-
“Wakeni Roho”Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 15
-
-
“Wakeni Roho”
“Msiwe wavivu katika kazi zenu. Wakeni roho. Mtumikieni Yehova.”—ROM. 12:11.
1. Kwa nini Waisraeli walitoa dhabihu za wanyama na matoleo mengine?
YEHOVA anathamini sana kuona watumishi wake wakijidhabihu kutoka moyoni ili kuonyesha kwamba wanampenda na wanajitiisha kwake ili kufanya mapenzi yake. Katika nyakati za zamani, Yehova alikubali dhabihu mbalimbali za wanyama na matoleo mengine. Waisraeli walitoa dhabihu na matoleo hayo kulingana na Sheria ya Musa ili wasamehewe dhambi zao na pia ilikuwa njia ya kuonyesha shukrani. Katika kutaniko la Kikristo, Yehova hajatuwekea takwa la kutoa dhabihu halisi kama hizo za kidesturi. Hata hivyo, katika sura ya 12 ya barua yake kwa Wakristo huko Roma, mtume Paulo anaonyesha kwamba bado tunatazamiwa kutoa dhabihu. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.
Dhabihu Iliyo Hai
2. Tukiwa Wakristo, tunaishi maisha ya aina gani, na hilo linahusisha nini?
2 Soma Waroma 12:1, 2. Katika sehemu ya kwanza ya barua yake, Paulo alionyesha waziwazi kwamba Wakristo waliotiwa mafuta, Wayahudi na wasio Wayahudi, walitangazwa kuwa waadilifu mbele za Mungu kwa imani, bali si kwa matendo. (Rom. 1:16; 3:20-24) Katika sura ya 12, Paulo anaeleza kwamba Wakristo wanapaswa kuonyesha shukrani kwa kuishi maisha ya kujidhabihu. Ili tufanikiwe, ni lazima tufanye upya akili zetu. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika ambayo tumerithi, tumetiishwa chini ya “sheria ya dhambi na kifo.” (Rom. 8:2) Kwa hiyo, tunahitaji kugeuzwa, yaani, “kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili [zetu],” kwa kubadili kabisa mielekeo yetu. (Efe. 4:23) Tunaweza tu kufanya badiliko hilo kamili kwa msaada wa Mungu na roho yake. Ni lazima pia tujitahidi kabisa, tukitumia ‘nguvu zetu za kufikiri.’ Inamaanisha kwamba tunapaswa kujitahidi kadiri tunayoweza ili ‘tusifanyizwe kulingana na mfumo huu wa mambo,’ pamoja na maadili yake mapotovu, burudani yake chafu, na mawazo yake yaliyopotoka.—Efe. 2:1-3.
3. Kwa nini tunashiriki katika utendaji wa Kikristo?
3 Pia, Paulo anatutia moyo tutumie ‘nguvu zetu za kufikiri’ ili kujihakikishia wenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Kwa nini tunasoma Biblia kila siku, kutafakari kuhusu yale tunayosoma, kusali, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme? Je, ni kwa sababu wazee wa kutaniko wanatuhimiza tufanye hivyo? Bila shaka, tunashukuru kwamba wazee wanatutolea vikumbusho vinavyotusaidia. Lakini tunashiriki katika utendaji wa Kikristo kwa sababu tunachochewa na roho ya Mungu kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kutoka moyoni. Zaidi ya hayo, sisi binafsi tunasadiki kwamba ni mapenzi ya Mungu tushiriki katika utendaji huo. (Zek. 4:6; Efe. 5:10) Pia, tunapata shangwe na uradhi mwingi tunapotambua kwamba kwa kuishi maisha kamili ya Kikristo tunaweza kukubaliwa na Mungu.
Zawadi Mbalimbali
4, 5. Wazee Wakristo wanapaswa kutumia zawadi zao jinsi gani?
4 Soma Waroma 12:6-8, 11. Paulo anaeleza kwamba “tuna zawadi zinazotofautiana kulingana na fadhili zisizostahiliwa tulizopewa.” Zawadi fulani ambazo Paulo anataja kama vile, kuhimiza na kusimamia, zinawahusu hasa wazee Wakristo, ambao wanahimizwa wasimamie “kwa bidii ya kweli.”
5 Paulo anasema kwamba waangalizi wanapaswa kuonyesha bidii hiyohiyo wakati wanapotumikia wakiwa walimu na wanapotimiza “huduma” yao. Inaonekana kwamba mistari mingine katika sura hiyo inaonyesha kwamba Paulo alikuwa akizungumza kuhusu “huduma” inayofanywa ndani ya kutaniko, au katika ule “mwili mmoja.” (Rom. 12:4, 5) Huduma hiyo ni sawa na ile inayotajwa katika Matendo 6:4, wakati ambapo mitume walitangaza hivi: “Tutajitoa kwa sala na kwa huduma ya neno.” Huduma hiyo inatia ndani nini? Wazee Wakristo wanatumia zawadi zao kuwajenga washiriki wa kutaniko. Wanaonyesha kwamba ‘wako katika huduma hiyo’ wakati wanapotoa kwa bidii mwongozo na maagizo kwa kutaniko kutoka katika Neno la Mungu kwa kusali na kujifunza, kufanya utafiti, kufundisha, na kulichunga kutaniko. Waangalizi wanapaswa kutumia zawadi zao kwa uangalifu na kuwatunza kondoo “kwa uchangamfu.”—Rom. 12:7, 8; 1 Pet. 5:1-3.
6. Tunaweza kufuata jinsi gani shauri la Waroma 12:11 ambalo ni andiko la msingi la habari hii?
6 Paulo anaongezea hivi: “Msiwe wavivu katika kazi zenu. Wakeni roho. Mtumikieni Yehova.” Tukigundua kwamba tuna mwelekeo wa kuwa wavivu katika huduma yetu, huenda tukahitaji kuchunguza tena mazoea yetu ya kujifunza kisha tusali kwa bidii zaidi na mara nyingi zaidi ili tupate roho ya Yehova, ambayo inaweza kutusaidia kuondoa uzembe wowote na kuwa tena wenye bidii. (Luka 11:9, 13; Ufu. 2:4; 3:14, 15, 19) Roho takatifu iliwatia nguvu Wakristo wa zamani ili waseme juu ya “mambo makuu ya Mungu.” (Mdo. 2:4, 11) Vivyo hivyo leo, roho hiyo inaweza kutuchochea tuwe na bidii katika huduma, wenye ‘kuwaka roho.’
Unyenyekevu na Kiasi
7. Kwa nini tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye kiasi katika utumishi wetu?
7 Soma Waroma 12:3, 16. Zawadi ambazo huenda tunazo zinategemea “fadhili zisizostahiliwa” za Yehova. Paulo anasema hivi katika andiko lingine: “Kuwa kwetu na sifa za kustahili vya kutosha hutoka kwa Mungu.” (2 Kor. 3:5) Kwa hiyo, hatupaswi kujitukuza. Tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba matokeo yoyote mazuri tunayopata katika huduma yetu yanatokana na baraka za Mungu, bali hayategemei uwezo wetu wenyewe. (1 Kor. 3:6, 7) Kuhusu jambo hilo, Paulo alisema hivi: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” Ni jambo la maana sana kwetu kujiheshimu, kuridhika na kupata shangwe katika utumishi wetu wa Ufalme. Hata hivyo, kuwa na kiasi, au kutambua mipaka yetu, kutatuzuia kushikilia sana maoni yetu. Badala yake, tunapaswa ‘kufikiri ili tuwe na akili timamu.’
8. Tunaweza kuepuka jinsi gani kuwa “wenye busara machoni [petu] wenyewe”?
8 Litakuwa jambo la upumbavu kwetu kujisifu kwa sababu ya mambo tunayotimiza. Ni “Mungu anayeikuza.” (1 Kor. 3:7) Paulo anasema kwamba Mungu amemgawia kila mshiriki wa kutaniko “kipimo cha imani.” Badala ya kujiona kuwa bora, tunapaswa kutambua mambo ambayo wengine wanatimiza kulingana na kipimo chao cha imani. Paulo anasema hivi tena: “Mwafikirie wengine kama vile mnavyojifikiria wenyewe.” Katika barua yake nyingine, mtume huyo anatuambia tusifanye ‘jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili tukiwaona wengine kuwa ni bora kuliko sisi.’ (Flp. 2:3) Tunahitaji jitihada nyingi na unyenyekevu wa kweli ili kutambua kwamba kila mmoja wa ndugu na dada zetu ni bora kuliko sisi katika njia moja au nyingine. Unyenyekevu utatuzuia kuwa “wenye busara machoni [petu] wenyewe.” Ingawa mapendeleo ya utumishi wa pekee yanaweza kuwafanya wengine wajulikane zaidi, wote watapata shangwe nyingi wakitimiza “mambo ya hali ya chini,” kazi za hali ya chini ambazo mara nyingi zinapuuzwa na watu.—1 Pet. 5:5.
