Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kristo Azungumza na Makutaniko
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Mei 15
    • Kristo Azungumza na Makutaniko

      “Haya ndiyo mambo asemayo yeye ashikaye zile nyota saba katika mkono wake wa kuume.”—UFUNUO 2:1.

      1, 2. Kwa nini tupendezwe na yale ambayo Kristo aliyaambia makutaniko saba huko Asia Ndogo?

      YESU KRISTO, Mwana-mzaliwa pekee wa Yehova, ndiye Kichwa cha kutaniko la Kikristo. Ili kutaniko la wafuasi wake watiwa-mafuta liendelee kuwa bila doa, Kristo analiongoza kwa kulipongeza na kulirekebisha. (Waefeso 5:21-27) Kwenye Ufunuo sura ya 2 na ya 3 tunaona jinsi Yesu alivyoyapongeza na kuyarekebisha makutaniko saba huko Asia Ndogo kupitia ujumbe wake wenye nguvu na upendo.

      2 Mtume Yohana alipewa maono kuhusu “siku ya Bwana” kabla ya kusikia maneno ya Yesu kwa yale makutaniko saba. (Ufunuo 1:10) “Siku” hiyo ilianza wakati Ufalme wa Kimesiya uliposimamishwa mwaka wa 1914. Kwa hiyo, yale ambayo Kristo aliyaambia makutaniko hayo ni muhimu sana siku hizi za mwisho. Kitia-moyo na ushauri wake hutusaidia kukabiliana na nyakati hizi hatari.—2 Timotheo 3:1-5.

      3. “Nyota,” “malaika,” na “vinara saba vya taa vya dhahabu” ambavyo mtume Yohana aliona, vinafananisha nini?

      3 Yohana alimwona Yesu Kristo aliyetukuzwa ambaye ‘anashika zile nyota saba katika mkono wake wa kuume’ na ‘anayetembea katikati ya vile vinara saba vya taa vya dhahabu,’ au makutaniko. “Nyota” hizo ni “wale malaika wa makutaniko saba.” (Ufunuo 1:20; 2:1) Wakati mwingine, nyota hufananisha malaika ambao ni viumbe wa roho, lakini Kristo hangetumia mwanadamu kuwaandikia viumbe wa roho ujumbe. Hivyo, kwa kufaa “nyota” hizo zinawakilisha waangalizi na mabaraza ya wazee watiwa-mafuta. Neno “malaika” linahusiana na kazi yao wakiwa wajumbe. Kwa sababu ya ukuzi wa tengenezo la Mungu, “msimamizi-nyumba mwaminifu” pia amewaweka rasmi wanaume wanaostahili miongoni mwa “kondoo wengine” wa Yesu, kuwa waangalizi.—Luka 12:42-44; Yohana 10:16.

      4. Wazee hunufaikaje kwa kusikiliza yale ambayo Kristo anayaambia makutaniko?

      4 “Nyota” hizo ziko kwenye mkono wa kuume wa Yesu, yaani, anaziongoza na kuzidhibiti, na zinapata ulinzi na kibali chake. Kwa hiyo, zinawajibika kwake. Kwa kusikiliza maneno yake kwa kila mojawapo ya yale makutaniko saba, wazee wa siku hizi wanapata kujua namna ya kushughulika na hali kama hizo. Bila shaka, Wakristo wote wanapaswa kumsikiliza Mwana wa Mungu. (Marko 9:7) Kwa hiyo, tunaweza kujifunza nini kwa kumsikiliza Kristo anapozungumza na makutaniko?

      Kwa Malaika Katika Efeso

      5. Efeso lilikuwa jiji la aina gani?

      5 Yesu alilipongeza na kulikaripia kutaniko la Efeso. (Soma Ufunuo 2:1-7.) Hekalu kubwa la mungu wa kike Artemi lilikuwa katika jiji hilo lililokuwa kituo cha dini na biashara yenye kusitawi, kwenye pwani ya magharibi ya Asia Ndogo. Ingawa ukosefu wa maadili, dini isiyo ya kweli, na uchawi ulienea sana katika jiji la Efeso, Mungu alibariki huduma ya mtume Paulo na wengine katika jiji hilo.—Matendo, sura ya 19.

      6. Ni katika njia gani Wakristo waaminifu-washikamanifu leo ni kama wale wa Efeso la kale?

      6 Kristo alilipongeza kutaniko la Efeso kwa kusema: “Mimi navijua vitendo vyako, na kazi yako ya jasho na uvumilivu, na kwamba huwezi kuhimili watu wabaya, na kwamba uliwatia kwenye jaribu wale ambao husema wao ni mitume, lakini wao sio, nawe uliwapata kuwa waongo.” Leo, makutaniko ya wafuasi wa kweli wa Yesu yana sifa hizohizo za kutenda mema, kufanya kazi kwa bidii, na kuvumilia. Hayastahimili ndugu wasio wa kweli wanaojifanya kuwa “mitume.” (2 Wakorintho 11:13, 26) Kama Waefeso, Wakristo waaminifu-washikamanifu leo ‘hawawezi kuwahimili watu wabaya.’ Kwa hiyo, ili kudumisha ibada ya Yehova ikiwa safi na kulinda kutaniko, wao hawashirikiani na waasi-imani wasiotubu.—Wagalatia 2:4, 5; 2 Yohana 8-11.

      7, 8. Kutaniko la Efeso lilikuwa na tatizo gani kubwa, nasi tunawezaje kushughulika na hali kama hiyo?

