeyote wa hawa angeweza kudai, katika maana yoyote, kwamba wao walikuwa kama mtume Paulo katika kuwa ‘bila hatia ya damu ya watu wote’?
17. Hispania ilitesekaje kwa sababu ya viongozi wa kidini wayo kushindwa ‘kufua panga zao ziwe majembe ya plau’?
17 Ongezea Ujeremani, Italia, na Abisinia taifa jingine ambalo limekuwa jeruhi kwa uasherati wa Babuloni Mkubwa—Hispania. Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe ya 1936-39 katika bara hilo, kwa sehemu, ilianzishwa kwa sababu ya serikali ya kidemokrasi kuchukua hatua ya kupunguza nguvu kubwa mno za Kanisa Katoliki la Roma. Vita hiyo ilipoanza, Franko, kiongozi Mfashisti Mkatoliki wa majeshi ya Kimapinduzi, alijieleza mwenyewe kuwa “Jenerali Mkuu wa Kikristo wa Krusedi Takatifu,” jina la cheo ambalo baadaye aliacha. Mamia ya maelfu kadhaa ya Wahispania walikufa katika kupigana. Mbali na hilo, kulingana na kadirio dogo, Wateteaji wa Taifa wa Franko walikuwa wameua kimakusudi wanachama 40,000 wa Popular Front, hali hao wa pili nao walikuwa wameua kimakusudi makasisi—watawa wa kiume, mapadri, watawa wa kike, na makasisi wapya 8,000. Hilo ndilo ogofyo na msiba wa vita ya wenyewe kwa wenyewe, ikionyesha hekima ya kutii maneno haya ya Yesu: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote ambao huchukua upanga watapotelea mbali kwa upanga.” (Mathayo 26:52, NW) Ni jambo lenye kunyarafisha kama nini kwamba Jumuiya ya Wakristo hujiingiza katika umwagaji-damu mkubwa hivyo! Kweli kweli viongozi wayo wa kidini wameshindwa kabisa kabisa ‘kufua panga zao ziwe majembe ya plau’!—Isaya 2:4, NW.
Wauza-Bidhaa Wasafiri
18. Ni nani walio “wauza-bidhaa wasafiri wa dunia”?
18 Ni nani walio “wauza-bidhaa wasafiri wa dunia”? Pasipo shaka sisi tungewaita leo wachuuzi, wanabiashara wakubwa-wakubwa, walanguzi chapuchapu na biashara kubwa-kubwa. Hii si kusema kwamba ni kosa kufanya biashara halali. Biblia huandaa shauri la hekima kwa watu wa biashara, ikiwaonya dhidi ya utovu wa haki, pupa, na kadhalika. (Mithali 11:1; Zekaria 7:9, 10; Yakobo 5:1-5) Pato lililo kubwa zaidi ni “kujitoa kwa ajili ya Mungu pamoja na ujitoshelevu.” (1 Timotheo 6:6, 17-19, NW) Hata hivyo, ulimwengu wa Shetani haufuati kanuni za uadilifu. Ufisadi ni tele. Unapatikana katika dini, katika siasa—na katika biashara kubwa-kubwa. Wakati kwa wakati vyombo vya habari hufichua kashifa, kama vile maofisa wa serikali wa vyeo vya juu kutumia vibaya mali ya serikali na kuuza silaha kimagendo.
19. Ni mambo hakika gani ya uchumi wa ulimwengu husaidia kueleza sababu kwa nini wauza-bidhaa wasafiri wa dunia hupata mtajo usiopendeleka katika Ufunuo?
19 Uchuuzi wa kimataifa wa silaha unapanda juu sana kupita dola 1,000,000,000,000 kila mwaka, huku mamia ya mamilioni ya wanadamu wakinyimwa lazima za maisha. Hilo ni baya vya kutosha. Lakini silaha huonekana kuwa tegemezo la msingi la uchumi wa ulimwengu. Katika Aprili 11, 1987, makala moja katika Spectator ya London iliripoti hivi? “Kuhesabu viwanda vinavyohusiana moja kwa moja, kazi 400,000 zinahusika katika U.S. na 750,000 katika Ulaya. Lakini ajabu ni kwamba, kadiri daraka la kijamii na kiuchumi la kuunda silaha linavyoongezeka, lile swali hasa la kama waundaji wanakingwa vizuri limesahauliwa.” Faida kubwa mno zinapatikana kadiri mabomu na silaha nyinginezo zinachuuzwa kotekote duniani, hata na kwa wanaoweza kuwa maadui. Siku moja huenda mabomu hayo yakarudi katika mteketeo wa moto kuwaharibu wale wanaoyauza. Ni kinyume kama nini! Ongezea hilo ulanguzi unaohusika katika biashara hii ya silaha. Katika United States pekee, kulingana na Spectator, “kila mwaka kwa njia isiyoelezeka Pentagoni hupoteza silaha na vifaa vya thamani ya dola milioni 900.” Si ajabu kwamba wauza-bidhaa wa dunia wanatajwa isivyopendeleka katika Ufunuo!
20. Ni kielelezo gani kinachoonyesha kujihusisha kwa dini katika mazoea yenye ufisadi ya shughuli za biashara?
20 Kama ilivyotabiriwa na malaika mwenye utukufu, dini imehusika sana katika mazoea yenye ufisadi ya biashara. Mathalani, kuna kujihusisha kwa Vatikani katika anguko la Banco Ambrosiano katika 1982. Kesi hiyo imejikokota muda wote wa miaka ya 1980, lile swali ambalo halijajibiwa likiwa: Fedha zilienda wapi? Katika Februari 1987 mahakimu wa Milani walitoa waranti ili makasisi watatu wa Vatikani wakamatwe, kutia na askofu mkuu mmoja Mwamerika, kwa mashtaka ya kwamba wao walikuwa washiriki kwenye ufilisi wenye udanganyifu, lakini Vatikani ilitupilia mbali ombi la kuwakabidhi wakahukumiwe. Katika Julai 1987, katikati ya makelele ya kuteta, zile waranti zilibatilishwa na Mahakama ya Rufani ya juu zaidi sana kwa msingi wa mwafaka wa zamani kati ya Vatikani na serikali ya Italia.
21. Sisi twajuaje kwamba Yesu hakuwa na uhusiano na mazoea ya kibiashara yenye kutilika mashaka ya siku yake, lakini sisi tunaona nini leo katika dini ya Kibabuloni?
21 Je! Yesu alijihusisha katika mazoea ya kibiashara yenye kutilika mashaka ya siku yake? La. Yeye hata hakuwa mwenye mali yoyote, kwa maana yeye alikuwa “hana mahali pa kulaza chini kichwa chake.” Mtawala mmoja kijana tajiri alishauriwa na Yesu hivi: “Uza vitu vyote ulivyo navyo na kugawia maskini, na wewe utakuwa na hazina katika mbingu; na uje uwe mfuasi wangu.” Hilo lilikuwa shauri jema, kwa maana lingaliweza kumwondolea mbali wasiwasi wote juu ya mambo ya kibiashara. (Luka 9:58; 18:22, NW) Kwa kutofautisha, dini ya Kibabuloni mara nyingi ina mafungamano mabaya na biashara kubwa-kubwa. Mathalani, katika 1987 Albany Times Union liliripoti kwamba msimamizi wa mambo ya kifedha wa akidayosisi ya Miami, Florida, U.S.A., alikubali kwamba kanisa lina hisa katika makampuni ambayo hufanyiza silaha za nyukilia, sinema zisizofaa, na sigareti.
“Ondokeni Katika Yeye, Watu Wangu”
22. (a) Sauti kutoka katika mbingu inasema nini? (b) Ni nini kilichoongoza kwenye mshangilio wa watu wa Mungu katika 537 K.W.K., na katika 1919?
22 Maneno yanayofuata ya Yohana yanaelekeza kwenye utimizo zaidi wa kigezo cha kiunabii: “Na mimi nikasikia sauti nyingine kutoka katika mbingu ikisema: ‘Ondokeni katika yeye, watu wangu, ikiwa nyinyi hamtaki kushiriki pamoja na yeye katika madhambi yake, na ikiwa nyinyi hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake.’” (Ufunuo 18:4, NW) Unabii wa anguko la Babuloni wa kale katika Maandiko ya Kiebrania unatia ndani pia amri ya Yehova kwa watu wake: “Kimbieni mtoke katikati ya Babuloni.” (Yeremia 50:8, 13, NW) Hali moja na hiyo, kwa sababu ya ukiwa unaokuja wa Babuloni Mkubwa, watu wa Mungu wanahimizwa sasa waponyoke. Katika 537 K.W.K. fursa ya kuponyoka kutoka Babuloni ilileta mshangilio mkubwa upande wa Waisraeli waaminifu. Katika njia iyo hiyo, kuachiliwa kwa watu wa Mungu kutoka utekwa wa Babuloni Mkubwa kuliongoza kwenye mshangilio upande wao. (Ufunuo 11:11, 12) Na tangu wakati huo mamilioni ya wengine yametii amri hiyo wakimbie.
23. Sauti kutoka katika mbingu inakaziaje umuhimu wa kukimbia kutoka katika Babuloni Mkubwa?
23 Je! ni jambo la muhimu kweli kweli kadiri hiyo kukimbia kutoka katika Babuloni Mkubwa, kujiondoa katika uanachama wa dini za ulimwengu na kujitenga kabisa? Ndivyo, kwa maana sisi tunahitaji kuchukua oni la Mungu juu ya dubwana hili la kale la kidini, Babuloni Mkubwa. Yeye hakuepa kumwita kahaba mkubwa. Kwa hiyo sasa sauti kutoka katika mbingu inamwarifu Yohana zaidi hivi kuhusu malaya huyu: “Kwa maana madhambi yake yametungamana pamoja moja kwa moja hadi kwenye mbingu, na Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki. Rudisha kwa yeye hata kama vile yeye mwenyewe alirudisha, na fanya kwa yeye mara mbili ya vile yeye alifanya, ndiyo, mara mbili ya hesabu ya alivyofanya; katika kikombe ambacho ndani yacho yeye aliweka mchanganyiko wekea yeye mara mbili ya mchanganyiko huo. Kwa kadiri ambayo yeye alijitukuza mwenyewe na akaishi katika anasa ya kutoona aibu, kwa kadiri hiyo mpe yeye teso na ombolezo. Kwa maana katika moyo wake yeye hufuliza kusema, ‘Mimi naketi nikiwa malkia, na mimi si mjane, na mimi sitaona kamwe ombolezo.’ Hiyo ndiyo sababu katika siku moja tauni zake zitakuja, kifo na ombolezo na njaa kuu, na yeye atachomwa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova Mungu, ambaye alihukumu yeye, ni imara sana.”—Ufunuo 18:5-8, NW.
24. (a) Ni lazima watu wa Mungu wakimbie kutoka Babuloni Mkubwa ili waepuke nini? (b) Wale wanaoshindwa kukimbia kutoka katika Babuloni Mkubwa wanashiriki naye madhambi gani?
24 Ni maneno yenye nguvu, hayo! Kwa hiyo tendo linatakwa. Yeremia alihimiza watu katika siku yake watende, akisema: “Kimbieni kutoka katikati ya Babuloni, . . . kwa maana ni wakati wa kisasi ambacho ni cha Yehova. Kuna tendeo ambalo yeye analipa kurudisha kwa yeye. Ondokeni katikati yake, O watu wangu, na kila mmoja aandalilie nafsi yake mponyoko kutoka kasirani yenye kuwaka ya Yehova.” (Yeremia 51:6, 45, NW) Katika njia kama hiyo, sauti kutoka katika mbingu inaonya watu wa Mungu leo wakimbie kutoka Babuloni Mkubwa ili wasipokee sehemu ya tauni zake. Hukumu za Yehova zilizo kama tauni juu ya ulimwengu huu, kutia na Babuloni Mkubwa, zinapigiwa mbiu sasa. (Ufunuo 8:1–9:21; 16:1-21) Watu wa Mungu wanahitaji kujitenga wenyewe na dini bandia ikiwa wao wenyewe hawataki kupatwa na tauni hizi na mwishowe kabisa wafe naye. Waaidha, kubaki ndani ya tengenezo hilo kungewafanya washiriki katika madhambi yake. Wao wangekuwa na hatia kama yeye ya uzinzi wa kiroho na ya kumwaga damu “ya wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.”—Ufunuo 18:24, NW; linga Waefeso 5:11; 1 Timotheo 5:22.
25. Ni katika njia zipi watu wa Mungu waliondoka katika Babuloni wa kale?
25 Ingawa hivyo, ni jinsi gani watu wa Mungu huondoka katika Babuloni Mkubwa? Katika kisa cha Babuloni wa kale, Wayahudi walikuwa sharti wafanye safari halisi kutoka katika jiji la Babuloni moja kwa moja hadi Bara la Ahadi. Lakini zaidi ya hilo lilihusika. Kiunabii Isaya aliambia Waisraeli hivi: “Geukeni mbali, geukeni mbali, ondokeni humo, msiguse kitu kisicho safi; ondokeni katikati yake, jitunzeni wenyewe safi, nyinyi ambao mnapeleka vyombo vya Yehova.” (Isaya 52:11, NW) Ndiyo, wao walipaswa waache mazoea yote yasiyo safi ya dini ya Kibabuloni ambayo yangeelekea kuitia kutu ibada yao kwa Yehova.
26. Wakristo Wakorintho walitiije maneno haya, ‘Ondokeni kutoka miongoni mwao na mwache kabisa kugusa kitu kisicho safi’?
26 Mtume Paulo alinukuu maneno ya Isaya katika barua yake kwa Wakorintho, akisema: “Msipate kuwa wenye kufungiwa nira isivyofaa pamoja na wasioitikadi. Kwa maana ni ushirika gani uadilifu unao pamoja na ukosefu wa kutii sheria? Au ni hisa gani nuru inayo pamoja na giza? . . . ‘Kwa hiyo ondokeni kutoka miongoni mwao, na kujitenga nyinyi wenyewe,’ asema Yehova, ‘Na acheni kabisa kugusa kitu kisicho safi.’” Haikuwa lazima Wakristo wa Korintho waache Korintho ili watii amri hiyo. Hata hivyo, wao walikuwa na lazima ya kuepuka kihalisi mahekalu yasiyo safi ya dini bandia, pamoja na kujitenga wenyewe kiroho na matendo yasiyo safi ya waabudu sanamu hao. Katika 1919 watu wa Mungu walianza kukimbia kutoka katika Babuloni Mkubwa kwa njia hiyo, wakijisafisha wenyewe mabaki yoyote ya mafundisho na mazoea yasiyo safi. Hivyo, waliweza kutumikia yeye wakiwa watu wake waliosafishwa.—2 Wakorintho 6:14-17, NW; 1 Yohana 3:3.
27. Ni milingano gani iliyopo kati ya hukumu juu ya Babuloni wa kale na juu ya Babuloni Mkubwa?
27 Anguko la Babuloni wa kale na ukiwa uliofuata lilikuwa adhabu kwa ajili ya madhambi yake. “Kwa maana moja kwa moja hukumu zake zimefika katika zile mbingu.” (Yeremia 51:9, NW) Hali moja na hiyo, madhambi ya Babuloni Mkubwa “yametungamana pamoja moja kwa moja hadi kwenye mbingu,” ili ziangaliwe na Yehova mwenyewe. Yeye ana hatia ya utovu wa haki, ibada ya sanamu, utovu wa adili, uonevu, unyakuzi, na uuaji kimakusudi. Anguko la Babuloni wa kale lilikuwa kwa sehemu, kisasi kwa yale ambayo lilikuwa limefanyia hekalu la Yehova na waabudu wa kweli wake. (Yeremia 50:8, 14; 51:11, 35, 36) Anguko la Babuloni Mkubwa na uharibifu wake utakaofuata hali moja na hiyo huonyesha kisasi kwa yale ambayo yeye amefanyia waabudu wa kweli katika muda wote wa karne zilizopita. Kweli kweli, uharibifu wake wa mwisho kabisa ni mwanzo wa “siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.”—Isaya 34:8-10; 61:2, NW; Yeremia 50:28.
28. Ni kiwango gani cha haki anachotumia Yehova kwa Babuloni Mkubwa, na kwa sababu gani?
28 Chini ya Sheria ya Musa, ikiwa Mwisraeli aliiba kutoka wananchi wenzake, alikuwa sharti alipe ili kurudisha angalau maradufu katika kufidia. (Kutoka 22:1, 4, 7, 9) Katika uharibifu unaokuja wa Babuloni Mkubwa, Yehova atatumia kiwango kinacholinganika na hicho cha haki. Yeye atapokea maradufu ya yale aliyotoa. Hakutakuwa na rehema kwa sababu Babuloni Mkubwa hakuonyesha rehema yoyote kwa majeruhi wake. Yeye alijilisha kidusia juu ya watu wa dunia ili kujidumisha mwenyewe katika “anasa ya kutoona aibu.” Sasa yeye atateseka na kuomboleza. Babuloni wa kale alihisi alikuwa katika hali ya usalama kabisa, akijigamba: “Mimi sitaketi kama mjane, na mimi sitajua hasara ya watoto.” (Isaya 47:8, 9, 11, NW) Babuloni Mkubwa huhisi yu salama. Lakini uharibifu wake, ulioamriwa na Yehova ambaye “ni imara sana,” utatukia chakachaka, kana kwamba “katika siku moja”!
[Maelezo ya Chini]
a New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
-
-
Jiji Kubwa LateketezwaUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 263]
“Wafalme . . . Walifanya Uasherati na Yeye”
Mapema katika miaka ya 1800 wauza-bidhaa wa Ulaya walikuwa wakiingiza kimagendo ndani ya China viasi vikubwa vya kasumba. Katika Machi 1839 maofisa Wachina walijaribu kukomesha uchuuzi huo usio halali kwa kukamata masanduku 20,000 ya dawa hiyo ya kulevya kutoka kwa wauza-bidhaa Waingereza. Hili liliongoza kwenye wasiwasi kati ya Uingereza na China. Mahusiano kati ya nchi hizo mbili yalipozorota, baadhi ya wamisionari Waprotestanti walihimiza Uingereza kwenda vitani, kwa taarifa kama hizi zifuatazo:
“Jinsi magumu haya yanavyoshangilisha moyo wangu kwa sababu mimi nafikiri huenda serikali ya Uingereza ikakasirishwa vikali, na Mungu, katika nguvu Zake huenda akavunjavunja migogoro inayozuia gospeli ya Kristo isiingie China.”—Henrietta Shuck, misionari wa Baptisti ya Kusini.
Hatimaye, vita ikafyatuka—vita ambayo leo hujulikana kuwa Vita ya Kasumba. Kwa moyo wote wamisionari walichochea Uingereza kwa maelezo kama haya:
“Mimi nalazimika kutazama nyuma juu ya hali ya sasa ya mambo sana sana si kuwa ni shauri la kasumba au la Uingereza, kuwa ndilo kusudi kubwa la Mwelekezo wa Kimungu ili kufanya uovu wa mwanadamu utii makusudi Yake ya rehema kuelekea China katika kupenya ukuta wayo wa kujitenga.”—Peter Parker, misionari Mkongrigeshonali.
Misionari mwingine Mkongrigeshonali, Samuel W. Williams, aliongeza hivi: “Mkono wa Mungu ni wazi katika yale yote ambayo yamefanyika kwa jinsi ya kutokeza, na sisi hatutii shaka kwamba Yeye ambaye alisema alikuja kuleta upanga juu ya dunia amekuja hapa na kwamba ni kwa ajili ya uharibifu mwepesi wa maadui Wake na kusimamishwa kwa ufalme Wake. Yeye atapindua na kupindua mpaka Yeye awe amemthibitisha Mwana-Mfalme wa Amani.”
Kwa mintarafu ya chinjo lenye kuogofya la wanataifa Wachina, misionari J. Lewis Shuck aliandika: “Mimi huona mandhari kama hizo . . . kuwa ala za Bwana za moja kwa moja katika kuondolea mbali takataka ambayo inazuia usongaji mbele wa Ukweli wa Kimungu.”
Misionari Mkongrigeshonali Elijah C. Bridgman aliongeza: “Mara nyingi Mungu ametumia mkono imara wa mamlaka ya kiserikali ili kutayarisha njia kwa ajili ya ufalme Wake . . . Chombo katika nyakati hizi zenye maana ni cha kibinadamu; nguvu yenye kuelekeza ni ya kimungu. Gavana mkuu wa mataifa yote ametumia Uingereza kuadhibu na kunyenyekeza China.”—Manukuu yamechukuliwa kutoka “Ends and Means,” 1974, insha ya Stuart Creighton Miller iliyotangazwa katika The Missionary Enterprise in China and America (Durusi la Harvard lililohaririwa na John K. Fairbank).
