-
Penda Uadilifu kwa Moyo Wako WoteMnara wa Mlinzi—2011 | Februari 15
-
-
Penda Uadilifu kwa Moyo Wako Wote
“Umependa uadilifu.”—ZAB. 45:7.
1. Ni nini kitakachotusaidia kufuata “mapito ya uadilifu”?
KUPITIA Neno lake na roho yake takatifu, Yehova anawaongoza watu wake katika “mapito ya uadilifu” au haki. (Zab. 23:3) Hata hivyo, kwa kuwa sisi si wakamilifu tuna mwelekeo wa kukengeuka kutoka katika njia hiyo. Ili turudi na kufanya mambo yaliyo sawa tunahitaji kujitahidi kabisa. Ni nini kitakachotusaidia kufanikiwa? Kama Yesu, ni lazima tupende kufanya mambo yaliyo sawa.—Soma Zaburi 45:7.
2. “Mapito ya uadilifu” ni nini?
2 “Mapito ya uadilifu” ni nini? Mapito ni njia nyembamba ya miguu. “Mapito” hayo yanategemea viwango vya Yehova vya uadilifu. Katika Kiebrania na Kigiriki, neno “uadilifu” linamaanisha jambo la “unyoofu,” na neno hilo linaonyesha hali ya kushikamana kabisa na kanuni za maadili. Kwa kuwa Yehova ni “makao ya uadilifu,” waabudu wake wanafurahi kumtegemea ili awaonyeshe njia nyoofu ya maadili ambayo wanapaswa kufuata.—Yer. 50:7.
3. Tunaweza kujifunza jinsi gani mambo mengi kuhusu uadilifu wa Mungu?
3 Tutampendeza Mungu kikamili ikiwa tu tutajitahidi kwa moyo wetu wote kujipatanisha na viwango vyake vya uadilifu. (Kum. 32:4) Ili tufanye hivyo, tunaanza kwa kujifunza yote tunayoweza kumhusu Yehova Mungu katika Neno lake, Biblia. Kadiri tunavyojifunza mengi kumhusu yeye na kumkaribia zaidi kila siku, ndivyo tutakavyozidi kupenda uadilifu wake. (Yak. 4:8) Ni lazima pia tukubali mwongozo wa Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu tunapohitaji kufanya maamuzi ya maana maishani.
Tafuta Uadilifu wa Mungu
4. Kutafuta uadilifu wa Mungu kunatia ndani nini?
4 Soma Mathayo 6:33. Kutafuta uadilifu wa Mungu kunatia ndani mengi zaidi ya kutumia wakati wetu katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Ili utumishi wetu mtakatifu ukubaliwe na Yehova, ni lazima mwenendo wetu wa kila siku upatane na viwango vyake vya juu. Ni lazima watu wote wanaotafuta uadilifu wa Yehova wafanye nini? Ni lazima ‘wavae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’—Efe. 4:24.
5. Ni nini kitakachotusaidia kushinda hali ya kuvunjika moyo?
5 Tunapojitahidi kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, huenda nyakati nyingine tukavunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda hali ya kuvunjika moyo inayodhoofisha sana na kujifunza kupenda na kutenda mambo ya uadilifu? (Met. 24:10) Ni lazima tusali kwa Yehova kwa ukawaida “tukiwa na mioyo ya kweli katika uhakikisho kamili wa imani.” (Ebr. 10:19-22) Iwe sisi ni Wakristo watiwa-mafuta au tuna tumaini la kuishi duniani, tunaonyesha imani katika dhabihu ya ukombozi au fidia ya Yesu Kristo na katika utumishi wake akiwa Kuhani wetu Mkuu sana. (Rom. 5:8; Ebr. 4:14-16) Gazeti la kwanza kabisa la Mnara wa Mlinzi lilitoa mfano ambao unaonyesha uwezo wa damu ya Yesu iliyomwagwa. (1 Yoh. 1:6, 7) Gazeti hilo lilisema hivi: “Ni jambo la hakika kabisa kwamba [wakati] kitu chekundu kabisa [kinapotazamwa] kupitia kioo chekundu katika mwangaza, kitu hicho kinaonekana kuwa cheupe; kwa hiyo, hata dhambi zetu zikiwa nyekundu sana, tunapokuja mahali ambapo Mungu anaweza kuziona kupitia damu ya Kristo, zinaonekana kuwa nyeupe.” (Julai [Mwezi wa 7] 1879, uku. 6) Yehova ametuandalia mpango mzuri ajabu kama nini kupitia dhabihu ya ukombozi ya Mwana wake mpendwa!—Isa. 1:18.