      7 Hata hivyo, Wakristo huko Efeso walikuwa na tatizo kubwa. “Nashika hili dhidi yako,” akasema Yesu, “kwamba umeacha upendo uliokuwa nao hapo kwanza.” Washiriki wa kutaniko walihitaji kuchochea tena upendo waliokuwa nao kwa Yehova hapo kwanza. (Marko 12:28-30; Waefeso 2:4; 5:1, 2) Sote tunapaswa kuwa waangalifu tusipoteze upendo tuliokuwa nao kwa Mungu hapo kwanza. (3 Yohana 3) Namna gani ikiwa tunatanguliza tamaa ya kuwa matajiri au kufuatia anasa maishani? (1 Timotheo 4:8; 6:9, 10) Badala ya kuwa na tamaa kama hizo, tunapaswa kuomba msaada wa Mungu kwa bidii ili kusitawisha upendo mwingi kwa Yehova na kushukuru kwa yale ambayo yeye na Mwana wake wametufanyia.—1 Yohana 4:10, 16.

      8 Kristo aliwahimiza Waefeso hivi: “Kumbuka ni kutoka katika nini umeanguka, nawe tubu na kufanya vitendo vya kwanza.” Namna gani kama hawangefanya hivyo? “Usipofanya hivyo,” akasema Yesu, “Mimi ninakuja kwako, nami hakika nitaondoa kinara chako cha taa kutoka mahali pacho.” Iwapo kondoo wote wangepoteza upendo waliokuwa nao hapo kwanza, kile ‘kinara cha taa,’ au kutaniko halingeendelea kuwapo. Kwa hiyo, tukiwa Wakristo wenye bidii na tujitahidi sana kuona kwamba kutaniko linaendelea kung’aa kiroho.—Mathayo 5:14-16.

      9. Tunapaswa kuyaonaje mafarakano?

      9 Waefeso walistahili kupongezwa kwa sababu walichukia “vitendo vya farakano la Nikolausi.” Mbali na yale yanayosemwa katika kitabu cha Ufunuo, hakuna habari hususa inayoonyesha chanzo, mafundisho, na mazoea ya farakano hilo. Hata hivyo, kwa kuwa Yesu alishutumu desturi ya kufuata wanadamu, tunapaswa kuendelea kuchukia mafarakano kama walivyofanya Wakristo wa Efeso.—Mathayo 23:10.

      10. Wale wanaosikiliza yale ambayo roho husema watapata nini?

      10 Kristo alisema, “Acheni yeye aliye na sikio asikie lile ambalo roho huyaambia makutaniko.” Alipokuwa duniani, Yesu alizungumza kwa kuongozwa na roho ya Mungu. (Isaya 61:1; Luka 4:16-21) Kwa hiyo, tunapaswa kusikiliza yale ambayo Mungu anasema sasa kupitia Yesu akitumia roho takatifu. Yesu alitoa ahadi hii akiongozwa na roho: “Kwake ambaye hushinda hakika nitamruhusu kula kutoka katika mti wa uhai, ambao umo katika paradiso ya Mungu.” Kwa watiwa-mafuta wanaosikiliza yale ambayo roho inasema, hiyo inamaanisha kutoweza kufa katika “paradiso ya Mungu” ya kimbingu, au kuwa mbele za Yehova. “Umati mkubwa” ambao pia husikiliza yale ambayo roho inasema, watafurahia kuishi katika dunia paradiso ambapo watakunywa kutoka kwa “mto wa maji ya uhai” na kuponywa kwa ‘majani ya miti’ iliyo kandokando ya mto huo.—Ufunuo 7:9; 22:1, 2; Luka 23:43.

      11. Tunaweza kuwachocheaje wengine wampende Yehova?

      11 Waefeso walikuwa wamepoteza upendo waliokuwa nao hapo kwanza, lakini namna gani hali kama hiyo ikianza kutokea kutanikoni? Kila mmoja wetu na awachochee wengine wampende Yehova kwa kuzungumzia njia zake za upendo. Tunaweza kuonyesha shukrani zetu kwa upendo ambao Mungu alionyesha kwa kutoa fidia kupitia Mwana wake mpendwa. (Yohana 3:16; Waroma 5:8) Inapofaa, tunaweza kutaja upendo wa Mungu tunapotoa maelezo ama tunapokuwa na migawo kwenye mikutano. Tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kulisifu jina lake katika huduma ya Kikristo. (Zaburi 145:10-13) Naam, maneno na matendo yetu yanaweza kuchochea tena au kuimarisha sana upendo ambao kutaniko lilikuwa nao hapo kwanza.

      Kwa Malaika Katika Smirna

      12. Historia hufunua nini kuhusu Smirna na mazoea yake ya kidini?

      12 Kutaniko la Smirna lilipongezwa na Kristo, aliye “‘Wa-Kwanza na Wa-Mwisho,’ aliyekuwa mfu akaja kwenye uhai tena” kupitia ufufuo. (Soma Ufunuo 2:8-11.) Jiji la Smirna (ambalo sasa ni Izmir, Uturuki) lilijengwa kwenye pwani ya magharibi ya Asia Ndogo. Wagiriki walihamia jiji hilo lakini likaharibiwa na Walidia wapata mwaka wa 580 K.W.K. Wale waliotawala baada ya Aleksanda Mkuu walilijenga tena jiji hilo katika sehemu tofauti. Hivyo jiji la Smirna likawa sehemu ya mkoa wa Asia wa milki ya Roma, na kituo cha biashara yenye kusitawi kilichokuwa maarufu kwa majengo yake ya umma yenye kuvutia. Hekalu la Tiberio Kaisaria lililokuwa katika jiji hilo lililifanya liwe kituo cha ibada ya maliki. Waabudu walipaswa kufukiza kiasi kidogo cha uvumba na kusema “Kaisari ni Bwana.” Wakristo hawangeweza kufanya hivyo kwa sababu ‘Yesu ndiye Bwana’ wao. Hivyo, walipatwa na dhiki.—Waroma 10:9.