[Picha katika ukurasa wa 264]
“Wauza-Bidhaa Wasafiri . . . Wakawa na Utajiri”
“Kati ya 1929 na mfyatuko wa Vita ya Ulimwengu 2, [Bernadino] Nogara [msimamizi wa mambo ya kifedha wa Vatikani] aligawia Vatikani jiji kuu na mawakili wa Vatikani kufanya kazi katika maeneo ya namna namna ya uchumi wa Italia—hasa katika nguvu za umeme, mawasiliano ya simu, karidhi na kazi za benki, njia za reli ndogondogo, na ufanyizaji wa zana za kilimo, saruji, na nyuzi za nguo za kubuniwa. Nyingi za shughuli hizi zilifanikiwa.
“Nogara alinyakua kampuni kadhaa kutia na La Società Italiana della Viscosa, La Supertessile, La Società Meridionale Industrie Tessili, na La Cisaraion. Akiunganisha hizi kuwa kampuni moja, ambayo aliita CISA-Viscosa na akaiweka chini ya usimamizi wa Baron Francesco Maria Oddasso, mmojapo makabwela wa Vatikani wenye kuitibariwa zaidi sana, kisha Nogara akaongoza mambo kwa werevu ili kampuni hiyo mpya itwaliwe na [kampuni] ya Italia iliyo kubwa zaidi sana ya kufanyiza nguo, SNIA-Viscosa. Hatimaye faida za Vatikani katika SNIA-Viscosa zikakua zikawa kubwa zaidi na zaidi, na baada ya wakati Vatikani ikachukua udhibiti—kama inavyoshuhudiwa na uhakika wa kwamba baadaye Baron Oddasso akawa makamu wa msimamizi.
“Ndivyo Nogara akapenya ndani ya kiwanda cha nguo. Yeye alipenya ndani ya viwanda vingine katika njia nyingine nyingine, kwa maana Nogara alikuwa mwenye vitimbi vingi. Mtu huyu asiye na ubinafsi . . . pengine alifanya mengi zaidi kutia uhai katika uchumi wa Italia kuliko mwanabiashara mwingine yeyote mmoja katika historia ya Italia . . . Benito Mussolini hakuweza kamwe kupata kabisa milki ambayo yeye aliotea ndoto, lakini yeye aliwezesha Vatikani na Bernadino Nogara kubuni utawala wa aina nyingine.”—The Vatican Empire, cha Nino Lo Bello, kurasa 71-3.
Hiki ni kielelezo kimoja tu cha ushirikiano wa karibu karibu kati ya wauza-bidhaa wa dunia na Babuloni Mkubwa. Si ajabu kwamba wauza-bidhaa hawa wataomboleza wakati mshirika wao wa kibiashara atakapokuwa hayupo tena!
-
-
Kuomboleza na Kushangilia Mwisho wa BabuloniUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 37
Kuomboleza na Kushangilia Mwisho wa Babuloni
1. “Wafalme wa dunia” watatendaje kwa kuitikia uharibifu wa ghafula wa Babuloni Mkubwa?
MWISHO wa Babuloni ni habari njema kwa watu wa Yehova, lakini mataifa yanauonaje? Yohana anatuambia: “Na wafalme wa dunia ambao walifanya uasherati na yeye na wakaishi katika anasa yenye utovu wa aibu watatoa machozi na kujipigapiga wenyewe kwa kihoro juu yake, wanapotazama moshi kutoka kuchomwa kwake, huku wao wakisimama mbali kwa sababu ya hofu yao ya teso lake na kusema, ‘Ni vibaya mno, ni vibaya mno, wewe jiji kubwa, Babuloni wewe jiji imara, kwa sababu katika saa moja hukumu yako imewasili!’”—Ufunuo 18:9, 10, NW.
2. (a) Kwa kuwa pembe kumi za ufananisho za hayawani-mwitu rangi-nyekundu-nyangavu zitamharibu Babuloni Mkubwa, ni kwa nini “wafalme wa dunia” wanahuzunikia mwisho wake? (b) Ni kwa nini hao wafalme wenye kihoro husimama mbali na jiji lililohukumiwa maangamizi?
2 Tendo-mwitikio la mataifa huenda likaonekana kuwa la kushangaza kwa sababu ya uhakika wa kwamba Babuloni aliharibiwa na zile pembe kumi za ufananisho za hayawani-mwitu rangi-nyekundu-nyangavu. (Ufunuo 17:16) Lakini Babuloni atakapokuwa hayupo, kwa wazi “wafalme wa dunia” watang’amua jinsi alivyokuwa mwenye mafaa kwao katika kutuliza watu na kuwatiisha. Viongozi wa kidini wamejulisha wazi vita kuwa vitakatifu, wakatenda wakiwa mawakili wa kuandikisha askari-jeshi, na wakahubiri vijana waingie katika mapigano. Dini imeandaa kisetiri cha utakatifu ambacho nyuma yacho watawala wafisadi wameendesha mambo katika kukandamiza makabwela. (Linga Yeremia 5:30, 31; Mathayo 23:27, 28.) Hata hivyo, angalia kwamba wafalme hawa wenye kihoro sasa wanasimama mbali na hilo jiji lenye kuhukumiwa maangamizi. Wao hawakaribii vya kutosha ili kuliauni. Wao wanahuzunikia kuona linaenda lakini hawahuzuniki vya kutosha kujihatarisha kwa ajili yalo.
Wauza-Bidhaa Watoa Machozi na Kuomboleza
3. Ni nani wengine wanaojutia kupita kwa Babuloni Mkubwa, na Yohana hutoa sababu zipi juu ya hilo?
3 Wafalme wa dunia sio pekee wanaojutia kupita kwa Babuloni Mkubwa. “Pia, wauza-bidhaa wasafiri wa dunia wanatoa machozi na kuomboleza juu ya yeye, kwa sababu hakuna wa kununua tena bidhaa yao kamili, bidhaa kamili ya dhahabu na fedha na jiwe la thamani na lulu na kitani nzuri na zambarau na hariri na rangi-nyekundu-nyangavu; na kila kitu katika mbao zenye kutiwa manukato na kila aina ya kitu cha meno ya tembo na kila aina ya kitu kutokana na mbao iliyo ya thamani kubwa zaidi sana na cha shaba na cha chuma na cha marimari; pia mdalasini na vikolezo vya Kihindi na uvumba na mafuta yaliyotiwa harufu nzuri na ubani na divai na mafuta ya zeituni na unga safi sana na ngano na ng’ombe na kondoo, na farasi na makochi na watumwa na nafsi za kibinadamu. Ndiyo, na tunda zuri ambalo nafsi yako ilitamani limeondoka kutoka kwa wewe [Babuloni Mkubwa], na vitu vitamu-vitamu vyote na vitu vya umaridadi vimepotelea mbali kutoka kwa wewe, na watu hawatavipata tena kamwe.”—Ufunuo 18:11-14, NW.
4. Ni kwa nini “wauza-bidhaa wasafiri” hutoa machozi na kuombolezea mwisho wa Babuloni Mkubwa?
4 Ndiyo, Babuloni Mkubwa alikuwa rafiki ya karibu na mteja mwema wa wauza-bidhaa wenye ukwasi. Mathalani, kwa muda wa karne zilizopita nyumba za watawa-waume, nyumba za watawa wa kike na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo zimejipatia kiasi kikubwa mno cha dhahabu, fedha, mawe ya thamani, mbao za thamani, na namna nyinginezo za ukwasi wa vitu vya kimwili. Na zaidi, baraka ya kidini imetolewa juu ya shamrashamra za ununuzi wa kianasa na karamu za ulafi, ulevi na uasherati zinazoandamana na mwadhimisho wa Krismasi wenye kuvunjia Kristo heshima na siku nyinginezo zinazoitwa eti takatifu. Wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo wamepenya ndani ya mabara ya mbali, wakafungua masoko mapya kwa ajili ya “wauza-bidhaa wasafiri” wa ulimwengu huu. Katika Japani ya karne ya 17, Ukatoliki, uliokuja pamoja na wachuuzi hata ulijihusisha katika vita vyenye uhasama wa daima. Ikiripoti juu ya vita yenye kukata maneno chini ya kuta za ngome ya Osaka, The Encyclopædia Britannica hutaarifu hivi: “Vikosi vya Tokugawa vilijikuta vikipigana dhidi ya adui ambaye bendera zake zilikuwa zimepambwa kwa msalaba na mifano ya Mwokozi na ya [Mt.] James, mtakatifu mfadhili wa Hispania.” Chamkano yenye kushinda ilinyanyasa na karibu imalize Ukatoliki katika bara hilo. Ushiriki wa kanisa katika mambo ya ulimwengu leo vilevile hautaliletea baraka.
5. (a) Sauti kutoka katika mbingu inaelezaje zaidi kuomboleza kwa hao “wauza-bidhaa wasafiri”? (b) Ni kwa nini wauza-bidhaa ‘wanasimama mbali’ pia?
5 Sauti kutoka katika mbingu inasema zaidi hivi: “Wauza-bidhaa wasafiri wa vitu hivi, ambao wakawa na utajiri kutokana na yeye, watasimama mbali kwa sababu ya hofu yao ya teso lake na watatoa machozi na kuomboleza, kusema, ‘Ni vibaya mno, ni vibaya mno—jiji kubwa, lililovikwa kitani nzuri na zambarau na rangi-nyekundu-nyangavu, na kurembwa kitajiri kwa madoido ya dhahabu na jiwe la thamani na lulu, kwa sababu katika saa moja utajiri mwingi hivyo umeteketezwa!’” (Ufunuo 18:15-17a, NW) Kwa sababu ya kuharibiwa kwa Babuloni Mkubwa, “wauza-bidhaa” wanaombolezea hasara ya mshirika wa kibiashara huyo. Kwa kweli, “ni vibaya mno, ni vibaya mno” kwao. Hata hivyo, angalia kwamba sababu za kuomboleza kwao ni za ubinafsi kabisa na kwamba wao—kama vile wafalme—‘husimama mbali.’ Wao hawakaribii sana vya kutosha ili wasaidie Babuloni Mkubwa.
6. Sauti kutoka katika mbingu inaelezaje kuomboleza kwa makapteni wa meli na mabaharia, na ni kwa nini wao hutoa machozi?
6 Simulizi laendelea: “Na kila kapteni wa meli na kila mtu ambaye husafiri kwa meli kokote, mabaharia na wale wote ambao hupata riziki kwa bahari, walisimama mbali na kupiga kilio kikuu walipotazama moshi wa kuchomwa kwake na kusema, ‘Ni jiji gani lililo kama jiji kubwa?’ Na wao wakatupa mavumbi juu ya vichwa vyao na kupiga kilio kikuu, wakitoa machozi na kuomboleza, na wakasema, ‘Ni vibaya mno, ni vibaya mno—jiji kubwa, ambalo katika hilo wale wote wenye mashua kwenye bahari, wakawa na utajiri kwa sababu ya ughali walo, kwa kuwa katika saa moja limeteketezwa!’” (Ufunuo 18:17b-19, NW) Babuloni wa kale alikuwa jiji la kibiashara na alikuwa na kundi kubwa la meli. Hali moja na hiyo, Babuloni Mkubwa hufanya biashara nyingi sana kwa kutumia “maji mengi” ya watu wake. Hiyo huandaa kuajiriwa kwa raia wake wengi wa kidini. Uharibifu wa Babuloni Mkubwa utakuwa dharuba ya kiuchumi kama nini kwa watu hawa! Hakutakuwa kamwe na chimbuko jingine la riziki kama yeye.
