-
“Bibi Mwenye Nywele Nyeusi wa Jangwa la Siria”Mnara wa Mlinzi—1999 | Januari 15
-
-
Maliki ‘Achochea Moyo Wake’ Dhidi ya Zenobia
Katika 270 W.K., Aurelian akawa maliki wa Roma. Majeshi yake yalishinda kwa mafanikio na kutia nidhamu wakatili wa kaskazini. Katika 271 W.K.—sasa akiwakilisha “mfalme wa kaskazini” wa unabii wa Danieli—Aurelian ‘alichochea mamlaka yake na moyo wake dhidi ya mfalme wa kusini,’ aliyewakilishwa na Zenobia. (Danieli 11:25a) Aurelian alituma baadhi ya majeshi yake moja kwa moja hadi Misri na kuongoza jeshi lake kuu kuelekea mashariki kupitia Asia Ndogo.
Mfalme wa kusini—chombo cha utawala kilichoongozwa na Zenobia—‘alijichochea’ afanye vita dhidi ya Aurelian “kwa jeshi kubwa mno na lenye nguvu nyingi” chini ya majenerali wawili, Zabdas na Zabbai. (Danieli 11:25b) Lakini Aurelian alitwaa Misri kisha akaanzisha safari ya uvumbuzi katika Asia Ndogo na Siria. Zenobia alishindiwa huko Emesa (sasa ni Homs), naye akakimbia kurudi Palmyra.
Aurelian alipolizingira Palmyra, Zenobia akitumaini kupata msaada, alitoroka na mwana wake kuelekea Uajemi, lakini alishikwa na Waroma kwenye Mto Frati. Wapalmyra walisalimisha jiji lao katika 272 W.K. Aurelian aliwatendea wakazi wa hapo kwa ukarimu, akapora vitu vingi sana, kutia ndani sanamu iliyokuwa katika Hekalu la Jua, na kuondoka kwenda Roma. Maliki Mroma hakumuua Zenobia, bali alimfanya awe kivutio kikuu katika mwandamano wake wa shangwe ya ushindi katika Roma mwaka wa 274 W.K. Huko alibaki akiwa mwanamke mkomavu mwenye daraja la kuheshimiwa wa Roma katika maisha yake yote.
Jiji la Jangwani Laharibiwa
Miezi kadhaa baada ya Aurelian kutwaa Palmyra, Wapalmyra waliwaua askari walinzi wa Roma ambao alikuwa amewaacha. Habari ya uasi huu ilipofikia Aurelian, mara moja Aurelian aliamuru askari wake warudi huko tena, na wakati huu walilipiza kisasi kwa kiwango kikubwa dhidi ya wakazi wote wa huko. Wale walionusurika kutokana na machinjo hayo yasiyo na huruma walipelekwa utumwani. Jiji hilo lenye fahari liliporwa na kuharibiwa kiasi cha kwamba halingeweza kurekebishwa. Hivyo, jiji hilo kubwa lenye shughuli nyingi lilirudia tena hali yake ya zamani—“Tadmori wa nyikani.”
Wakati Zenobia alipojasiria kukabili Roma, pasipo kujua yeye na Maliki Aurelian walitimiza mafungu yao wakiwa “mfalme wa kusini” na “mfalme wa kaskazini,” wakitimiza sehemu ya unabii uliorekodiwa kwa kina zaidi na nabii wa Yehova miaka 800 hivi mapema. (Danieli, sura ya 11) Akiwa mwenye utu wake wenye kutokeza, Zenobia alipendwa na watu wengi. Hata hivyo, la maana zaidi, lilikuwa fungu lake katika kuwakilisha chombo cha kisiasa kilichotabiriwa katika unabii wa Danieli. Utawala wake haukudumu kwa zaidi ya miaka mitano. Palmyra, jiji kuu la ufalme wa Zenobia, leo ni kijiji tu. Hata Milki yenye uwezo ya Roma tangu wakati huo imefifia na kuziachia nafasi falme za kisasa. Wakati ujao wa mamlaka hizi utakuwaje? Hali yao ya baadaye pia inaamuliwa na utimizo wa unabii wa Biblia.—Danieli 2:44.
-
-
“Bibi Mwenye Nywele Nyeusi wa Jangwa la Siria”Mnara wa Mlinzi—1999 | Januari 15
-
-
Urithi wa Zenobia
Aliporudi Roma baada ya kumshinda Zenobia, malkia wa Palmyra, Maliki Aurelian alijenga hekalu kwa ajili ya jua. Ndani yake aliweka sanamuumbo za mungu-jua alizoleta kutoka jiji la Zenobia. Likieleza juu ya mavumbuzi zaidi, gazeti History Today lasema: “Mojawapo ya matendo ya Aurelian yenye kudumu zaidi labda ni kuanzishwa, katika AD 274, kwa sherehe ya kila mwaka ya kutokea kwa jua wakati wa majira ya baridi kali ya kikomo cha jua, Desemba 25. Milki hiyo ilipopata kuwa ya Kikristo kuzaliwa kwa Kristo kulihamishwa hadi tarehe hiyo ili kufanya dini mpya ikubalike kwa wale waliofurahia sherehe za zamani. Ni kioja kwamba, hatimaye ni kwa sababu ya Malkia Zenobia kwamba . . . [watu] wanasherehekea Krismasi yetu.”
-