Chunguza Silaha Zako za Kiroho
6. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuchunguza silaha zetu za kiroho?
6 Nyakati zote, tunahitaji kuvaa “bamba la kifuani la uadilifu,” kwa sababu ni sehemu ya maana ya silaha za kiroho kutoka kwa Mungu. (Efe. 6:11, 14) Iwe tumejiweka wakfu kwa Yehova hivi karibuni au tumekuwa tukishiriki katika utumishi mtakatifu kwa makumi ya miaka, ni jambo la maana sana kwetu kuchunguza silaha zetu za kiroho kila siku. Kwa nini? Kwa sababu Ibilisi na roho wake waovu wametupwa chini katika ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-12) Shetani ana hasira, naye anajua kwamba ana wakati mfupi. Hivyo, amezidisha mashambulizi yake kuelekea watu wa Mungu. Je, tunathamini umuhimu wa kuvaa “bamba la kifuani la uadilifu”?
7. Tutajiendesha jinsi gani tukitambua kwamba tunahitaji “bamba la kifuani la uadilifu”?
7 Bamba la kifuani linalinda moyo halisi. Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, moyo wetu wa mfano ni hatari na una mwelekeo wa kuwa wenye hila au udanganyifu. (Yer. 17:9) Kwa kuwa moyo wetu una mwelekeo wa kufanya mambo yasiyofaa, ni jambo la maana sana kwetu tuuzoeze na kuutia nidhamu. (Mwa. 8:21) Tukitambua kwamba tunahitaji “bamba la kifuani la uadilifu,” hatutavua bamba hilo kwa muda kwa kuchagua kuburudishwa na mambo ambayo Mungu anachukia; wala hatutajiruhusu tutafakari kuhusu kutenda mambo yasiyofaa. Hatutapoteza wakati mwingi sana wenye thamani tukitazama televisheni. Badala yake, tutaendelea kujitahidi kufanya mambo yanayompendeza Yehova. Hata tukijikwaa kwa muda baada ya kushawishiwa na mawazo ya kimwili yasiyo ya uadilifu, tutasimama tena kwa msaada wa Yehova.—Soma Methali 24:16.
8. Kwa nini tunahitaji “ngao kubwa ya imani”?
8 “Ngao kubwa ya imani” ni kati ya silaha zetu za kiroho. Inatuwezesha “kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.” (Efe. 6:16) Kisha, kuwa na imani na kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote kunatusaidia kutenda mambo ya uadilifu na kubaki katika barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele. Kadiri tunavyojifunza kumpenda Yehova, ndivyo tutakavyothamini zaidi uadilifu wake. Lakini namna gani kuhusu dhamiri yetu? Inatusaidia jinsi gani tunapojitahidi kuupenda uadilifu?
Dumisha Dhamiri Njema
9. Tunafaidika jinsi gani kwa kudumisha dhamiri njema?
9 Wakati tulipobatizwa, tulitoa ombi kwa Yehova la kupata “dhamiri njema.” (1 Pet. 3:21) Kwa sababu tuna imani katika dhabihu ya ukombozi, damu ya Yesu inafunika dhambi zetu na hivyo tunakuwa na msimamo safi mbele za Mungu. Hata hivyo, ili tuendelee kuwa na msimamo huo safi, tunahitaji kudumisha dhamiri njema. Ikiwa nyakati nyingine dhamiri yetu inatushtaki na kutoa maonyo, tunapaswa kushukuru kwamba inafanya kazi vizuri. Maonyo hayo yanaonyesha kwamba dhamiri yetu haijakufa ganzi kuhusiana na njia za Yehova za uadilifu. (1 Tim. 4:2) Lakini dhamiri inaweza kutimiza daraka la ziada kwa ajili ya wale wanaotaka kupenda uadilifu.
10, 11. (a) Simulia jambo ambalo linaonyesha kwa nini tunapaswa kuisikiliza dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia. (b) Kwa nini tunaweza kupata furaha kubwa tukipenda uadilifu?