Kushangilia Juu ya Utowesho Wake
7, 8. Sauti kutoka katika mbingu inafikiaje upeo wa ujumbe wayo kuhusu Babuloni Mkubwa, na ni nani watakaoitikia maneno hayo?
7 Babuloni wa kale alipopinduliwa na Wamedi na Waajemi, Yeremia alisema kiunabii hivi: “Na juu ya Babuloni mbingu na dunia na wale wote walio ndani yazo kwa hakika watapiga kilio kikuu kwa kushangilia.” (Yeremia 51:48, NW) Wakati Babuloni Mkubwa aharibiwapo, sauti kutoka katika mbingu inafikisha ujumbe wayo kwenye upeo kwa kusema juu ya Babuloni Mkubwa hivi: “Uwe na nderemo juu yake, O mbingu, pia nyinyi watakatifu na nyinyi mitume na nyinyi manabii, kwa sababu kwa hukumu Mungu ametoza adhabu kutoka kwake kwa ajili ya nyinyi!” (Ufunuo 18:20, NW) Yehova na malaika watapendezwa sana kuona utowesho wa adui wa kale wa Mungu, kama vile watakavyopendezwa mitume na wale manabii Wakristo wa mapema, ambao kwa sasa wamefufuliwa na wamechukua cheo chao katika ule mpango wa wazee 24.—Linga Zaburi 97:8-12.
8 Kweli kweli, “watakatifu” wote,—wawe wamefufuliwa kwenda kwenye mbingu au wangali wanaendelea kuishi duniani—watapiga kilio kikuu kwa shangwe, kama vile utakavyofanya umati mkubwa wa kondoo wengine unaoshirikiana nao. Baada ya wakati kupita, watu wote waaminifu wa zamani watafufuliwa ndani ya mfumo mpya wa mambo, na wao vilevile watajiunga katika kushangilia. Watu wa Mungu hawakujaribu kujilipiza kisasi wenyewe juu ya wanyanyasaji wao wa dini bandia. Wao wamekumbuka maneno ya Yehova: “Kisasi ni changu mimi; mimi nitalipa, asema Yehova.” (Warumi 12:19; Kumbukumbu 32:35, 41-43, NW) Basi, Yehova amelipa sasa. Damu yote iliyomwagwa na Babuloni Mkubwa itakuwa imekwisha lipizwa kisasi.
Kuvurumisha Jiwe Kubwa la Kusagia
9, 10. (a) Sasa malaika kabambe anafanya na kusema nini? (b) Ni tendo gani kama hilo linalofanywa na huyo malaika wa Ufunuo 18:21 lilitukia katika siku ya Yeremia, na hilo lilitoa dhamana gani? (c) Tendo linalochukuliwa na malaika kabambe aliyeonwa na Yohana linatoa dhamana gani?
9 Jambo ambalo Yohana anafuata kuona linathibitisha kwamba hukumu ya Yehova juu ya Babuloni Mkubwa ni ya kukata maneno: “Na malaika kabambe akainua juu jiwe kama jiwe kubwa la kusagia na kulivurumisha ndani ya bahari, kusema: ‘Hivyo kwa mtupo wa kasi sana Babuloni jiji kubwa atavurumishwa chini, na yeye hatapatikana kamwe tena.’” (Ufunuo 18:21, NW) Katika wakati wa Yeremia, tendo kama hilo likiwa na maana kubwa ya kiunabii lilifanywa. Yeremia alivuviwa aandike katika kitabu “mabaa yote ambayo yangekuja juu ya Babuloni.” Yeye alimpa Seraya kitabu na kumwambia asafiri hadi Babuloni. Huko, akifuata maagizo ya Yeremia, Seraya alisoma julisho-wazi dhidi ya jiji hilo: “O Yehova, wewe mwenyewe umesema dhidi ya mahali hapa, ili kupakatilia mbali pasipate kuwa na mkazi ndani yapo, ama binadamu ama hata mnyama wa nyumbani, bali kwamba pawe mahali patupu tu penye ukiwa hadi wakati usio dhahiri.” Kisha Seraya akafungilia jiwe kwenye kitabu na kukitupa ndani ya mto Eufrati, akisema: “Hivi ndivyo Babuloni litazama chini na halitainuka kamwe kwa sababu ya baa ambalo mimi ninaleta juu yake.”—Yeremia 51:59-64, NW.
10 Kutupwa kwa kitabu ndani ya mto kikiwa kimefungiliwa jiwe kulikuwa dhamana kwamba Babuloni lingetumbukia ndani ya hali ya kutokomea kabisa, lisipate kupona kamwe. Kuona kwa mtume Yohana malaika kabambe akifanya tendo linalofanana na hilo hali kadhalika ni dhamana yenye nguvu kwamba kusudi la Yehova kuelekea Babuloni Mkubwa litatimizwa. Hali ya kuangamia kabisa ya Babuloni wa kale leo hushuhudia kwa nguvu sana kitakachoangukia dini bandia katika wakati ujao ulio karibu.
11, 12. (a) Sasa malaika kabambe anahutubiaje Babuloni Mkubwa? (b) Yeremia alitoaje unabii kuhusu Yerusalemu lililoasi imani, na huo uliashiria nini kwa ajili ya siku yetu?
11 Sasa malaika kabambe anahutubia Babuloni Mkubwa, kusema hivi: “Na sauti ya waimbaji ambao hujifuatanisha kwa kinubi na ya wanamuziki na ya wanafilimbi na ya wanatarumbeta haitasikiwa tena kamwe ndani ya wewe, na hakuna fundi wa kazi ya uchumi yoyote ambaye atapatikana tena wakati wowote ndani ya wewe, na hakuna sauti ya jiwe la kusagia itakayosikika tena wakati wowote ndani yako, na hakuna nuru ya taa ambayo itaangaza tena wakati wowote ndani ya wewe, na hakuna sauti ya bwana-arusi na ya bibi-arusi ambayo itasikiwa tena wakati wowote ndani ya wewe; kwa sababu wauza-bidhaa wasafiri wako walikuwa ndio watu wenye vyeo vya juu wa dunia, kwa maana kwa zoea lako la uwasiliano na roho mataifa yote yaliongozwa vibaya.”—Ufunuo 18:22, 23, NW.
12 Kwa semi zinazolinganika, Yeremia alitoa unabii kuhusu Yerusalemu asi-imani: “Mimi nitaharibu kutoka wao mvumo wa mchachawo na mvumo wa kushangilia, na sauti ya bwana-arusi na sauti ya bibi-arusi, na mvumo wa kinu cha mkono na nuru ya taa. Na bara hili lote lazima liwe mahali palipoteketezwa na kitu cha kutia kimako.” (Yeremia 25:10, 11, NW) Ikiwa ndiyo sehemu kuu ya Babuloni Mkubwa, Jumuiya ya Wakristo itakuwa magofu yasiyo na uhai, kama vile imeonyeshwa wazi sana na ukiwa wa Yerusalemu baada ya 607 K.W.K. Jumuiya ya Wakristo ambayo wakati mmoja ilishangilia kwa moyo mkunjufu na ikashughulika kwa kelele ya kila siku itajikuta yenyewe ikiwa imeshindwa na kutupiliwa mbali.
13. Ni badiliko gani la ghafula linalomfikilia Babuloni Mkubwa, na tokeo ni nini kwa “wauza-bidhaa wasafiri” wake?
13 Kweli kweli, kama vile malaika huyo anavyomwambia Yohana, Babuloni Mkubwa wote atageuka kutoka milki ya ulimwengu yenye nguvu, na kuwa bara-ukiwa kavu mithili ya mahame. “Wauza-bidhaa” wake, kutia na mamilionea wa vyeo vya juu, wametumia dini yake kwa kujinufaisha kibinafsi au kama kisetiri cha mabaya, na hao viongozi wa kidini wameliona kuwa jambo lenye kufaidi kushiriki pamoja nao katika umashuhuri huo. Lakini wauza-bidhaa hao hawatakuwa tena na Babuloni Mkubwa akiwa mshirika wao katika kufanya mabaya. Yeye hatayapofusha macho tena mataifa ya dunia kwa mazoea ya mafumbo yake ya kidini.
Hatia ya Damu Yenye Kutisha
14. Ni nini anayotoa malaika kabambe kuwa ndiyo sababu ya ukali wa hukumu ya Yehova, na Yesu alisema nini hali moja na hivyo wakati alipokuwa duniani?
14 Kwa kumalizia, malaika kabambe amwambia Yohana sababu ya Yehova kumhukumu Babuloni Mkubwa kwa ukali hivyo. “Ndiyo,” asema malaika, “katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24, NW) Alipokuwa duniani, Yesu aliambia viongozi wa kidini kwamba wao walistahili kutozwa hesabu kwa ajili ya “damu yote yenye uadilifu iliyomwagwa juu ya dunia, kutoka damu ya Abeli mwadilifu” na kuendelea. Kulingana na hilo, kizazi hicho kombokombo kiliharibiwa katika 70 W.K. (Mathayo 23:35-38, NW) Leo, kizazi kingine cha wanadini kinabeba hatia ya damu kwa ajili ya kunyanyasa watumishi wa Mungu.
15. Kanisa Katoliki katika Ujeremani ya Nazi lilikuwaje na hatia ya damu katika visa viwili?
15 Katika kitabu chake The Catholic Church and Nazi Germany, Guenter Lewy anaandika: “Wakati Mashahidi wa Yehova walipokandamizwa katika Bavaria Aprili 13 [1933] Kanisa hata lilikubali mgawo liliopewa na Wizara ya Elimu na Dini wa kuripoti juu ya washiriki wa farakano hilo walioendelea kuzoea dini hiyo iliyokatazwa.” Hivyo Kanisa Katoliki linashiriki daraka la kupelekwa kwa maelfu ya Mashahidi kwenye kambi za mateso; mikono yalo imetiwa madoa ya damu ya uhai wa mamia ya Mashahidi ambao walinyongwa. Wakati Mashahidi vijana, kama Wilhelm Kusserow, walipoonyesha kwamba wangekufa kijasiri kwa kupigwa risasi na kikosi cha wapiga risasi, Hitla aliamua kwamba kikosi cha wapiga risasi hakikuwafaa wakataaji kidhamira; kwa hiyo Wolfgang ndugu ya Wilhelm, akiwa na umri wa miaka 20, alikufa kwa njia ya gilotini. Wakati ule ule, Kanisa Katoliki lilikuwa likiwatia moyo vijana Wakatoliki Wajeremani wafe katika jeshi la bara-baba lao. Hatia ya damu ya hilo kanisa yaonekana wazi!