      13. Ingawa Wakristo wa Smirna walikuwa maskini kimwili, walikuwa matajiri katika maana gani?

      13 Mbali na dhiki, Wakristo wa Smirna walistahimili umaskini na labda walipatwa na magumu ya kiuchumi kwa sababu hawangeshiriki katika ibada ya maliki. Watumishi wa Yehova leo hupatwa na majaribu kama hayo. (Ufunuo 13:16, 17) Ingawa wale walio kama Wakristo wa Smirna ni maskini kimwili, wao ni matajiri kiroho, na hilo ndilo jambo muhimu zaidi!—Mithali 10:22; 3 Yohana 2.

      14, 15. Andiko la Ufunuo 2:10 linaweza kuwafariji watiwa-mafuta jinsi gani?

      14 Wayahudi wengi huko Smirna walikuwa “sinagogi la Shetani” kwa sababu walifuata mapokeo yaliyo kinyume cha Maandiko, wakamkataa Mwana wa Mungu, na kuwakufuru wafuasi wake waliozaliwa kwa roho. (Waroma 2:28, 29) Watiwa-mafuta wanaweza kufarijiwa sana na maneno haya ya Kristo: “Usiogope mambo uliyo karibu kuteseka. Tazama! Ibilisi atafuliza kutupa baadhi yenu ndani ya gereza ili mpate kutiwa kwenye jaribu kikamili, na kwamba mpate kuwa na dhiki siku kumi. Jithibitishe mwenyewe kuwa mwaminifu hata kufikia kifo, nami hakika nitakupa taji la uhai.”—Ufunuo 2:10.

      15 Yesu hakuogopa kufa kwa kutetea enzi kuu ya Yehova. (Wafilipi 2:5-8) Ingawa sasa Shetani anapigana vita na mabaki ya watiwa-mafuta, wao hawaogopi mateso ambayo lazima yawapate wakiwa kikundi, ambayo ni dhiki, kufungwa gerezani, au kuuawa kikatili. (Ufunuo 12:17) Wataushinda ulimwengu. Na badala ya shada la maua linalonyauka ambalo lilivaliwa na washindi kama taji katika michezo ya wapagani, Kristo anawaahidi watiwa-mafuta watakaofufuliwa “taji la uhai” mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. Kwa kweli hiyo ni zawadi yenye thamani kubwa kama nini!

      16. Tunapaswa kukazia fikira suala gani iwapo tunashirikiana na kutaniko kama la Smirna la kale?

      16 Namna gani, ikiwa tunashirikiana na kutaniko kama la Smirna la kale, iwe sisi tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani? Basi na tuwasaidie waamini wenzetu wakazie fikira sababu kuu inayofanya Mungu aruhusu mnyanyaso—ambayo ni suala kuhusu ni nani aliye na haki ya kutawala ulimwengu. Kila Shahidi wa Yehova anayeendelea kushika uaminifu-maadili, huthibitisha Shetani kuwa mwongo na huonyesha kwamba hata mwanadamu anayenyanyaswa, anaweza kutetea kwa uimara haki ya Mungu ya kutawala akiwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. (Mithali 27:11) Na tuwatie moyo Wakristo wengine wavumilie mateso na hivyo kuendelea kuwa na “pendeleo la kumtolea [Yehova] utumishi mtakatifu bila hofu kwa uaminifu-mshikamanifu na uadilifu mbele yake siku zetu zote”—hata milele.—Luka 1:68, 69, 74, 75.

      Kwa Malaika Katika Pergamamu

      17, 18. Pergamamu lilikuwa kituo cha ibada ya aina gani, na ni nini kingeweza kumpata mtu aliyekataa kushiriki ibada hiyo ya sanamu?

      17 Kutaniko la Pergamamu lilipongezwa na kurekebishwa pia. (Soma Ufunuo 2:12-17.) Ibada ya sanamu ilikuwa imeenea sana katika jiji la Pergamamu, lililokuwa umbali wa kilometa 80 kaskazini ya Smirna. Inaonekana kwamba mamajusi (watabiri wanaotumia nyota) Wakaldayo walikimbilia huko kutoka Babiloni. Wagonjwa walimiminika katika hekalu maarufu la Asclepius, mungu bandia wa uponyaji huko Pergamamu. Jiji hilo lililokuwa na hekalu ambalo lilitumiwa kwa ajili ya ibada ya Kaisari Augusto, limetajwa kuwa “kituo kikuu cha madhehebu ya kifalme katika milki ya awali.”—Encyclopædia Britannica, 1959, Buku la 17, ukurasa wa 507.

      18 Huko Pergamamu kulikuwa na madhabahu yaliyotumiwa kwa ajili ya ibada ya Zeusi. Jiji hilo pia lilikuwa kituo cha ibada iliyochochewa na Ibilisi ya kuwaabudu wanadamu. Si ajabu kwamba kutaniko la Pergamamu lilisemekana kuwa mahali ambapo “kiti cha ufalme cha Shetani” kilikuwa! Mteteaji wa enzi kuu ya Yehova angeweza kuuawa kama angekataa kumwabudu maliki. Ulimwengu bado uko chini ya mamlaka ya Ibilisi, na sasa nembo za kitaifa zinaabudiwa. (1 Yohana 5:19) Tangu karne ya kwanza hadi sasa, Wakristo wengi waaminifu wamefia imani, kama yule ambaye Kristo alimwita “Antipasi, shahidi wangu, aliye mwaminifu, aliyeuawa kando yenu.” Bila shaka, Yehova Mungu na Yesu Kristo wanawakumbuka watumishi hao waaminifu-washikamanifu.—1 Yohana 5:21.

      19. Balaamu alifanya nini, nao Wakristo wote wanapaswa kujihadhari na nini?

      19 Kristo pia alizungumza kuhusu “ufundishaji wa Balaamu.” Balaamu, nabii asiye wa kweli, alijaribu kuwalaani Waisraeli kwa sababu ya pupa ya vitu vya kimwili. Mungu alipogeuza laana yake ikawa baraka, Balaamu alishirikiana na Mfalme Balaki wa Moabu na kuwashawishi Waisraeli wengi washiriki katika ibada ya sanamu na mwenendo mchafu kingono. Wazee Wakristo wanahitaji kuwa imara kwa ajili ya uadilifu kama Finehasi, ambaye alipinga mbinu za Balaamu. (Hesabu 22:1–25:15; 2 Petro 2:15, 16; Yuda 11) Kwa kweli, Wakristo wote wanapaswa kujihadhari na ibada ya sanamu na kupenya kwa mwenendo mchafu kingono kutanikoni.—Yuda 3, 4.

      20. Ikiwa Mkristo yeyote anaanza kuwa na maoni ya uasi-imani, anapaswa kufanya nini?

      20 Kutaniko la Pergamamu lilikuwa katika hatari kubwa kwa sababu liliwaruhusu wale ‘walioshika sana ufundishaji wa farakano la Nikolausi’ waendelee kuwa miongoni mwake. Kristo aliliambia hivi kutaniko hilo: ‘Tubu. Usipofanya hivyo, mimi ninakuja kwako upesi, nami hakika nitapiga vita nawe kwa ule upanga mrefu wa kinywa changu.’ Wanaounga mkono mafarakano wanataka kuwadhuru Wakristo kiroho, nao wale walio na nia ya kuendeleza migawanyiko na mafarakano hawataurithi Ufalme wa Mungu. (Waroma 16:17, 18; 1 Wakorintho 1:10; Wagalatia 5:19-21) Ikiwa Mkristo yeyote anaanza kuwa na maoni ya uasi-imani na anataka kuyaeneza, maneno ya Kristo yanapaswa kuwa onyo kwake! Ili asije akapatwa na msiba, anapaswa kutubu na kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa wazee wa kutaniko. (Yakobo 5:13-18) Ni muhimu kufanya hivyo bila kukawia, kwa kuwa Yesu anakuja upesi kutekeleza hukumu.

      21, 22. Ni nani wanaokula “mana iliyofichwa,” nayo inawakilisha nini?

      21 Wakristo watiwa-mafuta waaminifu na waandamani wao waaminifu-washikamanifu hawapaswi kuogopa hukumu inayokuja. Wote wanaosikiliza ushauri wa Yesu unaotolewa kwa mwongozo wa roho takatifu ya Mungu watabarikiwa. Kwa mfano, watiwa-mafuta wanaoshinda ulimwengu wataalikwa kula kiasi fulani cha “mana iliyofichwa” na watapewa “kijiwe cheupe cha mviringo” chenye “jina jipya.”

      22 Waisraeli walipokuwa wakitangatanga nyikani kwa miaka 40, Mungu aliwapa mana kuwa chakula chao. Waliweka kiasi fulani cha “mkate” huo katika mtungi mdogo wa dhahabu uliokuwa ndani ya sanduku la agano na hivyo ukafichwa katika Patakatifu Zaidi pa tabenakulo, ambapo nuru ya kimuujiza iliwakilisha kuwapo kwa Yehova. (Kutoka 16:14, 15, 23, 26, 33; 26:34; Waebrania 9:3, 4) Hakuna aliyeruhusiwa kula mana hiyo iliyofichwa. Hata hivyo, wanapofufuliwa, wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta huvaa hali ya kutoweza kufa inayowakilishwa na kula “mana iliyofichwa.”—1 Wakorintho 15:53-57.

      23. “Kijiwe cheupe cha mviringo” na “jina jipya” humaanisha nini?

      23 Katika mahakama za Roma, kijiwe cheusi cha mviringo kilimaanisha kifungo, ilhali kijiwe cheupe kilimaanisha kuachiliwa huru. Yesu anapowapa “kijiwe cheupe cha mviringo” Wakristo watiwa-mafuta wanaoshinda, hiyo inamaanisha kwamba anawaona kuwa wasio na hatia, waliotakata, na safi. Kwa kuwa Waroma pia walitumia vijiwe vya mviringo kama tiketi ya kuingia kwenye sherehe muhimu, huenda “kijiwe cheupe cha mviringo” kikamaanisha kualikwa kwa mtiwa-mafuta mbinguni wakati wa ndoa ya Mwana-kondoo. (Ufunuo 19:7-9) Yaelekea “jina jipya” linamaanisha pendeleo la kuungana na Yesu wakiwa warithi-washirika katika Ufalme wa mbinguni. Bila shaka, mambo hayo yote huwatia moyo watiwa-mafuta na pia wale wanaoshirikiana nao kumtumikia Yehova, ambao wana tumaini la kuishi katika paradiso duniani.

      24. Tunapaswa kuchukua msimamo gani kuhusiana na uasi-imani?

      24 Ni jambo la hekima kukumbuka kwamba waasi-imani walihatarisha kutaniko la Pergamamu. Iwapo hali kama hiyo inahatarisha hali njema ya kiroho ya kutaniko tunaloshirikiana nalo, na tukatae katakata uasi-imani na kuendelea kutembea katika kweli. (Yohana 8:32, 44; 3 Yohana 4) Kwa kuwa walimu wa uwongo au watu fulani wenye mwelekeo wa kuasi imani wanaweza kupotosha kutaniko zima, ni lazima tudumishe msimamo imara dhidi ya uasi-imani, na tusiruhusu kamwe ushawishi mwovu utuzuie kuitii kweli.—Wagalatia 5:7-12; 2 Yohana 8-11.

