-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
NYAKATI ZOTE MHUBIRI ATARUDI
Hotuba za kuendeleza mawazo ya Kisovieti hazikutolewa kambini tu. Zilitolewa katika majiji makubwa kwa ajili ya umma. Wasemaji wenye uzoefu walitembelea hasa maeneo yaliyokuwa na Mashahidi wengi sana, kama vile Vorkuta, Inta, Ukhta, na Syktyvkar. Ndugu Gutshmidt anasema: “Mnamo 1957, msemaji mmoja alikuja kwenye Jumba la Utamaduni la wachimba migodi wa Inta, ambamo watu 300 walikuwa wamekusanyika. Alieleza imani za Mashahidi wa Yehova na jinsi wanavyohubiri. Baada ya kufafanua kwa usahihi mbinu za kuhubiri, ambazo zilitia ndani mapendekezo zaidi ya 15 tunayotumia katika ziara za kurudia, alisema: ‘Ikiwa hutampinga, nyakati zote mhubiri atarudi. Ikiwa bado humpingi katika ziara yake ya pili, atarudi mara ya tatu.’
“Kwa saa mbili alikuwa amezungumzia ziara sita kama hizo neno kwa neno kulingana na mbinu tulizotumia, naye akasoma maandiko yote yaliyotumiwa kutoka kwenye maandishi yake. Mke wangu, Polina, aliniandikia kuhusu hilo nilipokuwa nimefungwa katika kambi, naye akanieleza kwamba akina ndugu waliohudhuria hawakuamini waliyosikia. Baada ya hotuba hiyo, magazeti yalichapisha habari mbaya kuhusu Mashahidi, lakini hayakutoa ufafanuzi kamili kuhusu Ufalme. Isitoshe, hotuba hiyo yote ilitangazwa kwenye redio. Kwa sababu hiyo, maelfu ya wakaaji wa jiji walisikia jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyohubiri na mambo wanayohubiri.
“Mnamo 1962, msemaji kutoka Moscow alifika ili kutoa hotuba kuhusu Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuzungumzia historia yao ya kisasa, akasema hivi: ‘Kila mwezi mamilioni ya dola humwagika huko Brooklyn kupitia michango ya kusaidia utendaji wa Mashahidi katika nchi kadhaa. Lakini hakuna hata kiongozi wao mmoja aliye na kabati kubwa la nguo. Wote hula pamoja katika chumba cha kulia chakula, mtunza-chumba pamoja na msimamizi, na hakuna tofauti kati yao. Wote huitana ndugu na dada, kama vile sisi huitana komredi.’
“Kimya kilitanda katika jumba hilo. Kisha akaongeza, ‘Lakini hatutafuata mawazo yao, ingawa yanaonekana kuwa mazuri, kwa kuwa tunataka kuwa na utaratibu kama huo bila kumhusisha Mungu, tutategemea mikono na vichwa vyetu wenyewe.’
“Hilo lilitutia moyo sana kwa sababu kwa mara ya kwanza, tulisikia ukweli kuhusu Mashahidi wa Yehova ukisemwa na wenye mamlaka. Hotuba kama hizo pia ziliwapa watu wengi nafasi za kusikia ukweli kuwahusu Mashahidi wa Yehova kutoka kwa wenye mamlaka. Hata hivyo, watu walihitaji kujionea kuwa mafundisho ya Biblia yanaweza kuboresha maisha yao.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mnamo 1949, nilihamishwa hadi Inta, kwenye kambi ya wafungwa wa kisiasa. Mfumo wa kurekebisha wafungwa kwenye kambi hiyo ulikuwa na vizuizi vingi. Miongoni mwa wafungwa kulikuwa na hali ya kufungiana kinyongo, ufidhuli, upotovu wa maadili, kutojali, na kuvunjika moyo. Uvumi wa kwamba wafungwa wote kambini watapigwa risasi au watafungwa kifungo cha maisha, ulifanya hali ambayo tayari ilikuwa mbaya iwe mbaya hata zaidi. Chini ya hali kama hizo wafungwa kadhaa wakawa vichaa. Kwa sababu kulikuwa na watu wengi kambini ambao walikuwa wakiwapasha maaskari habari, wafungwa hawakuaminiana na walichukiana. Kila mtu aliishi kivyake bila kujishughulisha na wengine. Ubinafsi na pupa vilienea sana.
Kikundi kimoja cha wafungwa wanawake 40 hivi kilikuwa tofauti sana na wafungwa wengine. Kwa kawaida walikaa pamoja na kwa kushangaza walikuwa safi, wenye kuvutia, wenye huruma, na wenye urafiki. Wengi wao walikuwa wasichana na mabinti wadogo. Nilikuja kugundua kwamba walikuwa wafuasi wa dini, Mashahidi wa Yehova. Wafungwa waliwatendea kwa njia tofautitofauti. Wengine waliwatendea vibaya na kwa uhasama. Wengine walistaajabia tabia zao, hasa upendo miongoni mwao. Kwa mfano, mmoja wao alipokuwa mgonjwa, wengine wangepanga zamu ya kumhudumia. Kwenye kambi hiyo, hilo lilikuwa jambo lisilo la kawaida.
Nilishangazwa kwamba kikundi hicho kilikuwa na watu kutoka mataifa mengi, na bado, walikuwa na urafiki mkubwa miongoni mwao. Kufikia wakati huo nilikuwa nimekata tamaa kabisa ya maisha. Wakati fulani nilipokuwa nimevunjika moyo sana, nilikaa chini na kuanza kulia. Mmoja kati ya wasichana wale alinikaribia na kuniuliza, “Polina, kwa nini unalia?”
Nilimjibu, “Sitaki kuendelea kuishi.”
Msichana aliyeitwa Lidia Nikulina, alianza kunifariji. Alinieleza kusudi la uhai, jinsi Mungu atakavyosuluhisha matatizo ya wanadamu na mambo mengine mengi. Mnamo Julai (Mwezi wa Saba) 1954, niliachiliwa. Kufikia wakati huo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamenifundisha mambo mengi na nilifurahia kuwa mmoja wao.
-