16, 17. (a) Ni hatia gani ya damu ambayo ni lazima Babuloni Mkubwa ashtakiwe, na Vatikani ilikuwaje na hatia ya damu kuhusu Wayahudi waliouawa katika michinjo-chinjo ya Kinazi? (b) Ni katika njia gani moja ambayo kwayo dini bandia ina lawama kwa ajili ya kuuawa kwa mamilioni ya watu katika mamia ya vita katika nyakati zetu?
16 Hata hivyo, unabii unasema kwamba lazima Babuloni Mkubwa ashtakiwe kwa damu ya “wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.” Hakika hilo limekuwa kweli katika nyakati za ki-siku-hizi. Mathalani, kwa kuwa hila ya Katoliki ndiyo iliyomsaidia Hitla apate mamlaka katika Ujeremani, Vatikani inashiriki hatia ya damu iliyo mbaya sana juu ya Wayahudi milioni sita waliokufa katika michinjo-chinjo ya Kinazi. Na zaidi, katika nyakati zetu, watu zaidi ya milioni mia moja wameuawa katika mamia ya vita. Je! dini bandia ina lawama kwa habari hii? Ndiyo, kwa njia mbili.
17 Njia moja ni kwamba vita vingi vinahusiana na tofauti za kidini. Mathalani, jeuri katika India kati ya Waislamu na Wahindu katika 1946-48 ilichochewa na dini. Mamia ya maelfu ya maisha yalipotea. Pambano kati ya Iraki na Irani katika miaka ya 1980 lilihusiana na tofauti za kimafarakano, kukiwa na mamia ya maelfu waliouawa. Jeuri kati ya Wakatoliki na Waprotestanti katika Ailandi ya Kaskazini imetwaa maelfu ya maisha. Akichunguza uwanja huu, mleta habari za magazetini C. L. Sulzberger alisema hivi katika 1976: “Ni ukweli wenye kuhuzunisha kwamba pengine nusu au zaidi ya vita vinavyopiganwa sasa kotekote katika ulimwengu ama kwa wazi ni mapambano ya kidini ama yanahusu mabishano ya kidini.” Kweli kweli, imekuwa hivyo muda wote wa historia yenye msukosuko ya Babuloni Mkubwa.
18. Ni ipi njia ya pili ambayo kwayo dini za ulimwengu zina hatia ya damu?
18 Ni ipi ile njia nyingine? Kwa maoni ya Yehova, dini za ulimwengu zina hatia ya damu kwa sababu hizo hazikufundisha kwa kusadikisha wafuasi wazo ukweli wa matakwa ya Yehova kwa ajili ya watumishi wake. Hizo hazikufundisha watu kwa kusadikisha kwamba waabudu wa kweli lazima wamwige Yesu Kristo na kuonyesha wengine upendo bila kujali asili yao ya kitaifa. (Mika 4:3, 5; Yohana 13:34, 35; Matendo 10:34, 35; 1 Yohana 3:10-12) Kwa sababu dini ambazo zinajumlika kuwa Babuloni Mkubwa hazikufundisha vitu hivi, wafuasi wazo wamevutwa kuingizwa ndani ya kizingo cha vita vya kimataifa. Lo! jinsi hilo lilivyokuwa wazi katika vile vita viwili vya ulimwengu vya nusu ya kwanza ya karne ya 20, ambavyo vyote viwili vilianza katika Jumuiya ya Wakristo na vikatokeza kuchinjana kwa wanadini! Ikiwa wote wanaodai kuwa Wakristo wangalishikamana na kanuni za Biblia, vita hivyo havingaliweza kutukia kamwe.
19. Ni hatia ya damu gani yenye kutisha sana anayobeba Babuloni Mkubwa?
19 Yehova anaweka lawama la umwagaji-damu huu wote kwenye nyayo za Babuloni Mkubwa. Ikiwa viongozi wa kidini, hasa wale walio katika Jumuiya ya Wakristo, wangalifundisha watu wao ukweli wa Biblia, umwagaji-damu mkubwa sana hivyo haungalitukia. Kwa kweli, basi, kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja, Babuloni Mkubwa—yule kahaba mkubwa na milki ya ulimwengu ya dini bandia—lazima amjibu Yehova si kwa ajili ya “damu ya manabii na ya watakatifu” tu ambao yeye amenyanyasa na akaua bali pia kwa ajili “ya wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.” Kweli kweli Babuloni Mkubwa anabeba hatia ya damu yenye kutisha sana. Na apotelee mbali wakati uharibifu wake unapotukia!
-
-
Kuomboleza na Kushangilia Mwisho wa BabuloniUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 270]
Gharama ya Kuridhiana
Guenter Lewy anaandika katika kitabu chake The Catholic Church and Nazi Germany: “Kama Ukatoliki wa Ujeremani tangu mwanzo ungalishikamana na mwongozo wa kupinga kwa dhati utawala wa Nazi, historia ya ulimwengu ingaliweza kuchukua mwendo tofauti. Hata kama mng’ang’ano huu ungalikosa mwishowe kabisa kumshinda Hitla na kuzuia uhalifu wake mwingi, kwa oni hili ungaliinua sana hadhi ya kiadili ya Kanisa hilo. Gharama ya kibinadamu kwa ukinzani huu ingalikuwa kubwa bila kukanika, lakini dhabihu hizo zingalikuwa zimetolewa kwa ajili ya kusudi kubwa zaidi ya yote. Hitla akiwa haungwi mkono nyumbani, yamkini hangalithubutu kwenda vitani na kihalisi mamilioni ya maisha yangaliokolewa. . . . Wakati Wajeremani wapinga Unazi walipoteswa mpaka kifo katika kambi za mateso za Hitla, wakati weledi wa Polandi walipochinjwa, wakati mamia ya maelfu ya Warusi walipokufa kama tokeo la kutendwa kama Untermenschen [nusu-binadamu] wa Kislavi, na wakati binadamu 6,000,000 walipouawa kimakusudi kwa kuwa ‘si Waarya,’ maofisa wa Kanisa Katoliki katika Ujeremani walitegemeza utawala uliokuwa ukifanya uhalifu huu. Papa katika Roma, kichwa cha kiroho na mwalimu wa kiadili mkuu zaidi ya wote wa Kanisa Katoliki la Roma, alikaa kimya.”—Kurasa 320, 341.
-
-
Sifuni Yah kwa Hukumu Zake!Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 38
Sifuni Yah kwa Hukumu Zake!
1. Yohana anasikia maneno gani “kama sauti kubwa ya umati mkubwa katika mbingu”?
BABULONI MKUBWA hayupo tena! Kwa kweli hizi ni habari zenye shangwe. Si ajabu kwamba Yohana anasikia mipaazo yenye furaha katika mbingu! “Baada ya vitu hivi mimi nikasikia kilichokuwa kama sauti kubwa ya umati mkubwa katika mbingu. Wao walisema: ‘Halleluyah!a Wokovu na utukufu na nguvu ni za Mungu wetu, kwa sababu hukumu zake ni za kweli na za uadilifu. Kwa maana yeye ametekeleza hukumu juu ya kahaba mkubwa ambaye alifisidi dunia kwa uasherati wake, na yeye amelipiza kisasi cha damu ya watumwa wake katika mkono wake.’ Na mara hiyo kwa mara ya pili wao wakasema: ‘Halleluyah!b Na ule moshi kutoka kwake huendelea kupaa milele na milele.’”—Ufunuo 19:1-3, NW.
2. (a) Neno “Halleluyah” humaanisha nini, na Yohana kulisikia mara mbili kufikia hapa huonyesha nini? (b) Ni nani anayepokea utukufu kwa kuharibu Babuloni Mkubwa? Fafanua.
2 Halleluyah kweli kweli! Neno hilo humaanisha “Sifuni Yah, nyinyi watu,” “Yah” ikiwa ni namna ya kifupi cha jina la kimungu, Yehova. Tunakumbushwa hapa waadhi ya mtunga zaburi: “Kila kitu chenye kupumua—acheni kisifu Yah. Sifuni Yah, nyinyi watu!” (Zaburi 150:6, NW) Kusikia kwa Yohana korasi ya kimbingu yenye kuchachawa ikiimba “Halleluyah!” mara mbili kufikia hapa katika Ufunuo huonyesha mwendeleo wa ufunuo wa kimungu wa ukweli. Mungu wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ndiye Mungu yule yule wa Maandiko ya Kiebrania ya mapema zaidi, na Yehova ndilo jina lake. Mungu aliyesababisha anguko la Babuloni wa kale amehukumu na akaharibu sasa Babuloni Mkubwa. Mpeni utukufu kwa tendo hilo la uhodari! Nguvu iliyoongoza kwa werevu kuanguka kwake ilikuwa yake badala ya kuwa ya mataifa ambayo yeye alitumia kuwa vyombo vya kumwacha ukiwa. Yatupasa sisi kumsifu Yehova pekee kwa ajili ya wokovu.—Isaya 12:2; Ufunuo 4:11; 7:10, 12.
3. Ni kwa sababu gani kahaba mkubwa amestahili sana hukumu yake?
3 Ni kwa sababu gani kahaba mkubwa amekuwa mwenye kustahili sana hukumu hii? Kulingana na Sheria ambayo Yehova alitoa kwa Noa—na kupitia yeye kwa aina ya binadamu yote—kumwaga damu kimakusudi kunataka hukumu ya kifo. Taarifa hiyo ilitolewa tena katika Sheria ya Mungu kwa Israeli. (Mwanzo 9:6; Hesabu 35:20, 21) Zaidi ya hilo, chini ya Sheria ya Musa uzinzi wa kiroho na wa kimwili ulistahilisha kifo. (Walawi 20:10; Kumbukumbu 13:1-5) Kwa maelfu ya miaka, Babuloni Mkubwa amekuwa na hatia ya damu, na yeye ni mwasherati mbaya sana. Mathalani, sera ya Kanisa Katoliki la Roma ya kukataza mapadri walo kuoa imetokeza utovu wa adili mbaya sana upande wa wengi wao, na ni wengi wa hawa leo ambao wameambukizwa UKIMWI. (1 Wakorintho 6:9, 10; 1 Timotheo 4:1-3) Lakini madhambi yake makubwa, ‘yakitungamana pamoja moja kwa moja hadi mbinguni,’ ni matendo yalo yenye kugutusha ya uasherati wa kiroho—tendo hili la pili ni katika kufundisha mafundisho bandia na kujipanga upande mmoja na wanasiasa wafisadi. (Ufunuo 18:5) Kwa kuwa adhabu yake mwishowe imemfikilia, halaiki kubwa ya kimbingu sasa yarudisha mwangwi wa pili wa Halleluyah!