      25. Makala inayofuata itazungumzia ujumbe wa Kristo kwa makutaniko gani?

      25 Tumechochewa kama nini kuzungumzia maneno ya pongezi na ushauri ambao Yesu Kristo aliyetukuzwa alitoa kwa makutaniko matatu kati ya yale saba huko Asia Ndogo! Hata hivyo, Yesu akiongozwa na roho takatifu ana mengi pia ya kuyaambia yale makutaniko manne yaliyosalia. Ujumbe huo, kwa makutaniko ya Thiatira, Sardisi, Filadelfia, na Laodikia utazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Sikia Yale Ambayo Roho Husema!
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Mei 15
    • Sikia Yale Ambayo Roho Husema!

      “Acheni yeye aliye na sikio asikie lile ambalo roho huyaambia makutaniko.”—UFUNUO 3:22.

      1, 2. Ni ushauri gani unaorudiwa katika kila ujumbe ambao Yesu anatoa kwa makutaniko saba yanayotajwa katika Ufunuo?

      NI LAZIMA watumishi wa Yehova wasikilize maneno ambayo Yesu Kristo aliongozwa na roho kuyaambia yale makutaniko saba yanayotajwa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Kwa kweli, kila ujumbe una ushauri huu: “Acheni yeye aliye na sikio asikie lile ambalo roho huyaambia makutaniko.”—Ufunuo 2:7, 11, 17, 29; 3: 6, 13, 22.

      2 Tayari tumezungumzia ujumbe wa Yesu kwa malaika, au waangalizi wa Efeso, Smirna, na Pergamamu. Tunawezaje kunufaika na yale ambayo Yesu aliongozwa na roho takatifu kuyaambia yale makutaniko mengine manne?

      Kwa Malaika Katika Thiatira

      3. Jiji la Thiatira lilikuwa wapi, na lilikuwa maarufu kwa kutengeneza nini?

      3 “Mwana wa Mungu” analipongeza na kulikaripia kutaniko la Thiatira. (Soma Ufunuo 2:18-29.) Jiji la Thiatira (ambalo sasa ni Akhisari) lilikuwa limejengwa kwenye kijito cha Mto Gediz (Hermus la kale) magharibi mwa Asia Ndogo. Jiji hilo lilikuwa maarufu kwa utengenezaji wa vitu vya sanaa. Watengenezaji-rangi wa jiji hilo walitumia mizizi ya mmea fulani kutengeneza rangi nyekundu au ya zambarau iliyokuwa maarufu. Lidia, aliyegeuza imani na kuwa Mkristo wakati Paulo alipotembelea jiji la Filipi huko Ugiriki, alikuwa “muuzaji wa rangi ya zambarau wa jiji la Thiatira.”—Matendo 16:12-15.

      4. Kutaniko la Thiatira lilipongezwa kwa jambo gani?

      4 Yesu analipongeza kutaniko la Thiatira kwa matendo yake mema, upendo, imani, uvumilivu, na kwa huduma yake. Kwa kweli, ‘vitendo vyake vya juzijuzi vilizidi vile vya hapo zamani.’ Hata kama tumekuwa na sifa nzuri, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu maadili yetu.

      5-7. (a) Ni nani yule “mwanamke Yezebeli,” na ni nini ambacho kingefanywa kuhusu ushawishi wake? (b) Ujumbe wa Kristo kwa kutaniko la Thiatira huwasaidia wanawake wanaomwogopa Mungu wafanye nini?

      5 Kutaniko la Thiatira lilikuwa likivumilia ibada ya sanamu, mafundisho ya uwongo, na mwenendo mchafu kingono. Miongoni mwao mlikuwa na “mwanamke Yezebeli”—labda kikundi cha wanawake waliokuwa na tabia kama za Malkia Yezebeli mwovu wa Ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Wasomi fulani wanadokeza kwamba ‘manabii wa kike’ wa Thiatira walijaribu kuwashawishi Wakristo waabudu miungu ya kiume na ya kike ya shirika fulani la wanabiashara, na pia washiriki katika sherehe zenye vyakula vilivyotolewa kwa sanamu. Tusiruhusu mwanamke yeyote anayejisingizia kuwa nabii awapotoshe wengine katika kutaniko la Kikristo leo!

      6 Kristo alikuwa ‘karibu kumtupa mwanamke huyo Yezebeli aingie katika kitanda cha ugonjwa, na wale wanaofanya uzinzi pamoja naye katika dhiki kubwa, isipokuwa watubu vitendo vyake.’ Waangalizi wanapaswa kukataa kabisa mafundisho hayo maovu na ushawishi wake, na si lazima Mkristo afanye uasherati halisi au wa kiroho, au aabudu sanamu ili atambue kwamba “mambo yenye kina kirefu ya Shetani” ni maovu kabisa. Tukisikiliza onyo la Yesu, ‘tutashika sana lile tulilo nalo,’ na dhambi haitatutawala. Watiwa-mafuta waliofufuliwa wanapokea “mamlaka juu ya mataifa” kwa sababu wamekataa mazoea, uchu, na miradi isiyo ya kimungu, nao watajiunga na Kristo kuyavunja mataifa vipande-vipande. Makutaniko leo yana nyota za mfano, na watiwa-mafuta watapewa “nyota nyangavu ya asubuhi,” ambayo ni Bwana-arusi, Yesu Kristo, wanapofufuliwa kwenda mbinguni.—Ufunuo 22:16.