10 Tunapofanya makosa, dhamiri yetu inaweza kutuhukumu au kutusumbua. Kijana mmoja aliacha kufuata “mapito ya uadilifu.” Akawa na zoea la kutazama ponografia (picha au habari za ngono) na kisha akaanza kuvuta bangi. Alijihisi akiwa na hatia alipoenda katika mikutano na alijiona kuwa mnafiki aliposhiriki katika utumishi wa shambani, kwa hiyo, aliacha kushiriki katika utendaji huo wa Kikristo. Alisema hivi: “Lakini, sikujua kamwe kwamba dhamiri yangu ingenisumbua kwa sababu ya matendo yangu.” Akaongezea hivi: “Niliendelea kuishi maisha hayo ya upumbavu kwa miaka minne hivi.” Kisha akaanza kufikiria kurudi katika kweli. Ingawa alifikiri kwamba Yehova hangesikiliza sala yake, alisali tu na kuomba msamaha. Kabla ya dakika kumi kupita, mama yake alimtembelea na kumtia moyo aanze tena kuhudhuria mikutano. Alienda katika Jumba la Ufalme na kumwomba mzee mmoja ajifunze pamoja naye. Baada ya muda, alibatizwa, na sasa anamshukuru Yehova kwa sababu aliokoa uhai wake.
11 Je, hatujaona kwamba tunapata furaha kubwa tunapofanya mambo yaliyo sawa? Kadiri tunavyojifunza kupenda uadilifu na kutenda matendo ya uadilifu kwa ukamili zaidi, ndivyo tunavyopata shangwe zaidi tunapofanya mambo yanayompendeza Baba yetu wa mbinguni. Hebu fikiria jambo hili! Siku inakuja wakati ambapo wanadamu wote watakuwa na dhamiri ambayo inawaletea furaha tu; wataiga sifa za Mungu kwa ukamilifu. Kwa hiyo, acheni tusitawishe sasa ndani kabisa ya mioyo yetu sifa ya kupenda uadilifu na hivyo kumfanya Yehova ashangilie.—Met. 23:15, 16.
12, 13. Tunaweza kuzoeza dhamiri yetu namna gani?
12 Tunaweza kuizoeza namna gani dhamiri yetu? Tunapojifunza Maandiko na vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia, ni jambo la maana kukumbuka kwamba “moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” (Met. 15:28) Fikiria jinsi jambo hilo linavyotusaidia tunapokuwa na maswali au maulizo kuhusu kazi ya kuajiriwa, yaani, kazi ya mshahara. Ikiwa kazi fulani inapingana moja kwa moja na matakwa ya Kimaandiko, wengi wetu tunafuata haraka mwongozo ambao umetolewa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Hata hivyo, ikiwa hakuna jibu la wazi kwa swali fulani kuhusu kazi, tunapaswa kusali na kufikiria kanuni za Biblia.a Tunapaswa kufikiria kanuni kama ile ya kuepuka kuumiza dhamiri za wengine. (1 Kor. 10:31-33) Tunapaswa kufikiria hasa kanuni zinazohusu uhusiano wetu pamoja na Mungu. Ikiwa tunamwona Yehova kuwa halisi, tutajiuliza hivi kwanza: ‘Je, nikifanya kazi hii nitamhuzunisha Yehova na kumtia uchungu?’—Zab. 78:40, 41.
13 Tunapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi au Funzo la Biblia la Kutaniko, tunapaswa kukumbuka kwamba tunahitaji kutafakari kuhusu habari hiyo. Je, sikuzote tunajikuta tukipiga mistari haraka-haraka jibu la swali katika funzo na kuendelea na fungu linalofuata? Inaelekea kwamba kujifunza kwa njia hiyo hakuwezi kuongeza upendo wetu kwa ajili ya uadilifu au kutusaidia kusitawisha dhamiri inayotoa maonyo haraka. Ili tupende uadilifu, tunahitaji kujifunza kwa bidii na kutafakari kuhusu mambo tunayosoma katika Neno la Mungu lililoandikwa. Hakuna njia fupi au za mkato inapohusu kujifunza kupenda uadilifu kwa moyo wetu wote!
Njaa na Kiu kwa Ajili ya Uadilifu
14. Yehova Mungu na Yesu Kristo wanataka tuhisi jinsi gani kuhusu utumishi wetu mtakatifu?
14 Yehova Mungu na Yesu Kristo wanataka tuwe na furaha tunapofanya utumishi wetu mtakatifu. Ni nini kitakachochangia furaha yetu? Ni kupenda uadilifu! Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mt. 5:6) Maneno hayo yana maana gani kwa wale ambao wanatamani kupenda uadilifu?