4. Ni nini kinachofananishwa na uhakika wa kwamba moshi kutoka Babuloni Mkubwa “huendelea kupaa milele na milele”?
4 Babuloni Mkubwa amewashwa moto kama jiji lililoshindwa, na moshi wa kutoka kwake “huendelea kupaa milele na milele.” Wakati jiji halisi linapochomwa na majeshi yenye ushindi, moshi huendelea kupaa kwa muda ambao majivu ni yenye moto. Yeyote anayejaribu kulijenga tena linapoendelea kutoa moshi atachomwa tu na yale magofu yenye kutoa moshi. Kwa kuwa moshi kutoka kwake utainuka “milele na milele” katika kuonyesha hukumu yake yenye kukata maneno, hakuna yeyote atakayeweza wakati wowote kurudisha jiji hilo lenye dhambi. Dini bandia imetoweka milele na milele. Halleluyah, kweli kweli!—Linga Isaya 34:5, 9, 10.
5. (a) Wazee 24 na viumbe hai wanne wanafanya na kusema nini? (b) Ni kwa sababu gani kibwagizo cha Halleluyah ni cha kimelodia kuliko korasi za Halleluyah zinazoimbwa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo?
5 Katika njozi ya mapema zaidi, Yohana aliona kuzunguka kiti cha ufalme viumbe hai wanne, pamoja na wazee 24 ambao ni picha ya warithi wa Ufalme wakiwa katika cheo chao kitukufu cha kimbingu. (Ufunuo 4:8-11) Sasa yeye anawaona tena na wao wanangurumisha Halleluyah ya tatu juu ya uharibifu wa Babuloni Mkubwa: “Na wale wazee ishirini na wanne na viumbe hai wanne wakaanguka chini na kuabudu Mungu aketiye juu ya kiti cha ufalme, na kusema: ‘Ameni! Halleluyah.’”c (Ufunuo 19:4, NW) Basi, korasi tukufu hii ya Halleluyah ni katika kuongezea ule “wimbo mpya” wa sifa kwa Mwana-Kondoo. (Ufunuo 5:8, 9, NW) Wao wanaimba sasa kibwagizo cha ushindi wenye utukufu, wakimpa Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu utukufu wote kwa sababu ya ushindi wake wenye kukata maneno juu ya kahaba mkubwa, Babuloni Mkubwa. Halleluyah hizi zimelia kimelodia kwa mbali zaidi sana kuliko korasi za Halleluyah zozote zilizopata kuimbwa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ambamo Yehova, au Yah, amevunjiwa heshima na akadharauliwa. Wimbaji wa kinafiki kama huo unaoshutumu jina la Yehova umekomeshwa sasa milele!
6. Ni “sauti” ya nani inayosikiwa, nayo inahimiza nini, na ni nani wanaoshiriki katika kuitikia?
6 Ilikuwa katika 1918 ndipo Yehova alianza kuthawabisha ‘wale wanaohofu jina lake, wadogo na wakubwa’—wa kwanza wa hawa wakiwa wa wale Wakristo wapakwa-mafuta ambao walikuwa wamekufa wakiwa waaminifu, na ambao yeye alifufua na akawaweka katika vyeo vya kimbingu vya wazee 24. (Ufunuo 11:18, NW) Wengine hujiunga na hawa katika kuimba Halleluyah, kwa kuwa Yohana huripoti hivi: “Pia, sauti moja ikatokea katika kiti cha ufalme na kusema: ‘Mwe mkisifu Mungu wetu, nyinyi nyote watumwa wake, ambao huhofu yeye, wadogo na wakubwa.’” (Ufunuo 19:5, NW) Hii ni “sauti” ya Mneni wa Yehova, Mwana wake mwenyewe, Yesu Kristo, ambaye husimama “katikati ya kiti cha ufalme.” (Ufunuo 5:6, NW) Si mbinguni tu bali pia hapa duniani, “nyinyi nyote watumwa wake” shirikini katika kuimba, jamii ya Yohana iliyopakwa mafuta ikiwa inachukua uongozi duniani. Ni kwa kuchachawa kulikoje hawa hushiriki katika kutii amri: “Mwe mkisifu Mungu wetu”!
7. Baada ya Babuloni Mkubwa kuharibiwa, ni nani watakaokuwa wakisifu Yehova?
7 Ndiyo, wale wa umati mkubwa pia huhesabiwa wanapewa namba pia miongoni mwa watumwa hawa. Tangu 1935 hawa wamekuwa wakitoka katika Babuloni Mkubwa na wameona utimizo wa ahadi ya Mungu: “Yeye atabariki wale ambao huhofu Yehova, wadogo na wakubwa.” (Zaburi 115:13, NW) Wakati Babuloni Mkubwa aharibiwapo, mamilioni yao watajiunga katika ‘kusifu Mungu wetu’—pamoja na jamii ya Yohana na wingi wote wa kimbingu. Baadaye, wale wenye kufufuliwa duniani, wawe hapo kwanza walikuwa mashuhuri au la, bila shaka wataimba Halleluyah zaidi wanapojifunza kwamba Babuloni Mkubwa ametoweka milele. (Ufunuo 20:12, 15) Sifa yote imwendee Yehova kwa ushindi wake wenye kishindo juu ya kahaba huyo wa tangu zamani!
8. Korasi za sifa zilizoshuhudiwa na Yohana zapaswa kutupa sisi kichochezi gani sasa, kabla ya Babuloni Mkubwa kuharibiwa?
8 Hayo yote yanatupa sisi kichochezi kama nini tushiriki katika kazi ya Mungu leo! Watumishi wote wa Yah na wajitoe wenyewe kwa moyo na nafsi kutangaza hukumu za Mungu, pamoja na tumaini tukufu la Ufalme, sasa, kabla ya Babuloni Mkubwa kuondolewa katika kiti na kuharibiwa.—Isaya 61:1-3; 1 Wakorintho 15:58.
‘Halleluyah—Yehova Ni Mfalme!’
9. Ni kwa sababu gani Halleluyah ya mwisho ni yenye mvumo kamili, ni ya sauti timilifu, na ya hali ya juu sana?
9 Kuna sababu zaidi kwa kushangilia, kama vile Yohana aendeleavyo kutuambia: “Na mimi nikasikia kilichokuwa kama sauti ya umati mkubwa na kama mvumo wa maji mengi na kama mvumo wa ngurumo kubwa. Zikasema: ‘Halleluyah,d kwa sababu Yehova Mungu wetu, Mweza Yote, ameanza kutawala akiwa mfalme.’” (Ufunuo 19:6, NW) Halleluyah hii ya mwisho ndiyo inayofanya mbiu iwe yenye miraba minne, au yenye ulingano. Ni mvumo wa kimbingu wenye nguvu, wa hali ya juu kuliko korasi yoyote ya kibinadamu, yenye fahari ya kifalme zaidi ya poromoko la maji lolote la kidunia, na yenye kuvuvia hofu zaidi kuliko ngurumo yoyote ya kidunia. Mamiriadi ya sauti za kimbingu yanasherehekea uhakika wa kwamba “Yehova Mungu wetu, Mweza Yote, ameanza kutawala akiwa mfalme.”
10. Ni katika maana gani inaweza kusemwa kwamba Yehova huanza kutawala akiwa mfalme baada ya mteketeo wa Babuloni Mkubwa?
10 Ingawa hivyo, inakuwaje kwamba Yehova huanza kutawala? Mamileani yamepita tangu mtunga zaburi alipotangaza: “Mungu ni Mfalme wangu tangu zamani za kale.” (Zaburi 74:12, NW) Umaliki wa Yehova ulikuwa wa kale hata wakati huo, kwa hiyo korasi hiyo ya ulimwengu wote mzima ingewezaje kuimba kwamba “Yehova . . . ameanza kutawala akiwa mfalme”? Katika maana ya kwamba wakati Babuloni Mkubwa anapoharibiwa, Yehova hatakuwa tena na mshindani huyo mwenye kimbelembele akikengeusha utii kwake akiwa ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima. Dini bandia haitachochea tena watawala wa dunia wampinge. Wakati Babuloni wa kale alipoanguka kutoka utawala wa ulimwengu, Sayuni ilisikia mbiu ya ushindi: “Mungu wako amekuwa mfalme!” (Isaya 52:7, NW) Baada ya Ufalme kuzaliwa katika 1914, wazee 24 walipiga mbiu hii: “Sisi twashukuru wewe, Yehova Mungu . . . kwa sababu wewe umechukua nguvu kuu zako na umeanza kutawala ukiwa mfalme.” (Ufunuo 11:17, NW) Sasa, baada ya mteketeo wa Babuloni Mkubwa, kilio kinatamkwa tena: “Yehova . . . ameanza kutawala akiwa mfalme.” Hakuna kamungu kalikofanyizwa na mwanadamu kanakobaki kagombee enzi kuu ya Yehova, Mungu wa kweli!
Ndoa ya Mwana-Kondoo Imekaribia!
11, 12. (a) Yerusalemu wa kale liliitaje Babuloni wa kale, kuweka kiolezo gani kwa habari ya Yerusalemu Jipya na Babuloni Mkubwa? (b) Masongamano ya kimbingu huimba na kutangaza nini kwa ushindi juu ya Babuloni Mkubwa?
11 “Wewe mwanamke adui yangu”! Hivyo ndivyo Yerusalemu, mahali pa hekalu la ibada ya Yehova, liliita Babuloni mwabudu sanamu. (Mika 7:8, NW) Hali moja na hiyo, “jiji takatifu, Yerusalemu Jipya,” ambalo ni bibi-arusi mwenye washiriki 144,000, limekuwa na kila sababu ya kuita Babuloni Mkubwa kuwa adui yake. (Ufunuo 21:2) Lakini hatimaye huyo kahaba mkubwa amepatwa na msiba, janga, na angamio. Mazoea yake ya kuwasiliana na roho na wanajimu wake hayakumwokoa. (Linga Isaya 47:1, 11-13.) Ni ushindi mkubwa, kweli kweli, kwa ajili ya ibada ya kweli!
12 Kahaba mwenye kunyarafisha Babuloni Mkubwa, akiwa ametoweka milele, sasa uangalifu waweza kuelekezwa juu ya bibi-arusi bikira safi wa Mwana-Kondoo! Kwa sababu hiyo, masongamano ya kimbingu yaimba kwa mchachawo katika kusifu Yehova: “Acheni sisi tushangilie na tufurikwe na shangwe, na acheni sisi tumpe yeye utukufu, kwa sababu ndoa ya Mwana-Kondoo imewasili na mke wake amejitayarisha mwenyewe. Ndiyo, amepewa ruhusa kujipamba kwa kitani nyangavu, safi, nzuri sana, kwa maana kitani nzuri sana husimama kwa ajili ya matendo ya uadilifu ya watakatifu.”—Ufunuo 19:7, 8, NW.
13. Ni tayarisho gani kwa ajili ya ndoa ya Mwana-Kondoo limetukia kwa karne zote?
13 Kwa muda wa karne zote, Yesu amefanya tayarisho lenye upendo kwa ajili ya ndoa hii ya kimbingu. (Mathayo 28:20; 2 Wakorintho 11:2) Yeye amekuwa akisafisha 144,000 wa Israeli wa kiroho ili “yeye aweze kujiletea yeye mwenyewe kundi katika umaridadi walo, bila kuwa na doa au kunyanzi au lolote la vitu kama hivyo, bali kwamba limepaswa kuwa takatifu na bila waa.” (Waefeso 5:25-27, NW) Wakitaka kufikia “zawadi ya mwito wa juu wa Mungu,” kila Mkristo mpakwa-mafuta amelazimika kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yao, na kuvaa utu mpya wa Kikristo, na kufanya matendo ya uadilifu “kwa nafsi yote kama kwa Yehova.”—Wafilipi 3:8, 13, 14; Wakolosai 3:9, 10, 23, NW.
14. Shetani amejaribuje kuchafua wanaotazamiwa kuwa washiriki wa mke wa Mwana-Kondoo?
14 Kutoka Pentekoste 33 W.K. na kuendelea, Shetani alitumia Babuloni Mkubwa akiwa chombo chake katika kujaribu kuchafua wanaotazamiwa kuwa washiriki wa mke wa Mwana-Kondoo. Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, yeye alikuwa amepanda mbegu za dini ya Kibabuloni katika kundi. (1 Wakorintho 15:12; 2 Timotheo 2:18; Ufunuo 2:6, 14, 20) Mtume Paulo anaeleza wale ambao walikuwa wakipindua imani kwa maneno haya: “Kwa maana watu kama hao ni mitume bandia, wafanya kazi wadanganyifu, wakijigeuza umbile wenyewe kuwa mitume wa Kristo. Na si ajabu, kwa maana Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza umbile mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:13, 14, NW) Katika karne zilizoandama, Jumuiya ya Wakristo asi-imani, kama sehemu inayobaki ya Babuloni Mkubwa, ilijivisha yenyewe mavazi ya utajiri na pendeleo, “zambarau na rangi-nyekundu-nyangavu, . . . dhahabu na jiwe la thamani na lulu.” (Ufunuo 17:4, NW) Viongozi wayo wa kidini na mapapa waliandamana na maliki wenye kiu cha kumwaga damu kama vile Konstantino na Charlemagne. Yeye hakupambwa kamwe kwa “matendo ya uadilifu ya watakatifu.” Akiwa bibi-arusi bandia, kwa kweli yeye alikuwa kipeo cha udanganyi wa kishetani. Hatimaye, yeye ametoweka milele!
Mke wa Mwana-Kondoo Amejitayarisha
15. Kutiwa muhuri hutukiaje, na ni jambo gani linalotakwa kwa Wakristo wapakwa-mafuta?
15 Basi sasa, baada ya karibu miaka 2,000, wote 144,000 wa jamii ya bibi-arusi wamejiweka wenyewe tayari. Lakini ni kwenye pindi gani ya wakati inaweza kusemwa kwamba ‘mke wa Mwana-Kondoo amejitayarisha’? Kwa kuendelea, kutoka Pentekoste 33 W.K. wapakwa-mafuta wenye kuitikadi “walitiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa,” hii ni kwa kutazamia “siku ya kuachiliwa kupitia ukombozi” iliyokuwa ikija. Kama mtume Paulo alivyolisema jambo hilo, Mungu “pia ameweka muhuri wake juu yetu na ametupa sisi ishara ya kitakachokuja, yaani, roho, katika mioyo yetu.” (Waefeso 1:13; 4:30; 2 Wakorintho 1:22, NW) Kila Mkristo aliyepakwa mafuta ‘ameitwa na akachaguliwa,’ na amejithibitisha mwenyewe kuwa ‘mwaminifu.’—Ufunuo 17:14, NW.
16. (a) Kutiwa muhuri kwa mtume Paulo kulitimilizwa wakati gani, na sisi tunajuaje? (b) Ni wakati gani mke wa Mwana-Kondoo atakuwa ‘amejitayarisha’ kikamili?
16 Baada ya miongo ya mtihani, Paulo mwenyewe angeweza kujulisha wazi: “Mimi nimepiga vita njema, mimi nimekimbia mwendo hadi mwisho, mimi nimeshika imani. Kutoka wakati huu na kuendelea taji la uadilifu limehifadhiwa kwa ajili yangu mimi, ambalo Bwana, hakimu mwadilifu, atanipa mimi ikiwa thawabu katika siku hiyo, hata hivyo si mimi pekee, bali pia wale wote ambao wamependa udhihirisho wake.” (2 Timotheo 4:7, 8, NW) Kutiwa muhuri kwa mtume kunaonekana kulikuwa kumekamilika, hata ingawa alikuwa angali katika mnofu na bado angekabili ufia-imani. Hali moja na hiyo, wakati lazima uje ambao wale wote wanaobaki duniani wa wale 144,000 watakuwa wamekwisha kutiwa muhuri mmoja mmoja kuwa wao ni wa Yehova. (2 Timotheo 2:19) Huo utakuwa ndio wakati ambao mke wa Mwana-Kondoo atakuwa amekwisha jitayarisha kabisa—walio wengi sana wa 144,000 wakiwa wamekwisha pokea thawabu yao ya kimbingu na wale ambao wangali duniani wakiwa wamekwisha kukubaliwa mwishowe na kutiwa muhuri kuwa ni waaminifu.
17. Ni lini ndoa ya Mwana-Kondoo inapoweza kutukia?
17 Kufikia hapa katika jedwali ya wakati ya Yehova, wakati kutiwa muhuri kwa wale 144,000 kumefikia ukamilisho, malaika huachilia pepo nne za dhiki kubwa. (Ufunuo 7:1-3) Kwanza, hukumu inatekelezwa juu ya Babuloni Mkubwa aliye mithili ya kahaba. Kisha Kristo mwenye ushindi anasonga kwa haraka kwenye Har–Magedoni kuharibu sehemu inayobaki ya tengenezo la Shetani lililo duniani na, mwishowe, kutia Shetani na roho waovu wake ndani ya abiso. (Ufunuo 19:11–20:3) Ikiwa bado kuna wapakwa-mafuta wowote ambao wanaokoka wakiwa duniani, pasipo shaka wataingia ndani ya thawabu yao ya kimbingu upesi baada ya Kristo kukamilisha ushindi wake, wakajiunge na washiriki wenzao wa jamii ya bibi-arusi. Ndipo wakati uliowekwa na Mungu ufikapo, ndoa ya Mwana-Kondoo yaweza kutukia!
18. Zaburi ya 45 huthibitishaje mfuatano wa matukio kwa habari ya ndoa ya Mwana-Kondoo?
18 Simulizi la kiunabii katika Zaburi 45 (NW) linaeleza utaratibu wa matukio. Kwanza Mfalme aliyetawazwa apanda akawashinde maadui wake. (Mistari 1-7) Kisha ndoa yafanywa, bibi-arusi wa kimbingu akiwa anaandamana duniani na waandamani wake mabikira, umati mkubwa. (Mistari 8-15) Halafu ndoa yazaa matunda, aina ya binadamu iliyofufuliwa yainuliwa kwenye ukamilifu chini ya uangalizi wa “wana-wafalme katika dunia yote.” (Mistari 16, 17) Lo! ni baraka zilizoje zinazoandamana na ndoa ya Mwana-Kondoo!
Wenye Furaha ni Wale Walioalikwa
19. Ni ipi iliyo furaha ya nne ya zile saba katika Ufunuo, na ni nani wanaoshiriki furaha ii hii?
19 Sasa Yohana anarekodi furaha ya nne ya zile saba katika Ufunuo: “Na yeye [malaika ambaye amekuwa akifunulia Yohana vitu hivi] aniambia mimi: ‘Andika: Wenye furaha ni wale ambao wamealikwa kwenye mlo wa jioni wa ndoa ya Mwana-Kondoo.’ Pia, yeye aniambia mimi: ‘Hizi ndizo semi za kweli za Mungu.’” (Ufunuo 19:9, NW)e Wale walioalikwa kwenye “mlo wa jioni wa ndoa ya Mwana-Kondoo” ni washiriki wa jamii ya bibi-arusi. (Linga Mathayo 22:1-14.) Shirika la ki-bibi-arusi lililopakwa mafuta lashiriki furaha ya kuwa limepokea mwaliko huu. Walio wengi wa waalikwa tayari wamekwenda kwenye mbingu, mahali pa mlo wa jioni wa ki-ndoa. Wale ambao wangali duniani ni wenye furaha, vilevile, kwamba wao wana mwaliko huo. Mahali pao katika mlo wa jioni wa ki-ndoa kwenye mbingu pako salama. (Yohana 14:1-3; 1 Petro 1:3-9) Wakati wanapofufuliwa kwenda kwenye mbingu, ndipo bibi-arusi mzima, aliyeungamanika, ataanza na kuendelea kushiriki pamoja na Mwana-Kondoo katika ndoa yenye furaha ipitayo zote.
20. (a) Ni nini maana ya maneno haya: “Hizi ni semi za kweli za Mungu”? (b) Yohana aliathiriwaje na maneno ya malaika, na itikio la malaika lilikuwa nini?
20 Malaika huongeza kwamba “hizi ndizo semi za kweli za Mungu.” Neno hili “kweli” linatafsiri a·le·thi·nosʹ la Kigiriki na humaanisha “halisi” au “-a kutegemeka.” Kwa kuwa semi hizi kwa kweli zinatoka kwa Yehova, ni zenye kuaminika na zenye kutegemeka. (Linga 1 Yohana 4:1-3; Ufunuo 21:5; 22:6.) Akiwa mmoja aliyealikwa kwa karamu hiyo ya ndoa, lazima Yohana awe alijawa na shangwe kwa kusikia hilo na kwa kufikiria baraka zilizokuwa mbele kwa ajili ya jamii ya bibi-arusi. Kwa kweli, yeye alivutwa sana hivi kwamba malaika akalazimika kumshauri yeye, kama asimuliavyo Yohana: “Ndipo mimi nikaanguka chini mbele ya nyayo zake ili kuabudu yeye. Lakini yeye aniambia mimi: ‘Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa mwenzako tu na wa ndugu zako ambao wana kazi ya ushahidi kwa Yesu. Abudu Mungu.’”—Ufunuo 19:10a, NW.