      7 Kutaniko la Thiatira lilionywa lisivumilie ushawishi mwovu wa wanawake wenye kuasi imani. Ujumbe ambao Kristo aliongozwa na roho kutoa kwa kutaniko huwasaidia wanawake wanaomwogopa Mungu watosheke na mahali pao katika mpango wa Mungu leo. Hawajaribu kuwa na mamlaka juu ya wanaume wala kuwashawishi akina ndugu wafanye uasherati halisi au wa kiroho. (1 Timotheo 2:12) Badala yake, wanawake hao humletea Mungu sifa kwa kuweka kielelezo chema katika matendo na katika utumishi wao. (Zaburi 68:11; 1 Petro 3:1-6) Ikiwa kutaniko litalinda lilicho nacho—mafundisho na mwenendo safi, na pia utumishi wa Ufalme wanaouthamini sana—Kristo atakuja kulibariki wala si kuliangamiza.

      Kwa Malaika Katika Sardisi

      8. (a) Jiji la Sardisi lilikuwa wapi, na ni mambo gani yanayotajwa kulihusu? (b) Kwa nini kutaniko la Sardisi lilihitaji msaada?

      8 Kutaniko la Sardisi lilihitaji msaada haraka kwa sababu lilikuwa limekufa kiroho. (Soma Ufunuo 3:1-6.) Jiji la Sardisi lenye usitawi lilikuwa umbali wa kilometa 50 kusini ya Thiatira. Jiji hilo lilikuwa na utajiri kwa sababu ya biashara, mazao mengi ya kilimo, na utengenezaji wa mavazi ya sufu na mazulia, na wakati mmoja lilikuwa na watu wapatao 50,000. Kulingana na mwanahistoria Josephus, jiji la Sardisi lilikuwa na wakazi wengi sana Wayahudi katika karne ya kwanza K.W.K. Kati ya magofu ya jiji hilo kuna sinagogi na hekalu la mungu wa kike Artemi wa Efeso.

      9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa utumishi wetu ni wa kidesturi tu?

      9 Kristo alimwambia malaika wa kutaniko la Sardisi hivi: “Mimi navijua vitendo vyako, kwamba una jina kuwa uko hai, lakini wewe ni mfu.” Iwapo tunajulikana kuwa watu wa kiroho lakini hatujali sana mapendeleo ya Kikristo, basi utumishi wetu ni wa kidesturi tu na tuko “tayari kufa” kiroho. Kwa hiyo, tunahitaji ‘kuendelea kuzingatia akilini jinsi tunavyopokea na kusikia’ ujumbe wa Ufalme, na tunapaswa kuchochea tena jitihada zetu katika utumishi mtakatifu. Bila shaka tunapaswa kuanza kushiriki kwa moyo wote katika mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Kristo alionya kutaniko la Sardisi hivi: “Usipoamka, nitakuja kama mwizi, na hutajua hata kidogo ni saa gani nitakapokuja juu yako.” Namna gani leo? Hivi karibuni itatubidi tutoe hesabu kwa matendo yetu.

      10. Hata katika hali kama za Sardisi, huenda Wakristo wachache wamefaulu kufanya nini?

      10 Hata katika hali kama za Sardisi, huenda kuna wachache ambao ‘hawayatii unajisi mavazi yao ya nje, nao wanaweza kutembea pamoja na Kristo wakiwa wamevaa mavazi meupe, kwa sababu yanastahili.’ Nyakati zote mwenendo wao huwatambulisha kuwa Wakristo nao hudumu wakiwa safi bila kutiwa doa la kiroho au la kiadili na ulimwengu huu. (Yakobo 1:27) Hivyo, Yesu ‘hakika hatayafuta kwa vyovyote majina yao kutoka katika kitabu cha uhai, bali hakika atayakiri majina yao mbele ya Baba yake na mbele ya malaika.’ Wakiwa wametangazwa kuwa wanastahili kutembea pamoja na Kristo, watiwa-mafuta ambao ni jamii ya bibi-arusi watavikwa kitani nyangavu, safi, na bora ambacho hufananisha matendo ya uadilifu ya watakatifu wa Mungu. (Ufunuo 19:8) Mapendeleo mazuri ya utumishi watakayopata huko mbinguni huwachochea kuushinda ulimwengu huu. Wale wanaotarajia kuishi milele duniani watabarikiwa pia. Majina yao pia yanaandikwa katika kitabu cha uhai.

      11. Tufanyeje ikiwa tumeanza kusinzia kiroho?

      11 Hakuna mmoja wetu ambaye angependa kuwa katika hali yenye kusikitisha kiroho kama ile ya kutaniko la Sardisi. Lakini namna gani tukitambua kwamba tumeanza kusinzia kiroho? Tunapaswa kuchukua hatua mara moja kwa manufaa yetu wenyewe. Namna gani ikiwa tunavutiwa na njia zisizo za kimungu au tumeanza kulegea katika uhudhuriaji wetu wa mikutano au huduma yetu? Acheni tusali kwa bidii kupata msaada wa Yehova. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Kusoma na kujifunza Biblia kila siku pamoja na vichapo vya “msimamizi-nyumba mwaminifu” kutatusaidia kuendelea kuwa macho kiroho. (Luka 12:42-44) Kisha tutakuwa kama wale waliokuwa Sardisi ambao walipata kibali cha Kristo, na tutawatia moyo waamini wenzetu.

      Kwa Malaika Katika Filadelfia

      12. Unaweza kufafanuaje hali ya kiroho katika Filadelfia la kale?

      12 Yesu alilipongeza kutaniko la Filadelfia. (Soma Ufunuo 3:7-13.) Jiji la Filadelfia (ambalo sasa ni Alasehiri) lilikuwa kituo chenye ufanisi katika eneo ambapo divai ilitengenezwa, huko magharibi mwa Asia Ndogo. Hata Dionisio, mungu mkuu wa jiji hilo, alikuwa mungu wa divai. Yaonekana Wayahudi wa Filadelfia walishindwa kuwashawishi Wakristo Wayahudi huko kudumisha au kurudia desturi fulani za Sheria ya Musa.