15, 16. Kiu na njaa ya kiroho inaweza kutoshelezwa kwa njia gani?
15 Ulimwengu ambamo tunaishi unatawaliwa na yule mwovu. (1 Yoh. 5:19) Tunaposoma gazeti kutoka katika nchi yoyote, tunapata habari kuhusu ukatili na jeuri ambayo haijawahi kamwe kutokea! Mtu mwadilifu anaumia sana moyoni anapoona unyama ambao mwanadamu anamtendea mwanadamu mwenzake. (Mhu. 8:9) Sisi ambao tunampenda Yehova, tunajua kwamba ni yeye peke yake anayeweza kutosheleza kiu na njaa ya kiroho ya watu ambao wanatamani kujifunza uadilifu. Watu wasiomwogopa Mungu wataondolewa hivi karibuni, na wale wanaopenda uadilifu hawatateseka tena kwa sababu ya watu wanaokaidi au kuvunja sheria na kwa sababu ya matendo yao maovu. (2 Pet. 2:7, 8) Watapata kitulizo kikubwa kama nini!
16 Tukiwa watumishi wa Yehova na wafuasi wa Yesu Kristo, tunatambua kwamba wote walio na kiu na njaa kwa ajili ya uadilifu “watashibishwa.” Watatoshelezwa kabisa kupitia mpango wa Mungu wa kuleta mbingu mpya na dunia mpya ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Pet. 3:13) Basi, acheni tusivunjike moyo au kushangazwa kwamba uonevu na jeuri imetwaa au kuondoa kabisa uadilifu katika ulimwengu huu wa kishetani. (Mhu. 5:8) Yehova, Aliye Juu Zaidi, anajua mambo yanayotukia na hivi karibuni atawakomboa wale wanaopenda uadilifu.
Faidika kwa Kupenda Uadilifu
17. Taja faida fulani ambazo tunapata kwa sababu ya kupenda uadilifu.
17 Zaburi ya 146:8 inakazia faida kubwa ya kufuata mapito ya uadilifu. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova anawapenda waadilifu.” Hebu wazia! Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima anatupenda kwa sababu tunapenda uadilifu! Kwa sababu ya upendo wa Yehova, tuna hakika kwamba atatosheleza mahitaji yetu tunapotanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yetu. (Soma Zaburi 37:25; Methali 10:3.) Mwishowe, wale wanaopenda uadilifu ndio watakaofurahia dunia hii yote. (Met. 13:22) Idadi kubwa ya watu wa Mungu watathawabishwa kwa kupewa shangwe nyingi sana na uzima bila mwisho katika dunia maridadi itakayokuwa paradiso kwa sababu walitenda mambo ya uadilifu. Hata sasa, wale ambao wanapenda uadilifu wa Mungu wanapata thawabu ya kuwa na amani moyoni ambayo inachangia umoja katika familia zao na katika makutaniko yao.—Flp. 4:6, 7.
18. Ni mambo gani mazuri ambayo tunaweza kufanya tunapongojea siku ya Yehova?
18 Tunapongojea siku kuu ya Yehova ifike, ni lazima tuendelee kutafuta uadilifu wake. (Sef. 2:2, 3) Kwa hiyo, acheni tuonyeshe kwamba tunapenda kikweli njia za uadilifu za Yehova Mungu. Hilo linatia ndani kuvaa kikamili kabisa “bamba la kifuani la uadilifu” ili tuulinde moyo wetu wa mfano. Pia, tunahitaji kudumisha dhamiri njema, ambayo itatuletea furaha na kuufanya moyo wa Mungu wetu ushangilie.—Met. 27:11.
19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na habari inayofuata itazungumzia nini?
19 ‘Macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ (2 Nya. 16:9) Maneno hayo yanatufariji kama nini tunapofanya mambo yaliyo sawa huku tukipambana na ukosefu wa usalama, jeuri, na uovu ambao unazidi kuongezeka katika ulimwengu huu wenye misukosuko! Ni kweli kwamba huenda matendo yetu ya uadilifu yakawashangaza wanadamu wengi ambao wametengwa mbali na Mungu. Lakini tunajifaidi wenyewe sana tunaposhikamana na uadilifu wa Yehova. (Isa. 48:17; 1 Pet. 4:4) Kwa hiyo basi, acheni tuazimie kwa moyo kamili kuendelea kupata shangwe kwa kupenda na kutenda mambo ya uadilifu kwa moyo wetu wote. Hata hivyo, kuwa na moyo kamili kunatia ndani pia kuchukia uasi-sheria. Habari inayofuata itatuonyesha hilo linamaanisha nini.