21. (a) Ufunuo hufumbua nini kwa habari ya malaika? (b) Inawapasa Wakristo kuwa na mwelekeo gani kwa malaika?
21 Katika kitabu chote cha Ufunuo ushahidi wenye kutokeza umetolewa juu ya uaminifu na bidii-endelevu ya malaika. Wao wanahusika katika njia ya ukweli uliofunuliwa. (Ufunuo 1:1) Wao wanafanya kazi pamoja na wanadamu katika kuhubiri habari njema na kumimina tauni za ufananisho. (Ufunuo 14:6, 7; 16:1) Wao walipigana wakiwa upande wa Yesu katika kumtupa Shetani na malaika zake kutoka katika mbingu, na watapigana wakiwa upande wake tena kwenye Har–Magedoni. (Ufunuo 12:7; 19:11-14) Kweli kweli, wao wanaweza kuingia mbele za Yehova mwenyewe. (Mathayo 18:10; Ufunuo 15:6) Hata hivyo, wao ni watumwa wanyenyekevu tu wa Mungu. Hakuna nafasi katika ibada safi ya kuabudu malaika au hata kwa ibada ya kadiri, kuelekeza ibada kwa Mungu kupitia “mtakatifu” fulani au malaika. (Wakolosai 2:18) Wakristo wanaabudu Yehova pekee, wakifanya maombi yao kupitia jina la Yesu.—Yohana 14:12, 13.
Daraka la Yesu Katika Unabii
22. Malaika husema nini kwa Yohana, na maneno hayo yanamaanisha nini?
22 Ndipo malaika asema: “Kwa maana kutoa ushahidi kwa Yesu ndiko kunakovuvia kutoa unabii.” (Ufunuo 19:10b, NW) Jinsi gani hivyo? Hii humaanisha kwamba unabii wote uliovuviwa hutokezwa kwa sababu ya Yesu na daraka analotimiza katika makusudi ya Yehova. Unabii wa kwanza katika Biblia uliahidi kuja kwa mbegu. (Mwanzo 3:15) Yesu akawa Mbegu hiyo. Mafunuo yaliyofuata yalijenga jengo kubwa la ukweli wa kiunabii juu ya ahadi hii ya msingi. Mtume Petro alimwambia Kornelio asiye Myahudi mwenye kuamini: “Kwake yeye [Yesu] manabii wote hutoa ushahidi.” Yapata miaka 20 baadaye, mtume Paulo alisema: “Si kitu ahadi za Mungu ni nyingi kadiri gani, zote zimekuwa Ndiyo kwa njia yake yeye [Yesu].” (2 Wakorintho 1:20, NW) Baada ya miaka mingine 43, Yohana mwenyewe anatukumbusha: “Ukweli ulikuja kupitia Yesu Kristo.”—Yohana 1:17, NW.
23. Ni kwa nini cheo cha juu na mamlaka kubwa ya Yesu havipunguzi ibada tunayompa Yehova?
23 Je! hili lakengeusha kwa njia yoyote ibada tunayompa Yehova? La. Kumbuka maneno ya kutahadharisha ya malaika: “Abudu Mungu.” Yesu hajaribu kamwe kushindana na Yehova. (Wafilipi 2:6) Ni kweli, malaika wote huambiwa “wamsujudu” Yesu, na ni lazima uumbaji wote utambue cheo chake cha juu ili “kwa jina la Yesu kila goti lipigwe.” Lakini angalia, hili ni “kwa utukufu wa Mungu Baba” na kwa agizo lake. (Waebrania 1:6; Wafilipi 2:9-11) Yehova alimpa Yesu mamlaka yake kubwa, na kwa kukubali mamlaka hiyo, sisi tunampa Mungu utukufu. Ikiwa sisi tunakataa kutii utawala wa Yesu, ni sawa na kumkataa Yehova Mungu mwenyewe.—Zaburi 2:11, 12.
24. Ni matukio gani mawili yenye kupiga butaa ambayo sisi tunafikiria, na kwa hiyo ni maneno gani ambayo sisi tunapaswa kusema?
24 Hivyo, basi, acheni sisi kwa umoja tuseme yale maneno ya utangulizi ya Zaburi 146 mpaka 150: “Sifuni Yah, nyinyi watu!” Korasi ya Halleluyah na ingurume katika kutazamia ushindi wenye shangwe wa Yehova juu ya milki ya ulimwengu ya dini bandia ya Kibabuloni! Na shangwe na ienee pote ndoa ya Mwana-Kondoo ikaribiapo!
[Maelezo ya Chini]
a New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
b New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
c New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
d New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
e Ona pia Ufunuo 1:3; 14:13; 16:15, NW.
-
-
Sifuni Yah kwa Hukumu Zake!Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
[Picha katika ukurasa wa 273]
“Waraka kwa Sodoma na Gomora”
Chini ya hiki kichwa kikuu, Daily Telegraph ya London ya Novemba 12, 1987, iliripoti juu ya mjadala mbele ya Baraza Kuu la Kanisa la Uingereza. Huo ulitaka “Wakristo” wagoni-jinsia-moja waondolewe katika kanisa. Mwandikaji habari za nyusipepa Godfrey Barker alitaarifu hivi: “Askofu Mkuu wa Kantabari jana alionelea kwa huzuni: ‘Ikiwa [Mtakatifu] Paulo angaliandikia Kanisa la Uingereza waraka, sisi twaweza kuuliza kwa kufaa ingekuwa barua ya aina gani.’” Bw. Barker mwenyewe alitoa elezo hili: “Waraka kwa Sodoma na Gomora ndilo jibu,” na akaongeza: “Dakt. Runcie [askofu mkuu] aliwaza ingesomeka kama Warumi, [Sura ya] 1.”
Huyo mwandikaji alinukuu maneno ya Paulo kwenye Warumi 1:26-32: “Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu. . . . Wanaume nao . . . wakawakiana tamaa wakiyatenda yasiyopasa . . . wakijua sana hukumu ya haki ya Mungu, ya kwamba wayatendao hayo wamestahili mauti, wanatenda hayo, wala si hivyo tu, bali wanakubaliana nao wayatendao.” Yeye alimalizia: “[Mtakatifu] Paulo alihangaikia tu wale watu walio vitini. Tatizo la Dakt. Runcie ni wale watu walio katika mimbari.”
Kwa nini askofu mkuu ana tatizo kama hilo? Vichwa vikubwa katika Daily Mail ya London ya Oktoba 22, 1987, vilikuwa vimejulisha wazi: “‘Vikari mmoja kati ya watatu ni mgoni-jinsia-moja’ . . . Kampeni ya kuwatoa nje wagoni-jinsia-moja ‘ingefunga Kanisa la Uingereza.’” Ripoti hizo zilinukuu maneno ya “reverendi” katibu mkuu wa Chama cha Wakristo Wagoni-Jinsia-Moja wa Kike na wa Kiume akisema: “Ikiwa mjadala huu ungekubaliwa ungeangamiza Kanisa, na Askofu Mkuu wa Kantabari anajua hivyo. Kama tarakimu ya ujumla, sisi tunaitikadi kati ya asilimia 30 na 40 ya viongozi wa kidini wa Kanisa la Uingereza ni wagoni-jinsia-moja. Na wao ndio watu watendaji zaidi katika kuchangia huduma ya Kanisa.” Idadi zinazozidi kupungua za waenda-kanisani pasipo shaka kwa sehemu ni wonyesho wa kunyarafu huduma hiyo ya ugoni-jinsia-moja inayoongezeka sana.
Baraza kuu la kanisa liliamuaje? Idadi kubwa ya washiriki 388 (asilimia 95 ya viongozi wa kidini) ilipiga kura kwa kupendelea mjadala uliopunguzwa nguvu. Kuhusu hilo, The Economist ya Novemba 14, 1987, iliripoti hivi: “Kanisa la Uingereza linapinga mazoea ya ugoni-jinsia-moja, lakini si sana. Baraza kuu, bunge la kanisa, kwa kufikiria viongozi wa kidini wagoni-jinsia-moja, liliamua juma lililopita kwamba matendo ya ugoni-jinsia-moja, tofauti na uasherati na uzinzi, si dhambi: ‘yanapungukiwa tu kilicho bora’ kwamba ‘uhusiano wa ngono ni tendo la kujitoa kabisa linalofaa kufanywa ndani ya uhusiano wa ndoa wenye kufaa.’” Ikitofautisha msimamo wa Askofu Mkuu wa Kantabari na taarifa ya waziwazi ya mtume Paulo kwenye Warumi 1:26, 27, The Economist ilionyesha nukuu la maneno ya Paulo juu ya maelezo haya “[Mtakatifu] Paulo alijua aliyofikiri.”
Yesu Kristo pia alijua aliyofikiri na akayataarifu kwa maneno yaliyo wazi. Yeye alisema kwamba ‘ingevumilika zaidi kwa bara la Sodoma katika Siku ya Hukumu’ kuliko kwa wanadini walioupiga teke ujumbe wake. (Mathayo 11:23, 24, NW) Yesu alikuwa hapa akitumia mubaalagha (usemi uliotiwa chumvi) kuonyesha kwamba wale viongozi wa kidini waliokataa Mwana wa Mungu na fundisho lake walikuwa na hatia hata zaidi ya Wasodoma. Yuda 7 hutaarifu kwamba hao Wasodoma walipatwa na “adhabu ya kihukumu ya moto wa milele,” kumaanisha uharibifu wa milele. (Mathayo 25:41, 46) Basi, itakuwa kali kama nini hukumu ya wale wanaoitwa eti viongozi Wakristo ambao kwa upofu huongoza makundi yao yaliyopofushwa mbali na viwango vya juu vya kiadili vya Ufalme wa Mungu na kuwaingiza ndani ya njia endekevu, pujufu za ulimwengu huu! (Mathayo 15:14) Kuhusu dini bandia, Babuloni Mkubwa, sauti kutoka katika mbingu inaita kwa uharaka: “Ondokeni katika yeye, watu wangu, ikiwa nyinyi hamtaki kushiriki pamoja na yeye katika dhambi yake, na ikiwa nyinyi hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake.”—Ufunuo 18:2, 4, NW.
-