      13. Kristo ametumiaje “ufunguo wa Daudi”?

      13 Kristo ‘ana ufunguo wa Daudi,’ na hivyo amekabidhiwa mambo yote yanayohusiana na Ufalme na usimamizi wa nyumba ya imani. (Isaya 22:22; Luka 1:32) Yesu alitumia ufunguo huo kuwawezesha Wakristo wa Filadelfia la kale na kwingineko kupata mapendeleo na migawo inayohusiana na Ufalme. Tangu mwaka wa 1919, amemfungulia “mlango mkubwa” “msimamizi-nyumba mwaminifu” ambao unaongoza kwenye kazi ya kuhubiri Ufalme na hakuna mpinzani yeyote anayeweza kuufunga. (1 Wakorintho 16:9; Wakolosai 4:2-4) Bila shaka, mlango unaoongoza kwenye mapendeleo ya Ufalme umefungwa kwa wale wa “sinagogi la Shetani,” kwa kuwa wao si Waisraeli wa kiroho.

      14. (a) Yesu aliliahidi nini kutaniko la Filadelfia? (b) Tunawezaje kuepuka kuanguka katika “saa ya jaribu”?

      14 Yesu aliwaahidi Wakristo wa Filadelfia la kale hivi: “Kwa sababu ulitunza neno juu ya uvumilivu wangu, hakika mimi pia nitakutunza utoke katika saa ya jaribu, itakayokuja juu ya dunia nzima inayokaliwa, ili kutia jaribu juu ya wale wanaokaa juu ya dunia.” Tunapohubiri tunahitaji kuwa wavumilivu kama Yesu. Yeye hakukubali ashindwe na maadui bali aliendelea kufanya mapenzi ya Baba yake. Kwa hiyo, Kristo alifufuliwa na kupewa uhai usioweza kufa huko mbinguni. Tukishikamana sana na uamuzi wetu wa kumwabudu Yehova na kuunga mkono Ufalme kwa kuhubiri habari njema, hatutaanguka wakati huu wa jaribu, yaani, “saa ya jaribu.” ‘Tutafuliza kushika sana lile tulilo nalo’ kutoka kwa Kristo kwa kujitahidi kuendeleza mambo yanayohusu Ufalme. Watiwa-mafuta wakifanya hivyo watapata taji la kimbingu lenye thamani kubwa, nao waandamani wao washikamanifu watapata uhai wa milele duniani.

      15. Wale watakaokuwa “nguzo katika hekalu la Mungu” wanapaswa kufanya nini?

      15 Kristo aendelea kusema: “Yeye ashindaye—hakika mimi nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, . . . nami hakika nitaandika juu yake jina la Mungu wangu na jina la jiji la Mungu wangu, Yerusalemu jipya lishukalo kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu jipya.” Waangalizi watiwa-mafuta wanapaswa kutetea ibada ya kweli. Ni lazima wadumishe sifa zinazowastahilisha kuwa washiriki wa “Yerusalemu jipya” kwa kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na kuendelea kuwa safi kiroho. Hilo ni muhimu ikiwa wanataka kuwa nguzo katika hekalu la kimbingu lililotukuka na kuwa na jina la jiji la Mungu wakiwa raia wa kimbingu na pia kuwa na jina la Kristo wakiwa bibi-arusi wake. Na bila shaka, lazima wawe na masikio ambayo ‘yanasikia lile ambalo roho huyaambia makutaniko.’

      Kwa Malaika Katika Laodikia

      16. Ni mambo gani yanayotajwa kuhusu Laodikia?

      16 Kristo alilikaripia kutaniko la Laodikia lenye uvuguvugu. (Soma Ufunuo 3:14-22.) Jiji la Laodikia lilikuwa umbali wa kilometa 150 mashariki ya Efeso kwenye makutano ya njia kuu zilizotumiwa na wafanyabiashara katika bonde lenye rutuba la Mto Lycus. Jiji hilo lilikuwa limesitawi sana kiviwanda na lilikuwa na benki nyingi. Mavazi yaliyotengenezwa kwa sufu nyeusi iliyopatikana katika eneo hilo yalikuwa maarufu. Jiji la Laodikia lilikuwa na chuo mashuhuri cha tiba, na huenda dawa ya macho ya unga-unga ilitengenezwa huko. Asclepius, mungu wa dawa, alikuwa mmoja wa miungu mikuu ya jiji hilo. Yaelekea Wayahudi wengi waliishi Laodikia na yaonekana baadhi yao walikuwa matajiri sana.

      17. Kwa nini watu wa Laodikia walikaripiwa?

      17 Akizungumza na kutaniko la Laodikia kupitia “malaika,” Yesu anasema kwa mamlaka akiwa “shahidi mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Wakolosai 1:13-16) Watu wa Laodikia walikaripiwa kwa kuwa walikuwa “si baridi wala moto” kiroho. Kristo angewatapika kutoka kinywani mwake kwa sababu walikuwa vuguvugu. Haikuwa vigumu kwao kuelewa maneno ya Kristo. Eneo la Hierapolisi lililokuwa karibu lilikuwa na chemchemi za maji moto, na Kolosai lilikuwa na maji baridi. Kwa kuwa ilikuwa lazima kutumia mabomba ili kupeleka maji huko Laodikia, jiji lililokuwa mbali, yaelekea maji hayo yalifika huko yakiwa vuguvugu. Lakini katika sehemu nyingine maji hayo yalipita kwenye mfereji. Yalipokaribia Laodikia, yalipita kwenye mawe yaliyotobolewa ambayo yalikuwa yameunganishwa kwa saruji.

      18, 19. Leo Wakristo walio kama wa Laodikia wanaweza kusaidiwaje?