-
-
Je, Unachukia Uasi-sheria?Mnara wa Mlinzi—2011 | Februari 15
-
-
Je, Unachukia Uasi-sheria?
“Nawe [Yesu] ukauchukia uasi-sheria.”—EBR. 1:9.
1. Yesu alifundisha nini kuhusu upendo?
AKIKAZIA kwamba upendo ni jambo la maana, Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:34, 35) Yesu aliwaamuru wafuasi wake waonyeshane upendo wa kujidhabihu. Upendo huo ndio ungewatambulisha. Yesu aliwahimiza hivi pia: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.”—Mt. 5:44.
2. Wafuasi wa Kristo wanapaswa kusitawisha chuki kuelekea nini?
2 Hata hivyo, zaidi ya kuwafundisha wanafunzi wake kuhusu upendo, Yesu aliwafundisha pia jambo ambalo walipaswa kuchukia. Ilisemwa hivi kumhusu Yesu: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria [uovu].” (Ebr. 1:9; Zab. 45:7) Hilo linaonyesha kwamba hatupaswi tu kusitawisha upendo kwa ajili ya uadilifu bali pia ni lazima tusitawishe chuki kuelekea dhambi, au uasi-sheria. Ni vizuri kujua kwamba mtume Yohana alitaja hivi waziwazi: “Kila mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi anazoea pia kufanya uasi-sheria, na kwa hiyo dhambi ni uasi-sheria.”—1 Yoh. 3:4.
3. Kuhusiana na kuchukia uasi-sheria, habari hii itazungumzia mambo gani ya maisha?
3 Hivyo basi, tukiwa Wakristo tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninachukia uasi-sheria?’ Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunachukia mabaya katika mambo manne yafuatayo ya maisha: (1) mtazamo wetu kuelekea kunywa pombe kupita kiasi, (2) maoni yetu kuhusu mambo ya uchawi, (3) maoni yetu kuhusu mwenendo mpotovu wa kingono, na (4) mtazamo wetu kuelekea watu wanaopenda uasi-sheria.
Usiwe Mtumwa wa Pombe
4. Kwa nini Yesu alikuwa na uhuru wa kusema alipotoa onyo kuhusu kunywa pombe kupita kiasi?
4 Katika pindi fulani, Yesu alikunywa divai, akitambua kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Zab. 104:14, 15) Hata hivyo, hakutumia vibaya kamwe zawadi hiyo kwa kunywa kupita kiasi. (Met. 23:29-33) Hivyo basi, Yesu alikuwa na uhuru wa kusema alipotoa shauri kuhusu zoea hilo. (Soma Luka 21:34.) Kunywa pombe kupita kiasi kunaweza kuongoza kwenye dhambi nyingine nzito. Hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake, bali endeleeni kujazwa na roho.” (Efe. 5:18) Pia, aliwahimiza wanawake wenye umri mkubwa katika kutaniko wasiwe “watumwa wa divai nyingi sana.”—Tito 2:3.
5. Wale wanaoamua kunywa pombe wanaweza kujiuliza maswali au maulizo gani?
5 Ikiwa utaamua kunywa pombe, unapaswa pia kujiuliza hivi: ‘Je, nina maoni kama ya Yesu kuhusu kunywa pombe kupita kiasi? Ikiwa ninahitaji kuwashauri wengine kuhusu jambo hilo, je, nina uhuru wa kusema? Je, ninakunywa pombe ili kuepuka mahangaiko au kupunguza mikazo ya maisha? Ninakunywa kiasi gani cha pombe kila juma? Ninatenda jinsi gani mtu fulani anaposema kwamba huenda ninakunywa pombe kupita kiasi? Je, ninajitetea au hata kumfungia mtu huyo kinyongo moyoni?’ Kujiachilia kuwa watumwa wa pombe kunaweza kuharibu uwezo wetu wa kufikiria mambo vizuri na kufanya maamuzi yenye hekima. Wafuasi wa Kristo wanajitahidi kulinda uwezo wao wa kufikiri.—Met. 3:21, 22.
Epuka Mazoea ya Uchawi
6, 7. (a) Yesu alishughulika jinsi gani na Shetani na roho waovu? (b) Kwa nini mazoea ya uchawi yameenea sana leo?
6 Alipokuwa duniani, Yesu alimpinga kabisa Shetani na roho waovu. Alishinda kabisa mashambulizi ya Shetani ya moja kwa moja yaliyokusudiwa kuvunja ushikamanifu wake. (Luka 4:1-13) Alitambua pia na kushinda majaribu mengine yasiyo ya waziwazi ambayo yalikusudiwa kubadili mawazo na matendo yake. (Mt. 16:21-23) Yesu aliwasaidia watu waliostahili ili watoke chini ya utawala wenye ukatili wa roho waovu.—Marko 5:2, 8, 12-15; 9:20, 25-27.
7 Baada ya Yesu kuwekwa rasmi kuwa Mfalme mwaka wa 1914, alisafisha mbingu na kuondoa uvutano wenye kuchafua wa Shetani na roho waovu. Matokeo ni kwamba—sasa kuliko wakati mwingine wowote—Shetani ameazimia ‘kuipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufu. 12:9, 10) Hivyo, hatupaswi kushangaa kwamba mambo ya uchawi yameenea sana na watu wengi wanazidi kuvutiwa na mambo hayo. Ni hatua gani ambazo tunaweza kuchukua ili kujilinda?
8. Kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza jinsi gani kuhusiana na vitumbuizo anavyochagua?
8 Biblia inaonya waziwazi kuhusu hatari zinazohusiana na kuwasiliana na pepo. (Soma Kumbukumbu la Torati 18:10-12.) Leo, Shetani na roho waovu wanapotosha fikira za watu kupitia sinema, vitabu, na michezo ya kompyuta inayowachochea watu wapende mazoea ya uchawi. Kwa hiyo, tunapochagua vitumbuizo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Katika miezi iliyopita, je, nimechagua kutumbuizwa na sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya kompyuta, vitabu, au vichekesho ambavyo vinahusisha mazoea ya uchawi? Je, ninaelewa kwamba ni jambo la maana kupinga uvutano wa mambo ya uchawi, au je, ninapuuza hatari hizo? Je, hata nimefikiria jinsi ambavyo huenda Yehova atahisi kuhusu vitumbuizo ninavyochagua? Ikiwa nimekaribisha uvutano huo wa kishetani, je, kumpenda Yehova na kanuni zake za uadilifu kutanichochea kufanya uamuzi thabiti na kukataa kabisa uvutano huo?’—Mdo. 19:19, 20.
Tii Onyo la Yesu Kuhusu Mwenendo Mpotovu Kingono
9. Mtu anaweza jinsi gani kusitawisha upendo kuelekea uasi-sheria?
9 Yesu alitetea viwango vya Yehova kuhusu maadili ya ngono. Alisema hivi: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:4-6) Yesu alijua kwamba mambo tunayotazama yanaweza kuwa na uvutano juu ya moyo wetu. Kwa hiyo, alisema hivi kwenye Mahubiri yake ya Mlimani: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mt. 5:27, 28) Wale wanaopuuza onyo la Yesu kwa kweli wanasitawisha upendo kuelekea uasi-sheria.
10. Simulia jambo linaloonyesha kwamba mtu anaweza kuacha zoea la kutazama ponografia.
10 Shetani anawachochea watu kupenda mwenendo mpotovu wa kingono kupitia ponografia (picha au habari za ngono). Mfumo wa sasa wa mambo umejaa ponografia. Wale wanaotazama ponografia wanashindwa kuondoa katika akili zao mambo machafu ya ngono. Hata wanaweza kuwa na zoea la kutazama ponografia. Fikiria jambo lililompata Mkristo mmoja. Anasema hivi: “Nilitazama ponografia kisiri. Nilikuwa nikiwazia mambo yasiyo halisi ambayo nilifikiri kwamba hayakuhusiana na utumishi wangu kwa Yehova. Nilijua kwamba zoea hilo lilikuwa baya lakini nilijiambia kwamba bado Mungu anakubali utumishi wangu.” Ni nini kilichomfanya ndugu huyo abadili njia yake ya kufikiri? Anasema hivi: “Niliamua kuwaambia wazee kuhusu tatizo langu, ingawa hilo lilikuwa jambo gumu zaidi ambalo nimewahi kufanya.” Mwishowe ndugu huyo aliacha zoea hilo chafu. Anakubali hivi: “Baada ya kusafisha maisha yangu kwa kuacha dhambi hiyo, mwishowe nilihisi kwamba kwa kweli nilikuwa na dhamiri safi.” Ni lazima wale wanaochukia uasi-sheria wajifunze kuchukia ponografia.
11, 12. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunachukia uasi-sheria tunapochagua muziki?
11 Muziki na maneno yake yanaweza kuchochea sana hisia zetu na hivyo kuchochea moyo wetu wa mfano. Muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu na tangu zamani umetumiwa katika ibada ya kweli. (Kut. 15:20, 21; Efe. 5:19) Lakini ulimwengu mwovu wa Shetani unawachochea watu kupenda muziki unaotukuza maadili mapotovu. (1 Yoh. 5:19) Unaweza kujua jinsi gani kwamba muziki unaosikiliza unakuchafua au hapana?
12 Kwanza, unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, nyimbo ambazo ninasikiliza zinatukuza uuaji, uzinzi, uasherati, na kukufuru? Ikiwa ningemsomea mtu mwingine maneno ya nyimbo fulani ninazosikiliza, je, mtu huyo angeona kwamba ninachukia uasi-sheria, au je, maneno hayo yangeonyesha kwamba moyo wangu umechafuliwa?’ Hatuwezi kudai kwamba tunachukia uasi-sheria na wakati huohuo tunautukuza kupitia nyimbo. Yesu alisema kwamba “mambo yanayotoka katika kinywa hutoka moyoni, na mambo hayo humtia mtu unajisi. Kwa mfano, mawazo mabaya hutoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uwongo, makufuru.”—Mt. 15:18, 19; linganisha na Yakobo 3:10, 11.
Uwe na Maoni Kama ya Yesu Kuhusu Wale Wanaopenda Uasi-Sheria
13. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu wale ambao hawakutaka kuacha mwenendo wa dhambi?
13 Yesu alisema kwamba alikuja kuwaita watenda-dhambi, au watu wanaopenda uasi-sheria, ili watubu. (Luka 5:30-32) Hata hivyo, aliwaona jinsi gani wale ambao hawakutaka kuacha mwenendo wao wa dhambi? Yesu alitoa maonyo makali kuhusu kukubali kushawishiwa na watu kama hao. (Mt. 23:15, 23-26) Pia, alisema hivi waziwazi: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia. Wengi wataniambia siku hiyo [Mungu atakapoleta hukumu], ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’” Hata hivyo, atawakataa wale wanaozoea kufanya uasi-sheria bila kutubu, na atawaambia hivi: “Ondokeni kwangu.” (Mt. 7:21-23) Kwa nini watahukumiwa kwa njia hiyo? Kwa sababu watu hao hawamheshimu Mungu na wanawaumiza wengine kwa sababu ya mazoea yao ya uasi-sheria.
14. Kwa nini watenda-dhambi wasiotubu wanaondolewa katika kutaniko?
14 Neno la Mungu linaamuru kwamba watenda-dhambi wasiotubu waondolewe katika kutaniko. (Soma 1 Wakorintho 5:9-13.) Ni jambo la maana kufanya hivyo kwa sababu tatu hivi: (1) ili kufanya jina la Yehova libaki bila lawama, (2) ili kulinda kutaniko lisichafuliwe, na (3) ili kumsaidia mtenda-dhambi atubu ikiwezekana.
15. Ikiwa tunataka kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova tunapaswa kujiuliza maswali gani mazito?
15 Je, tuna maoni kama ya Yesu kuhusu watu ambao wameazimia kuendelea kutenda uasi-sheria? Tunahitaji kufikiria maswali haya: ‘Je, ninapaswa kuchagua kushirikiana kwa ukawaida na mtu ambaye ametengwa au ambaye amejitenga na ushirika wa kutaniko la Kikristo? Namna gani ikiwa ni mtu wa ukoo wa karibu ambaye sasa haishi nyumbani?’ Hali kama hiyo inaweza kujaribu kwelikweli upendo wetu wa uadilifu na ushikamanifu wetu kwa Mungu.a
16, 17. Mama mmoja Mkristo alipatwa na hali gani ngumu, na ni nini kilichomsaidia kuunga mkono mpango wa kuwatenga na ushirika watenda-dhambi wasiotubu?
16 Fikiria jambo lililoonwa kuhusu dada mmoja ambaye mwana wake ni mtu mzima na ambaye wakati mmoja alimpenda Yehova. Hata hivyo, baadaye maishani mwana huyo aliamua kuendelea kufanya uasi-sheria bila kutubu. Kwa hiyo, akatengwa na ushirika wa kutaniko. Dada yetu alimpenda Yehova, lakini pia alimpenda mwana wake na ilikuwa vigumu sana kwake kufuata agizo la Kimaandiko la kuepuka kushirikiana naye.
17 Ungempa dada huyo mashauri gani? Mzee mmoja wa kutaniko alimsaidia kutambua kwamba Yehova alielewa uchungu aliokuwa akihisi. Ndugu huyo alimwomba afikirie uchungu ambao bila shaka Yehova alihisi wakati wanawe fulani wa kimalaika walipoasi. Mzee huyo alizungumza naye na kumwonyesha kwamba ingawa Yehova anajua jinsi hali hiyo inavyoleta uchungu, anataka watenda-dhambi wasiotubu watengwe na ushirika. Dada huyo alithamini kwa moyo wote vikumbusho hivyo na akaunga mkono kwa ushikamanifu mpango wa kutenga na ushirika.b Ushikamanifu kama huo unafanya moyo wa Yehova ufurahi.—Met. 27:11.
18, 19. (a) Tukikatisha uhusiano na mtu anayeendelea na matendo ya uasi-sheria tunaonyesha kwamba tunachukia nini? (b) Matokeo yanaweza kuwa nini tukiwa washikamanifu kwa Yehova na mpango wake?
18 Ikiwa unapambana na hali kama hiyo, tafadhali kumbuka kwamba Yehova anakusikitikia. Unapokatisha uhusiano pamoja na mtu ambaye ametengwa au kujitenga na ushirika, unaonyesha kwamba unachukia mtazamo na matendo yaliyoongoza kwenye hali hiyo. Hata hivyo, unaonyesha pia kwamba unampenda mtenda-dhambi huyo na ungependa afanye jambo ambalo litamletea faida. Ukiwa mshikamanifu kwa Yehova kuna uwezekano mkubwa kwamba mtu aliyetiwa nidhamu atatubu na kumrudia Yehova.
19 Mtu fulani ambaye alikuwa ametengwa na ushirika na baadaye akarudishwa katika kutaniko aliandika hivi: “Ninafurahi kwamba Yehova anawapenda sana watu wake hivi kwamba anahakikisha tengenezo lake linabaki likiwa safi. Hatua ambayo huenda watu wa nje wakaona kwamba ni kali, kwa kweli inafaa na ni hatua ya upendo.” Je, unafikiri kwamba mtu huyo angesaidiwa kufikia uamuzi huo ikiwa washiriki wa kutaniko, kutia ndani familia yake, wangeendelea kuzungumza naye kwa ukawaida alipokuwa ametengwa na ushirika? Tunapounga mkono mpango wa Kimaandiko wa kutenga na ushirika tunaonyesha wazi kwamba tunapenda uadilifu na tunatambua kuwa Yehova ana haki ya kuweka viwango vya mwenendo.
“Chukieni Yaliyo Mabaya”
20, 21. Kwa nini ni jambo la maana kujifunza kuchukia uasi-sheria?
20 Mtume Petro anaonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda.” Kwa nini? Kwa sababu “adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Pet. 5:8) Je, mtu huyo atakuwa ni wewe? Hilo linategemea sana jinsi unavyojifunza kuchukia uasi-sheria.
21 Si jambo rahisi kusitawisha chuki kuelekea mambo mabaya. Tunazaliwa katika dhambi, na tunaishi katika ulimwengu ambao unatuchochea kufuata tamaa za mwili. (1 Yoh. 2:15-17) Hata hivyo, kwa kumwiga Yesu Kristo na kusitawisha upendo mwingi sana kwa ajili ya Yehova Mungu, tunaweza kufanikiwa kusitawisha chuki kuelekea uasi-sheria. Acheni tuazimie ‘kuchukia yaliyo mabaya,’ tukiwa na hakika kabisa kwamba Yehova ‘anawalinda washikamanifu wake; anawakomboa kutoka katika mkono wa waovu.’—Zab. 97:10.
-