-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KUPELEKWA UHAMISHONI SIBERIA
Licha ya upinzani wenye ukatili kutoka kwa wenye mamlaka, Mashahidi waliendelea kuhubiri kwa bidii. Hilo liliwakasirisha wakuu wa serikali huko Moscow. Shirika la KGB ndilo lililokasirishwa zaidi. Februari 19, 1951, maofisa wa shirika hilo walimwandikia Stalin barua iliyosema: “Ili kuzuia utendaji unaopinga Muungano wa Sovieti wa kikundi haramu cha wafuasi wa Yehova, MGB [Wizara ya Usalama wa Kitaifa, ambayo baadaye iliitwa KGB] ya USSR inaona ni muhimu kuwahamisha hadi wilaya za Irkutsk na Tomsk.” Shirika la KGB liliwajua Mashahidi wote na lilimwomba Stalin ruhusa ya kuwahamisha watu 8,576 kutoka jamhuri sita za Muungano wa Sovieti na kuwapeleka hadi Siberia. Stalin aliwaruhusu.
Magdalina Beloshitskaya anakumbuka: “Saa nane usiku Jumapili, Aprili 8, 1951, tuliamshwa mlango wetu ulipobishwa kwa kishindo. Mama aliruka kutoka kitandani na akakimbia na kumkuta askari amesimama mlangoni. ‘Mnapelekwa uhamishoni Siberia kwa sababu ya kumwamini Mungu,’ akatangaza. ‘Tunawapa saa mbili mpakie vitu vyenu. Chukueni chochote humu ndani, lakini hamruhusiwi kuchukua mbegu, unga, na nafaka. Pia hamruhusiwi kuchukua fanicha, vifaa vya mbao, na cherehani. Msichukue chochote kilicho nje ya nyumba. Bebeni tu shuka, blanketi, nguo, na mifuko yenu na mtoke.’
“Tulikuwa tumesoma katika vichapo vyetu kwamba kulikuwa na kazi nyingi upande wa mashariki wa nchi yetu. Sasa tulielewa kwamba wakati ulikuwa umefika wa kufanya kazi hiyo.
“Hakuna aliyelia. Askari alishangaa na kusema, ‘Hamjatokwa na machozi hata kidogo.’ Tulimwambia kwamba tangu 1948 tulikuwa tukisubiri kuhamishwa. Tulimwomba ruhusa tuchukue angalau kuku mmoja lakini akakataa. Askari hao waligawana mifugo yetu. Waligawana kuku wetu huku tukiwatazama. Mmoja alichukua watano, mwingine sita, na mwingine akapata watatu au wanne. Kuku wawili tu walipobaki, ofisa aliamuru wachinjwe nasi tukapewa kuku hao.
“Binti yangu mwenye umri wa miezi minane tu alikuwa amelala. Tuliuliza ikiwa tungeruhusiwa kubeba kitanda chake, lakini ofisa akaamuru kivunjwe-vunjwe. Kisha akatupa sehemu ambayo ingeweza kumbeba mtoto.
“Muda si muda, majirani walijua tunapelekwa uhamishoni. Mmoja wao alikuja na mfuko mdogo wenye mkate na tulipokuwa tukiondoka aliutupa ndani ya gari la kukokotwa lililokuwa limetubeba. Askari aliuona na akautupa nje. Tulikuwa watu sita, yaani, mimi, Mama, ndugu zangu wawili, mume wangu, na binti yetu mwenye umri wa miezi minane. Tulipotoka kijijini, tuliingizwa haraka ndani ya gari na kupelekwa kwenye kituo kikuu cha eneo hilo ambako hati zetu zilijazwa. Kisha tukabebwa kwa lori na kupelekwa kwenye kituo cha reli.
“Ilikuwa Jumapili, siku yenye jua lenye kupendeza. Kituo hicho kilikuwa kimejaa watu—wanaohamishwa na waliokuja kutazama. Lori lililokuwa limetubeba lilisimama karibu na behewa la gari-moshi ambamo ndugu zetu tayari walikuwa. Gari-moshi lilipojaa, askari walihakikisha kila mtu yumo kwa kutumia jina lake la pili. Behewa letu lilikuwa na watu 52. Wale waliokuja kutuaga walianza kulia. Lilikuwa jambo la kustaajabisha kwani hata hatukuwajua wengine kati yao. Lakini wao walijua kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova na tulikuwa tunapelekwa uhamishoni Siberia. Gari-moshi lilipiga honi kwa nguvu. Kisha akina ndugu wakaanza kuimba wimbo katika Kiukrainia: ‘Upendo wa Kristo na uwe pamoja nanyi. Tukimpa Yesu Kristo utukufu tutakutana tena katika Ufalme wake.’ Wengi wetu tulikuwa na tumaini hakika na imani kwamba Yehova hatatuacha. Tuliimba mistari kadhaa. Kuimba kwetu kuligusa mioyo sana hivi kwamba baadhi ya askari wakaanza kulia. Kisha gari-moshi likaanza kuondoka.”
“KINYUME NA ILIVYOTARAJIWA”
Dakt. N. S. Gordienko, profesa katika Chuo Kikuu cha Herzen huko St. Petersburg, anaeleza katika kitabu chake kile ambacho wanyanyasaji walitimiza. Aliandika hivi: “Matokeo yalikuwa kinyume na ilivyotarajiwa; walitaka tengenezo la Mashahidi wa Yehova liwe dhaifu katika Muungano wa Sovieti, lakini wakaliimarisha. Katika makao mapya ambako hakuna mtu alikuwa amesikia kuhusu Mashahidi wa Yehova, ‘waliwaambukiza’ wenyeji kupitia imani yao na uaminifu wao kwa imani hiyo.”
Mashahidi wengi walizoea mazingira mapya haraka. Makutaniko madogo yalianzishwa na kugawiwa maeneo. Nikolai Kalibaba anasema: “Kuna wakati huko Siberia tulihubiri nyumba kwa nyumba, au ni sahihi zaidi kusema kwamba tulihubiri kutoka nyumba moja kisha tukaruka nyumba mbili au tatu kabla ya kuhubiri nyumba nyingine. Lakini hilo lilikuwa hatari. Tulifaulu jinsi gani? Tulijaribu kufanya ziara ya kurudia baada ya mwezi mmoja hivi. Tulianza mazungumzo kwa kuuliza, ‘Je, mnauza kuku, mbuzi, au ng’ombe?’ Kisha tungebadili mazungumzo yahusu Ufalme. Shirika la KGB liligundua hilo na makala ilichapishwa katika gazeti kuwaonya watu wasizungumze na Mashahidi wa Yehova. Makala hiyo ilisema kuwa Mashahidi walienda nyumba kwa nyumba wakiuliza ikiwa kuna mbuzi, ng’ombe, na kuku, lakini tulichokuwa tukitafuta hasa ni kondoo!”
Gavriil Livy anasema: “Akina ndugu walijaribu kuhubiri ingawa maofisa wa KGB walikuwa wakiwachunguza. Ikiwa watu katika Muungano wa Sovieti walishuku kuwa unajaribu kuzungumza nao kuhusu dini, waliwajulisha polisi mara moja. Bado tuliendelea kuhubiri ingawa hatukupata matokeo yoyote mwanzoni. Lakini baada ya muda, kweli ilianza kubadili baadhi ya wenyeji. Mmoja alikuwa mwanamume Mrusi ambaye kwa kawaida alilewa sana. Alipojifunza kweli, alipatanisha maisha yake na kanuni za Biblia na akawa Shahidi mwenye bidii. Ofisa wa KGB alimwita na kumwambia: ‘Unashirikiana na akina nani? Hao Mashahidi wote ni Waukrainia.’
“Ndugu huyo alijibu: ‘Nilipokuwa mlevi nililala kwenye mitaro, nanyi hamkujishughulisha nami. Sasa kwa kuwa nimekuwa mtu wa kawaida anayetii sheria, hilo haliwafurahishi. Waukrainia wengi wanaondoka Siberia, lakini wanaacha Wasiberia ambao wamefundishwa na Mungu jinsi ya kuishi.’”
Baada ya miaka michache, ofisa mmoja kutoka Irkutsk aliwaandikia hivi wenye mamlaka huko Moscow: “Wafanyakazi kadhaa wa eneo hili wamesema kwamba wote kati ya hawa [Mashahidi wa Yehova] wanapaswa kupelekwa eneo mmoja huko kaskazini ili wasiwasiliane na mtu mwingine yeyote na waelimishwe upya.” Wenye mamlaka huko Siberia na huko Moscow hawakujua wafanye nini ili kuwanyamazisha Mashahidi wa Yehova.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 101]
Mashahidi waliohamishwa walijijengea nyumba huko Siberia
[Picha katika ukurasa wa 102]
Magdalina Beloshitskaya na familia yake walipelekwa uhamishoni Siberia
-