      18 Leo watu walio kama watu wa Laodikia hawana joto lenye kuchochea wala baridi yenye kuburudisha. Kama maji yenye uvuguvugu, watatapikwa kutoka kinywani! Yesu hataki wawe wasemaji wake wakiwa ‘mabalozi watiwa-mafuta walio badala ya Kristo.’ (2 Wakorintho 5:20) Wasipotubu watapoteza pendeleo lao la kuwa watangazaji wa Ufalme. Watu wa Laodikia walitafuta utajiri wa kimwili na ‘hawakujua walikuwa wenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na vipofu na uchi.’ Ili kumaliza umaskini wao wa kiroho, upofu, na uchi, leo watu wowote walio kama wale wa Laodikia, wanahitaji kununua kutoka kwa Kristo “dhahabu iliyosafishwa” ambayo ni imani iliyojaribiwa. Wanahitaji pia kununua “mavazi meupe ya nje” ya uadilifu na “dawa ya macho” ambayo huboresha uwezo wa kuona mambo kwa njia ya kiroho. Waangalizi Wakristo hufurahi kuwasaidia kuona uhitaji wao wa kiroho ili wawe “matajiri katika imani.” (Yakobo 2:5; Mathayo 5:3) Isitoshe, waangalizi wanahitaji kuwasaidia watumie ‘dawa ya kiroho ya macho,’ yaani, wakubali na kufuata mafundisho, ushauri, kielelezo, na mtazamo wa akili wa Yesu. Hiyo ni dawa ya kuponya “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha.”—1 Yohana 2:15-17.

      19 Yesu huwakaripia na kuwatia nidhamu wote anaowapenda. Waangalizi wanaotumikia chini yake wanapaswa kufanya vivyo hivyo kwa upole. (Matendo 20:28, 29) Watu wa Laodikia walihitaji ‘kuwa wenye bidii na kutubu,’ na kurekebisha maoni na maisha yao. Je, baadhi yetu tumeanza kutotilia maanani sana utumishi wetu mtakatifu kwa Mungu maishani? Basi na ‘tununue dawa ya macho kutoka kwa Yesu’ ili tuweze kutambua umuhimu wa kuwa wenye bidii katika kuutafuta kwanza Ufalme.—Mathayo 6:33.

      20, 21. Ni nani wanaokubali kumfungulia Yesu ‘anapobisha’ mlango leo, nao wana matarajio gani?

      20 Kristo anasema, “Tazama! Mimi nimesimama mlangoni na kubisha. Ikiwa yeyote asikia sauti yangu na kuufungua mlango, hakika mimi nitakuja ndani ya nyumba yake na kula mlo wa jioni pamoja naye na yeye pamoja nami.” Mara nyingi Yesu alitoa maagizo ya kiroho alipokuwa akila. (Luka 5:29-39; 7:36-50; 14:1-24) Sasa anabisha mlango wa kutaniko lililo kama lile la Laodikia. Je, washiriki wake watamfungulia, wachochee tena upendo wao kwake, wamkaribishe katikati yao, na kumruhusu awafundishe? Wakifanya hivyo, Kristo atakula pamoja nao, nao watanufaika sana kiroho.

      21 “Kondoo wengine” leo wanamkaribisha Yesu kwa njia ya mfano, na kwa kufanya hivyo watapata uhai wa milele. (Yohana 10:16; Mathayo 25:34-40, 46) Kristo atampa kila mtiwa-mafuta anayeshinda pendeleo la ‘kuketi pamoja naye katika kiti chake cha ufalme, kama vile yeye alivyoshinda na kuketi pamoja na Baba yake katika kiti Chake cha ufalme.’ Naam, Yesu anawaahidi watiwa-mafuta wanaoshinda thawabu tukufu ya kuketi pamoja naye katika kiti cha Ufalme, upande wa kuume wa Baba yake huko mbinguni. Nao kondoo wengine wanaoshinda wanatarajia kuishi katika dunia nzuri sana chini ya utawala wa Ufalme.

      Mambo Ambayo Sote Tunajifunza

      22, 23. (a) Wakristo wote wanawezaje kunufaika na yale ambayo Yesu aliyaambia makutaniko saba? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

      22 Bila shaka Wakristo wote wanaweza kunufaika sana na yale ambayo Yesu aliyaambia yale makutaniko saba huko Asia Ndogo. Kwa mfano, kwa kutambua kwamba Kristo alitoa pongezi ilipohitajika, wazee Wakristo wenye upendo huchochewa kupongeza mtu mmojammoja na makutaniko ambayo yanaendelea vizuri kiroho. Wazee huwasaidia waamini wenzao walio na udhaifu mbalimbali watumie Maandiko kuboresha hali hizo. Sote tunaweza kuendelea kunufaika na ushauri mbalimbali ambao Kristo aliyapa yale makutaniko saba, mradi tunaufuata bila kukawia huku tukisali kwa bidii.a

      23 Siku hizi za mwisho si wakati wa kujikalia tu, kufuatia vitu vya kimwili, au kitu chochote kinachoweza kufanya tumtolee Mungu utumishi wa kijuujuu tu. Kwa hiyo, makutaniko yote na yaendelee kung’aa kama vinara vya taa ambavyo Yesu ataviacha mahali pake. Tukiwa Wakristo waaminifu, na tuazimie sikuzote kumsikiliza Kristo anaposema na pia kusikiliza yale ambayo roho inasema. Hivyo, tutapata shangwe ya kudumu na kumtukuza Yehova tukiwa wachukuaji wa nuru.

      [Maelezo ya Chini]

      a Andiko la Ufunuo 2:1–3:22 linazungumziwa pia katika sura ya 7 hadi ya 13 ya kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki