-
Kimbia Shindano la Mbio kwa UvumilivuMnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 15
-
-
Kimbia Shindano la Mbio kwa Uvumilivu
“Acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”—EBR. 12:1.
1, 2. Mtume Paulo alilinganisha maisha ya Kikristo na nini?
KILA mwaka, mashindano ya mbio za masafa marefu yanafanywa katika sehemu mbalimbali. Wale ambao wanaonwa kuwa wakimbiaji hodari wanaingia katika mashindano hayo wakiwa na kusudi moja tu—kushinda. Lakini wakimbiaji wengine wengi wanaoshiriki katika mashindano hayo wanajua kwamba hawawezi kushinda. Hata hivyo, jambo la maana ambalo wanajivunia ni kukimbia mpaka mwisho wa mashindano.
2 Katika Biblia, maisha ya Kikristo yamelinganishwa na shindano la mbio. Mtume Paulo alikazia jambo hilo katika barua yake ya kwanza aliyowaandikia Wakristo wenzake katika jiji la kale la Korintho. Aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba wakimbiaji katika mbio wote hukimbia, lakini ni mmoja tu anayepokea tuzo? Kimbieni kwa namna ya kwamba mweze kupata tuzo.”—1 Kor. 9:24.
3. Kwa nini Paulo alisema kwamba ni mtu mmoja tu anayeshinda zawadi?
3 Je, Paulo alikuwa akisema kwamba mtu mmoja tu kati ya Wakristo hao ndiye angepata tuzo au zawadi ya uzima na wengine wote wangekimbia bure? Hapana! Wakimbiaji katika mashindano ya mbio walifanya mazoezi na kujikaza kwa bidii wakiwa na kusudi moja, kuwa washindi. Paulo alitaka Wakristo wenzake wajikaze kwa njia hiyo wanapotafuta uzima wa milele. Kwa kufanya hivyo, wangetumaini kupata zawadi ya uzima. Ndiyo, katika shindano la Kikristo, wote wanaokimbia mpaka mwisho wanapata zawadi.
4. Tunahitaji kuchunguza nini kuhusu shindano la mbio ambalo limewekwa mbele yetu?
4 Maneno hayo yanatutia moyo, lakini pia yanatufanya tufikirie kwa uzito jinsi tunavyokimbia mbio ya uzima leo. Kwa nini? Kwa sababu zawadi, yaani, uzima wa milele, mbinguni au katika Paradiso duniani, ni tumaini ambalo haliwezi kulinganishwa na kitu chochote. Ni kweli kwamba shindano hilo ni la masafa marefu na linachosha; kuna vizuizi, vikengeusha-fikira, na hatari nyingi njiani. (Mt. 7:13, 14) Inasikitisha kwamba wengine wamepunguza mwendo, wameacha kukimbia, au hata kuanguka njiani. Ni mitego na hatari gani zilizo katika shindano la mbio ya uzima? Unaweza kuziepuka jinsi gani? Unaweza kufanya nini ili umalize na hivyo kushinda shindano hilo la mbio?
Tunahitaji Uvumilivu ili Tushinde
5. Paulo alieleza nini katika Waebrania 12:1 kuhusu shindano la mbio?
5 Katika barua aliyowaandikia Wakristo Waebrania huko Yerusalemu na Yudea, Paulo alizungumzia tena mambo mbalimbali kuhusu michezo au mashindano ya mbio. (Soma Waebrania 12:1.) Hakueleza tu sababu ya kukimbia katika shindano hilo, bali pia jambo ambalo mtu anapaswa kufanya ili kushinda. Kabla ya kuchunguza mashauri ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo aliwaandikia Wakristo Waebrania ili tuone mambo tunayoweza kujifunza, acheni tuchunguze kile kilichomchochea Paulo kuandika barua hiyo na kile alichokuwa akijaribu kuwatia moyo wasomaji wake wafanye.
6. Wakristo walipata upinzani gani kutoka kwa viongozi wa kidini?
6 Wakristo wa karne ya kwanza, hasa wale walioishi Yerusalemu na Yudea, walikabiliana na majaribu na matatizo mengi. Walipata upinzani mkali kutoka kwa viongozi wa dini ya Kiyahudi, ambao bado walikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu. Mapema, viongozi hao walifanikiwa kumshtaki Yesu Kristo kuwa mchochezi na kufanya auawe kama mhalifu. Na walikuwa wameazimia kuendelea na upinzani wao. Katika kitabu cha Matendo, tunasoma masimulizi mengi yanayoeleza jinsi walivyowatisha na kuwashambulia Wakristo, na walianza baada tu ya matukio ya kimuujiza siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Bila shaka, hilo lilifanya maisha ya Wakristo hao waaminifu yawe magumu.—Mdo. 4:1-3; 5:17, 18; 6:8-12; 7:59; 8:1, 3.
7. Wakristo ambao Paulo aliandikia walikuwa wakiishi katika nyakati gani ngumu?
7 Wakristo hao walikuwa pia wakiishi katika kipindi kilichotangulia uharibifu wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Yesu alikuwa amewaambia kuhusu uharibifu ambao ungekuja juu ya taifa la Kiyahudi lenye kukosa uaminifu. Pia, aliwaambia wafuasi wake kuhusu matukio ambayo yangetukia kabla tu ya mwisho huo, na aliwapa maagizo ya waziwazi kuhusu yale ambayo wangefanya ili kuokoka. (Soma Luka 21:20-22.) Hivyo basi, wangefanya nini? Yesu aliwaonya hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja.”—Luka 21:34.
8. Ni nini ambacho huenda kilisababisha Wakristo fulani kupunguza mwendo au kuacha kukimbia?
8 Paulo alipoandika barua yake kwa Waebrania, miaka karibu 30 ilikuwa imepita tangu Yesu atoe onyo hilo. Je, mtazamo wa Wakristo hao ulibadilika baada ya muda kupita? Wengine walishindwa kuendelea kwa sababu ya upinzani na wakakengeushwa fikira na shughuli za kila siku za maisha na hivyo wakakosa kufanya maendeleo ya kiroho ambayo yangewatia nguvu. (Ebr. 5:11-14) Inaelekea wengine walifikiri kwamba maisha yangekuwa rahisi zaidi ikiwa wangeishi tu kama Wayahudi wengi waliowazunguka. Kwa vyovyote vile, Wayahudi hao hawakuwa wamemuacha Mungu kabisa; walikuwa bado wanafuata Sheria yake kwa kadiri fulani. Wakristo wengine walikuwa wameshawishiwa au kutishwa na watu fulani katika kutaniko ambao walisisitiza kwamba watu wafuate kabisa mapokeo na Sheria ya Musa. Paulo angesema nini ili kuwasaidia ndugu zake Wakristo waendelee kuwa macho kiroho na kuvumilia katika shindano la mbio?
9, 10. (a) Mwishoni mwa sura ya 10 ya Waebrania, tunasoma kitia-moyo gani cha Paulo? (b) Kwa nini Paulo aliandika kuhusu matendo ya uaminifu ya mashahidi wa nyakati za kale?
9 Inapendeza kuona jinsi Paulo alivyoongozwa na roho ya Mungu kujaribu kuwatia nguvu Wakristo Waebrania. Katika sura ya 10 ya barua yake, Paulo alieleza kwamba Sheria ilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja” na akaonyesha waziwazi thamani ya fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo. Mwishoni mwa sura hiyo, Paulo aliwahimiza hivi wasomaji wake: “Mnahitaji kuwa na uvumilivu, ili kwamba, baada ya kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi. Kwa maana bado ‘muda kidogo sana,’ na ‘yeye anayekuja atafika naye hatakawia.’”—Ebr. 10:1, 36, 37.
10 Katika Waebrania sura ya 11, Paulo anaeleza kwa ustadi maana ya kuwa na imani ya kweli katika Mungu. Na anaonyesha hilo kwa kutaja mifano ya kihistoria ya wanaume na wanawake walioonyesha imani. Je, alikuwa akizungumzia mambo ya ziada yasiyo ya lazima? Hapana. Mtume huyo alijua waabudu wenzake walihitaji kutambua kwamba ili kuwa na imani walipaswa kutenda kwa ujasiri na kuvumilia. Mfano mzuri sana uliowekwa na watumishi hao waaminifu wa nyakati za kale wa Yehova ungewatia nguvu Wakristo hao Waebrania kupambana na majaribu na matatizo waliyokuwa wakikabiliana nayo. Hivyo, baada ya kutaja matendo ya imani ya watu hao washikamanifu wa nyakati za kale, Paulo alisema hivi: “Kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi linalotuzunguka, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”—Ebr. 12:1.
‘Wingu la Mashahidi’
11. Kufikiria lile ‘wingu kubwa la mashahidi’ kunaweza kuwa na matokeo gani juu yetu?
11 ‘Wingu kubwa la mashahidi’ halikuwa wingu la watazamaji tu, ambao walikaa kitako ili kutazama shindano la mbio, timu, au mkimbiaji ambaye walimpenda akishinda. Badala yake, walishiriki wakiwa kama wakimbiaji katika shindano la mbio. Nao walifanikiwa kukimbia katika shindano hilo mpaka mwisho. Ingawa sasa wamekufa, wanaweza kuonwa kuwa wakimbiaji hodari ambao wanaweza kuwatia moyo wakimbiaji wapya katika shindano hilo la mbio. Wazia jinsi ambavyo mkimbiaji angehisi ikiwa angejua kwamba amezungukwa, au anatazamwa na wakimbiaji bora zaidi. Je, hangechochewa kujikaza kabisa au hata kufanya yote anayoweza katika shindano hilo? Mashahidi hao wa kale wangeweza kutoa ushahidi kwamba mtu anaweza kushinda shindano hilo la mbio la mfano, hata liwe lenye kuchosha kadiri gani. Kwa hiyo, kwa kuendelea kufikiria mfano wa ‘wingu hilo la mashahidi,’ Wakristo hao Waebrania wa karne ya kwanza wangepata ujasiri na hivyo ‘kukimbia kwa uvumilivu shindano la mbio,’ na sisi pia tunaweza kufanya hivyo leo.
12. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya watu ambao Paulo alitaja?
12 Waaminifu wengi ambao Paulo alitaja walikuwa na hali kama zetu. Kwa mfano, Noa aliishi wakati ulimwengu wa kabla ya Gharika ulipokuwa ukikaribia kwisha. Sisi pia tunaishi karibu na mwisho wa mfumo huu wa mambo. Abrahamu na Sara waliagizwa watoke katika nchi yao ili kwenda kuendeleza ibada ya kweli na kungojea ahadi ya Yehova itimizwe. Tunatiwa moyo kujikana wenyewe na hivyo kupata kibali cha Yehova na baraka ambazo ameweka akiba kwa ajili yetu. Musa alisafiri katika jangwa lenye kutisha, akielekea kwenye ile Nchi ya Ahadi. Sisi pia tunaishi katika ulimwengu huu mwovu unaokaribia kwisha na tuko safarini kuelekea kwenye ulimwengu mpya ambao Yehova ametuahidi. Ni jambo la maana kwetu kutafakari kuhusu maisha ya watu hao waaminifu. Tunaweza kuiga mambo ambayo watu hao walipatwa nayo, na pia mambo waliyofanya ili kumpendeza Yehova na kujifunza kutokana na mambo ambayo hayakumpendeza.—Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11.
Ni Nini Kilichowasaidia Kufanikiwa?
13. Noa alipambana na hali gani ngumu, na ni nini kilichomwezesha kuzishinda?
13 Ni nini kilichowasaidia watumishi hao wa Yehova kuvumilia na kufanikiwa katika shindano la mbio? Ona yale ambayo Paulo aliandika kumhusu Noa. (Soma Waebrania 11:7.) Kuja kwa “gharika ya maji duniani [ambayo ingeharibu] wote wenye mwili” lilikuwa jambo ambalo Noa ‘alikuwa bado hajaona.’ (Mwa. 6:17) Ni jambo ambalo halikuwa limewahi kutukia kabla ya hapo, jambo la ajabu kabisa. Hata hivyo, Noa hakuwa na shaka au hata kufikiri kwamba gharika haingeweza kuja kamwe. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa na imani kwamba jambo lolote ambalo Yehova alisema, angetimiza. Noa hakufikiri kwamba jambo ambalo aliombwa afanye lilikuwa gumu sana. Badala yake, “alifanya vivyo hivyo.” (Mwa. 6:22) Tukifikiria mambo yote ambayo Noa alipaswa kufanya, yaani, kujenga safina, kukusanya wanyama, kujaza chakula ndani ya safina kwa ajili ya wanadamu na wanyama, kuhubiri ujumbe wa kuonya, na kujenga hali ya kiroho ya familia yake, haikuwa rahisi kwake kufanya “vivyo hivyo.” Hata hivyo, imani ya Noa na uvumilivu wake uliokoa uhai na kumletea yeye na familia yake baraka nyingi.
14. Ni majaribu gani ambayo Abrahamu na Sara walivumilia, na wanatufundisha somo gani?
14 Abrahamu na Sara ndio wanaofuata kwenye orodha ya Paulo ya ‘wingu la mashahidi linalotuzunguka.’ Waliambiwa waondoke na kuacha maisha yao ya kawaida huko Uru, na hawakuwa na hakika kuhusu wakati wao ujao. Lakini waliweka mfano mzuri kwa kuwa na imani isiyoyumba-yumba na kutii katika nyakati za majaribu. Kwa kufaa, Abrahamu anaitwa “baba ya wale wote walio na imani,” kwa sababu alijidhabihu sana kwa ajili ya ibada ya kweli. (Rom. 4:11) Paulo alitaja tu mambo makuu kwa sababu wasomaji wake walijua vizuri maisha ya Abrahamu. Hata hivyo, Paulo anatufundisha hapa somo kubwa sana: “Katika imani hawa wote [kutia ndani Abrahamu na familia yake] walikufa, ijapokuwa hawakupata utimizo wa zile ahadi, bali waliziona kwa mbali na kuzikaribisha na kutangaza hadharani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda katika nchi.” (Ebr. 11:13) Ni wazi kwamba imani yao katika Mungu na uhusiano wao wa kibinafsi pamoja naye uliwasaidia kukimbia katika shindano hilo kwa uvumilivu.
15. Kwa nini Musa alichagua kubadili njia yake ya maisha?
15 Musa ni mfano mwingine mzuri wa mtumishi wa Yehova katika ‘wingu hilo la mashahidi.’ Musa aliacha maisha mazuri sana ya utajiri, “akachagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu.” Ni nini kilichomchochea kufanya hivyo? Paulo alijibu hivi: “Alikaza macho kwenye malipo ya thawabu. . . . Aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Soma Waebrania 11:24-27.) Musa hakukengeushwa na “kufurahia dhambi kwa muda.” Musa alimwona Mungu na ahadi zake kuwa halisi sana hivi kwamba alionyesha uvumilivu na ujasiri wa pekee. Alijitahidi sana bila kuchoka kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri na kwenda katika Nchi ya Ahadi.
16. Kwa nini Musa hakuvunjika moyo alipokatazwa kuingia katika Nchi ya Ahadi?
16 Sawa na Abrahamu, Musa hakuona utimizo wa ahadi ya Mungu katika maisha yake. Kabla tu ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Mungu alimwambia Musa hivi: “Kutoka mbali utaiona nchi, lakini hutaingia katika nchi ninayowapa wana wa Israeli.” Ilikuwa hivyo kwa sababu mapema yeye na Haruni, ‘walitenda isivyofaa kumwelekea Mungu katikati ya wana wa Israeli kwenye maji ya Meriba,’ walipokasirishwa na uasi wa watu. (Kum. 32:51, 52) Je, Musa alivunjika moyo au kuwa na kinyongo? Hapana. Alitangaza baraka juu ya Waisraeli na akamalizia kwa maneno haya: “Una furaha, Ee Israeli! Ni nani aliye kama wewe, kikundi cha watu kinachofurahia wokovu wa Yehova, aliye ngao ya msaada wako, na Yule aliye upanga wako wa adhama?”—Kum. 33:29.
Mambo Tunayojifunza
17, 18. (a) Kuhusu shindano letu la mbio ya uzima, tunaweza kujifunza nini kutokana na ‘wingu la mashahidi’? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?
17 Baada ya kuchunguza maisha ya wale wanaofanyiza ‘wingu la mashahidi linalotuzunguka,’ ni wazi kwamba ili tukimbie shindano la mbio mpaka mwisho, ni lazima tuwe na imani kabisa katika Mungu na ahadi zake. (Ebr. 11:6) Hatupaswi kuwa na imani ya kijuu-juu tu; imani inapaswa kuwa jambo kuu katika maisha yetu. Tofauti na wale wasio na imani, watumishi wa Yehova wanajua kwamba kuna wakati ujao mzuri ambao amewaahidi. Tunaweza ‘kumwona Yeye asiyeonekana’ na hivyo kukimbia shindano la mbio kwa uvumilivu.—2 Kor. 5:7.
18 Shindano la mbio ambalo Wakristo wanakimbia si rahisi. Hata hivyo, tunaweza kufanikiwa kumaliza shindano hilo. Katika habari inayofuata, tutachunguza msaada mwingine ambao unaweza kutusaidia.
-
-
‘Kimbieni Ili Kwamba Mpate Tuzo’Mnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 15
-
-
‘Kimbieni Ili Kwamba Mpate Tuzo’
“Kimbieni kwa namna ya kwamba mweze kupata tuzo.”—1 KOR. 9:24.
1, 2. (a) Paulo alitumia mfano gani ili kuwatia moyo Wakristo Waebrania? (b) Watumishi wa Mungu wanatiwa moyo wafanye nini?
KATIKA barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo alitumia mfano mzuri sana wa shindano la mbio ili kuwatia moyo Wakristo wenzake. Aliwakumbusha kwamba hawakuwa wakikimbia peke yao katika shindano la mbio ya uzima. Walikuwa wamezungukwa na ‘wingu kubwa la mashahidi,’ ambao walifanikiwa kumaliza shindano hilo. Kukumbuka matendo ya imani na bidii ya wakimbiaji hao wa nyakati za kale kungewachochea Wakristo Waebrania wasonge mbele na wasiache kukimbia katika shindano lao la mbio.
2 Katika habari iliyotangulia, tulizungumzia maisha ya watu fulani kati ya ‘wingu hilo la mashahidi.’ Wote walionyesha kwamba imani isiyoyumba-yumba iliwawezesha kubaki washikamanifu kwa Mungu, kana kwamba walikuwa wakisonga mbele katika shindano la mbio mpaka mwisho. Tunaweza kujifunza somo fulani kutokana na jinsi walivyofanikiwa. Kama tulivyozungumzia katika habari hiyo, Paulo aliwatia moyo hivi watumishi wenzake, kutia ndani sisi: “Acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”—Ebr. 12:1.
3. Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na shauri la Paulo kuhusu wakimbiaji katika michezo ya Wagiriki?
3 Kuhusu shindano la mbio za miguu, ambalo ni kati ya mashindano yaliyopendwa sana zamani, kitabu kimoja (Backgrounds of Early Christianity) kinatuambia kwamba “Wagiriki walifanya mazoezi na walishindana wakiwa uchi.”a Wakimbiaji walikimbia wakiwa uchi kwa sababu hawakutaka kitu chochote chenye uzito kiwazuie kushinda tuzo au zawadi. Ingawa leo tunaweza kuona kukimbia uchi kuwa ukosefu wa kiasi na heshima, Wagiriki hao walikimbia hivyo wakiwa na kusudi moja tu la kushinda zawadi. Wazo la Paulo lilikuwa kwamba ili kushinda zawadi katika shindano la mbio ya uzima, ni jambo la maana kwa wakimbiaji kuondoa katika maisha yao kitu chochote ambacho kinaweza kuwazuia kupata zawadi ya uzima wa milele. Hilo lilikuwa shauri zuri kwa Wakristo Waebrania, na ni shauri zuri kwetu leo pia. Ni uzito au mizigo gani ambayo inaweza kutuzuia kupata zawadi katika shindano la mbio ya uzima?
“Tuondoe Kila Uzito”
4. Watu katika siku za Noa walijishughulisha sana na mambo gani?
4 Paulo alitushauri “tuondoe kila uzito.” Hilo linatia ndani kila kitu ambacho kinaweza kutuzuia kukazia fikira kikamili shindano la mbio na kutuzuia tusijitahidi kabisa kumaliza shindano hilo. Ni vitu gani vinavyoweza kutuongezea uzito? Yesu anatusaidia kuelewa jambo hilo. Alizungumza kuhusu wakati wa Noa, ambaye alikuwa mmoja wa watu wenye imani waliotajwa na Paulo. Yesu alieleza hivi: “Sawa na vile ilivyotukia katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa pia katika siku za Mwana wa binadamu.” (Luka 17:26) Yesu hakuwa akizungumza hasa kuhusu uharibifu mkubwa sana ambao utakuja; alikuwa akizungumza kuhusu namna watu walivyokuwa wakiishi. (Soma Mathayo 24:37-39.) Watu wengi katika siku za Noa hawakupendezwa na mambo ya Mungu, wala hawakujaribu kumpendeza. Ni nini kilichowakengeusha fikira? Si mambo yasiyo ya kawaida. Yalikuwa mambo ya kawaida ya maisha kama vile kula, kunywa, na kuoa. Kama Yesu alivyosema, tatizo lao hasa lilikuwa kwamba “hawakujali.”
5. Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanikiwa kumaliza shindano la mbio?
5 Kama Noa na familia yake, tuna mambo mengi ya kufanya kila siku. Tunahitaji kufanya kazi ili kujitunza wenyewe na familia yetu. Hilo linaweza kuchukua sehemu kubwa ya wakati, nguvu, na mali zetu. Ni rahisi kuhangaikia sana mahitaji ya maisha hasa tunapokuwa na matatizo ya kiuchumi. Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, pia tuna madaraka mengine ya kiroho ambayo ni ya maana. Tunahubiri, tunatayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na tunafanya funzo la kibinafsi na ibada ya familia ili tuendelee kuwa na nguvu kiroho. Ingawa Noa alikuwa na mambo mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, “alifanya vivyo hivyo.” (Mwa. 6:22) Bila shaka, ikiwa tunataka kumaliza kukimbia shindano la mbio ya Kikristo ni jambo la maana kupunguza uzito tunaobeba na pia kuepuka kujitwika mzigo wowote usio wa lazima.
6, 7. Tunapaswa kukumbuka mashauri gani ya Yesu?
6 Paulo alimaanisha nini aliposema tuondoe “kila uzito”? Bila shaka, hatuwezi kujiondolea kabisa kila daraka tulilo nalo. Kuhusiana na hilo, kumbuka maneno haya ya Yesu: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” (Mt. 6:31, 32) Maneno ya Yesu yanamaanisha kwamba hata vitu vinavyoitwa eti vya kawaida kama vile chakula na nguo vinaweza kuwa mzigo au vitu vya kukwaza tukivitanguliza maishani.
7 Fikiria maneno haya ya Yesu: “Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” Maneno hayo yanamaanisha kwamba Baba yetu wa mbinguni, Yehova, atatimiza sehemu yake ili kutosheleza mahitaji yetu. Kwa hakika, kuwa na “vitu hivi vyote” hakumaanishi kupata kila kitu tunachopenda au tunachotaka. Hata hivyo, tunaambiwa tusihangaikie “vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa.” Kwa nini? Baadaye, Yesu aliwashauri wasikilizaji wake hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.
8. Kwa nini huu hasa ndio wakati wa ‘kuondoa kila uzito’?
8 Mstari wa kumalizia mbio uko tu mbele yetu. Ni jambo lenye kuhuzunisha kama nini ikiwa tutajiruhusu tulemewe na mizigo mizito isiyo ya lazima ambayo inaweza kutuzuia tukiwa karibu sana kumaliza mbio! Hivyo, shauri hili la mtume Paulo ni lenye hekima kwelikweli: “Ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu.” (1 Tim. 6:6) Tukichukua kwa uzito maneno ya Paulo, tutakuwa na nafasi nzuri zaidi ya kupata ile zawadi.
“Dhambi Ambayo Hututatanisha kwa Urahisi”
9, 10. (a) Maneno “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi” yanamaanisha nini? (b) Tunaweza kutegwa au kutatanishwa jinsi gani?
9 Zaidi ya kuondoa “kila uzito,” Paulo alisema tuondoe pia “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” Hiyo inaweza kuwa nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kutatanisha kwa urahisi’ linapatikana mara moja tu ndani ya Biblia, katika mstari huo. Msomi mmoja anayeitwa Albert Barnes alisema hivi: “Kama vile mkimbiaji wa wakati huo alivyokuwa mwangalifu ili asivae nguo ambayo ingemfunga miguu na kumzuia asikimbie, ndivyo Mkristo anavyopaswa hasa kuondoa kitu chochote kama hicho kinachoweza kumzuia asikimbie.” Mkristo anaweza kutatanishwa jinsi gani hivi kwamba imani yake idhoofike?
10 Mkristo hapotezi imani yake kwa ghafula tu. Hilo linaweza kutokea hatua kwa hatua, na hata bila kujua. Mwanzoni mwa barua yake, Paulo alionya kuhusu hatari ya ‘kupeperushwa’ na kusitawisha “moyo mwovu unaokosa imani.” (Ebr. 2:1; 3:12) Nguo ya mkimbiaji ikimtega miguu, bila shaka ataanguka. Hatari ya kutegwa ni kubwa hasa ikiwa mkimbiaji anapuuza hatari ya kuvaa nguo fulani wakati anapokimbia. Ni nini kinachoweza kumfanya apuuze hatari hiyo? Labda ni kutojali au kujiamini kupita kiasi au vikengeusha-fikira fulani. Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na shauri la Paulo?
11. Ni nini kinachoweza kufanya tupoteze imani?
11 Tunapaswa kukumbuka kwamba mambo ambayo huenda tunafanya kwa siku nyingi ndiyo yanayosababisha tupoteze imani. Msomi mwingine anasema kwamba “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi” ni ile “dhambi iliyo na uvutano mkubwa zaidi juu yetu kwa sababu ya hali zetu, udhaifu wetu, na watu tunaoshirikiana nao.” Wazo ni kwamba mazingira yetu, udhaifu wetu wenyewe, na watu tunaoshirikiana nao ni mambo ambayo yanaweza kuwa na uvutano mkubwa juu yetu. Mambo hayo yanaweza kudhoofisha imani yetu au hata kufanya tuipoteze.—Mt. 13:3-9.
12. Ni vikumbusho gani ambavyo tunapaswa kuchukua kwa uzito ili tusipoteze imani?
12 Kwa miaka mingi, mtumwa mwaminifu na mwenye busara amekuwa akitukumbusha kuwa waangalifu kuhusu mambo tunayotazama na kusikiliza, yaani, mambo ambayo mioyo na akili zetu zinakazia. Tumeonywa kuhusu hatari ya kujitatanisha kwa kutafuta sana pesa na mali. Tunaweza kukengeushwa na vitumbuizo vinavyovutia sana au vitu vingi vipya vinavyotengenezwa siku baada ya siku. Ni hatari sana kuona kwamba mashauri kama hayo yanatunyima uhuru na yanawahusu tu wengine, na kwamba sisi tumekingwa kutokana na hatari hizo. Ulimwengu wa Shetani unatutatanisha kwa njia za ujanja na za udanganyifu. Kutojali, kujiamini kupita kiasi, na vikengeusha-fikira vimewaangusha wengine, na mambo hayo yanaweza kuharibu tumaini letu la kupata zawadi ya uzima.—1 Yoh. 2:15-17.
13. Tunaweza kujilinda jinsi gani na uvutano mbalimbali wenye kudhuru?
13 Kila siku, watu walio katika ulimwengu wa Shetani wanajaribu kutushawishi ili tuwe na miradi, mwenendo, na kufikiri kama wao. (Soma Waefeso 2:1, 2.) Lakini tunaweza kuamua jinsi tutakavyotenda tunaposhawishiwa na mawazo hayo. “Hewa” ambayo Paulo alitaja inasababisha kifo. Tunapaswa kuwa macho kila mara ili tusisongwe, au kukosa hewa safi, na hivyo kushindwa kumaliza shindano la mbio. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kukimbia katika shindano hilo la mbio? Kwa kweli Yesu ndiye mkimbiaji mkamilifu anayetuongoza katika shindano hilo. (Ebr. 12:2) Pia, tuna mfano wa Paulo ambaye alijiona kuwa kati ya wakimbiaji katika shindano la mbio ya Kikristo na akawahimiza waamini wenzake wamwige.—1 Kor. 11:1; Flp. 3:14.
Jinsi ‘Unavyoweza Kupata Tuzo’
14. Paulo alikuwa na maoni gani kuhusu jinsi alivyoshiriki katika shindano la mbio?
14 Paulo alikuwa na maoni gani kuhusu jinsi alivyoshiriki katika shindano la mbio? Katika maneno yake ya mwisho kwa wazee wa Efeso, alisema hivi: “Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu.” (Mdo. 20:24) Alikuwa tayari kudhabihu kila kitu, kutia ndani uhai wake, ili kumaliza shindano hilo la mbio. Bidii na kazi yote ambayo Paulo alifanya kuhusiana na habari njema ingekuwa ya bure ikiwa angeshindwa kumaliza shindano hilo. Hata hivyo, hakujiamini na kufikiri kwamba bila shaka angefanikiwa kushinda shindano hilo la mbio. (Soma Wafilipi 3:12, 13.) Alisema hivi mwishoni mwa maisha yake akiwa na uhakika wa kadiri fulani: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.”—2 Tim. 4:7.
15. Paulo aliwatia moyo jinsi gani wakimbiaji wenzake katika shindano la mbio?
15 Zaidi ya hayo, Paulo alikuwa na tamaa kubwa ya kuona Wakristo wenzake wakimaliza shindano la mbio bila kushindwa njiani. Kwa mfano, aliwatia moyo Wakristo huko Filipi wafanye kazi kwa bidii kwa ajili ya wokovu wao. Walihitaji kuendelea “kulishika sana neno la uzima.” Aliendelea kusema hivi: “Ili niwe na sababu ya kufurahi katika ile siku ya Kristo, kwamba sikukimbia bure wala kufanya kazi kwa bidii bure.” (Flp. 2:16) Vivyo hivyo, aliwatia moyo hivi Wakristo Wakorintho: “Kimbieni kwa namna ya kwamba mweze kupata tuzo.”—1 Kor. 9:24.
16. Kwa nini kusudi au zawadi inapaswa kuwa wazi katika akili zetu?
16 Katika shindano refu la mbio, kama vile mashindano ya masafa marefu, mstari wa kumalizia hauonekani mwanzoni. Hata hivyo, katika muda wote wa shindano hilo, mkimbiaji anakazia fikira mstari huo wa kumalizia. Anakazia fikira zaidi mstari wa kumalizia anapojua kwamba yuko karibu kutimiza kusudi lake. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo katika shindano letu la mbio. Kusudi, au zawadi, inapaswa kuwa halisi kwetu. Hilo litatusaidia kupata zawadi hiyo.
17. Imani inahusika jinsi gani katika kuendelea kukazia fikira zawadi?
17 Paulo aliandika hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Ebr. 11:1) Abrahamu na Sara walikuwa tayari kuacha maisha ya starehe na kuishi wakiwa “wageni na wakaaji wa muda katika nchi.” Ni nini kilichowasaidia kufanya hivyo? ‘Waliona kwa mbali utimizo wa ahadi za Mungu.’ Musa alikataa “kufurahia dhambi kwa muda” na pia “hazina za Misri.” Alipata jinsi gani imani na nguvu za kufanya hivyo? “Alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.” (Ebr. 11:8-13, 24-26) Inaeleweka kwa nini Paulo alisema kwamba kila mmoja wa watu hao alitenda “kwa imani.” Imani iliwawezesha kuepuka kukazia fikira majaribu na matatizo yaliyowapata na ikawasaidia kuona mambo ambayo Mungu alikuwa akifanya na yale ambayo bado angefanya kwa faida yao.
18. Tunaweza kuchukua hatua gani ili kuepuka “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi”?
18 Tukitafakari juu ya wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11 na kuiga mfano wao, tunaweza kusitawisha imani na kuepuka “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Ebr. 12:1) Pia, tunaweza ‘kufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri’ kwa kukusanyika pamoja na watu ambao wanasitawisha imani kama hiyo.—Ebr. 10:24.
19. Una maoni gani kuhusu kuendelea kukazia fikira zawadi?
19 Tunakaribia mwisho wa shindano letu la mbio. Ni kana kwamba tunaona mstari wa kumalizia shindano hilo. Kupitia imani na kwa msaada wa Yehova, sisi pia tunaweza ‘kuondoa kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.’ Ndiyo, tunaweza kukimbia kwa namna ya kwamba tuweze kupata tuzo au zawadi, yaani, baraka ambazo Mungu na Baba yetu, Yehova, aliahidi.
[Maelezo ya Chini]
a Michezo hiyo iliwachukiza Wayahudi wa nyakati za kale. Kitabu cha pili cha Makabayo ambacho hakikuongozwa na roho takatifu, kinasema kwamba Wayahudi wengi walikasirika wakati Kuhani Mkuu Yasoni aliyekuwa mwasi-imani alipopendekeza kujengwa kwa jumba la mazoezi huko Yerusalemu ili kuwafanya watu wafuate utamaduni wa Ugiriki.—2 Mak. 4:7-17.
-