Umoja Wetu wa Kikristo
9. Kwa nini Paulo anawalinganisha Wakristo waliozaliwa kwa roho na viungo vya mwili?
9 Soma Waroma 12:4, 5, 9, 10. Paulo anawalinganisha Wakristo watiwa-mafuta na viungo vya mwili, wanapotumikia kwa umoja chini ya Kichwa chao, Kristo. (Kol. 1:18) Anawakumbusha Wakristo waliozaliwa kwa roho kwamba mwili una viungo vingi, lakini vina kazi tofauti na kwamba ‘ingawa ni wengi, wao ni mwili mmoja katika muungano na Kristo.’ Vivyo hivyo, Paulo aliwahimiza hivi Wakristo watiwa-mafuta huko Efeso: “Na tukue kwa upendo katika mambo yote ndani yake yeye aliye kichwa, Kristo. Kutoka katika yeye mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hutoa kile kinachohitajiwa, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kinachofaa, hutokeza ukuzi wa mwili ili huo ujijenge wenyewe katika upendo.”—Efe. 4:15, 16.
10. “Kondoo wengine” wanapaswa kutambua mamlaka gani?
10 Ingawa “kondoo wengine” si sehemu ya mwili wa Kristo wenye washiriki wengi, wanaweza kujifunza mengi kutokana na mfano huo. (Yoh. 10:16) Paulo anasema kwamba Yehova ‘alivitiisha vitu vyote chini ya miguu ya Kristo, na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.’ (Efe. 1:22) Leo, kondoo wengine ni sehemu ya “vitu vyote” ambavyo Yehova ameweka chini ya ukichwa wa Mwana wake. Wao pia ni kati ya “mali” ambazo Kristo amemkabidhi ‘mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara.’ (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, wale walio na tumaini la kuishi duniani wanapaswa kutambua kwamba Kristo ni Kichwa chao na kujitiisha kwa mtumwa mwaminifu na mwenye busara na Baraza lake Linaloongoza na pia kwa wanaume waliowekwa rasmi kuwa waangalizi katika kutaniko. (Ebr. 13:7, 17) Hilo linachangia umoja wa Kikristo.
11. Umoja wetu unategemea nini, na Paulo alitoa shauri gani lingine?
11 Umoja huo unategemea upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:14) Kwenye Waroma sura ya 12, Paulo anakazia hilo anaposema kwamba upendo wetu unapaswa kuwa “bila unafiki” na kwamba “katika upendo wa kindugu” tunapaswa kuwa na “upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.” Hilo linatufanya tuheshimiane. Mtume Paulo anasema hivi: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” Bila shaka, hatupaswi kufikiri kwamba upendo ni hisia tu ya moyoni. Tunapaswa kufanya yote tunayoweza ili kudumisha usafi wa kutaniko. Anapotoa shauri lake kuhusu upendo, Paulo anaongezea hivi: “Chukieni maovu, shikamaneni na mema.”
Njia au Mwendo wa Ukaribishaji-Wageni
12. Tunajifunza nini kuhusu ukaribishaji-wageni kutokana na Wakristo wa Makedonia ya kale?
12 Soma Waroma 12:13. Kuwapenda ndugu zetu kutatuchochea ‘kushiriki pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao’ na kulingana na uwezo wetu. Hata ikiwa tuna vitu vichache vya ulimwengu huu, tunaweza kushiriki na wengine vitu tulivyo navyo. Akiandika kuhusu Wakristo wa Makedonia, Paulo alisema hivi: “Wakati wa jaribu kubwa chini ya mateso shangwe yao nyingi na umaskini mkubwa ulifanya utajiri wa ukarimu wao uwe mwingi. Kwa maana hilo lilikuwa kulingana na uwezo wao halisi, ndiyo, mimi nashuhudia, kupita uwezo wao halisi, nao kwa kupenda kwao wenyewe waliendelea kutuomba kwa kusihi sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili na kushiriki katika huduma iliyokusudiwa watakatifu [huko Yudea].” (2 Kor. 8:2-4) Ingawa Wakristo wa Makedonia walikuwa maskini, walikuwa wakarimu sana. Waliona kuwa ni pendeleo kushiriki vitu vyao vya kimwili pamoja na ndugu zao maskini wa Yudea.
13. Maneno “fuateni mwendo wa ukaribishaji-wageni” yanamaanisha nini?
13 Maneno “fuateni mwendo wa ukaribishaji-wageni” yametafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki ambalo linamaanisha kuchukua hatua ya kwanza. Tafsiri ya Biblia ya The New Jerusalem Bible inatafsiri hivi maneno hayo: “Tafuta nafasi za kuwa mkaribishaji-wageni.” Nyakati nyingine ukaribishaji-wageni unaonyeshwa kwa kumwalika mtu fulani kwa ajili ya chakula, na tunastahili pongezi ikiwa tunafanya hivyo kwa upendo. Lakini tukichukua hatua ya kwanza ya kuwaalika wengine, tutagundua njia nyingine nyingi za kuwa wakaribishaji-wageni. Ikiwa hali yetu ya kiuchumi au ya kiafya haituruhusu kuwaalika wengine kwa ajili ya chakula, tunaweza kuwaonyesha ukaribishaji-wageni kwa kuwaalika kwa ajili ya kikombe cha kahawa, cha chai, au kinywaji cha aina nyingine.
14. (a) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ukaribishaji-wageni” linatokana na maneno gani? (b) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawajali wageni katika huduma?
14 Ukaribishaji-wageni unahusisha mtazamo wetu. Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “ukaribishaji-wageni” linatokana na maneno mawili ya msingi ambayo yanamaanisha “upendo” na “mgeni.” Tuna maoni gani kuhusu wageni, au watu tusiowajua? Wakristo wanaojitahidi kujifunza lugha nyingine ili wawahubirie habari njema wageni kutoka nchi nyingine ambao wamehamia katika eneo la kutaniko lao wanaweza kwa kweli kuonwa kuwa kati ya watu wanaofuata mwendo wa ukaribishaji-wageni. Bila shaka, wengi wetu hatuwezi kujifunza lugha nyingine. Hata hivyo, sote tunaweza kushiriki kikamilifu katika kuwasaidia wageni kwa kutumia vizuri kijitabu chetu Good News for People of All Nations (Une bonne nouvelle pour des gens de toutes nations), ambacho kina ujumbe wa Biblia katika lugha nyingi. Je, umepata matokeo mazuri kwa kutumia kijitabu hicho katika huduma?
Hisia-Mwenzi
15. Yesu aliweka jinsi gani mfano katika kufuata shauri la Waroma 12:15?
15 Soma Waroma 12:15. Shauri la Paulo katika mstari huo linaweza kuelezwa kwa maneno machache tu: Onyesha hisia-mwenzi. Tunahitaji kujifunza kuelewa na hata kuhisi kama mtu mwingine anavyohisi, iwe ana shangwe au amehuzunika. Ikiwa tunawaka roho, hisia zetu za shangwe au huruma kwa wengine zitaonekana. Wanafunzi 70 wa Kristo waliporudi wakiwa na shangwe baada ya kampeni ya kuhubiri na kuanza kusimulia matokeo mazuri ya kazi yao, Yesu mwenyewe ‘akawa na shangwe sana katika roho takatifu.’ (Luka 10:17-21) Alifurahi pamoja nao. Kwa upande mwingine, Yesu ‘alilia pamoja na watu waliokuwa wakilia’ wakati rafiki yake Lazaro alipokufa.—Yoh. 11:32-35.
16. Tunaweza kuonyesha jinsi gani hisia-mwenzi, na ni nani hasa wanaohitaji kufanya hivyo?
16 Tunataka kufuata mfano wa Yesu katika kuonyesha hisia-mwenzi. Mkristo mwenzetu anaposhangilia, tunataka kushangilia pamoja naye. Vivyo hivyo, tunapaswa kuwahurumia ndugu na dada zetu kwa sababu ya uchungu na maumivu yao. Mara nyingi, tunaweza kuwafariji sana waamini wenzetu ambao wanateseka kihisia ikiwa tutachukua wakati wa kuwasikiliza kwa huruma. Na nyakati nyingine, huenda tukaguswa moyo sana na hivyo kuonyesha hisia-mwenzi zetu za kweli kwa machozi. (1 Pet. 1:22) Wazee, hasa, wanapaswa kufuata shauri ambalo Paulo alitoa kuhusu kuonyesha hisia-mwenzi.
17. Tumejifunza mambo gani kutokana na Waroma sura ya 12, na ni mambo gani yatakayozungumziwa katika habari inayofuata?
17 Katika mistari ambayo tumezungumzia katika andiko la Waroma sura ya 12 tumepata mashauri tunayoweza kutumia katika maisha yetu binafsi tukiwa Wakristo na katika uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu. Katika habari inayofuata, tutachunguza mistari inayobaki ya sura hiyo, ambayo inaonyesha jinsi tunavyopaswa kuwaona na kushughulika na watu walio nje ya kutaniko la Kikristo, kutia ndani wapinzani na wale wanaotutesa.
-
-
“Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 15
-
-
“Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”
“Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—ROM. 12:18.
1, 2. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake onyo gani? (b) Tunaweza kupata wapi mashauri yanayoonyesha jinsi ya kukabiliana na upinzani?
YESU aliwaonya wafuasi wake kwamba wangepingwa na mataifa ya ulimwengu, na jioni iliyotangulia kifo chake, aliwaeleza sababu. Aliwaambia mitume wake hivi: “Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.”—Yoh. 15:19.
2 Mtume Paulo alijionea ukweli wa maneno hayo ya Yesu. Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, kijana aliyeambatana naye, Paulo aliandika hivi: “Wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha, kusudi langu, imani yangu, ustahimilivu wangu, upendo wangu, uvumilivu wangu, mateso yangu, masumbufu yangu.” Kisha Paulo akaongezea hivi: “Kwa kweli, wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:10-12) Katika sura ya 12 ya barua yake kwa Wakristo huko Roma, Paulo alitoa mashauri yenye hekima yaliyoonyesha jinsi walivyopaswa kukabiliana na upinzani. Maneno yake yanaweza kutupatia mwongozo katika wakati huu wa mwisho.
“Fanyeni Mambo Mema”
3, 4. Shauri la Waroma 12:17 linaweza kutumiwa jinsi gani (a) katika familia iliyogawanyika kidini? (b) tunaposhughulika na majirani?
3 Soma Waroma 12:17. Paulo alieleza kwamba tunapochukiwa, hatupaswi kulipiza kisasi. Ni jambo la maana sana kwa washiriki wa familia zilizogawanyika kidini kutii shauri hilo la Paulo. Mwenzi wa ndoa Mkristo anapinga kishawishi cha kulipiza kisasi kwa kuepuka kusema maneno yasiyo ya fadhili au kutenda bila fadhili. Hakuna faida yoyote ya ‘kulipa uovu kwa uovu.’ Badala yake, mtazamo kama huo unaweza tu kufanya hali iwe mbaya zaidi.
4 Paulo anapendekeza jambo bora la kufanya: “Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote.” Ikiwa mume asiye mwamini anasema mambo mabaya kuhusu imani ya mke wake ambaye ni mwamini, mke huyo anaweza kuzuia ugomvi mbaya sana usitokee nyumbani kwa kumwonyesha mume wake fadhili za kweli. (Met. 31:12) Carlos, ambaye sasa ni mshiriki wa familia ya Betheli, anasimulia jinsi ambavyo mama yake alishinda upinzani mkali sana kutoka kwa baba yake kwa kuendelea kuonyesha fadhili na kuitunza nyumba vizuri. “Alitutia moyo sisi watoto tumheshimu baba sikuzote. Alisisitiza kwamba nicheze na baba mchezo wa Kifaransa wa kuviringisha mipira chini (boules) hata ingawa sikupenda mchezo huo. Lakini hilo lilimfurahisha baba.” Mwishowe alianza kujifunza Biblia kisha akabatizwa. Kuhusu ‘kufanya mambo mema machoni pa watu wote,’ mara nyingi Mashahidi wa Yehova wameshinda chuki kwa kuwasaidia majirani wao wakati wa misiba.
Kuyeyusha Upinzani kwa “Makaa Yenye Moto”
5, 6. (a) Ni katika maana gani “makaa yenye moto” yanakusanywa juu ya kichwa cha adui? (b) Simulia jambo la kwenu lililoonwa ambalo linaonyesha jinsi kufuata shauri la Waroma 12:20 kunavyoweza kuwa na matokeo mazuri.
5 Soma Waroma 12:20. Bila shaka, Paulo alipochagua maneno yaliyo katika mstari huo, alikuwa akifikiria yale tunayosoma kwenye Methali 25:21, 22: “Ikiwa mtu anayekuchukia ana njaa, mpe mkate ale; na ikiwa ana kiu, mpe maji anywe. Kwa maana unakusanya makaa ya moto juu ya kichwa chake, na Yehova mwenyewe atakupa thawabu.” Paulo alipotoa shauri lililo katika Waroma sura ya 12, hakumaanisha kwamba makaa hayo ya mfano ni ya kumwadhibu au kumwaibisha mpinzani. Badala yake, inaonekana kwamba maneno ya methali hiyo pamoja na yale ambayo Paulo aliwaandikia Waroma, yalihusu njia iliyotumiwa zamani ya kuyeyusha mawe yenye chuma. Msomi Mwingereza wa karne ya 19, Charles Bridges alisema hivi: “Funika kabisa chuma kigumu juu na chini kwa kukusanya makaa yenye moto juu yake, na ukiweke chuma hicho juu ya moto. Ni mioyo michache sana iliyo migumu hivyo, ambayo haiwezi kuyeyushwa na nguvu nyingi sana za upendo wenye subira, unaojinyima, na wenye kuchoma.”
6 Sawa na “makaa yenye moto,” matendo ya fadhili yanaweza kuchochea mioyo ya wapinzani na labda kuyeyusha chuki yao. Matendo ya fadhili yanaweza kuwavutia watu na kuwafanya wawe na mtazamo mzuri kuelekea watu wa Yehova na ujumbe wa Biblia ambao wanahubiri. Mtume Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.”—1 Pet. 2:12.
‘Fanya Amani na Watu Wote’
7. Amani ambayo Kristo anawaachia wanafunzi wake ni nini, na inapaswa kutuchochea kufanya nini?
7 Soma Waroma 12:18. Katika jioni ya mwisho ambayo Yesu alikuwa pamoja na mitume wake, aliwaambia hivi: “Ninawaachia ninyi amani, ninawapa amani yangu.” (Yoh. 14:27) Amani ambayo Kristo anawaachia wanafunzi wake ni utulivu wa moyoni ambao wanapata wakati wanapohisi kwamba wanapendwa na kukubaliwa na Yehova Mungu na Mwana wake mpendwa. Amani hiyo ya moyoni inapaswa kutuchochea kuishi na wengine kwa amani. Wakristo wa kweli ni wapenda-amani na wafanya-amani.—Mt. 5:9.
8. Tunaweza jinsi gani kuwa wafanya-amani nyumbani na katika kutaniko letu?
8 Njia moja ya kuwa mfanya-amani katika familia ni kutatua haraka iwezekanavyo hali yoyote ya kutoelewana badala ya kuruhusu hali hizo ziwe mbaya zaidi. (Met. 15:18; Efe. 4:26) Hilo linahusu pia kutaniko la Kikristo. Mtume Petro anaonyesha kwamba kufuatia amani kunahusiana na kuuzuia ulimi. (1 Pet. 3:10, 11) Yakobo pia, baada ya kutoa shauri kali kuhusu kuutumia vizuri ulimi na uhitaji wa kuepuka wivu na ugomvi, aliandika hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki. Zaidi ya hayo, mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.”—Yak. 3:17, 18.
9. Tunapaswa kukumbuka nini tunapojitahidi “kufanya amani na watu wote”?
9 Katika maneno yake yaliyo kwenye Waroma 12:18, Paulo anaonyesha kwamba haitoshi tu kufanya amani katika familia na katika kutaniko. Anasema kwamba tunapaswa “kufanya amani na watu wote.” Hilo linatia ndani majirani, wafanyakazi wenzetu, wanashule wenzetu, na watu tunaokutana nao katika huduma yetu ya hadharani. Hata hivyo, mtume Paulo anafafanua zaidi shauri lake kwa kusema hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi.” Hilo linamaanisha kujitahidi kadiri tunavyoweza ili “kufanya amani na watu wote” lakini hatupaswi kulegeza kanuni za Mungu za uadilifu.
Kisasi Ni cha Yehova
10, 11. ‘Tunaiachia nafasi ghadhabu’ katika maana gani, na kwa nini hilo linafaa?
10 Soma Waroma 12:19. Hata tunaposhughulika na “wale wasio na mwelekeo unaofaa” kuhusu kazi yetu na ujumbe wetu, kutia ndani wale wanaotupinga moja kwa moja, tutaendelea “kujizuia chini ya uovu” na kutenda kwa “upole.” (2 Tim. 2:23-25) Paulo anawashauri Wakristo wasijilipizie kisasi lakini ‘waiachie nafasi ghadhabu.’ Paulo anazungumzia ghadhabu gani? Hakumaanisha kamwe kwamba tunapaswa kumwaga ghadhabu yetu wenyewe. Kwa wazi, tunaiachia nafasi ghadhabu ya Mungu. Tukiwa Wakristo, tunajua kwamba si daraka letu kulipiza kisasi. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu; usijionyeshe umewaka hasira ili tu kufanya uovu.” (Zab. 37:8) Naye Sulemani alishauri hivi: “Usiseme: ‘Nitalipiza uovu!’ Mtumaini Yehova, naye atakuokoa.”—Met. 20:22.
11 Jambo la hekima la kufanya wakati wapinzani wanapotuumiza ni kumwacha Yehova aamue ikiwa atawaadhibu na pia aamue wakati unaofaa wa kufanya hivyo. Ili kuonyesha kwamba alikuwa akizungumza kuhusu ghadhabu ya Yehova, Paulo aliongezea hivi: “Imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Linganisha na Kumbukumbu la Torati 32:35.) Ikiwa tungejaribu kujilipizia kisasi, tungekuwa tukitenda kwa kimbelembele, na kuchukua daraka la Yehova. Kwa kuongezea, tukifanya hivyo tutakuwa tukionyesha kwamba hatuamini ahadi hii ya Yehova: “Mimi nitalipa.”
12. Ghadhabu ya Yehova itafunuliwa wakati gani, na jinsi gani?
12 Mapema katika barua yake kwa Waroma, Paulo alisema hivi: “Ghadhabu ya Mungu inafunuliwa kutoka mbinguni juu ya watu wote wasiomwogopa Mungu na wasio waadilifu ambao wanaikandamiza kweli katika njia isiyo ya uadilifu.” (Rom. 1:18) Ghadhabu ya Yehova itafunuliwa kutoka mbinguni kupitia Mwana wake wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Hilo litakuwa “uthibitisho wa hukumu ya uadilifu ya Mungu,” kama Paulo alivyoeleza katika moja ya barua zake zilizoongozwa na roho takatifu: “Hii inazingatia kwamba ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu kuwalipa dhiki wale wanaowafanyia ninyi dhiki, lakini, kwenu ninyi mnaopata dhiki, kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.”—2 The. 1:5-8.
Kuushinda Uovu kwa Wema
13, 14. (a) Kwa nini hatushangai tunapopata upinzani? (b) Tunaweza kuwabariki jinsi gani wale wanaotutesa?
13 Soma Waroma 12:14, 21. Tukiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi zake, tunaweza bila wasiwasi kutumia nguvu zetu zote katika kazi ambayo ametupatia, kazi ya kuhubiri ‘habari njema ya ufalme katika dunia yote inayokaliwa.’ (Mt. 24:14) Tunajua kwamba utendaji huo wa Kikristo utaamsha hasira ya maadui wetu, kwa kuwa Yesu alituonya hivi: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mt. 24:9) Kwa hiyo, hatushangai wala kuvunjika moyo tunapopata upinzani. Mtume Petro aliandika hivi: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata. Kinyume chake, endeleeni kushangilia kwa maana ninyi ni washiriki katika mateso ya Kristo.”—1 Pet. 4:12, 13.
14 Badala ya kuwachukia wale wanaotutesa, tunajitahidi kuwafundisha, huku tukitambua kwamba huenda wengine wao wanatenda hivyo kwa kutojua. (2 Kor. 4:4) Tunajitahidi kutii shauri hili la Paulo: “Endeleeni kuwabariki wale wanaowatesa; muwe mkibariki wala msiwe mkilaani.” (Rom. 12:14) Njia moja ya kuwabariki wapinzani wetu ni kusali kwa ajili yao. Yesu alisema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Endeleeni kuwapenda adui zenu, kuwafanyia mema wale wanaowachukia, kuwabariki wale wanaowalaani, kusali kwa ajili ya wale wanaowatusi.” (Luka 6:27, 28) Mtume Paulo alijua kutokana na maisha yake mwenyewe kwamba mtesaji anaweza kugeuka na kuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo na mtumishi mwenye bidii wa Yehova. (Gal. 1:13-16, 23) Katika barua nyingine, Paulo alisema: “Tunapotukanwa, tunabariki; tunapoteswa, tunavumilia; tunapoharibiwa sifa, tunasihi.”—1 Kor. 4:12, 13.
15. Ni njia gani bora ya kuushinda uovu kwa wema?
15 Hivyo basi, Mkristo wa kweli anatii maneno ya mstari wa mwisho wa Waroma sura ya 12: “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” Chanzo cha uovu wote ni Shetani Ibilisi. (Yoh. 8:44; 1 Yoh. 5:19) Katika ufunuo ambao mtume Yohana alipewa, Yesu alifunua kwamba ndugu zake watiwa-mafuta ‘wamemshinda [Shetani] kwa sababu ya damu ya Mwana-Kondoo na kwa sababu ya neno la kutoa kwao ushahidi.’ (Ufu. 12:11) Hilo linaonyesha kwamba njia bora ya kumshinda Shetani na uvutano wake mwovu juu ya mfumo wa sasa wa mambo ni kwa kufanya mema kupitia kazi yetu ya kutoa ushahidi na kuhubiri habari njema ya Ufalme.
Kushangilia Katika Tumaini
16, 17. Andiko la Waroma sura ya 12 limetufundisha nini kuhusu (a) jinsi tunavyopaswa kutumia maisha yetu? (b) jinsi tunavyopaswa kutenda katika kutaniko? (c) jinsi tunavyopaswa kuwatendea watu ambao wanapinga imani yetu?
16 Mazungumzo yetu mafupi kuhusu sura ya 12 ya barua ya Paulo kwa Wakristo huko Roma yametukumbusha mambo mengi. Tumejifunza kwamba tukiwa watumishi waliojiweka wakfu kwa Yehova, tunapaswa kuwa tayari kujidhabihu. Huku tukichochewa na roho ya Mungu, tunatoa dhabihu hizo kwa kupenda kwa sababu nguvu zetu za kufikiri zimetusadikisha kwamba hayo ni mapenzi ya Mungu. Tunawaka roho na kutumia zawadi zetu mbalimbali kwa bidii. Tunatumika kwa unyenyekevu wote na kiasi, na kufanya yote tunayoweza ili kulinda umoja wetu wa Kikristo. Tunafuata mwendo wa ukaribishaji-wageni na kuonyesha hisia-mwenzi ya kweli.
17 Andiko la Waroma sura ya 12 linatupatia pia mashauri mengi kuhusu jinsi tunavyopaswa kukabiliana na upinzani. Hatupaswi kulipiza kisasi. Tunapaswa kujitahidi kuushinda upinzani kwa matendo ya fadhili. Tunapaswa kujitahidi sana kuishi kwa amani na watu wote kwa kadiri inavyowezekana, bila kuvunja kanuni za Biblia. Tunapaswa kufanya hivyo katika familia, katika kutaniko, kuelekea majirani wetu, kazini, shuleni, na katika huduma yetu ya hadharani. Hata tunapokabili upinzani wa moja kwa moja, tunajitahidi kabisa kuushinda uovu kwa wema, huku tukikumbuka kwamba kisasi ni cha Yehova.
18. Ni mashauri gani matatu yanayotolewa kwenye Waroma 12:12?
18 Soma Waroma 12:12. Kwa kuongezea mashauri hayo yote yenye hekima na yenye faida, Paulo anatoa mashauri mengine matatu. Kwa kuwa hatuwezi kamwe kufanya mambo hayo yote bila msaada wa Yehova, mtume Paulo anatushauri ‘tudumu katika sala.’ Hilo litatuwezesha kufuata shauri lake lingine la ‘kuvumilia chini ya dhiki.’ Mwishowe, tunahitaji kukazia akili zetu wakati ujao ambao Yehova ametuahidi na ‘kushangilia katika tumaini’ la uzima wa milele, iwe ni mbinguni au duniani.
-