Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • KESI ILIYOTANGAZWA SANA

      Ripoti iliyotumwa Moscow na ofisa fulani wa serikali kutoka Irkutsk ilisema hivi: “[Mashahidi wa Yehova katika Wilaya ya Irkutsk] walifanya utendaji mwingi kwa siri. Katika miezi sita ya mwisho ya mwaka wa 1959, shirika la KGB liligundua mashini tano za kuchapishia zilizokuwa kwenye chumba cha chini.” Mashini hizo zilikuwa katika miji ya Zima na Tulun, huko Siberia na pia vijiji vya Kitoy, Oktyabr’skiy, na Zalari. Baada ya mashini hizo kugunduliwa, waliohusika katika uchapishaji huo walikamatwa.

      Ndugu wanne waliokamatwa mwanzoni waliandikisha taarifa kuhusu uchapishaji wa vichapo. Kwa hila, wapelelezi waliwalazimisha ndugu hao kuandikisha taarifa hizo. Kisha KGB ikabadilisha taarifa hizo na kuzichapisha kwenye magazeti ya habari. Ndugu hao wanne waliachiliwa huru na ndugu wengine wanane wakashikwa. Kesi yao ingesikilizwa huko Tulun Aprili 1960. KGB ilifanya mipango ili kesi hiyo itangazwe sana. Walipanga kuwatumia wale ndugu wanne kuwa mashahidi wa upande wa mashtaka. Wengi katika makutaniko walifikiri kwamba ndugu hao walikuwa wakishirikiana na KGB.

      Wapelelezi wa KGB walinuia kutumia kesi hiyo kuvunja imani ya Shahidi yeyote ambaye angefika mahakamani na kuchochea watu wawachukie Mashahidi. Wakiwa na hilo akilini, wapelelezi wa KGB walipanga watu watembelee chumba kimoja cha chini ambacho akina ndugu walikitumia kuchapisha vichapo kwa miaka mingi. Muda si muda, kulikuwa na uvumi kuhusu utendaji wa “madhehebu” ya siri. Siku ya kesi ilipofika, ukumbi wa mahakama ulijaa watu zaidi ya 300, kutia ndani waandishi wa habari wa magazeti na televisheni, na wengine wao walisafiri kutoka Moscow. Pia Mashahidi wengi wa Yehova walikuwepo.

      VURUGU MAHAKAMANI

      Hata hivyo, bila kutarajia, mipango ya KGB ilianza kuharibika. Ndugu walioandikisha taarifa hizo waligundua kosa lao. Siku moja kabla ya kesi, wote waliazimia kufanya chochote wanachoweza ili kumpa Yehova utukufu. Wakati wa kesi, walisema kwamba walikuwa wamedanganywa na kwamba taarifa walizoandikisha zilikuwa zimebadilishwa. Kisha wakatangaza hivi: “Tuko tayari kuketi kizimbani pamoja na ndugu zetu.” Kukawa na vurugu mahakamani.

      Zaidi ya hayo, walipokuwa wanaulizwa maswali, ndugu waliokuwa kizimbani walifaulu kuyajibu bila kuwasaliti wengine. Kwa mfano, wakati hakimu alipomuuliza Grigory Timchuk ni nani aliyetengeneza mashini ya kuchapishia nyumbani kwake, alijibu, “Mimi ndiye niliyeitengeneza.” Alipoulizwa ni nani aliyechapisha vichapo, alijibu, “Ni mimi.” Alipoulizwa ni nani aliyekuwa akivisambaza vichapo hivyo, alijibu, “Ni mimi.” Alipoulizwa ni nani aliyenunua na kumletea karatasi, kwa mara nyingine alijibu, “Mimi ndiye niliyefanya hivyo pia.” Kisha mwendesha-mashtaka akamuuliza: “Kwani wewe ni nani? Je, wewe ndiye meneja, mleta-bidhaa, na mfanyakazi?”

      “BARUA HIYO ILITUTIA MOYO SANA!”

      Ilipoonekana hakuna mashahidi upande wa mashtaka, mwendesha-mashtaka aliwashutumu akina ndugu kwamba walikuwa wamepanga njama na wageni. Ili kuthibitisha hilo, alitoa barua kutoka kwa Nathan H. Knorr wa Betheli ya Brooklyn. Mikhail Savitsky, mmoja kati ya akina ndugu waliohudhuria kesi hiyo, anasema: “Kwa sauti mwendesha-mashtaka alianza kusoma barua moja kutoka kwa Ndugu Knorr aliyowaandikia akina ndugu katika Muungano wa Sovieti, ambayo ilikuwa imenaswa na KGB. Mashahidi waliokuwa ukumbini, waliona barua hiyo kama zawadi kutoka kwa Yehova. Ilitutia moyo sana! Tulisikia mashauri yenye hekima kutoka katika Biblia na tulitiwa moyo kuwatumikia ndugu zetu kwa upendo na kuwa waaminifu chini ya majaribu. Isitoshe, Mashahidi wa Yehova walihimizwa wamtegemee Mungu katika mambo yote, wamwombe hekima na mwongozo, na pia washirikiane kwa ukaribu na ndugu waliowekwa rasmi. Mwendesha-mashtaka aliisoma barua hiyo kuanzia mwanzo hadi mwisho. Tulisikiliza kwa makini sana. Ni kana kwamba tulikuwa tumehudhuria kusanyiko!” Ingawa ndugu hao walihukumiwa vifungo mbalimbali, wote waliohudhuria walibaki imara katika azimio lao la kumtumikia Yehova.

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Kwenye miji ya Irkutsk na Tomsk na baadaye kwenye majiji mengine ya Urusi, vikundi vya akina ndugu vilivyojitenga na tengenezo viliendelea kuongezeka. Mnamo Machi 1958, vikundi hivyo vilikuwa vimeanzisha ‘halmashauri yao ya nchi’ vikitazamia itatambuliwa na makutaniko yote.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki