-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 205]
Milton Henschel akitoa hotuba kwenye Kusanyiko la Kimataifa la 1992 la “Wachukuaji Nuru” katika Uwanja wa Kirov, St. Petersburg
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“TUNA FURAHA NA UHURU ULIOJE!”
Kwa sababu nchi ya Finland ipo karibu na Urusi, Baraza Linaloongoza liliiomba ofisi ya tawi ya Finland isaidie kupanga kusanyiko la kimataifa huko St. Petersburg, Urusi lililofanyika, Juni 26 hadi 28, 1992. Akina ndugu walihisije kukusanyika kwa uhuru baada ya kuishi chini ya marufuku ya zaidi ya miaka 50? Ndugu mmoja anakumbuka: “Tulikuwa maelfu kwenye uwanja wa kusanyiko. Machozi yalibubujika bila kukoma. Ilikuwa furaha na uhuru ulioje! Hatukuwazia kuwa na uhuru kama huo katika mfumo huu wa mambo. Lakini Yehova aliwezesha jambo hilo. Tulikumbuka jinsi tulivyotengwa katika seli tukiwa watano katika kambi yenye ua mrefu na wanne kati yetu wangempasha joto yule wa tano kwa zamu. Uwanja wa kusanyiko ulikuwa na ukuta mrefu. Lakini hatukutaka kutoka hapa. Hatuwezi kueleza hisia hiyo.
“Tulilia muda wote wa kusanyiko. Tulilia kwa shangwe ya kuona muujiza huo. Ingawa tulikuwa na umri wa zaidi ya miaka 70, tulitembea kana kwamba tuna mabawa. Tulisubiri uhuru huo kwa miaka 50. Kwanza Yehova aliruhusu tuhamishwe hadi Siberia, kisha tufungwe gerezani na kwenye kambi. Lakini sasa tulikuwa katika uwanja wa kusanyiko! Yehova ana nguvu kuliko mtu mwingine yeyote. Tulisimama tukitazamana na tukalia. Hakuna yeyote aliyeamini hilo lilikuwa likitukia. Baadhi ya vijana walituzunguka na kutuuliza: ‘Mna tatizo lolote? Je, kuna mtu yeyote aliyewaumiza?’ Lakini hatungeweza kujibu kwa sababu ya kulia. Huku tukilia, mmoja wetu alisema, ‘Tunalia kwa shangwe!’ Tuliwasimulia jinsi tulivyomtumikia Yehova miaka mingi chini ya marufuku. Na sasa hatukuweza kuamini kwamba ghafula Yehova amebadili kila kitu.”
Baada ya kusanyiko hilo lisilosahaulika, ofisi ya tawi ya Finland iliombwa itume mapainia wa pekee 15 nchini Urusi. Julai 1, 1992, Hannu na Eija Tanninen, wenzi wa ndoa wenye bidii kutoka Finland, walifika huko St. Petersburg. Mwanzoni, jambo gumu zaidi walilokabili ni kujifunza Kirusi. Baada ya somo lao la kwanza katika lugha hiyo, walienda kuhubiri na kuwatolea watu funzo la Biblia. Hannu anakumbuka hivi: “Katika miaka ya mapema ya 1990, karibu kila mtu alitaka kujifunza Biblia. Tulipohubiri barabarani, watu walitueleza walipoishi. Wote walitaka vichapo. Ikiwa ungempa mmoja gazeti au trakti, wengine kumi walipoiona walikuja na kuomba vichapo. Watu walichukua vichapo na wakaanza kusoma hapohapo barabarani au kwenye gari-moshi.”
Kuanzia Oktoba 1992, mapainia wengi wa pekee walitoka Poland pia. Kikundi cha kwanza kilitia ndani dada waseja. Baada ya muda mfupi, kikundi cha pili kutoka Poland kiliwasili na kikatumwa St. Petersburg.
-